Jiue Mwenyewe Sehemu ya Pili
KIJASUSI

Ep 02: Jiue Mwenyewe

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Pili

IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE


Simulizi : Jiue Mwenyewe

Sehemu Ya Pili (2)

Gina alikuwa kasimama kando ya ua kubwa katika Uwanja wa ndege wa jeshi, Terminal One, alipoona gari ya Scoba inaingia, akajitokeza na kuiendea, moja kwa moja alimwendea Kamnda Amata.

“Umependeza dear! Utafikiri unaenda harusini,” Gina akamwambia Kamnda huku akimkumbatia na kumbusu.

“Yeah, ukipendeza namna hii kamwe adui zako hawatajua kama ni mtu wa hatari, watalegeza silaha zao na kukukaribisha kahawa,” Kamanda akajibu huku akimtoa Gina kifuani mwake, akamtazama usoni, “Gina, nitahitaji msaada wako wa hali na mali.”

“Sawa Boss!”

Kamanda akatoka na kuiendea ndege ndogo iliyokuwa tayari kwa ajili yake kumfikisha Mwadui, akafunguliwa mlango na kuingia ndani yake, akaketi na kufunga mkanda. Safri iaanza.

§§§§§

Saa tisa mchana Kamanda Amata alitua katika uwanja mdogo wa ndege wa Mwadui, uwanja uliojengwa pembezoni kidogo mwa mgodi huo. Kwa kuwa alikuwa peke yake, haikuchukua muda kutoka nje ya ndege hiyo na moja kwa moja kuelekea jengo lenye ofisi za utawala.nakapokelewa na wafanyakazi na na inspekta wa polisi aliyekuwa hapo akimsubiri baada ya kupewa taarifa ya ujio wake.

“Karibu Mwadui mkuu,” alimkaribisha.

“Asante sana Afande, nipe taarifa ya hapa na nini kimetokea,” kamanda akamwambia yule Inspekta huku wakiongozana kuingia ndani ya jengo la utawala pamoja na wafanyakazi wachache wenye nyadhifa za juu katika Mgodi huo. Wakaketi kwenye ofisi ya Makivango.

“Kwanza poleni sana kwa matatizo, hebu niambieni vyema, ilikuwaje, nani amefanya mauaji haya na kuchukua hizo almasi?” akauliza.

“Alikuja Mheshimiwa Waziri wa Nisahati na Madini, akifguatana na vijana wa jeshi la polisi wawili waliovalia sare za jeshi hilo, walikuja kwa ndege ya Serikali…” Inspekta alieleza hali yote ilivyokuwa kadiri nay eye alivyoambiwa na kuandika kwenye kijidaftari chake.

“Mnaweza kunambia hiyo ndege ilifika hapa saa ngapi?” akauliza tena.

“Ndege ilitua hapa kati ya saa 5:20 na 5:40 hivi asubuhi ya leo.” Akajibu msemaji wa ofisi hiyo.

“Sawa, na ninyi mlikuwa amkimtegemea Waziri saa ngapi na kwa lipi?” Kamanda akatupa swali.

“Tulimtegemea muda huohuo, lakini alikuwa anakuja kwa ajili ya kukagua mgodi, badala yake tukapewa taarifa ameagizwa kuchukua almasi kwani zilihitajika serikalini kwa shughuli ya haraka, na alikuwa na uthibitisho ambao ni barua kutoka Ikulu,” akajibu.

Kamanda Amata akatikisa kichwa na kuuliza tena maswali kadhaa, kisha akaomba kukiona chumba cha Dr. McLean, akapelekwa. Alisimama mlangoni, akakiangalia jinsi kilivyo na kupangwa vilevile, kilichokosekana ni mhusika tu wa ofisi hiyo ambaye tayari muda huo alikuwa barafuni kwatika hospitali ya Shinyanga.

Alisogea na kuketi kwenye kiti cha mgeni akikitazama kile cha Dr. McLean, akazungusha macho yake huku na kule, akasimama na kuzunguka upande wa pili, akaanzalia huku na kule kisha akafungua mlango wa chooni akatazama vizuri zaidi, alakifungia ndani ya choo hicho, alitazama kila kilichomo kwa makini kabisa, hakukuwa na kipya zaidi ya sinki la choo, sehemu ya kuogea, magazeti na majarida katika mfuko maalumu uliobanwa nyuma ya mlango. Akageuka huku na kule, kisha akatoka.

“Ok, sasa naomba nipeleke kwenye ofisi ya Boharia,” akapelekwa na kuikagua kwa mtindo uleule, kisha wakarudi wote pamoja.

“Sawa, hakuna la zaidi, naomba niende lakini, ofisi hizo mbili zisiguswe na mtu yeyote mpaka mtakapopata taarifa nyingine,” akamgeukia yule Afisa na kumuuliza, “Enhe ofisi hii ambayo ni mapokezi nani anahusika (…) nahitaji kuonana naye,” akasema.

“Aaa huyu dada tumemuhifadhi kituo cha polisi ili kuisaidia polisi,” akajibu Inspekta.

“Ok, nahitaji kumuona,” akasisitiza.

Kamanda Amata akatoka pamoja na Inspekta wa polisi na vijana wawili kutoka jeshi hilo, kwa kutumia gari ya polisi walielekea kituo kikuu cha wilaya ambako huko alihifadhiwa Katibu Muhtasi wa ofisi ile.

Mnamo saa kumi za jioni walifika katika kituo hicho na kukuta makundi ya watu waliokuwa pembeni mwa jengo hilo wakiongea hili na lile kama ilivyo kwa kituo chochote cha polisi, wapo waliokuja kuwaona ndugu zao, wapo waliokuja kuwawekea dhamana ndugu zao, wapo waliokuwa kwa hili na ile lakini pia wapo waliokuja kujaribu kuvunja sheria ya nchi, kupenyeza rupia ili kesi zao ziuawe kimazingara.

Kamanda Amata akifuatana na yule Inspekta moja kwa moja walielekea katika moja ya ofisi za kituo hicho, ofisi ilikuwa tupu isipokuwa meza moja ya chuma, viti viwili vya chuma upande huu na upande ule wa meza, Kamanda Amata akakalia kiti kimoja kile ambacho kipo upande wa mlango, ambacho kwa vyovyote angetakiwa kukaa mgeni au mtuhumiwa kama inabidi wakati mwenyeji wake angekaa kwenye kile kinachoutazama mlango ili amuone mgeni wake au mtuhumiwa wake anapoingia, Amata alifanya tofauti. Mara mlango ukafunguliwa nyuma yake, akiwa anatazama simu yake kubwa aina ya Iphone, Kamanda Amata aliweza kuona yanayotukia nyuma yake, mwanadada aliye na nywel;e timu timu, alikuwa akiingizwa ndani ya chumba hicho akiwa na pingu mkononi mwake huku akiongozwa na WP mmoja.

“Mheshimiwa, ungekaa upande ule ili huyu akae huku,” yule WP alitoa maelekezo kwa Amata.

“Asante, lakini kwa leo nampa upendeleo wa pekee, muweke aketi kule mimi nitaketi hapa,” Kamanda akajibu. Yule WP akampeleka msichana yule katika kiti cha upande wa pili. Mara nyingi sana kosa hili hufanywa na wengi, kumuweka mtuhumiwa au mtu ambaye unajua kabisa anaweza kukusababishia hatari Fulani upande wa mlango, kama ana silaha yoyote akikudhibiti huwezi kumkimbia, lakini kumbe ukikaa wewe mlangoni yeye upande usio na mlango basi unaweza kumkimbia au kumdhibiti asitoroke.

“Mfungue pingu, huyu sio Mtuhumiwa, mnafanya kosa,” Kamanda akatoa amri, “Kisha utupishe kidogo,” akaongeza. Baada ya pingu zile kufunguliwa, yule WP akatoka na kuwaacha wawili hao peke yao ofisini. Kamanda Amata akainua uso wake na kumtazama yule binti. Alikuwa mweupe wa wastani, nywele ndefu ambazo kabla ya mkasa huo ilionekana zilikuwa katika mtindo mzuri sana, macho yake yaliyokuwa yamelegea kidogo yalimfanya Amata kujua kuwa mwanadada huyu hutumia miwani kwa kuona na kusoma. Alimtazama kwa makini sana, akashusha macho yake taratibu, akasimama kifuani, kifua kilichokuwa kikipanda na kushuka kwa hofu, yote hayo kamnda aliyang’amua kwa sekunde kadhaa, kwa jumla aligundua kuwa msichana huyo hajaolewa kwani alikuwa na kila dalili za kuwa singo.

“Naitwa Kamanda Amata,” alijitambulisha bila kificho mbele ya mrembo huyo. Na hapo aliuona mshtuko wa wazi kutoka kwa huyo binti aliye mbele yake, aligutuka na kuacha midomo wazi kiasi kama mtu aliyeona Malaika aliyemtokea ghafla.

“Kamanda Amata!” akashangaa na kuuliza kwa sauti ndogo.

Msichana huyo hakuamini kama mbele yake kakutana na mtu aliyekuwa akimsoma tu kwenye riwaya, hakuwahi kufikiri kama yupo kiumbe hai mwenye ina na sifa hizo, hakuamini, alitikisa kichwa akakumbuka visa kadhaa vya kijasusi vilivyomhusisha kijana huyo kama mpelelezi namba moja wa serikali, anayetatua migogoro iliyogubikwa na siri nzito kwa siri vilevile. Hakuwahi kujua kama mtu huyo yupo, sasa alikuwa mbele yake, hata hivyo hakuamini.

“Naitwa Makivango,” naye akajitambulisha kwa kitetemeshi.

“Usiogope Makivango, nimekuja kukutoa na kukuacha huru kama mwanzo, lakini nimekuja nataka kuongea na wewe mambo kadhaa yaliyojiri pale ofisini kwenu leo asubuhi, akameza mate. Kwa kuanza alimtaka Makivango ajieleze juu ya maisha yake kwa kifupi, hapo Kamanda Amata alipata kujua kuwa Makivango ni binti wa Kichaga, aliyezaliwa huko Lushoto mkoni Tanga katika hospitali ya Mlalo miaka kama ishirini na tatu iliyopita na kukulia huko Lushoto ikiwa na kupata elimu ya msingi na kadhalika. Hakika Kamanda Amata hakuwa mbali na ukweli kwani alipomuona tu, muonekano wake ulijieleza, Mchaga wa Rombo.

“Niambie, juu ya kisa kilichotokea leo ofisini kwako,” Kamnda akamuomba, na Makivango akaeleza kila kitu kuanzia kufika kwao, walikuwa wangapi na ni nani na ni nani kwa wale aliowajua. Kisha Kamnda akaanza kuuliza maswali ambayo kwayo labda yangempa mwanga katika kisa hicho tata.

“Mlikuwa mnategemea ugeni huo saa ngapi?”

“Tuliutegemea saa tano kama na nusu hivi.”

“Na ulikuwa unajua kuwa ugeni huo ulikuwa unakuja kufanya nini?”

“Kwa taarifa za wizara, tuliajulishwa kuwa ugeni huo unakuja kwa ajili ya kutembelea na kukagua mgodi.”

“Umesema kuwa ulimgundua McLean akiwa ameuawa ofisini mwake wakati ulipokuwa ukipeleka kahawa, je ulitegemea kukuta watu wangapi ndani ya ofisi hiyo?”

“Kwa kweli nilitegemea watu wawili tu kwani wale vijana wa polisi na wengine walikuwa wakishughulikia kupakia almasi ndegeni.”

“Na ulipomkuta Mc Lean ameuawa, je ulimkuta mtu mwingine ofisini?”

“Hapana, alikuwa peke yake.”

“Na huyo mgeni mwingine ambaye ni Waziri wa Nishati na Madini uliuyetarajia kumkuta, ulimuona alipotoka?”

Hapo Makivango akatulia kidogo, sekunde kadhaa zikapita, akashusha pumzi na kumeza mate, akajaribu kukumbuka jambo.

“Hapana, sikutazama kama alikuwepo maana akili yangu ilipaa baada ya kuona mwili wa Mc Lean.”

“Ok, kwa hiyo inawezekana alijificha nyuma ya mlango au kabatini?”

“Mh!” Makivango akaguna, “Labda lakini sina uhakika kwa kuwa milango ile ni ya aluminiam, ile ya kuslide.

“Sasa unafikiri alikuwa wapi, au alipita na wewe hukumuona?” lilikuwa ni swali linguine ambalo lilimpa shida Makivango.

“Hapana, hapana, hakutoka kabisa na ofisini hakuwepo,” akajibu huku akipumua kwa nguvu.

“Je kuna mlango wowote wa siri kwenye ofisi ya Mc Lean ambao mtu anaweza kuutumia kutoka nje bila kujulikana?”

“Hapana, sidhani kama kuna kitu kama hicho,” akajibu.

“Basi hilo lilikua pepo, au we unasemaje?” kamanda akauliza tena lakini mara hii akitoa cheko la mbali kidogo.

“Swali la mwisho,” kamnda akatamka, na Makivango akamtazama Kamanda usoni kidogo kisha akashusha macho yake chini.

“Unafikiri, Waziri mwenye dhamana anaweza kuja na kuua bosi wako kisha vibaraka wake au yeye kuua mtu was too, na kuchukua almasi ambazo ni mali ya serikali?”

“Hapana haiwezekani,” makivango akajibu.

“Kwa hiyo unataka kunambia ni nani aliyeweza kuja na ndege ya serikali na kufanya hujuma hiyo, majambazi? Au magaidi?” Kamanda akahoji. Makivango akatulia kimya, hakuwa na jibu, alibaki kumwemwesa tu.

“Makivango!” Kamanda akaita. Makivango akanyanyua uso wake na kumtazama usoni, machozi yalikuwa huku na huku, mashavu yake yaling’aa kwa chozi hilo, uzuri wake uliojificha nyuma ya vipodozi vya kisasa ulidhihirika wazi, Kamanda akatabasamu, akahisi moypo wake ukipiga harakaharaka, ikawa zamu yake kutazama chini, kisha akamtazama tena Makivango.

“Ok mrembo, kama kutakuwa na lolote ninalolihitaji nitakutafuta, kwa sasa utaachiliwa huru, lakini, usizungumze na mtu yeyote juu ya hili, hata mpenzi wako usimwambie lolote, ukikiuka ujue ndio mwisho wako,” Kamanda Amata akamaliza na kuinua simu ya mezani hapo akazungusha namba Fulani kisha akaita mtu wa upande wa pili.

WP yuleyule aliyemleta Makivango alikuja tena na ile pingu mkononi, nyuma yake akafuata yule Inspekta.

“Naomba mfanye utaratibu wenu, huyu aachiwe huru, aendelee na shughuli zake lakini kila baada ya siku mbili aje hapa kuripoti, na asipoonekana atafutwe mara moja mpaka utata huu ukipatiwa ufumbuzi.

Baada ya dakika kadhaa Makivango aliachiwa huru na kupewa masharti hayo na polisi. Kamanda Amata aliagana na Inspekta na kumwambi kuwa muda wowote ataonana naye kama atahitaji msaada zaidi.

“Naweza kukusindikiza mpaka nyumbani kwako?” Kamanda akamuuliza Makivango.

“Nitashukuru,” alijibu kwa unyonge. Kamanda Amata akakodi tax akaingia pamoja na Makivango, wakaondoka eneo lile.

DAR ES SALAAM saa 10:23 jioni

MADAM S alikuwa hajanyanyuka kutoka kitini kwake tangu alipoagana na Kamanda Amata, yalikuwa yamepita masaa takribani sita, hata hamu ya chakula hakuwa nayo, mawazo lukuki yalimtawala kichwani.

Simu ya mezani kwake ikaita, akainyakuwa na kuitega sikioni.

“Ndiyo Kamanda, tumesitisha kila aina ya uchunguzi mpaka tupate jibu kutoka kwako,” akaongea na mtu wa pili. Baada ya mazungumzo mafupi, Madam S alimwita Kamanda kurudi Dar es salaam mara moja.

USIKU WA SIKU HIYO

KAMANDA Amata akiwa na Madam S pamoja na Chiba walikuwa Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Dar es salaam kwa kikao cha kazi.

“Kwa hiyo, unasema ndege iliondoka hapa saa ngapi?” Kamanda Amata alimuuliza Mkuu wa Idara ya mambo ya anga anayeratibu safari za ndege kutoka na kuingia nchini.

“Ndege ya serikali, iliondoka saa moja kamili asubuhi, ikaelekea North Mara, taarifa tulizonazo ni kuwa, ilifika kule saa mbili asubuhi na wakaondoka tena saa nne kuelekea Mwadui ambako saa tano na dakika ishirini walitua pale,” Mkuu wa Idara akatoa ufafanuzi.

“Sawa, nimekuelewa, je; kwa sasa baada ya ile ndege kuruka pale Mwadui, mmeweza kuiona imeelekea wapi?” Madam S aliuliza.

“Ile ndege baada ya kuruka Mwadui, ilionekana kuelekea Kaskazini, na ikatupotea kwenye rada zikiwa zmebaki kilomita chache kufika mpakani na Uganda,” akaeleza.

“Ok, naomba muendelee kuitafuta popote ilipo, na mtupe taarifa pindi tu mkiiona,” Madam S akatoa amri. Wakanyanyuka na kutoka katika ofisi hiyo. Safari ilielekea kwa Katibu wa Wizara usiku huohuo.

Mtaa wa Masaki, Mtaa wa wadosi, Scoba alikunja kona kushoto na kufuata barabara ndogo iingiayo kwenye nyumba za pembezoni, nyumba ya kwanza, ya pili, ya tatu, akaegesha gari pembeni na kusimama. Wote wakashuka na kuliendea lango la jumba hilo la bei mbaya, mali ya serikali. Wakakaribishwa na mlinzi wa kimasai aliyekuwa akilinda mlangoni, haikuwa tabu kwao kuruhusiwa kuingia katika kasri hilo.

Waliyemhitaji walimkuta sebuleni akiwa kajipumzisha huku mtoto wake akiwa pembeni anamsomea kitabu cha Hujuma, alipowaona wageni hao, akamwambia yule mtoto akalale na angemwita baadae.

“Karibuni sana, karibuni ndani, mnanitisha usiku wote huu kutembelewa na watu nisiowafahamu,” akawakaribisha huku akiwapa mikono kwa zamu, kisha wote wakaketi chini, akashusha pumzi, “Ndio labda tufahamiane,” aliongea akionekana kuwa na hofu.

“Sisi ni watu wa Idara ya Usalama,” Madam S alitambulisha kwa ujumla wao, “samahani kwa kukuvamia usiku huu, lakini kwetu ulikuwa ni muda muafaka sana kuonana nawe, najua mpaka hapo umefahamu nini tunataka kuzungumza nawe,” akaongeza kusema.

“Yeah, ndiyo, nawasikiliza wakuu, lakini kabla hatujaendelea na mazungumzo, ningependa kuona vitambulisho vyenu,” akawaomba. Kila mmoja akatoa kitambulisho na kumuonesha, akajiridhisha navyo kwani alijua vitambulisho vya Usalama wa Taifa vinavyokuwa, hivyo kungekuwa na kughushi kwa aina yoyote ile angetambua pia, lakini majina yaliooneshwa katika

“Tuna jambo moja tu, Mheshimiwa kujua, kama ujuavyo tukio lililotokea leo asubuhi huko Mwadui, unaweza kunambia katika msafara wa Waziri ni nani na nani walifuatan nae?” Madam S akahoji.

“Ulikuwa ni msafara wa watu kumi na tano, wakiwemo Wabunge saba wa kamati ya madini, waziri kivuli wa Nishati na Madini na wageni wane kutoka mataifa ya Canada na Uingereza zaidi ya hapo ni watendaji wa Wizara akiwamo katibu Muhtasi wa Waziri mwenyewe,” akajibu kwa ufasaha.

Kwa jibu hilo Kamanda Amata, akili yake ikafanya kazi harakaharaka akamuuliza, “Unafahamu lolote juu ya mpango wa wizi wa Almasi uliofanyika leo?”

“Mpango kama mpango, kiukweli siujui, labda kama Mheshimiwa Waziri alikuwa na mpango binafsi katika hilo, lakini mimi hakuna ninachojua kabisa,” akajibu.

“Ok, naomba kupata taarifa kamili za watu wote waliokuwa ndegeni, kuanzia walikozaliwa, wanakoishi na wanafanya nini, napenda kupata usiku huu, nikiwa na maana ama twende ofisini kwako sasa au unipatie kwa njia yoyote lakini usiku huu, kwa sababu kama ujuavyo, kumetokea wizi wa almasi, upotevu wa ndege ya serikali watu wote waliopo ndani yake,” Kamanda akamaliza na kujiegemeza kitini, Madam S akatikisa kichwa juu chini kushiria kuwa karidhika na hilo lililosemwa.

“Taarifa zao zote ninazo kwa sababu pia ni wajibu kuzihifadhi kwa dharula yoyote kwa mfano kama hii, niko tayari kuwapa ushirikiano wowote mtakao,” akajibu huku akinyanyuka na kuchukua fylana yake iliyokuwa kitini akaivaa, na saa yake nayo akaiandaa kuivaa mkononi mwake, lakini kabla hajaiweka mkononi, sauti ya Kamanda ikamshtua.

“Samahani, saa yako ni nzuri sana naweza kuiona?” akaomba.

“Bila shaka,” akampatia Kamanda Amata.

Kamanda Amata, akaitazama kidadisi sana saa ile na kuigeuza geuza huku na huko.

“Umeipenda?” akauliza

“Kwa kweli ni saa ya gharama sana kati ya saa za gharama,” Kamanda akajibu huku macho yake bado yakiitalii.

Wakati bado akiishangaa ile saa, mwenyeji wao akatoka pale sebuleni na kuelekea chumbani akiwataka kumsubiri kwa dakika kadhaa. Ni nafasi hiyo ambayo Chiba, mtaalama wa mawasiliano na teknolojia ya kompyuta katika Idara ya Kijasusi ya Tanzania, alipomnyang’anya ile saa Amata, kwa haraka akaifungua pini yake ya pembeni, akaichomoa na kuichomeka kwa chini kwenye tundu dogo sana lililo katikati ya mfuniko, mfuniko wake ukaachia upande mmoja, akabana kitu Fulani kwa ncha za kidole chake na kukivuta, kisha akairudishia kama ilivyokuwa na muda huohuo mwenyeji wao alikuwa akifika sebuleni. Akampa saa yake huku akimwuliza, “Mzee uko juu, hii saa uliipata duka gani?”

“Aaa nimepewa zawadi na hawa wageni wa Uingereza walioondoka na Mheshimiwa Waziri, tulipokutana kule Geneva kwenye mkutano wan chi zinazoongoza kwa uchimbaji wa madini duniani nay a kwetu ilikuwa mojawapo, ni saa nzuri sana kiukweli,” alijibu huku wakiwa wanatoka.

Usiku huo ndani ya ofisi ya Katibu huyo wa wizara, TSA walipata taarifa za wote waliokuwa ndegeni na Waziri. Walipoona zinatosha, wakaondoka na mwenyeji wao na kumsindikiza mpaka nyumbani kwake kisha wao wakageuza gari na kurudi.

Wakiwa ndani ya gari yao huku Scoba akiedelea kuwapeleka wanakokutaka, ukimya ulitawala kwa jozi ya dakika, kila mmoja mawazo yake yalipaa huku na kule.

“Mnajua!” Chiba aliwagutusha, wote wakamtazama isipokuwa Scoba, akajikohoza kidogo, ile saa ile, ina kifaa cha kunasa mawasiliano ya watu, hivi tulivyokuwa tunaongea pale, kuna watu wamenasa yote tuliyokuwa tukiyazungumza,” Chiba akawaeleza, Madam S akashtuka kidogo na kukodoa macho.

“Unajua, Chiba, mi ile saa niliistukia mapema kwa sababu, katika kioo pale juu katikati ya mishale kuna kajitaa kekundu kanawaka na kuzima na wakati tunaongea kakawa kanawaka harakaharaka, lakini kwa macho tupu huwezi kukaona kirahisi kutokana na rangi yake, ndiyo maana niliposhtukia ile saa nikatoa miwani yaku ambayo wengi hujua ya kusomea na kuivaa ndipo nilipouona ule mwanga kiurahisi zaidi,” Amata akawaeleza.

“Ndiyo, ulipoichukua, mimi nilishajua ni saa ya mtindo gani, ndio maana nikakunyang’anya nikijua nini nadhamiria kufanya na nikafanikiwa, nimeondoa chip ambayo inanasa na kutuma mawasiliano kwa wahusika lakini pia nimeondoa memory card ya simu, kwa kuwa bila memory card ile mic haiwezi kufanya kazi, sasa tutaujua ukweli ulivyo, tusikilize mazungumzo yote tangu mwanzo tukiwa na muda,” Chiba alieleza.

Muda huohuo, simu upepo iliyofungwa ndani ya gari ikakoroma kuashiria kuna taarifa inataka kuingia, Madam akampa ishara Scoba airuhusu.

Kutoka katika ile simu ikasikika sauti ya mtu kama anayeongea kutoka mbali, mara moja walitambua ni mtaalamu wa mambo ya anga kutoka JWTZ ambako rada kubwa kabisa Afrika yenye uwezo wa kuona ndege yoyote inayoingia katika mpaka wa Afrika alikuwa akiongea. Madam S akaongeza sauti kidogo ili wote wasikie.

(…) kwa vipimo vyetu vya chombo cha kunasa muelekeo wa ndege, ndege aina ya Foker Friendship, iliyoruka Mwadui saa tano na dakika hamsini na moja ilielekea Kaskazini Mashariki, lakini baada ya dakika arobaini, ndege hiyo ilishuka chini sana kitaalamu tunaita ‘low attitude’ hapo haikuonekana tena, sasa hatujui kama imeanguka au imetua mahali …

Ilimaliza taarifa ile.

Kamanda Amata akashusha pumzi, na kuwatazama wenzake, kisha akainua mkono na kuiotazama saa yake, ilikuwa saa sita za usiku.

“Madam,” Kamanda akaita.

“Kamanda,” Madam akajibu, wakatzamana.

“Naanza kupata wasiwasi, hapa hatujui nani hasa tunayemchunguza, au nini tunachokitafuta, nafikiri sasa tuanze kufanya chunguzi sambamba maana muda unaisha, kama inawezekana, hiyo ndege itafutwe kuanzi usiku huu kwa nguvu zote za angani, ardhini na majini, wakati sisi tunasaka watuhumiwa na usalama wa watu wetu, maana mwizi wetu anazidi kusonga mbele, tutamkosa,” Kamanda aliongea kwa hisia kali. Chiba akaunga mkono.

“Ok, naungana nanyi nyote, sasa naomba tuonane ofisi ndogo haraka usiku huu, ita Dr Jasmine na Gina dakika kumi,” Madam akatoa uamuzi. Kamanda Amata alimtazama mwanamama huyu ambaye daima aliamini vijana wake, hakupuuza hata siku moja mpango au hoja inayotolewa na mmoja wa vijana wake hasa katika kazi zao.

Kamanda Amata alimpanda sana Madam S hasa kwa umakini wake wa kazi, na maamuzi yenye majibu chanya siku zote, hakuwa mtu wa dharau ila alithamini hata tone la maji ya vua lidondokalo kutoka juu ya paa, alikuwa mwanamke wa chuma, aliyepitia mihangaiko, majanga, na mateso mengi katika kazi yake hiyo, alikuwa mtu mzima, weusi wa nywele wake ulikuwa ukimezwa na weupe. Lakini ukali na umakini wa macho yake bado uling’aa daima, alikuwa na kipaji cha kujua unalotaka kusema kabla hujafungua kinywa chako.

Alikuwa na IQ ya hali ya juu sana, aliaminiwa sana kwa usiri wa mambo na ndiyo ilikuwa nidhamu ya kazi yao, yupo tayari hata umkate kichwa lakini hawezi kukwambia chochote ambacho hataki wewe ukijue. Idara ya ujasusi ilipoanzishwa na Rais wa awamu ya kwanza hasa wakati wa lile sakata la hujuma ambalo mwanausalama namba moja aliyekuwa akifanya kazi kwa siri sana na Mwalimu Nyerere, The Chamelleone kama alivyojiita kwa kificho alipopendekeza kuanzishwa idara hiyo, hakuna mtu aliyefaa kuiongoza zaidi ya mwanamke huyu, na mpaka sasa ilikuwa ngumu kwake kustahafu kwa jinsi alivyoaminiwa.

Ni idara ya siri sana ambayo kazi zake hufanywa kimya kimya lakini kwa umakini wa hali ya juu sana. Kila aliyefanya kazi katika idara hii alikuwa na utambulisho wake mbele ya jamii, tofauti na kazi yenyewe, hivyo ilikuwa ngumu kutambulikana kiurahisi, isipokuwa na watu wachache hasa wale walioko katika baraza la usalama la Taifa. Madam S alishastahafu kazi katika ofisi yake ya awali ya Usalama wa Taifa, na inajulikana hivyo. Lakini kumbe alihamishwa ofisi kwa siri na sasa alijulikana kama msatahafu isipokuwa tu huitwa kwa shughuli maalum ikibidi kuwa wazi.

Ukiachana nay eye, vijana wake wote walikuwa na shughuli mbalimbali za kufanya zinzowakutanisha na jamii kila siku. Chiba, yeye alikuwa ni mwalimu wa kukodi katika idara ya Teknohama pale chuo kikuu cha Dar es salaam, wakati Kamanda Amata alikuwa akimiliki ofisi ya kufaulisha mizigo ya AGI Investiment akiwa na Gina kama katibu muhtasi wake. Dr Jasmine daima alipatikana Muhimbili kama daktari bingwa mpasuaji lakini pia alifanya kazi sana katika kitengo cha magonjwa ya akili ‘Psychiatric department’.

Scoba, kama anavyojulikana alikuwa ni dereva Tax na wengi walimjua kwa hilo, Tax yake aina ya Toyota Carina iliyochoka kidogo, ilikuwa ikiegeshwa karibu kabisa na jengo la wizara ya Elimu ambao ni mitaa miwili tu unafika ofisi ya Madam S, ofisi maalum ya kusaidia Wazee hasa wale wanaofuatilia madai yao ya mafao ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Usiku wa saa sita na dakika arobaini na sita, watu wote hawa sita walikuwa wamewasili katika ofisi ndogo, ofisi ya Madam S, kwanza kila mmoja alikuwa anapata Kahawa ili kuchangamsha akili yake.

KIKAO CHA USIKU USIKU…

Usiku wa saa sita na dakika arobaini na sita, watu wote hawa sita walikuwa wamewasili katika ofisi ndogo, ofisi ya Madam S, kwanza kila mmoja alikuwa anapata Kahawa ili kuchangamsha akili yake.

“Kiukweli hii ni kali ya mwaka, tangu nimeanza kazi hii sijawahi kupambana na janga kama hili,” Madam S alaianzisha mazungumzo, kila mmoja alimuunga mkono.

“Ee maana wengione huwa wanaiba mapesa kiufisadi lakini huyu safari hii kaamua kuchukua almasi kabisa na ndege ya serikali,” akadakia Dr. Jasmin.

“Katumiwa, kwa vyovyote vile, hakuna Mtanzania mwenye ujasiri kama huo endapo hakuna nguvu kubwa nyuma yake,” Scoba akaongeza.

“Ok, sasa tupo hapa kwa ajili ya kupanga mpango kazi, lazima hii kesi kesho asubuhi kwenye saa nne hivi tuwe tumepata mwanga Fulani maana kutakuwa na kikao cha Baraza la Usalama la Taifa saa tano ya asubuhi,” Madam S aliongea huku akijiweka katika kiti chake na wengine wote walikuwa tayari wakijiweka sawa, kusikiliza, hawakutakiwa kuandika popote ili walitakiwa kila kinachoongelewa kikae kichwani kwa kuwa ni siri, “Chiba!” akaita.

“Kuna nini kwenye hiyo chip?” akamwuliza.

“Bado, nilikuwa nahangaika nayo hapa, inaonekana imefungwa kwa namba ambazo mpaka nijue kombineshen yake ni kazi kubwa, lakini kabla ya hiyo saa nne kesho nakuhakikishia nitakuwa nimetegua kitendawili hata ikibidi niende America kwa kazi hii nitakwenda,” akajibu na wote wakacheka hasa kwa sentensi ya mwisho.

“Mpaka muda huo Madam, tutakuwa tumepata ufumbuzi,” Kamanda akamalizia.

“Ok, sasa nataka tufanye kazi katika mtindo wa pembetatu, siku zote mfumo wa pembetatu huwa unaleta mafanikio haraka sana,” Madam akawaambia. Wote wakatingisha vishwa juu-chini kuashiria wako pamoja na mkuu wao, “Mkuu wa nchi kachanganyikiwa, haelewi kipi ni kipi, na hapa ni sisi tu tunaotegemewa, make mkijua polisi na wapelelezi wao, nao wanafanya upelelezi juu ya hili lakini sisi tupo mbele zaidi, sasa nimefakiria tufanye hivi, Chiba na Kamanda Amata mtakuwa shamba hakikisheni mnafungua hiyo chip na pia mnachambua taarifa zote za hao watu tuliopewa majina yao na Mheshimiwa Katibu, hakikisheni mnajua mpaka saa ngapi huwa wanaenda haja, hiyo ni pembe ya kwanza. Gina na Dr Jasmine mtaondoka hapa usiku huu kwenda Shinyanga, moja, nataka Dr. Jasmine ukafanyie uchunguzi maiti ya Mc Lean na Boharia wake, ujue silaha iliyotumika kuwaua ili tufananishe na silaha anayomiliki Mheshimiwa Waziri ili tuanze kuoanisha mambo, muda unakimbia, tatu, Gina, kazi yako ni kuhakikisha usalama wa Dr. Jasmin, kunusa kila hatari inayozunguka na kuishughulikia, ukihitaji msaada unanitaarifu mara moja, hiyo ni pembe ya pili.

Scoba utakuwa bega kwa bega na marubani wa jeshi ambao wanakusubiri muondoke, mkaitafute hiyo ndege pande hizo za Mwanza mpaka Uganda, wakati huo meli ya jeshi kikosi cha maji pale Mwanza nayo itakuwa kwenye doria, hiyo ni pembea ya tatu. Nafikiri tumeelewana, kuna swali?”

Ukimya ukatawala kati ya wote, majukumu waliyopewa yalikuwa yanajieleza kabisa, hakuna ambaye hakuelewa kilichosemwa na Madam. Kila mtu akajipapasa kiunoni mwake, na kujikuta yuko vizuri, bastola na kashkash nyingine zilikuwa mahala pake. Gina alikuwa bado kamtumbulia macho Madam S.

“Gina, vipi mbona unashangaa?” kamanda akauliza.

“Kazi niliyopewa, du! Mi nilijuwa ama Kamanda awe na mimi au awe na Dr. Jasmine, sasa wanawake tupu tutafanikiwa kweli endapo kutatokea ambush?” Gina akauliza.

“Gina, ingekuwa mwanamke hawezi kitu, Ikulu isingenipa hiki kitengo nyeti, na mimi ninsingekuteua wewe kukupa TSA 5. Kumbuka wewe na Amata mna taaluma moja, na taaluma yenu inatakiwa kila upande, sijataka ubaki hapa, nimetaka uende Shinyanga nina maana yangu, huo ni mtihani wako wa kwanza, mi nazeeka, nikistahafu au nikifa hii nafasi haina mtu zaidi ya Kamanda Amata je nani atashika kitengo cha Kamanda kama si wewe? Nimemaliza, wote mtawanyike.

Usiku huo kila mtu aliondoka na kuingia katika jukumu alilopewa, Gina na Dr. Jasmine walifuatana mpaka Uwanja wa ndege ambapo Gina na Dr. Jasmine walipata ndege ya kukodi kuelekea Shinyanga na Scoba aliingia Uwanja wa Jeshi ‘Air wing’ wa kikosi namba 603. Kamanda Amata, Chiba na Madam S walielekea Shamba.

SHINYANGA saa 8:15 usiku

Ndege ndogo ya kukodi ilitua katika uwanja mdogo wa ndege wa Shinyanga, Gina na Dr. Jasmine waliteremka na kuingia kwenye jengo la wageni.

“Karibuni sana,” wakakaribishwa na mwanadada aliyevalia nadhifu kabisa, alionekana wazi kuwa ni mfanyakazi wa hapo, wakakamilisha itifaki zote za uwanjani hapo ikiwa pamoja na kufanyiwa ukaguzi kisha wakaingia kwenye tax iliyoitwa na mwanadada huyo, wakaondoka zao.

Moja kwa moja usiku huo, walifika katika hospitali ya mkoa ya Shinyanga, wakaonana na mhudumu wa chumba cha maiti aliyekuwa zamu.

“Ndiyo sijui niwasaidie nini?” aliwauliza, Dr. Jasmine alikuwa amesimama jirani kabisa na yule Mhudumu ilhali Gina alikuwa nyuma kama hatua tano hivi akichezea simu yake.

“Nahitaji kuuona mwili wa Mc Lean na Mr. Ngosha waliouwa Mwadui sasa hivi,” Jasmin akajibu.

“We ni nani?” yule Mhudumu akauliza.

“Mimi ni Daktari wa jeshi la polisi, nimetumwa kutoka Makao makuu Dar es salaam,” akamwonesha kitambulisho. Yule Mhudumu akanywea, akampa ishara ya kumfuata, akamfungulia mlango mkubwa wa kuingia ndani ya chumba hicho. Hakikuwa kikubwa sana, kulikuwa na jokofu lenye uwezo wa kuhifadi miili ishirini tu, hivyo mingine ilikuwa imehifadiwa kwenye vitanda vya chuma.

“Huu hapa ni wa Mc Lean,” alimuonesha Dr. Jasmine, “Na huu huku wa Mr. Ngosha,” akamwambia.

“Ok, sasa kokota hivyo vitanda, lete kwenye chumba cha uchunguzi, bila shaka ni hiki sivyo?” Jasmine akauliza. Yule Mhudumu akajibu kwa kichwa.

Dakika mbili baadae ile miili yote miwili ikawa ndani ya chumba kile alichokuwa Jasmine. Akavali gloves zake na kuweka vizuri mask na ile miwani kubwa inayomkinga macho, kisha akajivika joho la kijani na kuanza kazi yake.

“Sasa wewe kaendelee na kazi yako nyingine, hapo nje nimemweka mtu, naomba asiingie huku mtu yeyote nafanya kazi hii kwa dakika ishirini tu, sawa?” akamwambia Mhudumu.

“Sawa,” yule Mhudumu akajibu bila taabu.

MWANZA saa 8:50 usiku

Helkopta ya jeshi ilikuwa ikipita katika anga la Mwanza kuelekea ziwani, ikiwa katika msako wa kuityafuta ndege ya serikali iliyopotea mchana wa siku iliyopita baada ya kutumiwa katika wozi wa almasi.

Katika ziwa Victoria kulikuwa na meli ya jeshi nayo ikitalii hapa na pale, wakitumia vyombo mbalimbali kutazama kama wanaweza kuona chochote kinachohusiana na ndge hiyo. Mawasiliano kati ya wale waliokuwa katika ndege na hawa walioko melini yaliunganishwa moja kwa moja na wale walio katika rada ya jeshi kule Ngelengele mkoani Morogoro.

“Elekea upande wa Magharibi nyuzi 121, shuka chini mpaka attitude 100,” yalikuwa maelekezo kutoka kwa wale walioko Ngelengele. Scoba na yule Rubani wa Jeshi waliiteremsha ile chopa kama walivyoelekezwa, hakika mtu aliyewaelekeza hakukosea hata kidogo, kwani walivyokuwa wakizunguka walikuwa wakiona kitu kisichoeleweka katikati ya misitu ndani ya Uganda kilomita chache sana kutoka ziwani.

“Kuna kitu tunachokiona katikati ya msitu, tuna wasiwasi nacho kama ni ndege kutokana na kinavyong’aa kwa mbalamwezi,” Scoba alitoa taarifa.

“Ok, Ok, nenda chini zaidi ili uone kwa ufasaha,” wakapewa maelekezo, “Kama kuna uwezekano wa kutua basi tueni kabisa.”

Ile chopa ilipita karibu kabisa na kuhakikisha ni ndege iliyotua katika barabara finyu sana.

“Yeah, ni ndege ya serikali, tumeiona vizuri kabisa,” walitoa taarifa na kisha kurudi Mwanza, hawakuweza kutua eneo lile kwakuwa hawakuwa na uhakika wa usalama katika eneo hilo, wangeweza kushambuliwa kama adui alikuwa kawawekea mtego. Scuba alikumbuka maneno ya Chiba, alipowaambia kwenye kikao kuwa wote wawe na tahadhari kwani adui kwa vyovyote atakuwa amejua anatafutwa baada tu ya kuondoa ile chip ya mawasiliano kutoka kwenye saa ya Katibu wa Wizara.

Taarifa zilifika mara moja kwa Madam S, kwani ndani ya jumba lao huko Gezaulole, Shamba, waliweza kunasa mawasiliano yote yaliyokuwa baina ya ile helkopta, meli na mtaalam wa anga huko Ngelengele. Alikurupuka kitandani na kuwafata Kamanda Amata na Chiba waliokuwa katika chumba maalum cha kompyuta na kuwapa taarifa.

Ilikuwa ni furaha kwa wote.

SHAMBA saa 8:30 usiku

“Ehne, na ninyi mmefikia wapi katika uchunguzi wenu?” Madam alimwuliza Kamanda Amata.

“Aaaah, majibu sio mabaya, hawa Watanzania waliofuatana na Waziri taarifa zao hazina mashaka sana, ila hawa Wazungu wane ndio bado ninachimba zaidi,” Kamanda alijibu.

“Mpaka ulipofikia…” Madama alisema

“Mpaka nilipofikia kuna huyu Bwana Mark Steuben, tajiri mkubwa sana huko Uingereza, anafanya biashara ya madini na mataifa mbalimbali duniani, ana kampuni kubwa iitwayo Cunglia Cold Mines, ambayo ofisi zake zipo katika mji mdogo wa Cunglia, katikati ya Uingereza. Labda anaweza kumshawishi mtu yeyote kufanya wizi kama ule kwa kumpa pesa nyingi sana.” Kamanda akajibu.

“Ok,” Madam S akaitikia huku akitikisa kichwa chake.

“Halafu kuna huyu Bwana Dregen. Amewakilisha kampuni moja ya kuuza madini iliyoko huko Canada katika jiji la Ontario, nimejaribu kuingia kwa unnndani zaidi way eye na kampuni yenyewe, kampuni ya Robinson Dia-Gold LTD. Kampuni hii ipo Ontario, na inamilikiwa na tajiri mkubwa wa huko Canada anaitwa Bwana Robinson Quebec,” akamlizia hapo.

“Very Good Kamanda, umeona hao wote wana makampuni ya madini kwa hiyo kuna uwezekano wa kushawishi wizi huo au kufanya wizi huo, yote yana wezekana, endelea kuchambua zaidi, anagalia na wigo wa marafiki zao kibiashara duniani kote na Afrika ili tuona kama kuna muungano na popote panapoweza kutupa jibu,” Madam alitoa maelekezo.

Kamanda Amata akamuonesha alama ya dole gumba.

“Chiba nipe ripoti,” akamgeukia Chiba aliyekuwa bize na kompyuta zake.

“Nimefanikiwa kufungua codes zilizowekwa, ila kazi ilikuwa ngumu sana, lakini hakuna cha maana sana isipokuwa chip hii ilikuwa inahifadhi kumbukumbu kwa njia ya sauti kutoka pande wa Mheshimiwa na kuzituma kwa hawa jamaa, sasa hapa ninachotaka kufanya ili tujue ilikuwa inapeleka wapi hasa, na nani alikuwa anazipokea, inabidi tuiunganishe tena, halafu ndio nijaribu kuona codes zake zinavyooana hapo tutajua upande gani na wapi inatuma taarifa, itakuwa rahisi kumpata mtu wetu au watu wetu,” Chiba alieleza kitaalamu kabisa.

“Ok, kama vipi fanya hivyo asubuhi, sijui utaipataje ile saa ya yule mzee na muda wote iko mkononi,” Madam S alionesha mashaka.

“Usijali, mimi ndio Chiba, huwa sishindwi kitu, nitaiunganisha hapahapa kwa kutumia vifaa vyangu na ninauhakika itafanya kazi.”

“All the best,” madam alimaliza na kutoka.

§§§§§

Dr. Jasmin alimaliza kazi yake, ile miili ikarudishwa mahala pake, akavua maguo aliyokuwa amevaa na kuyaweka vizuri kwenye mfuko wa plastiki, kisha kwenye mkoba wake, akatoka akifuatana na yule Mhudumu, nje walimkuta Gina akiwa anazungukazunguka huku na huko, akampaigia mruzi, Gina akarudi mara moja.

“Asante sana,” akamshukuru yule Mhudumu na kumpa noti ya Sh 10,000 za Kitanzania.

“Vipi, kuna lolote?” akamwuliza Gina.

“Nina wasiwasi, kuna gari imepita hapa kama mara mbili, imezunguko huku, ndio nilikuwa naitazama nijue inashughuli gani,” Gina alijibu ok.

“Vipi, umepata lolote?” Gina akamwuliza.

“Yeah, nimepata majibu yenye utata kabisa, lakini hata hivyo…” akasita kidogo, akampa Ishara Gina ya kutazama kwenye ua kubwa lililofanya kichaka cha kuogofya, Gina akageuka kwa chati na kuona kivuli cha mtu aliyetulia kama mti mkavu sambamba na mti wenyewe, akajiweka tayari kiakili na kimwili. “Tutaongea baadae,” Dr. Jasmine akamwambia Gina huku wakiharakisha kulifuata lango la hospitali hiyo.

Hakukuwa na mtu kwenye vijia vya hospitali hiyo, isipokuwa manesi na madaktari waliokuwa wakipishana usiku huo kwa kazi mbalimbali. Gina alitazama nyuma na kuona watu wawili waliokuwa wakiwafuata taratibu ambao waliachana kama mita mbili katikati yao. Mbele yao kulikuwa na mtu mwingine aliyevalia kidaktari, Gina akili yake ikafanya kazi kwa haraka zaidi, mwili wake ukasisimka, akaiona hatari hiyo, akamgonga Jasmine kwa kiwiko, “Una bastola?” akamwuliza.

“Ndiyo!” akajibu.

“Iweke tayari, funga kiwambo kwa siri, pale mbele kuna korido mbili wewe nenda kushoto mimi niende kulia tuona watagawanyika vipi kisha tuwashambulie, hakuna kubakisha kitu, muda mbaya huu,” Gina alimwambia Jasmine ambaye aliitikia kwa kichwa. Dr Jasmine akatoa bastola yake kwa chati ndani ya mkoba wake huku mkono ukifunikwa na koti lake la kidaktari, alipoishika sawia, akaliweka juu koti lake la kidaktari hivyo hakuna aliyeona kama ana bastola mkononi mwake. Wale watu bado walikuwa wakiwafuata kwa nyuma.

Mara wakafika kwenye zile pacha za korido ambapo korido nyingine ilikatisha na kufanya alama ya jumlisha, Dr Jasmine akakunja kushoto na Gina akakunja kulia, kila mmoja akashika njia yake. Wale watu wawili walipofika pale, wakagawana njia mmoja kushoto na mwingine kulia, yule daktari naye alikunja upande wa Jasmine. Gina aliona tukio zima, alipofika mbela kidogo akasimama akajifanya anaweka kiatu chake vizuri….

Yule mtu aliyekuja upande wa Gina akamkaribi huku mkono wake ukijishika kiunoni, alikuwa akitoa bastola, amechelewa, Gina alirusha teke moja kali la nyuma na kiatu alichovaa chenya kisigino kirefu kikamtoboa sehemu Fulani ya tumbo, Gina akarudi wima, wakati yule mtu akijishika tumbo, tayari Gina alikuwa hewani akamtandika mateke mawili yaliyompeleka chini, yule mtu akajiinua haraka ili akabiliane na Gina, Gina aliona upande wa Jasimine, yule aliyevaa kidaktari akigeuka tayari na bastola mkononi kumlipua Gina.

Gina kwa haraka, alimkamata adui yake na kumuweka kati kisha akajirusha upande wa pili na ile risasi ikamfumua vibaya yule mtu akabwagwa chini kama kiroba.

Dr. Jasmine, alisimama ghafla, na yule kijana akamwekea bastola mgongoni.

“Tembea hivyohivyo ongoza mpaka garini,” alimwamuru. Jasmine hakuonesha upinzani, akatembea lakini hatua tatu aliposikia ile sauti ya bastola ya yule aliyevaa kidaktari, akatumia nafasi hiyohiyo, aligeuka ghafla na kuupiga mkono wa yule kijana kwa mkoba wake, bastola ikaanguka chini, yule mtu alijirusha kuiokota, ikapigwa teke na kwenda upande wa pili, kabla hajainuka, yule mtu alishtukia teke kali la usoni, hakuna alichokiona zaidi ya nyota nyota. Akiwa katika hali hiyo, Dr. Jasmine alijiandaa kumpa shambulizi la pili, akachelewa, konde moja kali likatua sahavuni na kumpepesua Jasmi mpaka kwenye ukingo wa korido, wakati huo yule aliyevaa kidaktari alikuwa na bastola mkononi akimjia Jasmine kwa haraka, kabla hajafika, paji la uso wake likafumuka, risasi ya Gina iliyotoka upande wa nyuma ikafanya vitu vyake. Gina akakimbia na kujirusha hewani miguu yake miwili ikatua katika mgongo wa yule mtu mmoja aliyempiga konde Jasmine, akamsukuma na kujigongaq kwenye ukuta wa wodi, Gina akamfikia na kumkamata ukosi wa shati, akamdidimiza bastola kinywani mwake.

“Sema, nani bosi wenu? Nani kawatuma?” Gina akauliza.

“Si- si-mjui…” akajibu kwa kigugumizi huku macho yamemtoka.

“Sitaki kupoteza muda, sema haraka,” Gina akang’aka huku midomo ikimtetemeka, akatoa ile bastola kinywani mwa yule mtu na kuifyatua, akampiga gotini na kufumua mifupa.

“Aaaaaa, aaaaaa unaniua mimi! Iiiiiiii, mama weeee, ona damu sasa zinatoka,” yule mtu alilia kama mtoto.

“Utasema au husemi?” Gina aliuliza tena.

“Nasema, nasema, usiniue tena…”

“Haya sema,” Gina alimwamrisha

“Tumetumwa na Don Swa…” kabla hajamaliza kusema alitoa macho kama mjusi kabanwa na mlango.

“Ambushhhhhhh!!!!!” Dr. Jasmine alipiga kelele, Gina akamwachia yule mtu na kuruka kinyumenyume akatua kwenye pipa la taka, akaanguka nalo, Dr. Jasmine akamshika mkono wakainuka na kutimua mbio, walijirusha kwa pamoja na kupenye dirishani wakaingia katika wodi ya watoto, wakatimua mbio na kutokea mlango wa nyuma.

“Wazingile wazingile,” sauti ilisikika.

“Watatokea huku, we pita kule,” mwingine aliamuru.

“Kwani kuna nini jamani?” Muuguzi mmoja aliuliza baada ya kuona watu asiowajua wakiingia wodini mwake.

“Kuna majambazi wawili wa kike tunawasaka, sisi ni polisi, mmewaona wameelekea wapi?” akauliza.

“Wamepita pale kwenye hako kamlango kadogo,” mgonjwa mmoja akaropoka, msinambe.

Gina na Jasmine, wakatulia tuli ndani ya chumba cha kubadilishia nguo wauguzi. Yule mtu aliyepewa maelekezo, akatembea kwa hadhari kubwa kuingia katika kile chumba, akasukuma mlango kwa mtutu wa SMG aliyoidhibiti mikononi mwake, ukimya ukamlaki, zaidi ya ukimya huo ni nguo tu zilizokuwa zikining’inia. Dr. Jasmine akatoka akiwa amevaa vazi lake la kidaktari, stethoscope yake shingoni, mikono mfukoni. Alipoukariia mlango akakutana uso kwa uso na mtutu wa bunduki.

“We vipi huku na libunduki lako?” akamwuuliza.

“Tunatafuta majambazi wawili wa kike,” yule bwana akajieleza.

“Sasa majambazi ndio wakimbilie wodini, si watakamatwa tu, hakuna mtu huko,” Dr. Jasmine akajibu, huku akipishana na yule mtu, akakiendea kitanda kimojawapo chenye mgonjwa aliyewekewa drip, akamwangalia, “Unaendeleaje?” akamwuliza.

“Naendelea vizuri,” akamjibu. Wakati anaongea na huyo mgonjwa alikuwa akimwangalia kwa chati yule mtu ambaye alitoka ndani ya chumba kile, na kuondoka zake.

§§§§§

“Wagonjwa na wafanyakazi hawatoi ushirikiano, twendeni zetu kabla wakuda hawajafika, lakini hakikisheni mianya yote ya kutokea nje ya hospitali hii inabanwa, wasitoke humu leo wala kesho,” yule mtu aliwaeleza wenzake huku akikwea Land Cruiser lenye rangi za polisi na namba za usajili za serikali. Wakaondoka zao.

Walipofika nje wakateremka na ile gari ikaondoka peke yake.

“Wewe, wewe na wewe mtasubiri hapa mlango mkuu, nyie wawili, kuna mlango wa pale pembeni mkaweke ulinzi wa siri, na nyie wawili kule nyuma, sawa?” akawapa majukumu.

“Sawa Kiongozi.”

“Mkiwaona wanajitokeza, signal yetu ni ileile,” alipomaliza kuwaelekeaza akatokomea kizani. Utulivu ulirejea katika pembe za hospitali ile, maana wagonjwa wengine walipona baada ya kusikia milio ya risasi, watu walizagaa ikiwamo wagonjwa na wauguzi, walinzi nao walikuwa pale. Waliisitiri miili ya waliokufa kwa kuifunika na kuiacha hapo kungoja itifaki za kipolisi.

§§§§§

Simu ya Kamanda Amata ikaita, simu pekee ambayo ikiita lazima kuna jambo, akaichukua na kuifyatua kisha akaweka sikioni.

“…Kamanda, tupo msambweni, tumeshaangusha watatu na hapa tumezingirwa, lakini hatujui watu hawa ni polisi au vipi, kwani wamefika na gari ya polisi…” Gina aliongea kwa kunong’ona.

“Oh, poleni sana, mko salama?” Kamanda akauliza.

“…Tuko salama,”

“Kazi ya ofisi mmemaliza?” akauliza.

“…Ndiyo tumemaliza… hawa watu hawajaondoka, wanatusubiri nje kwa vyovyote… msaada please…” Gina akakta simu.

Kamanda Amata akampa taarifa hiyo Madam S.

“Shiit, kumbe adui tunae humuhumu! Ina maana ni polisi wanaotumwa kutekeleza haya, basi nimeelewa, hapa una mikono ya watu, sasa unawasaidiaje na unajua wazi kuwa fimbo ya mbali…” Madam akang’aka.

“Tulia Madam, nishapata wazo,” Kamanda akajibu kisha akaiendea simu ya mezani, akazungusha tarakimu kadhaa, akasubiria.

“…Hello, Central Police Station hapa, tukusaidie nini?…” sauti ya WP iliijibu simu hiyo kutoka kituo kikuu cha Shinyanga.

“Kuna mauaji pale hospitali ya mkoa wa Shinyanga, naomba amkashughulikie,” kisha Kamanda akakata simu, akairudisha mahala pake na kuinua ile ya mfukoni, “Fanyeni kila mnaloweza mtoke haraka, nimewataarifu polisi,” akamwambia Gina.

§§§§§

Gina na Dr. Jasmine wakatoka haraka na kutembea harakaharaka mpaka kwenye maegesho maalumu ya gari za hospitali, wakaikuta ambulance imeegeshwa pale, dereva alikuwa amesinzia ndani, wakamgongea wakaingia.

“Vipi?” akauliza kwa mgutuko.

“Polisi,” Gina akamjibu na kumuonesha kitambulisho cha polisi, “Sasa sikia, tutoe hapa na gari yako kama unavyopeleka mgonjwa Muhimbili, kisha we tuache uwanja wa ndege urudi, mtu yeyo akikuuliza baadae mwambie ni polisi walikuchukua, haya haraka.”

Yule dereva hakuwa na hiana akaliwasha na kuwasha kimwerumweru kule juu na kulitoa mahala pake, alifunguliwa lango kuu na kutoka kisha akaongeza kasi kuelekea Uwanja wa ndege.

4

SCOBA akiwa na vijana wa jeshi la Wananchi waliozingira vichaka ambapo ndege ya serikali ya Tanzania ilionekana kutua, kilomita chache ndani ya mpaka wa Uganda. Ilikuwa ni kwenye barabara ndogo ambayo hata hawakuijua ilitokea wapi na kwenda wapi, hakukuwa na tatizo lolote, pori lilikuwa salama kabisa. baada ya kuhakikisha usalama huo, walivuta hatua huku wenzao wenye mitutu wakiwa wamelala kimya nyasini tayari kutoa ulinzi kama kuna lolote baya, Scoba aliufungua mlango wa ndege ulioonekana haukufungwa sawasawa, akatumia periscope kuangalia ndani, kulikuwa na watu waliokuwa wamelala vitini, shaghalabaghala, akaingia, pamoja na wale wapiganaji wa JW.

Walikagua kila mtu bila kumshika ili wasipoteze ushahidi wa alama za vidole. Kulikuwa na abiria kumi na moja, abiria wane hawakuwepo kadiri ya hesabu waliyopewa na Katibu wa Wizara.

Scuba na wale maofisa wa jeshi walikagua vizuri mpaka kwenye chumba cha marubani na kuwakuta wote wakiwa kwenye usingizi mzito, Scoba alianza kujisikia kizunguzungu na kichwa chake kuwa kizito, akawapa ishara wale maofisa kutoka nje ya ndege hiyo haraka.

“Kuna dawa kali ya usingizi,” akawaeleza wenzake mara baada ya kunywa maji mengi na kunawa mengine.

SAA 4: 15 asubuhi.

MWANZA-Hospitali ya Sekou Toure

KATIKA wodi ya watu maalumu (V.I.P) walikuwa wamelazwa watu kumi na nne, abiria kumi na moja na marubani watatu waliotolewa kwenye ndege ile na kufikishwa hapo kwa helkopta za jeshi la Tanzania.

Madam S na timu yake walikuwa wamejificha kwenye moja ya vyumba vinavyotumika kama ofisi kwenye hospitali hiyo. Aliwatazama kwa zamu mmoja baada ya mwingine, “Hongereni kwa kazi,” akamtazama Gina, “Safi sana mkamwana, umekomaa sasa, sikutegemea kama kutakuwa na hali hiyo pale Shinyanga, lakini umefanya vema, sio mbaya,” akamsifia.

“Wakati tunamsubiri Dr. Jasmine atupatia majibu ya hao watu huko, yujadili jambo, kwa nini Waziri afanya yote haya? Kwa manufaa ya nani,” Madam S akaanzisha mazungumzo.

“Hapana nikioanisha matukio, sidhani kama Mheshimiwa Waziri kafanya haya, hawa jamaa ni wataalam, swali dogo Madam, wamepataje gari la polisi kuwavamia hawa akina Jasmine, fikiria, gari iliyokuja kuleta askari pale Shinyanga na ile iliyokuja kwanza ni ileile na pale kituoni wanasema haikutoka, hawa ni Wataalam tunapambana na wajuzi, naamini sasa Waziri kafichwa mahala Fulani,” Kamanda akajibu.

“Chiba, alama za vidole kutoka kwenye ndege zinaleta majibu gani?” Madam akauliza.

“Hakuna majibu Madam, inaonekana watu hawa walijipanga kwani walivaa gloves,” Chiba alieleza.

Madam S akatikisa kichwa kana kwamba kaingiwa na mdudu sikioni, “Hivi ile ndege mmeikagua vizuri kweli?” akauliza.

“Wanasema wameikagua kila kona,” akajibu Scoba.

“Ok, ngoja waamke hawa ndio watatupatia habari nzima na kuanzia hapo sasa tutajua mbivu na mbichi, Kamanda Amata kazi yangu ya jana ulifikia wapi?” Madam akaendelea kukusanya maelezo na kuyameza kichwani mwake.

“Kuhusu Robinson Dia-Gold LTD?”

“Yeah!”

“Kuna kitu kimenisumbua kidogo, na lazima tukiangalie kwa makini na mapana kama kina uhusiano wowote na hili,” Kamnanda alianza.

“Enhe!” Madam akajiweka tayari na kila mtu akatega sikio.

“Nimejaribu kupitia mambo mengi juu ya kampuni na mmiliki wake, kati ya ambayo nimeyawekea alama ni hili lifuatalo, tajiri wa Robinsoni Dia-Gold LTD alikuwa na rafiki mkubwa wa kibiashara na muuza madini mkubwa huko Afrika Kusini aliyekuwa anamiliki kampuni ya The Great Khumalo Mines, na huyu Khumalo alikuwa na hisa nyingi katika kampuni ya Robinson, na katika kuendelea kusoma taarifa hizo ni kuwa huyu Khumalo aliuawa miaka miwili iliyopita, sikuona umaana wa mauaji hayo hata kama watu hao walikuwa marafiki, lakini sasa tarehe ya mauaji ilikuwa bado siku nne kampuni ya Robinson agawe faida za wenye hisa, na kama ingekuwa hivyo basi Khumalo angepata pesa nyingi sana kiasi kwamba kampunin hiyo ya Robinson ingetikisika kiuchumi, hapa nina wasiwasi, je si Robinson aliyetekeleza mauaji haya?” Kamanda akatulia.

Wote ndani ya chumba hicho wakabaki kimya hakuna aliyeongea, mara mlango ukasukumwa na Dr. Jasmine akaingia akiwa katika mavazi ya kawaida.

“Ndio Jasmine, lete habari sasa,” Madam alimdaka.

“Yah, Madam, baada ya kufanya uchunguzi wa kitabibu kupitia damu za wahanga, nimegundua kuwa watu wale wote walipewa dawa aina ya Mandrax, kwa kiwango kikubwa sana kiasi kwamba hadi kuamka itachukua si chini ya masaa kumi na mbili yajayo,” akatulia.

“Itawezekanaje, walispray?” akauliza Madam.

“No!” Scoba akadakia, “Sasa Napata picha, ile ndege tumekuta Oxygen Mask zote zimefunguka, ina maana waliunganisha na njia ya hewa kisha wakakasitisha mzunguko wa hewa ya kawaida, kiasi kwamba Rubani lazima afungue zile mask kuwasaidia abiria wake, hivyo ni rahisi wote kuivuta kwa mara moja,” akamaliza.

Madam S akatikisa kichwa kuashiria ameelewa.

“Madam, sasa unaamini kuwa tunaopambana nao wamajipanga kiasi gani, kwa sababu mpaka hawa watu wa kutupa sisi mwanga waamke, adui yetu atakuwa amefika Mars,”…

“Usemalo ni kweli kabisa, Dr. Jasmin vipi hakuna vjia yoyote ya kuwafanya waamke mapema?” Madam S akauliza.

“Hapana, ni vizuri tuwangoje waamke wenyewe pia kwa usalama wa afya zao,” akajibu Jasmine.

“Ok, turudi kwenye hoja yetu, Kamanda Amata,” Madam akaendeleza mjadala.

“Nilikuwa nahitaji mawazo yenu kama mnaona kuna uzito katika mauji ya Khumalo na hisa za kampuni ya Robinson,” akaendelea Amata.

“Tena kumbuka kumbukumbu zinaonesaha kuwa Khumalo amekoswakoswa kuuawa mara kadhaa, si mara moja, kwa mujibu wa mtandao wake ambao mpaka sasa haujafungwa bado,” Chiba aliongezea.

Madam S aliendelea kuwasikiliza vijana wake walivyokuwa wakitiririsha maelezo.

“Nimewaelewa vyema, sasa naona kuna muunganiko katika mauaji ya Khumalo na huyu mtu anayejiita Robinson sasa tunaunganisha vipi na tukio hili?” akauliza.

“Madam, simple tu, kwenye ndege kulikuwa na mtu ambaye alikuwa anaiwakilisha kampuni ya Robinson Cold Mines, hivyo inawezekana Robinson kafanya uharamia huu ama kwa kushirikiana na Waziri au kwa hujuma yoyote maana anaonekana ni mtu wa mbinu sana, hivyo hatoshindwa kufanay kama wale Waisrael waliokuja Uganda na kuwaokoa ndugu zao waliotekwa na Idd Amin, wakiwa na sare za UPDF, ndege ya Uganda, muda waliofika ni uleule ambao Idd Amin alitakiwa kufika pale, nani alijua kama wale ni Waisrael?” Gina akaongeza neno.

Ukimya ukatawala.

§§§§§

Watu Fulani wawili walikuwa wameketi katika chumba kilichojengwa chini ya ardhi katika moja ya nyumba za kifahari huko Mwanza, Pasiansi, muda wote walikuwa kimya hakuna aliongea na mwingine, katikati yao kulikuwa na chombo kidogo kama redio, kilichounganishwa na na kompyuta ndogo kabisa, chombo hicho kilikuwa kikitoa sauti ya watu waliokuwa wakiongea kwenye kikao Fulani. Watu hao walikuwa ama wakitabasamu au wakiongea kwa simu zao maalum kutoa taarifa kwa watu wao juu ya mpango unaopangwa na wale walio kikaoni. Mara hii mmoja akamtazama mwenzake na kumsemesha.

“Vipi hapo? Tumefanikiwa, bado?” akamwuliza yule mwingine

“Fifty Fifty kaka” akajibu yule mwingine.

“Yaani huyu fala wao anayejifanya anajua sana maswala ya kompyuta, ningemuona ana akili kama angeichoma moto hiyo chip lakini kuendelea kuihifadhi akijua kwamba haifanyi kazi kwa kuitoa kwenye ile saa, imekula kwake, tena sasa ndio tunapata data za kutosha za jinsi wanavyojipanga,” Mwingine akajibu.

“Lakini mi nawaogopa hawa jamaa, mpaka wamegundua juu ya Khumalo, Robinson ina maana wapo hatua chache sana kutufikia, huyo mtu wa kompyuta sio mjinga, lazima kuna kitu anafanya, hivyo hapa tuwe na tahadari kubwa ikiwezekana tuondoke zetu kwani kuendelea kuwa hapa kunaweza kutuletea tabu,” yule wa pili akaongeza na mwenzake akatikisa kichwa kuafiki.

“Ok mpe ripoti Boss!” akamwambia mwenzake ambaye alichukua simu yenye anenna ndefu na kuanza kuongea na mtu wa upande wa pili.

“Ok, anasema tuhamishe makazi, maana yake tuondoke sasa, mpaka mambo yakitulia, tuje kufanya awamu ya pili, lakini kwa hili labda yule mtu wetu atashtuka,” akaongea yule aliyekuwa na simu, kisha wakasubiri kidogo kabla ya kuzima hako kajimtambo kao.

§§§§§

Wakati mazungumzo yakiendelea kati ya Madam S na watu wake, mara kompyuta ndogo ya Chiba ikachora aina flani ya mistari kuwa kuna mawimbi yanakatwa, akaigeukia na kuacha mjadala ule kisha akaanza kubofyabofya hapa na pale ili kujua ni vipi, alikuwa anatabasamu wakati akafanya hilo.

“Kamanda!” akaita, Kamanda Amata naye akaungana naye. Chiba akanakili namba Fulani zilizoonekana katika kompyuta yake na kisha akaingiza kwenye software nyingine, ramani ya ulimwengu ikajionesha dhahiri, akaendelea kucheza na namba zile kujaribu kuoanisha na vipimo halisi vya ardhi. Wakati huo wote walikuwa wamemzunguka Chiba kuangalia nini anafanya.

Chiba akageuka na kukuta kazungukwa, “Pasiansi kitalu namba 164 au 165 au 166 au 167 moja wapo,” akasema.

“Kuna nini?” Madam akauliza.

“Hapo ndipo mawasiliano yetu yanapotua,” akaeleza wakati akaisimama na kuchukua bastola yake akaiweka sawa na kuipachika kiunoni, Kamanda Amata akafanya hivyo, Gina nae akaunga.

Wakatoka wote na kuteremka ngazi kisha wakachukua gari ndogo yenye vyoo vyeusi wakaingia, Scoba akakamata usukani, wakapotea mtaani.

“Kama wasingezima huo mtambo wao, nisingeweza kuwagundua walipo,” Chiba alieleza.

“Ina maana watakuwa wanajipanga kuondoka hao, kwa nini wazime?” kamanda akauliza.

“Unajua, inaonekana walikuwa wakiendelea kunasa mazungumzo yetu, sasa kama wamesikia hatua ambayo tumefikia, hata ningekuwa mimi ningefunga virago na kuondoka haraka,” Chiba akaongeza kusema.

“Madam, hawa watu wasikimbie, zuia ndege zote kuruka pale Mwanza Airport,” kamanda akatoa rai.

“Dah! Umenena,” Madam S, akainua simu yake na kupiga kwa Meneja wa Uwanja wa ndege kuomba ndege hata moja isiruke.

Muda si mrefu walifika mtaa wa Pasiansi, wakatafuta namba hizo na kuona nyumba nne zenye namba hizo zilizofuatana. Wakateremka kwenye gari yao, Madam S akaelekea dukani na kununua kinywaji lakini hapo alipo alihakikishwa ana uwezo wa kuziona nyumba zote hizo. Kisha Chiba, Kamanda na Gina wakatawanyika ilhali Scoba alikuwa akiendesha taratibu gari yake kati ya nyumba hizo.

Nyumba ya kwanza, ilikuwa nyumba ya kawaida kulikuwa na wapangaji tu, mwenye nyumba hakuwapo hapo.

Nyumba ya pili kulikuwa na familia moja inayoishi, ilikuwa nyumba ya kawaida tu. Nyumba ya tatu ilikuwa ni nyumba kubwa ya kisasa yenye kila kinachohitajika katika nyumba, bustani kubwa yenye bembea na maua ya kuvutia ilikuwa, na mfanyakazi tu aliyeonekana kumwagilia maji bustani hiyo ya kuvutia.

Gina akalijongelea geti na kubonyeza kengele, yule mfanyakazi akasogea.

“Nikusaidie nini dada?” akauliza kwa lafudhi ya Kisukuma.

“Namuulizia mwenye nyumba, yupo?” akauliza.

“Mwenye nyumba? Mi tangu nianze kazi hapa sijawahi kumuona mwenyenyumba, ni wageni tu wanaokuja na kuondoka,” akajibu.

“Fungua mlango,” Gina akaamuru.

“Sasa uwende wapi? Hakuna mtu humo ndani,” akasema huku akifungua geti na Gina akapita ndani.

Kamanda Amata akaiweka bastola yake vizuri, akaipachika miwani yake usoni akitazama pale mlangoni ambako Gina aliingia na kuielekea nyumba hiyo. Scoba akainua bunduki kubwa aina ya AK 47 iliyofungwa lensi yenye nguvu na kupachika dirishani, akaitazamisha kule kunako lile jumba, huku akichungulia taratibu kutazama kama kuna mtu yeyote ambaye ataleta tabu ili amfumue bila huruma.

“Usiende huko, hakuna mtu dada,” yule mfanyakazi akamwambia Gina. Wakati huohuo Kamanda Amata akaingia pale getini akasimama akitazama. Gina akaukaribia mlango mkubwa wa jumba hilo, Kamanda Amata akamtazama yule mfanyakazi ambaye aliuacha ule mpira wa maji na kuliendea bomba ambalo ameliunganisha na ule mpira wa maji, akaacha kumtazama Gina na kumfuata yule mfanyakazi taratibu.

Yule mfanyakazi akalififikia bomba na kufunga maji, wakati huo huo Kamanda Amata akasikia kama mtu akipiga kelele na mara kimya ghafla, akageuka nyuma hakumuona Gina.

“Gina, Gina, Ginaaaa!!!” akaita kwa nguvu, na muda huo huo Madam S na Chiba walijitoma katika uwa huo.

“Vipi?” Chiba akauliza akiwa na bastola mkononi.

“Gina amepotea ghafla,” Kamanda akajibu. Wakati akigeuka kutazama kule bombani alimshuhudia yule mfanyakazi akianguka vibaya kwenye wigo wa jumba hilo. Akamkimbilia, alikuwa anavuja damu, mguu wake umevunjwa kwa risasi mbaya kabisa.

“Ulikuwa unakimbia ee? Haya nieleze, umefanya nini?” Kamanda akauliza huku akiwa kamkanyaga kwenye jeraha lake, “Husemi? We sugu sio? Ujue sicheki na mtu sasa?” Kamanda Amata aliushika mguu wa yule mfanyakazi na kuuzungusha vibaya.

“Aaaaaaa niache, nasema…” akapiga kelele

“Sema, yule mwanamke yuko wapi?”

“Kuzimu, kaingia kuzimu!” akajibu.

“Kuzimu ndio wapi?

“Kuzimu, kuzimu? Kwani we hukujui Kuzimu?” akamwuliza Amata. Kamanda akaunyonga kwa nguvu ule mguu.

“Aaaaaaaaaaaiiiiiiiigggggghhhhhhh!!!!!” mifupa ya mguu ilitawanyika vibaya.

“Na wenye nyumba wako wapi?” Kamanda akauliza.

“Hii nyumba ya wageni, wameondoka,” akajibu.

“Wameenda wapi?”

“Sijui, walikuwa hapa wiki mbili kaini leo wameondoka,” akazidi kutoa maelezo.

“Ok, wametoka saa ngapi na wamesema wabakwenda wapi?” Kamanda akazidi kuhoji

“Mi sijui kaka, niache basi,”

“Nioneshe, Kuzimu ni wapi?” akambana. Yule kijana akiwa na maumivu makali akamwonesha mkono kwenye bomba alilokuwa akitumia kuunganisha mpira wa maji. Kamanda Amata akamwacha na kuliendea lile bomba.

“Hey, go to hell,” yule mfanyakazi akampigia kelele Amata. Kamanda alipogeuka nyuma alijikuta akitazamana na domo la Revolver, iliyokuwa imeshikwa barabara mkononi mwa yule kijana, ubaridi ukamteremka Kamanda kuanzia utosini mpaka unyanyoni. Paji lake la uso lilitengeneza makwinyanzi ya hasira, “Niue kama una shabaha!” akasema. Yule kijana akatoa usala wa ile bastola tayari kumlipua Kamnda, hakuwa na masihara hata kidogo.

ONTARIO-CANADA

JOPO la watu watatu lilikuwa limekutana tena kwa siri, ndani ya chumba chao cha mikutano kilicho chini ya ardhi lakini chenye kila kitu ambacho mwanadamu atakihitaji, walitazamana na kujikuta wote wapo.

“Karibuni tena,” alisema yule aliyeonekana kama kiongozi wa kikao kila mara, “Haya semeni kwa kifupi, kikao chetu ni dakika tisa tu na tano za mwisho ni kufanya maamuzi.”

Mmoja wao ambaye alikuwa mweusi, yaani Mwafrika lakini sijui ni wan chi gani alianza, “Tumeweza kupata mzigo, lakini ile nchi ni hatari sana, sasa hivi msako mkali unafanyika na baadhi ya vibaraka tuliowaweka wamekwishapoteza maisha, nina wasiwasi na sisi kujulikana, over,” alimaliza kuongea, na hakutakiwa kuongea tena.

“Taarifa nilizozipata kutoka katika mtambo wetu ulioko huko Afrika Mashariki ni kuwa idara ya kijasusi ya Tanzania imeingia kazini kufanya uchunguzi wa sakata hili, kama wangefanya polisi wa kawaida hakika nisingekuwa na wasiwasi, lakini idara yao ya ujasusi ni hatari sana ni bora utafutwe na CIA watachelewa kukupata lakini TSA ni hatari sana, over!” mtu wa pili akasema na kisha kunyamaza kimya kwani muda wake ulikwisha.

Yule kiongozi wao, akashusha pumzi ndefu na kuwatazama watu wake, “Hatutakiwi kuwa na mashaka, tunajua ni nini tunachofanya, huu ni mkataba na mkataba lazima ufanyike kadiri ya makubaliano yaliyomo ndani, sasa tupo kwenye kurasa zizlizofungwa kwa pini za dhahabu, kama hatoshtuka, tukimaliza hizo tutafika kurasa ya mwisho ambayo ni kummaliza yeye mwenyewe.” Akatulia kidogo na kuwatazama upya kisha akasema, “Lakini sasa hapa kuna kazi mpya inaingia na ni lazima tuishughulikie kabla ya kutekeleza mpango wa pili wa kurasa zenye pini ya dhahabu, nendeni tukutane hapa baada ya masaa kumi na nne tujue tunafanya nini,” akamaliza.

Wote wakatawanyika…

Wote wakatawanyuka na kutawanyika, katika kikao hicho hakuna aliyetakiwa kuhoji chochote isipokuwa kuitikia na kuongeza wazo tu

Mwanza

GINA ALIJIKUTA AKIDONDOKA KATIKA CHIMO au chumba kidogo chenye ukubwa wa mita moja nanusu ya mraba. Alianguka juu ya vitu vigumu, alijisikia maumivu sana, akajaribu kunyanyuka akipapasa huku na huko, giza lilitawala. Miguuni mwake alikuwa akihisi kama mikono ya watu ikimshika miguu mara kwa mara, wakati mwingine akahisi anakanyaga kitu kama nazi lakini hakuweza kuona chochote kutokana na giza nene ndani ya shimo lile. Akaingiza mkono mfukoni mwake kutafuta simu, akaitoa, akawasha tochi na kumulika ndani ya shimo hilo. Lo! Gina alishtuka sana akabaki katumbua macho! Mifupa ya watu ilijazana ndani ya chumba hicho kidogo, vitu alivyoviona kama nazi vilikuwa ni mafuvu ya binadamu. Akatetemeka kwa hofu, alihisi kama amefika kuzimu.

“Shiit!” akang’aka, huku akitetemeka sana, akainua simu yake na kubonya namba za Kamanda Amata, akaweka sikioni, hakuna kitu. Simu hiyo haikuita kabisa alipoichunguza akakuta ikimuonesha hakuna mtandao eneo hilo. Akachanganyikiwa, akatazama kwa kumulika kuta za shimo au chumba hicho, zilikuwa kuta laini sana zisizo na hata mkwaruzo, zilikuwa zimewekwa marumaru, harufu ya uvundo ilikuwa imetawala ndani yake. Hakujua afanye nini. Nitafia humu? Akajiuliza akikata tama.


Madam S na Chiba walikuwa ndani ya jumba hilo, kila mmoja bastola mkononi wakikagua chumba kimoja baada ya kingine. Kila chumba walichopita kilikuwa tupu, ni vitanda na vitu vingine tu.

“Chiba, nilinde,” Madam akamwambia Chiba kisha akaibana bastola yake kwenye kiuno cha suruali aliyovaa, akaanza kufungua kabati moja moja, kila moja lilikuwa tupu, zaidi ya mataulo na mashuka hakukuwa na jipya. Akatoka na kuingia chumba kingine, nako vivyo hivyo, akapita vyumba kama vinne hivi. Akiwa katika ujia mdogo wa kuelekea maliwato, akauona mlango mwingine pembeni, Chiba akiwa nyuma yake na bastola mkononi iliyokamatwa kwa mikono miwili tayari kutii amri yoyote itakayoamuriwa alikua nyuma ya Madam S akitazama kila kona kwa makini.

Katika masikio yao wote walikuwa wamepachika vifaa maalumu vilivyowafanya kuweza kuwasiliana muda wote, hivyo walikuwa wakisikia mahojiano ya Amata na yule kijana huko nje. Mlango ulio mbele ya Madam S ulikuwa umefungwa, aliutikisa tena na tena lakini ulifungwa kabisa, akaichomoa bastola yake na kukifumua kitasa, ukaachia, ndani kulikuwa ni kama stoo, vikolokolo vya ufundi na vitu mbalimbali vililundikana, akaishusha bastola yake na kuiweka tena kiunoni, akavuta hatua moja na kufika mlangoni, akasita kuingia, akatanguliza mkono aone kama kuna hatari yoyote ambayo ingemshambulia. Ghafla vitu kama misumari vilifyatuka kwenye pande mbili za yale mashelf na kutawanyika kila kona.

“Aaaaaaiiigghhh Shiiit!” Madam alilalamika maumivu pale msumari mmoja ulipotoboa kiganja cha mkono wake.

“Madam!!” Chiba akaita. Madam S akamuoneshea ishara ya mkono kuwa abaki pale pale na vilevile. Madam S akachomoa kale kamsumari mkononi mwake, kisha akatoa kitambaa chake cha shingoni na kujifunga kiganjani akidhibiti damu kutotoka kwa wingi. Alipohakikisha yuko sawa, akafanya tena mtindo uleule, akatanguliza mkono ndani ya chuma kile, hakukutokea chochote. Chumba hicho kilitegwa silaha maalumu ambapo mtu yeyote asiye rafiki na nyumba hiyo akiingia angeshambuliwa na bomu la misumari lakini kama ni mwenyeji anajua nini cha kufanya kwanza. Madam S akaingia na kutazama yale mashelfu yalivyojipanga. Hakugusa kitu, alikuwa akitazama tu, baadae akaanza kugusa na kutikisa hapa na pale, mahala fulani chini ya moja ya mashelfu hayo kulikuwa na kipande cha marumaru ambacho kilitofautiana ua moja na vingine. Si rahisi kwa mtu wa kawaida kugundua tofauri hiyo, akakikanyaga na mara shelf moja lililombele yake likasogea pembeni taratibu na kuacha mlango mmoja uliofungwa. Akashika kitasa na kukinyonga, ule mlango badala ya kufunguka ukafyatuka kwa juu na kuwa kama unaoanguka kwenda ndani taratibu, mbele yake kulibaki na uwazi ambao ni sawa na chumba kidogo, akasita kuingia.


Kamanda Amata alitulia palepale akipanga cha kufanya, hakuweza kugeuka kwani alijua wazi kuwa kwa kugeuka kwake basi kijana huyo angefyatua bastola yake.

“Ua!” akatamka. Yule kijana hakuelewa, wakati akishangaa, alijikuta akitupwa nyuma na kujibamiza kwenye nguzo ya umeme, akaanguka chini, marehemu, risasi ya Scoba ilifanya vitu vyake. Kamanda Amata akaliendea lile bomba na kutazama koki yake, ndipo alipogundua kuwa katikati ya koki kuna swichi ndogo ya rangi ya bronze, akajaribu kubonyeza na kuishika bila kuachia.

Mbele ya mlango wa kuingia nyuma kubwa pakafunguka, na shimo la urefu wa futi nane likawa wazi, ndani yake, mifupa, mafuvu na mabaki ya binadamu yalijazana, Gina alikuwa ndani yake.

“Kamandaaaa!!!” akaita. Kamanda akasikia sauti ya Gina, akamwita Scoba na kumwambia atazame humo ndani. Scoba akatoka garini na bunduki yake mkononi mpaka pale akachungulia ndani akamuona Gina. Scoba akatazama huku na kule, akaenda pembeni na kuchukua bomba la chuma lililolazwa pembeni, akaja nalo na kuweka katikati ya ile milango ya lile tundu, akaizuia isijifunge.

“Achia Kamanda,” akamwambia Amata ambaye bado alikuwa kaishikilia ile swichi, ile milango ikarudi lakini ilizuiwa na lile bomba. Scoba akakimbia garini na kutoa kamba ngumu ya kuvutia gari, akarudi na kwa pamoja na Amata wakatumbukiza huku kipande wakishika wao.

“Gina, Shika kamba hiyo,” Scoba akamwambia Gina kisha wakaanza kumvuta juu mpaka walipomtoa, lo!

“Hawa watu ni wakatili sana, ina maana ni watu wangapi wamefia kwenye shimo hili?” akauliza Kamanda.

“Na serikali haijui lolote, mnasikia tu mtu kapotea lakini hamumwoni tena,” Scoba akajisemea kwa sauti ya chini, hii lazima ifanyiwe kazi.

“Gina unajisikiaje?” Kamanda akamwuliza.

“Mwili unauma maana niliangukia juu mifupa, lakini niko poa,” akajibu. Akaitazama simu yake sasa ilimuonesha kuwa mtandao unapatikana.

“Vipi? Mbona washangaa?” Kamanda akamwuliza Gina.

“Nashangaa kule chini simu yangu ilikata mtandao lakini hapa inasoma,” Gina akaeleza.

“Lazima wafanye hivyo kwani bila hivyo hapa pangejulikana kitambo sana,” Kamanda akajibu, “Ok, Gina na Scoba wekeni ulinzi nje hakikisha watu wanakaa mbali na eneo hili, mi naenda ndani kuwasaidia Madam na Chiba,” akatoa maelekzo.

Timu nzima ya TSA ilikuwa katika eneo la jengo hilo, hii ilikuwa ni mara ya kwanza watu hawa hatari wa serikali ya Tanzania kuwapo katika kazi moja, hii ilimaanisha kazi ilikuwa nzito na haikutaka lelemama.

Ndani ya jumba lile Madam S alikuwa ameteremka chini kabisa ya jengo na wakati huohuo Amata aliungana nao.

“Usalama!” Kamanda akatamka.

“Usalama!” Chiba akajibu, bila hivyo ilikuwa ni rahisi kwa Chiba kufyatua risasi yake.

“Nje kwema vipi humu?”

“Utata mwingi Kamanda,” Chiba akajibu.

“Ok, shuka kwa Madam mi naweka ulinzi wenu,” akamwambia Chiba, na wakati huo Chiba akashusha bastola yake na kuiweka kiunoni, akateremka ngazi kwenye ule mlango na kuungana na Madam kule chini. Huko chini Madam S alifika katika chumba kimoja kilichojengwa chini ya ardhi, kilikuwa ni chumba chenye mitambo mingi ya kielektroniki, Chiba naye akafika.

“Hapa ndipo walipokuwa wakinasa mawasiliano yetu,” akamwambia Madam.

Kisha wakatzama huku na kule kwenye vyumba vingine, chumba kimoja wakakuta kimefungwa.

“Chiba, vunja mlango!” Madam akamwamuru. Chiba aliruka teke moja kali kwa miguu miwili akauvunja mlango na kubaki wazi. Hawakuamini wanachokiona.

“Mheshimiwa!!!” Madam alang’aka na kuingia haraka ndani ya kile chumba, kisha Chiba akafuata.

Alikuwa Waziri wa Nishati na Madini, amefungwa katika kiti, usingizi mzito ulikuwa umempitia, Madam S akatazama huku na kule akamgusa hapa na pale.

“Haraka hospitali,” akamwambia Chiba, wakamwita Kamanda akateremka haraka, kwa kushirikiana walimtoa mahala pale na kumbeba mpaka juu.

“Scoba, ita polisi, waambie wafike hapa haraka sana,” Madam akatoa amri. Mwili wa Waziri ukapandishwa mpaka kwenye sebule kubwa, Madam S akapiga simu kwa Dr. Jasmin na kumwamuru afike haraka.

Dakika tano baadae, tayari vijana wa FFU wenye silaha za kutosha walifika na kutawanyika kuazunguka nyumba nzima, alkadhalika RPC wa Mwanza alifika kujionea hali halisi, wakati huo tayari Madam S na vijana wake washaingia garini, Mheshimiwa akapakiwa kwenye gari la wagonjwa na Dr. Jasmin alikuwa akimpa huduma ya kwanza, wakaondoka mahala pale.


ITAENDELEA

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Tatu

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment