Jiue Mwenyewe Sehemu ya Tatu
KIJASUSI

Ep 03: Jiue Mwenyewe

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Tatu

IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE


Simulizi : Jiue Mwenyewe

Sehemu Ya Tatu (3)

Hali ya hewa ilikuwa imetulia kabisa katika Uwanja wa ndege wa Mwanza, abiria walioahirishiwa safari kwa muda walikuwa wamechoka kusubiri wakimlalamikia Meneja wa Uwanja kuwa kwa nini hawapi sababu ya kucheleweshewa safari zao. Wenye viherehere walikuwa washafika ofisini kwa Meneja huyo na kuanza kuchonga midomo yao.

“Kwa nini mnatufanyia hivyo jamani, nusu saa sasa imepita,” mmoja alilalama.

“Kama mmeshindwa kazi semeni bwana sio mnakuwa wababaishaji tu,” mwingine akadakia huku akirusha mikono yake juu huku na huko.

“Yaani nchi hii bwana, kila kitu wanachukulia kawaida tu,” sauti upande wa pili wa abirai ikasikika.

Meneja wa Uwanja kwa kutumia kipaza sauti cha matangazo akawatangazia watu ili kuwashusha presha.

“Mtusamehe ndugu abiria, kusimamaishwa kwa safari hatujaamua sisi wenyewe, hii ni amri ya serikali haina swali wala jibu ni matekelezo tu.”

Muda huo huo gari moja nyeusi ikasimama maegeshoni mwa uwanja huo. Madam S akifuatana na Kamanda Amata wakateremka na kutembea harakaharaka kuelekea katika ofisi ya Meneja huyo, wakamkuta ofisini huku askari wa polisi wakiwa mlangoni.

“Mnaenda wapi?” wale polisi wakawauliza.

“Tuna shida na Meneja,” Madam akajibu.

“Hamuwezi kumuona kwa sasa, ana kazi nyingi,” yule polisi akajibu.

“We! Usinipotezee muda, hujui unaongea na nani sawa?” Madam akaongea kwa hasira wakati huohuo Kamanda Amata alikwishafungua mlango na kuingia ndani, walimkuta Meneja kajiinamia.

“Oh, karibuni sana,” yule Meneja akawakaribisha mara baada ya kujitambulisha kwake, “Sasa tangu mliposema kuwa tuzuie ndege yoyote isiondoke tumefanya hivyo na mpaka sasa ndege zote nne zilizokuwa ziruke ndani ya saa mbili hizi bado zipo na abiria wake kama unavyowaona almanusura wanitoe macho ndiyo maana nimeweka polisi hapo mlangoni,” akaeleza.

“Ok, sasa ni hivi, kuna watu tunaowatafuta, lakini hatujui hata sura zao wala majina yao, kwa hiyo tutafanya gwaride la utambuzi sasa kwa abiria wote,” Madam akaeleza.

Dakika tano baadae, abiria wote 130 waliokuwa uwanjani hapo walipangwa na kutakiwa kuingia katika ofisi ya Meneja mmoja baada ya mwingine kisha kuelekea kwenye ndege zao. Zoezi lilichukua saa nzima, mahojiano makali ya kujua wapi unatoka, unakwenda na unafanya nini yalichukua nafasi lakini hayakuzaa matunda.

“Hapa hakuna mhalifu, wote wanaonekana raia wema tu,” Kamanda akasema, “Je; kuna ndege nyingine yoyote iliyoondoka kabla ya hizi?” akauliza.

“Ndiyo ipo ndege ya kukodi ya shirika la Darair , imeruka saa moja kabla hamjapiga simu,” meneja akajibu.

“Ilikuwa na abiria wangapi?”

“Imeondoka na abiria watatu tu, wawili wanaume na mmoja mwanamke,wote ni raia wa kigeni,” Meneja akaeleza.

“Ok, kama inawezekana nahitaji kujua taarifa zao kutoka kwa wakala wa kampuni hiyo zaidi ya hapo naomba uruhusu watu waondoke maana wamenuna wasije kupasuka,” Kamanda akaongea na kuchomekea utani kidogo ili kumfanya Meneja huyo asiogope sana.


Mikononi mwa Kamanda Amata na Madam S kulikuwa na picha sita za watu watatu, kila mmoja alitolewa nakala mbili za picha yake.

“Stephen Peterson, raia wa Norway, mfanyabiashara za madini, umri miaka 32, anaishi Texas Marekani, yupo nchini kwa wiki moja,” Kamanda Amata akamaliza kusoma, akaiweka pembeni taarifa hiyo, akachukua nyingine.

“Richard Clouch, mwandishi wa habari wa gazeti la Mirror la Uingereza, anaandika habari za Biashara na Uchumi naye alikuwa nchini kwa wiki moja anishi Manchester ana miaka 30,” akaiweka pembeni na kuchukua ya yule mwanamke, akaitazama mara mbili mbili.

“Jesca Jenny ana miaka 29, raia wa Honolulu, Mtalii, alikuwa nchini kwa wiki moja,” hii kidogo ilimvutia Kamanda Amata hasa ukizingatia jinsi watu hawa wenye taaluma tofauti kuwa pamoja. Alivutiwa zaidi na mwanamke huyu, akaitazama ile picha ya yule kwa umakini wa hali ya juu.

“Umesema wanaondoka na ndege gani?” akamwuliza mhudumu wa ofisi hiyo.

“Kwa taarifa za tiketi zao, wanaondoka na KLM leo saa sita usiku, wameelekea Dar es salaam sasa,” akajibu.

Kamanda Amata akamtazama Madam S, akamwona jinsi sura yake sasa ilivyoanza kuupoteza usichana na kuingiwa na uzee wa ghafla, “Mama, ni sawa?” akamwuliza.

“Si sawa hata kidogo,” akamgeukia yule mhudumu, “Ndege yenu iliyowasafirisha hawa watu imeshatua Dar es salaam?” akatupa swali.

“Ndiyo imetua nusu saa ilopita,” akajibu.

“Ok, asante sana, usihofu, tatizo ni kuwa hawa watu walikuwa nchini na kufanya kazi tofauti na vibali vyao ndio maana tunawafuatilia,” Kamanda akamweleza yule binti kisha wakaagana.

HOSPITALI YA SEKOU TOURE

JASMINE, ALITULIA KITINI mbele yake akiwa na jopo zima la TSA, akainua bilauri yake yenye Tusker baridi akapiga mafunda matatu ya nguvu kisha akashusha pumzi ya kuridhika.

“Mheshimiwa vipi?” Kamanda akauliza.

“Ataamka muda si mrefu, kwani walimchoma sindano mbaya ya usingizi, lakini dawa waliyoitumia inambadala wake hivyo tumemchoma sindano nyingine ambayo itamzimua na kumwamsha mara moja,” akajibu Dr. Jasmine.

“Good,” akajibu Madam na kujiegemeza kwenye kiti hicho cha chuma, mara akakumbuka kitu, akajiweka sawa, “Jasmine, maana tumekuwa na mengi sana, hebu nambie kule Shinyanga mlipata nini?”

“Aaah, nilifanya uchunguzi wa miili kama ulivyoagiza, lakini kuna utata kidogo kwani maiti ya Mc Lean inaonekana na jeraha jembaba la bunduki ya kisasa inayotumiwa na majasusi wengi duniani ambayo haitoi sauti na ni ndogo pia sio rahisi mtu kuitambua kuwa ni bunduki, huwa inavaliwa kama saa ya mkono, na mtumiaji akikunja ngumi kisha kuirudisha chini, bunduki hiyo hujifyatua kwani trigger yake iko chini na ufyatua kwa kukandamizwa,” akawaeleza.

Madam akahifadhi hayo yote kichwani mwake. Akamtazama Kamanda Amata, “Niambie!”

“Sasa naanza kuingiwa na wasiwasi kama ni kweli Mheshimiwa waziri kafanya uhalifu huu, lakini pia labda wamemzunguka kama alishirikiana nao, ngoja aamke,” Kamanda akaeleza. Mara mlango ukagongwa, Dr. Jasmine akafungua, alikuwa muuguzi mmoja aliyekuja kumwita Daktari huyo, wakatoka haraka haraka na muuguzi yule.

Dakika kumi baadae Jasmine alirudi nakuleta habari njema, Mheshimiwa kaamka. Madam S na vijana wake waliinuka na wote wakaelekea kumwona Mheshimiwa huyo.

Chumba kipana cha V.I.P kilichokuwa na kila kitu ndani, kitanda kizuri, vinywaji vya kutosha na kila kitu, Kamanda alikitazama chumba hicho mwanzo mpaka mwisho. Ingekuwa Watanzania wote wanatibiwa hivyo wasingeogopa kifo, Kamnda akawaza.

Mheshimiwa Waziri alikuwa ameketi kwa msaada wa kitanda hicho, akiwatazama waliokuwa mbele yake, mara moja akamtambua Madam S.

Wakati huo wote Madam S alikuwa anajaribu kutazama hali ya Waziri huyo, kama ni ya woga, kutetemeka au kuna tofauti yoyote ile ambayo itamfanya amgundue kuwa ni mualifu.

Dr. Jasmine aliwaomba wasiohusika wapishe kwanza ili wafanye kazi yao. Sasa chumba kilibaki na watu saba tu.

“Pole sana Mkuu,” Madam alimpa pole.

“Asante sana, watu wabaya sana jamani,” akasema kwa sauti ya tabu kidogo.

“Unajua kuwa una kesi ya kujibu?” Madam akamuuliza.

“Kesi! kesi gani?” Mheshimiwa Waziri akajibu kwa kuuliza akionekana kushangaa kwa hilo. Madam S aliuliza makusudi tu ili kuona atalipokea vipi swala hilo.

“Unatakiwa Dar es salaam sasa hivi! Ukajibu tuhuma zako mbele ya Rais na kisha utapandishwa kizimbani,” Madam akamwambia bila kucheka.

DAR ES SALAAM

MADAM S NA KIKOSI CHAKE WALIKUWA wamekutana Shamba kama kawaida yao wanapokuwa na hoja nzito za kutafutia ufumbuzi, safari hii walikuwa na Mheshimiwa Waziri waliyemleta hapo kwa siri, taarifa za kupatikana kwake zilibanwa, hakuna chombo cha habari wala taasisi yoyote iliyoruhusiwa kutoa habari hiyo. Mheshimiwa Waziri alikuwa akipata kahawa huku akiendelea na matibabu chini ya Daktari Jasmine. Baada ya kuwa kapata nafuu na anaweza kuongea vizuri, akawekwa kwenye chumba maalum cha mazungumzo kilichokuwa na meza moja na viti vitatu tu, lakini upande wa pili Chiba alikuwa kwenye mitambo akisikiliza kila kitu ambacho waziri huyo alitakiwa kuzungumzia tuhuma hizo. Walikuwa wakisubiriwa watu watatu muhimu katika jumba hilo ‘Shamba’.

Dakika tano baadae, gari maalumu ya idara ya TSA iliyokuwa ikiendeshwa na Scoba ilikuwa ikiingia kupitia mlango wa nyuma wa jengo hilo kongwe maeneo ya Gezaulole, iliingia na kuegeshwa ndani kabisa mwa egesho la siri. Rais, Makamu wake na Waziri mkuu waliteremka, wakapokelewa na Madam S na Gina, wakakaribishwa ndani na kupitishwa moja kwa moja mpaka kwenye chumba maalum walichoandaliwa. Mpaka wanafika hapo waheshimiwa hao hawakujua wako wapi kwani gari waliotumia kufika nayo hapo haikuwa ikionesha chochote kutoka ndani hivyo abiria hakujua ni wapi anapelekwa.

“Sasa hapa ni wapi?” Waziri mkuu akamuuliza Gina.

“Mheshimiwa hapa nimahali pasipojulikana na mtu, hata mimi mwenyewe sipajui,” kisha wote wakacheka.

Kila mtu alipokuwa tayari katika mahala pake, Madam S na Kamanda Amata wakaanzisha mazungumzo na mheshimiwa waziri. Waziri hakujua kama kuna ugeni mzito ndani ya jengo hilo.

“Tulitua na ndege katika uwanja mdogo wa North Mara majira ya saa tatu asubuhi, nikiwa na wageni wangu wote na ujumbe niliofuatana nao, tukiwa pale tulifanya kila tulichotakiwa kufanya, tulikagua mgodi katika vitengo muhimu, tukaongea na meneja na wafanyakazi baadhi kuwasikiliza kero zao na pia kujua ufanisi wa kazi zao…”

Kamanda Amata akakatisha, “…Nikukatishe Mheshimiwa, hebu niambie juu ya wageni wako waliofuatana nawe, unawajua kiasi gani hasa hawa wa kutoka nje,” akahoji.

“Yeah, wale jamaa mwanzoni niliwaona ni watu wenye nia nzuri ya uwekezaji kwa sababu mmoja alikuwa ni muwakilishi wa kampuni ya Robinson Dia-Gold Mines ya Canada, na mwingine ni kutoka Cunglia Cold Mines ya Uingereza kila upande walikuja wawili, na watu hawa nilikutana nao miezi sita iliyopita karika mkutano maalumu wa uwekezaji huko Geneva ambako nilikwenda nikifuatana na katibu wangu.”

Mheshimiwa Waziri alielezea mengi sana juu ya safari hiyo.

“Ok, Sasa unajua una kesi gani ya kujibu?” Kamanda akamwuliza.

“Hapana na ndio maana nashangaa, sijui kesi yoyote ninayotuhumiwa kama ipo,” waziri akajibu, Madam S na kamanda Amata wakatazamana. Kisha wakawasha TV ndogo na kumuonesha habari iliyorekodiwa kutoka TVT ikielezea wizi wa almasi na vifo vya watu wawili huku yeye waziri akituhumiwa. Hali ya mshangao na mshtuko ilionekana ghafla usoni mwake, akaanza kupumua kwa nguvu.

“Tulia Mheshimiwa, usihofu, hii ni habari iliyotokea ndani ya masaa sabini na mbili yaliyopita, na wewe ni mhusika,kabla ya kupandishwa kizimbani tukakuleta hapa kwanza ili tujue ukweli,” Madam akaeleza.

“Haya tuambie uko vipi na tuhuma hizi, kwa nini umefanya wizi huu wa mali ya wavuja jasho wa Tanzania,” Kamanda akapiga swali la moja kwa moja.

“Hapana, hapana, sihusiki, nashangaa imekuwaje, unajua kilichotokea, mnajua mimi sikuwepo duniani kwa muda mpaka nimejikuta pale Mwanza hospitalini.”

“Haya, tuambie, nini unakumbuka cha mwisho katika safari yako?” Kamanda akauliza, “Naomba usiwadanganye Watanzania, kwa kuwa wewe umeiba na inafahamika hivyo,” Kamanda akamalizia.

“Hapana unajua nini, mnajua kilichotokea? Sasa naanza kuelewa, sasa naelewa, naelewa, tulipokuwa angani wakati tukitoka Mara kwenda Mwadui, tulikumbwa na hali mbaya ya hewa, (akatulia kidogo) kisha tukatangaziwa na rubani kutumia barakoa za oksijeni, basi, basi, hapana sikumbuki kingine, kweli, mi sijaiba, sihusiki…” Mheshimiwa alikuwa kama anaweweseka, hali hiyo ilijionesha wazi, Madam S akatikisa kichwa.

“Mheshimiwa,” akaita, “Mheshimiwa!” akaita tena, ukimya ukatawala, Dr. Jasmine akaingia haraka na mtungi wa kusaidia kupumua (Oxygen Concetrator), akamwekea puani kumsaidia kupumua, kisha kwa msaada na Kamanda Amata wakamtoa kitini na kusaidiana kumbeba mpaka kwenye kitanda, Dr. Jasmine akafanya kazi ya ziada ya kumuwekea drip ya glucose, kisha akachukua vifaa vya kupimia presha (sphygmomanometer na stethoscope ), akaviunganisha na kuchukua vipimo, dakika moja na sekunde kadhaa, akaitoa masikioni ile Stethoscope na kulegeza ile mashine ya presha pale mkononi mwa Mheshimiwa.

“Presha imeshuka, muacheni apumzike kwanza,” Dr. Jasmine aliwaeleza.

Mheshimiwa Rais na makamu wake pamoja na waziri mkuu, walibaki wakitazamana.

“Nini hiki?” Rais akamuuliza Waziri Mkuu.

“Hapa kuna utata, tena utata mkubwa sana hapa mimi ni kama naangalia muvi au nasoma vitabu vya kina Willy Gamba au Joram Kiango, sielewi elewi tu,” Waziri Mkuu akajibu. Mara mlango ukafunguliwa, Madam S akaingia katika chumba hicho.

“Ndio Madam!” Rais akadakia.

“Kama hivyo Mkuu, lakini usijali, ukweli wote utaupata na taarifa itakuja Ikulu ndani ya masaa sabini na mbili kwani tuna watu kumi na nne wa kufanya nao mahojiano,” Madam akawatoa hofu.

“Nakuamini sana pamoja na vijana wako, naona jinsi mlivyojipanga, lakini hebu nipe maoni yako maana hapa nakosa cha kuwajibu Watanzania, nakosa cha kuongea na waandishi wa habari juu ya kadhia hii, Ikulu haikaliki,” Rais akamwambia Madam S.

“Hatuwezi kusema kahusika katika wizi au la, ila tutakapohoji wengine tutaoanisha mambo kisha tutajua kipi ni kipi na hapo sasa ndiyo tutaingia kazini kukamata waliohusika, hata wawe wanaishi Pluto au juani kote tutaenda, tupe muda Mheshimiwa Rais. Leo jioni tutakuwa na awamu ya pili ya mahojiano na watu wengine, tutajua mbichi na mbivu,” akamaliza.


Usiku huo tayari Kamanda Amata alikuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Nyerere akaijaribu kuona kama anaweza kuwakamata watu wake, alikuwa amezinasa picha zao kichwani. Aliegesha gari akateremka na kufunga mlango nyuma yake. Akiwa ndani ya suti nadhifu iliyoficha moja ya bastola zake anayoipenda sana, Kamanda Amata akatembea taratibu kuelekea ofisi ndogo ya KLM. Pale alimkuta mwanadada mrembo akiwa ametulia ofisini mbele akitazama kompyuta kubwa aliyokuwa akiitumia kutatulia matatizo yake kikazi. Akakaribishwa naye akakaribia, akavuta kiti akakaa.

“Naitwa George Kamasi,” akajitambulisha uongo kisha akampa kitambulisho yule mwanadada, akakipokea na kukisoma, kilimwelezea Kamanda Amata kama George Kamasi, mwajiriwa wa Wizara ya Mambo ya Ndani katika jeshi la Polisi kitengo cha uchunguzi wa makosa ya Jinai. Yule mwanadada akamrudishia, “Ehne bwana Kama… mh! Na hilo jina lako mpaka linatapisha,” akasema yule mwanadada.

“Uwe na adabu unapoongea na watu usiowajua,” Kamanda akapiga mkwara.

“Nikusaidie nini?” akauliza kwa utulivu baada ya kuona bastola iliyolazwa mezani kwa utulivu.

“Naomba unipe orodha ya wasafiri wako hasa wanaoelekea Uingereza, Canada na Honolulu,” Kamanda akaomba. Yule mwanadada akafanya harakaharaka kuitoa orodha hiyo kwenye mashine yake akaprinti na kumpa Kamanda Amata. Amata akaitazama haikumfurahisaha sana kwani Honolulu hakukuwa na abiria yoyote anayekwenda huko, Uingereza kulikuwa na abiria kumi na tano lakini wote walikuwa wanafunzi wa chuo kimojawapo cha huko ambao walikuja kwa utalii wa kimasomo na Canada kulikuwa na watu wawili, lakini wote wanawake. Akashusha pumzi. Ina maana wametucheza shere? Akajiuliza, akachukua zile karatasi na kuzikunja kisha akazitia katika mfuko wandani wa koti.

“Umeridhika?” yule mwanadada akauliza.

Kamanda Amata akamkazia jicho baya, “sijaridhika,” akamwambia.

“Sasa mimi nifanyeje ili uridhike?”

“Ulale na mimi leo,” Kamanda akamjibu bila kucheka.

“Ha ha ha ha huwa silali na wanaume ovyo ovyo, mi matawi ya juu nalala na Mapedeshee,” akajibu huku akinyanyuka.

“Hebu tulia hapo unaenda wapi? Unafikiri mi nimekuja kucheza hapa, akatoa karatasi nyingine na kumpatia, zilikuwa karatasi tatu, zenye picha za watu watatu tofauti.

“Hawa ni nani?” akauliza.

“Nataka uwatambue hao watu, kama wamekuja hapa kukata tiketi siku za nyuma, au unao katika ndege yako, hao ni majambazi wa Kimataifa na ukiwatetea leo unalala selo mwanamke jeuri,” Kamanda akazungumza kwa sauti kavu. Yule mwanadada akatazama zile picha, akachukua namba za tiketi zao na kuingiza kwenye mfumo wao wa kompyuta.

“Hamna watu kama hawa kwenye ndege yetu, kwanza tiketi zao ni feki, ona,” akamgeuzia kioo cha kompyuta, kisha akaongeza, “kama waliwaambia kuwa wanasafiri na ndege yetu leo, hatuna hawa abiria kaka.”

Kamanda Amata au Amata Ric akachukua zile karatasi zake na kurudisha kunakohusika. Akanyanyuka na kusimama wima.

“Ok, asante, na lile nililokwambia la kulala na mimi, tumeishia wapi?” Kamanda akachokoza.

“Heee! Hebu nitokee huko, we unafikiri mi wa kulalwa hovyo hovyo tu, nina watu wangu wenye pesa sio kama wewe unayetegemea kamshahara ka Wizara mwisho wa mweli, go fish,” akasema huku akimtazama Amata kwa jicho la dharau, mwisho akasonya.

“Ok, una maneno machafu wewe, ila ujue tu utaishia mikononi mwangu iwe kwa heri au kwa shari,” Kamanda akatoka na kuondoka.


“Yaani bila shaka yoyote tulitekwa, nakumbuka tukiwa tuko angani dakika thelathini baada ya kuruka kutoka Mara, hewa ndani ya ndege ilikuwa nzito sana, mzunguko wake ukawa hafifu, nilipotazama kwenye vipimo vyetu, vikaniashiria kuwa kuna shida katika mfumo wa oksijeni, hivyo sikuwa na budi ili kuokoa abiria wangu nikawaamuru kutumia hewa ya mtungi kwa kuvaa barakoa maalum kwa kazi hiyo, baada ya kuzivaa nikajikuta nashindwa kupumua sawasawa, kifua kinakuwa kizito, mwili unaishiwa nguvu, nikaitoa na kuitupa kando,” Rubani wa serikali aliyekuwa katika ndege ya msafara wa waziri alieleza kinagaubaga.

“Baada ya hapo uliona nini?” Madam akauliza.

“Baada ya hapo niliona kama kivuli cha mtu anayeingia ndani ya chumba cha rubani na kuwatoa wenzangu vitini, hapo sikuona tena kilichoendelea,” akajibu.

“Pole sana Kepteni. Kuna wizi mkubwa sana uliofanyika na ndege yako imetumiwa kubeba kasha tano za almasi zenye thamani ya Shilingi za Kitanzania Trillion moja kwa hesabu ya haraka haraka,” Madam akamweleza. Yule Rubani akashtuka na kupigwa na hamaniko, “Lo! Itakuwa walewale wazungu, maana hata kabla hatujaondoka walikuwa wadadisi sana, mara waniulize aina ya ndege ninayoirusha, mfumo wake ukoje, mara hiki mara kile, ah, mi nikawa nawapotezea tu,” akawaambia.

Baada ya saa moja ndani ya chumba hicho cha mahojiano alikuwamo mwanadada mmoja mrembo tu, aliyesuka nywele zake kwa mtindo wa rasta za Kimasai zilizomkaa vizuri, Madam S alimkaribisha kitini na kuketi katika mtindo wa kutazama. Madam S alimtazama mwanadada huyo kwa dakika tano bila kumsemesha neno, kisha akafungua kinywa chake.

“Umeolewa?” akamwuliza.

“Hapana,” naye akajibu kwa sauti ya unyonge.

“Una bwana au mchumba?”

“Ndio, nina mchumba tutafunga ndoa mwezi ujao,” akaeleza.

“Nieleze Historia yako kwa kifupi,” Madam alimwomba na yule dada akafanya hivyo.

“Kwani samahani mama, hapa ni wapi nafanya nini? Ni haki yangu kujua kama Mtanzania,” yule mwanadada akauliza.

“Ok, we ni Mtanzania mzuri unayejua unachotakiwa kujua, hapa ni Hospitali ya vichaa, wewe umeletwa hapa baada ya kukamatwa ukitembea bila nguo mitaani,” Madam akamweleza.

“What? Mimi?” akashtuka na kusimama.

“Ndiyo wewe, ulikuwa unazunguka mtaani bila nguo kabisaaaaaa, ndio maana nikakuuliza una mchumba au Bwana,” Madam akamwelewesha.

Upande wa pili wa chumba, Chiba alipasua cheko aliloshindwa kuzuia, lakini bahati nzuri sauti haipiti chumba cha pili na wala haiwezi kuingilia ile rekodi anayoifanya ya mahojiano hayo.

Gina naye alikuwa hoi kwa kucheka, “mwe! Huyu bibi huyu anajijua mwenyewe, sasa ona alivyomvuruga dada wa watu halafu mwenyewe yuko sirias,” Gina alimwambia Chiba.

“Hebu nambie, cha mwisho unachokumbuka katika maisha yako, ulikuwa wapi?” Madam akaanza.

“Nilikuwa Musoma katika mgodi wa North Mara,” akajibu.

“Ulienda kufanya nini?”

“Nilifuatana na msafara wa waziri na wawekezaji wake katika kutembelea migodi ya serikali.”

“Enhe baada ya hapo,” Madam akahoji.

“Sijui kwa kweli na hisi tulipata ajali, maana tukiwa kwenye ndege hali ya hewa ilikuwa mbaya sana, sikumbuki kilichotokea zaidi isipokuwa nikajikuta hospitali,” akajibu. Kisha Madam S akamweleza kila kitu juu ya sakata la madini, yule mwanadada aliishiwa nguvu kabisa, macho yakamtoka pima.

“Usiposema ukweli, unafungwa, kwa maana wenzako wote wametoroka we ndio tumekukamata,” Madam akamtishia, “Uliwaonaje hao wawekezaji?” akaongeza swali.

“Aaa nimekutana na wawekezaji au wafanyabiashara wengi pale wizarani kwa kuwa mimi ofisi yangu ni mambo ya mawasiliano, ila hawa walikuwa walikuwa wahuni sana, halafu walikuwa hawatulii kwenye; mara chooni, mara kwa mhudumu wa ndege, mara sijui vitu gani, mmoja akawa ananitaka kimapenzi pindi tukirudi Dar,” akaeleza. Maneno haya yakamgusa Madam S, tofauti na wengine wote, huyu alijibu zaidi.

“Ulimkubalia?” akauliza.

“Hapana, ila alinipa kadi yake ya biashara kuwa tukirudi nimtafute ikiwezekana nikamtembelee Ulaya au yeye angekuja tena kwa ajili yangu,” akaeleza.

“Hongera mwenzetu umejipolea ‘Nyanyamkala’ la kizungu, sasa ungewasiliana naye vipi?” akauliza tena. Madam S alikuwa na maswali madogo madogo lakini yaliyoleta tija kwa kazi hiyo. Yule mwanadada akatoa kadi ya kibiashara akampa Madam S.

“Alinipa card yake hii hapa,” akamwonesha Madam S. akaichukua na kuigeuza geuza, akaitazamisha kwenye kioo kikubwa ambacho kama si mjanja huwezi kujua kama ni kioo, kisha akaigeuza upande wa pili na kuiweka mezani.

Kitendo cha kufanya hivyo, upande wa pili Chiba alielewa, hivyo aliipiga picha ile kadi kutoka upande wa pili na kuingia kumbukumbu zake kwenye kompyuta yake bila mwenye nayo kujua. Kutoka upande wa pili walipo Chiba na Gina, Chiba akaiingiza ile taswira ya kadi katika kompyuta maalum, iliyounganishwa na mtandao wa uhalifu duniani, akaagiza imletee majibu juu ya namba za simu, picha na maelezo mengine.

Madam S, akamruhusu yule mwanadada akapumzike, Dr. Jasmine akaingia na kumchukua kisha akampeleka katika chumba chake cha siri.

JOPO LILE LA WATU WATATU lilikutana tena mahala palepale, kama kawaida kila mmoja huwa ana njia yake ya kufika hapo, wakamkuta mkuu ameketi akiwasubiri, lakini alikuwa katika hali tofauti sana.

“Ndiyo Mkuu tumekutana kama ilivyo ada, tupe ripoti yako ulivyotuahidi kisha tujue tunafanya nini,” alipendekeza mjumbe mweusi.

“Tunahitaji kufanya kazi ya ziada ndugu zangu, kama tetesi zilivyokuwa kwanza lakini sasa nimeanza kuogopa, vijana wetu wamerudi, mzigo wa Almas umefika tulipoutaka ufike bila tabu, lakini njama imeteguliwa, wale jamaa wa TSA wameweza kugundua kuwa wizi ule haujafanywa na waziri wao, na hii inanitisha kwa sababu mpango wetu ulikuwa yule waziri afie mle ndani ili asionekane tena, kwa mtindo huo tungewajengea imani Watanzania kuwa ni waziri aliyefanya hivyo. Sasa wamempata, kambi yetu ya Mwanza imepekuliwa na kila kitu kiko wazi, hawa jamaa wanataka kupiga hatua ya pili, wanataka kuachana na ya nyumbani na kuwasaka wale makomandoo wetu tuliowatuma. Wakianza kuwachunguza na kufanikiwa kuwagundua, mambo yataharibika,” aliwaambia wajumbe walioonekana kupigwa na butwaa la mwaka.

“Yaani kanchi kale kanajifanya kana idara nzuri ya usalama? Tumewashinda CIA kwenye sakata la kuiba data pale Langley na mpaka leo wamekili kushindwa, tumewazidi kete KGB na tukapata siri za wanaotafutwa na majasusi hao, nini TSA? Ni kuwamaliza tu kabla hatujafanya kazi nyingine, kama ni kikwazo ni kuwapoteza tu, mbona kazi hiyo ni ndogo, kisha Tanzania itajikuta inaamka bila Jasusi hata mmoja,” akaongea kwa hasira yule Mwarabu.

“Sawa lakini tunafanyaje?” yule mkuu akawarudishia uamuzi.

“Tupeleke kikosi chetu cha siri, kikawapeleleze kikiwagundua na udhaifu wao basi ni kuutumia na kuwamaliza, wakati wao wanaomboleza, sisi tunamalizana na mtu wetu,” yule mweusi akaongea.

“Good Idea,” (wazo zuri) Mkuu akaitikia.

“Sasa naomba kila mmoja kwenye idara yake akahakikishe analifanya hilo, tukutane tena masaa sita yajayo tumalize kazi.

DAR ES SALAAM – SHAMBA

MADAM S ALISHUSHA FAILI DOGO yaani lenye kurasa chache mezani pake, katika ofisi ya siri huko ‘Shamba’, alijiridhisha na taarifa zote zilizowekwa na Chiba katika faili hilo juu ya mtu anyeitwa George Mc Field, Komandoo mtoro wa jeshi la Serbia, anayejihusisha na kazi za kukodi kufanya matukio yenye utata kama haya. Alikuja Tanzania mara ya pili akiwa bado ana kumbukumbu juu ya sakata la walilolipa utambulisho kama ‘Mwanamke Mwenye Juba Jeusi’ jinsi alivyoponea chupuchupu dhidi ya mkono wa Kamanda Amata, na mwenyewe alikiri kuwa huyo ni ‘Mwanaume wa chuma’. Kwa jinsi alivyoweza kujibadili kitaalamu akiwa huko kwao, aliamini wazi kuwa hatoweza kugundulika na mahasimu wake ambao walisikitika kuikosa roho yake akiwemo Madam S.

Madam S analikumbuka jina hili, anatabasamu anapogundua kuwa, mtu huyo kajibadilisha sura na muonekano wake lakini kashindwa kujibadilisha mbinu zake. Bomu dogo la misumari lililolipuka kwenye moja ya vyumba vya lile jumba kule Mwanza na kumuumiza Madam S mkononi lilimkumbusha lile ambalo lililipuka miaka kadhaa nyuma katika jumba la daktari mmoja huko Keko na kumuumiza kijana wake Amata, lilitegwa na Mc Field, hivyo hakuona ajabu kukutana tena na jina hilo.

“Ndege mjanja hunasa katika tundu bovu,” akajisemea huku akilisukuma lile faili pembeni na kulivuta lingine nalo akalichambua kutazama ndani yake kuna nini, mauaji tata ya Khumalo mwaka mmoja na nusu uliopita, lakini faili hilo halikukamilika kwani hakukuwa na taarifa za kutosha kutoka Afrika Kusini kama sakata hilo lilipatiwa ufumbuazi au la. Chiba alimaliza kurasa ya mwisho kwa kuweka kiulizo na kishangao, na chini akaweka sentensi moja yenye maneno ‘Khumalo na wizi wa almasi Tanzania,’ Madam S akagonga gonga kidole chake kwenye faili hilo, hii ilionesha mwanamama huyu anahitaji kujua jambo katika kisa hicho. Alikuwa peke yake ofisini, wakati wengine wote wametawanyika, isipokuwa Dr. Jasmine ambaye daima alikuwa jirani sana na Madam S hii ilitokana pia na umri kumtupa mkono. Akainua mkono wake, akacheza na saa yake kisha akaongea maneno fulani, akatulia na kusubiri.


Simu ya Kamanda Amata ikaita kwa sauti ya chini, akaichomoa mfukoni, akajua tu kuwa ni simu ya kirafiki ambayo haina madhara yoyote.

Akaitoa na kutazama, akatabasamu, Jenny.

Kamanda Amata alikwisha msahau mrembo huyu kutokana na kubanwa na majukumu, alipoona jina hilo likirukaruka kwenye kioo cha simu yake moyo wake ukachanua kwa furaha kama ua la saa sita, akavuta kumbukumbu za msichana huyo, katibu muhtasi wa ofisi ya mkurugenzi wa Mgodi wa Mwadui ambaye sasa ni Marehemu, Mc Lean.

Akabonyeza kitufe cha kijani na kuiweka jirani naye sio sikioni.

“Za saa hizi bro,” sauti ya Jenny ikasikika ikiongea kwa chini kidogo kana kwamba anaogopa kufumaniwa.

“Nzuri, unaendeleaje?” Kamanda akamjibu.

“Niko poa, sasa sikiliza…”

Kamanda kichwa chake kikafunguka mara moja, mrembo huyu anataka kumwambia nini, “Nakusikia, niambie,” akamjibu.

“Kuna kitu nimekiokota hapa lakini sijui ni kitu gani, labda wewe unaweza kukitambua, nimekihifadhi,” akamwambia Kamanda.

“Kikoje?”

“Sijui nikielezeeje, ni kama kikadi fulani laini kina rangi ya kijani, hiki kitu sijawahi kukiona ofisini, nimekikuta chooni,” akaeleza. Kamanda Amata hakuona umaana sana lakini hata hivyo kutokana na kazi yake huwa hatakiwi kumpuuza hata kipepeo au dondola, kila kitu kwake huwa kina maana na kinahitaji kufanyiwa kazi.

“Ok, usikitupe, kifiche, nitakupigia na kukuelekeza cha kufanya,” Kamanda akajibu na kukata simu. Alijaribu kuvuta taswira kuwa ni kitu gani lakini hakupata jibu la haraka haraka. Akampa Chiba hiyo taarifa, Chiba akamsisitizia Amata kutopuuza hata unyoya wa kuku.

“Kaka fanya juu chini tukipate inawezekana ikawa ni moja ya vitu vitakavyotusaidia,” alimwambia. Kamanda Amata akainua simu na kumpigia Jenny.

“Kesho, hakikisha unafika Mwanza na kuchukua ndege ya mchana kuja Dar, usikiache hicho kikadi maana ninakihitaji kuliko wewe,”nakamwambia na kukata simu. Wakati huohuo saa yake ikamfinya kuashiria kuna ujumbe unaingia. Akaruhusu na kuuvuta nje mkanda mdogo wenye ujumbe huo.

…Wahi kabla pilau halijachacha…

Akacheka kwa luga hizo za Madam S. Akafungua mlango wa gari na kuuyaacha maegesho ya Uwanja wa Ndege, polepole akaondoka zake.


Ndani ya afisi ya mwanamama huyo, Kamanda Amata akatua faili alilokuwa akilisoma, akaliweka mezani na kumtazama Madam S, akatikisa kichwa.

“Mbona kazi hii inataka kututoa jasho? George Mc Field yupo hapa, tena katika sakata hili? Sasa nimeelewa, nimeelewa nini kinaendelea, tuna kazi nzito sana,” akasema huku akinyanyuka na kulielekea jokofu lililokuwa likibaridisha vinywaji.

“Achana na hilo, nataka uende Afrika Kusini nakupa masaa sita tu ya kufanya kazi pale na kurudi, hivyo siku 2 tu uwe hapa kuanzia sasa ninavyoongea,” Madam S akamwambia Amata.

“Madam, hili halijaisha linakuja lingine tena?” akauliza.

“Hapana, ni hilihili, nataka ukafanye uchunguzi juu ya mauaji ya Khumalo, mazingira ya kifo, muuaji ikiwezekana uje na picha ya muuaji kama aliwahi kuonekana au ni shetani, maana hata shetani picha yake ipo, nimemaliza, potea! Hilo ni moja ya kesi hizihizi, na mimi utanikuta hapahapa siondoki mpaka urudi,” akamaliza.

“Sawa Madam, nimekuelewa,” akajibu.

Ilikuwa ni safari ya dharula lakini ni moja kupata majibu ya mambo fulani fulani ambayo yangeweza kutoa mwelekeo wa sakata zima linalosumbua vichwa vya wanausalama hawa. Baada ya saa moja Kamanda Amata alikuwa angani kuelekea Durban Afrika ya Kusini, akiwa ndegeni kwenye chumba cha V.I.P alikuwa akifikiri wapi pa kuanzia.

Saa sita maana yake sihitaji kulala, aliwaza bila jibu.

UWANJA WA NDEGE WA KIMATAIFA

WA LUIS BOTHA-DURBAN S.A

‘Ukipita kwenye nyayo za mbwa utajua tu kaelekea wapi’ Kamanda Amata alikumbuka sentensi ya mwisho ya Madam S alipokuwa akiagana naye.

Nianzie wapi? Polisi, ofisini au nyumbani kwake? Alijiuliza na kukosa majibu. Akaitazama saa yake, ilikuwa ni saa tatu asubuhi, akateremka kutoka katika ndege hiyo, akakaribishwa na hali ya hewa ya upepo wa bahari. Kwa hatua za taratibu sana akajivuta kuelekea kwenye jengo la ukaguzi na moja kwa moja akaiendea kaunta na kukutana na mwanadada mmoja aliyekuwa hapo.

“Hauna mzigo wowote?” yule dada akauliza.

“Hapana, niko hivi unavyoniona,” Kamanda akajibu.

“Ok, karibu sana Durban Mr. James Ka..”

“..Kariuki, James Kariuki,” akamalizia Kamnada.

“Jisikie upo nyumbani,” yule mwanadada akamkaribisha.

“Asante.”

Saa nne na dakika tano ilimkuta mbele ya ghorofa la wastani, lililopambwa kwa maandishi mazuri yanayosomeka, KHUMALO TOWER, aliyatazama na kisha akavuta hatua na kuifikia kaunta ya mapokezi iliyokuwa na askari wanne wa kampuni binafsi ya ulinzi. Alipowaeleza kuwa anahitaji kufika katika ofisi za The Great Khumalo, akakaribishwa bila taabu. Akavuta hatua na kuchukua lifti akapanda mpaka ghorofa ya saba.

Mbele yake kulikuwa na meza kubwa ya kisasa ambayo ilitanguliwa na mwanamke mmoja wa miaka thekathini hadi thelathini na tano hivi, alionekana kuwa ndiye aliyechukua cheo cha Mkurugenzi wa kampuni hiyo. Haikumchukua muda Kamanda kujua kuwa binti huyo ana unasaba wa karibu na marehemu kwani mbele kabisa ya meza hiyo kulikuwa na kibao chenye maandishi ya dhahabu Ms. Lereti Khumalo M.D.

“Karibu sana, japokuwa sina miadi na wewe ila nitakusikiliza kwa kuwa umetoka mbali kama ulivyonieleza,” yule mwanadada alimwambia Amata mara baada ya kujitambulisha.

“Asante kwa ukarimu wako mrembo, naitwa Mr. James Kariuki, ni Mkenya ninayeishi Tanzania, nimekuja bila miadi lakini nina jambo muhimu la kibiashara la kuzungumza,” akajieleza, lakini akaona kamshtuko fulani kutoka kwa yule mwanadada.

“Biashara gani? Kama almasi za wizi hatununui,” Lereti akamkatisha.

“Ha! Umejuaje?” Kamanda akajifanya kushangaa.

“Najua, nina habari zote za juu ya huo wizi kupitia vyombo vya habari, lakini ninyi Watanzania mmekuwa mabwege sana hata mnaibiwa kijinga na waziri wenu! Mnakamata na kunyonga tu,” akaeleza, mara hii alioneka kutulia vizuri kitini, “haya niambie biashara hiyo!”

“Nataka almasi,” Kamanda akaanzia hapo.

“Unataka almasi?” yule binti akarudia hiyo sentensi kwa kuuliza.

“Ndiyo, almasi hii imepotea mwaka mmoja na nusu, na mi nimetumwa kuitafuta, nimeambiwa wewe utanisaidia,” wakacheka pamoja na kugongesha mikono yao.

“Eeeh, Lereti, samahani, ninahitaji kujua mambo fulani kutoka kwako kwani nimekuja kikazi zaidi,” akaeleza mara hii kwa utulivu.

Lereti akatega sikio.

“Nahitaji ikiwezekana tuwe wawili tu,” akamwambia. Lereti akakunja uso na kuukunjua.

“Ni ngumu sana, ongea hapa, kama haiwezekani basi haiwezekani kwani ufalagha daima nakuwa nao na mpenzi wangu tu, sina falagha nyingine mimi.”

“Nipe nafasi.”

Baada ya mvutano, Lereti akakubali lakini kwa masharti magumu sana.

“Itabidi uvumilie kwa sababu bado nina machungu na kifo cha baba yangu, naogopa falagha na watu nisiowajua,” akaeleza huku akisimama. Mara vijana wanne wakaingia, wakamkagua Kamanda wakachukua bastola zake mbili na vitu vyote vya hatari, wakaweka pembeni, wakamfunga pingu mikono yake kwa nyuma na miguu pia ili asiweze kufanya lolote la hatari. Akaingizwa katika chumba cha wastani chenye kitanda kimoja kidogo, akaketishwa hapo na wale jamaa wakaondoka, dakika chache akaingia Lereti, na kuketi mbele yake.

“Haya unasemaje? Dakika kumi tafadhali.”

“Lereti, pole sana kwa kifo cha baba yako lakini hongera kwa kuweza kuendeleza biashara na kampuni yake, huu ni urithi tosha kwenu,” Kamanda akazungumza, “hivi gawio lenu la hisa kutoka kwa Robinson Dia-Gold LTD mlichukua?” akauliza.

Lereti alimkazia macho Kamanda, “wewe ni nani mbona unataka kujua mambo ya ndani sana?” akauliza, “hatukuchukua kabisa na wala sitaki kusikia.”

“Ok, je unafikiri kifo cha baba yako kinahusiana na hili?” Kamanda akarusha swali. Lereti akabaki midomo wazi, hakuwahi kufikiri wala kuwaza juu ya mambo hayo mawili kuwa na uhusiano.

“Kiukweli sijui kama vina husiana ijapokuwa ni wiki ileile baba alitakiwa kwenda Canada ila ndo hivyo,” akajibu.

“Mlifanikiwa kumpata au kumgundua muuaji?”

“Hapana, hata polisi na wana usalama wameshindwa kumpata mpaka leo mpaka kesho,” akajibu. Kamanda akatikisa kichwa juu-chini.

“Unataka tuongee nini Mr. Kariuki?”

“Juu ya kifo cha baba yako,” akamjibu kwa mkato. Lereti alishtuka sana.

“We kama nani?” akauliza.

“Mpelelezi pekee duniani aliyepewa kazi ya kuchunguza kifo cha baba yako,” akajibu.

Lereti akajikuta kwenye dimbwi la sintofahamu, amwamini au hasimwamini? Kitendawili.

“Mpelelezi, ina maana wewe ni mwenyeji wa South Africa?” akauliza.

“No, mimi nimetoka Tanzania, kumbuka Tanzania na Afrika Kusini tuna urafiki wa enzi na enzi, sasa serikali ya Tanzania haikuona haja ya kufumbia macho mauaji ya baba yako ambaye ni mfanya biashara maarufu hakuna asiyemjua, nami nimetumwa, usione kimya, tupo kazini na nina saa nne tu nirudi kwetu ili uchunguzi zaidi uendelee, tumkamate muuaji,” Kamanda akaeleza.

Lereti akatabasamu baada ya habari hiyo, akabonya kitufe fulani na wale vijana wakaingia.

“Mfungueni, mpeni vitu vyake,” akawaambia, wakafanya hivyo. Amata akawa huru tena.

“Sasa labda twende polisi wakakueleze kiundani walipofikia au kuishia,” Lereti akamwambia Amata.

“Haina haja, niambie wapi baba yako alipouawa, hapo ndipo ninapopataka hasa,” Kamanda akamwambia, baada ya hapo yakafuatia mazungumzo kidogo na baadae wakatoka wote mpaka nje ya jengo hilo, binti huyu alikuwa akilindwa na watu watatu wenye silaha na walioekana ni wapiganaji haswa.

“Mr. Kariuki, familia yangu ina maadui wengi ndio maana unaona mazingira yako hivi, samahani kwakukuona na kukufanya kama mhalifu,” akamwambia.

“Usijali,” akamtuliza. Wakaingia garini na kuondoka.

Bila shida, akamtajia jina akampa na jina la gereza. Kamanda akaagana naye, akaondoka na kurudi kwenye gari, akamkuta Lereti akimsubiri.

“Vipi?” akauliza kwa shauku.

“Unamjua Mesobhuja Annie?” akauliza Kamanda.

“Ndiyo, amefungwa kuwa yeye ni muuaji,” akajibu.

“Nataka kumuona,”

“Yupo gerezani huwezi kumuona kiurahisi namna hiyo,” Lereti alijibu.

GEREZA KUU KWAZULU NATAL

BAADA YA ITIFAKI MBALIMBALI na kujitambulisha kwa uwazi kwa wakuu hao wa gereza, Kamanda Amata alipewa dakika nne tu kumuona mwanamke huyo.

“Nihakikishie nitatoka humu, nimechoka si mimi niliyeua,” akajieleza Mesobhuja.

“Ndiyo, ukinieleza ukweli, utaachiwa na ndiyo maana nipo hapa,” Kamanda akamfariji.

“Alikuwa mwanamke, sijui aliingiaje ndani ya kile chumba cha kutolea huduma, nilikuwa nammasage mteja wangu akiwa kalala kifudifudi, mara ghafla niliondolewa na mwanamke huyo, Mzungu mwenye nywele ndefu, sikumjua, akanipa ishara ya kutulia kimya, nikaogopa sana, alifanya mauaji ya haraka kwa kumvunja uti wa mgongo, yule alikuwa ni muuaji by professional. Kisha aliwaita walinzi kuwa kuna shida. Nao akawaua kwa kuwagonganisha vichwa vyao kwa nguvu, kisha akaondoka. Basi! Nimejitetea sana kuwa si mimi muuaji lakini wapi, nimefungwa hapa kifungo cha maisha, nisaidie jamani, unihurumie dada, sikumuua baba yako.”

Maneno hayo toka kwa Mesobhuja yalimtoa machoa Lereti.

“Niambie, unakumbuka alivaaje mwanamke huyo?” Kamanda Amata akamwuliza.

“Ndiyo, alivaa suruali bluu angavu, brauzi nyeusi, na kikoti chenye rangi kama ya suruali yake, nywele alizifunga nyuma kwa kutumia mpira, alikuwa na miwani nyeusi, na alipovua mara moja kuniangalia, macho yake yanatisha kwa jinsi alivyojiweka make up,” akajibu.

“Unakumbuka muda? Hata kwa kuhisi,”

“Ilikuwa ni kati ya saa tatu narobo asubuhi na saa nne hivi,”

“Ok, asante, usijali tunalifanyia kazi,” Kamanda Amata akamwambia na kisha wakatoka.

Lerethi na Kamanda Amata wakatoka na kuwashukuru viongozi wa gereza hilo, akamwamuru dereva amrudishe katika jengo la Monte Blanc.

“Huko kuna nini?” Lereti aliuliza.

“Naenda kumalizia kazi, kisha naondoka zangu,” akajibu.

Walifika na kuingia tena, kama kawaida watu walikuwa wakimtazama sana mwanadada huyo kwa jinsi alivyo na umbo la kibantu, aliyependeza kwenye suti yake nadhifu kabisa, akizunguka na walinzi huku na huku.

“Mtoto wa Khumalo,” sauti zenye maneno au minong’ono kama hiyo zilisikika kwa waliosimama.

Kamanda Amata kwa utundu wake alifanikiwa kufika katika chumba kinachohifadhi kumbukumbu zote za usalama za jengo hilo, kulikuwa na kijana mmoja anayefanya kazi ndani yake. Alimsikiliza Kamanda Amata shida yake na baada ya kuoneshwa kitambulisho halisi cha Kamanda kinachomueleza kama Mpelelezi namba moja Tanzania na Afrika alikuwa haishi kutetemeka. Akavuta droo na kuchomoa disc moja akakiendea chombo maaluma na kuitumbukiza, kisha akawa anaangalia matukiao ya siku hiyo.

Akarudisha picha zile za CCTV mpaka picha ya mwaka mmoja na nusu uliopita, tarehe ile aliyouawa Khumalo, 16 Julai akairudisha mpaka saa 3:15 asubuhi na kutazma matokeo. Kama alivyotarajia, picha ya saa 3:47 ilimuonesha muuaji wa Khumalo, alivaa vilevile kama alivyoelekezwa na Mesobhuja, akarekodi kipande hicho na kisha kuondoka nacho, akamwachia randi 100 kijana huyo kisha akapotea.


Katika Uwanja wa Ndege wa Louis Botha, Kamanda Amata alikuwa akiagana na Lereti Khumalo. Binti huyu alishindwa kujizuia akamkumbatia kijana huyu shababi.

“Asante Kariuki, kwa saa hizi chache nimefurahi kuwa nawe, nakutakia kila lakheri ufanikiwe kumkamata huyo hayawani, na ukifanikiwa nitakupa zaidi nzuri sana ambayo sijawahi mpa yeyote duniani, unijulishe,” akamwambia Amata huku chozi likimtoka, “you are so Intelligency person,” akamalizia.

Lereti hakutaka kumwachia Kamanda, alibaki kumkumbatia huku chozi lake likitua kwenye koti la suti ya kijana huyo.

“Nahitaji kwenda,” akamwambia Lereti huku akiitazama saa yake kutokea mgongoni mwa mwanadada huyo, ilikuwa zimetimia saa tano. Kumbe nimeweza, akawaza. Lereti akamuachia kamanda, “ni muda mfupi lakini nahisi moyo wangu umekuamini sana kwa kila kitu,” Lereti akaeleza ya moyoni.

“Usihofu ni kawaida,” Kamanda akajibu huku akimpa kadi biashara kwa ajili ya mawasiliano, na Lereti akafanya vivyo hivyo.

Daima huwa ni vigumu sana kwa Kamanda Amata au mtu yeyote mwenye kazi kama yake kujitambulisha waziwazi ijapokuwa alichokifanya yeye ni kujitambulisha wazi lakini bado kwa kujificha, alijikuta anaukonga moyo wa mwanadada huyu mrembo mtoto wa Marehemu Gervas Khumalo, binti pekee katika familia lakini aliyeaminiwa sana na wazazi wake kuliko hata kaka zake watatu waliomtangulia. Alikuwa msomi anayejua maswala ya utawala mwenye Shahada ya Uzamivu katika nyanja hiyo, aliogopwa na wasomi kwa kuwa alikuwa ‘ngangari’ katika kutetea hoja au kitu, alikuwa na uwezo mkubwa wa kugeuza uongo kuwa ukweli na ukweli kuwa uongo. Wanaume walimdondoshea mate ya tamaa na uchu lakini hawakuwa na nafasi hata chembe ya kusema lolote, waliishia kula kwa macho. Kila mtu, hata walinzi wake walimshangaa pale uwanja wa ndege kumkumbatia mwanaume, tena aliyemuona kwa mara ya kwanza tu, asiyemjua kwa undani, ama kweli ‘Mapenzi yamerogwa’ aliandika mwandishi mmoja mashuhuri nchini Tanzania, Hussein Wamaywa.

07

IKULU – DAR ES SALAAM

MHESHIMIWA RAIS, HAKUAMINI KILE anachokiona mezani pake. Alikuwa katika ofisi yake ya siri kabisa, Kilimanjaro Square. Ofisi ambayo hata katibu wake hakuwahi kuingia na funguo zake daima alijua yeye anaziweka wapi. Akatikisa kichwa, akauma meno kwa hasira. Kabrasha moja lenye jalada jekundu lilikuwa mkononi mwake likibeba maandishi makubwa ya rangi ya dhahabu ‘The Order Of Being a President’, ndani yake mlikuwa na makubaliano au mkataba kati yake na wale waliokubali kumuweka madarakani kwa makubaliano maalumu. Kwa kuwa alishaambiwa kuwa nusu ya utawala wake akabidhi migodi yote mikubwa kwa maswahiba hao au tuwaite wahisani na wafadhili kwa lugha tuliyoizoea alijikuta hana la kufanya baada ya kugundua kuwa kipindi cha utawala kinamtupa mkono.

Kumbe miaka mitano si mingi, aliwaza huku akikuna kichwa chake ilhali hakikuwa kikiwasha.

Mshtuko mkubwa ulimfika pale alipokutana na sentensi finyu chini ya ukurasa wa mwisho kuwa, hatuwezi kufika kurasa ya mwisho bila kutekeleza kurasa inayoitangulia, moyo ulimpasuka, midomo ikamcheza, akashika pini ya dhahabu na kuifungua kurasa iliyobanwa barabara ambayo hakutakiwa kuifungua kabla. Kurasa yenye pini za dhahabu.

Utakuwa umetugeuka kwa kukiuka makubaliano yetu

Tutachukua madini na na mali nyingine kwa nguvu ili kurudisha gharama ulizotuingiza wakati wa kukupeleka Ikulu.

Tutachukua madini kwa jinsi tunayojua sisi, na hata ukijua kuwa ni sisi basi pia ujue kuwa umechelewa, usifanye lolote, bali utulie katika kiti chako, legeza ulinzi ili tufanikishe.

Kumbuka mkataba wetu, faida yetu lazima irudi mara tatu ya pesa tuliyowekeza.

Mwisho wa mkataba wetu ni huu, ukifungua kurasa hizi, ukazikaidi, tunaondoka na Roho yako

Kumbuka tupo kila mahali, mpaka kwenye kiti ulichokalia

Marafiki zako tunaokupenda sana.

Akashusha pumzi ndefu, mikono ilikuwa ikimtetemeka.

Nimekwisha, kwa nini nilijiingiza huku? Akawaza na kuwazua, hakuna jibu.

Tama mbaya, tena mbaya sana, Mh. Rais alijikuta katika hali ngumu, mwili ulilowa jasho wakati ofisi hiyo ilijazwa kwa baridi la mashine ya kupoza hewa.

Akajiuliza mengi, akagundua migogoro mingi na vita vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi mbalimbali hasa nchi za dunia ya tatu ni inaweza kuwa ni ‘matekelezo ya mikataba’. Akaikumbuka Nigeria, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Mali, Afrika ya Kati, Somalia na nchi mbalimbali za Kiafrika zilizoingia kwenye migogoro mizito, akakumbuka marais waliouawa wakiwa nyadhifani, wakiwa bado wanakula maisha ya ufalme wao. Akajikuta akili yake ikitengana na ubongo.

Migogoro mingi katikla nchi zinazoendelea inasababishwa na mabwanyenye kutoka mataifa beberu ya nchi za dunia ya kwanza, ambazo zinapanga nani atatawala pale na nani kule ili wao wapenyeze fikra na tawala zao dhalimu. Bara la Afrika ni bara lililoathirika sana na Siasa za mtindo huu. Vita vilitawala kila kona, hakuna aliyejua amani, kila mtu alijijengea mazingira ya kujilinda yeye na familia yake, vikundi vya kigaidi viliiibuka kila wakati na kila mahali, jiuliuze vinapigania nini kwa maslahi ya nani, hata wapiganaji wenyewe hawajui na hawana jibu.

Kila kukicha, kule kumelipuliwa, 500 wametekwa, 200 wameuawa. Vyombo vya habari vya mataifa makubwa vinawekeza katika nchi masikini kutengeneza habari mbaya za Afrika, wanazisababisha wao na wanazitengeneza wao, wanaieleza historia mbaya ya bara letu. Sisi wenye bara letu hatukumbuki hata kutangaza historia nzuri na ya kupendeza ya Afrika na kubadili fikra za ulimwengu huu, kwa kuwa tunafanya kila kitu chini yao, basi hata habari za Afrika tunanakili kutoka katika vyombo vyao wenyewe. Hao ndio ‘King Makers’, nipe madini nikupe Bunduki, Jiue mwenyewe.

“No! Nooooooooooo!!!!” alipiga kelele bila kujijua akiwa katika ofisi ile, na hakuna aliyesikia kutoka nje, akaanza kuhema kwa nguvu, ofisi ile aliiona ndogo kama kiberiti, alihisi hatoshi.

Wataniua, akawaza. Aibu, akajijibu.

Haiwezekani, nina Askari Polisi watalinda migodi, nina Jeshi la Wananchi watapambana na udhalimu wowote dhidi ya nchi yangu, nina Askari Magereza watawafunga wote watakaoleta shida dhidi ya utawala wangu awe mweusi au mweupe, nina watu wakakamavu wa Usalama wa Taifa watanilinda kila ninakokwenda hakuna risasi itakayokifikia kichwa change. Hawaniwezi, hawaniwezi kabisa. hapa nitamuweka yule, mgongoni kwangu atakaa yule kule, nitaongeza body guards kutoka wanne wa sasa watakuwa nane wa karibu, na kumi na sita watakaotawanyika, nitabadilisha gari la kutembelea, nitaagiza jipya, la kisasa lisilopenya risasi wala kulipuka kwa moto. Ah! Lakini wanaotengeneza gari si ni wao wenyewe, sasa nifanyeje, simwamini mtu, kama waziri katumiwa kuonekana kaiba almasi kumbe ni wao wenyewe waliojigeuza katika maumbo na sura, hawa ni hatari, nifanyeje, nisitoke ndani. Sasa nikialikwa kwenye shughuli za hadhara, itakuwaje, watanidungua.

Aaaaaa, ok sasa nakumbuka, walinidungua pale Bunju, lo! Hawakuniua, hawakushindwa kufanya hivyo, kwa nini nimechelewa kujua hili? Nani alitekeleza anayeweza kuupenya usalama wa nchi yangu uliotukuka ndani na nje, atakuwa mtaalam sana huyo, dereva wangu naye ni mwanajeshi, mpiganaji anayejuwa kuendesha gari katika ‘Defensive Driving’, ilikuwaje hakuona kama tunadunguliwa?

        Yote yalikuwa ni mawazo, akiwa anatazama saa aliyokuwa akiiona mishale yake ikikimbia kuliko kawaida, akiwa amelowa jasho kuliko, Mheshimiwa Rais alichanganyikiwa, yote yalikuja kwa mara moja. Aliona saa 24 za siku hazotoshi labda mchana uwe na saa 72, miezi kumi na mbili ya mwaka michache sana, labda ingekuwa ishirini hivi. Akajiegemeza kitini, akashusha pumzi, mwanga wa taa ulimpiga machoni, akayafinya.

Alihisi kuetetemeka mwili mzima, akafungua tai na kuitupa huko, akalegeza vifungo vya koti na shati lake apate hewa ingawaje mashine ya kupoza hewa ilikuwa ikiunguruma kwa nguvu zote.

Akafunga lile kabrasha, akalitia kwenye droo, akafunga kwa namba anazojua yeye.


Katika ofisi za wanausalama ndani ya jengo la Ikulu, mlio wa hatari ulisikika, Johnson Cheka, mwanausalama mwenye amri ya mwisho ya kusema Rais afanye hivi au asifanye alikuwa wa kwanza kutoka na kupiga hatua kumi na tano kufika pale kwenye mlango wa kuingia katika makazi ya Rais ambayo yapo ndani ya Ikulu, akafungua mlango na kuingia haraka, akaufikia mlango wa ofisi hiyo ndogo, akautikisa, umefungwa, akajaribu kuufungua umefungwa, akachomoa funguo zake za ajabu na kufanikiwa kuufungua, akamkuta rais amejilaza mezani akivujwa jasho jingi. Mara moja akamsogelea na kumwinua, kwa taabu kidogo akamfikisha kwenye kochi kubwa sebuleni, akainua redio yake na kumwita daktari huku yeye akiifuna afisi ile. Dakika moja tu daktari akafika, mara moja na kumchukua mpaka ghorofa ya chini ambako kuna hospitali ndogo yenye kila kitu iliyojengwa maalumu kwa familia ya Rais.

Johnson Cheka alisimama pembeni mwa kitanda akitazama pilikapilika za daktari na muuguzi wake. Dakika tano baade hali ikatulia. Cheka akamwita Mkuu wa itifaki akamweleza kubadili ratiba zote za Rais kwa siku tatu, hakutakiwa kuonana na mtu yeyote, alitakiwa kupumzika. Ilileta mshtuko kwa kila aliyejua, lakini bado ilikuwa ni siri kubwa sana.

Madam S alipata taarifa ya hali ya Rais, hakuweza kuchelewa, siku hiyohiyo alifika Ikulu kumjulia hali Mkuu wa Nchi kwa namna moja, bosi wake. Yeye haina tabu kufika anapotaka, alikaribishwa na kuongozwa mpaka aliko mkuu huyo. Mara baada ya kuwasili, Rais akatabasamu kumwona, akawataka wengine kutoka nje ili abaki kwa muda na mwanamama huyo.

“Nahitaji kufuma upya kikosi cha ulinzi,” ilikuwa ni kauli ambayo ilipenya masikioni mwa Madam S.

“Kwa nini,” Madam akauliza.

“Hali ya kiusalama ni mbaya, kwangu na kwa nchi,” akamweleza.

“Najua, sasa wataka kufanya nini?” Madam akauliza kwa kuwa alijua wazi kuwa kubadilisha au kuimarisha kikosi cha ulinzi cha Rais au kuwa na wasiwasi na walinzi wake tayari kuna jambo na jambo lenyewe kubwa si dogo.

“Nitakwambia, maana nikishaweka mambo sawa, wewe utahusika kujua,” akamwambia Madam S.

Kamanda amata aliwasilisha ripoti yake kwa Madam S na jopo zima la TSA juu ya mauaji na muuaji wa Mr. Gervas Khumalo.

“Sasa tuna nini lingine la kutafuta?,” Madam aliuliza, kisha akaongeza, “ huyu mwanamke, ndiye huyu tuliletewa picha kutoka Ufaransa, ndiye huyu tulicholewa picha na mchoraji wetu baada ya sakata la msafara wa rais, hizi hapa zinafanana kabisa, ni nani mwanamke huyu? Yuko wapi na anataka nini? Hilo ndilo la msingi sasa kuona, siwezi kusema akamatwe au aachwe, kwanza huyu ni nani?” Madam S akang’aka, alionekana wazi kuwa na hasira siku hiyo. Ukimya ukachukua nafasi yake, hakuna hata aliyekohoa. Kisha akaendelea kuleta utata mwingine.

“Sikilizeni, tena sikilieni kwa makini sana, rais anataka kufumua kikosi cha usalama na kukipanga upya, mimi nimemhoji sana kwa nini akanipa siri ifuatayo, siku msafara wake ulipodunguliwa, amegundua uzembe wa hali ya juu sana kiasi kwamba sasa anataka hata dereva wake achunguzwe…”

Kamanda akamkatisha, “sasa atafumua wapi ataacha wapi…?”

“Mi sijui, lakini yeye atakapokutana na mkurugenzi wa Usalama wa Taifa watajua,” akajibu.

“Inabidi kweli dereva achunguzwe, vipi kama hakuwa dereva tunayemjua? Chiba akauliza.

“Ndiyo utata, maana waziri walimtengeneza watashindwaje dereva, hakuna haja ya kupoteza muda, dereva inabidi afanyiwe uchunguzi haraka,” Madam akaongeza na kumpa kazi hiyo Scoba aitekeleze haraka iwezekanavyo.

ITAENDELEA

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Nne

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment