Wakala wa Giza sehemu ya Tano
KIJASUSI

Ep :05 Wakala wa Giza

SIMULIZI Wakala wa Giza
Wakala wa Giza sehemu ya Tano

IMEANDIKWA NA: HASSAN O MAMBOSASA

*********************************************************************************

Simulizi: Wakala Wa Giza

Sehemu ya Tano (5)

Haikuwa jambo geni sana kwa vijana wa mtaani kuzozana kuhusu masuala kama hayo au ushabiki wa mpira pamoja na ushabiki wa wasanii wa kizazi kipya, walikuwa wakifikia hata hatua ya kukunjana mashati na hata kuzuka mzozo kama walikuwa ni mahasimu waliokkuwa wakiwindana kwa muda mrefu. Mzozo huo waliokuwa wanawekeana huweza kuisha hata ndani ya dakika tu tangu utokee na hata vijana waliokuwa wakigombana wakawa kama hawakuwa na mzozo, ugomvi wa aina hii ulikuwa ukijulikana kama ugomvi wa kisela kwani wahusika wake hawakuwa na visirani baada ya mzozo huo kuisha. Urafiki baina yao hurejea palepale ugomvi unapoisha, kwa mtu ambaye atawakuta vijana wa aina hii wakiwa wameacha kugombana na wakiongea masuala mengine ya mtaani basi anaweza kusema kuwa hakukuwa na ugomvi baina yao. Mtu asiyezoea ugomzi wa aina hii wa vijana wa mitaani akiwa wanagombana basi anaweza kusema vijana hao wamerukwa na akili baada ya kupatana, pia anaweza kutokwa na kicheko kabisa akiwaona baada ya kutokea kwa ugomvi huo.


Adhana ya alasiri ilipokuwa ikitolewa kikao cha ghafla kilikuwa kimeitishwa ndani ya kambi ya kina Wilson, wachache waliokuwa wamebakia kabla Norbert hajapitisha fagio la chuma katika kuwafagia ndiyo walikuwa wakihudhuria kikao hicho cha muda mfupi baada ya taarifa ya kupoteza fahamu kwa Mufti kuwafikia. Wilson, Mzee Ole,Josephine na L.J Ibrahim ndiyo walikuwa wahudhuriaji wa kikao hicho cha ghafla walichokuwa wamerkiitisha muda huo wa saakumi kasoro alasiri. Ingawa yalikuwa yamebaki masaa machache kuanza kwa mapinduzi bado walikuwa na wasiwasi kwa kutoonekana kwa wenzao ambao walikuwa pamoja kikazi tangu wanaanza harakati hizo, kutokuwepo kwa Kamishna Wilfred na Thomas ni jambo ambalo lilikuwa likiwaumiza kichwa kwa muda mrefu sana wasijue walikuwa eneo gani hadi muda huo.

Simu zao zote hazikuwa hewani na hata taarifa juu ya eneo walilokuwepo walikuwa hawana, walikuwa wamechanganywa sana na suala hilo ingawa hawakuwa wamekata tamaa kabusa juu ya suala hilo. Hawakuwa wakijua kabisa fagio la chuma lile lililokuwa limefagia utawala mbovu wa Mzee Ole miaka kadhaa iliyopita ndiyo lilikuwa limefagia watu hao waliokuwa wakiwatafuta ambapo moja tu ndiyo alikuwa anapumua kati yao wawili hao waliopitiwa na fagio la chuma, walikuwa wakiumiza kichwa zaidi kwa kutoonekana kwa wenzao muhimu waliohitajika kwa siku hiyo muda wa usiku katika kuhakikisha utawala wa Rais Zuber ulikuwa unaondolewa.

“Jamani kuna anayejua Thomas na Kamishna walipo au kuna mwenye taarifa yao nyingine?” Mzee Ole Aliuliza huku akiwatazama wenzake usoni, kimya kilipita pasipo swali hilo kujibiwa. Kila mmoja alikuwa akimtazama mwenzake usoni akitegemea anaweza kutoa jibu la swali hilo, hakuna hata mmoja aliyenyanyua mdomo wake kujibu swai hilo kuweza kuwaridhisha aua kuwapa ahueni katika mioyo yao juu ya kutoonekana kwa watu muhimu sana ambao walikuwa ni sehemu ya mpnago wao uweze kutimia.

“Kama hamna basi kuna tatizo haiwezekani kabisa watu hawa wasiwepo hap bila kuwepo taarifa yeyote ile, mke wa Kamishna anadai mume wake hajaonekana nyumbani kwake tangu usiku alipotoka. Asubuhi ya leo nayo Thomas tangu alipotoka hajaonekana, jamani sasa wasipoonekana hawa tutakaa tulitegmee jeshi tu” Mzee Ole aliongea kwa mara nyingine, kimya kilichukua nafasi na hakuna mwingine aliyekuwa akiongea baada ya maelezo hayo.

Zilipita daika takribani mbili na hakuongea mtu yoyote kutokana na kutokuwa na taarifa ya uhakika juu ya jambo hilo, wakiwa wapo ndani ya kimya hicho simu ya Mzee Ole iliita. Wote kwa pamoja waligeuza macho kwa mzee Ole baada ya kusikia mlio huo wa simu yake na akapokea, wenzake wote walikaa kimya kumpa nafasi nzuri Mzee Ole aongee na simu hiyo.

“Ndiyo kijana……..Yes nimepata taarifa za kulipuka kwa hoteli ya Enot…….Oooooh! Shit!….sawa sawa nitumie kwa Whatsapp niione” Mzee Ole alipomaliza kuongea na simu hiyo tayari alikuwa ameshachoka bila kazi ngumu yenye kumchosha kumfanya achoke, aliwatazama wenzake ambao walikuwa wakimtazama kwa shauku sana kujua kile alichokuwa amekipata kutoka kwa mtu aliyekuwa amempigia simu.

“Kaka vipi kuna nini?” Wilson aliuliza

“Ole vipi kuna tatizo” L.J Ibrahima naye aliuliza.

“jamani mambo ni mabaya kabisa” Mzee Ole alianza kuongea kwa taratibu kisha akawatazama wenzake katika nyuso zao na akaendelea “Mlipuko uliotokea katika hoteli ya hapo mbele nadhani mmeusikia kwa siku ya leo, sasa kwa taarifa za kusikitisha ni kwamba mwili uliokutwa mule ndani umeungua hadi hautambuliki ni wa mwenzetu. Thomas ndiye huyo aliyeungua hadi hatambuliki”.

“Ohhh! No! Imekuwa vipi hapo?” Wilson aliuliza akisimama wima kutokana na kupagawa na taarifa aliyokuwa amepewa na kaka yake.

“Wilson mdogo wangu tulia basi basi sijamaliza, kabla ya tukio kamera za ulinzi za hoteli hiyo zilimuona Thomas akiingia eneo la mapokezi katika hoteli hiyo na alitaja chumba ambacho kulikuwa na mwanamke na mwanaume ambao waliokuwa wameingia. Watu hao waliokuwa wametangulia kabla yake walikuwa wakisubiria ujio wake wake, alipoingia yeye ndiyo kamera hizo zikamnasa kwani hakukuwa na mwingine yoyote aliyeingia ndani ya chumba hicho baada ya watu hao” Mzee Ole alimtuliza mdogo wake kisha akaendelea kuongea kuwaeleza wenzake kuhusu taarifa ile, maelezo yake hayo yalikuwa ni yenye kuhuzunisha kwa kila mmoja na pia yalikuwa ni yenye kushtua kwa moyo wa Josephine kwani alihisi alikuwa akikaribia kugundulika kuwa yeye ndiye aliyemkamatisha Thoams na yeye ndiye alikuwa amepita hapo mapokezi na pia ni yeye ndiye alikuwa yupo ndani ya chumba hicho.

Wakati wakiwa wanaendelea kuumia na habari hiyo simu ya Mzee Ole ilitoa mlio wa kuingia ujumbe mfupi wa maneno, Mzee Ole aliichukua simu yake hiyo kwa haraka sana na akaufungua ujumbe huo uliouwa umeingia ndani ya simu yake kwa muda huo. Wote walikuiwa wameinamisha vichwa vyao kasoro Josephie ambaye alikuwa akimtazama Mzee Ole kwa macho ya huzuni ingawa moyoni alikuwa na hofu kubwa sana.

Uso wa mzee Ole ulikuwa amkini sana katika kukitazama kioo cha simu ambapo sauti ya Thomas akiulizia kuhusu chumba ambacho alikuwa ameambiwa aingie ilisikika, wote walipoisikia sauti hiyo walitulia kimya wakimtazama Mze Ole ambaye alikuwa makini akitazama kioo chake. Alikuwa akiangalia video ambayo ilikuwa ipo simu yake hadi ilipoisha ndipo na yeye akmpa simu L.J Ibrahim ambaye aliangalia video hiyo na alipoimaliza akampa simu Wilson. Naye aliiangalia video hiyo hadi ilipoisha akampatia simu Josephine, alipoipokea simu hiyo na kuiangalia video ambayo walikuwa wakiiangalia wenzake moyo wake ulipiga kwa nguvu ingawa alifanikiwa kuuficha huo mshtuko wa moyo wake kwa. Alimuona Thomas akiwa eneo la mapokezi na akijitambulisha kuwa alikuwa na mgeni wake katika chumba cha hoteli hiyo, video hiyo iliishia pale Thomas alipokuwa ameelekezwa mahali chumba hiko kilipo na akawa anapanda ngazi kwa kasi aweze kuwahi huko juu akiwa na hisia kali juu ya Josephine. Video hiyo ilimfanya Josephine awe na mashaka zaidi akihisi kuna jingine linaweza kuzuka kwake kwa muda huio, alirudisha simu mikononi mwa MZee Ole kisha akaenda kuketi kwenye kochi akiwa amenyamza kimya tu.

“Damn! Huyu ni Norbeert tu hakuna mwingine na huyuhuyu ndiye aliyefanya Mufti awe hospitali” Wilson aliongea kwa hasira sana.

“Wilson cool down brother, ishu ya Mufti labda ni mshtuko tu wa kawaida usimuhisi Norbert. Kikubwa amemaliza kazi yake na mpango unaelekea kufanikiwa” Mzee Ole aliongea kumuambia mdogo wake kisha akawatazama wenzake waliobakia na kusema “jamani tunazidi kuteketea kwa uwepo wa mtu huyu anayeitwa Norbert, Thomas ni tayari na bado anatuwinda sasa inabidi tuwe makini na sisi tumuwinde pia kwa usiku huu wa leo. General muda wako wa kwenda kuhakikisha kikosi kinamuondoa Zuber ndiyo huu, Josephine na Wilson mnatakiwa muende Aga Khan jioni ya leo mkachunguze kipi kilichomfanya Mufti awe na mshtuko hadi akawa vile. Ikiwa ni mpango wa Norbert wa kumfanya atoe siri mummalize upesi kabla hajafungua kinywa chake katika kuyaongea mambo yetu, muda wa kazi sasa hatutakubali kushindwa hadi Zuber atoke Ikulu afungwe”.

“Sawa kaka, Josephine twende” Wilson aliongea hukua kiwa tayari ameshasimama.

“Kanuni moja tu katika kummaliza kama ni msaliti, matumizi ya silaha ni marufuku tumeelewana?! Na kama mkitumie muweke viwambo vya kuzuia sauti” Mzee Ole aliwaambia

“Tumekuelewa” Wote kwa pmoja waliitikia kisha wakaondoak eneo hilo wakimuacha MZee Ole na L.J Ibrahim wakiwa wamebakia


Majira ya saa kumi na moja jioni Mufti alizinduka tangu alipoanguka kwa mshtuko akiwa ofisini kwake, alijikuta yupo kwenye mazingira tofauti na aliyokuwa hapo awali na wala hakuwa ameelewa alikuwa amefika vipi kwenye mazingira hayo. Kumbukumbu hazikuwa zimekaa sawa alipozinduka na wala hakuwa ametambua kwa haraka kipi kilichokuwa kimempata, kitu cha kwanza alichokifanya baada ya tu ya kufungua macho ilikuwa kuangaza pande zote. Hapo alijitambua alikuwa yupo ndani ya chumba cha wodi kutokana na mandhari ya chumba hicho kujionesha wazi, mita kadhaa kutoka hapo alipolazwa alimuona muuguzi wa kiume akiwa ametulia kwenye kiti akimtazama kwa umakini hasa baada ya kubaini kuwa alikuwa tayari ameshaamka. Ilikuwa ni habari njema sana Mufti kuamka na ilimbidi Muuguzi huyo atimue mbio kwenda kwa daktari kutoa taarifa ya kuamka kwa Mufti, Muuguzi huyo alikuwa akisubiria kwa hamu sana kuamka kwake na alipoona alikuwa amefumbua macho alinyanyuka haraka na akatoka ndani ya wodi hiyo aende kutoa taarifa kwa Daktari aliyekuwa akimtibu Mufti tangu alipofika hapo hospitali akiwa hajitambui.

Muuguzi huyo alipokuwa amemuacha Mufti peke yake ndipo kumbukumbu ya kile kilichokuwa kimemtokea hadi akapoteza fahamu kilimrudia katika kichwa chake, huzuni ndiyo iliyofuata katika kuutawala moyo wake baada ya kukumbuka kitu hicho kilichokuwa kimemfanya apoteze fahamu hadi muda huo anarudiwa nazo. Moyo ulimuuma sana na alitamani hata atafute njia aweze kuiokoa familia yake, njia hiyo hakuwa nayo na waliposhikiliwa hakuwa anapatambua hata kidogo. Akiwa bado anafikira kuhusu hilo suala mlango wa wodi aliyopo ulifunguliwa taratibu ambao ulimfanya Mufti aelekeze macho yake moja kwa moja mlnaogoni, alimuona Muuguzi wa kike akiingia huku akiwa amebeba ua kubwa sana la plastiki lenye kadi katikati yake. Mhudumu akiwa amejifunmga shungi safi alimsogelea Mufti hadi karibu yake na akamsabahi kisha akampatia kadi hiyo pamoja na maua.

Muuguzi huyo hakuongea jambo jingine alitoka wodini humo haraka sana, Mufti alibaki akiyatazama hayo maua aliyopewa. Kadi iliyopo ndani ya maua hayo ilikuwa ni yenye kumtakia afya njema, aliifungua kadi hiyo akiwa na tabasamu hafifu sana katika uso wake akijua alikuwa amejuliwa hali na mmoja wa washirika wake. Ndani ya kadi hiyo alikutana na kikaratasi kilichobandikwa ambacho kilikuwa kimeandikwa kwa mwandiko wa kalamu ya mkono wala si kwa kuchapwa kama yalivyokuwa maandishi mengine yaliyopo kwenye kadi hiyo, kikaratasi hicho kilimfanya Mufti aifunge kadi na akakichukua pekee ambacho kilikuwa na maneno machache sana ambayo yalijionesha dhahiri yalikuwa na maana kubwa sana.

‘Mpango ni uleule Mufti, fuata maelekezo yangu familia yako itakuwa salama. Hivi sasa unatakiwa uite mkutano wa waandishi wa habari kisha ukiri umesambaza uzushi dhidi ya Rias Zuber na uliyoyaongea hayana ukweli wowote. Isifike saa nne usiku leo huo ujumbe uwe tayari umeshafika kwa watanzania wote tena uwataje na washirika wako wote, ukimaliza hayo familia yako itakuwa salama na ukikaidi utajuta

N001′

Mufti alipomaliza kuusoma ujumbe huo tayari kijasho kilikuwa kikimtoka, hakuwa na ujanja mwingine na alitambua wazi ujumbe ulikuwa unatoka kwa N001. Aliweka mikono kwenye kichwa chake akijifikiria kuhusu suala hilo na alipoitoa alimkumbuka yule binti aliyekuwa amemletea ujumbe huo ambaye tayari alikuwa ameshatoweka, akili za Mufti zilimpa hisia kwamba huyo binti ndiye mbaya wake mwenyewe aliyekuwa akimtafuta na pia ndiye aliyekuwa ameshikilia familia yake.

“We binti weee!” Mufti alipayuka huku akitoka kitandani na lakini uwepo wa dripu ulimzuia asifike mbali kwani sindano aliyochomwa ilianza kumletea maumivu. mkononi, aliishikilia kwa haraka sindano hiyo ili aweze kuitoa lakini kabla hajaitoa mlango wa wodi hiyo ulifunguliwa. Mufti alipeleka jicho mlangoni akamuona yule Muuguzi wa kiume akirejea akiwa pamoja na Daktari, aliwapuuzia na aliendelea kuitoa ile sindano jambo lililowafanya wamkimbilie hadi pale kitandani na kumshika mikono yote kwa nguvu.

“Niacheni mie nikamfuate huyu mshenzi!” Alifoka kwa nguvu akiwa hafurukuti kwa jinsi alivyoshikiliwa kwa nguvu, Daktari na muuguzi huyo waliendelea kumshikilia Mufti kwa nguvu sana hadi alipotulia mwenyewe na kuacha kufanya fujo. Hapo walimuachia na wakabaki wakimtazama kwani machozi tayari yalikuwa yameshachukua nafasi yake machoni mwake, Mufti alianza kulia kwa muda mrefu kimyakimya na alipoacha kulia alimtazama Daktari aliyekuwa amekuja.

“Nahitaji kuongea na waandishi wa habari muda huu huu” Alimuambia Daktari huyo ambaye alikuwa akifahamiana naye sana na alikuwa ni Daktari ambaye ni rafiki yake mkubwa sana, Daktari huyo aliposikia kauli yake hiyo alimkubalia kwa kutikisa kichwa huku akimtazama Mufti kwa tabasamu hafifu.

YALIYOJIFICHA HADHARANI

Mnano saa moja jioni ndani ya wodi aliyokuwa amelazwa Mufti tayari ilikuwa na halaiki ndogo ya watu waliokuwa wameshika kamera na wengune wakiwa na vifaa vya kunasia sauti,wengine walikuwa na kalamu na karatasi wakinukuu kile kilichokuwa kikiongelewa hapo. Ilikuwa ni muda ambao Mufti aliamua mwenyewe kukiri kile alichokuwa kakisema kuwa ni uzushi na pia ni muda ambao alikuwa akikiri kuwa Rais Zuber hakuwa na hatia hata kidogo, aliamua mwenyewe kukubaliana na masharti ya Norbert ya kuamua kukiri makosa yake ili ainusuru familia yake ambayo ilikuwa ipo mikononi mwa Norbert aliyekuwa yupo kwa maslahi ya taifa zima na si kwa Maslahi ya mtu mmoja au kikundi kidogo cha watu waliokuwa wapo kinyume na matakwa ya taifa.

Udhaifu wake ndiyo uliokuwa umeshikiliwa na Norbert na hakuwa na ujanja mwingine wa kuuokoa udhaifu huo mikononi mwake zaidi tu ya kueleza kile kilichokuwa kinahitajika kujulikana na umma wa watanzania, uamuzi aliokuwa amefikia ni kukifikisha kitu hicho kwa umma wa watanzania ili ainusuru familia ambayo aliamini kabisa ilikuwa kwa mtu hatari ambaye alikuwa hana mzaha na kile alichokuwa akikifanya. Sifa za N001 ambazo amewahi kuzisikia kutoka kwa viongozi mbalimbali katika nchi za Afrika ya mashariki ndiyo zilimfanya azidi kuwa na hofu na familia yake, uwezo alionao N001 wa kumuondoa mtu ndani ya dakika kadhaa ndiyo ulimfanya awe na hofu zaidi na familia yake.

Hakuna mtu aliyekuwa hamjui mpelelezi huyo kila akitajiwa namba yake ya kipelelezi, wote walikuwa wakimjua vyema alikuwa ni mtu mwenye zaidi ya hatari akiwa kazini. Hata nje ya bara la Afrika mtu huyu walikuwa wakimjua ni nani ndiyo sembuse ndani ya bara hili asijulikane, kufikia mwaka huo tayari alikuwa ameingia katika wapalelezi bora wa dunia hii. Kile aliyekuwa akifungua katika tovuti ya umoja wa mataifa iliwaorodhesha wapelelezi hawa tayari alikuwa ameshamtambua huyu mpelelezi ingawa hakuwahi kuiona picha yake.

Ndani ya tovuti hiyo ilikuwa ikionekana kivuli sehemu ya picha na chini ya kivuli hicho ilionekana namba yake ya kipelelezi ndani ya EASA, haikuwa inajulikana yupo nchini gani kwa muda huo wala haikuwa inajulikana ni raia wa nchi gani. Sehemu ya kuonesha nchi anayotoka ndani ya tovuti hiyo kulikuwa kukionekana ukanda anaopatikana tu, hivyo haikuwa ikijulikana yupo nchi gani kati ya nchi tano za ukanda wa Afrika ya mashariki. Rekodi ya kazi yake bora ilikuwa imebaki kwenye vichwa vya watu ndani ya dunia hii waliopata kumsikia, tangu afanikishe kukamatwa kwa gaidi Brown Stockman ambaye alizishinda nchi nyingi za Ulaya na kutoroka aliweza kubaki kuwa katika rekodi hiyo ya wapelelezi bora wa dunia.

Sifa hizo alizokuwa nazo mtu aliyekuwa akimtambua kama N001 bila ya kumtambua jina lake kutokana na washirika wake kutomuweka wazi juu ya hilo kuwa wamemjua huyo mtu, zilimfanya akubali mwenyewe kukiri ubaya wake aliokuwa ameufanya kwa Rais Zuber. Washirika wake walikuwa wamemficha juu ya utambulisho wa huyo mtu kwakuwa hakuwa anajishughulisha zaidi kwenye mpango huo baada ya kazi ya kumchafua Rias Zuber tu itapokamilika, hivyo hakuwa amemjua Norbert Kaila ndiye huyohuyo aliyekuwa akimsumbua muda huo yupo kitandani katika wodi ya hospitali ya Aga khan. Tangu kuuawa kwa Akosfu Edson baada ya kufanya kosa kubwa yeye bila ya kutambua,viongozi wote wa dini waliokuwa kwenye mpango huo hawakuaminiwa tena. Ndiyo maana hata kwenye mipango mizito dhidi ya Norbert kwenye ngome ya Wilson wao hawakuwepo, walikuwa wakipewa mpango baadaye na L.J Ibrahim baada ya wote kuukubali mpango huo. Mufti katika mpango wa kina L.J Ibrahim alikuwa ni kama muwa tu na muda huo kazi yake ilikuwa imeisha baada ya kutiwa mdomoni na kutemwa, si yeye tu hata Askofu naye alikuwa hivyohivyo ni wa kutumika ingawa wote walikuwa wakijiona thamani yao katika mpango huo ilikuwa ni ya milele tu hata baada ya kupata mgao.

Akiwa mbele ya waandishi wa habari Mufti alijikohoza kusafisha koo lake kisha akatoa salamu kuwasalimia wanahabari hao pamoja na umma wa watanzania waliokuwa wakishuhudia moja kwa moja kile alichokuwa akikiongea muda huo, baada ya hapo alimshukuru Mungu kwa kuweza kumjalia ameweza kuzinduka kwa muda huo tangu alipopoteza fahamu. Aliongea mengi sana ya utangulizi asieleweke alikuwa anaongea nini lakini waandishi wa habari waliweka ustahimilivu wa kumsikiliza na pia kurusha kile alichokuwa akikiongea moja kwa moja, alitumia takribani dakika ishirini nzima katika kuongea ya utangulizi kisha akaamua kuingia kwenye dhamira ya kile kilichomfanya aamue kuongea na waandishi wa habari baada tu ya kupata na fahamu.

CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Wengi wa waandishi waliona ilikuwa ni wasaa mzuri wa kuongea na kiongozi huyo wa dini ambaye kupatwa kwake kwa mshtuko kuliitikisa jamii nzima ya kitanzania wakihofia alikuwa amekumbwa na kadhia nyingine kwa maneno aliyokuwa ameyatoa kwenye hotuba yake ya siku hiyo. Jamii ya watanzania walikuwa na hamu ya kusikia kile alichokuwa akitaka kukizungumza baada ya kuzinduka kwake kwa siku hiyo kwani tayari alikuwa ametokea kuwa kipenzi cha watanzania wa dini karibia zote ndani ya muda mfupi tu tangu kutolewa kwa hotuba yake, ilikuwa ni habari ambayo ilikuwa na soko kwa magazeti na hata kutazamwa na televisheni mbalimbali. Hivyo waandishi wa habari waojali habari zenye kuuza zaidi gazeti na kuongeza mamia ya watazamaji waliipa kipaumbele ndiyo maana walikuwepo hapo kwa muda huo.

“Allah (s.w) najua ndiye aliyenipa fahamu hizi ili niweze kutimiza kile nilichokuwa natakiwa nikitimize kwa umma huu wa watanzania, Sina budi nimshukuru zaidi na zaidi hata kama akinichukua kwa mara nyingine nitakuwa nimekamilisha kile nilichokuwa nahitajika kukikalimilisha ili watanzania waondokane na upofu huu niliowaweka na pia wawe wenye kuona nuru ilipo walikimbie giza na mawakala wake. Ndugu waislam na wale wasio waislamu nimekuwa wakala wa giza kwa kipindi kirefu sana na nikifanya yale yaliyokuwa yakienda kinyume na maamrisho ya Allah (s.w), leo hii nimeamua kuwa muwazi kwenu ili iwe funzo kwa viongozi wakubwa wa dini na pia waumini kuwa kila baya lina mwisho wake. Nimeshiriki katika njama nyingi katika kiongozi wa dini ikiwemo kuuza viwanja vya waislam kwa wawekezaji, kuwa upande mmoja na wale waliomuua viongozi wenzangu wa dini, mkuu wa majaeshi na pia. Nikiwa kama mwanadamu napasa kuwaomba radhi kwani nimekosea kama wanadamu wengine walivyokuwa wakikosea, nimechukua uongozi wa taasisi ya kiislamu na nimeikuta taasisi hiyo ikiwa na vitega uchumi vingi sana na hata maeneo yenye rasilimali chungu nzima ila niliviuza kwa maslahi binafsi na watu wachache ambao wapo serikalini na wengine watu maarufu Tanzania. Nilikuwa mtekelezaji mzuri sana wa yale niliyokuwa nikiwausia waumini wa dini ya kiislamu kutoyafanya, nikishirikiana na viongozi wengine wa dini hata kwa upande wa pili katika kuyafanya mambo kama hayo. Leo hii mabaya yangu yote hayo niliyokuwa nikiyafanya mwisho wake ni familia yangu kuingia hatiani, mke wangu na binti yangu” Mufti alisitisha kuongea baada machozi kumzidi kiwango na akayafuta, waandishi wa habari walikuwa wakisikitika sana kwa yale aliyokuwa akiyafanya, milango ya wodi yote ilikuwa wazi alipokuwa akitoa hotuba hiyo kutokana na uwepo waandishi wa habari wengi pamoja na wauguzi waliokuwa wapo sehemu ya mlangoni wakisikiliza maneno hayo ya Mufti.

“Kikubwa zaidi na kibaya nilichokifanya ni kusimama kwenye mimbari takatifu kutoa hotuba yenye uzushi katika eneo takatifu, kutumia imani za waumini juu yangu katika kuwaenezea uongo ambao waliuamini moja kwa moja ili tu serikali ya Rais aliyeleta maendeleo ndani ya nchi hii kuweza kupinduliwa na jeshi la wananchi wakiwa wameridhia kupitia kwetu sisi viongozi wa dini. Watanzania kwa ujumla napenda mtambue kuwa ndani ya siku mbili zijazo maneno niliyoyaongea yanapaswa yarudiwe tena yaleyale na Askofu mmoja maarufu hapa nchini ikiwa na yeye ni sehemu ya mpango wetu, pia tukaona haitoshi tukamsambazia uzushi Professa Moses Gawaza aliyeliletea taifa hili heshima kubwa kuwa ndiye muuaji wa Jeneral Augustin Kulika, wanajeshi wa JWTZ waliokuwa nyumbani kwake na Askofu Edson ambaye alikuwa mwenzetu. Kutokana na uzushi huu tuliokuwa tumemuwekea Professa tumemfanya aweze kuishi kama digidigi akikwepa mkono wa dola yote ni kutokana na ukaribu wake na Mheshimiwa Rias, tulijali tu pesa wala si kujali kile kilichokuwa kikiwaumiza wao kwa tuhuma hizi za kizushi. Najua nimepatiwa pumzi hii kwa muda mchache tu niweze kuwatoa tongotongo macho watanzania wote ili waweze kuona kiufasaha kile kilichokuwa kinahitajika kukiona, uzito wa mambo haya ninayoyaongea sidhani kama nitaweza kuiona siku ya kesho labda muweza wa yote aaamue hivyo na si vinginevyo”. Mufti aliongea na alipofikia hapo alisita kwa mara ya pili na akachukua bilauri ya maji na akanywa mafunda kadhaa huku akihema kwa kasi.


MASAKI

Saa moja jioni ikiwa inakaribia Mwanaume mmoja mtu mzima alikuwa amekaa kwenye kochi sebuleni akiangalia taarifa ya habari katika kituo cha televisheni cha BBC cha nchini Uingereza kujua kile kilichojiri huko nje ya bara la Afrika, mwanaume huyu tayari alikuwa na habari ya kile kilichotokea mchana wa siku hiyo na hadi taarifa ya kulazwa kwa Mufti. Hakuwa na habari kabisa ya kuitishwa mkutano wa waandishi wa habari na Mufti huyo baada ya kuzinduka kwake ambayo ilikuwa imebaki muda mfupi iweze kuanza, akiwa yupo na bilauri ya Shurubati mkononi alikuwa akifuatilia kwa umakini sana juu ya kile kilichokuwa kikiendelea kwenye kituo cha BBC. Macho yake alikuwa ameyaelekeza kwenye televisheni wala hakutilia maanani hata mke wake alipokuja kukaa pembeni yake akiwa anamtazama yeye usoni, Mwanaume huyu aliendelea kuangalia televisheni kutokana na kuvutiwa sana. Mwanamke huyo alipoona mume wake hamuangalii aliamua kumuwekea mkono begani mwake na kupelekea mume wake huyo ageuke na kumtazama.

“Mume wangu jamani huoni kama saa moja ndiyo hiyo inakaribia” Mwanamke huyo alimuambia mume wake.

“Saa moja hii kuna nini mama Salma”

“Jamani hujui kama Mufti ameitisha waandshi wa habari habari baada ya kuzinduka na anaongea live”

“Ohhh! Kuna la muhimu labda hebu weka tuangalie” Mwanume huyo aliongea huku akimpatia mke wake rimoti ya luninga, Mwanamke huyo kwa haraka zaidi aliibadilisha chaneli aliyokuwa akiitazama mume wake hadi wakafikia chaneli ya kitanzania ambayo ilikuwa ikikua kwa kasi sana ambayo ndiyo iliku inaonesha tukio hilo muhimu. Tayari neno live lilikuwa limeshaonekana kwenye kioo cha luninga yao na vipaza sauti mbalimbali vilikuwa vipo mbele ya kitanda cha hospitali mbele ya Mufti ambaye alikuwa amevaa mavazi maalum ya hospitali. Wote kwa pamoja waliweka macho yao kwenye televisheni kuangalia kile kilichokuwa kikiendelea kwa muda huo, mnamo saa moja kamili Mufti alianza kuongea na wao wakawa wanafuatilia kwa umakini sana muda wote aliokuwa akiongea utangulizi wa maongezi yake kabla hajaingia moja kwa moja kwenye kiini cha jamo alilokuwa akilitaka kuliongea.

“Mufti naye anatia siasa si aongee kama ana jipya nahisi huyu alitaka tu watanzania wamjue kama yupo hai hamna jingine lolote” Mwanaume huyo aliongea akionekana kutopendezwa na utangulizi wa Mufti.

“Jamani mume wangu si utulie kidogo tu aongee hadi amalize ndiyo useme hivyo” Mwanamke huyo alimtuliza mume wake.

“Hapa hakuna la maana naona kuna….” Mwanaume aliendelea kukosoa kile kilichomfanya Mufti aitishe waandishi wa habari lakini mke wake alimzuia baada ya Mufti kuanza kuomba radhi kabla hajaanza kupasua jipu ili watanzania waondokane na damu chafu iliyokuwa imejificha ndani ya jipu hilo, alipoanza kueleza juu ya uovu wake alioufanya mwaaume huyo alitulia kimya mwenyewe na akasikiliza kwa umakini sana. Alipofika katika eneo ambalo Mufti alikuwa amefichua mengi sana aliyokuwa hayafahamu uvumilivu wa kuendelea kusikiliza ulimshinda, alijikuta akisimama kwa haraka kisha akatoa simu yake mkononi na akatafuta sehemu ya majina kwenye simu yake hadi alipolipata jina ambalo alikuwa akilitafuta akapiga. Alisubiri simu hiyo ikiita na wala hakuwa ameweka macho yake kwenye televisheni tena, simu aliyokuwa anapiga iliita kwa muda mrefu sana jambo ambalo lilimfanya atembee hapo sebuleni kwake kama vile amewehuka akisubiria simu yake iweze kupokelewa na mtu aliyekuwa anampigia kwa muda huo. Mtetemo wa simu yake ya mkononi baada ya kupokelewa ulilitetemesha kidogo shavu lake, hapo mtu huyo alibaini kuwa simu hiyo ilikuwa imepokelewa na mtu aliyekuwa akimpigia.

“John upo wapi sasa hivi……sasa ondoka nyumbani kwako sasa hivi ukiwa na pingu…..nahitaji sasa hivi uende Aga khan hakikisha Mufti unamtia nguvuni na anakuwa yupo chini ya ulinzi akimaliza tu maongezi hayo…..wahi haraka sana nahisi maisha yake yako hatarini na tukimkosa yey basi tutakuwa tumekosa shahidi mzuri wa juu ya mabaya walizofanya” Mwanaume huyo aliongea kisha akakata simu kwa haraka na akarudi kuketi kwenye kochi jirani na mkewe akiangalia luninga. Aliendelea kusikiliza mazito yaliyokuwa yamefichika ambayo Mufti alikuwa akiyafichua wa muda huo, akiwa anaendelea kuangalia kile kilichokuwa kikiendelea kwenye luninga jambo la ghafla ambalo lilimuacha mdomo wazi alilishuhudia likitokea hapo kwenye luninga. Jmabo hilo hakutarajia kabisa kama lingetokea katika eneo kama hilo, Mwanaume huyo alinyanyuka kwenye kochi kwa ghafla na mikono akaweka kichwani baada ya kulishuhudia jambo hilo. Si pekee aliyeshangazwa na jambo lile lililotokea bali hata mke wake naye lilimshangaza sana kutokea kwenye mazingira kama hayo, mke wake alibaki akiwa ameweka viganja vya mikono yake mdomoni baada ya kushuhudia kile kilichokuwa kimetokea muda huo.

“Kostebooo!” Mzee huyo aliita kwa nguvu baada ya kushuhudia kile ambacho kilikuwa kimetokea hapo kwenye luninga, haikupita dakika moja askari wa jeshi la polisi mwenye V moja begani aliingia kwa haraka hadi sebuleni hapo akapiga saluti.

“Afande” Aliitikia Askari huyo mwenye cheo cha kostebo

“Tayarisha gari haraka sana tunaenda Aga khan sasa hivi” Alitoa amri

“Afande” Askari huyo aliitika kwa haraka sana kisha akatoka nje, mwanaume huyo naye hakuchelewa aliondoka sebuleni hapo aliingia ndani ambapo alikaa kwa daika kadhaa na alipotoka alikuwa amevaa nguo nyingine tofauti na alizokuwa nazo hapo awali.

“Mke wangu natoka mara moja naenda huko mwenyewe” Alimuambia mke wake

“si ungeagiza vijana wako mume wangu haina haja ya kwenda”

“No inabidi niende mwenyewe hii ishu si ndogo, kuwa IGP haimaanishi ndiyo kila kitu nitume tu”

“mmh! Sawa baadaye basi, kuwa mwangalifu”

“Usihofu kuhusu hilo” Alimtoa hofu kisha akatoka sebuleni hapo kwa kasi sana kuelekea ulipo mlango wa kutokea nje, hakuwa mwingine ila ni mkuu wa jeshi la polisi nchini IGP Rashid Chulanga kwa mara nyingine anaamua kwenda kushuhudia kile alichokuwa amekiona kwenye luninga ambacho hakutarajia kama kitatokea muda huo.


“Ninaomba radhi kwa hili niilolifanya kwa watanzania wote, nimewafanya wasiwe na imani na kiongzi wao kisa tu mapinduzi ya jeshi yaweze kutokea kama ambavyo nilivyokuwa nimepewa kazi hiyo na mshirika wangu ambaye kwa sasa ndiye kiongozi wa jeshi ndani ya nchi hii. Chanzo cha yote hayo hadi kutaka kuondolewa madarakani kwa Rias wetu mpendwa ni ndoa ya jinsia moja, ndugu watanzania wote napenda mfahamu kuwa rais wetu aligomea kusaini mkataba huu ambao alikuwa alipwe pesa nyingi sana ambazo zimezidi hata utajiri wote wa baadhi ya matajiri hapa nchini Tanzania. Mapenzi yake na uzalendo wake ndiyo vimechangia asiweze kukubali kuleta jambo hili nchini, kukataa kwake huku kumesababisha watu hawa ambao walikuwa wakitaka lihalalishwe wale njama na sisi pamoja na waziri mmojawapo wa serikali anayeitwa….” Mufti hakumalizia kulitaja jina la hiyo kwani mshtuko mkubwa sana ulikumba kifua chake na mdomo wake ukabaki kuwa wazi kama alikuwa amebanwa na pumu kali, eneo la kifuani mwake kulionekana damu ikitifuka kwa nguvu. Aliangukia mto uliokuwa nyuma yake kwa taraitibu na akawa ana hema kwa tabu sana, tukio hilo lilishuhudiwa na waandishi wa habari ambao walikuwa wapo hapo kwenye wodi hiyo wakisikiliza maneno yake.

Haikuhitaji elimu ya ziada kutambua kuwa alikuwa amepigwa risasi ya kifua na silaha iliyotumika ilikuwa imewekwa kiwambo cha kuzuia sauti ndiyo maana haikusikika sauti pindi mfyatuaji wake alipoipa ruhusa ya kutoka nje ya bomba lake. Kilichofuata baada ya hapo ilikuwa ni mvurugano wa watu waliokuwa eneo hilo kukimbia baada ya kushudia tukio hilo, waandishi wa habari hasa wa kike pamoja na wauguzi waliokuwa wapo karibu na eneo hilo walitoa mayowe ya uoga na wote walikimbia ndani ya chumba hicho huku waandishi wa habari wa kiume wenye mioyo ya ujasiri pekee wakawa wamebaki humo ndani wakipiga picha tukio zima lilitokea.

Muda huo ndiyo IGP Chulanga alishuhudia katika luninga nyumbani kwake kupigwa risasi huko kwa Mufti hadi akanyanyuka kwenye kochi, tukio hilo ndiyo lilimfanya afunge safari kwenda kwenye hospitali hiyo mwenyewe ingawa alikuwa amemtuma afisa wa chini yake aende. Karibu watanzani nchi nzima waliokuwa wakitumia luninga walikuwa wakishuhudia jambo hilo lilivyotokea huku wachache wasiotumia luninga walikuwa wakisikiliza kupitia redio ambapo walilisikia suala lote lililotokea huko wodini alipokuwa amelazwa Mufti. Chuki dhidi ya L.J Ibrahim akiwa ni mtu pekee aliyetajwa kwenye mpango ndiyo zilijengeka katika mioyo yao, wengi wao walisikitika sana walipogundua kuwa walikuwa wakimuhukumu asiye na hatia na hata kumtilia uharibifu yule ambaye hakuwa na hatia.

Mufti kupigwa risasi katika muda mbao alikuwa akimtaja mmoja wa mawaziri waliopo chini ya baraza la mawaziri ambalo linaongozwa na Rais Zuber alikuwa yupo katika usaliti huo, suala hilo lilichukua sura yake nyingine kabisa katika vyombo vya habari vya kawaida na hata mitandao ya kijamii baada ya kusemwa na Mufti ambaye hakulimalizia kwani risasi ilipenya kwenye kifua chake ambayo ilitosha kabisa kumfanya asiendelee kuongelea suala hilo na pia kuwatawanyisha wanahabari waliokuwa wapo eneo hilo. Kupigwa risasi kwa Mufti akizungumza suala hilo ilikuwa ni kuaminisha kabisa umma wa watanzania kuwa alikuwa akiongea ukweli, wananchi moja kwa moja waliamini kuwa Mufti alikuwa ameongea ukweli ambao ulikuwa unaelekea mahala pabaya kama Mufti angeendelea kuongea na kuzuia kuendelea kuwaweka pabaya wahusika ndiyo risasi ikatumika kumnyamazisha.

Hadi DCP John anawasili ndani ya eneo hilo la hospitali tayari baadhi ya askari wajeshi la polisi walikuwa wameshawasili hapo, Mufti alikuwa tayari amekimbizwa chumba cha upasuaji ili waweze kuyaokoa maisha yake baada ya kubainika bado alikuwa akipumua kwa shida. Alikuta maaskari wakiwa wameweka utepe maalum katika eneo ambalo Mufti alikuwa amepigwa risasi kuzuia watu wasiingie na ulinzi wa hospitali hiyo ulikuwa umeimarishwa na maaskari hao huku msako wa mtuhumiwa ukiendelea. DCP John alipokea saliuti kutoka kwa maaskari tofauti ambapo aliingia moja kwa moja hadi kwenye wodi aliyokuwa amelazwa Mufti, alitazama mazingira yote yaliyokuwa yapo hapo ndani kwa umakini mkubwa sana akabaini uwepo wa kamera ya ulinzi. Alipoiona kamera hiyo alitoka moja kwa moja ndani ya wodi hiyo kwa haraka sana akaeleka mapokezi katika hospitali hiyo, alitumia dakika mbili kutoka wodi aliyokuwa amelazwa Mufti hadi mapokezi akawa amefika kutokana na umbali uliopo.

Alipofika hapo mapokezi DCP John akiwa yupo ndani ya mavazi ya kiraia alitoa kitambulisho cha kazi na akajitambulisha halafu akasema, “nahitaji kuonana na mhusika wa chumba cha kuongozea CCTV kamera sasa hivi”

“Sawa afande subiri niwape taarifa” Msichana aliyekuwa mapokezzi aliongea

“what?! Hebu nyanyuka hapo na unipeleke haraka sana kwani hawajui uwepo wa askari eneo hili” DCP John alimjia juu Msichana huyo aliyekuwa amevaa mavazi ya kiuguzi

“Lakini ndiyo utaratibu wetu jamani” Muuguzi huyo aliongea kujitetea

“Binti hebu nitolee upuuzi unajua nipo kazini hapa, toka uongoze njia unanipotezea muda kama mtuhumiwa yupo ndani ya hiii ya hospitali si atatoroka hadi muda huo!”

“Lakini..”

“Shut up usinifundishe kazi eti nisubiri nasema toka hapo kwenye desk la receiption uniongoze kabla sijamuita Daktari mkuu wa hii wa hospitali, unampangia Kamishna msaidizi kazi ya kufanya binti siyo. Sirudii tena kukuambia nauliza hivi tunaenda au hatuendi?”

“Sawa nakupeleka”

“Haya ongoza njia haraka sana”

Yule Muuguzi hakuleta pingamizi zaidi aliamua kumpeleka DCP John kule alipokuwa akitakiwa kwenda kwa muda huo akaendelee na uchunguzi wake juu ya balaa lililomtokea hapo hospitalini, tayari alikuwa anajua alikuwa amemtibua DCP John kwa muda huo ndiyo maana alikubali mwenyewe kufuata kile alichokuwa akikitaka kwa muda huo. Mawazo yake DCP John alikuwa ni polisi wa kawaida ndiyo maana hata alifikia hatua ya kujifanya anamuelewesha pale alipokuwa amempa amri, kujitambulisha kwa DCP John bila kumtajia cheo chake ndiyo jambo ambalo lilimfanya aamini DCP John alikuwa ni askari wa kawada tu hata alipomuonesha kitambulisho kilichokuwa kimekamilika kimaelezo hakuwa na muda wa kukikagua kabisa aliamini alikuwa akiongea na askari wa kawaida tu. Hata alipotajiwa cheo baada ya kuwa amemkasirisha bado hakuwa akiamini kutokana na umri aliokuwa nao DCP John kuwa na cheo hicho, alizoea kuona Makamishna na makamishna wasaidizi wa jeshi la polisi wakiwa ni watu wazima si kama alivyokuwa akimuona DCP John kwa muda huo.

Walipokuwa wakielekea hicho chumba chenye mitambo ya kuongozea kamera ndiyo walianza kuamini kuwa kile kilichokuwa kikielezwa na DCP John ilikuwa ni kweli tupu kwani maaskari kila alipokuwa wakipita walikuwa wakimpigia saluti DCP John hata wale waliokuwa na nyota mabegani mwao jambo ambalo lilimfanya Muuguzi huyo azidi kuwa na hofu kwa kujifanya muongeaji sana na hata kitambulisho cha DCP John kutokitazma kwa ufasaha. Alikuwa akimpeleka DCP John huku akiwa na hofu ndani ya moyo wake kutokana na hasira alizokuwa amemuonesha pale mapokezi wakati akimuambia kuhusu jambo hilo, baada ya muda wa dakika kadhaa walikuwa tayari wameshafika kwenye mlango wa chumba cha kuongozea kamera ambao ulikuwa na kengele maalum mlangoni. Muuguzi huyo aliibonyeza kengele hiyo na haikupita muda mlango wa chumba hicho ulifunguliwa, alitoka kijana aliyekuwa amevaa mavazi ya walinzi wa hospitali hiyo ambapo alitoa tabasamu tu alipomuona DCP John katika eneo hilo.

“Karibu Afande” Kijana huyo alimkaribisha

“Asante, nahitaji kulijua jina lako “ DCP John aliiitikia ukaribisho kasha akaomba kulijua jina la huyo kijana aliyemkaribisha katika eneo hillo, muda huohuo Yule Muuguzi baada ya kumfikisha katika eneo hilo alianza kuondoka akijua tayari yalikuwa yameshaisha.

“Wee! Unakwenda wapi bado hayajakwisha haya, leo hii mpaka kwenye uongozi wa hospitali hii ndiyo yatakuwa yameisha subiri hapa” DCP John alimuambia Muuuguzi huyo ambaye alizidi kuingiwa na hofu zaidi

“Afande naitwa Godwin ndiyo mhusika mkuu wa chumba hiki cha kuongezea kamera katika hospitali hii, vipi afande huyu dada yetu kakufanyaje?” Kijana huyo alijitambulisha kisha akauliza kuhusu huyo muuguzi ambaye hadi muda huo tayari machozi yalianza kumlenga akifikiria kupelekwa kwenye uongozi wa juu wa hospitali hiyo.

“Huyu hana adabu anachelewesha kazi, atasubiri hapa mpaka tutoke humo ndani nitakapomalizana na wewe. Tunaweza kuingia ndani nahitaji kujua kila kitu kilichokuwa kikiendelea kabla ya tukio hili” DCP John aliongea na Godwin alikubali kuingia naye ndani huku Yule Muuguzi akiwa amebaki mlangoni akiwa na uoga wa kupoteza kibarua chake mbele ya Askari ambaye aliamini kabisa alikuwa na jazba ya kucheleweshwa kile alichokuwa akikihitaji. Binti Yule aliendelea kusubiri pale akijua kuwa kazi ilikuwa imeisha lakini baada ya dakika moja tu DCP John alitoka nje akamkuta binti huyo tayari machozi yalikuwa yanamtoka kwa kuhofia kupoteza kibarua chake, alipomuona DCP John alimtazama kwa huruma sana akitarajia huruma hiyo itaweza kumshawishi DCP John aweze kumsamehe asimpeleke kule alipokuwa akitarajia kumpelekea kwa muda ambao atakuwa tayari ameshamalizana na kijana wa chumba cha kuongozea kamera.

“Binti” DCP John aliongea alipotoka nje ya chumba hicho huku akimtazama Yule Muuguzi ambaye alinyanyua kichwa chake akamtazama DCP John aliposikia kuiitwa kwake na afisa huyo wa ngazi ya juu katika jeshi la polisi.

“Nenda mapokezi binti kutokea kwa tukio hili si kwamba huduma za hospitali zimesimama kumbuka kuna mamia ya wagonjwa wanawasili ndani ya hospitali hii mapokezi panahitaji mtu” DCP John alimuambia.

“Afande nisamehe niko chini ya miguu yako” Muuguzi huyo aliongea huku akilia akijaribu kumpigia magoti DCP John lakini alizuiwa.

“Haina haja binti mimi kaendelee na kazi ila nidhamu uwe nayo unapokuwa kazini binti na uendane na mazingira yalivyo si kujifanya unajua kila kitu kuhusu kazi ya mtu, nikiharibu kazi lawama pia kwangu” DCP John aliongea kwa upole tofauti na alivyokuwa na ukali kama alivyokuwa akiongea hapo awali alipofika kwenye mapokezi ya hospitali hiyo, Muuguzi alionekana kutoamini kutokana na imani aliyokuwa nayo juu ya polisi wakiwa wana hasira kuwa ni watu ambao kusamehe ni ngumu sana. Alibaki akiwa ana mshangao asiamini kile alichokuwa ameambiwa na DCP John kwa muda huo na hata tabasamu hafifu lilianza kuonekana katika uso wake alipoambiwa maneno hayo, alimshangaa tu DCP John kwa maneno yake aliyokuwa ameyaongea ndani ya muda ambao alikuwa akitarajia kufukuzwa kazi yake aliyokuwa akiitegemea.

“Nidhamu ni muhimu binti izingatie sana, siwezi kukufanya ufukuzwe kazi kwakuwa najua ndiyo msingi wako wa maisha hivyo usiwafanye wengine wakaharibu kazi zao kwa kufanya kazi vile ulivyokuwa ukitaka wewe ni mbaya sana hiyo kwani wana hofu ya kuharibiwa kazi kama ulivyokuwa nayo wewe. Unangoja nini nenda sasa ukaendelee na kazi au nikupeleke uongozi wa juu kwa kukaa hapa huko mapokezi hamna mtu” DCP John aliongea maneno hayo huku akimtazama Muuuguzi huyo kwa uso wa upole sana, Muuguzi huyo bado hakuwa ameondoka alibaki akimshangaa Dcp John. DCP John aliamua kumkazia macho na kumpa mkwara wa kimsihara ambao ulifanya Muuguzi huyo wa kike atabasamu kisha akageuka akimuacha DCP John naye akiwa anatabasamu kisha akasikitika baada ya Muuguzi huyo kuanza kuondoka, baada ya Muuguzi huyo kuondoka DCP John aliingia ndani ya chumba cha kuongozea kamera kwa mara nyingine.


MUDA MFUPI KABLA

Hata kabla hotuba mkutano na waandishi wa habari na Mufti haujaanza ndani ya hospitali ya Aga Khan tayari Josephine alikuwa ameshawasili ndani ya hospitali hiyo akiwa na kitambulisho cha wauguzi wa hospitali hiyo, aliingia hadi ndani kabisa katika vyumba vya wauguzi wa hoospitali hiyo na akabadili nguo alizokuja nazo akavaa nguo nguo za wauguzi wa hospitali hiyo ambapo katika sare yake hiyo alivaa ni mfumo wa suruali ambayo ilifanya umbo lake lionekane vyema na hata aliivaa hiyo ili aweze kuwa na wasaa mzuri wa kufanya kazi ambayo ilikuwa imemleta mahali hapo. Kichwani alikuwa amevaa wigi ambalo lilikuwa limembadilisha kabisa na asitambulike kwa urahisi na mtu yeyote aliyekuwa akifahamiana naye kama akikutana naye katika maeneo hayo, usoni alikuwa amevaa miwani ya plastiki ambayo haikuwa na tofauti kabisa na miwani za wenye matatizo ya macho ambayo ilimfanya azidi kuonekana na muonekano tofauti kabisa.

Baada ya kuvaa hivyo Josephine hakucheza mbali kabisa na maeneo ya karibu na wodi ambayo alikuwa amelazwa Mufti akiwa na lengo moja tu la kumuangamiza Mufti ikiwa atatoa siri za mpango wao uliokuwa upo mbioni kutimia, alikaa katika eneo hilo akiwa yupo tayari kukabiliana na hali yoyote itakayokuwa imejitokeza katika eneo hilo la hospitali kwa muda huo ilimradi tu Mufti aende kaburini akiwa ametoa siri za mpango wao uliokuwa unampa ulaji. Muda ambao waandishi wa habari walikuwa wakiingia ndani ya hospitali hiyo kwa lengo la kuitikia wito wa Mufti wa kuzungumza nao kwa jioni hiyo, tayari alikuwa ameshajisogeza jirani kabisa na wodi hiyo lakini kutokana na watu waliokuwa wapo humo ndani alikosa kabisa nafasi ya kumuua Mufti. Alikaa kwenye kundi la wauguzi ambao waliokuwa wamesogea karibu na wodi hiyo kusikiliza kile ambacho alikuwa akikiongelea Mufti, uwepo wa waandishi wa habari uliwavuta zaidi wauguzi wa hospitali hiyo kusikiliza kile alichokuwa akikiongea Mufti kwa muda huo aliokuwa amewaita hapo. Wauguzi hao walijazana mahala hapo ndiyo walikuwa wametoa kichaka kizuri ambacho kilimvutia huyo malikia wa chui(Leopard Queen) kama alivyokuwa akijiita akiwa katika kazi hizo, wakati waandishi wa habari wakitayarisha kamera zao kawa ajili ya kufanya mahojiano na Mufti yeye alikuwa akifikiria tu namna ya kupenya katika kundi la watu hao na kumuua Mufti pasipo kugundulika na mtu yeyote aliyekuwa yupo katika eneo hilo. Akiwa anayafikiria masuala hayo simu yake iliingia ujumbe mfupi wa maneno ambao ulimfanya kusogea pembeni na kuusoma ujumbe huo, hakuwa tayari kuusoma ujumbe huo akiwa katikati ya kundi la wauguzi hao wa kike kwani alikuwa akitambua kabisa tabia ya wanawake ya kutia jicho katika mahali ambapo palikuwa hapawahusu hivyo alihofia kujikaanga mapema kwa mafuta ya mwili wake mwenyewe mithili ya kondoo.

“Shosti shem nini huyo” Mmoja wa wauguzi alimuuliza akijua ni mwenzao katika hospitali hiyo, Josephine alimtazama kisha akaachia tabasamu jambo ambalo lilifanya kundi hilo la wauguzi kumcheka kimyakimya wakijua alikuwa amewakimbia ili kuwasiliana na mpenzi wake na aliogopa kuwasiliana naye akiwa yupo katikati yao.

“Hapana chezea mzee wewe utaenda kujificha mwenyewe uchat naye” Muuguzi mwingine alidakia kwa sauti ya wastani huku akiusindikiza mzigo wa Josephine uliokuwa ukileta fujo alipokuwa akiwahi kwenda kujibu ujumbe mfupi ambao ulikuwa umeingia kwenye simu ambao alikuwa akiamini kabisa ulikuwa ukitoka kwa Wilson.

Alipofika kwenye kona moja ya kumbi nyembamba(korido) za hospitali hiyo kusipokuwa na mtu aliitoa simu hiyo na kuusoma ujumbe ambao ulikuwa umeandikwa, ‘tayari nipo ndani nimevaa kofia ya cowboy nimebeba kamera kubwa ya kizamani Mufti ni asusa yangu ikiwa atatoa siri hivyo niachie mimi huyo’

Alipomaliza kuusoma ujumbe huo alitoa tabasamu hafifu kisha akaifunga simu yake ya kisasa kwa kubonyeza kitufe cha kuzima mara moja na kupelekea mchoro wa siri ujiweke kwenye kioo cha simu hiyo, baada ya hapo alirudi kule alipokuwa amekaa na wauguzi wenzake akatulia akiwa kama msikilizaji wa kile alichokuwa anataka kukiongea Mufti. Maneno ya Mufti yalipoanza alitulia kimya akiwa anasikiliza kile kilichokuwa kikitarajiwa kuzngumzwa na Mufti baada ya kuamka huko, kundi la wauguzi wenzake walikuwa wakidhani kuwa Mufti alikuwa akieleza kukumbwa na balaa lililomfanya apoteze fahamu. Walikuwa wakitarajia angezidi kuwaumbua wabaya wake ambao alikuwa amewataja hapo awalina kuwashutumu kuwa ndiyo chanzo cha kifo hiko, alipoanza kuongea walivumilia na kumsikiliza hata kwa maneno ya lugha ya kiarabu aliyokuwa akiyatumia kwenye utangulizi wa hotuba yake hadi akaingia kwenye maneno ya lugha ya kiswahili. Alipoanza kukiri uovu wake wengi wa wauguzi hao waliweka viganja vya mikono yao kwenye vichwa vyao kwa kutoamini walipokuwa wakisikia maneno hayo, walijuta hata kumpa huduma mtu kama huyo aliyekuwa akifanya mambo mabaya kama hayo ambayo alikuwa ameyakiri mwenyewe mbele ya vyombo vya habari. Maneno hayo yalipofikia hapo simu ya Josephine iliita ambapo ilimlazimu anyanyke aende kwenye eneo alilokuwa awali wakati anaenda kusoma ujumbe mfupi wa maneno ulioingia kwenye simu yake, alipofika kwenye eneo hlo aliipokea simu yake kisha akatoa kitambaa akakiweka jirani na mdomo wake.

“Ndiyo mheshimiwa…..ndiyo tupo ndani ya hospitali….sawa mheshimiwa ngoja nimuambie Wilson aliyekuwa ndani…..sawa”Simu ilikatwa na Josephine alifungua sehemu ya majina kwenye simu yake akaitafuta namba ya Wilson kisha akaipiga na akaiweka simu sikioni kuisikiliza ilivyokuwa ikiunganisha hadi ilipoaanza kuita.

“Maliza kazi Mheshimiwa kashacharuka” Aliongea baada ya simu kupokelewa kisha akakata simu baada ya kumaliza kuongea na akairudisha simu kwenye mfuko wa suruali yake ya kitabibu, alirudi katika eneo alilokuwa amekaa hapo awali pamoja na wauguzi wengine wa hospitali hiyo

<><><><><><><><><><><><>><><>

Baada ya Wilson kupigiwa simu na Josephine ilikuwa inamsihi amalize kazi iliyokuwa imemleta ndani ya eneo hilo, alishikilia kamera ya kubwa na ya kizamani aliyokuwa amekuja nayo humo ndani kisha akaweka jicho sehemu ya kuweka jicho wakati anachukua mkanda. Alikuwa amebeba kamera ambayo yalikuwa yakitumika kipindi cha nyuma sana kwenye baadhi ya vituo vya televisheni nchini, alipokuwa ameweka jicho ndani ya kamera hiyo kila mtu aliyekuwa yupo karibu yake alidhania alikuwa akichukua mkanda wa video kwa ufasaha katika kamera hiyo ambayo ilikuwa imewekwa kwenye misimamio(stand) yake. Jambo ambalo hawakutambua ni kuwa ndani ya kamea hiyo kulikuwa na mashine kweli ya kuchukua mkanda lakini pia kulikuwa na silaha inayotumia risasi ndogo kama bastola za kawaida, tundu la kutolea risasi hiyo lilikuwa lipo juu ya lensi ya kamera hiyo na muda huo aliokuwa akiweka chini kwenye kamera hiyo alikuwa akimlenga Mufti kwa kutumia silaha hiyo. Baada ya kuhakikisha kuwa Mufti alikuwa yupo kwenye usawa wa tundu la risasi alishikilia mshikio ambao ulikuwa upo chini ya kamera hiyo, aliuvuta mshikio huo kwa taratibu na risasi ilitoka na ikaenda kumpata Mufti kwenye kifuo chake moja kwa moja. Ulipokuwa ukitokea mparanyiko wa watu wakijua wamevamiwa ili wanusuru maisha yao yeye aliichomoa kamera yake kwenye kisimamio na kuutoa waya wa kipaza sauti kwa haraka na kuushika mkanda wa kuivaa begani akaivaa kisha akajichanganya na waandishi wa habari wengine kukimbia kuelekea nje ya hospitali hiyo. Alifanikiwa kutoka nje ya hospitali bila kutiliwa shaka lakini alipokuwa huko nje alipokuwa akielekea ndiyo shaka ilikuwa zaidi.

Kitenda cha kutoka nje ya hospitali hiyo akijifanya anakimbia kuokoa maisha yake hakujua kabisa muonekano wake ulikuwa umeshamtia shaka Norbert ambaye tayari alikuwa ameshafika katika hospitali hiyo tangu Mufti akiwa anaaanza kutoa maelezo yale. Norbert hakuwa ameingia ndani ya hospitali hiyo bado alikuwa yupo nje ya hadi Mufti alipopigwa na risasi, taarifa za kupigwa risasi kwa Mufti alikuwa ameshazipata kutoka kwa Eva ambaye alikuwa yupo ndani. Wilson alipotoka akiwa katika muonekano wake wa kiutuzima pamoja na kamera yake kubwa ambayo hakuwa ameiacha, hapo ndipo Norbert alikuwa amemtilia shaka na alianza kumfuatilia shaka Wilson ambaye bado hakumjua kama alikuwa ni Wilson huyo. Wilson alionekana kukimbia mbio sana lakini Norbert naye akiwa amevaa kofia iliyokuwa imeufunika uso wake alikuwa akitimua mbio sawa na yeye na alikuwa anamfuatilia kwa kasi ya kawaida. Wilson alikuwa akikimbia kwa kasi huku akiishikilia kamera yake isiweze kuanguka , alikuwa akiifuata barabara ya Sea view baada ya kuyavuka makutano ya barabara ya Obama, Sea view na barabara ya Ufukoni. Hakuwa akiangalia nyuma kabisa yeye alikuwa akitimua mbio hadi alipofika kwenye shule ya msingi Almutazir iliyopo pembezoni mwa barabara ya Sea view ndiyo akakumbuka kuangalia nyuma kuona kama alikuwa anafuatiliwa, alipoangalia nyuma hakubahatika kumuona yeyote aliyekuwa akimfuatilia kwani Norbert alishawahi kujibana kwenye mti uliopo pembezoni mwa barabara. Hapo Wilson aliendelea kukimbia kama kawaida akiwa anaivuka shule ya msingi Almutazir hadi akafika mbele kidogo ambapo alivua kofia aliyokuwa amevaa akaitupa kisha akangalia tena nyuma, Norbert aliwahi kubana kwa mara nyingine kwenye gari ambalo lilikuwa limeegeshwa pembezoni mwa barabara. Wilson alipoona haoni mtu alivuka barabara akawa anaelekea ufukweni akiwa yupo huru kabisa akijua kuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa akimfuatilia kwa muda huo, alipovuka barabara alikuwa yupo karibu kabisa na ufukwe wa bahari katika eneo lenye mwanga hafifu kabisa pamoja na nyasi fupi zilizopo mita kadhaa kutoka ulipo mchanga wa ufukweni mwa bahari. Norbert alikaza mwendo katika kumsogelea Wilson pasipo yeye mwenyewe kujua kama alikuwa akisogelewa na mtu kama huyo mwenye kila aina ya hatari akiwa yupo katik kazi yake hiyo ya upelelezi, Norbert alimpofika kabisa Wilson kwa nyuma alimshika begani kisha akaavua kofia. Wilson aligeuka kwa haraka baada ya kushikwa begani na Norbert na kwa msaada wa mwangaza hafifu wa eneo hilo aliweza kumtambua kabisa alikuwa ni Norbert huyo aliyekuwa amemgusa begani, Norbert pia aliweza kutambua kuwa aliyekuwa ametoka ndani ya hospitali ile akiwa kama mwandishhi wa habari alikuwa ni Wilson ambaye ndiyo yupo mbele yake kwa hatua tatu tu.

“Oooh!” Damn!” Wilson aliongea kwa mshangao uliochangayika na hofu baada ya kumuona Norbert maeneo hayo katika muda ambao hakutarajia kukutana naye tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wenzake kama alivyokuwa akikutana naye hapo awali, aliona hatari kubwa ilikuwa ipo mbele yake ila hakutaka kujileta kijinga mbele ya mtu hatari kama huyo ambaye yupo kazini kuhakikisha mpango wao unaharibika, kitendo cha haraka alichokifanya Wilson baada ya hapo ilikuwa ni kumrushia Norbert kamera yake ambayo ndani ilikuwa na silaha ambayo ilitumika kumfanya Mufti asiendelee kuwaharibia mipango yao mbele ya watanzania. Kamera hiyo nzito aliirusha usoni mwa Norbert ambaye alihama pembeni haraka sana ikapita ikaanguka chini, kitendo cha Norbert kuhama pembeni ndiyo Wlson aliitumia kama nafasi ya kugeuka nyuma na kuanza kukimbia kwa nguvu zake zote ili amuepuke Norbert. Alikuwa akitambua wazi kabisa hawezi kupambana na mtu kama huyo ambaye uhatari wake alikuwa ameshauona kupitia habari alizosikia juu yake hasa kutangulia mbele za haki kwa wenzake na chanzo kikubwa ikiwa ni Norbert.

Norbert naye hakutaka kumuachia kabisa Wilson amtoroke kijinga namna hiyo, aliamua kumkimbiza kwa nguvu zake zote ambapo tayari muda huo Wilson alikuwa ameshaelekea kwenye mchanga wa ufukweni akawa anakimbia kuufuata upande wa kaskazini ambao kulikuwa na kampuni ya Tanzania Safaris Zanzibar Travel holidays. Norbert alimkimbiza kwa nguvu zote na akawa anatumia kasi yake aliyokuwa akiitumia kipindi yupo kwenye mafunzo ya hatari kabisa ambayo alikuwa akipewa nchini Cuba baada tu ya kuchukuliwa na EASA kwa mara ya kwanza, haikumuwia muda mwingi kwa kutumia kasi hiyo kwani tayari alikuwa ameshamfikia Wilson na akawa yupo naye karibu kabisa akiwa yupo katika kasi sawa naye baada ya kupunguza kasi alipomfikia karibu naye. Wilson alikuwa akitumia nguvu zaidi katika kukimbia huku akiwa amebana mdomo kwa nguvu sana asiweze kuvuta pumzi kwa kutumia mdomo, akiwa bado yupo kwenye mbio na kasi yake hiyo Norbert aliupiga teke dhaifu mguu wake mmoja na kupelekea ugongane na mguu mwingine kisha aanguke vibaya na kubiringita kwenye mchanga.

“Aaaah!” Alitoa sauti ya kukata tamaa kwa kuangushwa na Norbert huku akiwa anasalimiana na mchanga huo wa ufukweni.

Norbert baada ya kumpiga teke hilo lililomfanya abiringite aliamua kumfuata kwa kasi kipindi alipokuwa akibiringita, kabla hata hajasimama kwa kubiringita huko Norbert alimuongeza teke la dochi ambalo lilikuja kumpata sawia kwenye mbavu hadi Wilson alitoa mguno wa maumivu. Aliendelea kumsogelea Wilson ambaye bado alikuwa anabiringirita hadi aliposimama kabisa akawa anaugulia maumivu ya dochi hilo la mbavu, Wilson alikuwa akihisi sehemu hiyo ya mbavu kama alikuwa amepigwa na chuma kutokana na nguvu za miguu alizonazo Norbert ambazo ndiyo alizitumia kumpiga dochi hilo la mbavu.

Norbert alisimama karibu kabisa na Wilson akawa anamuamgalia Wilson jinsi alivyokuwa akiugulia maumivu ya pigo alilokuwa amempatia, tayari Wilson alikuwa ameshaweka ugumu katika moyo wake katika kupambana na Norbert jambo ambalo lilikuwa ni kosa kubwa sana kwake. Alikuwa hajajiweka sawa kiakili ndiyo aweze kupambana na Norbert, ndiyo maana hata alipomuona alikimbia ili asikutane naye kwani hakuwa amejiweka katika hatua ya kupambana naye. Laiti kama tangu mwanzo angekuwa ameiweka akili vizuri katika kupambana na si kumkimbia mtu kuwa hamuwezi, ingemsaidia sana aweze kupambana na mtu huyo ambaye kwa sasa alikuwa amemuweza akiwa hana ujanja kabisa wa kukimbia kwani ukaribu aliokuwa yupo naye haukumfaa kabisa katika kumtoroka mtu huyo. Kukimbia kwake ilikuwa ni sawa kumkimbia mamaba kwenye mto wakati ng’ambo ya mto ni mbali sana, jambo ambalo haliwezekani kabisa kutokea kwani mamba kaumbwa na kasi kwenye maji.

Kitendo cha Wilson kumkimbia Norbeet ni ishara kubwa ya kutomuweza kimapigano, tayari mwili wake hadi moyo wake ulikuwa umeshakiri hivyo ndiyo maana akamkmbia katika eneno ambalo walikuwa wapo wawili tu hapakuwa na mtu mwingine na hata kama wangepigana basi wangepigana wawili tu si kupigana na mtu mwingine. Wilson akiwa hapo chini alikuwa akijaribu kufikiria jinsi ya kumtoroka tu Norbert na si kingine katika eneo hilo, tayari alikuwa ameshapunguzwa nguvu kwa pigo alilokuwa amepewa na sasa alikuwa na nguvu dhaifu zaidi kuliko hata nguvu alizokuwa nazo hapo awali alipokuwa akijaribu kumkimbia katika eneo hilo. Ili asionekane kuwa alikuwa amekubali kushindwa kikondoo tu aliamua kujiinua akasimama na akawa anatazamana na Norbert. Alijitahidi asioneshe kuwa amejeruhiwa lakini mwili uliokuwa umepata hitilafu hiyo ulikuwa unamsaliti kabisa na kupelekea atoe ishara zote kwa Norbert kuwa amejeruhiwa, kila alipokuwa akihema kwa huko kujeruhiwa kwake alikuwa akipatwa na maumivu kwenye mbavu jambo ambalo lilimfanya azidi kumpa ishara ya kufumba macho kwa maumivu adui yake.

Akili ya kukiri kuwa alikuwa hawezi kabisa kusimama na mwanaume mwenzzake huyo kimapigano ndiyo zilikuwa zipo kichwani mwake, muda huo aliokuwa akimtazama Norbeet aligeuza jicho pembeni kutazama katika upande wa nyuma kwa namna ya kijanja zaidi ili akimbie akiwa amepata nafasi tu ya kukimbia katika eneo hilo. Alikuwa akitafuta nafasi za dhahabu ambazo zote zilikuwa zimebanwa kisawasawa, hata nafasi ya makaa ya mawe katika kutoroka katika eneo hilo hakuipata mbele ya mjanja wa wajanja ambaye alikuwa yu mwenye uwezo wa kujua ujanja wa kila namna kutokana na akili nyepesi aliyokuwa nayo kichwani.

“Mwanamama usijaribu kukimbia nitategua mbavu yako nyingine” Norbeet kwa kujua adui yake hayuko tayari kimapigano alizidi kumchanganya kabisa, maneno hayo yalikuwa ni tusi zito sana kwa mwanaume mwenye kukamilika kila kitu kwenye mwili wake kama Wilson Ole.

“Hii sasa ni too much” Wilson alijisemea moyoni baada ya kuona kuwa alikuwa amedhalilishwa vya kutosha na adui yake huyo, alijua kabisa alikuwa amegundulika hawezi kupambana naye ndiyo maana akamdharau namna hiyo.

Wilson hasira zilimzidi kichwani akiona dharau hizo zilikuwa zimezidi kabisa hadi kufikia hatua hiyo, hata kama hakuwa akiweza kupambana na mtu kama Norbert aliona hakufaa kuitwa mwanamama. Tusi hilo alilokuwa ameitwa na Norbert lilimfanya hata uoga aliokkuwa nao kwa Norbert umuondoke papo hapo, moyo wa liwalo iwe ndiyo ulikuwa umeingia ndani ya muda huo. Hakung’amua kabisa hilo ndiyo Norbert ndiyo alikuwa analitaka na si kumpiga tu kama anapiga punda aliyegoma kwenda, hasira tayari zilikuwa zimeishaivamia akili ndani ya muda huo. Mawazo ya kupambana kisa amedhalilishwa kwa kuitwa jina baya, ndiyo yalikuwa yamechukua taji la ufalme katika mishipa yake ya fahamu ndani ya mwili wake kwa muda huo.

Aling’ata kabisa papi za midomo yake za chini kwa jinsi hasira zilivyokuwa zikimuongoza ndani ya mwili wake, viganja vya mikono yake alivikunja kwa nguvu sana na kutengeneza ngumi iliyokuwa ikitetemeka kama miguu ya mcheza sarakasi akiwa anatembea juu ya kamba.

Bila ya kusita alinyanyua mguu wake mmoja akapiga hatua moja mbele kwa kasi, na alipoongeza hatua ya pili tayari alikuwa ametoka na ngumi mbili za usawa wa usoni kama vile alikuwa ni mcheza masumbwi mzuri sana akiwa ulingoni akipambana na mpinzania wake. Alikuwa akiulenga uso wa Norbet kwa ngumi hizo ambazo zote zilikuwa zimelenga upande mmoja,alirusha ngumi hizo huku akiwa amesahau kabisa kuwa mchezo huo aliokuwa akiutumia kurusha ngumi ulikuwa na lengo lake. Mchezo haukuwa umeundwa kwa ajili ya kumuumiza adui bali ulikuwa umeundwa kwa ajili ya kujizuia usiumizwe na adui yako, ngumi alizokuwa amerusha Wilson zote zilikosa lengo baada ya Norbeet kuanza kuyumba kulia alipotupa ngumi ya kushoto na kisha akayumba kushoto alipotupa ngumi ya kulia. Baada ya kuyumba namna hiyo Norbert alimrudisha Wilson nyuma kwa teke la kusukuma la kifua ambalo lilimfanya ayumbe nusura adondoke, Wilson alipojiweka baada ya kuyumbishwa na teke hilo alikunja ngumi zake akiziweka usawa mbele ya uso wake kisha akamfuata Norbert kwa kasi sana na alipomkaribia aliamua kurusha ngumi ya walioshindwa mapambano maarufu kama kota(kwa watu wauswahilini ngumi hii siyo ngeni kwao hurushwa kwa kuzunguka kama feni).

Ngumi hiyo Norbert aliinama ikapita, Wilson alileta nyingine ya mkono wa kulia kama ile baada ya mkono wakushoto kukosa lengo. Ngumi hiyo ya pili aina ya kota nayo ilikosa lengo kabisa na Norbert aliinama tena akampa akili Wilson ya kujaribu ngumi nyingine kutokana na kuinama huko.

Wilson bila ya kuchelewa alijaribu ngumi kuchimbua maarufu kama upper cut wale uswahilini hupenda kuiita ambakati kutokana na kushindwa kulitamka jina lake kwa ufasaha, ngumi hiyo Norbert nayo aliiona kwakuwa Wilson alikuwa akitumia nguvu nyingi katika kuzirusha ngumi na kupelekea ishara muhimu za mwili wake zinazoashiria kutoka kwa ngumi ya aina hiyo Norbert kuziona. Kitendo cha haraka alichokifanya Norbert ilikuwa ni kutegesha kiwiko chake usawa wa chini ya kidevu ambapo ngumi hiyo ilikuwa ikija, ngumi ya Wilson yote iliishia kwenye mfupa wa kiwiko kilichokomaa cha Norbert hadi vidole vyake vikateguka na kutoa sauti ya kugoka.

“Aaargh!” Alitoa ukelele wa maumivu kwa kuumia mkono wake na hakujua kabisa alikuwa amefanya kosa jingine.

Ukelele wake huo uliambatana na kusindikzwa na ngumi nzito ya uso iliyotoka kwa Norbet pamoja na teke zito la pembeni la kutumia kisigino ambalo lilitua kwenye kifua cha Wilson hadi akaenda chini kabisa, alikuwa amevunjwa mifupa ya kifuani kwa mara nyingine na Norbert kwa teke hilo la nguvu sana. Wilson alianguka chini akajua kabisa mwisho wake ndiyo ulikuwa huo kwa muda huo, Norbert alipoona mpinzani wake alikuwa ameanguka chini aliitazma saa yake mkononi kisha akasonya.

“Napoteza muda tu hapa” Aliongea kwa dharau na kisha akamsogelea Wilson ambapo alimuachia mapigo ya karate katika sehemu mbalimbali za mwili wake,pigo la mwisho alilimalizia katika mfupa wa koo wa Wilson na huo ndiyo ukawa mwisho wa Wilson kujaribu kupambana naye. Baada ya kumaliza kwa pigo hilo hakutaka kupoteza katika eneo hilo yeye aliamua kuvaa kofia yake kisha akaondoka taratibu hadi barabarani, alipofika barabarani alitembea kwa mwendo wa taratibu akiwa anarudi kwenye makutano ya barabara ya Sea view,Ufukoni na Obama ambako ni upande kulipokuwa na hospitali ya Aga khan kwa karibu.


Baada ya kuingia ndani ya chumba cha kuongozea kamera alipokuwa Godwin, DCP John alimuamru auweke mkanda wa kamera ziliyopo pale kwenye wodi ya Mufti. Godwin aliuweka ule mkanda ambao ulikuwa ukionesha katika eneo ambalo waandishi wa habari walikuwa wamekaa wakiwa wanasikiliza maneno ya Mufti,pia katika upande ambao Mufti alikuwepo kwa kioo kingine. DC John alitumia muda huo kuangalia mwandishi wa habari mmoja baada ya mmoja na akajikuta akiwa amevutika kumuangalia mwandishi wa habari aliyekuwa na kamera ya kizamani akiwa amejibana pembeni katika eneo ambalo alikuwa akichukua mkanda wa video katika nyuzi arobaini na tano wakati kamera zingine zilikuwa zikichukua mkanda wa video kwa nyuzi tisini kamili. Alitazama kwa umakini mwandishi wa habari huyo akiwa yupo ametegesha kamera yake tu akiwa hatii jicho katika sehemu ya kuchukulia mkanda huo, alikuwa amevaa spika za masikioni na waya mmojawapo ulikuwa umetoka kwenye kamera yake na kwenda hadi kwenye moja ya vipaza sauti ambavyo vilikuwa vimewekwa mbele ya Mufti.

DCP John alikuwa akimtazama mwandishi wa habari huyo kwa umakini sana hadi pale Mufti alipopigwa risasi na akamuona mwandishi wa habari akiwa kama mwenye kushtuka baada ya risasi kupenya kwenye kifuo cha Mufti, ajabu aliposhtuka alitazama kushoto na kulia na alipooona waandishi wa habari wengine wakiwa wanchanganyika kutoka nje kuokoa maisha yeye alichomoa waya wa kipaza sauti chake kisha akainyanyua kamera yake kwa wepesi wa hali ya juu na akaivaa shingoni kisha akatoka kwa kasi sana. Mkanda huo wa video ulipofikia hapo DCP John alimwambia Godwin ausimamishe haraka naye akatii, ilikuwa imeganda katika sehemu ambayo mwandishi wa habari huyo alikuwa akiuvuka mlango huo.

“Mh! Waandishi wa habari wenye kamera ndogo na za kisasa waliposhuhudia risasi ikitua kifuani kwa Mufti walikimbia, kwanini huyu mwenye kamera kubwa tena la analojia akumbuke kuibeba kamera hiyo kama kweli likuwa amechanganywa na tukio hilo. Apate hata muda wa kuuchomoa waya wa mike ya kamera yake na kukimbia kwa haraka. Inawezekana vipi?” DCP John alijiuliza maswali kichwani mwake, mikono alikuwa ameiweka kidevuni huku viwiko vya mikono vikiwa vipo juu ya meza kubwa ambayo mbele yake kulikuwa na vioo vingi vya tarakilishi ambapo viwili kati ya hivyo ndiyo vilikuwa vikionesha kile alichokuwa akikiangalia.

“Hebu urudie tena huo mkanda” Alimpa amri Godwin ambaye aliurudisha nyuma tena mkanda huo wa video na ukaanza kuonesha upaya kile alichokuwa akikiangalia hapo awali, safari hii

aliutazama mkanda huo kwa umakini wa hali ya juu sana.

DCP John alikuwa akiyatazama matendo yote aliyokuwa akiyafanya mwandishi huyo wa habari aliyekuwa amevalia kama mtu mzima asiyeenda na wakati, alimtazama kwa umakini sana wakati akizungumza maneno yaliyomfanya awaite waaandishi wa habari yeye hakuwa na umakini kabisa wa kamera yake alikuwa yupo akimtazama Mufti tu. Alimuona akitoa simu yake mkononi akiandika ujumbe wa maneno kisha akairudisha mfukoni, baada ya hapo aliendelea kutulia tu eneo hilo akiwa anamtazama tu Mufti na baada ya muda alishtuka kisha akarudisha jicho kwenye kamera yake halafu akasimama tena wima akawa anamtazma tu Mufti.

Ilipita kipindi cha muda wakati Mufti akiendelea kuzungumza ambapo alimshuhudia akiwa ametulia tu, baada ya Mufti kuanza kutaja majina ya wasaliti yeye alikuwa akimtazama kwa umakini sana. Haikupita hata muda mrefu alitumbukiza mkono kwenye mfuko wa suruali yake akatoa simu yake kisha akagusa kwenye kioo hicho cha kugusa cha simu hiyo na akaiweka sikioni. Alisikiliza simu hiyo ikiwa sikioni kwa sekunde kadhaa kisha akairudisha tena mfukoni, baada ya hapo aliweka jicho kwenye kamera yake kwa umakini sana huku akiwa anaipeleka pembeni kidgo na akasita kuipeleka na kushika kitu kama plstiki kilichokuwa kipo chini ya kamera hiyo akakirudisha nyuma kwa haraka. Muda huohuo kioo kingine cha tarakilishi kilichokuwa kipo pembeni ya kioo kile alichokuwa akiangalia DCP John kilioensha jinsi kifua cha Mufti kilivyotifuka damu kwa risasi.

“Hapohapo rudisha tena nyuma kidogo” Alimuamuru Godwin ambaye alitiii amri hiyo na kuurudisha mkanda huo wa video nyuma, aliangalia tena kisha akamuamuru asimamishe pale mwandishi yule alipokuwa akichukuliwa na kamera ya ulinzi kwa mbele ambapo kamera yake ilionekana vizuri sana.

“Kuza hiyo kamera niione vizuri” DCP John aliamuru naye akatii amri, Dcp John aliona tundu juu ya kamera ya mwandishi huyo wa habari ambalo lilimfanya asikitike sana baada ya kujua kuwa huyo ndiye alikuwa ni mwandishi wa habari aliyekuwa amempiga risasi Mufti. Bila ya kuchelewa DCP John aliingiza mkono kwenye mfuko wa suruali yake akatoa simu ya ake ya kisas kabisa ya kuguza kioo.

“Una USB cable hapo” Alimuuliza Godwin

“Ndiyo upo” Godwin alijibu kisha akafungua mtoto wa meza akatoa waya maarufu wa kuunganisha tarakilishi na simu ya mkononi kwa ajili ya uhamishaji mafaili, alimpa waya huo DCP John ambaye aliuchomeka kwenye simu yake na kisha akauchomeka kwenye mashine ya tarakilishi.

“Ingiza hizo viedo zote mbili kwenye memory card ya simu yangu”DCO John alitoa amri baada ya kuruhusu mtindo wakuhamisha mafaili katika simu yake, Godwin bila ya kuchelewa aliingiza video hizo mbili zote.

“Asante kwa ushirikiano wako kijana” DCP John alimuambia huku akimpatia mkono.

“Karibu muda wowote” Godwin aliikubali shukrani hiyo.

DCP John baada ya kuchukua ushahidi huo kwenye simu yake hakuwa na cha kupoteza humo ndani ya chumba cha kuongozea kamera, alitoka nje kwa haraka sana akimuacha Godwin akiwa anaendelea na kazi nyingine zilizokuwa zikimuhusu.


Majira ya saa tatu usiku Mufti aliondolewa kwenye chumba cha upasuaji baada madaktari kufanikiwa kuitoa risasi kuitoa risasi iliyokuwa ipo ndani ya kifua chake, alikuwa yupo katika hali mbaya sana na alipotolewa ndani ya chumba hicho alikimbizwa haraka katika eneo la wagonjwa mahututi akiwa yupo chini ya ulinzi mkalina pingu moja ikiwa mguuni mwake katika chumba cha pekee yake kati ya vyumba vingi vya wagonjwa mahututi. Ulinzi ndani ya wodi hiyo ulikuwa ni imara zaidi na nje na ndani ya wodi hiyo kulikuwa kumewekwa askari mwenye silaha ambaye alikuwa na jukumu la kuhakikisha maisha ya Mufti yanakuwa yapo salama kwa muda huo ambao alikuwa akihitsjika kuwa hai kuliko kitu chochote na jeshi la polisi.

Muda huo tayari IGP Chulanga alikuwa ameshawasili katika hospitali akakuta kazi kubwa ikiwa tayari imeshafanywa na vijana wake waliokuwa wana utiifu wa hali ya juu wakiwa katika eneo lao la majukumu, kila alichokuwa akikitazma ndani ya hospitali hiyo tayari kilikuwa kimeshatekelezwa vile alivyokuwa akitaka yeye na kumfanya awe kimya na awe hana cha ziada cha kuongea kwa muda huo ambao kazi zote zilikuwa zimetimia tayari. Alikuwa akipewa maelezo yote na DCP John ambaye tayari alikuwa yupo eneo hilo akiwa amesimamia kila kitu kwa uadilifu wa hali ya juu, baada ya kukagua kila kitu na kuhakikisha kuwa kitu kilikuwa vile alivyokuwa akitaka yeye alirudi katika eneo la mapokezi akiwa na DCP John.

Yule msichana wa mapokezi aliyekuwa akimletea jeuri DCP John alikuwa haishi kumtazama afande huyo kijana aliyekuwa na cheo kikubwa sana, roho yake ya huruma ilikuwa imemvutia sana na hakutegemea kama atakuwa na moyo wa namna hiyo akiwa kama askari aliyekuwa ameudhiwa.

Muda ambao IGP Chulanga akiwa amekaa kwenye makochi ya mapokezi pamoja na DCP John yeye hakuisha kabisa kumtazama kama alikuwa akisikiliza kile ambacho maafisa hao wa ngazi za juu wa jeshi la polisi walichokuwa wakikijadili kwa muda huo. Hakuwa akitilia maanani kabisa maongezi ya wanausalama hao zaidi ya kuwa yupo makini kuutazama tu uso wa DCP John ambaye wala hakuwa na habari naye kabisa yeye alikuwa akisikiliza maongezi ya mkuu wake wa kazi.

“John nimependezwa na kazi yako, hongera sana” IGP Chulanga alimpongeza

“asante mkuu” DCP John alishukuru

“sasa wewe endelea kuhakikisha vijana hawaleti uzembe hawa maana itakuwa aibu sana kwetu”

“Sawa mkuu usihofu kuhusu hilo”

“Narudia tena hakikisha hawaleti uzembe hawa vijana na kuepelekea mtu aliyekuwa yupo chini ya ulinzi wetu tena kafungwa pingu mguuni aweze kupata madhara zaidi”

“Sawa mkuu usihofu kabisa kuhusu hilo kazi hii imefika kwangu tegemea mazuri”

“Nakutegemea ndiyo maana nategemea mazuri kwako wewe ni kijana shupavu sana”

“Kikubwa ni yupo hai katika mikono yetu na jukumu la kuhakikisha anakuwa salama hadi anapata siha njema ni la kwetu sisi vijana wako”

“Haswa kabisaa nafikiri…..” IGP Chulanga alikatishwa na mlio wa simu yake mkononi ambayo alikuwa kaishika mkononi kwa muda huo, aliitazama simu hiyo akaona jina la N001 likiwa halina namba kama ilivyokuwa kawaida yake akiwapigia akiwa kazini. IGP Chulnga alipoona jina hilo alitambua wazi alikuwa akipigiwa simu na Mwanausalama mkubwa sana ambaye alikuwa akiogopeka na maadui kutokana na ufanisi wake anapokuwa kazini, hakutaka hata kupoteza hata sekunde zingine kuiacha simu hiyo iite yeye aliipokea kisha akaiweka sikioni.

“Ndiyo N001……..unasema mtuhumiwa yupo wapi?…….. ok ok tunaenda kumuangalia sasa hivi” Simu hiyo ilikatwa na IGP Chulanga alishusha pumzi halafu akamtazama DCP John ambaye alikuwa tayari akisubiria jambo jipya pale alipoisikia namba ya utambulisho ya Norbert ikitajwa na IGP Chulanga.

“John huyu N001 sijui ni mshirikina maana simuelewi, hebu twende ukaone mwenyewe mtuhumiwa kashammaliza na kamuacha ufukweni kwenye barabara ya Sea view”

“Etiii?!” DCP John alijifanya kushangaa lakini alikuwa akitambua wazi kuwa ilikuwa ni jambo la kawaida sana kwa Norbert kufanya kazi namna hii.

“Kibaya zaidi kamkata kauli tayari ili asiendelee kuishi kwa ubaya alioufanya, hebu tukimbie mara moja hapo ufukweni na vijana”

Baada ya kuongea maneno hayo IGP alinyanyuka kwenye kochi akifuatiwa na DCP John, kundi la maaskari wenye silaha walifuatana nao kwa pamoja kutoka nje ya hospitali hiyo. Walikimbia kwa pamoja mchakamchaka kwenda huko ufukweni kwenda kuangalia kile walichokuwa wameambiwa na Norbert kwa njia ya simu, ndani ya dakika kadhaa tayari walikuwa wameshafika katika eneo hilo la ufukweni na wakawa wanakimbia kuufuata uelekeo wa mbele ambapo kulikuwa na kuna alama za viatu kuashiria kuwa kuna watu walikuwa wanakimbizana. Walienda kwa umbali mfupi hatimaye wakauona mwili wa Wilson ukiwa umelala mchangani ukiwa hauna uhai, wote kwa pamoja walipouona mwili huo waliusogelea karibu zadi ili waweze kumtambua alikuwa ni nani huyo mhalifu aliyekuwa ametumwa kuja kumuua Mufti lakini alishindwa kutokana na risasi yake kutofanikiwa kuutoa uhai wa mlengwa.

Wote kwa pamoja walijikuta wakiwa hawaamini baada ya kusogea karibu kwa kumuona mtu ambaye hawakuwa wakidhania kabisa kama angeweza kujihusisha na shughuli za kihalifu ndani ya nchi hii, alikuwa ni mtu aliyekuwa akiheshimika kutokana na utajiri alionao na pia alikuwa ni mtu aliyekuwa akionekana ni mtaratibu mno. Chuki za wananchi juu ya kaka yake hazikuwa zikimpata yeye kutokana na moyo aliokuwa akisadia watu, watu masikini ndani ya nchi hii walikuwa wakimtambua vyema mtu huyo ambaye alikuwa akiwasaidia sana hata kuwapa ajira katika miradi yake.

Si IGP Chulanga wala Askari wengine waliokuwa wameambatana naye walikuwa wakitarajia kuwa aliyekuwa amefanya tukio alikuwa ni mtu huyo, DCP John ndiyo pekee katika moyo wake hakuwa akishangaa ingawa katika uso wake alikuwa ameweka mshangao mkubwa sana. Alikuwa tayari ameshatambua alikuwa ni mmoja wa watu wabaya lakini hakuwa amejua kuwa ndiyo alikuwa amefanya tukio hilo, nguo zake ambazo alimuona nazo kupitia ule mkanda wa video ambao tayari alikuwa amemuonesha IGP ndiyo ulimfanya aamini kabisa alikuwa ni Wilson kwani umbile la mwili wake bado lilikuwa ni lile na halikuwa na ishara yeyote ya kupungua wala kuongezeka.

“ama kweli umdhaniaye siye kumbe ndiye, sikutegemea kabisa kama mtu kama huyu ndiye atakuwa adui wa taifa hili hadi atumike kuja kujaribu kufanya mauaji” IGP Chulanga aliongea.

“Mkuu unajua bado siamini lakini ule mkanda unaeleza kila kitu” DCP John aliongea akijifanya kutoamini.

“John ndiyo hivyo imeshatokea, na hapa hamna uchunguzi wa zaidi hata mchoro hauna haja kwa mtu kama huyu aliyeuawa na mwanausalama anayeijua kazi yake” IGP Chulanga aliongea kisha akawageukia Askari aliokuja nao akawaambia, “hakikisheni mnaangalia huko nyuma hadi muipate kamera yake aliyotumia kufanyia tukio”

“Mkuu” Maaskari hao walitii amri wakapiga saluti na kugeuka nyuma kisha wakawasha kurunzi zao na kuanza kufanya msako.

KUTI KAVU KUKATIKA

(MWISHO WA WABEMBEAJI)

Hali si shwari kabisa tangu taarifa za Mufti kuwa yupo hai zilipofika kwenye meza ya wahusika ambao walikuwa wakitaka kwa udi na uvumba kumuua Mufti, ilikuwa ni kama pigo kwao kusikia jambo hilo ambalo lilikuwa likiwapa wahka sana. Ilikuwa ni ndani ya nyumba moja ya kifahari iliyokuwa ipo Mbezi beach, watu wa ndani ya nyumba hiyo walikuwa wapo tumbo joto baada ya kuvuja kwa siri zao kupitia kwa mwenzao ambaye alikuwa amewekewa mtego na Norbert. Ilikuwa ni nyumba ya waziri mmoja maarufu sana ndani ya serikali ya Rais Zuber ambaye alikuwa akihusika kwa asilimia zote ndani ya mpango huo wa kutaka kuipindua nchi, wziri huyu alikuwa akifanya mambo hayo kwa siri sana na hata kwenye baadhi ya mikutano ya siri hakuwa akitokea kabisa zaidi ya wanamapinduzi wenzake kumfahamu vilivyo.

Alikuwa aemahidiwa nafasi ya uwaziri mkuu katika serikali itayoundwa na Mzee Ole pmaoja na kitita kikubwa sana cha fedha ikiwa tu atakubali kuunga mkono mapinduzi hayo. Mipango yote iliyokuwa ikipangwa juu ya mpango huo alikuwa akiijua vyema, aliamua kujihusisha katika mapngo huo kwa namna ya siri kwa kuhofia mambo yakiharibika angeweza kupatiwa ushahidi wakuweza kumuweka hatiani. Hivyo hakukaa kwenye vikao vyao hata kama ukipatikana ushahidi wa picha basi hatakuwemo ndani yake, bado alikuwa akijulikana sana na wenzake ndiyo maana Mufti alifikia hatua ya kutaka kumtaja jina lake lakini Wilson alimuwahi kumnyamazisha kwa kutumia silaha aliyokuwa nayo. Baada ya kunyamazishwa huko kwa Wilson alipiga simu haraka akamuhitaji Mzee Ole afike ndani ya nyumba yake ambayo ilikuwa haitumiwi na familia yake na ndiyo hapo wakaja kwenye nyumba hiyo wakiwa wawili tu. Muda huo L.J Ibrahim alikuwa akijiandaa kwenye kuongoza vikosi vya majeshi vilivyokuwa vimeizunguka ikulu akiamini kazi ilikuwa imeisha hata kama alitajwa kuwa alikuwa akihusika ndani ya mpango huo.

Mheshimiwa huyo hali ilikuwa tete sana kwake ilifikia muda huo akaona mambo yalikuwa yamekaa vibaya sana kiupande wake, muda huo walikuwa wamekaa kwenye chumba maalum cha mkutano ndani ya nyumba yake hiyo wakiwa wawili tu waanzishaji wa serikali mpya ijayo ya Tanzania, waanzishaji wa serikali yenye hila ya watanzania ndiyo walikuwa wamekaa humo ndani. Mzee Ole alikuwa yupo kwenye hali ya kawaida sana kwakuwa aliwahi kukumbwa na mazito zaidi ya hayo, Waziri huyu alikuwa yupo kwenye hali tete kwakuwa ni mara yake ya kwanza kukumbwa na balaa kama hilo akiwa anacheza mchezo mchafu wa siasa.

“Mzee Ole hii ni mbaya huoni kama akizinduka yule ndiyo heshima yangu imekwisha” Aliongea kwa wqasiwasi mkubwa akiwa amesimama kwenye chumba hicho cha mkutano na Mzee Ole alikuwa ametulia kwenye kiti hana hofu yoyote ile.

“Relax ndugu ni hali ya kawaida sana katika siasa”

“Nitaanza vipi kurelax Mzee Ole ikiwa huyu mtu bado anapumua hata Wilson alivyompiga risasi bado tu hakufa”

“Nani kakwambia yule Mufti ataiona siku ya kesho mpaka aje kupata fahamu na kukutaja”

“Mzee Ole una uhakika juu ya hilo au unataka kuniletea siasa”

“Fikiri mara mbili uwepo wa Leopard Queen kama nurse ndani ya hospitali ile unafikiri yupo kwa ajili ya kazi gani”

“ok kama yupo ndani mwambie ammalize haraka sana kabla huyo N001 hajaja pale”

“Hilo ndiyo la muhimu la kusema na si kupanic haraka namna hiyo, hukujua siasa ni mchezo mchafu. Msafi anapakazwa uchafu anaonekana mchafu na mchafu anajisafisha kwa njia haramu anaonekana msafi, hii ndiyo siasa”

“Sawa mpigie basi Leopard Queen umuambia amalize kazi Mzee Ole tutachelewa kabisa fikiria IGP yupo tayari ndani ya eneo la hospitali huoni wakiongezeka TISS pia kazi itakuwa ngumu zaidi”

“(Mzee Ole aliposikia kauli hiyo alimpatia simu Waziri huyo) Piga hii hapa”

Waziri bila kuchelwa alinyakua simu nna kupiga namba za Jospehine kisha akaweka simu sikioni, aliisubiri kwa muda mrfu sana simu hiyo ilipokuwa inaita hadi ilipokelewa ndiyo alifungua mdomo wake na kuongea.

“Leopard Queen maliza kazi nzi watajaa hapo iwe mbaya kwetu……ok ni njema kama upo karibu wewe maliza tu”

Baada ya kuongea maneno hayo na Josephine alikata simu na aliketi chini kwenye kiti, simu aliiweka mezani na akamsogezea Mzee Ole aliyekuwa amempatia aongeee nayo.

“Vipi kasemaje?”

“Yupo karibu na wodi aliyolazwa anaenda kumaliza kazi baada ya IGP na baadhi ya maaskari wake muhimu kutoka walipopata taarifa ambayo haijui ni taarifa ipi?”

“sasa ulikuwa unahofu nini akiwepo huyo Mufti haponi ujue, hata kama leo akongea ukweli jua mapinduzi yapo palepale hakuna wa kuyazuia”

“Lakini bado tutaonekana tumechukua nchi kinguvu kwa maslahi ya watu fulani”

“Sasa hofu yako nini kwa ajili ya hilo mimi nikiwa Rais wewe waziri mkuu, tufanye maajabu mengi kwenye maendeleo ya Tanzania naamini tutawaziba midomo wote hao”

“tatizo mataifa ya nje yatatuchukulia vipi?”

“Hilo siyo tatizo kabisa future Prime minister, tulete maendeleo ya maana uone kama hatujawafanya waone kama ilikuwa ni haki tosha kumuondoa Zuber aliyekuwa akijifanya ana misimamo hadi akatae dola milioni 600”

“Ok nimekupata sasa hivi, nafikiri kazi pekee iliyobakia kutusaidia ni jeshi tu na si nyingineyo”

“Ndyio hivyo na Ibrahima kaingia mwenyewe kazini tegemea makubwa zaidi”

“Nina imani naye maana jeshi lipo chini ya amri yake, tutegemee makubwa siyo nitegemee”

“Kabisaa”

“Hivi sasa kidogo nimetulia maana amani haikuwepo”

“Utulie kabisa usiwe na hofu hakuna litakaloharibika kabisa”


Askari aliyekuwa amepewa jukumu la kumlinda Mufti alikuwa yupo makini akiendela na kazi yake kwa muda huo, hakuwa akizubaisha hata kidogo macho yake ili asije akafanya uzembe akiwa yupo kazini na kuleta lawama kwa wakubwa zake au hata akaadhibiwa kwa uzembe wake huo alioufanya. Bunduki aina ya SMG T56 ndiyo ilikuwa ipo mikononi kwenye kiti kilichokuwa kimewekwa pembeni ya mlango wa wodi hiyo ambacho ndiyo alikuwa amekikalia, alikuwa akiangaza macho yake katika kila pande zilizokuwa zikimzunguka katika eneo hilo. Ukimya wa eneo hilo ambalo ndiyo ilikuwa ni njia pia ya kupita kuelekea kwenye vyumba vingine haukumfanya kabisa apoteze umakini akiwa yupo kazini, alikuwa yupo makini sana katika kuhakikisha kuwa Mufti anakuwa salama katika muda huo hadi anapatwa na fahamu.

Akiwa amekaa nje ya wodi akiendelea kuhakikisha usalama wa Mufti unakuwepo, kwenye upande wa kushoto alitokea Muuguzi wa kike mwenye umbo tata ambaye alikuwa amevaa miwani ya macho. Muuguzi huyo alikuwa amebeba baadhi ya vifaa vya kitabibu akiwa anakuja katika njia hiyo aliyokuwa amekaa askari huyo aliyekuwa ana silaha yake. Muuguzi huyo alikuwa akitembea kwa haraka sana akionekana ni mwenye kuwahi katika wodi ambayo ilikuwa ina mgonjwa aliyekuwa akitaka huduma kwa haraka sana. Kamba za viatu za muuguzi huyo zilikuwa zimelegezwa na kutembea kwa haraka hivyo kulifanya kamba hizo zifunguke kabisa, Muuguzi huyo hakuonesha kujali kwa jinsi kamba hizo zilivyofunguka yeye alikaza mwendo tu akionekana ni mwenye haraka sana.

Askari aliyekuwa akilinda kwenye mlango wa wodi aliyokuwa amelazwa Mufti alipomuona jinsi alivyokuwa mrembo na alivyokuwa akitembea kwa hraka hadi mzigo mdogo uliokuwa kifuani ukawa unaleta fujo hafifu, alibaki akimtazama tu. Askari huyo alianza kumtazama kuanzia kuanzi juu kisha akashusha macho yake hadi kati,alipoyapeleka macho yake chini alijionea mwenyewe kamba za viatu vya muuguzi huyo tayari zilikuwa zimefunguka na alikuwa akitembea kwa haraka tu.

“Oooooh! Si ajali hii ngoja nijionee mwenyewe nijipatie ujiko kumsadia akiisalimia hii sakafu” alijisemea Askari huyo kisha akarudisha macho kama alivyokuwa kawaida.

Muuguzi alikaza mendo zaidi akionekana yupo katika kuwahi katika sehemu ambayo alikuwa anaenda,hakuonekana kabisa kumtilia maanani Askari ambaye alikuwa yupo katika mlango wa wodi ambayo Mufti alikuwa amelazwa. Alipofika usawa aliokuwepo Askari huyo alikanyaga kamba za viatu vyake, hapo alijikuta akielekea kusalimiana na sakafu ya eneo hilo hata vifaa alivyobeba vilianza kutangulia kabla yake. Ili kumzuia asianguke na kuumia Askari huyo alinyanyuka kwa haraka sana na akawahi mikono yake kukamata kifua na tumbo kisha akamgeuza na kuwa ameshika kiuno laini cha huyo Muuguzi, alimshikilia barabara asiweze kwenda chini akiona alikuwa amepata ushindi wa kuweza kuonekana alikuwa anajali sana watu wasije kuumia.

“Anti yaani unajali usalama wa wengine lakini wako wewe huujali, si ungeumia jamani” Askari huyo alimuambia Muuguzi huyo akionekana ni mwenye kumuonea huruma sana kwa jinsi alivyokuwa akienda kusalimiana na sakafu, pamoja na kumuambia maneno hayo bado hakuwa amemuinua Muuguzi huyo alikuwa bado kamshikilia vilevile.

Miwani ya muuguzi huyo ilikuwa imemuanguka kwa muda huo na alikuwa amefumba macho baada ya kunusurika kuanguka, Askari huyo aijikuta akimtazama Muuguzi akiwa amefumba macho.

Hakujua kuwa Muuguzi huyo hakuwa amefumba macho yake kabisa bali alikuwa amefumba kihila, hakujua kabisa hiyo ilikuwa ni hila ya huyo Muuguzi aliyekuwa akimvuta aingie kwenye mtego ambao tayari alikuwa ameshaingia katika mtego wake.

Askari huyo hakujua kabisa huyo aliyekuwa amemshikilia ndiye alikuwa akilinda asiweze kufanya jambo baya kwa Mufti, bunduki nayo tayari alikuwa ameshaisahau kwenye kiti kwa papara tu za kwenda kuushika mwili wa binti mrembo kama huyo.

Aliona ameushika mwili wa mwanamke huyo mrembo hadi akawa anajisikia faraja sana kwa kuweza kumshika lakini hakutambua kuwa alikuwa ameingia kwenye kichaka cha chatu, akiwa bado ameendelea kumshika vilevile hakutambua kuwa chatu huyo alikuwa tayari ameshamuingiza kwenye mawindo yake.

Ghafla bila kutarajia miguu ya yule Muuguzi ambaye hakuwa mwingine ila ni Josephine, iliidaka shingo ya Askari huyo kwa kasi ya ajabu sana bila yeye mwenyewe kutarajia. Josephina alijitoa kwenye mikono ya huyo Askari kwa haraka sana lakini miguu yake haikuwa imetoka shingoni,kwa kasi ya ajabu alienda chini kisha akamvuta Askari huyo shingo yake na kumpeleka ukutani kwa mtindo ambao hutumiwa sana na wacheza judo. Askari huyo alijikuta akienda kubinuka na kisha akasambaratika ukutani kwa kupigiza mgongo, bado hata hajafikiria kuhusu pigo lile maumivu yake aweze kujiandaa na pigo jingine Josephine alimshindilia kisigino cha kwenye kifua alipotua chini tu. Pigo hilo lilimfanya askari huyo ajigeuze akiwa hapo sakafuni kutokana na maumivu aliyokuwa ameyapata, Josephin hakutaka hata kumsuburi anyanyuke yeye alimuongeza pigo jingine la nyuma ya kisogo hadi akapoteza fahamu papo hapo.

“Kwa tamaa zenu mtaangamia kama kuku wanaume nyinyi” Josephine aliongea kwa sauti ya chini kisha akaingia kwenye wodi ambayo alikuwa amelazwa Mufti, alifunga mlango wa wodi hiyo kisha akageuka kule kwenye kitanda mbapo alikuwa amelazwa Mufti akiwa hajitambui. Mlio wa mashine iliyokuwa iikionesha shinikizo la damu la Mufti pamoja na mapigo ya moyo ndiyo ulimkaribihsa humo ndani hadi akaangalia pale kitandani.

Alimuona Mufti akiwa amelala huku mashine ya kusaidia kupumua ikiwa imefungwa mdomoni, kulikuwa na dripu ya damu pembeni ikiwa inatiririka. Josephine hakutaka kupoteza muda akiwa ndani ya wodi hiyo, alienda moja kwa moja hadi jirani na kitanda alichokuwa amelazwa Mufti.

Alipofika kwenye kitanda hiko aliangalia kule mlangoni kwa kushuku jambo lakini akaona bado kuo kimya, hapo alirudisha macho alipokuwa amelala Mufti kisha akasonya.

“Upumzike kwa amani Mufti” Aliongea kisha akachomoa mashine iliyokuwa ikisaidia Mufti kupumua bila hata huruma, mlio wa mashine iliyokuwa ikisaidia kupumua kwa Mufti ndiyo ulifuata lakini Josephine hakutaka uendelee wakati mtu huyo akiwa anapigania uhai wake kwa muda huo.

Alichoamua kukifanya kwa muda huo ilikuwa ni kushika shingo ya Mufti na kuizungusha akaivunja kabisa, huo ndiyo ukawa mwisho wa Mufti ndani ya dunia hii kwa kuisaliti dini yake na pia kuisaliti nchi. Alilipwa kwa kile alichokuwa akikifanya akiwa ndani ya dunia bila kujali uwepo wa Mungu, sasa alikuwa akijiandaa kwenda kulipwa zaidi kwa kile alichokuwa amekifanya.

Josephine alipomaliza kazi iliyomleta humo ndani aliona hakuna umuhimu wa kuendela kubaki humo na ilimlazimu atoke nje ya chumba hicho, alienda haraka hadi akiwa anajiandaa kutoka ndani ya chumba hicho. Alipofungua mlango tuu alikutana na mdomo wa bunduki ambayo ilikuwa imeegemeza kwenye mlango kizembe na askari wa jeshi la polisi. Kufungua kwake mlango kulisababisha mdomo wa bunduki hiyo uingie ndani zaidi, Josephine aliyumba pembeni mdomo wa bunduki hiyo ulipokuwa ukitaka kumsukuma kutoka na askari aliyekuwa ameishika bunduki hiyo kuwa alikuwa amekandamiza mlango wa wodi hiyo.

Bila kuchelewa bunduki hiyo ilipomkosa aliidaka bunduki hiyo akaivuta na kupelekea Askari huyo aje mbele bila kutarajia, aliachia goti lake kwa nguvu sana ambalo lilimpata Askari huyo kwenye kifua na akaiachia bunduki ambayo ilibaki katika mkono wake. Askari huyo mwingine alibaki akiumia huku simu yake ya upepo aliyokuwa ameichomeka kwenye kiuno chake ikitoa sauti.

“Tunakuja tupo njiani!” Sauti ya kutoka ndani ya simu hiyo ya upepo ilisikika na hapo Josephine akabaini kuwa taairfa kutoka kwa maaskari wengine ilikuwa imeshafika na walikuwa wapo njiani wanakuja, bila kuchelewa aliitoa ile bunduki kibebea risasi kisha akakichukua ili yule Askari asifanye chochote lile ikiwa atakuwa anakimbia.

Alitoka ndani ya wodi hiyo kwa kasi sana akaeleka katika upande ambao ulikuwa unaelekea mwisho wa ukumbi wa mrefu wa wodi hizo, alipofika mwisho alikutana na ngazi nyingine ambazo zilikuwa zikipanda kuelekea ghorofa ya juu. Josephine alipofika hapo hakuelekea kwenye ngazi bali alifungua kioo cha dirisha lililokuwa lipo pembeni, alitoka nje ya dirisha hilo kisha akashika mabomba ambayo hupeleka uchafu chini kutoka vyoo vya ghorofani. Alishuka na mabomba hayo kwa utaalamu mkubwa sana hadi chini akatokea kwenye eneo la nyuma ya hospitali hiyo, hapo alipitia njia za panya hadi akatoka nje ya hospitali hiyo bila kujulikana na yeyote.


SAA NNE USIKU

Yakiwa masaa mawili pekee mapinduzi hayo haramu yaliyokuwa yamepangwa kutokea ndani ya nchi ya Tazania, wanajeshi wa majeshi yote ya ulinzi na usalama waliokuwa wapo nje ya Ikulu walikuwa wakijiweka tayari kwa kazi mbili tofauti zilizokuwa zimewaleta katika eneo. Kikosi kimoja che jeshi kilichokkuwa kimetangulia mbele ambacho kilikuwa kikosi cha ardhini kilikuwa kikijiweka sawa kuweza kulinda usalama wa Mheshimiwa Rais pamoja na waliokuweno humo ndani, wengine waliosalia walikuwa wakijiandaa kuhakikisha kuwa Mheshimiwa Rais alikuwa akitoka ndani ya Ikulu hiyo kwa mujibu wa amri waliyokuwa wamepewa.

Kikosi kimoja kilikuwa kikisikiliza amri ya Rais na kikosi kingine kilikuwa kikisikiliza amri ya Jenerali feki aliyekuwa akijihesabia kuwa yeye ni mkuu wa majeshi rasmi. Kambi zote za vikosi hivyo zilikuwa zikiweka sawa mawasiliano baina ya watu wao waliokuwa wapo kwenye operesheni hiyo,ni operesheni fagio la chuma dhidi ya opersheni mapinduzi.

Operesheni fagio la chuma ilikuwa inataka kuhakikisha kuwa inafagia taka moja iliyokuwa imebaki ambayo ilikuwa ikisababisha hayo,operesheni mapinduzi ilitaka kuhakikisha kuwa inampindua Rais aliyemo madarakani na kuleta Rais wao mpya waliyekuwa wakimtaka wao. M.J Belinda akiwa ndiyo kamanda wa kikosi cha fagio la chuma kilichokuwa kipo mbele ya ikulu alikuwa akihakikisha kuwa hakuna jambo lolote litakalo hairbika kwenye operesheni hiyo, alikuwa akiwasiliana na makamanda waliopo chini yake kwa kutumia vinasa sauti na si simu za upepo ili asiweze kuingiliana mawasiliano na wanajeshi wa kikosi cha majini ambao walikuwa tayari wapo nyuma yao wakisubiri wao ndiyo waanze kazi. Wanajeshi wa majini wote walikuwa wakifikiria kuwa M.J Belinda na kikosi chake walikuwa wapo upande wao hivyo walikuwa wakiwa tegemea wao sana kuliko kitu kingine chochote ndani ya operesheni hiyo ambayo walikuwa wakifuata amri za mkubwa wao kijeshi aliyekuwa akiwaamuru kufanya kile alichokuwa akitaka wao wafanye.

Vifaa vya mawasiliano baina ya kambi hizo za dharura za vikosi viwili tofauti ndiyo zilikuwa zikiendela kwa muda huo, mara chache wao kwa wao walikuwa wakiwasiliana wakihimizana wajiandae kwa ajili ya mapinduzi. Wale waliokuwa wapo mbele walikuwa wakiwaambia wenzao kuwa wapo tayari na walikuwa wakisubiri saa itimie tu jambo ambalo halikuwa na ukweli wowote ndani yake, ilipotimia saa na nusu L.J Ibrahim alitoka na kwenda kuangalia vikosi vyake kama vipo sawa na alipohakikisha vipo sawa alichukua simu ya upepo ambayo alikuwa akitumia kuwasiliana na M.J Belinda aliyekuwa ni kamanda wa kikosi cha ardhi kilichokuwa kipo mbele yao.

“Bado saa moja na nusu hadi hivi sasa tuanze operesheni yetu, msilewe maneno ya kiongozi wa dini aliyewekwa kitimoto kuubatilisha ukweli wake, ikitimia muda kamili ni kuhakikiha mnaanza operesheni tena ikibidi kuingia ndani” Aliongea akiwa ameshika simu ya upepo

“Mkuu” Sauti ya M.J Belinda iliitikia

“Operesheni ni kumuondoa Zuber tu na si kuharibu mali yoyote ya Ikulu, narudia tena si kuharibu mali yoyote ya Ikulu. Kuua hakuna labda iwabidi. Tunaelewana!”

“Mkuu”

“Vizuri, silaha ziwe tayari kabisa kwa muda huu”

“Sawa mkuu”

Baada ya kumaliza kuongea na simu alitoa tabasamu la ushindi akiamini kuwa alikuwa amemaliza kila kitu, hakujua kabisa kuwa huyo aliyekuwa akimuonesha kuwa yupo kwa ajili ya kutii amri zake alikuwa yupo kinyume kabisa na jinsi alivyokuwa akionesha utiifu kwa kwake. Yeye aliona kuwa kazi ilikuwa imeshaisha na sasa muda huo kilichokuwa kimebaki ni kwenda kumtoa Rais Zuber madarakani ili aingie kibaraka mkubwa wa waktu weupe waliokuwa wana nia mbaya na nchi hii, L.J Ibrahim baada ya kutoka hapo alienda kwenye ufukwe wa bahari ya hindi ambapo alikuta boti ndogo ikiwa inamsubiri, alipanda kwenye boti hiyo ambayo ilianza safari muda huohuo kuelekea kwenye Nyambizi ya kijeshi ambayo hadi muda huo bado ilikuwa imeibuka juu ikisubiria operesheni iishe ili vikosi virudi ndani ndiyo izame tena chini.


Ndani ya Ikulu muda huo Moses pamoja na maafisa wengine wa usalama wa taifa walikuwa tayari wameshajiandaa vilivyo, walikuwa wapo tayari kukabiliana na hali yoyote itakayojitkeza humo ndani kwa muda wowote ambao walikuwa wamewekewa ahadi ya kuvamiwa na jeshi. Ikulu nzima ilikuwa imesheheni wanausalama hao ambao walikuwa wana silaha ndogo zenye hatari kubwa, walikuwa wamejipanga vilivyo kwenye maeneo mbalimbali ya Ikulu ambayo yalikuwa yamejificha kwa muda huo wa usiku.

Rais Zuber hadi muda huo hakuwa amelala kama zilivyo siku nyinge ambazo alikuwa akishinda bila kulala kutokana na hofu aliyokuwa nayo juu ya mapinduzi aliyokuwa ameambiwa, alikuwa yupo ndani ya chumba cha mawasiliano pamoja ulinzi ndani ya ikulu akiangalia kile ambacho kilikuwa kikiendela baina yake na wanausalama wake na hata mawasiliano yaliyokuwa yakiendela.

Moses alikuwa yupo naye akiwa na silaha yake iliyokuwa imening’inia kwapani na nyingine kiunoni, alikuwa amevaa shati pamoja na suruali ya kitambaa na miguuni alikuwa amevaa viatu vigumu vya ngozi. Yeye ndiye alikuwa akitoa amri kuu baada ya Rais Zuber muda huo ndani ya ikulu hakukuwa na mwingine yeyote aliyekuwa akipinga amri zao, muda huo walikuwa wakiangalia mazingira ya hapo ndani ya ikulu kwa umakini sana kuhakikisha hakiharibiki kitu.

“Mheshimiwa usiwe na shaka kabisa ndani ya usiku huu, ikiwa kama operesheni fagio la chuma ndiyo ilikuleta wewe Rais mzalendo kabla hata haujafanyika uchaguzi mwingine ambao ulikupatia ushindi vilvile. Basi operesheni hii itahakikisha utaendelea kubaki madarakani kwa miaka mitano yako awali na hadi ukigombea tena ukipata ushindi” Moses aliongea huku akimshika Rais Zuber bega.

Tabasamu hafifu ndiyo lilimtoka Rais Zuber baada ya kupokea maneno hayo kutoka kwa Moses aliyekuwa yupo naye bega kwa bega kwa kipindi kirefu sana,imani ya kuwa vijana wake bado wapo pamoja naye ndiyo ilizidi kujengeka kwa muda huo.

Mawasiliano kati yao na vijana wao waliokuwa nje ndiyo yaliyokuwa yakiendelea kwa muda huo waliokuwa wapo kwenye kila pande ndani ya Ikulu hiyo, kila kitu kilikuwa kinaenda sawa na salama kama kilivyokuwa kimetakiwa kwenda. Jambo hili lilimfanya ndiyo azidi kuwa na imani ndani ya moyo wake wakupata ushindi ndani ya muda wa uuliopangwa ukifika, wasiwasi kidogo wa kushindwa nao haukuacha kabisa kumzonga ndani ya muda huo. Hakuwa mwenye kujiamini kwa asilimia mia moja kuwa alikuwa akielekea kufanikiwa na kurudi katika hali ya kawaida ya kuaminiwa na wananchi wake waliokuwa na mapenzi makubwa naye hapo mwanzoni. Kila alipokuwa akifikiria uwepo wa wanajeshi wa kikosi cha maji alikuwa na wasiwasi mkubwa sana wa kuendelea kusalia madarakani, hofu aliyokuwa nayo juu ya kikosi hicho ilikuwa ni kutokea kwa upinzani mzito sana kati ya kikosi hicho na kile kilichokuwa kinamtetea yeye. Aliona upinzani huo ungeweza kusababisha vita ndani ya eneo hilo kwani kila kikosi kilikuwa kimejiandaa vilivyo katika eneo hilo.

Alibaki akimuomba Muumba ndani ya moyo wake aweze kupita katika wakati mgumu,muda huo vijana wake walikuwa wapo makini sana katika kupeana traarifa ya kile kinachoendelea nje ya eneo hilo na hata ndani ya eneo hilo kuhakikisha kuwa hakuna kinachoharibika ikiwa wao wapo ndani ya eneo hilo.

Ulinzi ulikuwa ni wenye kuridhisha ndani ya eneo hilo la ikulu na hata nje ya eneo kwa maaskari wa JWRZ kikosi cha ardhini, mawasiliano ya siri ndiyo yalikuwa yanaendela baina yao na utumiaji wa vifaa vya mawasiliano vyenye kujilinda visiingiliwe ndiyo ulikuwa ukitumika wakiwa wapo ndani ya eneo hilo kuhakikisha kuwa hakuna kinachoharibika.

Viongozi wa vikosi katika pande zote mbili walikuwa wakiwasiliana kila muda, Moses na M.J Belinda bado hawakuacha kuwasiliana wakiwa wapo ndani ya maeneo tofauti kuhakikisha kuwa hakuna kitakachoenda vibaya ndani ya muda huo.


SAA TANO KAMILI USIKU

Taarifa ya kuuawa kwa Mufti ilisambaa kama moto wa kifuu baada ya kuwafikia wanahabari waliokuwa wapo nje ya wodi hiyo, habari ya kujeruhiwa maaskari waliokuwa wapo katika eneo hilo wakilinda maisha ya Mufti nayo ilisambaa kwa muda mfpi tu kutokana na upanuzi mkubwa wa vyomba vya habari nchini Tanzania. Hadi inatimia muda huo hakuna mtu kutoka ndani ya Tanzania ambaye alikuwa hajajua kile kilichokuwa kimetokea ndani ya hospitali ya Aga kahan kukiwa na ulinzi mkali wa polisi waliokuwa wanahakikisha hapatwi chochote.

Lawama zote waliangushiwa maaskari wa jeshi la polisi waliokuwa wapo katika eneo hili wakilinda usalama wake, kila aliyekuwa akitumia mitandao wa kijamii alikuwa akililaumu jeshi la polisi kwa uzembe waliokuwa wameufanya hadi auawe akiwa yupo katika mikono yao. Hakuna aliyekuwa akijua kuwa polisi hao walikuwa wakipambana na mwanamke mwenye uwezo zaidi yao hivyo aliwazidi ujuzi na kuweza kumuangamiza Mufti.

Wale waliokuwa wakitambua juu ya jambo hilo hawakuweza kabisa kuwalaumu askari hao, wale ambao hawakuwa wakijua kile kilichokuwa kimetokea ndani ya hospitali hiyo na wala hawakuwa wakijua chochote juu ya muuaji huyo walibaki wakitumia mitandao ya kijamii kama sehemu za kumwaga tuhuma zao. Walibaki wakituma vifungu vya maandishi vile walivyokuwa wakivijua wao vichwani mwao kwakuwa mitandao hiyo ilikuwa na sehemu inayowauliza kile kilichopo ndani ya mawazo yao.

Taarifa hiyo ilikuwa ni sherehe kubwa sana kwa Waziri pamoja na Mzee Ole bada tu ya kuipokea kutoka kwa Josephine aliyekuwa tayari amemaliza wajibu wake ndani ya hospitali hiyo, walishangilia sana walipokuwa wapo ndani ya nyumba ya waziri huyo baada ya taarifa hiyo kuwafikia. Sasa walijiona wapo huru zaidi baada ya taarifa hiyo kuweza kuwafikia, hofu ya kuumbuka ilikuwa imeshapotea kabisa kwa waziri huyo ambaye alikuwa na shaka sana na heshima yake aliyokuwa amejijengea akiwa yupo ndani ya wizara yake. Hakuwahi kuhisiwa kuwa alikuwa ni mtu mwenye nia mbaya sana na nchi hii, hata kwa Rais Zuber alikuwa ni miongoni mwa mwaziri wake aliokuwa akiwaamini tangu ateuliwa kuwa Rais kabisa baada ya kuwa rais wa mpito kwa muda wa miaka kadhaa tangu alipopinduliwa Mzee Ole na jeshi.

“Sasa roho nyeupe kabisa” Waziri alisema huku akiwa na tabasamu usoni

“Mambo hayaharibiki ikiwa Josephine yupo, sasa tusubiri ya Wilson” Mzee Ole naye alimuambia.

“Wilson baada ya kumpiga risasi naye sijajua aliishia wapi maana taarifa sijaipata”

“Nafikiri tumngojee aweze kurejea maana simu yake haipatikani hadi muda huu”

“Mdogo wangu namjua mimi itakuwa kazima simu baada ya kufanya tukio akiwa na wenge la tukio alilolifanya”

“Hata mimi nahisi hivvyo, sasa kesho tuchukue nchi tupate mpunga wetu”

“Hilo ndiyo lilobaki tu Waziri mkuu wangu, wananchi wakilalamika sana ni kuwaletea maendeleo kama ya Afrika ya kusini kwa mwaka mmoja tu watakuwa na imani na sisi”

“Kabisa Rais wangu ni muda wa wewe kuwafanya waamini walikuwa wakikuhitaji rais kama wewe,watanzania ni kama kuku tu hawawezi kukumbuka mahali walipopigwa jiwe wakati anakula mchele hivyo hurudi tena”

“Sasa hizo akili zao ndiyo iwe mbinu ya kuweza kuwakamata kisawasawa”

“Kabisa Mheshimiwa Rais”

“(Mzee Ole aliposikia anaitwa Mheshimiwa Rais laicheka) ndiyo ushaanza kunipa cheo mapema yote hata kiapo sijaapa kwa mara nyingine”

“Sasa si tayari umepita, bado saa moja tu Ikulu yote isafishwe ile na Zuber atoke”

“Na kweli sasa hizi yupo kitimoto huko kama kasikia ni waziri wake anahusika na kumsaliti basi atamuhisi wa fedha maana hawakai meza moja kabisa”

“Mimi hawezi kunihisi kamwe maana ananiamini sana kumbe uaminifu wangu kwake ni silaha, Mheshimiwa Rais mkumbatie adui ndiyo utammaliza kirahisi na mimi nafanya hivyohivyo”

“Mbinu nzuri sana hiyo, ndiyo atakuja kujua kuwa umdhaniaye ndiye kumbe siye”

“Ndiyo atajua si kila kizungusho kilichosimama na namba moja ni sifuri niyngine ni herufi O”

“Yeye kaona kimiminika cheupa akajua ni maziwa nyingine ni uji wa chokaa ukiugeuza kinywaji kinakuua”

“Kabisa Mheshimiwa Rais ndiyo atajuta kuwa na ukaribu nami akijua ni mzalendo mwenzake wa kukataa pesa,uzalendo wa sasa ni kuikubali pesa kwa namna yoyote ile kwani ndiyo kila kitu”

“Upo sahihi kabisa waziri mkuu wangu, hebu mpigie Wilson kwa mara nyingine kama atakuwa hewani mwambie asikawie huko kuna Norbert anaweza kumuingiza kwenye anga zake”

Waziri alichukua simu yake ya mkononi kwa mara nyingine akampigia Wilson akijua ataweza kuwa hewani aongee naye, muda huo hakuna kati yao aliyekuwa akitambua kuwa Wilson tayari ni marehemu. Wala hakuna aliyekuwa akitambua tayari Norbert waliyekuwa wakidhani bado hajamuweka Wilson kwenye anga zake tayari alikuwa amemuweka kwenye anga zake, tayari alikuwa amemuangamiza.

Mzee Ole alijua ni hofu tu aliyokuwa nayo mdogo wake ndiyo maana alikuwa amezima simu yake, simu ya Wilson haikuwa hewani kabisa kwa muda huo waliokuwa wakimpigia na kila wakijaribu kwa mara nyingine majibu yalikkuwa yaleyale. Wote walishangazwa na hali ile maana haikuwa kawaida kwa Wilson kuzima simu kwa muda mfefu tangu awepo kwenye kazi kama hizo.

“Aisee hapatikani tena kuna nini?” Waziri aliuliza swali lisilo na jibu kwao wote

“Hebu mpigie Leopard Queen umuulize huenda akawa na jibu” Mzee Ole alimtoa hofu, Waziri alipiga namba ya Josephine muda huohuo.

Simu hiyo iliiita kwa muda mfupi tu na kisha ikapokelewa,hapo aliweza kutuliza hofu aliyokuwa nayo kwao na akaona ni muda huo wa kumuulia juu ya Wilson.

“Leopard Queen Wilson yupo wapi?……Unamaamisha nini kuniambia hujui inamaana hukuwa naye huko?……Alitoka baada ya kufanya tukio lake na wewe ukabaki ndani……je wewe umeongea naye hata kwa simu baada ya tukio hilo?….,,Ok fanya haraka urudi Ngomeni Mzee Ole anakuja hukohuko sasa hivi” Waziri aliongea baada ya simu yake kupokelewa na Josephine, alipokata simu hiyo alimuangalia Mzee Ole kisha akatikisa kichwa ishara ya kukataa.

“Vipi mbona hivyo?” Mzee Ole aliuliza

“Hata Leoprad Queen anasema hajamuona na wala hampati kwenye simu”

“Ok inabidi sasa niende Ngomeni nikamtazame huenda amerudi na ameamua azime simu kutuliza kichwa si unajua huyu mdogo wangu akifanya tukio lolote huwa anapenda asiwasiliane na mtu na kisha hunywa pombe sana”

“Sawa Mheshimiwa Rais wewe nenda ngomeni sasa hivi kamuangalie, utakutana na Leoprd Queen hukohuko”

“Sawa tuonane kesho ikulu”

Mzee Ole hakutaka kupoteza muda alitoka ndani ya nyumba hiyo na akaingia ndani ya gari lake alilokuwa amekuja nalo katika eneo hilo, lango la nyumba hiyo lilifunguliwa na gari hilo likatoka kwa mwendo wa wastani sana na likaongeza mwendo baada ya kuingia barabara kuu.


SAA TANO NA NUSU

Habari ya kugundulika mtu aliyempiga risasi ambaye ni mfanya biashara maarfu na pia mdogo wa aliyekuwa Rasi wa Tanzania Mzee Filbert Ole, ilivuja kwenye mitandao ya jamii kwa muda mfupi tangu polisi wafanikiwe kujua juu ya uwepo wa mwili wake pamoja na vifaa alivyovitumia kwenye tukio hilo.

Kupitia kwa waandishi wa habari wa kujitegemea haikueleweka habari hiyo ilikuwa imegunduliwa na nani kwani polisi walikuwa wamefanya kwa usiri sana kuuleta huo mwili katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya Aga khan. Maaskari hao wa jeshi la polisi walishtuka kusambaa kwa habari hiyo ambayo ilikuwa imechukuliwa ni usiri mkubwa sana, habari hiyo ilianza kugunduliwa na wauguzi wa hospitali hiyo ambao walikuwa wengi wao hawajui juu ya mtu aliyeuawa ufukweni. Wauguzi hao waliipata habari hiyo kwenye simu zao za mikononi ambapo walishangazwa sana na taarifa hiyo, habari hiyo ilienea sana na hatimaye hata ikawafikia IGP Chulanga na DCP John waliokuwa wapo kwenye chumba maalum cha hospitali hiyo wakifanya mahojiano na Askari polisi aliyekuwa akimlinda Mufti ambaye tayari alikuwa ameshazinduka hadi muda huo.

“Hizi taarifa zimevuja vipi jamani?” IGP Chulanga aliuliza muda huo ambao tayari walikuwa wameshaanza kumuhoji Askari huyo.

“Mkuu tuendelee na mahojiano huenda ni Norbert Kaila yupo kazini si unajua nchi hii hakuna mwandishi mwenye ujanja katika kusaka habari kama yeye” DCP John alimuambia

“Huenda itakuwa ni yeye, mwandishi wa habari ni mjanja sana huyu, ok tuendelee naye” IGP Chulanga alikubali wazo la DCP John.

“Private Fred ukimuona huyo msichana unaweza kumkumbuka?” DCP John aliuliza

“Ndiyo ninaweza kumkumbuka mkuu” Private Alfred aliyekuwa na jukumu la kumlinda Muti aliongea

“Ok nadhani tuna mtalamu wa kuchora katika hao vijana hebu aitwe mara moja” IGP Chulanga aliposikia hivyo alitoa amri, DCP John kwa haraka alitoa simu yake ya upepo akatoa amri hiyo kisha wote wakawa wameacha kumuhoji wakiwa wanamsubiri Askari huyo aweze kufika.

Baada ya dakika tano mlango wa chumba walichokuwepo ulifunguliwa, aliingia askari mwenye cheo cha Inspekta ambaye alitoa saluti alipomuona IGP katika eneo hilo.

“Karibu Inspeka” IGP Chulanga alimkaribisha

“Asante mkuu” Inspekta huyo aliitikia

“nahitaji usikiliza maelezo ya Private hapa na kisha uchore sura ya mtuhumiwa atafutwe kuanzia hivi sasa” IGP Chulanga aliongea

Hakukuwa na muda wa kupoteza Askari huyo alianza wajibu haraka sana, karatssi pamoja na kalamu ya risasi vililetwa, muda huo huo Pirvate Fred alianza kutaja sifa na muonekano wa mtuhumiwa kama alivyoapata kumuona muda mfupi ulipita ambao alimshambulia hadi akapoteza fahamu. Haikumchukua muda mrefu sana kazi hiyo ikawa imekamilika kabisa mchoro huo ulioneshwa kwa Private Fred ambaye alishtuka na akashangaa sana alipouona mchoro huo.

“Private ndiye huyo” IGP Chulanga aliuliza baada ya mchoro huo kukamilika.

“Kabisa mkuu ndiye yeye huyohuyo” Private Fred alijibu

“Una uhakika ndiyo yeye?” IGP Chulanga aliuliza tena

“Ndiyo mkuu nina uhakika” Alijibu.

“Itazame vizuri tena halafu uniambie je una uhakika ndiyo yeye” IGP Chulanga alisema na Private Fred aliitazama picha kwa umakini sana kisha akatikisa kichwa kukubali.

“Ndiyo mkuu ni yeye” Alijibu vilevile

“Ok kuanzia hivi sasa wauguzi wa hospitali nzima wakusanywe, milango ya hospitali ifungwe hakuna mtu kungia wala kutoka” IGP Chulanga alitoa amri hiyo akiamini kuwa muuaji hakuwa ametoka ndani ya hospitali hiyo hadi muda huo, hakujua kuwa tayari alikuwa ameshachelewa hadi anatoa uamuzi huo ndani ya muda huo kwani Jospeine huyo aliyekuwa akionekana kwenye mchoro alikuwa ameshatoweka ndani ya eneo hilo.

“Mkuu” Wote waliitikia na muda huo huo simu za upepo zilitumika kuwapa taarifa maaskari waliokuwa wapo ndani ya eneo hilo la hospitali, milango ya hospitali hiyo ilifungwa mara moja na ulinzi katika maeneo ya ndani ya hospitali hiyo uliimarishwa mara dufu.

Wauguzi wa hospitali hiyo pamoja na madaktari walikusanywa sehemu moja kwa haraka sana, maaskari wa jeshi la polisi waliznguka kila uapnde wa hospitali hiyo kuhakikisha kuwa hakukuwa na muuguzi yeyote aliyekuwa anasalia katika chumba au wodi yeyote.

Muda huo wodi zote na vyumba vya ofisi za wauguzi na madaktari zilibaki tupu kabisa na hakukuwa na yeyote aliyebakia, wote walikuwa wamekusanywa kwenye chumba maalum cha mkutano ndani ya hospitali hiyo. Wote waliketi kwenye viti chumbani hapo wakiwa hawajui kile kilichokuwa kimefanya hadi wakaitwa katika eneo hilo.

IGP Chulanga pamoja na DCP John waliingia katika eneo hilo wakiwa wapo pamoja na Daktari mkuu kisha wakawasalimu watu ote waliokuwa wapo katika eneo hilo, madaktari pamoja na wauguzi wote waliitikia salamu hiyo wakiwa na hofu sana juuu ya kukusanywa kwao huko ndani ya muda huo tena kwa ghafla sana wakiwa hawalelewi chanzo cha wao kukusanywa hivyo katika eneo hilo ni nini haswa.

“Kuweni na amani ndugu zanguni najua wote mna hofu sana juu ya kukusanywa huku kwa muda huu, ni zoezi dogo sana lililofanya tuwakusanye namna hii na zoezi hili linahitaji sana ushrikiano wenu katika kulikamilisha. Muda mfupi uliopita Mufti mkuu wa Tanzania ameuawa akiwa wodini amelazwa tena aliyemuua alikuwa amevaa mavazi ya kiuguzi na pia akiwa na kitambulisho kabisa. Sasa basi hatujapata uhakika kabisa wa kuweza kusema kuwa muuguzi ni mmoja kati yenu au kajichomeka katika kundi lenu. Hivyo kuna karatasi zina mchoro wa sura ya huyo muuaji zimepigwa photocopy na zitapita kwenu kila mmoja, hivyo naomba ambaye atakuwa anamtambua mwanamke huyo anyooshe mkono mara moja” IGP Chulanga aliongea, muda huohuo ndani ya chumba hicho waliingia maaskari wenye karatasi ambazo walizisambaza kwa wauguzi na madaktari wote ndani ya chhumba hucho kwa haraka sana.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Haikuchukua hata dakika tano toka karatasi hizo zisambazwe, kikundi cha wauguzi wa kike ambacho ndiyo kilikuwa kinaongea na Josephine wakati Mufti akiongea na waandishi wa habari walinyoosha mikono yao kwa pamoja. Baadhi ya madaktari wa hospitali hiyo nao walinyoosha mimono yao kuonesha kumtambua Josephine.

“Ok mliomtambua huyo itabidi mfanyiwe mahojiano,kaeni upande huu” IGP Chulanga alitoa amri na waguzi pamoja na madaktari hao wakasogea katika upande ambao walikuwa wameambiwa wakae kwa muda huo.


SIASA NAYO NDANI

Kitendo cha polisi kuzidiwa ujanja na Josephine hadi akafanikiwa kumuua Mufti ilikuwa ni nafasi nyinge kabisa ambayo ilivyokewa ni kama ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu sana na mwanachama wa chama cha upinzani ambacho kilikuja kushika kasi sana baada ya kufutwa kwa chama cha PTP kilichokuwa kikiongozwa na Fibert Ole. Chama hicho cha siasa kilikuwa kipo chini ya mwanasiasa Simon Leonard aliyekuwa akihaha kwa kila namna aweze kupata wafuasi wengi katika kipindi hiko aweze kumtia presha Rais Zuber Ameir, taarifa hiyo ya kuzidiwa ujanja yeye aliiona kama ilikuwa ni njia pekee ya kuweza kuwashutumu polisi ili aweze kujichukulia wafuasi.

Taarifa hiyo ilipofika kwenye mikono yake kitu cha kwanza alichokifanya ni kufungua katika kurasa zake za mitandao mbalimbali, alishusha lawama kwa polisi kuuawa kwake Mufti. Simon alijionesha ni namna gani alivyokuwa ameguswa sana na suala hilo, huku akimuita Mufti mtu aliyekuwa amejitolea muhanga kuweza kuwaumbua madhalimu wa taifa hili. Alishutumu sana jeshi la polisi kwa kuacha hadi akauawa kwa kutumia maneno dhanifu ambayo yalikuwa yapo ndani ya ubongo wake, katika shutuma hiyo aliweza kutengeneza tuhuma nyingine kwa kutumia kigezo cha jeshi la polisi kuwa ni chombo cha serikali.

Aliihusisha serikali nzima huku akitaja serikali iyo ilikuwa imewaajiri maaskari wasio makini kabisa kwa kazi zao hadi Mtuhumiwa anauawa kwenye mikono yao, katika kurasa zake muda huo alikuwa ameandika makala hiyo ambayo kwa siasa zaidi alimlaumu hata IGP kwa kuwa na maasakri wa aina hiyo. Kulaumu huko kulienda hadi akamlaumu waziri wa mambo ya ndani kwa kuwa na IGP aliyepo chini ya wizara yake ambaye hayupo makini kwa vijana aliokuwa nao, bado hakuishia hapo Simon alipeleka lawama hadi kwa Rais Zuber kwa kuteua Waziri ambaye anafuga wazembe waliopo chini ya wizara yake. Mwansiasa hiyo alipotuma makala hiyo haikuchukua muda watu waliisoma sana, wale waliokuwa na kawaida ya kunakiri walifanya hivyo wakawatumia kila mmoja wao.

Wapo waliompa sifa kwa kuliona suala hilo na wapo pia waliokuwa wakimsema vibaya wakimuambia kuwa alikuwa akitaka umaarufu kupitika migongo ya watu. Asilimia kubwa ya wanachi bado walikuwa na uchungu kwa kuweza kuwafanyia mabaya watu muhimu ndani ya nchi yao ikiwemo Rais Zuber aliyeleta mafanikio kwa muda aliokuwepo madarakani, hivyo ilikuwa ni kama alikuwa akiwazidisha uchungu wale wasio na ustahimilivu na wale wasio na staha walimtukana kabisa.

Maoni ya watumiaji mbalimbli wa mitandao ya kijamii Simon alikuwa akiyasoma akiwa yupo na tarakilishi yake pambeni akiway upo mke wake chumbani kwake, matusi hayo hayakumkasirisha ndiyo kwanza yalimfanya atabasamu tu hadi mke wake akashangaa.

“Haya mwenzangu kipi kinachokufanya utabasamu kwa kashfa na matusi ya hao” Mke wake alimuuliza.

“Wafuasi wanakuja kwa kutukanwa sana kuliko hata kusifiwa” Simon alimuambia.

“Kivipi?”

“Huyu aliyenitukana sasa hivi ataenda kumuambia mwingine juuu ya makala yangu na jinsi ilivyomchefua, unajua ni nini kinafuata hapo? Huyo aliyepewa taarifa atatamani kuisoma na yeye aijue na ndiyo hapo wananiletea wafuasi tu,kwani si kila atakayeisoma atakuwa na hisia sawa wapo wataovutika nayo na kuwa wafuasi wangu wataniona ninajali sana”

“Mhh! Kweli hiyo siasa sikuwezi we mwanaume”

“Huu ni mchezo mchafu tuachie tunaouweza usiouweza kaa kando”

“Haya ngoja mi nilale mwanasiasa endedelea”

“Ukiamka utakuta magazeti tayari wamechapisha hiyo habari huku wanahabari wamenikosoa kabisa”

“Ujiandae kwa hilo”

“Watakuwa hawanibomoi bali ndiyo kwanza wananijenga na watakuwa wanafanya kazi ya kufuatilia makala zangu online waweze kupata habariza kuuza, wanapata hela kwa maneno yangu huku wananuongezea wafuasi tu” Simon alimaliza kuongea maneno hayo na akafunika tarakilishi yake ya mapakato kisha akajitupa kitandani pamoja na mke wake, alikuwa akitumia akili ya kisiasa ambayo aliona kabisa ilkikuwa ikielekea kumpa mafanikio kwa muda huo huo hadi miaka kadhaa mbele kwenye uchaguzi mkuu wa Tanzania.

Hakujali kutukanwa wala kukosolewa alichojali yeye ilikuwa kujiongezea wafuasi tu kwenye chama chake kichanga ambacho kimevitingisha vyama vingine tangu akianzishe, alikuwa ana lengo moja tu la kukitingisha chama tawala tu na ndiyo juhudi ameanza.

BAADA YA KUTOKA BARABARA YA SEA VIEW

Baada ya kufanya tukio la kumungamiza Wilson alitoweika katika eneoo la ufukweni kwa haraka sana, Norbert hakuwa na sehemu nyingine ya kwenda isipokuwa kwa wapinzani wake wakubwa walipokuwa wameweka kambi.

Akiwa ndani ya usafiri wake alielekea moja kwa moja hadi Msasani mahali alipofikia awali kipindi anakuja kuichunguza nyumba ya Wilson, aliegesha gari kwenye Bar ileile aliyokuwa ameegesha kabla ya kuelekea ndani ya nyumba ya Wilson. Akiwa ndani ya mavazi yaleyale aliyokuwa amevaa awali pamoja na kofia yake iliyokuwa imeufunika sehemu kubwa ya suso wake, alipitia mlango wa nyuma wa bar hiyo kama alivyokuwa amefanya siku ile wakati anakuja kupeleleza. Njia ileile aliitumia na akaja kutokea jirani kabisa na lango kubwa, alitembea kwenye barabara ileile hadi alipofika usawa wa lilipo geti la nyumba ya Wilson maarufu kama Ngome. Norbert alipofika hapo kwa haraka kabisa alitoa kichupa kidogo sana mfukoni mwake kinachofanana na kichupa cha uturi wa gesi wa mwilini(body spray), alifungua kichupa hucho na alijipuliza sehemu za mdomoni pamoja na pembeni ya mashavu yake. Hakuishia hapo alifungua vifungo vya shati lake halafu akavifunga hovyo, hakika alikuwa akionekana ni kama mlevi aliyekuwa amekosea njia akaingia jirani na geti la nyumba hiyo. kile kichupa alichojipulizia nacho kilitoa harufu kabisa ya pombe hivyo kumfanya aonekane alikuwa amelewa.

Baada ya kufanya hivyo alikirudisha kichupa hicho ndani ya mfuko wake kisha alijisogeza karibu kabisa na geti hilo, alipokuwa analikaribia geti hilo alianza kuyumba kilevi huku sehemu kubwa ya uso wake ikiwa imezibwa na kofia aliyokuwa amevaa. Alipofika getini kabisa Norbert alikutana na mwanga mkali sana kutoka kwenye taa maalum zilizopo hapo getini ambao ulimfanya ainamishe uso wake chini, aliweka mikono kabisa kichwani kujikinga na mwanga huo kama mtu aliyekuwa akijikinga na mvua isiweze kumnyeshea. Kuyumba ndiyo kulikuwa jadi yake kwa muda huo wote aliokuwa hapo, Norbert aliamua kuinua macho juu huku akihakikisha uso wake wote hauonekani kwenye taa hizo za mwanga mkali zilizokuwa zipo hapo getini alipozitazama taa hizo alirudisha uso chini kwa nguvu sana kisha akatoa mguno wa kukereka baada ya kuzitazama taa hizo. Alipiga hatua moja tena mbele hadi akalifkia kabisa geti hilo na akajigonga nalo, aliyumba baada ya kujigonga nao lakini hakuanguka alijiweza kujizuia.

“Aaaargh! Ama kweli kuoa mfipa aliyezaliwa na Mpemba ni tabu, ona sasa kashaanza kuniwekea mazingaombwe yake mapema yote hii saa ishirini na moja” Norbert aliongea kilevi sana huku akiitoa simu yake ya mkononi na kutazama saa ambapo alikuta ikiwa inaonesha ni saa tatu usiku ikiwa katika mfumo wa masaa ishirini na nne ndiyo maana alisema saa ishirini na moja. Ilikuwa ni muda ambao bado kabisa hata IGP Chulanga alikuwa hajapata mchoro wa muuaji wa Mufti.

“Ona sasa anajifanya kawa Mungu na yeye kawasha jua lake linaniwakia hapa utosini mwangu usiku huu, mbele ya mlango kaipoteza nyumba kimazingara kaweka kontena. Pumbafuuu! Anataka majirani wanione mimi chizi siyo yaani nidhanie nipo kwenye eneo la bandari kwenye makontena. Uchawi wake haunipati ng’oo nasema hata kama ni kontena nitaingia ndani hivyohivyo anione mimi mchawi zaidi” Norbert alizidi kuongea kilevi muda huo alikuwa akijifanya kuwa haelewi ile iliyokuwa hapo juu ni taa akijifanya anaona ni jua kwa ulevi kumkolea. Alijifanya pia halitambui kuwa hilo hapo mbele yake ni geti yeye aliita kontena lilokuwa amewekewa na mke asione nyumba.

“We! Mbwa ndiyo umetoa mlango siyo kwa uchawi wako sasa mimi napanda juu naingilia batini” Alizidi kujitoa akili na muda huo alianza kuliparamia geti akionekana kuelekea juu, vituko vyake havikuchukua muda mlinzi wa hapo getini tayari alikuwa ameshaviona na alifungua mlango wa pembeni wa kupitia watu.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Alipoufungua tu mlango huo ambao ulitoa sauti hafifu ambayo ilisikika wazi kwenye masikio ya Norbert, alibaki tu akimtazama Norbert ambaye alikuwa akionesha juhudi za wazi kabisa za kuliparamia gati lakini alionekana kutoweza kabisa. Norbert naye alijifanya kutomuona mlinzi huyo na aliendelea kufanya juhudi za kuparamia geti hilo hadi pale mlinzi alipopiga kiatu chake chini kwa nguvu sana kumshtua, mlio wa kiatu hicho ulimfanya Norbert ashtuke kwa nguvu sana hadi akaachia geti alilokuwa amelishikilia wakati akijaribu kupanda. Norbert alianguka hadi chini, yule mlinzi aliyekuwa yupo hapo getini alibaki tu akimtazama Norbert akimuona ni mlevi aliyekuwa amepotea njia.

Baada ya kuanguka chini alijiinua kivivu sana na akaweza kusimama wima ingawa bado alikuwa akipepesuka kilevi, aligeuza uso wake na akatazama kule alipokuwa yupo yule mlinzi aliyepiga kiatu chini kwa nguvu hadi akashtuka kimaigizo na akajiangusha chini.

“Anhaaa! We bwege kumbe ndiye unayeniibia mke wangu yaani bora umejitokeza mwenyewe pumbavu zako, ndiyo ukamwambia huyo malaya augeuza huo mlango wa kuingia ndani upande huo ili mimi nisiingie ndani ule vizuri asali yangu” Norbert aliongea kilevi kumuambiaMlimnzi huyo ambaye hakujibu chochote zadi ya kuishia kumtazama tu.

“Muone kwanza dume zima una mahips” Norbert alizidi kuropoka na safari hii akambeza Mlinzi huyo juu ya suruali aliyokuwa amevaa ya sare ya kazi kutokana na kutuna sehemu za mapaja kwenye mfuko ya surusli hiyo, Mlinzi bado alikuwa amekaa kimya huku akiwa amefumbata mikono kifuani mwake.

“Kwanza nina wasiwasi na uanaume wako usije ukawa msagaji wewe, mwanaume gani ana manyonyo dume jike wewe umekuja kumsaga mke wangu” Alizidi kumbeza Mlinzi na safari alimtaniaa juu ya kutuna shati la kiulinzi kifuani kutokana na uwepo wa mifuko mikubwa kama iliyopo kwenye suruali yake, maneno hayo yalikuwa ni yenye kuudhi lakini Mlinzi huyo aliamua kuzuia hasira zake.

“Haloo wewe! toka hapo ulevi wako usikupeleka pabaya, hapa ni nyumbani kwa watu wazito nitakuharibu sasa hivi!” Mlinzi aliamua kumkoromea Norbet akiamini alikuwa ni mlevi aliyekuwa amepotea njia

“Hao wazito wana kilo ngapi au ndiyo umeniletea wasagaji wenye hela uwasage pamoja na huyo mke wangu ndani, mkaugeuza mlango kichawi ukajua sitauona kwa taarifa yako nimeuona huo hapo tena mmeufanya mdogo kabisa” Norbert aliendela kuropoka kama ilivyo kawaida yake, baada ya kuongea maneno hayo aliutazama mlango mdogo wa kupitia watu aliopitia yule Mlinzi vizuri.

Aliutazama kwa sekunde kadhaa mlango wa geti kisha akaropoka, “Wajinhga nyinyi ndiyo mmeamua kuung’a mlango wa mbao ngumu za mkaratusi niliyokuwa nimeuweka kwa hela nyingi mmeuweka huo wa bati mtanieleza leo” Alipoongea maneno alianza kumfuata mlinzi kwa kasi sana akiwa na miondoka ya kilevi, alipomkaribia alirusha ngumi nztio ya kilevi ambayo Mlinzi huyo aliikwepa akaenda chini moja kwa moja akaangukia kifua.

“Haaa! Huyu mwanamke ndiyo kakuongeza uchawi ili usiweze kupigwa siyo” Norbert aliongea huku akijinyanyua kwa tabu, alifanikiwa kunyanyuka kilevi na alisimama huku akiyumba sana.

Eneo alilokuwa amesimama Norbert kwa muda huo kulikuwa na kamera ya ulinzi iliyokuwa imefungwa juu kidogo ya kichwa chake kwenye ukuta, kamera hiyo ndiyo ilikuwa ikichukua matukio yote ya hapo nje. Mlinzi huyo hakujua kama kumkwepa Norbert hadi akaelekea upande huo alikuwa amefanya kosa kubwa sana, ilikuwa ni bora hata angemrudisha kwa pigo la nguvu kulekule alipokuwa awali kuliko alivyomkwepa.

Kamera hiyo ya ulinzi ilipoanza kuzunguka tu Norbert aliiona na aliitazama huku akiyumba, aliweka mkono mdomoni kwa mshangao kama alikuwa amegundua kitu cha ajabu sana.

“Alaaaa! Wajinga nyinyi si ndiyo uchawi wenu huu hadi nyumba siioni naona kontena” Norbert aliongea na kwa haraka sana akairuka juu akaishika kamera hiyo ya ulinzi akavuta hadi akaiharibu, tendo hilo lilimuundhi sana mlinzi huyo ambaye alione kabisa huyu aliyekuwa akiamini ni mlevi alikuwa akitaka kumuhairibia kazi yake.

Uvumilivu wake wa kuvumilia matusi yote aliyokuwa ametukanwa na Norbert ulifika kikomo hadi muda huo, hasira zilianza kumpanda ndani ya kichwa chake na akabaki akimuangalia Norbert aliyekuwa ameanguka chini kilevi baada ya kurukia kamera hiyo na kuiharibu hadi ikazima ikawa haifsnyi. Mlinzi hakutaka kabisa kuendelea kuangalia vituko alivyokuwa akivifanya Norbert, aliona huo ndiyo ulikuwa ni muda wa yeye kumuadhibu ili ashike adabu asiweze kuingia katika eneo kama hilo hata awe mlevi kupita kiasi. Alichomoa rungu lake alilokuwa amechomeka kiunoni na aliamua kumfuata Norbert kwa kasi pale alipokuwa amelala nchini baada ya kuanguka, alijua kuwa alikuwa ameanguka kilevi na hawezi tena kuinuka kumbe ilikuwa ni hila ya Norbert ya kuweza kumvuta ndani ya anga zake aweze kumpa haki yake.

Mlinzi yule alipomkaribia Norbert alishusha rungu lake kwenye kifua cha Norbert kwa hasira akiamini lingempata, rungu lake hilo lilitua kwenye sakafu ya eneo na halikuweza kabisa kumapata Norbert kwani tayari alikuwa amejibiringisha mbele zaidi. Mlinzi alimposogelea zaidi alikutana na mtama wa haraka sana kutoka kwa Norber ambaye aliuzunguka mguu wake kama feni, alianguka hadi chini na hata kabla hajafikiria kitu kingine cha kufanya alipokuwa ameanguka mguu mzito wa Norbet ulitua kwenye kifua chake ambaye hakuelewa alikuwa ameinuka muda gani.

Hakuwa Norbert yule mwenye sauti ya kilevi pamoja na muondoko ya kuyumba bali alikuya yupo imara kabisa, Mlinzi alibaki akiduwaa asiamini kabisa kwa kile alichokuwa amekiona.

Akili yake akiwa bado yupo chini hapo ilimtuma aupeleke mkono wake kiunoni alipokuwa ameweka silaha yake ili aeze kuichomoa kuweza kumdhibiti Norbert, tayari alikwishatambua kuwa alikuwa amevamiwa na mtu aliyekuwa akijua nini anachokifanya na wala hakuwa mlevi kama alivyokuwa akidhania hapo awali.Akili ayake hiyo tayari ilikuwa imeshasomwa barabara na akili shupavu na nyepesi aliyokuwa nyo Norbert, kitendo cha yeye kugusa tu sehemu ya kiunoni Norbert aliupiga mkono wake. Bila ya kuchelewa alimuongeza teke jingine la kwenye mbavu hadi Mlinzi huyo akatoa ukelele wa kuuumia ambao ulimfanya Norbert apepese macho kwa haraka sana katika pande zote. Alipoona pako kimya alizidi kumpa kipigo mlinzi huyo hadi alipohakikisha kuwa alikuwa kalegea kabisa, hapo alimuinua na kumuingiza ndani kwa kutumia lango mdogo.

Alimburuza hadi yalipo makazi ya mlinzi wa eneo hilo akamuweka chini katika eneo hilo ambalo lulikuwa na mitambo mbalimbali ya ulinzi pamoja na silaha za kujihami.

“Inamaana huyu mtu nisingemjia kwa njia hii basi kiama changu kilikuwa kinakaribia kabisa, kwa silaha hizi” Norbert alijisemea kisha akamuongeza mlinzi yule teke jingine akiwa yupo naye humo ndani na nyumba ndogo ya ulinzi.

Mlinzi alizidi kutoa miguno ya maumivu kwa teke hilo alilokuwa amepigwa, Norbert hata hakujali maumivu yake yeye alimuinua akamuweka kwenye kiti cha humo ndani. Alifanya haraka sana akatafuta kamba imara iliyokuwa ipoo humo ndani ambazo hutumika hasa na wacheza sarakasi, alimfunga ile kamba kwenye kiti hicho kwa nguvu sana kuhakikisha kuwa hawezi kutoka akiwa yupo katika eneo hilo. Baada ya kumfunga kamba hiyo Norbert ndipo alikaa kwenye kiti kingine kilichokuwa kipo katika eneo hio, mawazoni mwake alikuwa na lengo la kumbana tu Mlinzi yule aweze kusema juu ya kile alichokuwa akikitafuta ambacho kingeweza kumsaidia katika kukamilisha kazi iliyokuwa imemleta katika eneo hilo.

“Wakubwa zako wapo wapi?” Alimuuliza lakini hakuambulia jibu lolote zaidi ya Mlinzi huyo kuinamisha uso chini kwa kiburi sana.

“Mfumo wa hiii nyumba kiulinzi upoje?” Aliuliza tena akiwa hatilii maanani swali lile la kwanza ambalo lilikuwa halijajibiwa na Mlinzi huyo, kimya kingine ndiyo kilifutata na si kujibiwa swali kama alivyokuwa akitarajia yeye baada ya kuuliza.

“Ohoo! Kiburi sana wewe ngoja nikuoneshe kuwa kuna viburi zaidi yako katika dunia hii” Norbert aliongea kisha akatoka hadi katika eneo lenye silaha ndani ya chumba hicho, alichukua kikasha kidogo chenye rangi nyeupe akaja nacho hadi mbele ya huyo Mlinzi.

Norbet alikifungua kikasha hicho akatoa bomu dogo sana la kutegesha kwa saa kisha akalitega na kuliweka karibu ya mlinzi huyo chini ya kiti alichokuwa amemfunga huyo.

Mlinzi huyo alianza kuingiwa na hofu alipoliona bomu hilo likiwa limetegwa jirani kabisa na na yeye na huyo aliyekuwa akilitega wala hakuwa ni mwenye kumuonea huruma ndiyo kwanza alikuwa akitabasamu kabisa akiona kile alichokuwa akikifanya kilikuwa ni kitu kizuri sana na kibaya kwa adui yake.

“Una dakika mbili tu za kuweza kuishi sali sala zako za mwisho tu ndugu” Alimuambia huku akianza kutembea kutoka nje ya chumba hicho

Yule Mlinzi alipoona hali ni hiyo hakika uzalendo ulimshinda kabisa na akajuta hata kuwa kiburi kwa mtu kama huyo asiyetaka kuoneshewa kiburi, aljaribu kujiiinua na kujitoa kwenye kiti hicho lakini hakuweza hata kidogo na ndiyo kwanza Norbert alikuwa akitoka nje ya chumba hicho akiwa anatembea kwa majigambo kabisa baada ya kumaliza kufanya hivyo.

“Weee! Subiri usiniache hapa sitaki kufa mimi” mwenyewe alisalimu mari

“Umepewa nafasi unajifanya mbishi haya bishana na bomu hilo lisilipuke kama wewe mbishi kweli” Norbert alimuambia akiwa anafungua malngo.

“Nipo tayari kukuambia kila kitu naomba usiniache na bomu hili” Aliongea kwa unyonge sana.

“Ok Unaweza kuongea nakusikiliza au niondoke”

“Hapana hapana nitakuambia kila kitu, hakuna mtu huko ndani kwa sasa wote wametoka, ulinzi wa nyumba hii asilimia kubwa unaongozwa na mitambo na si walinzi wengi ukitaka kuzuia usionekane adui chukua rimoti ya geti na utembee nayo” Aliongea ukweli mwenyewe ambao ulimfanya Norbert arudi hadi pale alipokuwa amemfungia na akalichukua lile bomu, Norbert alilisimamisha muda wake wakulipuka kisha akamtazam Mlinzi huyo usoni.

“Rimoti ya kufungua geti hilo inafanya kazi umbali ule ilipo nyumba?”

“Ndiyo inafanya kazi kabisa hata ukiwa mbali zadi ya nje ya nyumba”

“Ok asante kwa maelezo yako ngoja nikusafirishe ulimwengu mwingine kwa dharura kidogo” Norbert alipoongea maneno hayo alimuachia pigo la kisogoni Mlinzi huyo hadi akazirai papo hapo.

Baada ya kumaliza kazi hiyo alichukua rimoti maalum ya kufungulia geti ambayo ilikua ikitumika kulifungulia geti hilo, alitoka ndani ya ofisi hiyo la mlinzi na kuelekea ilipo nyumba ya Wilson ambayo ndiyo ngome yenyewe iliyokuwa ikitumiwa na kundi zima ambalo kwa sasa limesalia watu watatu tu.


DAKIKA ISHIRNI KABLA YA MAPINDUZI

Kifaa maalum ambacho huwa anakitumia mlinzi wa ngome akiwa yupo mbali na eneo hilo ili kujua magari ya wakubwa zake yamefika, kilipiga mlio ambao ulimjulisha wazi Norbert kuwa kulikuwa na gari mlangoni. Norbert alipokitazama kifaa hicho aliona gari aina ya toyota hilux ya rangi nyeusi ikiwa ipo getini, gari hiyo ndiyo kwanza ilikuwa imefika na haikuwa hata imepiga honi kuamrisha geti lifunguliwe. Norbert alipokuwa akikitazama kile kifa aliona kabisa sura ya dereva wa gari hilo ambaye alimfanya atabasamu tu kwa kumuona kwake, alikuwa amemuona Josephine akiwa yupo kwenye usukani akiwa hapo getini.

Bila ya kuchelewa alibonyeza kitufe kimoja kwenye kifaa hiko na geti lilifunguka, gari hilo liliingia ndani na haukuchukua hata muda gari nyingine aina ya Range rover sport ilifika hapo getini. Norbert alikuwa akitazama kifaa hiko kwa umakini sana, alimshuhudia dereva wa gari hio akiwa ni Mzee Ole akiwa ndiyo anarejea Ngomeni akiwa amepishana na Josephine kwa sekunde kadhaa. Alilifungua geti kwa mara nyingine na gari hilo liliingia ndani kisha akalifunga, baada ya kufanya hivyo alitulia kimya akiwa yupo ndani ya nyumba hiyo kwa upande wa sebule wa kulia chakula akiwa amekaa kwenye eneo lenye giza akiwa anatazama kwa umakini sebuleni palipo na mwanga wa taa kubwa. Bado aliendelea kutulia paleaple kwenye eneo hilo akiwa anawasubiria kwa hamu maadui zake ambao alijua kabisa hawakuwa na silaha yeyote ya kujihami, silaha zote walizokuwa wanazitumia wao alikuwa amezikusanya na muda huo alikuwa ameziweka kwenye meza hiyo ya chakula akiwa anawasubiria kwa hamu sana.

Kila aina ya silaha ya kujihami alikuwa ameiweka hapo mezani hata zile silaha ambazo wao walikuwa wakizificha sehemu zisiwezekane kwa urahisi kutambulika kuwa kulikuwa kumefichwa sialha.

Muda ambao wenyeji wa eneo hili walikuwa hawajarejea ambao alikuwa amewahi mapema sana ndiyo alioutumia katika kupekua kila sehemu ya karibu na eneo hilo, maadui zake hawakuwa na hili wala lile juu ya uwepo wa mbaya wao ndani ya nyumba hiyo.

Norbert naye aliendelea kuvuta subira akiwa yupo ndani ya eneo hilo, macho yake yote yalikuwa yapo mlangoni akiwa na imani kwa asilimia zote lazima maadui zake watumie mlango huo kwani mingurumo ya magari yao ilikuwa imeishia kwenye eneo la kuegesha magari kwa dharura nje ya nyumba hiyo. Mingurumo ya magari hayo hadi inazimika alikuwa tayari ameshatambua kuwa maadui zake walikuwa wameegesha katika eneo la nje ya nyumba hiyo mitaa kadhaa kutoka baraza la nyumba hiyo lilipo. Aliendelea kusubiri akiwa ameuwekea moyo wake subira na si papara yoyote aweze kutimiza kile alichokuwa akitaka kukitimiza katika eneo hilo, milio ya viatu ilianza kusikika ikikaribia eneo la barazani katika nyumba hiyo ambayo nilimfanya akae tayari kwa lolote lile ambalo lingeweza kujitokeza ndani ya eneo hilo.

Kusikika kwa milio hiyo kuliendelea kusikika hadi kulipoikairibia mlango mkuu wa kuingilia nyumbani hapo, hapo milio hiyo ilitulia kwa muda ambapo ndiyo kulizdi kumfanya Norbert atege masikkio yake yaliyokuwa yanasikia sawia katika kusikiliza vizuri. Haikupita muda mlio wa kutiwa funguo katika kitasa cha hapo mlango ulisikika, mlio wa kutekenywa kwa funguo ndiyo ulifuatia na kisha kitasa kikanyongwa kwa nguvu sana.

Mlango ulifunguliwa na Norbert alimshuhudia Mzee Ole akiingia kwa pupa ndani ya nyumba hiyo, Josephine naye alifuatia kuingia ndani ya nyumba hiyo akiwa anatembea kwa taratibu tu akiwa anayatzama mazingira ya hapo ndani kama vile ndiyo kwanza alikuwa anayaona.

“Nilikwambia Wilson kasharudi huyu ona hii taa kaiwasha nani sasa wakati tuliizima” Mzee Ole aliongea

“Sasa kwanini aaache gari kule kwenye parking hadi muda nalichukua, amerudi na miguu kwahiyo?” Josephine aliuliza

“Punguza hofu Leopard Queen huyu kachangayikiwana na kummpiga risasi mtu si bure yupo huko juu anajinywea pombe” Mzee Ole aliongea kisha akatazama makini kule mezani chupa za pombe zikiwa zipo chini karibu na kingo ya sebule hiyo katika eneo ambalo giza ndiyo lilikuwa linaanza, akiwa hata hajatia neno lolote kuhusu zile chupa simu yake ya mkononi iliita ambayo ilimfanya aache kitazama chuo hizo.

“Ndiyo kijana sems….pole ya nini kijana mbona sikuelewi…ndiyo sijui chochte kinachoendelea hebu nijuze basi….unasemaa Wilson amekutwa na polisi akiwa ni mfu!” Aliongea baada ya kuipokea simu hiyo ambayo ilimfanya ashindwe hata kuendela kuishikilia na aliiachia ikaanguka hadi chini ikavunjika.

Josephine alikuwa amepigwa na mshngao sana aliposikia taarifa hiyo wala hakuwa amewaza juu ya kuwashwa kwa taa hizo ikiwa Wilson tayari kulikuwa na dalili tosha hakuwa amefika ndani ya nyumba hiyo. Alibaki akimtazama tu Mzee Ole ambaye uchungu ulikuwa umembana tayari ingawa machozi yalikuwa hayamtiririki kabisa, alikuwa ameinamisha kichwa chini. Ujasiri wake aliokuwa nao kipindi akiwa jeshini kabla hajaingia uwanja wa siasa ndiyo ulikuwa upo ndani ya moyo wake kwa muda huo ndiyo maana machozi hayakuwa yakimtoka kabisa, alikuwa asikitika kwa huzuni huku uso wake akiwa ameukunja kwa nguvu sana

“Aaaargh! Sasa naona ameamua kuikata furaha yangu, Aaaaargh!Norbert!” Mzee Ole aliongea kwa nguvu sana akiwa hajui kuwa huyo anayemuiita yupo hapo kwa umbali mita chache tu.

“My name(jina langu)” Norbert aliitika kidharaua na kusaabishwa wote kwa pamoja watazame kule kwenye sebule ya chakula kwa mshngao.

Mshtuko ndiyo uliyokuwa imeipata mioyo ya kina Josephine na Mzee Ole kwa kumuona Norbert akiwa mahala hapo katika muda ambao hawakutarajia kabisa atakuwepo, macho yalikuwa yapo upande ule wa meza ya kulia chakula wakionekana kutoamini kabisa kwa kile walichokuwa wamekiskiaa katika muda huo.

Hawakuweza kuona chochote katika upande ule wa meza ya kulia chakula kutokana na giza nene lililokuwa lipo upande ule kwa muda huo wa usiku, mapigo ya moyo ndiyo yalikuwa yakienda mbio zadi kuliko hata akili zao za kufikiri jinsi ya kukabili mtu hatari kama huyo aliyekuwa yupo ndani ya himaya yao katika muda ambao hawakutarajia kabisa kama angeweza kufika ndani ya himaya hiyo. Hakika wasiwasi huondoa kabisa uwezo wa kufikiri wa mwanadamu akiwa nao ndani ya moyo wake, hiyo ndiyo ilikuwa kwa Mzee Ole na Josephine baada ya kusikia sauti ya Norbert kaika eneo hilo tena ikionekana alikuwa akiwangojea kwa hamu sana kwa kipindi cha muda mrefu walichokuwa wametoka ndani ya Ngome yao.

Josephine aliyekuwa amevaa nguo ya mazoezi chini(trck suit) pamoja na fulana yenye ukosi mnene alikuwa ameingiwa na wasiwasi haswa alipofikiria kuwa ndani ya siku hiyo hawakuwa wamebeba silaha yao zaidi ya ile ambayo alikuwa nayo Wilson walipokuwa wanaenda kummaliza Mufti. Alijilaumu kabisa kwa kosa hilo alilokuwa amelifanya la kutobeba silaha akiwa anatoka ndani ya nyumba hiyo na laiti kama angelikuwa ameebeba angeweza kuitumia kwa muda huo akiwa ndani ya ngome yao penye uvamizi.

Hiyo haikuwa kwake tu bali hata kwa Mzee Ole aliyekuwa na lawama hizo ndani ya nafsi yake kwa kuacha silaha zikiwa zote zipo ndani ya maficho katika nyumba hiyo, Mzee Ole pia aliulaumu uamuzi wake wa kuwaambia kina Wilson na Josephine wasibebe silaha walipokuwa wanaenda tukioni ili wafanye tukio kimyakimya. Aliona muda huo laiti kama angekuwa amewaruhusu kubeba silaha basi angeweza kabisa kuwa na mtu ambaye angemmaliza Norbert ndani ya muda mfupi tu, hapo ndiyo aliona umuhimu wa kutembea na siaha hata akiwa anaenda kwa rafiki yake ili iweze kumsadia kwani laiti kama ndani ya muda huo angekuwa anayo basi wangekuwa ni wao wakijiamini na ingekuwa ni zamu ya Norbert kuwa na wasiwasi nao lakini siku hiyo walikuwa wamewahiwa wao na sasa hawakuwa na ujanja wowote ule ndani ya muda ambao hawakuwa wamemuona adui yao alikuwa yupo namna gani. Akili ya Mzee Ole tayai ilikuwa imefikia mwisho kabisa katika kubuni mbinu huku akili ya Josephine ikiwa imejiwa na mbinu mpaya kabisa ndani ya kichwa chake akiwa hata hajui kuwa kama angeweza kupata mbinu kama hiyo katika muda huo.

Josephine alikuwa amekumbuka uwepo wa silaha za dharurra ambazo huwa wanazichomeka hapo sebuleni, alikukmbuka kabisa kuwa silaha hizo ndiyo zingeweza kumkomboa ndani ya muda huo. Alizungusha mboni yake ya jicho kwa wepesi zaidi akaona kochi lililokuwa lipo karibu yake ambalo ni kochi la kukaa watu watatu, kitendo cha haraka alichokifanya baada ya kuona kochi hilo hilo ilikuwa ni kujibirisha kwa nguvu sana hadi jirani na kochi hilo. Alifanya ushupavu wa hali ya juu kwa kupiga teke sehemu ya kwenye kochi hilo aina ya sofa ambayo ni chini ya sehemu ya kukalia katika eneo ambalo mtu akikaa basi nyama za nyuma ya ugoko ndiyo hugusa. Alipofanya hivyo sehemu ya kukalia ya kwenye kochi ilifunguka kama mlango wa jokofu la kugandisha mabarafu,kwa haraka zadi alitia mkono ndani ya eneo ambalo mto wa kulaia wa kochi hilo ulifunguka akatoka na bastola aina ya IMD Desert eagle ambazo ndiyo silaha zao wanazozitegema katika kazi hizo.

Kitendo kingine cha haraka alichokifanya ni kupiga sarakasi kwa nguvu sana kwenda pembeni kutoka katika eneo ambalo lilikuwa mkabala na eneo alilokuwepo Norbert, eneo hilo alibakia Mzee Ole ambaye muda huo tayari alikuwa ameshaanza kutabasamu huku akimtazama Norbert.

“Sawasawa Norbert najua ndiyo jina lako na umajileta mwenyewe bila ya kukutafuta, karibu kwenye mdomo wa mamba kijana” Mzee Ole alianza kuongea kwa kejeli, huku akigeuza jicho akimtazama Josephine aliyekuwa yupo pembeni katika eneo kulikuwa na kitufe ambacho alikibonyeza.

Taa zilizokuwa zipo ndani ya sebule ya chakula ambazo hazikuwa zikiwashwa kwa umeme wa kawaida ziliwaka ndani ya muda huo na kumfanya Norbert aonekane akiwa amekaa kwenye kiti na wala hakuwa na wasiwasi wowote.

“Ulipozima taa hiyo kwa kutumia siwchi iliyopo hukohuko ulidhani ndiyo umezuia usionekane, hapana hujafnikiwa kuzuia usionekane Norbert kuna taa za sola ambazo haziwashwi na siwchi hiyo” Mzee Ole alizidi kuongea kwa dharau kisha akacheka kama vile siye yeye aliyekuwa akisikitika kwa kuambiwa taarifa ya kifo cha mdogo wake.

Josephine alisogea hadi pale alipokuwa amesimama Mze Ole na mkono wake mmoja ukiwa umeshika silaha ambayo alimuelekezea Norbert, uso wake ulikuwa na hasira sana hasa akikumbuka mtu huyo ndiyo alikuwa Muuaji mkubwa aliyeua wenzao na hata mpenzi wake. Alikuwa akimtazama Norbert kwa macho ya chuki sana akiamini kuwa siku hiyo ndiyo ilikuwa ni arobaini yake na hakuwa na uwezo wa kutoka kwa shabaha alizokuwa nazo akiwa ameshika silaha mkononi mwake, shabaha hadi muda huo ilikuwa ipo katika kichwa cha Norbert tu ili aweze kumuangamiza na si kuendelea kusikiliza ngonjera zake ambazo huzileta akiwa amewekewa silaha ili aweze kumpoteza adua yake lengo.

Mbinu hiyo tayari alikwisha itambua tangu siku ile alipoitumi kumuua Benjamin na sasa hakuwa tayari kuiruhusu imuhadae naye, alidhamiria kwa lengo moja tu ni kumuangamiza Norbert bila hata kuanza kusikiliza maneno yake ambazo huwa na maudhi pamoja na kukasirisha mtu ili amtoe nje ya lengo alilokuwa ameweka juu yake. Kukutana na Norbert katika sehemu tofauti kulimfanya amuelewe vizuri juu ya mbinu yake hiyo na hakuwa tayari kumruhusu aitumie ndani ya muda huo amuue yeye kama alivyowaua Thomas na Benjamin.

“Norbert jua leo ndiyo siku yangu ya kulipiza kisasi jihesabie umekwisha” Aliongea akiwa na hasira sana kwa mwanaume huyo aliyelala naye zaidi ya mara moja.

“Ohoo unataka ulipe kisasi kwa mimi kumuaa mpenzi wako siyo nadhani ushachelewa kabisa Josephine a.k.a Leopard Queen, Mungu hakupenda kabisa nife na bastola hiyo uliyoishika hivyo huwezi kuniua wewe” Norbert aliongea kwa kujiamini.

“Anhaa! Nidyo uanvyojidanganya hivyo sasa jihesabie umeenda wewe na sikupi nafasi utoe ngonjera zako zenye maudhi kama ulivyofanya kwa mpenzi wangu ukampoteza lengo na kumuua. Kwaheri Norbert” Aliongea kisha akakiminya kitufe cha kufyatua riasi mara moja shabaha ikiwa kwenye kichwa cha Norbert.

DAKIKA TANO KABLA KUTIMIA SAA SITA KAMILI USIKU

Muda huo tu ulipofikia tu M,J Belinda alichukua simu yake ya mkononi na kuanza kutuma ujumbe uliojaa kielelezo katika sehemu mbili tofauti, baada ya kuhakikisha kuwa kila kitu kip sawa alikiweka vizuri kinasa sauti kisha akawa anatzama mbele kwenye mitambo ya Tarakilishi ambayo ilikuwa ikionesha wazi ramani ya eneo walilokuwepo hapo.

“Kaeni tayari masection kamanda wote kwa ajili ya kazi, Platoom sajenti wote anza kupanga watu wako vizuri mmenipata?!” Aliongea kwenye kinasa sauti chake kisha akamgeukia kijana aliyekuwa akichakarika na tarakilishi kuangalia maeneo yote yaliyokuwa yamezunguka wenzao.

“Hakikisha unakava wenzako vizuri hawa wapizani wenu hawako nyuma yenu tu bali wapo hata pande zingine, usiweke macho kenye upande huo weka macho hata huko nyuma ya Ikulu vijana wakigeuka kwani kwani adui anaweza kutokea mahali popote pale ndani ya muda wowote. Tunaelwana” Alimpa maelekezo huku akitazama muda ulivyokuwa unayoyoma na ulikuwa umebaki ni dakika tatu yaani saa sita kasoro dakika tatu usiku kuweza kutimia siku ya mapinduzi yaliyokuwa ymeendaliwa na kina L.J Ibrahim na washirika wake


Upande wa wanajeshi wa maji L.J Ibrahim alikuwa yupo ndani ya moja ya Nyambizi akiwa anaangalia kila kitu jinsi kilivyokuwa kikiendelea ndani ya muda huo. Hali iliyokuwepo ndani ya muda huo ilikuwa ni ya kuridhisha sana kwa asilimia kwa mia moja kiupande wake, alikuwa akifanya kila aina ya mwasilianao na vijana wake waliokuwa wapo nchi kavu na hao waliokuwa wapo majini waliokuwa wamebakishwa kama kikosi cha akiba ikiwa makomandoo waliopo ndani ya Ikulu wataweza kuwazidi vijana wake kutokana na opersheni haikutakiwa kutumia siala nzito ya aina yoyote ile ambayo ingesababisha uharibifu ndani ya ikulu iliyokuwa na mpango pakipambazuka ili Mzee Ole ndiyo awe mtumiaji wa Ikulu hiyo kwa miaka yote iliyobakia na ataendelea kutawala. Akiwa amekaa hapo akiwa tazama vijana wake waliyokuwa wapo kwenye mitambo ya tarakilishi aliona kila kijana wake akitoa simu ya mkononi ndani ya muda huo, vijana hao waliangalia simu zao hizo kisha wakazirudisha kwenye suruali zao.

“Hey nyinyi nani kawaruhusu kuingia na simu kwenye operesheni kama hii, haya kaziwekeni chumba chenu cha kubadili nguo kwenye makabati na mziffungie mrudi hapa” L.J Ibrahim aliwakoromea, aliona kama alikuwa anawawajibisha lakini hakujua kama alikuwa amefanya kosa kubwa sana kuwaruhusu hao vijana waende kwenye cumba chao hicho.

Vijana hao walitii na kunyanyuka kwenye viti vyao na muda huo wakimuacha akiwa ameshika simu ya upepo, walipotea katika upeo wa macho yake kwenda huko kuziweka simu alipokuwa amewaamuru.

“Eeeeeh! Mugiso hakikisha vijana wanakava pande zote hawa wa huku nimewaondoa mara moja wameingia na simu eneo la kazi” Aliongea kwa kutimia simu ya upepo.

“Mkuu” Sauti ya Mugiso ilisikika ikitii amri ya L.J Ibrahima liyokuwa amempa ndani ya muda huo

SAA SITA KAMILI USIKU

Sauti ya vyuma vikilia baada ya kubonyezwa kifyatulio cha bastola ndiyo ilisikika ndani ya muda huo ambao Josephine aliifyatua bastola yake ili alipe kisasi cha kuuawa kwa mpenzi wake, ulikuwa ni mlio ambao uliokuwa ukiashiria kuwa bastola hiyo haikuwa na risasi ndani yake. Josephine alibaki akiwa amepagwa sana kutoka na hali hiyo aliyokuwa ameiona ndani ya muda ambao alikuwa akitarajia kumundoa Norbert ndani ya dunia hii kulipa kisasi chake.

“Nilikwambia Mungu hakunipangia niuliwe na bastola hiyo uliyokuwa umeishika nadhani hukunielewa nafikiri sasa maana ya maneno hayo niliyokwambia umeipata” Norbert alimwambia huku akimtazama akiwa anatabsamu tu.

“Wakati naingia ndani ya nyumba hii nilipekua kila sehemu na nikaziona silaha zenu zote na ndiyo hizi ninazo hapa mezani muda huu, nilikuachia moja tu ambayo ndiyo hiyo niliyoitoa risasi nikijua mtajifanya wajanja sana mkijiona ni wenyeji ndani ya nyumba hii. Komandoo na ninja kama mimi huwa sina ugeni na nyumba yoyote iliyopangwa silah kijeshi. Mbinu zote mnazozitumia ni mbinu ambazo si ngeni kwangu first class wa EASA” Norert aliwaambia.

“Hata kama Norbert leo ufe wewe au tufe sisi ila hutatoka ndani ya nyumba hii kukosa silaha haimaanishi ndiyo hatuwezi kupambana” Mzee Ole alioongea huku akikunja mikono ya shati lake. Josephine naye aliitupa bastola chini

“Ohooo kumbe ngoja sasa niondoe hizi zana” Norbert aliwaambia kisha akachukua silaha zote alizokuwa amezichukua akafungua dirisha na kuzituoa nje, alipomaliza hivyo alitembea mwendo wa taratibu sana akawa anawafuata maadui zake waliokuwa wamekaa tayari kwa ajili ya kupambana naye.

Kitendo cha yeye kutia mguu kwenye ardhi ya sebuleni ilikuwa ni kukaribishwa kwa mateke mawili ya kwa pamoja kutoka kwa Josephine aliyoyaachia kwa kasi kubwa sana, aliyapangua yote yakawa yamekosa lengo. Hajakaa sawa Mzee Ole alileta masumbwi imara kabisa tofauti na Norbert alivyotarajia kutoka kwa Mzee huyo ambaye hakuwahi kumuona hata mara moja akipambana, Maumbwi hayo aliyumba kushoto la mkono wa kulia likapita na aliyumba kulia la mkono wa kushoto likapita. Hata kabla hajatahayari alisikia teke la kifua likimpiga kutoka kwa Josephine hadi akaanguka chini papo hapo lakini aliwahi kujibiringisha kiufundi akakaa sawaa tena kuweza kupambana na nao. Norbert alijitazama sehemu ya kifuani akaona alama ya kiatu cha Josephine kwenye shati ambayo aliipangusa kwa mikono yake kisha akalegeza vifungo vya shati lake na akafungua mikono ya shati na akaikunja vizuri.

Aliwafuata wote kwa pamoja ambapo kwa Josephine alikutana na ngumi ambayo aliipangua kisha akamuachia konde zito la kwenye komwe lililompeleka hadi chini, Mzee Ole alimlenga na teke la kwenye kisogo ambalo lilimkosa baada ya kuinama kisha akauchota mguu wake ambaye alienda kupigiza mgongo wake kwenye sakafu.

Hakutaka hata kuwapa nafasi alimfuata Josephine ambaye ndiye alikuwa akijiinua hapo chini alipokuwa, alimshambulia kwa ngumi mfululizo kisha akampiga teke la nguvu la bega ambalo lilisababisha ayumbe hadi akajigonga kwenye ukuta akaanguka chini tena. Alipohakikisha Josephine yupo chini alitaka kugeuka kumfuata Mzee Ole lakini aijikuta akisukumwa na teke la mgongo, alipogeuka alikutana na Mzee Ole akija huku katanguliza miguu mbele kwa mateke ya kumaliza mchezo. Norbert alihama pembeni kwa haraka sana kisha akamuachia Mzee Ole teke la mbavu akiwa bado yupo kulekule juu hadi akaruka kwenye meza ya kulia chakula iliyokuwa ipo upande huo alipomsukumia. Meza hiyo ilivunjika papo hapo kutokana na uzito aliokuwa nao Mzee Ole.

Hakutaka hata kusubiri kwa nusu dakika alimfuata Josephine ambaye alikuwa akijizoa chini kwa muda huo aweze kusimama, alimpa teke la chini ya kidevu ambalo hupigiwa sehemu chini ya vidole vya miguu hadi damu zake zikaruka. Josephine aliyumba kutokana na pigo hilo na hata kabla hajaugulia maumivu ya pigo hilo Norbert alimpiga mateke mawili ya sehemu zote za mbavu kushoto na kulia kisha akamshindilia na teke la miguu miwili kifuani. Josephine alienda kujipigiza kwenye mlango wa kuingilia ndani sehemu ya mgongoni na kisha akawa anasambaratika sakafuni, hata kabla hajafika chini alikutana na teke jingine la uso kutoka kwa Norbert ambalo lilimfanya arushwe pembeni akaenda kujigonga kwenye ukingo wa kochi ambao huwa na mbao ngumu tu pasipo kuwepo kwa godoro laini.

“Sikuwahi kuwaza kuwa nitakuja kupigwa teke na mtoto wa kike kijinga namna hiyo” Norbert aliongea kisha akamnyanyua Josephine akiwa hatamaniki kwa jinsi alivyokuwa akivuja damu usoni mwake, alimpiga ngumi mbili za nguvu sana kwenye taya kisha akamuongeza teke jingine la kifuani ambalo lilimfanya adondokee kwenye kochi.

Hakutaka kumuachia apumzike hata kidogo akiwa kwenye kochi alimvuta nguo yake akaanguka hadi chini na akamuongeza teke jingine la mbavu hadi Josephine akaachia mguno wa maumivu ambao haukushawishi Norbert amuonee huruma zadi ya kumsonya tu.

Alimshika ukosi wa fulana yake aliyokuwa ameivaa akamuinua juu lakini hata kabla hata hajampa pigo jingine alisikia ukelele wa Mzee Ole ukitoka nyuma yake, ukelele huo ulimjulisha wazi kuwa alikuwa amebeba kitu ambacho alikuwa akija kumpiga nacho kutokana na jinsi alivyokuwa akiutoa. Ulikuwa ni ukelele ambao ulishiria alikuwa akiachia pigo la kutumia zana ya mkono, Norbert aliupousikia hakutaka kufanya kitu kingine kingine chochote aliuachia ukosi wa fualna ya Josephine kisha akaruka pembeni kwa haraka sana.

Kitendo cha kusogea pembeni tu alipishana na upepo mzito wa kuletwa kwa chuma cha kuchomekea pazia ambalo lilimkosa na likatua kwenye mgongo wa Josephine ambaye alitokwa na damu mdomoni kisha akatoa ukelele akaenda sakafuni.

Mzee Ole alipoona amekosa lengo lake na akampata mtu mwigne hakutaka kabisa kuwa na muda wa kujilaumu yeye alinyanyua chuma kupeleka upande ule kule aliokuwa Norbert yupo lakini hata kabla hajalifikisha alikutana na teke la mbavu la pembeni kutoka kwa Norbert hadi chuma likamtoka mkononi akiwa hajakaa hata sawa alikutana na mvua ya ngumi kutoka kwaa Norbert ambazo zilimrudisha kwa nyuma katika upande ambao kulikuwa na mlango wa kioo. Ngumi hizo zilimfanya aegmee kioo lakini kabla hajafanya jambo jingine lolote, teke zito kutoka kwa Norbert lilimpata pale alipojaribu kusogea mbele kumkabili hadi akarudi nyuma akavunja kioo akaingia ndani ya mlango huo. Alienda kupigiza mgongo wake katika sehemu yenye mtungi wa gesi wa kuzimia moto hadi akaanguka chini na akatulia papo hapo.


Ilipotimia saa sita kamili usiku L.J Ibrahim alitoa amri kwa kikosi cha M.J Belinda kuanza kazi, pia aliamrisha kikosi cha vijana wake kiichoppo chini ya M.J Mugiso kuanza vilevile.

Amri hiyo ilipofiika kwa M.J Belinda alikipa amri kikosi chake tofauti na amri aliyokuwa ameitoa mkuu wake kicheo, M.J Belinda yeye alikiammrisha kikosi chake waipe mgongo ikulu na kuelekeza silaha zote upande ambao kipo kikosi cha majini kikiwa kimeleekezza silaha zao.

“Viongozi wa kombania zote kaeni tayari kwa lolote, iwe kufa au kupona lengo letu ni kumlinda Amiri jeshi mkuu tu, fagio la chumaaa” M.J Belinda aliongea

“Fagiaaaaa” Sauti ya wanajeshi wake ilisikika huko nje ambayo ilimfanya atoe tabsamua tu. Baada ya kutoa amri hiyo sauti ya kukoroma kwa simu yake upepo ilisikika ndani ya muda huo ambayo ilimfanya aiweke jirani na mdomo wake.

“Wee! Belinda kwanini unaenda kinyume na amri zangu unamtetea msaliti na unapinga amri za mkuu wako” Sauti ya L.J Ibrahim ilisikika.

“Siwezi kupinga amri za senior kuliko wote ambaye akiwepo wewe na yeye huwa nalazimika kumpigia saluti yeye tu na siyo wewe msaliti uliyemuua General kwa tamaa ya pesa. Pia umeua wengine wengi kisa tu Ole arudi madarakani, mkuu wangu ni Amiri jeshi mkuu tu na si wewe” M.J Belinda aliamua kumwambia ukweli L. Ibrahima ambao ulizidi kumchanganya sana.

Baada ya kutoka kwa amri hiyo L.J Ibrahim akiwa anajishughulisha kukuna kichwa chake aangalie mbinu nyingine ya kufanya ghafla kikosi chote cha majini kilichokuwa kipo chini ya amri yake nacho kiligeuka nyuma kikawa kimekaa kama walivyokuwa wamekaaa kikosi cha rdhini kuilinda Ikulu.

“Fagio la chumaaa!” Ilisikika sauti ya M,J Mugiso ikiongea kwenye kipaza sauti kilichopo ndani ya hema na sauti ikasambaa nje

“Fagiaaaaa!” Sauti ya wanajeshi la maji pamoja na nchi kavu wote kwa pamoja zilisikika zikiitikia, muda huo huo ndege za kivita za jeshi la anga zilianza kurandaranda kuizunguka ikulu hiyo kuongeza ulinzi kwa Rais Zuber

KIFO CHA NYANI MITI HUTELEZA

L.J Ibrahim hakuamini macho yake kwa kile alichokuwa akikiona ndani ya muda huo akiwa yupo nyuma ya vijana wa kikosi cha maji waliokuwa wapo ndani ya Nyambizi, ajabu ilipotolewa tamko la pili la fagio la chuma na M.J Mugiso hadi vijana hao waliokuwa wapo nyuma ya tarakilishi walinyoosha ngumi zao na kusema neno ‘fagia’.

“Hey! Nyinyi ndiyo nilichowaamrisha hiko!” Aliwakaripia wote kwa pamoja na kupelekea vijana wote waliokuwa wamempa mgongo wageuze viti vyao vya kuzunguka na kumtazama L.J Ibrahima ambaye alikuwa mpole mwenyewe kwa kile alichokionea. Vijana wote walikuwa wameshika bastola na walimuelekezea kwa pamoja akawa hana ujanja wowote, alibaki akiwa haamini kile kile kilichokuwa kimetokea.

“Mnafanya nini nyinyi?” Aliwauliza akiwa na taharuki kuu moyoni mwake

“Tunatimiza wajibu wetu wa kulilinda taifa hili dhidi ya wavamizi na wasaliti kama wewe, umeshiriki kumuua General hata Mufti alitangaza ila mkamuua tena halafu unataka kumpindua Rais aliyeboresha jeshi na maslahi yote ya wanajeshi” Mmoja wa wale maaskari wataalamu wa tarakilishi alimuambia.

“Tena simu zetu zilipoingia ujumbe mfupi kutoka kwa Madam Belinda ulikuwa ni video na picha ya kile unachokifanya kwa maslahi binafsi angalia mwenyewe” Askari mwingine alimrushia simu ya mkononi ambayo aliifungua akakuta kila kitu ambacho kilimfanya azidi kunyongea akiona hana ujanja mwingine tena.

“Maluteni mimi si mkuu lakini shusheni silaha zenu chini” Alijipa ujasiri na kuongea kuangalia kama wangeweza kutii mari hiyo.

“Hatukutambui kama mkuu wetu zaidi ya kuwatambua Amiri jeshi mkuu, Meja jenerali Belinda na Meja jenrali Mugiso basi wewe si mmoja wetu na hapa tupo kwa ajili ya kukumata ufike kule unapostahiki kufika msaliti kama wewe. Afande mkamate huyo” Luteni yule wa kwanza kuongea alimpa amri mwenzake ambaye alinyanyuka na kwenda kumtia nguvuni L.J Ibrahim.

“Hey! Mnafanya nini mimi ni three star general mkubwa wenu” Alilalalmika wakati akitiwa nguvuni na luteni huyo.

Baada ya kumuona Mzee Ole amesambaratika sakafuni Norbert aliamua kumsogelea Josephine ambaye alikuwa amelala kfudifudi, alimgeuza na kumfanya alale chali kisha akamtazma hali yake. Alimkuta akiwa anakoroma tu akiwa hajitambui kutokana na chuma lile kutua kwenye mgongo wake, alimtazma kwa muda kisha akaachia tabasamu hafifu sana.

“Ndiyo malipo yako hayo hutopata nguvu mpaka matibabu wakati ukija kutiwa nguvuni na polisi” Aliongea akiwa na uhakika kuwa hakuwa na anamsikia, alipoongea mameno hayo alirudisha macho yake kule alipokuwa yupo Mzee Ole akajikuta akitokwa na mguno wa mshangao.

Mzee Ole hakuwepo kwenye eneo alilokuwa ameanguka hapo awali na hakujua alikuwa ameelekea wapi, alipoangalia vizuri katika eneo ambalo alikuwa ameangukia kwa pembeni aliona kuna mlango ambao haukuwa ukijulikana hapo awali wala hakuuona ukiwa umefunguliwa na kurudishwa tu. Norbert alitoka hadi ulipo ule mlango na akaufungua taa za mwanga mkubwa ziliwaka humo ndani ambapo aliweza kuona ndani ya mlango huo kulikuwa kuna nini, Kulikuwa na ukumbi mrefu sana uliokuwa umetengenezwa kwa muundo wa duara kama ilikuwa wanapita ndani ya bomba. Norbert aliamini kwa asilimia zote kuwa Mzee Ole atakuwa amepitia njia hiyo kuweza kumkimbia, aliamua kufunga mlango ili aweze kumkimbilia lakini alipoufunga alijikuta akiwa hana namna.

Kitendo cha mlango ule kufungwa tu taa za mahala hao zote zilizima na kisha mionzi mekundu ikajitokeza kwa mbele ambayo alikuwa akiijua wazi ilikuwa ikiunguza ikiwa ikigusa mwili wa mtu.

“Oooh Damn it!” Aliongea kwa hasira na akaufungua tu mlango huo na taa zote zikawaka mionzi hiyo ikapotea, aliamua kukimbia kwa kasi kwani mlango ule ulikuwa ukipitisha muda ulikuwa unajifunga wenyewe.

Hii aliijua kwakuwa aliamini Mzee Ole hakuwa amepita katika mlango huo ukiwa umejifunga na ulijifunga wenyewe. Kwa kasi yake pamoja na pumzi zote alifanikiwa kulivuka eneo lenye mionzi ile yenye rangi nyekundu akatokea kwnye eneo lenye mfuniko unaoingia chini, Norbert aliungua mfuniko huo tahadhari kisha akachungulia chini. Aliona kulikuwa na maji mengi yakiwa yamekusanyika kwenye eneo lililojengewa kama bandari, eneo aliokuwa ameliona huko kwa mtazamo kabisa alilijua likuwa limechimbbwa kuelekea baharini ndiyo maana maji hayo ya baharini yalikuwa yakiingia hapo ndani kwenye bandari hiyo ndogo sana. Alipoangaza vizuri ndani ya eneo hilo alimuona Mzee Ole akihangaika kuwasha boti iliyokuwa imeegeshwa jirani na eneo hilo, hapo alitambua kabisa Mzee huyo alikuwa akipanga kutoroka baada ya kuona ngoma aliyokuwa anaicheza ilikuwa imemzidi uwezo. Norbert hakutaka kabisa kupoteza muda yeye aliingia ndani ya mfuniko huo na alishuka chini kwa kutumia ngazi za chuma zilizokuwa zimejengewa kwenye mfuniko huo.

Alishuka kwa haraka sana lakini alipokuwa yupo katikati ya ngazi hiyo ndiyo boti hiyo aliyokuwa akihangika Mzee Ole kuiwasha iliwaka, alizidi kuongeza kasi ili amuwahi lakini alipofika chini tayari Boti ya Mzee Ole ilikuwa imeanza kuondoka. Norbert aliikimbiza kwa pembeni boti hiyo akiwa na lengo la kurukia lakini Mzee Ole aliongeza mwendo ikamuacha mbali kabisa, ilimbidi asimame na arudi pale kwenye maegesho ya boti hizo akachukua boti nyingine ambayo aliiwasha kisha akaigeuza kuelekea kule alipokuwa ameelekea Mzee Ole. Alimkimbiza kwa nguvu sana akiwa anapita ndani ya njia hiyo iliyo na upana kiasi ikiwa imejengewa mithili ya njia mtaro wa maji mkubwa, aliongeza kasi ya boti hadi akafanikiwa kuiona boti ya Mzee Ole ikiwa ndiyo ipo kwenye mlango wakutokea humo ndani ambao ulijifungua ikatoka nje. Naye aliongeza mwendo hadi akafanikiwa kutoka nje na sasa wakawa wametokea jirani na ufukwe wa Msasani kwenye eneo lenye mawe sana, ule mlango uliojifungua kwa nje ulikuwa na umbile la jiwe ambapo ni ngumu sana mtu kutambua kuwa huo ni mlango.


Baada ya kuhakikisha kuwa ulinzi wa kuilinda Ikulu M.J Belinda na M.J Mugiso walikutana na wote wakasimamaa sehemu moja wakiwa jirani kabisa na Nyambizi aliyokuwa ameingia L.J Ibrahim, haikuchukua hata muda mrefu I.L Ibrahim alitolewa akiwa ameshikwa vilivyo na wale maluteni wenye jukumu la kuongoza Tarakilishi zilizopo ndani ya Nyambizi hiyo. Aliletwa hadi mbele ya maaskari hao ambao walikuwa wadogo kwake kicheo ambao kwa muda huo tayari walikuwa wakimuona dhalili sana, alipofikishwa mbele yao alishindwa hata kuwatazama kutokana aibu iliyokuwa imemuingia juu ya kile alichokuwa akikifanya na sasa kimemuondolea thamani chote.

“Ukiwa mpigaji mzuri wa chenga basi ujue na kukwepa rafu Ibrahim si Luteni jenerali tena, ona sasa hujui kukwepa rafu umepigwa rafu kwa chenga zako haramu. Kwa sasa wewe haikufai kuvaa vyeo kama hii ukiwa unalidhalilisha jeshi tukufu hebu mtoeni” M.J Belinda aliongea na kwa pamoja maluteni wawili walishika vifungo vya mabegani vya kombati alilokuwa amelivaa L.J Ibrahim wakavifungua kisha wakavitoa vyeo alivyokuwa amevishwa Ibrahim, hawakuishia hapo walitoa hadi pongezi zilizpo juuu ya mifuko kifuani ya kombati lake. Baada ya hapo maluteni hao walimsukuma hadi alipokuwa yupo M.J Belinda akiwa amesimama na M.J Mugiso.

Alimpofikia tu M.J Belinda alikutana na teke kali sana la pembeni ambalo lilimpeleka chini moja kwa moja akabiringita hadi katika upande ambao kulikuwa na wanajeshi wakiwa wamesimama ambapo aliangukia miguu wako.

Akiwa ameangukia hapo chini L.J Ibrahim akili ilimcheza kwa haraka na akaona njia pekee ya kuweza kujiokoa ni kuwatumia hao wanajeshi na si vinginyevyo, hakutaka kupoteza miguu alimchota miguu mmoja wa wanajeshi hao na akachukua silaha ya Mwanajeshi huyo kisha akasimama wima na kuilekeza kule alipo M.L Belinda na M.J Mugiso.

“Sasa sifi peke yangu bali nakufa na mmoja wa wakubwa zenu” L.J Ibrahim aliongeaa akiikoki bunduki hiyo ambayo ilikuwa tayari imeshakokiwa na kupelekea risasi moja iruke nje katika sehemu ya kutoa maganda ya risasi.

Alikuwa kaishika vizuri bunduki aina ya AK47 akiwa amewalekezea wakubwa waliokuwa wapo katika eneo hilo, alipotaka kuifaytua tu alikutana na mvua ya risasi kutoka kwa wanajeshi wengine ambazo zilimpata katika sehemu mbalimbali za mwili wake na huo ndiyo ukawa mwisho wake wa kufanya mabaya yote aliyokuwa ameyafanya akiwa mkubwa jeshi.

“Mshahara wa dhambi ni umauti tu, Mugiso tangaza operesheni fagio la chuma imefanikiwa” M,.J Belinda aliongea na M.J Mugiso alipiga saluti kisha akaelekea eneo lenye kipaza sauti kwa ajili ya kutangaza.


Baada ya kusikika rai ya fagio la chuma kwa vikosi vyote hadi wanausalama waliokuwa wapo humo ndani ya Ikulu waliitikia, tumaini la kurudi madarakani ndiyo lilirudi katika uso wa Rais Zuber aliposikia operesheni hiyo yenye kuondoa wasalitiwa taifa ikiwa imeungwa mono na wanajeshi wote wa jeshi la wananchi wa Tanzania. CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Furaha ndiyo ilizidi kupita maelezo alipoona kuwa alikitarajia kurudi tena katika imani ya wananchi wake, haikuchukua hata muda mlio wa fataki ulisikika kwa nje huku wanajeshi wakishangilia. Alipochungulia nje aliona neno “fagio la chuma’ likiwa limejichora angani. Furaha aliyokuwa nayo ilimzidi kabisa akajikuta akitoka nje kwenda kuangalia, baadhi ya wainzi walifutana naye kwenda kuhakikisha anakuwa salama ndani ya muda huo wote anaokuwa yupo huko.

Haikuchukua hata muda toka toke nje M.J Mugiso alitangaza juu ya kufanikiwa kumuondoa duniani msaliti wa taifa ambaye alikuwa akijaribu kuwashambulia alipokuwa chini ya ulinzi. Alitangaza opersheni hiyo ilikuwa imefanikiwa kwa muda huo na sasa Amiri jeshi mkuu atabaki kuwa Rais Zuber tu na si vinginevyo, furaha ilimzidi sana aliposikia kauli hiyo na hakuamini kabisa wanajeshi waliokuwa wamepanga kumtoa madarakani ndiyo hao waliamua kumtetea.

Mwenyewe aliamua kutoka hadi nje ya ikulu akiwa yupo na walinzi wake, wanajeshi waliokuwa wapo nje ya eneo la Ikulu waliipata taarifa yake ya kuja nje ya Ikulu na walijipnga vizuri kiheshima. Rais Zuber alifika hadi walipo wanajeshi hao ambao wote walipiga saluti kiheshima, alifika hadi pale ulipokuwa upo mwili wa L.J Ibrahim na akautazama kisha akatikisa kichwa kukubali kazi ya vijana wake.

Baada ya hapo aliomba kipaza sauti ambapo kililetwa cha dharura hadi mbele yake, alikipokea kipaza sauti hicho na kukiweka jirani na mdomo wake.

“Najivunia sana kuwa na vijana kama nyinyi ndani ya nchi hii mliokataa kufuata amri za msaliti huyu wa taifa na kufuata amri zangu, ujasiri wenu na uzalendo wenu mlionionesha usiku huu wa leo ni ishara tosha kwa maadui wa taifa hili watambue kuwa ndani ya taifa hili hakuna mchezo na wala wanausalama wake hawafai kuchezewa niwapongeze kwa hilo vijana wangu. Operesheni fagio la chumaaa!” Aliongea na kisha mwishoni akamalizia rai ya operesheni hiyo ambayo inafanyika kwa mara ya pili.

“Fagiaaaa!” Wanajeshi wote waliitikia kwa pamoja.

Hadi muda huo operesheni inakaribia wale wasiolala wakiona kuna mahala kutawapa ugali wa siku tayari walikuwa wameshafika eneo hilo na walikuwa wakirusha moja kwa moja kila kilichokuwa kikiendela, ni waandishi wa habari wa vyombo vya habari mbalimbali duniani tayari walikuwa wamefika katika eneo hilo wakiwa na vifaa vyao wakiorusha kile kilichokuwa kikiendelea.


Ndani ya maji ya bahari ya hindi kwa usiku huo ulikuwani mfukuzano mkubwa sana baina ya Mzee Ole na Norbert, Mze Ole akijaribu kukimbia na Norbert akijaribu kumtia nguvini msaliti huyo wa taifa. Hadi mafataki hayo yanalia wao walikuwa wapo ndani ya maji wakiendelea na mfukuzano huo, Mzee Ole alipoona maandishi ya operesheni fagio la chuma angani tayari alikuwa ameona hali ya kukata tamaa ikiwa ipo mbele yake kwa muda huo na alijua tayari mambo yameharibika. Hakutaka kusimama yeye alizidi kuongeza mwendo wa boti na kuzidi kumkimbia Norbert ambaye alikuwa nyuma kwa mita kadhaa aweze kumfikia, alikuwa akimtazama Norbert kila muda ilia jue alikuwa amefikia wapi muda huo. Walizidi kutokomea katikati ya bahari ya hindi wakiwa wanaelekea mashariki, ndani ya usiku ambapo bahari ilikuwa imetulia wao ndiyo walizidi kuleta fujo na kuzidi kuyatibua maji. Norbert aipoona anazidi kuelekea mbali zadi alitoa simu ya mkononi na mkono mwingine akawa ameshikilia usukani, alipiga namba zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye simu yake na akaiweka sikioni.

“Salum nenda kwenye ile nyumba ya Wilson ukamtie pingu yule Josephine sasa hivi amezorai utamkuta sebuleni” Aliongea baada ya simu kupokelewa kisha akaikata na kuirudisha mfukoni.

Siku zote kama mtu hakuwa ameangiwa atoroke basi hawezi kutoroka kamwe, Mzee Ole alikuwa akikimbia aweze kutoroka lakini hakuwa anatambua kamwe kilichokuwa kipo mbele yake huko anapoelekea. Laiti kama angelikitambua kilichopo mbele yake basi asingejaribu kukimbia kuelekea huko anapoelekea, akiwa anazidi kutokomea huko katikati ya bahari ya Hindi mbele aliona meli kubwa ikija kwa mwendo wa taratibu sana akiwa ameacha nayo kwa umbali mfupi. Mzee Ole alijaribu kuikwepa meli lakini usukani wa boti hiyo ulipinga amri yake na haukukata kona hata kidogo, alibakia akiukata usukani huo na kuunyoosha huku mapigo yake ya moyo yakimuenda mbio lakini hakuweza kabisa kukata kona. Akili ya kuruka pembeni hakuwa nayo kabisa kwa muda huo bali alikuwa ametawaliwa na akili ya kukata kona tu aweze kuikwepa hiyo meli, wala hakujua kabisa kuhangaika huko kukata kona ndiyo alikuwa anazidi kukairibia hiyo meli kubwa.

Alikuja kupata akili ya kuruka tayari alikuwa yupo karibu na meli hiyo na hakuweza kufanya hivyo, kwani kishindo kikubwa ndiyo kulifuatia baada boti yake kugonga meli hiyo na kisha mlipuko ukachukua nfasi yake.

Mzee Ole pamoja na udhalimu wake ndiyo akawa ameishia namna hiyo akijaribu kuukimbia umauti ambao hakujua ulikuwa upo huko anapoelekea, alisahau kuwa umauti humzunguka mwanadamu katika kila pande aliyopo hadi yanamtokea hayo.

Norbert alipoona tukio hilo alipunguza mwendo wa boti yake na kisha akaigeuza kurudi kule alipokuwa ametoka baada ya kazi yake kukamilika, aliongeza mwendo ambapo alitumia muda mfupi tu akawa amefika ufukweni akaiacha boti hiyo na karejea kule ilipo ile nyumba ya Wilson. Alifika akakuta magari ya kampuni ya kipelelezi ya EASA nje na ndani ya nyumba hiyo huku wapelelezi wa idara ya open service wakiendelea na uchunguzi mdogo, aliiingia ndani kabisa ya nyumba hiyo akakutana na Salum aliyempa ile kazi ya kumkamata Josephine.

“Vipi umemkamata?” Alimuuliza

“Sijamkuta nimekuta tu damu zikiwa zipo sakafuni” Salum alijibu.

“Shit! Bora ningemmaliza tu huyu mwanamke sasa katoroka”

“Inaonekana ni ana mafunzo ya ziada”

“Nahisi atakuwa hatari huyu mbele kama akipona kwa kipigo kile, kwa sasa kazi imeisha ngoja nikampumzike endeleeni na kazi”

“sawa mkuu”

Norbert alitoweka ndani ya eneo hilo akiwa amemaliza kazi yake, aliacha watu wengine ambao wakionekana na polisi si shida ila yeye hakutaka kubaki hapo kwakuwa hakutakiwa aonekane na wengine wowote zadi ya majasusi wenzake,


WIKI MOJA BAADAYE

UWANJA WA NDEGE WA KIMATAIFA MWALIMU NYERERE

Eneo la kusubiri wanaowasili na ndege walikuwa wamekaa Norbert, Moses, Norene,Jerry, Dokta Hilary na Irene, wote kwa pmoja walikuwa wamekuja kumpokea mgeni wao ambaye ndiyo kwanza alikuwa hajawasili ila masaa yake ya kuwasili ndiyo yalikuwa yakikaribia.

Baada ya nusu saa ya kumsubiri mgeni wao hatimaye watu walianza kutoka katike eneo hilo la kuwasili wageni, Moses alipoona watu hao alisimama juu akiwa na hamu kabisa ya kumsubiri huyo mgeni aliyekuwa anawasili. Haikuchukua hata muda mrefu Beatrice alionekana akija huku akiburuza begi, Moses alipomuona alimkimbilia akaenda kumkumbatia mke wake ambaye hakuwa ameonana naye kwa muda mrefu sana. Hakujali watu waliokuwa wapo katika eneo hilo yeye alionesha furaha ya ukweli ya kumuona mke wake akiwa mzima na salama, Beatrice naye alifurahi hadi machozi ya furaha yakawa yanamtoka kwa kumuona Mume wake akiwa ni mzima na salama.

“I miss you so much my love(nimekukumbuka sana mpenzi wangu)” Beatrice aliongea

“Miss you more my Queen(nimekukumbuuka zaidi malikia wangu)” Moses naye aliongea

“We mgeni wenyeji wengine hujawaona hadi umemuona mzee mzima tu” Irene aliropoka na kupelekea wote wacheke

“Heee! We bibi nawe” Beatrice aliongea akitazama Irene kwa mshangao huku akimuachia Moses.

“nawe nini yaani kama tumekaa hapa magogo vile” Irene aliongea huku akinyanyuka na kukumbatiana na rafiki yake kipenzi tangu wakiwa shule. Alipomaliza hapo alienda kukumbatiana na Dokta Hilary shemeji yake wa toka yupo shule.

“Naona alikuwa na sumu mwilini bibie ndiyo akaiwahi dawa kwa jamaa pale kaipata ndiyo anatukumbuka na sisi” Norbert naye alitia neno na kusababisha wote wacheke.

“Shem na wewe vituko havikuishi” Beatrice aliongea huku akikumbatiana na Norbert na kicheko ndiyo kilikuwa kimemtawala.

“Samaki hawezi nacha kuogelea hata siku moja, vipi salama lakini” Norber aliongea na kumjulia hali.

“Salama tu sijui kwako”

“Mungu ansaidia”

Baada ya kusalimiana na Norbert alienda hadi kwa Norene akakumbatiana naye huku Jerry mtoto wa Norbert akiwa amewashikilia miguu, walisalimiana kama alivyosalimiana na wengine kisha akambeba Jerry.

“Toto hujambo wewe” Beatrice alimuambia Jerry

“Sijambo mam mdogo shikamoo, halafu una tabia mbaya umenikimbia” Jerry aliongea

“Marihabaa,mmmh! Sijakukimbia toto nilienda kukuchukulia zawadi sasa nimerudi” Beatrice alidanganya na Jrry akamkumbatia kabisa.

“Nataka zawadi mam mdogo” Aliongea.

“Tena mwanangu usikubali hapo mdake hiyo shingo kabisa zawadi yako akupe huyo” Norbert alidakia na kupelekea wote wacheke.

Wote kwa pamoja walitoka eneo hilo la kupokea wageni, waliondoka kurudi walipotokea baada ya kumpokea Beatrice aliyekuwa yupo nje ya nchi kwa siku nyingi sana.

MWISHO!!

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment