Isabel Ndani ya Mpango Hasi Sehemu ya Nne
KIJASUSI

Ep 05: Isabel Ndani ya Mpango Hasi

SIMULIZI Isabel Ndani ya Mpango Hasi
Isabel Ndani ya Mpango Hasi Sehemu ya Tano

IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE


Simulizi : Isabel Ndani Ya Mpango Hasi

Sehemu ya Tano (5)

Tonton alifungua mlango wa chumba chake, hakuamini alichokiona, Anaconda alikuwa amelala

chini chali damu zikiwa zimetapakaa na kuanza kuganda huku chumba chote kikiwa na hewa nzito. Tonton alitikisa kichwa, hakujua la kufanya alipotupa jicho mezani laptop yake ndogo (note book) haikuwepo, alichanganyikiwa, alitazama huku na huku na kuichomoa bastola yake kisha kwa mwendo wa minyato aliusogelea mlango wa bafuni ambako bado maji yaliendelea kumwagika, hakuna kitu, alirudi na kuangalia kwenye kibaraza cha nje, bado hakuna mtu, akasonya na kurudisha bastola yake kiunoni. ‘Hapa hapana usalama’ alijisemea na moja kwa moja aliliendea begi lake chumbani na kukuta lipo kama alivyoliacha, alichukua dokumenti zake na hati za safari na kutoka chumbani mle. Akiwa chini anatoka katika lifti alipishana na askari polisi wane wakiingia kupandisha juu, moja kwa moja akapita na kuondoka zake, njiani alikuwa akiendesha gari huku akiwa na mawazo mengi, kwanza aliona wazi kuwa bwawa limeingia luba, hamna la kufanya, alifikiria tu kwanza kufika chimbo ili akajipange upya na wenzake waliosalia chimboni. Aliiacha barabara ya Msimbazi na kuchukua ile ya Morogoro kuelekea posta lakini katika makutano ya Umoja wa vijana alikunja kulia na kuipita ile ya Lumumba mpaka Nkurumah na kurudi mpaka mataa ya Kamata na kukunja kushoto kuelekea Kurasini.

Honi za hatari zilipigwa na geti likajifungua lenyewe, bila kuuliza aliingia ndani kumkuta Jomse akiwa kajiinamia huku mkono mmoja ukiwa unaminyaminya mbavu zake. Kelele ya mlango ilimfanya kushtuka na kuikamata bastola yake tayari kwa kazi.

“Oh Ton, bienvenue mon ami” Jomse alimkaribisha kwa lugha yao ya kifaransa, “Ton, kazi hii imeshatuelemea, yule bibi nimeshindwa kummaliza, sijui itakuaje, sijui nimtafutie wapi, amekuwa mbogo aliyejeruhiwa” Jomse alipigisha viganja vya mikono yake kwa ishara ya kukata tamaa na kutikisa kichwa chake kushoto kulia.

“Jomse, Anaconda ameuawa, nahisi si mwingine ni Amata aliyefanya kazi ile” Ton alifikisha taarifa, Jomse alipatwa na mshtuko mkuu alibaki midomo wazi na mikono ikimtetemeka, alipiga ngumi mezani na meza ile ya kichina iliyotengenezwa kwa cheapboard ailigawanyika vipande viwili. Aliichukua bastola yake na kuitazama kwa makini ‘Kisasi’ alijisemea, akiwa kaukunja uso wake kwa hasira.

“Wangu Amata, wako Bibi, Meno ya Mamba atabaki hapa kumlinda Isabel”


Kompyuta ya Kamanda Amata ilikuwa ikiisoma flash aliyoichukua kule hotelini, siri nyingi na za kutisha zilikuwa zikipita katika kioo cha kompyuta ile, Amata alibaki kapigwa na butwaa, akili ilimsimama na meno kumchezacheza, hapa ndipo aligundua hatima ya mpango hasi ambayo katika memory card aliyopewa na Isabel kipande hiki hakikuwapo. Aliendelea kusoma na kupata majina kadhaa ya madigala wa mpango huo duniani, aligundua kuwa kumbe ni nchi za Maghalibi ndizo zinazofadhili mapinduzi hayo kwa faida yao wenyewe, Amata alizama katika lindi la mawazo, akiwaza na kuwazua, akipanga na kupangua.

Alipogeuka kuielekekea simu yake na ndipo alipojikuta kuwa hayupo peke yake.

“Tulia hivyo hivyo!” sauti ilimkoromea kutoka upande ule, Amata hakuwa na la kufanya

“Simama taratibu” aliamriwa na kutii bila shuruti “Kwa mwendo wa taratibu ongoza nje ya nyumba yako kupitia geti kubwa”, Amata alifanya hivyo na kufika nje ambako aliikuta gari ndogo aina ya Toyota Altezza ikiwa buti wazi “Ingia kwenye buti, ukileta matata nafumua ubongo wako sasa hivi” Amata alitazama huku na huku “Usijaribu kuleta shida ingia twende”, Kamanda Amata na ujanja wake wote aliingia ndani ya buti ya gari hiyo, Jomse aliruka kwa wepesi na kulifunga buti lile Amata akiwa ndani, kisha akaingia garini na kuondoka kwa kasi.

“Kamanda Amata nimemtia mkononi” Jomse alikuwa akiongea kwa simu na mtu mwingine “Vema, hakikisha unamhifadhi vizuri mpaka amri nyingine itapotolewa” sauti ya kike kutoka upande wa pili ilisikika

“Sawa Madam, nitahakikisha hilo, hawezi kunitoroka huu ndiyo mkono wa Shetani” Jomse alimalizia kauli yake.

Kamanda Amata akiwa ndani ya buti hakuweza kujinyoosha kutokana na udogo wa buti lile, aliuinua mkono wake wa kushoto uliokuwa na saa kubwa ya kisasa akabofya kitu Fulani pembeni

mwa saa hiyo, kidoti chekundu kikawa kinawakawaka juu ya kioo cha saa hiyo, aliisogeza karibu na kinywa chake na kuongea maneno Fulani, kisha akabofya tena sehemu nyingine, sasa kidoti cha kijani kikawa kinawakawaka, akatulia kimya butini akisubiri hatima yake huku akihesabu kona ya kwanza mpaka ya mwisho kulia ama kushoto.

Gari ilisimama, kamanda Amata alihisi geti likifunguliwa na sauti zilizoongea kifaransa zilimfikia masikioni mwake, alielewa yote yaliyoongelewa, na baada ya sekunde kadhaa gari ile iliingizwa ndani na geti kufungwa nyuma yake, gari ikasimama

“Kuwa muangalifu, hajafungwa huyo” Jomse alimuamuru Meno ya mamba ambaye alibaki pale kuweka ulinzi kwa Isabel na jingo zima kwa ujumla.

“Huyo msichana mpumbavu ameamka?” Jomse aliuliza tena

“Hapana bado hajaamka, na sijui kama ataamka maana hali yake ni mbaya sana” Meno ya mambo alimjibu Jomse.

“Ah Muache afe tu, ijapokuwa Madam Rose alikuwa anamuhitaji lakini hatuna la kufanya” Jomse alimueleza Meno ya Mamba. Amata aliposiki kauli hiyo aliumia sana kwa kuwa aligundua kuwa Isabel lazima atakuwa ametekwa na kuwekwa huku, na kwa vyovyote atakuwa kwenye hali mbaya kutokana na mateso makali.

“Suka taratibu, usilete makeke, la, hii SMG itakufumua vibaya na mwili wako utakuwa chakula cha samaki usiku huu” sauti kavu ya Meno ya mamba ilisikika masikioni mwa Amata. Kamanda Amata alishuka kutoka kwenye buti ya gari ile na kusimama kwa miguu yake miwili, mikono yake ikiwa juu aliona asifanye makeke yoyote kwani alishajua kuwa Isabel yupo eneo hilo, japokuwa kwake haingekuwa kazi ngumu kuwadhibiti wote wawili.

“Geuka nyuma yako na uongoze njia unayoiona”

Amata alitii na kufuata kijia hiko huku mikono yake ikiwa juu kama alivyoamuriwa. Hatua chache alijikuta katika ubaraza mpana tu, ukiwa na viti viwili na kighorofa kimoja, chini sakafuni aliona mwili wa binadamu aliolala bila uhai, Amata alipigwa na butwaa aliutazama mwili ule kwa haraka haraka akagundua kuwa si mwingine ni Isabel alikuwa amelala chini na mwili wake kutupwa kama wa mbwa. Hasira kali zilimshika Kamanda Amata hakujua afanye nini, alitamani aukimbilie ule mwili kujua kama una uhai au la, lakini alishindwa japo alikuwa anaumia sana

Ikulu ya Dar es salaam

Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa tayari katika suti yake ya kijivu na msafara wake wa watu wa usalama, walijipangwa kwa safari ya uwanja wa ndege, tayari kwa safari ya Washington ambako alialikwa kwa mkutano maalum na Rais wa Marekani Mheshimiwa Barack Obama. Kila kitu kilikuwa kimekwishapangwa, watu wa usalama tayari walikuwa wameandaa kila kinachobidi kwa ajili ya kutekeleza na kuhakikisha kuwa mheshimiwa Rais anafika safari yake salama na kurudi salama, ujumbe anaosafiri nao tayari ulikuwa ndani ya ndege kule uwanja wa ndege terminal 1 wakiwa wanamsubiri tu mheshimiwa Rais.

“5H-ONE, Gulfsream Aerospace G-V SP G550, ndege ya serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania, inaomba njia kuruka saa tatu na dakika thelathini usiku huu” sauti ilisikika katika chombo maalum cha muongoza ndege katika mnara mkubwa wa kuongozea ndege ulio upande wa kusini wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Kambarage Nyerere.

“5H-ONE, Gulfsream Aerospace G-V SP G550, unaruhusiwa kuruka kupitia upande wa mashariki” sauti ya muongoza ndege iliruhusu kuondoka kwa ndege ya Rais baada ya kuhakikisha anga yote ipo salama kabisa.

Wakiwa wameketi sawia na mheshimiwa Rais katika kaofisi kake kadogo ndani ya ndege hiyo tayari kwa sfari kuelekea DC Washington. Dakika chache tayari ndege ile ilikuwa imeiacha ardhi ya Tanzania na kupasua anga kwenda anga ya kimataifa, ikiwa chini ya uangalizi wa Rubani mzoefu Capt Maga Junior na wasaidizi wake wawili.

Madam S, aliiangalia ndege ile inapopotelea mawinguni upande wa Vingunguti, yeye na wengine waliomsindikiza mheshimiwa Rais walianza kuchukua magari yao tayari kwa kurudi kwenye shughuli zao nyingine, mara alihisi saa yake kubwa ya mkononi inamfinya kwa vijimeno maalum vilivyo chini ya saa hiyo, alihisi kuna kitu, akaingia haraka kwenye gari yake na kubonyeza kitufe Fulani pembeni ya saa hiyo, mara ikaanza kupiga ukulele kwa sauti ya chini ikitoa kamkanda kembamba ka plastiki kalikokuwa na maadishi Fulani.

‘Att:Hakikisha mheshimiwa Rais haondoki, hiyo ndege imetegwa bomu kwenye control box na italipuka akiwa angani, fanya hima, mimi nimetekwa na sijui nilipopelekwa, fanya hima Tena Sana Aisee’, madam S alishuka kwenye gari akiwa kama aliyechanganyikiwa hakuwa anjua afanye nini, alichukua simu yake na kubofya namba Fulani.

“Hallo, naomba urudi uwanjani haraka sana kuna dharula” simu ilifika kwa waziri wa ulinzi aliyekuwa tayari amekwishaondoka lakini gari yake bado ilikuwa njia panda ya air port kuelekea mjini, dreva wa gari hiyo aina ya Toyota Land Cruiser V8 aliligeuza na kurudi uwanja wa ndege, mara gari zilizofuata nyuma, kwa kitendo kile nazo zilirudi hasa zile za usalama.

“Madam nini tena?” waziri wa ulinzi mheshimiwa Machura alimuuliza Madam S ambaye alimkuta nusu kachanganyikiwa akiongea peke yake. Akampa ule mkanda uliotoka katika saa yake, naye akausoma, akashika kichwa hakujua la kufanya. Walibaki wanahangaika akili zikiwa zimewaruka kwa kiasi Fulani, kizaazaa!

Kamanda Amata alisoma kipande cha mwisho cha mpango hasi katika flash disk aliyoichukua kule valley View Hotel, ikionesha kuwa baada ya mauaji ya watu muhimu, wa mwisho kabisa ni Rais wan chi ambaye atategewa bomu kwenye ndege yage yake itakayoruka tarehe 26 June 2013 saa tatu na nusu usiku, bomu hilo limepangwa kulipuka dakika arobaini na tano baada ya ndege kuruka, lilikuwa limetegwa kwenye control box inayosambaza umeme katika ndege hiyo ya kisasa kabisa ambayo hakuna nyingine kama hiyo Afrika, kwa jinsi walivyofunga bomu hilo ilikuwa ni pale rubani anaporuhusu magurudumu kurudi ndani ndipo nalo linajiwasha na kuanza kuhesabu dakika 45 tu na kulipuka.

“Simama apo hapo!” sauti ya Jomse ilimuamuru Kamanda Amata. Meno ya mamba alimsogelea Amata ili amfunge katika kiti kilicho jirani hapo.

“Kaa chini usilete fujo, muda wetu umeisha wa kuwa nchini kwenu, dakika chache tutakuwa ndani ya nchi yetu” Jomse alimueleza Amata ambaye alishikwa na hasira kali, akihesabu dakika za bomu lile lililotegwa katika ndege ya Rais, hakujua kama itwezekana kuokoa janga hilo au la, alitamani kama yeye angekuwa pale uwanjani ahakikishe mwisho wake. Alipohakikisha amemfunga barabara, Meno ya mamba aliirejesha bastola yake kiunoni na kutembe hatua chache na kumsukasuka Isabel kwa mguu wake, Isabel hakutikisika.

Mara simu ya Jomse iliita

“Mission clear, popo ameruka, subiri majibu” Jomse alitoa cheko la dharau


Meno ya mamba aliirejesha bastola yake kiunoni na kutembe hatua chache na kumsukasuka Isabel kwa mguu wake, Isabel hakutikisika.

Mara simu ya Jomse iliita

“Mission clear, popo ameruka, subiri majibu” Jomse alitoa cheko la dharau songa nayo sasa..

“Kamanda Amata, sasa dunia itatikisika kwa hofu kuu kwa kusikia mlipuko mbaya wa ndege ya Rais wako, ha ha ha ha” alijigamba, “Sisi ndiyo wanamapinduzi, unakumbuka Rwanda na Burundi mwaka 1994, tulimtungua Rais Abiyarimana na mwenzake Ndadaye!? Mliiona kama hadith ee! Ni sisi na sasa tuko hapa Tanzania, kamwe hamuwezi kukomesha juhudi, nakuwekea TV hapa uone dakika 40 zijazo breaking news” sauti hiyo ilimkosesha raha Amata alitamani amrukie na kumg’ata ama kumeza kabisa kiumbe huyo. Waziwazi Amata alifura kwa hasira, akaanza kuopumua kwa nguvu na kifua chake kipana kikipanda na kushuka, akiwatazama kwa macho ya hasira watu hawa wakati wanamuwekea TV mbele yake umbali wa mita kama saba hivi.

Jomse alichukua simu yake iliyokuwa mezani wakati huo na kubonyeza namba Fulani kisha akaweka sikioni.

“Yes. Hello, kutoka point A mission Clear, panga vikosi kuanza kazi mara moja pindi nikikupa taarifa” alikata simu na kuiweka mfukoni.

“Unasikia we mbwa, tayari majeshi ya waasi yameshakaa katima mapori ya Nyakanazi, na mengine yapo hapa Dar, tukitangaza tu nchi inapinduliwa dakika moja tu, na wewe ukishuhudia halafu utakuwa maiti, na yule bibi kizee wako muda si mrefu ataletwa hapa, na mtu wa kuwaua yuko Burundi anakuja, ha ha ha ha!” Jomse aliongea kwa daharau ya hali ya juu. Kamanda Amata kwa nguvu zote alijinyanyua kitini na kukinyanyua kiti kwa miguu yake na kukirusha kwa kukipiga mbele, kumbe kiti kile kilikuwa hakijafungwa pamoja naye, kilinyanyuka kwa kasi na kutua kichwani kwa Meno ya mamba, akiwa sasa mikono yake iliyofungwa pamoja imebaki nyuma, alimuona Jomse akija kwa kazsi pale alipo, Kamanda Amata lijikunja kwa kuruka na kuipenyeza miguu yake ndani ya wigo wa mikono iliyofungwa kuelekea nyuma na sasa mikono ile ilikuwa mbele, alinyanuka kwa kasi na kupiga double kick iliyotua kifuani mwa Jomse na kumpepesua hata bunduki yake kumtoka mikononi na kudondokea mbali, alipotua tu sakafuni kwa miguu miwili alipigwa mtama wa nguvu ambao ulimnyanyua juu na kabla hajatua aliichanua miguu yake na kuwatandika wote wawili kila mmoja teke la nguvu la mguu wake. Meno ya mamba alitema meno kadhaa. Kamanda Amata alijiviriga kutoka pale alipokuwepo na kuiwahi bastola iliyokuwa chini, kabla hajafika alipigwa teke la sikio na kumfanya kupoteza uelekeo, alijigeuza chali na kumuona Jomse akiwa na shortgun mikononi mwake, Amata hakujali, akiwa bado yupo chini alimpiga Jomse teke la nguvu nyuma ya vivigino lililomfanya aanguke chali kama mzigo kabla hajatulia, mguu uleule ulitua juu ya tumbo la Jomse, ukelele wa maumivu ulisikika, wakati Meno ya mamba akija kwa kasi kumkabili Kamanda Amata ambaye alikuwa amelala pale chini, alishuhudia kichwa cha Meno ya mamba kikitawanyika vibaya na mwili wake kurushwa mita kadhaa ukiwa hauna uhai.

Gina akiwa bado hajasusha mkono wake wenye bastola yake aina ya Makarov, bastola ya kirussia iliyotengenezwa mwaka 1949 na bwana Nikolay Makarov na kuanza kutumika rasmi mwaka 1951 ilishafanya kazi yake kama ilivyoamuriwa.

“Freeze, bastard” Gina alimuamuru Jomse aliyekuwa akijaribu kujitutumua pale chini, Jomse alijifanya asikii na kutaka kuichuku ile short gun mara Makarov ya Gina ilicheua tena na kuvunja mkono wa Jomse, yowe la maumivu lilimtoka.

Mara polisi kadhaa waliingia ndani ya jengo lile wakiongozwa na Inspekta Simbeye, walimfungua kamanda Amata na kumchukua Isabel baada ya kugundua kuwa bado alikuwa na uhai, haraka sana wakamkimbiza Hospitali ya jeshi la wananchi Lugalo.

“Naomba muhakikisehe huyu mtu anafika makao makuu ya polisi leo kwa mahojiano hata kama ana maumivu ya mkono sijali, mimi naelekea uwanja wa ndege, kuna muasi mmoja bado hajakamatwa na hayupo hapa” kamanda Amata alitoa amri huku akiingia katika gari ile iliyomleta, Toyota Altezza na kuigeuza kwa kasi na kuondoka eneo lile kuelekea uwanja wa ndege.

Kwa maelekezo ya Amata, Inspekta Simbeye alitoa amri kwa redio call maeneo muhimu yote yawekwe ulinzi ili kumnasa muasi huyo, kuanzia stendi ya Ubungo, Posta eneo zinaoondoke bot za

Zanzibar, Uwanja wandege wenyewe. Mji wa Dar es salaam ulijawa na askari kanzu kufanya msako huo, mawasiliano ya redio za polisi muda wote yaligubikwa na habari za wapi ameonekana au wapi kuna dalili. Maelekezo machache waliyoyapata jinsi alivyo yaliwafanya watu wa mtindo huo kuishi kwa shida usiku huo

Tonton akiwa bado hajui kilichompata Jomse na Meno ya Mamba bado alikuwa katika harakati za kumsaka Madam S, ama awe hai au maiti, aliiangalia saa yake aliona inakaribia saa nne za usiku, akiwa amepaki gari yake katika njia panda ya uwanja wa ndege terminal one, bomu la mkono aina ya grunet lilikuwa juu ya kiti cha gari yake huku akijifanya anatengeneza tairi akisubiri msafara ule wa wanausalama utoke kule uwanja wa ndege ili afanye yake. Alikuwa hakika amejizatiti kwa kila hali, walktalk yake iliita akaichukua na kupata maelekezo Fulani kisha akairudisha kitini na kusubiri kidogo akiwa ndani ya overall. Akiwa katika kushangaashangaa mara mbele yake ilipita Toyota Altezza nyeusi kwa kasi ya ajabu ikielekea uwanja wa ndege, Ton aliiangalia kwa makini akaingiza mkono mfukoni na kuinua simu yake na kubofya namba Fulani na kuiweka simu yake sikioni, lakini simu ile haikujibiwa, aliipiga tena hali ilikuwa ileile, akachanganyikiwa afanyeje maana aliona Jomse kaelekea airport na gari yake sasa akawa katika njia panda kama alipo, amfuate au asubiri pale kadiri ya maelekezo aliyoyapata, alizunguka huku na huku akiwa kama mtu aliyechanganyikiwa.

Mabishano makali yalikuwa kati ya Madam S na waziri wa ulinzi, Madam S aling’ang’ani ndege ile ishuke haraka iwezekenavyo wakati waziri wa ulinzi akisema kuwa hawana la kufanya ndege imeshakwenda hakuna jinsi ya kuiokoa. Akiangalia simu yake dakika thelathini zilikuwa zimekatika tangu ndege ile iache ardhi.

Tairi za Toyota Altezza zililalamika katika lami Amata alipokuwa akiingia uwanjani pale,

“Vipi Madam? Bado nimewaambia ndege ile ina bomu itue hapa tufanye kinachowezekana, ah!” Amata aliingia kwenye gari yake na kuondoka kwa kasi kuelekea katika mnara wa kuongezea ndege, alipaki gari na kukwea ngazi huku akikimbia, aliingia akiwa anathema.

“Samahani, naitwa Kamanda Amata kutoka idara ya usalama wa taifa kitengo maalumu,” alitoa kitambulisho na kuwaonesha maofisa hao.

“Tukusaidie nini Kamanda?”

“Naomba muamuru ndege ya Rais irudi haraka sana, bila kuchelewa” “Sasa unajua….” Mdada mmoja alitaka kutoa hoja zake za kitaaluma

“Unapoteza muda, harakaaaaa…” Amata alimkatisha kwa ukulele na kutaka kumkata kibao. “5H-ONE, Gulfsream Aerospace G-V SP G550, kitendo bila kuchelewa unaombwa kuirudisha ndege uwanjani kwa sababu za kiusalama”

“5H-ONE, Gulfsream Aerospace G-V SP G550, Captain Maga Junior amekusikia, naomba njia” Lugha zaidi za kitaalamu zilifanyika na ndege ile ilikunja kipande cha mkia wake na kuelemea upande mmoja ikigeuka kurudi ilikotoka.

Simu katika chumba cha rubani iliita, captaina aliipokea na kujibu maswali aliyoulizwa na wana usalama waliokuwa kwenye msafara wa Rais kuelekea Washington, wote wakatulia vitini wakisubiri kujua nini kilijiri.

“Kama Kamanda Amata ameamuru, basi kuna jambo.” Mmoja wao alimueleza mwingine.

Gari za zima moto na zile za uokoaji tayari zilikuwa zimewasili katika eneo la uwanja wandege wa jeshi tayari kukabili lolote, makomandoo kadhaa wa jeshi walikuwa tayari eneo lile, kwa ujumla hali ilikuwa tete uwanjani pale, ndge za abiri zilizotakiwa kuruka na kutua zilizuiliwa kwa muda ili anga ibaki nyeupe na kuziacha nyota na mbala mwezi tu.

Gari mbili za zimamoto zilikuwa mwanzo wa barabara itumikayo kwa kuruka au kutua zikiwa tayari kabisa kwa kazi hiyo.

Kamanda Amata akiwa na Madam S, waliangalia saa zao kwa pamoja ilkuwa ni saa nne usiku na dakika moja, zilibaki dakika kumi na nne tu ili bomu lile lilitegwa lifanye kazi yake, akili ya Amata ilikuwa ikismama kila wakati, alijiuliza kwa nini wamalize kazi yote halafu iwaharibikie mwisho, haikuingia akilini. Kwa mbali waliona taa ziking’aa upande wa Kipawa, kuashiria kuwa sasa kazi ya hatari inaamka, kila mtu alijipanga sehemu yake tayari kwa kazi hiyo, kamanda Amata alisogea karibu na wale makomandoo wa jeshi tayari kwa kazi ya uokoaji.

Saa nne na dakika sita, 5H-ONE ndege ya kisasa ya serikali kwa matumizi ya Rais, ikiwa inaongozwa na rubani mzoefu kwa kazi hiyo Captain Maga Junior, ilikanyaga ardhi ya Dar es salaam na kwa kasi ya ajabu ilipitiliza mpaka maeneo ya Kipunguni kisha kukunja kona na kurudi pale uwanja wa jeshi si kwa mwendo ule wa maringo tena, bali kwa mwendo wa kasi kidogo, gari za zima moto zilishaizunguka alkadhalika na zile za wagonjwa zilikuwa pale. Milango ya ndege ilifunguliwa na ngazi maalumu ya plastiki linalojazwa upepo lilifyatuliwa na mtu wa kwanza kutolewa ni mheshimiwa Rais, na moja kwa moja alichukuliwa na kuondolewa eneo lile kwa gari maalum, kisha wakafuatia wengine.

Kamanda Amata alikuwa tayari katika chumba chenye mitambo ya umeme ya ndege hiyo, control room, bomu lile lilikuwa limefungwa sambamba na na nyaya zinazosambaza umeme katika ndege ile, nyaya zaidi ya mia mbili ziliingia na kutoka eneo lile na nyaya sita ziliingia kwenye lile bomu na kutokea upande wapili kisha kufungwa katika fyuzi fulanifulani. Kijasho chembamba kilimtoka Amata hakujua nini cha kufanya, saa ya bomu lile ilisoma bado dakika mbili ili ifike muda wake. Akiwa na koleo ya kukata nyaya ya umeme alishindwa waya upi auanze, mwekundu au mweusi, wa njano au buluu au ule mweupe, kweli alichanganyikiwa. Kawaida huwa kuna nyaya tatu lakini kwa nini bomu hili lina nyaya sita, hilo ni jambo lililomchanganya, alijaribu kukumbuka kanuni aliyofundishwa alipokuwa mafunzoni huko Cuba jinsi ya kutegua mabomu lakini alijikuta ameisahau. Saa ya lile bomu ilionesha kuwa imebaki dakika moja na sekunde kadhaa, Amata alikuwa ameloa jasho mikono ikimtetemeka, sasa alioamua lolote na liwe, maana ukataji wa nyaya hizo unatakiwa uende kwa mpangilio maalum na ukikose utafanya muda wa bomu lile uishe haraka na kusababisha mlipuko. Alitazama haraka haraka na kuugundua waya wa kwanza primer, akaukata, bado saa ile iliendelea kwa mwendo wa kawaida, akatafuta waya wa pili waya wa reactor, akaupata na kuukata, sasa zilibaki nyaya nne, alijihisi kama kujikojolea maana saa ya bomu lile ilisoma bado sekunde hamsini, hamna muda wa kufikiria iliyobaki ni kukata zote.


Katika uwanja ule ukimya ulitawala usiku ule utafikiri hakuna mtu, ni mingurumo ya gari tu iliyosikika lakini binadamu wote walikuwa kimya wakasubiri hatima ya ndege hiyo na kamanda Amata aliyepo ndani yake, kila mtu alisali kwa dini yake, Ee Mungu iokoe Tanzania. Madam S alibubujikwa kwa machozi akiwa anauma meno hakujua afanye nini alibaki kutazama tu saa yake iliyomwambia bado sekunde takribani kumi, hakuna Amata wala dalili za kuonekana kwake nje. Alipogeuka nyuma hakumuona waziri wa ulinzi, ambaye muda wote alikuwa hapo nyuma yake. Hakulifuatilia hilo macho yake yote yalikuwa juu ya Amata na ile ndege ya Rais yenye thamani kubwa kabisa Africa ‘Airforce one ya Tanzania’.

Kamanda Amata, huku mikono ikimtetemeka alikata waya wa kwanza kati ya zile nne, wa pili na alipokata wa tatu ‘Ignition Timer’ saa ile ilisimama na kuacha kutoa ule mlio wake ikiwa imebaki sekunde moja kulipuka, saa ile ilisimama ikiwa imejiandika 00:00:01.

Amata alishusha pumzi ndefu, alijishika mikono kifuani moyo wake ulikuwa ukienda mbio, alijihisi kama mtu aliyetoka mautini.

Huko nje, ilipobaki sekunde tano makomandoo wa jeshi waliamuru watu wote kulala chini, na zilipokwisha bado hakuna mlipuko uliotokea. Walianza kusimama mmoja mmoja.

Madam S sasa alitokwa na machozi ya furaha alipomuona Amata akitoka katika ule mlango wa ndege mkononi akiwa amekamata lile bomu ambalo limeshindikana kulipuka.

Hakuna aliyeamini anachokiona, waandishi waliokuwa wamesimama mbali walisogea na kupata picha za shujaa huyu na kumhojo maswali mbalimbali, ilikuwa fujo uwanjani hapo.

Kamanda Amata aliingizwa kwenye gari na kufungiwa milango na gari ile iliondoka eneo lile.

Gari aina ya Toyota Altezza ilisimama karibu kabisa na ile gari ndogo iliyofanywa kama imeharibika tairi, Tonton alitoka kwenye kichaka cha michingoma na kuisogelea kwa hadhari kubwa kwa maana aliijua ile gari ilikuwa ikitumika na Jomse.

“Hali si nzuri tuondoke haraka,” waziri wa ulinzi bwana Machura alimwambia Tonton na wote wakaingia ndani gari hiyo na kutokomea pande za Gongo la mboto.

“Mzee vipi?” Ton aliuliza

“Mambo si mambo kijana, hapa ni kujiokoa tu, na jinsi ninavyojua nchi hii si ajabu wameshabana kona zote”

“Oh God” Ton alisikitika. Gari ile iliendeshwa kwa kasi sana, walipita Pugu na kufika Chanika kisha mvuti mpaka mitaa ya Samvula Chole.

“Madam S, naomba uombe kibali cha kumuweka chini ya ulinzi mheshimiwa Machura” Amata alimueleza madam S huku akifyatua kiti kujilaza.

“Kwa nini?”

“Naomba utekeleze hilo haraka madam, wewe ndiye mwenye sauti, si mimi”

Bila kupinga madam S alipiga simu kwa mkuu wa polisi msaidizi baada ya kifo cha IGP na kuomba kibali hicho, bila kipingamizi kibali kilitolewa. Defender ya polisi ikiwa na polisi wenye silaha nyumbani kwa Machura, waziri wa ulinzi, walipigwa na butwaa nyumba ilikuwa tupu, hakuna mtu, si familia wala yeye mwenyewe, ni mlinzi tu ndiye alikuwa amebaki pale. Maelezo waliyoyapata kutoka kwa mlinzi yule yaliwakata maini, walielezwa kuwa familia ya Machura iliondoka yote jana asubuhi, lakini haikujulikana ni wapi ilielekea, taarifa ilifikishwa kwa haraka mahali husika.

Akiwa njiani kuelekea kituo cha polisi kati, kamanda Amata aliipata taarifa ile kupitia simu iliyopigwa kwa madam S.

“Shiiiit” Amata aliongea kwa hasira, “Hawezi kutukimbia hata kidogo,” alichomoa simu yake mfukoni na kubofya namba fulani, kisha akaiweka sikioni.

“Hello … sio kivile… sasa sikia naomba uwasiliane na watu wa uwanja wa ndege ikiwezekana upate orodha ya abiria walioondoka jana kwa kila ya kila kampuni, haraka tafadhali” akakata simu mara tu baada ya kumaliza kuongea.

Madam S aliipaki gari yake pembeni kidogo ya kituo cha polisi, haraka Amata alishuka na wote wawili wakaelekea ndani.

“Upande huu tafadhali” afande aliyekuwa kaunta aliwaelekeza kuwa waingie kushoto, huko walimkuta Inspekta Simbeye akiwa amefura kwelikweli na Jomse akiwa kwenye kiti cha chuma akiwa na hali mbaya.

“Bastard!” Madam S aling’aka kwa hasira alipomuona Jomse, “Ulifikiri hii nchi ni ya baba yako?!, ‘Mimi mwanamapinduzi, mxiuuuuui, kawapindue hao hao’” alimuiga kwa sauti ya kubana pua.

Jomse hakuweza hata kuinua kichwa kwa jinsi alivyokuwa na maumivu makali, aliisikia tu sauti ya mwanamama yule aliyempa kibarua kigumu kule ofisini kwake. Wakiwa katika majadiliano hayo waligundua kuwa Jomse hali yake ilizidi kuwa mbaya.

“Hebu pelekeni Muhimbili, hakikisheni anapona ili atumikie kifungo chake ndani ya nchi hii” Amata alisema hayo na kutoka akifuatiwa na madam S. Baada ya kupata ripoti ya kuwa Isabel tayari yuko hospitali ya jeshi, Amata na madam S walifarijika, wakaagana na Inspekta Simbeye “Kama kuna lolote basi tutakutaarifu”, kisha wakaondoka zao.

Simu ya Amata ikaita. “Yes, niambie…”

“Tayari nimepata orodha zote, amri nyingine tafadhali” sauti ya kikakamavu ya Gina ilisikika. “Vizuri, msichana mrembo, tukutane ofisini sasa hivi, bila kuchelewa.” Dakika tano tu wote walikuwa ofisini pamoja na madam S, Amata akiwa na madam S walizipitia orodha zote, wakiwa karibu na kukata tama, chati ya mwisho kabisa ya shirika la ndege la Kenya ndipo waligundua majina ya familia ya Machura, ilionesha wametoka Dar kwenda Kigali kupitia Nairobi. Madam S alitikisa kichwa chake juu chini kuonesha amegundua kitu.

“Madam, mheshimiwa Machura, waziri wa ulinzi anahusika kwa kiasi kikubwa sana katika kuandaa mapinduzi haya ushahidi upo, kwa nini aondoshe familia yake? Ai alijua kuwa kitakaponuka familia yake iwe salama wakati Watanzania wanateketea”

Madam S alionekana kushikwa na hasira mpaka paji la uso wake likawa na mikunjomikunjo kadhaa, alipiga ngumi mezani na kujishika kiuno akimwangalia Amata.

“Hakuna kuchelewa, mpigie simu Simbeye msako uanze mpaka atiwe nguvuni kabla jua kuchomoza, kisha sisi twende kwa mzee ametuita haraka sana”

Dakika chache tu nchi nzima ilikuwa kwenye tahadhari kubwa hasa sehemu za mipakani ambako ilisemekana kuwa tayari kuliandaliwa majeshi ya waasi ambao walipata mafunzo maalumu katika misitu ya Nyakanazi, mapakani kabisa mwa Tanzania na Burundi, operesheni maalum ikatangazwa na kwa kuwa vijana wetu wa JWTZ walikuwa makini kazi hiyo haikuwa na mzaha hata kidogo, huku vijana wa polisi wakiwa wamelibana jiji la Dar es salaam katika kila uchochoro unaotoka nje ya jiji hilo ili Machura asitoroke.

Mheshimiwa Rais, alionekana kuchanganyikiwa kwa namna Fulani, hakuamini ni nini kinachoendelea. Akiwa amekaa kwenye meza yake kubwa na ile ya mbele walikuwapo waziri wa mambo ya ndani, jeshi la kujenga taifa, mkuu wa kitengo maalum usalama wa taifa madam S, na pembeni yake alikuwapo Kamanda Amata, kiti kimoja kilikuwa wazi.

Mheshimiwa Rais aliwaangalia wote kwa zamu.

“Asante sana kijana pamoja na madam pale, si kwamba mmeniokoa mimi bali mmeliokoa taifa, ambapo lingeingia kwenye mapinduzi na mauaji ya kimbali ambayo yangesababisha na watu wachache wenye uchu wa kutawala dunia” alinyanyuka na kuwapa mikono “Naomba nipate taarifa fupi ya yote haya ili sasa tujue kama tumemaliza au la” macho yote ya waliokuwa kikaoni yakaelekea kwa madam S na kamanda Amata.

Taarifa fupi ilitolewa na kila mtu katika kikao kile alibaki mdomo wazi.

Mheshimiwa Rais alielezwa kila kitu na hatua zilizochukuliwa na vyombo mbalimbali vya usalama nchini, kwa hatua hizo alitoa pongezi za dhati kwa wote, lakini kama kuna jambo lilimuuzi ni juu ya waziri wa ulinzi, hakuamini kabisa kama mzee huyo aliyeheshimika sana angeweza kuingia katika wimbi hilo la kupanga mapinduzi. Mheshimiwa alitikisa kichwa kwa masikitiko.

“Naomba kwa udi na uvumba, akamatwe ili aje ajibu maswali yake” Rais alitoa msisitizo. Miaka mine nyuma

Kinshasa-RDC

Mkutano uliowakutanisha mawaziri wa ulinzi wote wa nchi za SADC ulifanyakia katika hoteli ya kimataifa ya Hilton mjini Kinshasa. Kama kawaida ya mikutano hiyo ilikutanisha watu wa aina

mbalimbali, Tanzania iliwakilishwa na mheshimiwa Godfrey Francis Machura mzaliwa wa Kigoma, ambaye kiasili kabisa wazazi wake walihamia Kigoma wakitokea Congo, yeye alisoma na kujenga maisha yake yote hapo hata kujiunga na siasa katika chama cha TANU enzi hizo mpaka sasa CCM.

Jioni moja katika hoteli hiyo alikutana na wageni asiyowatarajia, wanaume watatu wa kizungu, mmoja akiwa kama chotara, pamoja na mwanamama mmoja wa Kiafrika mwenye maringo ya kuvutia mwanaume yeyote rijali.

Walikuwa na sera kubwa moja tu, kumhadaa mheshimiwa huyu ili kuweza kuipenya ngome ya kiulinzi ya Tanzania na kuweza kutekeleza mpango wao dhalimu walioudhamiria kama walivyofanya katika nchi kadhaa hapa Afrika. Kwa pesa nyingi walizo nazo, walimuahidi yeye mwenyewe kupata utajiri wa hali ya juu kama hilo lingetekelezwa.

Baada ya mkutano ule, mheshimiwa Machura hakuishiwa na ziara za mara kwa mara kwenda Kigali na Bujumbura, huko ndiko walikokuwa wakipanga huo Mpango Hasi. Ilishapangwa kuwa pindi tu mambo yakiwa sawa yeye na familia yake wangeenda kuishi Kigali ambako alishapewa nyumba kubwa na yenye hadhi. Tamaa ya pesa iliufanya moyo wake kuwa tayari kulisaliti taifa lililomlea na kumpa njia ya maisha, hakika shukrani ya punda ni mateke.

Kama kuna habari iliyomfariji mheshimiwa Rais katika kikao kile ni juu ya msichana Isabel. “Bado taifa lina wazalendo, kama msichana huyu angepuuza juu ya hilo nini kingalitokea?!” aliuliza kwa mshangao.

Wote walibaki kimya, hakuna hata aliyekohoa katika kkao kile, kwa kila mmoja wazo tofauti lilikuwa likipita kichwani mwake akiwaza hiki na kuwazua kile kule. Kila mtu kwa muda huo alikuwa amekodolea ukutani ambapo kwa kutumia projector waliweza kuusoma mpango hasi hatua moja baada ya nyingine. Na walipomaliza kusoma kila mtu alishika tama kwa msikitiko, kimya kikatawala.

Baada ya kimya cha muda mheshimiwa aliuvunja ukimya huo “Sasa naomba turudi kwenye majukumu, halafu nitwaomba tena tukutane baada ya mambo haya kutulia, siku za usoni” alimaliza na kunyanyuka, wote walinyanyuka na kutoa heshima zao kisha kupeana mikono na kuondoka eneo hilo nyeti.


Kigali – Rwanda

Chiba aliipaki gari yake katika maegesho, kabla hajashuka katika gari hiyo aliiweka tayari bastola yake na kuibana sawia katika mkanda maalumu uliofungwa kwa kifuani, aliivaa miwani yake myeusi yenye uwezo wa kuona nyuma na kurekodi sauti ya mtu anayeongea naye. Alipoona kuwa amejikamilisha aliinyanyua simu yake ya upepo na kuwasiliana na watu walio nje kidogo ya maegesho hayo ambao walikuja kwa kazi moja tu, kazi muhimu. Alipoona kuwa wako tayari, aliteremka na kuliendea ghorofa moja wapo kati ya mengi ya yaliyojengwa eneo hilo kwa madhumuni ya kupangisha watu, bila kujua kuwa wengine wanaowapangisha hawana utu hata kidogo. Alikwea ngazi kwa kukimbia kidogo mpaka ghorofa ya pili, milango mingi ilimzunguka aliinua macho na kusoma vijinamba vilivyobandikwa milangoni. B 6T, akatikisa kichwa kuonesha kuwa ni sahihi kama alivyoelekezwa, alichomoa earphone yake na kuipachika sikioni kwa minajiri ya kuwasiliana na wale walo nje, kisha akabonyeza kitufe chekundu kilichopo mlangoni hapo.

Sekunde kadhaa, mlango ulifunguliwa na msichana wa kadirio la umri wa miaka ishirini alijitokeza kichwa tu.

“Karibu, nikusaidie nini?” alimkaribisha Chiba kwa lugha ya Kinyarwanda. Msichana huyu mwenye mwili mwembamba na shingo ndefu alitoa tabasamu ambalo lilimfanya Chiba atulie kwanza baada ya network zake kukatika ghafla kwa kukutana na binti mwenye shingo ya upanga. “Naitwa Tonton, nimemkuta madam Rose?” Chiba aliongopa jina.

Yule msichana alisita kidogo akamwangalia kijana huyo ambaye mkono mmoja wa kulia ulikuwa ndani ya koti lake kana kwamba anataka kutoa hela katika mfuko wake wa shati.

“Hayupo,” alijibu msichana yule huku akirudisha mlango kuufunga, Chiba aliweka mguu na kuuzuia.

“Msichana! Nina shida ya muhimu, nahitaji kumuona madam Rose sasa hivi” “Nimekwambia hayupo”

“Amekwenda wapi?”

“Mi sijui, nimemuona akiondoka tu.” Chiba alibaki hana la kufanya, alitafakari kwa muda kidogo na kupata uamuzi.

“Ok” akageuka kuondoka, hamad, domo la bastola lilikuwa likimtazama usoni pindi tu alipogeuka. “Tulia! Toa bastola yako” amri ilitoka kwa mtu huyo chotara, Frank, aliyekuwa tayari katika nyumba hiyo. Chiba aliitoa bastola yake na kuiweka chini, kisha yule msichana akaichukua.

“Ingia ndani,” amri ya pili ilifuata na Chiba akatii.

Katika sebule ile kubwa Chiba aliketishwa kwenye moja ya sofa zilizo hapo na Frank akaketi kwenye sofa lingine kwa mtindo wa kutazamana.

“Mmemuua Mandi, na wengine, mmeona haitoshi sasa mmekuja hadi huku, mnajifanya FBI au Interpool?” Frank alimuuliza Chiba huku akinyooshea ile bastola iliyoonekana wazi haina masikhara.

“Zaidi ya hapo” Chiba alijibu kwa dharau. Frank alichukizwa na jibu lile na kufayatua risasi moja iliyochimba kwenye sofa lile sentimeta chache katikati ya mapaja yake, Chiba alitetemeka na kijasho cha ghafla kilimtoka kwa mbali.

“Ha ha ha ha kumbe unaogopa kufa, ha ha ha ha!” Frank alicheka kwa dharau, “Kwa taarifa yako madam Rose, hivi tunavyozungumza bado dakika kumi tu apae kuelekea Belgium kwa mapumziko, madam ni untouchable,” alipokuwa akisema hayo Chiba hakupoteza muda, alijisukuma kwa nguvu pamoja na lile sofa na kupindukia upande wa pili, sofa lile likamfunika, kitendo hicho cha haraka kilimchanganya Frank, akaweka vizuri bastola yake na kufyatua risasi kadhaa kwenye sofa lile lakini tayari Chiba alishaliacha sofa lile peke yake. Hakuwa na silaha, alinyanyua bilauri iliyokuwa mezani na kuirusha, moja kwa moja ilitua katika uso wa Frank na kumpoteza malengo, yule msichana kule jikoni alikimbilia sebuleni ndipo alipodakwa na Chiba na kuwekwa ngao, huku Chiba akiwa tayari na kisu kutoka mikononi mwa msichana yule.

“Weka bastola chini, au la nakata koromeo la Malaya huyu” Chiba aliongea kwa gadhabu wakati huo tayari matone ya damu yalioneka yakidondoka sakafuni, kisu kile kilianza kuikata ngozi ya juu ya shingo la msichana yule. Frank hakuwa na ujanja aliiweka bastola chini, kisha Chiba alimuamuru kutoka eneo lile na kuuelekea mlango, naye akatii. Chiba hakuujua ujanja wa Frank, alipoufikia mlango kitendo bila kuchelewa aliichomoa bastola iliyokuwa upande wa nyuma wa suruali yake na kufyatua risasi mbili mfululizo, la, Chiba alijitupa upande wa pili na kuikamata bastola aliyoiacha Frank. Risasi za Frank ziliishia kifuani mwa yule msichana, akajibwaga chini akiwa marehemu. Frank aliduwaa alionekana wazi kachanganyikiwa kwa kitendo kile. “Rooooosssseeee! Madam Roooooseeeee” alilia kwa uchungu, ndipo Chiba alipogundua kuwa kumbe yule alikuwa ndiye madam Rose lakini alipata shaka kutokana na picha aliyopewa ofisini. ‘Ni yeye au si yeye?’ alijiuliza, mara akakumbuka kuwa yupo katika mapambano.

“Freeze” alimpigia kelele Frank, “Weka bastola chini” alimuamuru na Frank akatii. Mara mlano ukafunguliwa na watu wawili wakaingia, kwa ishara waliyopewa na Chiba wakamtia pingu Frank. “Tuambie huyu ni nani?” Chiba alimuuliza Frank huku akielekeza mkono wake kwa yule marehemu msichana. Frank hakujibu alibaki kumwangalia tu usoni, “Nakuuliza wewe!” Chiba aling’aka lakini alichokipata ni kutemewa mate usoni kitendo kilichomuudhi sana, kwa hasira

alimvamia Frank na kumchoma na peni ya chuma eneo la shingoni, Frank alitoa yowe la uchungu. “Sema, madam Rose yuko wapi?” Chiba aliuliza tena. Lakini kabla hajapata jibu simu iliyokuwa juu ya kikabati kidogo ikaita kwa sauti kali, Chiba akaiendea na kuinyanyua ‘madame Rose’ ilijiandika kwenye kioo, Chiba aliichukua na kumpelekea Frank.

“Ongea naye, kwa lugha yenu ya kawaida, weak loud speaker wote tusikie mwambia aje hapa haraka, ukigeuza neno nautawanya ubongo wako” Chiba alimaliza na kutegua kiguu cha usalama cha bastola yake na kuruhusu risasi kuingia chemba kisha akainyooshea kwa Frank usawa wa paji la uso.

“Yes, madame” Frank alipokea

“Hey Francoise, unikute hapa Kichukiro highway, nimeshapata ndege ya kukodi tuondoke joni hii” “Sawa madame lakini tuna…”

“…Mna nini Francoise, mambo yameharibika kama kuna kinachoshindikana acha njoo wewe” “Eh madam hali ya dada ako ni mbaya uje mara moja” mara simu ikakatika. Frank akanyanyuliwa na kuwekwa juu ya sofa kubwa pamoja na wale watu wawili, wakawasha television na kusubiri windo lao.

Ama kweli ndege mjanja hunasa kwenye tundu bovu, madam Rose aliingia kwenye maegesho kwa kasi ya hatari na gari yake aina ya Rambolghin, akapaki na kutembea harakaharaka kuelekea ngazi za jengo hilo, hakushtuka kabisa alipompita mwanaume mmoja katika ngazi hizo akiongea kwa simu huku akicheka, moja kwa moja aliuendea mlango na kuufungua kuingia ndani, nusura azimie baada ya kulakiwa na mwili wa marehemu uliyolala bila kuguswa kwenye dimbwi la damu mbichi. “Uuuuuuiiiiiii !” alipiga ukelele wa mshtuko na kujikuta akidakwa na watu asiyowajua na kutiwa pingu, kisha kuwekwa juu ya sofa lingine na kumuona swahiba wake Frank akiwa amelowa damu katika shati lake.

“Idara ya usalama wa taifa Tanzania kushirikiana na idara kama hiyo ya nchini Rwanda tunawaweka chini ya ulinzi kwa jaribio la kufanya mapinduzi huko Tanzania.” Madam Rose alishindwa afanye nini alibaki mdomo wazi, kapatikana. Hakuamini jinsi alivyonasa kwenye mtego wakijinga wakati amekwishakwepa mbinu nyingi za watu kama hawa sehemu mbalimbali za ulimwengu.

Bila ubishi, waliongoza chini na gari maalum yenye vyoo vyeusi na vinene visivyopitisha risasi lilifika hapo na kuwapakia.

“Mnatupeleka wapi?” madam Rose aliuliza.

“Hupaswi kujua, utaona ukifika” Chiba alimjibu. Safari hiyo ikaishia uwanja wa ndege, wakiwa na soksi katika vichwa vyao hawakuweza kuona hata wapi wanaelekea, walipakiwa kwenye ndege maalum na safari ya kwenda Dar es salaam ilichukua nafasi yak echini TSA namba 2, Chiba wa Chiba.

“Ina maana hamnijui mimi? Mbona mnaleta mambo ya ajabu?” Machura aliongea kwa hasira aliposimamishwa na askari wa checkpoint maeneo ya Igumbilo, Iringa. Alikuwa akijaribu kutoroka kwa kutumia njia hiyo mpaka Mbeya ambako angeweza kuingia nchi jirani lakini alipofika hapo check point gari yake haikuwa na budi kusimama kutokana na mageti yaliyowekwa hapo kuzuia njia. Ilikuwa ni saa nane usiku, kibaridi kikali kikipuliza.

“Nitapiga simu kwa RPC wenu na ninyi wote mtimuliwe kazi” aliendelea kung’aka huku akiwa anazungukazunguka huku na kule. Mabishano yalipokuwa yamezidi, Machura alipiga simu kwa RPC Kamuhanda wa Iringa, kweli akili ni nywele. RPC Kamuhanda aliona simu yake ikiwakawaka alipoiinua kwenye kioo alikuta jina la mheshimiwa mkubwa serikalini, akaitazama kisha akaiweka sikioni na kuipokea.

“Hello mheshimiwa waziri …”

“…Yes, .. a a a … Kamanda, vijana wako wananizuia njia hapa Igumbilo, hawajui kama nipo katika majukumu ya kiserikali? Naomba uwaamuru haraka waniruhusu kupita na kisha hawa wote walio

zamu sasa hivi wachukuliwe hatua za kinidhamu”

“Ok, naomba ngoja niwapigie mara moja, hawana nidhamu kabisa kwa nini wakuzuie, wana kigezo gani? Lazima niwaadabishe,” RPC Kamuhanda aliikata simu ya Machura na kuivuta simu yake ya upepo tayari kutoa taarifa hiyo.

“Na mtaona sasa…ninyi hamjui kuwa mimi namuwakilisha Rais!” alimaliza kuongea huku akiingia katika gari yake.

“Vipi?” Ton aliuliza.

“…Check point Igumbilo, iruhusu gari ya mheshimiwa ipite mara moja ni amri, ova” “….Tumekusoma, tunatekeleza, ova”

Geti likafunguliwa na gari ile ikapita kuendelea na safari, huku Machura akiwaoneshea kidole cha kati askari wale.

Karibu kabisa na njia panda ya kupandishia Iringa mjini, Land Rover Defender ya kituo cha polisi Iringa ilisimama katikati ya barabara ikwa imewasha taa zote full, juu ikiwa na vijana wawili wenye SMG na chini kulikuwa na vijana wanne wenye silaha pia. Ton aliendesha kwa mwendo wa taratibu,

“Aaaggghhh! Shit, nini tena!” Machura alipiga kelele huku akipigapiga mikono yake kwenye mapaja yake kwa hasira.

“Unaombwa kujisalimisha, wewe pamoja na uliyekuwa naye garini” sauti ilisikika kutoka nyuma, Machura alipogeuka alikuta Land Cruiser ya buluu ya polisi ikiwa nyuma yao, mbio za sakafuni huishia ukingoni.

“Unaombwa kujisalimisah, kwa kutoka nje ya gari hiyo mikono hewani, tii sheria bila shuruti” sauti ile ilirudia tena kutoka kwenye megaphone.

“Napambana!” Ton alimueleza Machura huku akimuonesha bomu la kurushwa kwa mkono. “Ha ha ha ha…” sawa kijana umejiandaa vyema nakuaminia.

Ton alifungua mlango na kutoka nje huku mikono ikiwa hewani lakini ilikuwa ni vigumu kumgundua kama kashika kitu mkononi, walipotaka kumfuata alirusha bomu lile kwenye Land cruiser na kishindo kikubwa kilisikika, ile Cruiser ikanyanyuliwa kama box tupu lipeperushwavyo na kimbunga, hali ya mkanganyiko ilitwaa nafasi badala ya utulivu, Ton na bastola yake mkononi alijaribu kuwalenga polisi wale, kwa shabaha yake nzuri aliweza kumpata wa juu katika defender iliyosimama upande wa pili. Machura alishindwa kuvumilia alitoka garini na bastola mkononi akijaribu kufyatua hewani huku akijitahidi kukimbia lakini tumbo lilimzidi uzito. Moshi ukiwa umetapakaa kila mahali, ving’ola vya gari za faya na polisi vilisikika kutoka Iringa mjini. Machura alimshuhudia Tonton akichakazwa kwa risasi kutoka kwa polisi aliyefika na pikipiki, hapo akaona hapamfai bora aiponye nafsi yake, alianza kutimua mbio kufuata barabara ya kuelekea Mbeya lakini hakufanikiwa, alipoambiwa asimame aligeuka na kumfyatulia risasi polisi yule ambaye alibwagwa chini na kupoteza uhai, kabla Machura hajajiweka tayari alijikuta akichakazwa na risasi zilizotoka katika SMG ya polisi mwingine aliyebaki juu ya defender na kumlaza juu ya daraja hilo akiwa hana uhai.

“Mwanaharamu we! Nani aliyekwambia unaweza kuukimbia mkono wa dola?” ilikuwa ni sauti ya RPC alipokuwa akiuangalia mwili wa Machura ukiwa kwenye machela tayari kuhifadhiwa kwenye chumba cha maiti cha hospitali ya mkoa wa Iringa.

Baada ya mwezi mmoja lugalo hopspitali

Isabel alikuwa akifanya mazoezi ya kutembea katika korido za hospitali ya jeshi ya Lugalo, huku akifuatiwa kwa ukaribu na daktari wa mifupa wa hospitali hiyo Meja Kihanga.

“Naona sasa unapata nafuu sana Isabel” alimwambia Isabel ambaye alikuwa mbele yake akitumia fimbo maalum za kutembelea.

“Ee dokta, leo si kama siku zilizopita, hata naweza kukunja mguu” “Usijali utatembea tena”

Isabel aliendelea kufanya mazoezi, leo hii alifanya mazoezi kwa bidii sana, moyoni akiwa na furaha ya ajabu, hakujua furaha ile ilitokea wapi, alifarijika kuowaona ndugu na rafiki zake waliokuja kumsalimu mara kwa mara. Alipoona inatosha alirudi wodini kupumzika.

Baada ya masaa machache

“Isabel, kuna wageni wanataka kukuona” muuguzi aliyevalia sare nadhifu za kazi alimpa ujumbe huo Isabel.

“Waambie waje”

“Wewe ndiye unayetakiwa kwenda kuwaona walipo”

Isabel alisita na kukaa kimya kwa muda, alionekana wazi kuwa woga umemuingia ghafla. “Usiogope Isabel, hapa ni sehemu salama sana, jiandae nikupeleke” yule muuguzi alimuambia Isabel. Isabel alijiandaa na kisha alijinyanyua tayari kwa kwenda kuonana na wageni hao. Yule muuguzi alipotaka kumpa kiti cha magurudumu, Isabel alikataa na kutaka kutembea mwenyewe. Kwa mwendo wa taratibu akisindikizwa na yule muuguzi Isabel alijikongoja mpaka chumba kidogo kilichokuwa na viti sita vilivyoizunguka meza kubwa ya chakula, aliketi kwenye moja ya viti hivyo lakini mpaka muda huo alikuwa ni yeye na yule muuguzi tu.

Mara mlango mwingine ukafunguliwa watu watatu wakaingia ndani ya chumba hicho aliyetangulia alikuwa an sare za kijeshi zilizochafuka kwa vyeo vingi vingi, ilionesha wazi kuwa alikuwa mtu wa cheo cha juu sana jeshini, nyuma yake kulifuatiwa na mwanamke wa makamo alivalia nadhifu suti ya rangi ya jani la mgomba na nywele zake zilikuwa ni mchanganyiko nyeusi na nyeupe, mtu ambaye Isabel angestahili kumwita mama au hata bibi kabisa, mwisho kabisa alimalizia kijana mtanashati, akiwa ndani ya suti ya khaki ya mtindo wa codroy, fasheni ya vijana. Isabel alitua jicho lake kwa kijana huyu ambaye alimtambua mara moja bila kificho, Kamanda Amata.

Wote walichukua nafasi zao na kuketi.

“Isabel !” yule mwenye manyota alimuita na kumgutusha kutoka katika lindi la mawazo, “Samahani kwa kukusumbua, tumekuja mara moja kukusalimu, mbele yako mimi naitwa Meja Jenerali Chipatikila, kutoka hapa hapa Lugalo, huyu unayemuona hapa anaitwa Madam S pamoja na kijana Amata nadhani unamfahamufahamu” yule Meja alimaliza kutambulisha upande mmoja wa meza ile. Wote walimwangalia Isabel ambaye tabasamu lake halikujificha usoni mwake. “Mimi ninaitwa Isabel kutoka Kigoma” Isabel alijitambulisha kwa kifupi tu.

“Isabel, kwanza pole sana kwa misukosuko yote uliyoipata katika sakata hili ambalo ulijikuta ndani yake” Madam S aliongea kwa pozi kama kawaida yake “Mimi na ofisi yangu tutanatoa shukrani sana kwa msaada wako katika hili, hatuna muda wa kuzungumza mengi ila hapa kuna ujumbe tuliokuletea, ujumbe muhimu sana, usome mwenyewe tafadhali”. Kamanda Amata alimpatia Isabel bahasha maalum nyeupe. Isabel aliipokea na hakujua nini kilichopo ndani yake, kilichomshtua ni nembo kubwa iliyoonekana hapo juu iliyopambwa kwa rangi nzuri, yenye picha ya bibi na bwana walioshika pembe za ndovu, ngao ya Taifa, aliigeuzageuza. Kisha kwa mikono ya kutetemeka aliifungua kwa makini na kutoa karatasi iliyokuwa ndani yake, karatasi kubwa kidogo iliyoandikwa kwa mashine maalumu.

‘…Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeuthamini mchango wako wa uzalendo, wa

kuwa tayari kuutoa uhai wako kwa ajili ya Taifa lako (…). Kutokana na hayo yote mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anakupa mualiko maalum siku ya tarehe 9 Disemba, katika viwanja vya Ikulu saa kumi jioni katika hafla fupi ya kutunukia nishani mbalimbali kwa wananchi waliofanya makubwa katika kupiagania taifa lao, na wewe ukiwa mmoja wao…’

Iliandika sehemu ya barua hiyo na mwisho kumaliziwa na saini ya Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Isabel alishusha pumzi, kijasho chembamba kilimtoka mwilini, alihisi tumbo lake kama linalegea, hofu kuu iliujaza moyo wake. Maishani mwake hakuwah kufikiri hata siku moja kama atakuja hata kuliona tu jingo la Ikulu ya nchi, hakuwahi kufikiria hata kama atakuja kumuona Rais an chi sembuse kumshika mkono! Aliirudisha bahashani barua ile na kumkabidhi Madam S.

“Samahani mama, utanikabidhi siku nikiondoka” alimwambia madam S.

Siku ya Uhuru na Jamhuri Viwanja vya Ikulu – Dar es salaam

Muziki laini wa tarumbeta ulikuwa ukisikika kutoka katika brass band ya jeshi la Magereza kutoka Ukonga, waliopendezeshwa kwa sare zao nadhifu zenye rangi ya kijani na fito za njano, wote wakiwa wamevalia gloves nyeupe mikononi mwao na kuketi katika mtindo wa kupendeza, kila mmoja akikitumia chombo chake kwa ustadi huku macho yakisoma michoro Fulani katika karatasi zilizo mbele ya kila mmoja, wimbo unaoitwa Mashujaa uliotungwa na hayati Marijani Rajabu ulikuwa ukipigwa na kikundi hicho kwa ufundi wa hali ya juu.

Wageni mbalimbali walikuwa wakiingia katika viwanja hivyo kadiri ya mialiko waliyopelekwa, mabalozi na wawakilishi wa taasisi mbalimbali walimiminika katika viwanja hivyo, alkadhalika milio hadimu ya ndege wa kupendeza aina ya Tausi ilikuwa ikiongeza utamu wa shughuli hiyo.

Punde kidogo iliwasili BMW nyeusi iliyong’azwa kwa rangi safi, ikiwa inatembea taratibu kuelekea viwanja hivyo nyuma ilikuwa inafuatiwa na gari moja ya polisi na gari kadhaa binafsi ambazo zote zilikuwa zimewasha taa za vimulimuli vya kibuluu kwenye show za mbele za gari hizo. Ile BMW ilisimama katika zuria jekundu mlango ukafunguliwa, kila mtu alisimama akijuwa kuwa sasa mheshimiwa anaingia, walisahau kama mheshimiwa wanayemtarajia yumo ndani hapo. Msichana mfupi, mnene mwenye macho ya duara na mashavu yenye kubonyea atabasamupo aliteremka kwenye gari hiyo, akiwa anasaidiwa kwa kutembea kwa fimbo maalum ya kutembelea aliweza kuvuta hatua fupifupi juu ya zuria hilo huku nyuma akifuatiwa na kijana mmoja nadhifu na mwanamama wa makamo. Aliketi kwenye kiti cha mbele kabisa na nyuma yake kulikuwa na hao wapambe wake, muziki uliendelea, waandishi wa habari, wapiga picha za mnato na mjongeo walikuwa bize luchukua picha ya kupamba magazeti yao ya siku inayofuata, picha bora ya Isabel aliyekuwa ameketi hapo ambaye tangu mwanzo walishindwa kuipata picha hiyo.

Mara muziki ulinyamaza na watu wote wakasimama, kutoka mlango mkubwa wa Ikulu, mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alionekana wazi, mwenye tabasamu la bashasha kama kawaida wake, alisalimiana na watu waliokuwa mbele kabisa ambao ni vigogo wa serikali, kisha kabala ya kusema lolote aliteremka ngazi na kwenda kumpa mkono Isabel.

‘(…) leo hii taifa letu lingekuwa kwenye hali mbaya ya mauaji, damu isiyo na hati ingezijaza barabara zetu za majumba yetu. Ni hali inayohudhi lakini wengine huifurahia. Si kila mtu ni adui wa taifa lake, wapo wenye maopenzi na uzalendo wa kweli, wapo tayari kupigania hata kufa kwa ajili taifa lao, hao ndiyo tunaowataka katika Afrika na dunia yote. (…)wote mtakuwa mashahidi, mmesikia juu ya mapinduzi yaliyopangwa kufanyika, lakini vyombo vyetu imara vya ulinzi

vimeweza kuidhibiti hali hiyo, ninavishukuru sana kwa niaba ya Watanzania wote. Lakini kila jambo lina mwanzo, safari hii kijana mdogo, msichana mbichi kaonesha uzalendo wa hali ya juu wa kulipigania taifa lake, aliona ni bora afe yeye lakini mamilioni ya Watanzania waokoke na janga hilo. Tunahitaji watu kama hao, huyu ni mfano kwenu nyote Watanzania.’

Ilikuwa sehemu ya hotuba ya Rais iliyopigiwa makofi na vigelele na wote waliopo katika hafla hiyo.

‘(…) tumekusanyika hapa si kama mlivyozoea, leo ni siku ya pekee, tunaposherehekea miaka 50 ya Uhuru, tunatoa nishani moja ya uzalendo kwa msichana huyu shujaa, na jina lake litaandikwa katika kitabu cha mashujaa, na kumbukumbu yake itaingia katika makumbusho ya taifa.

Kwa niaba ya Watanzania napenda kutoa shukrani za dhati kwa dada Isabel na kuwataka vijana wote kuwa na moyo huohuo na si kushabikia tu siasa.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika, Mungu mbariki Isabel.’

Vifijo na nderemo viliisindikiza hotuba hiyo tamu. Baada ya mshereheshaji kuongea kidogo, Isabel alinyanyuka kitini na kusindikizwa kuelekea eneo maalum lililotengwa kwa tukio hilo, vimulimuli vya picha vilimulika kila upande.

Isabel alisimama mbele ya Rais, WP aliyeandali alisogea kwa ukakamavu na kupiga mguu mmoja chini kisha akanyanyua kisahani kidogo, mheshimiwa Rais alichukua kitu Fulani chenye rangi ya dhahabu na kukipachika upande wa kushoto wa kifua, katika suti ya Isabel, kicha akachukua kitu mfano wa cheti kilicho ndani ya fremu maalum na kumkabidhi Isabel, kishapo akampa mkono na kusimama naye kwa picha. Baada ya wapiga picha kupata picha za kutosha tukio hilo lilifuatiwa na dhifa maalum kwa wageni waliofika.

Baada ya tuko hilo ikia kama shukrani, serikali ilijitolea kumlipia masomo Isabel ndani na nje ya nchi, kuwajengea makazi bora nay a kisasa yeye na wazazi wake huko Kasulu, Kigoma. Na alipopona kabisa alirudi chuoni kuendelea na masomo yake na heshima aliyopewa na taifa iliendelea kubaki naye daima, tangu kwa wazee hata watoto.

HATIMA

Baada ya yote hayo, sheria ya Tanzania iliwahukumu kifungo cha maisha na kazi ngumu madam Rose, Frank na Jomse katika magereza tofauti tofauti baada ya makubaliano kati ya serikali hizi tatu.

Mwili wa Machura ulizikwa kwao Kigoma bila heshima yoyote ya kiserikali, mwili wa Tonton ulisafirishwa na ndugu zake kurudi kwao Burundi kwa taribu za maazishi.

“Asante sana kamanda Amata” Isabel alimshukuru Amata na kumpa mkono

“Nikushukuru wewe kwa kutuokoa katika hili, kutuokoa dhidi ya Mpango Hasi” Amata aliirudisha shukrani ile.

Wote wawili walinyanyua bilauri zao zilizojaa mnvinyo aina ya St Anne na kugonga cheers huku madam S akiwapiga picha ya kumbukumbu.

© richard MWAMBE ‘2013

≈ MWISHO ≈

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment