Dimbwi la Damu Sehemu ya Nne
MAISHA

Ep 04: Dimbwi la Damu

SIMULIZI Dimbwi la Damu
Dimbwi la Damu Sehemu ya Nne

IMEANDIKWA NA: ERIC SHIGONGO

*********************************************************************************

Simulizi: Dimbwi La Damu

Sehemu ya Nne (4)

Shabir alimpiga Victoria kwa mateke na ngumi bila huruma, akilalamika kitendo cha Victoria kuitoa mimba ya mtoto wake! Victoria alilia akiomba msaada lakini hakuna mtu aliyejitokeza kumsaidia. Baadaye alimvuta kwenda bafuni ambako alimwonyesha kama kipande cha nyama na kitoto kidogo kilichokuwa katika sinki la choo! “Wee kenge! Umeua mtoto wangu kweli? Nikupe adhabu gani?”

“Nisamehe baba sikuwa na jinsi nimefanya hivi kwa sababu sikutaka kumuudhi Leah, amenisaidia sana katika maisha yangu!”

“Leah? Ndio nani unayemwogopa kiasi cha kufikia kuua mtoto wangu? Leo utanikoma na humu ndani hulali, huli mpaka utakufa kwa mateso!” Alisema Shabir kwa sauti nzito ya kukwaruza na kuanza kumvuta hadi nje ya nyumba alimtupa na kufunga mlango nyuma yake na kurudi hadi chumbani ambako alichukua mzinga wa pombe kali na kuumimina wote mdomoni! Alitaka alewe alale bila kusikia kilio cha Victroria nje ya nyumba.

Victoria alilala ardhini akilia huku damu zikiendelea kumtoka, hakupata msaada wowote hadi asubuhi mlango ulipofunguliwa na Shabir kutoka nje! Hakumsaidia kitu chochote zaidi ya kumwangalia kwa jicho la dharau kisha mlango wa nyumba na kuingia ndani ya gari lake kuondoka kwenda kazini.

“Wewe kipofu! Leo utashinda hapo na kifo chako kitakukuta hapohapo!”

“Baba nisamehe!” Victoria aliendelea kuomba msamaha.

Kweli siku hiyo Victori alishinda nje bila kula chakula na Shabir aliporudi kutoka kazini jioni hakumruhusu kuingia ndani ya nyumba yake wala kumpa chakula, alilala nje akinyeshewa na mvua na kuumwa na mbu wengi! Kwa siku tatu mfululizo alilala nje bila kula na Shabir hakujali kila siku alimwambia kikatili kuwa alisubiri kifo chake ili amfukie nyuma ya nyumba.

Tumbo lilimuuma sana na joto la mwili wake lilipanda kupita kiasi alitetemeka kwa baridi, maumivu ya tumbo aliyokuwa nayo hakuwahi kufikiria kama yapo duniani! Mara nyingi aliumwa tumbo akiwa mtoto lakini hata siku moja hakuugua tumbo la mateso kama hilo.

Hakuwa na la kufanya aliamini kweli kifo chake kilikuwa kimefika, alishangaa ni kwanini Shabir alikuwa na roho mbaya kiasi hicho! Pamoja na kumlilia ampeleke hospitali bado Shabir hakujali akidai Victoria aliua hivyo ilikuwa ni lazima na yeye afe.


Nicholaus Hospitali:

Hali yake ilikuwa nzuri kidogo ingawa usoni alikuwa ameungua sana! Uso wote na sehemu ya mbele ya tumbo ulibabuka lakini macho yake yalikuwa salama kabisa, kwa hilo alimshukuru Mungu! Mzee Mohamed alikuwa amekaa pembeni mwa kitanda chake, ni siku hiyo ndiyo walipata muda mrefu zaidi wa kuongea.

“Tafadhali nieleze ni kitu gani kilikupata kijana!”Mzee Mohamed alimuuliza Nicholaus.

“Ni habari ndefu sana, itachukua muda mrefu sana kuielezea!”

“Nieleze tu nielewe!”

“Nilizaliwa nchini Tanzania, katika familia ya mfanyabiashara aliyeitwa Patrick, tulizaliwa mapacha yaani mimi na dada yangu niliyemwacha Tanzania. Tukiwa watoto wazazi wetu walifariki kwa ajali ya gari lao kugongwa na treni, pacha wangu pia alikuwemo katika ajali hiyo na kuambulia upofu!” Nicholaus alisimulia kila kitu mpaka jinsi alivyojikuta akibambikiwa madawa ya kulevya sababu ya kutamani kwenda nje ya nchi.

“Baada ya kukamatwa ulifanywa nini?”

“Nilipelekwa kwenye kiwanja cha wazi ambako nilifungwa kwenye mti ili nipigwe risasi maana sheria ya nchi yenu wafanyabiashara wa madawa hupigwa risasi mbele ya halaiki ya watu!”

“Sasa ilikuwaje ukaokoka?”

“Tetemeko!”

‘Tetemeko lilifanya nini?”

“Kabla hawajanipiga risasi lilitokea tetemeko la ajabu na ardhi ilipasuka, maaskari wote waliingiwa na woga na kujikuta wakitupa bunduki zao na kuniacha nikiwa nimefungwa katika mti ili nife kwa tetemeko!”

“Uliokokaje?”

“Msichana mmoja wa Kitanzania aliyefanya kazi katika ubalozi wa Tanzania nchini Iran, alikuja na kunifungua kutoka mtini wakati tetemeko likiendelea, baada ya kufunguliwa tulikimbia tukijaribu kujiokoa lakini mbele ardhi ilipasuka na sote tukadumbukia shimoni na kufunikwa na udongo kwa juu! Tukiwa ndani ya shimo hilo jiwe kubwa lilimkandamiza msichana aliyeniokoa na kufa, nilikaa kwa siku chini ya ardhi kwa siku nne ndipo nikaokolewa.

Nicholaus alipofika sehemu hiyo mzee Mohamed alifumba macho yake na kuonekana kuvuta kumbukumbu zake na alipofumbua macho yake alimwangalia Nicholaus usoni kwa makini.

“Nimekukumbuka!”

“Uliniona Tehran wakati nataka kupigwa risasi siyo?”

“Hapana nilikuona siku ulipookolewa kutoka katika udongo!”

“Ulikuwepo siku hiyo?”

“Ni mimi niliyefanya kazi ya kukuokoa baada ya serikali kusitisha zoezi hilo siku ya tatu!”

“Nisaidie baba sitaki kufa!”

“Usiwe na shaka nitakusaidia!”Alisema mzee Mohamed na kuichomoa simu yake ya mkononi kutoka katika kanzu yake na kuponyea namba fulani dakika kama kumi baada ya kupiga simu hiyo kijana mmoja aliingia mbio hadi chumbani.

“Inuka twende kijana!”

“Wapi?”

“Wewe nifuate tu!”

Nje waliingia ndani ya gari dogo jeupe liliondoka kwa kasi ya ajabu kama lilikuwa likitorosha kitu na aliyetoa amri ya kwenda kwa kasi alikuwa mzee Mohamed mwenyewe. Moyoni kwa Nicholaus kulijawa na wasiwasi mwingi, alihofia sana biashara ya kuchunwa ngozi! Hakumfahamu vizuri mzee Mohamed na hakuelewa alikokuwa akipelekwa.

“Baba mnanipeleka wapi?”

“Ninajaribu kukuokoa kwani ninajua wazi kuwa utatafutwa!”

Kilomita kama tano hivi mbele gari lilisimama mbele ya ngome kubwa na ndefu na nje ya ngome hiyo kulikuwa na idadi kubwa ya walinzi waliovaa magwanda ya kijeshi wote wakiwa na bunduki mikononi mwao! Walilipigia saluti mbele ya gari na lango lilifunguliwa, Nicholaus alishangazwa na heshima ambayo mzee Mohamed alipewa!

“Karibu Nicholaus hapa ndipo nyumbani kwangu nikiwa visimani!”

“Ahsante mzee!” Alijibu Nicholaus na wote waliingia ndani wakifuatana, ndani walikuta walinzi wengine wasiopungua hamsini wakiwa mbele ya lango la ukuta mwingine! Walilipiga saluti gari na mzee Mohamed alitingisha kichwa! Walipita kuta kubwa tatu ndio wakalifikia jumba la kifahari aliloishi mzee huyo tajiri!

“Unaishi hapa na nani?”

“Nilikuwa niikiishi hapa na mke wangu lakini haitakuwa hivyo tena!”


Mzee Mohamed alimtafutia daktari wa kumtibu mpaka vidonda vyake vyote vikapona na kuacha hali ya kubabuka usoni ambayo daktari alisema angebaki nayo maisha yake yote na pia kulikuwa na makovu makubwa.

Alipopona mzee Mohamed alimpa kazi ya umesenja, akawa anafuata barua za kampuni posta na kuzisambaza! Hiyo ndiyo ilikuwa kazi yake ya kwanza katika kampuni ya Gulf gas limited iliyomilikiwa na mzee Mohamed mwenyewe!

Hali ya kubabuka usoni ilimfanya Nicholaus ajulikane sana miongoni mwa wafanyakazi wenzake kwa sababu hapakuwa na mtu mwingine mwenye sura ya aina hiyo, lakini si sura peke yake iliyompa umaarufu bali pia uchapakazi! Nicholaus alifanya kazi yake vizuri na kwa uaminifu kiasi kwamba baada ya miezi sita ya kazi hiyo mzee Mohamed aligundua juhudi yake na kumpandisha cheo.

Alimfanya ajifunze udereva wa magari na alipohitimu miezi mitatu baadaye akawa dereva wake mwenyewe, alimpenda kupita kiasi na alizunguka naye kila mahali na waliishi wawili ndani ya nyumba yao. Maisha ya Nicholaus tayari yalishakuwa mazuri lakini siku zote hakumsahau dada yake! Bado alikitunza kipande cha noti walichogawana akiamini ipo siku wangekutana wakiwa hai na kukiunganisha kama walivyokubaliana!

“Ipo siku nitakuja kwenda Tanzania kumfuata dada yangu najua anateseka sana na roho inaniuma kupita kiasi!”

Visima vya mzee Mohamed vilikuwa ndio visima vilivyoongoza kwa kutoa mafuta mengi zaidi katika nchi za Ghuba na mafanikio hayo yote yalikuja kutokana na uchapaji kazi aliokuwa nao mzee Mohamed mwenyewe! Pamoja na kuwa na umri wa miaka 65 bado alifanya kazi kwa nguvu kupita kiasi jambo lililowatia morali wafanyakazi wake.


Ilikuwa ni siku ya Jumapili ya mwisho wa mwezi wa tisa! Mzee Mohamed na Nicholaus walikuwa ndani ya gari wakitoka visimani kurejea nyumbani baada ya kazi ngumu, siku hiyo mzee Mohamed alikuwa akiendesha gari mwenyewe na Nicholaus alikaa upande wa abiria.

Ndani ya gari kulijaa vicheko wakiongea hili na lile, kifupi walikuwa marafiki wakubwa! Ghafla Nicholaus alishtuka kuona gari linaacha njia kuelekea porini, alipomwangalia mzee Mohamed aliona ametupa shingo yake pembeni! Kwa haraka kabla gari halijadumbukia mtaroni Nicholaus aliudaka usukani.

“ Baba! Baba! Baba! Vipi?” Aliita Nicholaus na baadaye kuuliza lakini mzee Mohamed alikuwa kimya kabisa akikoroma na kutoa mapovu mdomoni! Nicholaus akielewa hiyo ilikuwa ni hatari alimsukuma mzee Mohamed pembeni na kuukalia usukani, akafanikiwa kulirejesha gari barabarani kabla halijapinduka.

Aliliendesha gari hilo kwa kasi kwenda moja kwa moja hadi mjini Baghdad kwenye hospitali ya AgaKhan ambako mzee Mohamed alipokelewa akiwa mgonjwa mahututi! Madaktari walipompima waligundua kuwa alipatwa na kiharusi sababu ya kupanda kwa shinikizo la damu! Upande mmoja wa mwili wake ulionekana kupooza, mdomo na jicho lake upande wa kulia vilipinda!

Alilazwa hospitalini kwa muda wa miezi miwili akipata matibabu ndipo hali yake ikabadilika na kuwa nzuri kiasi ingawa mkono wake wa kulia na mguu bado viliendelea kupooza.

Hakuna hata ndugu mmoja wa mzee Mohamed aliyekuja hospitali kumwona wala kuulizia hali yake katika kipindi chote alicholazwa hospitali, kwa utajiri aliokuwa nao halikuwa jambo la kawaida. Jambo hilo lilimshangaza sana Nicholaus kiasi cha kushindwa kujizuia kuuliza.

“Hawawezi kuja!”

“Kwanini?”

“Wao hudai mimi naringa sababu ni tajiri, binafsi nakushukuru sana Nicholaus kwa msaada ulionipa wewe ni ndugu yangu wa dhati na Mungu atakulipia! Kuna wakati nawaza hivi kama nisingekufahamu ingekuwa vipi leo?”

“Usijali baba!”

“Vipi maendeleo visimani, ni nani anasimamia?”

“Kazi inaendelea vizuri wafanyakazi wa visima A,B,C wote nimewachagulia kiongozi wao na wale wa visima D,F,E na G pia nimewawekea viongozi wao na mimi ndiye nashikilia nafasi yako, napokea taarifa za kazi zao kila siku! Uzalishaji umeongezeka maradufu! Wiki iliyopita visima vyote vilitoa mapima 150,000 badala ya 100,000 kama ilivyokuwa zamani!

“Kweli?” Mzee Mohamed aliuliza kwa mshangao hakutegemea mtoto mdogo kama Nicholaus angeweza kuisimamia kazi yake vizuri kiasi hicho.

“Ndiyo baba!”

“Nicholaus umekua! Nalazimika kuamini utaendesha vizuri kazi katika kipindi chote cha ugonjwa wangu mpaka nitakapopona?”

“Hakuna tatizo baba kaa upumzike na uwe na amani mimi mwanao nipo!”


Fikra za mzee Mohamed zilikuwa tofauti na mipango ya Mungu kwani hakupona wala kurejea katika afya yake ya zamani! Hali yake ilizidi kuwa mbaya zaidi katika miezi sita iliyofuata hatimaye alifariki dunia! Siku chache kabla ya kifo chake aliandika wosia mbele ya wanasheria kuwa mali zake zote aliziacha mikononi mwa Nicholaus akimwita mtoto wake katika wosia huo.

Visima vyote pamoja na majengo aliyokuwa nayo katika nchi za Ghuba yakawa ya Nicholaus, hakuacha kitu hata kimoja mikononi mwa ndugu zake! Kufumba na kufumbua Nicholaus akawa miongoni mwa matajiri akiwa katika umri mdogo kupita kiasi! Hakuna aliyekuwa tayari kuliamini jambo hilo!

Wakati akiwa masikini wasichana wengi walikataa uhusiano na Nicholaus kimapenzi kwa sababu ya makovu aliyokuwa nayo usoni! Lakini alipoamka tajiri wasichana wengi walianza kujigonga kwake na miezi mitatu tu baada ya mzee Mohamed kufariki alimwoa Suraia, binti mzuri na mjukuu wa mfalme wa Kuwait!

Baada ya ndoa yao Nicholaus alibadili jina na kuitwa Abdulwakil, Alimshukuru sana Mungu kwa utajiri aliokuwa ameupata. Mwaka mmoja baada ya ndoa yao walizaa mtoto wa kiume waliyemwita Patrick kama kumbukumbu ya baba yake mzazi.

Ni mwaka huo huo alisafiri na familia yake kuja hadi Arusha kwa lengo la kumfuata dada yake, alikutana na taarifa kuwa nyumba ya Shabir aliyoishi na Victoria pamoja na Leah iliungua kwa moto usiku na iliaminika kuwa wote waliteketea ndani ya moto huo!

Kilikuwa kilio kikubwa mno kwa Nicholaus kugundua kuwa pacha wake hakuwa duniani,tena alikufa katika mateso makali ya kuungua na moto. Alirudi Iraq akiwa na simanzi kubwa moyoni na aliuahidi moyo wake kutorudi tena Tanzania.

“Pamoja na kuwa amekufa nitakitunza kipande hiki cha noti kama kumbukumbu yake!”


Maumivu ya tumbo:

Siku ya nne tumbo lilivimba kupita kiasi na homa iliongezeka zaidi! Victoria alijua anakufa, hilo kwake halikuwa na mjadala tena! Kwa maumivu aliyokuwa nayo aliona ilikuwa ni bora kufa kuliko kuendelea kuishi lakini kitu pekee kilichomuumiza moyo ni kaka yake Nicholaus, hakupenda kabisa kufa kabla ya kukutana naye na kuunganisha noti zao.

Ghafla muunguro wa gari ulisikika nje ya ngome yao na mara kengele ilianza kulia! Ilikuwa ni ishara nje kulikuwa na mtu aliyetaka kufunguliwa! Aliposikiliza vizuri ingawa kwa mbali alisikia sauti ya Leah pamoja na Manjit! Akajua mkombozi amefika alijaribu kunyanyuka kwa lengo la kwenda langoni kufungua, lakini hatua tatu mbele alishindwa na kuanguka chini!

Leah alikishuhudia tukio hilo kupitia katika tundu lililokuwepo katika lango hilo, hapakuwa na njia nyingine ya kufanya ziadi ya kumwomba dereva wa teksi iliyowaleta aparamie ukuta na kuingia hadi ndani na kulifungua lango, Leah alikimbia hadi mahali alipoanguka Victoria, alishangazwa na hali aliyomkuta nayo, machozi yalimdondoka kwa uchungu.

“Vicky! Vicky! Vicky!”Aliita Leah.

“Mh!”Victoria aliitika kwa kuguna!’

“Imekuwaje? Baba yuko wapi?”

“Na….umwa! Sana nipeleke hospitali Leah!”

Hapakuwa na sababu ya Leah kuendelea kuuliza ingawa alijua kulikuwa na tatizo, kilichokuwa muhimu wakati huo ni Victoria kupelekwa hospitali haraka iwezekanavyo! Walimbeba na kumpakia ndani ya teksi na kwa haraka walimkimbiza hospitali ya Canadian Fellowships Consultant hospita ambako daktari waliyemkuta alishangazwa na hali aliyokuwa nayo mgonjwa!

“I cant deal with this case it needs a specialist in Gaenocology!”(Siwezi kumshughulikia mgonjwa huyu anahitaji bingwa wa magonjwa ya wanawake) alisema daktari huyo na palepale bila kupoteza muda alinyanyua simu na kupiga namba fulani dakika chache tu baadaye mzee wa makamo aliingia.

“Can I have a per vaginal examination tray?”(Unaweza kunipa vifaa vya kupimia sehemu za siri?)

“Yes doctor!”(Ndiyo daktari)

“And gloves too!”(Na glovusi pia)

Nesi alimpa daktari vifaa vyote alivyoomba na daktari alianza kumpima Victoria sehemu za siri, alichukua usaha katika pamba kwa lengo la kuupima.

“This is a septic incompete abortion, to be accurate we need to do an Ultra sound urgently and take pus for culture and sensitivity ok?”(Hii ni mimba iliyotoka nusu halafu ikaingiliwa na wadudu ili kuwa na uhakika zaidi tunahitaji kupiga picha tumboni na kuwakuza wadudu waliomo katika usaha ili tujue ni dawa gani itawaua!)

“Sawa daktari!” aliitikia nesi na vipimo vyote vilichukuliwa majibu yalipotoka yalionyesha kila kitu alichokisema daktari kilikuwa sawa mfuko wa uzazi wa Victoria ulikuwa umeoza na haukufaa tena!

“Nothing can be done to save her life except doing histerectomy!”( Hakuna kinachoweza kufanyika ili kuokoa maisha yake isipokuwa kuutoa kabisa mfuko wake wa uzazi!) daktari alimwambia Leah.

Mpaka muda huo Shabir alikuwa hajafika hospitalini pamoja na kupewa taarifa kuwa mke wake alirudi kutoka Bombay kumpeleka Victoria hospitali, Leah alishindwa kuelewa ni kitu gani hasa kilitokea akiwa safarini.

“What are the results for culture and sensitivity?”(Majibu ya wadudu waliokuzwa katika usaha yanasemaje?) Madaktari waliulizana katika mkutano wao.

“There are lots and lots of gram negative bacilli!”(Kuna wadudu wengi sana waitwao bacilli!)

“To which antibiotics are they sensitive?”(Wanakubali kutibiwa na dawa gani?)

“Avelox alone!”(Avelox peke yake)

“Sure?”(Kweli?)

“Then prescribe Avelox!(Basi mwandikie Avelox)

Pamoja na matibabu yote hayo bado hali ya Victoria haikuwa nzuri na Leah aliendelea kuishi naye wodini kwa siku saba akitibiwa yeye na mtoto wake Manjit walikuwa hospitalini siku ya nane madaktari waliamua kumpeleka Victoria chumba cha upasuaji ambako mfuko wake wa uzazi ulitolewa.

“So, she will never bear children?”(Kwa hiyo hatazaa kabisa maishani mwake?)

“That’s the truth, but her life is also very important!”(Huo ndio ukweli lakini maisha yake pia ni muhimu sana)

“Kweli!”

Siku hiyo jioni baada ya Victoria kuletwa wodini kutoka chumba cha upasuaji, Leah alipewa ankara za matibabu yote aliyopewa Victoria tangu alazwe hospitali, kwa sababu hakuwa na pesa aliondoka na Manjit kwenda nyumbani kumwomba pesa Shabir.

“Ningekuwa na mtu mwingine wa kunisaidia nisingekwenda kwa Shabir!” aliwaza Leah wakati akitembea kutoka hospitali.

Walikuta mlango wa nyumba ukiwa wazi hiyo halikuwa jambo la kawaida kwa mlango wa nyumba yao kuachwa wazi! Hilo liliwashtua kidogo lakini hawakujali waliingia hadi ndani.

“Mh mama kuna harufu ya kitu gani?”Manjit aliumuuliza mama yake.

“Sijui ni kitu gani lakini ni mnyama ameoza!”

Ilikuwa harufu mbaya na kali mno, Leah na Manjit walishindwa kuelewa ilitokea sehemu gani ndani ya nyumba! Walijaribu kuita jina la Shabir lakini hakuna mtu aliyeitika, kwa sababu gari lilikuwa nje waliamini asilimia mia moja Shabir alikuwa ndani! Ilikuwa si kawaida yake kutoka nje ya ngome bila gari.

Ilibidi wabadili na kuanza kuita jina la bibi Sundra wakiamini alikuwemo ndani, hawakuelewa kuwa alishaachishwa kazi na Shabir muda mrefu ili apate nafasi ya kumbaka Victoria kwa urahisi, waliita jina la bibi Sundra kwa muda mrefu lakini bado hawakuitikiwa walishindwa kuelewa kulikuwa na nini ndani ya nyumba na harufu ilizidi kuwakera.

“Mama ni nini lakini?”

“Hata mimi sifahamu lakini hii harufu ni kama inatokea huko ndani!”

“Wapi chumbani kwenu?”

“Ndiyo!”

“Basi nenda kaangalie labda kuna panya amefia ndani!”

“Lakini tangu lini nyumba hii ina panya?”

“Hata mimi sijui, lakini kaangalie tu mama!”

Leah aliondoka sebuleni na kuanza kutembea kwenda chumbani, kadri alivyokikaribia chumba chao cha kulala ndivyo harufu ilivyozidi kuongezeka, mlango ulikuwa wazi aliusukuma na kuingia hadi ndani ambako harufu ilizidi kuongezeka kiasi cha kumfanya abane pua yake kwa vidole! Aliangaza huku na kule kuona kama kulikuwa na kitu kilichofia humo ndani lakini hakukiona, aliangalia uvunguni chini ya meza na hata darini lakini hakukuwa na kitu chochote.

“Manjit!”

“Naam mama!”

“Mbona hakuna kitu?”

“Kweli?” Aliuliza Manjit akielekea chumbani, alipoingia naye harufu ilimshinda na kujikuta akibana pua yake.

“Sasa tufanye nini?”

“Mpigie kwanza baba simu aje akupe pesa za malipo tupeleke hospitali, hii harufu tutakuja kuishughulikia baadaye!”

“Sawa!” Aliitikia Leah kisha akakaa kitandani na kunyanyua simu iliyokuwa pembeni mwa kitanda chao, ulikuwa ni muda mrefu hajalala kwenye kitanda chake na alitamani kufanya hivyo lakini suala hilo lilikosa umuhimu kwa wakati huo kwani alihitaji pesa upesi ili akalipe hospitali na matibabu ya Victoria yaendelee.

Alinyanyua simu na kupiga namba za ofisini kwa Shabir kwanza akifikiri labda siku hiyo gari lake lilikuwa bovu aliamua kutumia teksi, simu haikupokelewa hata baada ya kuwa amepiga zaidi ya mara tano! Iliita tu kwa kipindi kirefu na kukatika.

“Sijui wamefunga sababu hakuna anayepokea!”

“Mama jaribu simu yake ya mkononi!”Manjit alimshauri mama yake na kweli Leah akaanza kupiga namba za simu ya mkononi ya Shabir, alishangaa ilipoanza kuita humohumo ndani ya chumba! Wote wawili walishangaa na kushindwa kuelewa ni wapi alikokuwa Shabir kwa wakati huo kwani kuwepo kwa simu yake ndani kulimaanisha hata yeye mwenyewe alikuwa ndani au hakuwa mbali na nyumbani.

“Labda amekwenda dukani tujaribu kumsubiri!” Leah alimwambia Manjit.

Walisubiri kwa karibu masaa mawili mpaka Manjit akaanza kusinzia bila Shabir kuonekana walijikuta wakianza kuingiwa na wasiwasi, ilikuwa si rahisi hata kidogo kwa mtu makini kama Shabir kuondoka nyumbani kwenda matembezini na kuacha nyumba ikiwa wazi, fikra za Leah zilianza kumfanya ahisi Shabir alikuwa ametekwa na majambazi na si ajabu alikuwa ameuawa lakini jambo hilo hakudiri hata kidogo kumwambia mtoto wake Manjit.

“Mama nataka kukojoa!”

“Vua uingie chooni ukojoe lakini tafadhali usichafue choo!”

“Sawa mama!” Manjit aliitikia kisha kunyanyuka akielekea kwenye choo kilichokuwa ndani ya chumba hicho, alifungua mlango na kuanza kuingia ndani huku suruali yake ikiwa imefunguliwa zipu tayari kwa kukojoa, alisimama mbele ya shimo la choo na kuanza kuachia mkojo wake taratibu kabla hajamaliza alinyanyua uso wake kuangalia juu tena bila sababu yoyote ni huko ndiko macho yake yalipambana na mwili wa mtu aliyevimba ukining’inia kwenye ubao uliokuwa darini. Alipoviangalia viatu vya mtu aliyekuwa akining’inia aligundua vilikuwa viatu ya baba yake.

“Mama! Mama! Mama! Njoo uone baba huyu hapa!” Alipiga kelele Manjit akikimbia kwenda nje ya choo.

“Niniiii?”

“Baba yupo chooni!”

“Chooni? Anafanya nini?”

“Ananing’inia darini!” Alijibu Manjit lakini maneno hayo kwa Leah yalimaanisha kitu kikubwa zaidi, bila kujiuliza mara mbili alijua Shabir alikuwa amejinyonga na si ajabu harufu iliyosikika ilikuwa ni ya mwili wake ulioharibika, hakuwa mwongo wala hakuidanganya nafsi yake ni kweli mume wake Shabir alikuwa akining’inia darini mwili wake ukiwa umevimba kupita kiasi! Leah alianza kulia bila kujua kilichopelekea mume wake achukue uamuzi mbaya kiasi hicho.

“Kuna nini kilichotokea hapa?” Aliuliza Leah huku akilia, alimkumbatia mtoto wake na wote waliendelea kulia.

Dakika chache baadaye Leah aliona kipande cha karatasi kikiwa sakafuni, alikichukua na kuanza kukisoma! Ni hicho ndicho kilimpa angalau picha ya kichotokea ingawa haikuwa picha halisi, kiliandikwa:

Mke wangu Leah,

Nimechukua uamuzi huu kwa sababu kitendo nilichokifanya kisingekufurahisha, nimekukosea sana naomba unisamehe na pia niombee sana msamaha kwa Victoria kama atapona! Mwambie ni shetani aliyeniingia mpaka nikajikuta nikifanya mambo niliyomtendea, alikuwa mtoto mwema na mtiifu ambaye hakustahili hata kidogo unyama nilioufanya! Najuta kufanya kosa hilo, naomba umshughulikie mpaka apone! Mimi natangulia kuzimu na ninajua adhabu yangu itakuwa mbaya sana, acha nikutane nayo kwa sababu ninastahili.

Ni mimi mumeo

Marehemu Shabir.

Leah aliisoma barua hiyo mpaka mwisho, ndiyo ilimpa jibu kuwa Shabir hakunyongwa bali alijinyonga mwenyewe lakini haikumpa jibu la kwanini alijinyonga na ni kitu gani alimfanyia Victoria mpaka akaamua kuchukua uamuzi huo, kwa mbali akilini mwake alihisi labda Shabir alimbaka Victoria mpaka kumpa ujauzito! Kichomfanya afikirie hivyo ni mazingira ya safari yake ya Bombay, ilikuwa ya ghafla mno na haikuwa na sababu ya kuwepo na Shabir kusisitiza Victoria abaki, kitu kingine kilichomfanya awaze hivyo ni ugonjwa uliokuwa ukimsumbua Victoria, kuwa mimba iliharibika na kuozesha mfuko wake wa uzazi.

“Mimba aliitoa wapi Victoria kama sio kwa Shabir?” Aliwaza Leah huku akilia machozi.

Baadaye aliamua kupiga simu polisi kuwataarifu juu ya tukio lililotokea, dakika kama kumi baadaye polisi walifika wakiwa na magari yao na kugonga mlango wa nyumba, Leah alitoka na kwenda kuwafungulia. Waliingia moja kwa moja hadi ndani na Leah aliwapeleka hadi chumbani kwake na kuwafungulia mlango wa choo, walimwona Shabir akining’inia darini.

“Nyie mlikuwa wapi mpaka ameharibika kiasi hiki? Mlikuwa hamjagundua tu?”

“Tulikuwa safarini Bombay, tulirudi siku nane zilizopita na kumkuta msichana tuliyemwacha hapa nyumbani na baba akiwa hoi bin taaban, tena alikuwa hapo nje! Tukamchukua na kumpeleka hospitali ambako alilazwa na kugundulika alitoa mimba vibaya na mfuko wake wa uzazi ukaharibika, tumekaa hospitalini mpaka leo bila mume wangu kuja kutuona! Tuliporudi hapa ndipo tukakuta harufu hii mnayoisikia, tulianza kutafuta ni kitu gani kilikuwa kikinuka namna hiyo, mwanzoni tulifikiri ni panya amekufa lakini baadaye tukamkuta humu akining’ini….!” Leah alishindwa kumalizia na kuangua kilio, askari aliyekuwa jirani alimkumbatia na kuanza kumfariji.

“Kitu gani kingine mlikikuta?’

“Ni hii barua tu!”

“Hebu niione!” Aliuliza askari mmoja mwenye nyota tatu begani.

Leah alimkabidhi askari yule barua na akaanza kuisoma hadi mwisho, alipomaliza alitikisa kichwa chake kisha akamuangalia Leah kwa macho ya huruma usoni.

“Najua kilichotokea!”

“Ni nini?”

“Nitakueleza baadaye, hebu vijana teremsheni huo mwili!”Aliamuru mzee huyo na palepale maaskari walivaa glovusi mikononi na kuushusha mwili wa Shabir kutoka darini, waliubeba na kuupeleka moja kwa moja hadi kwenye gari ambako waliupakia, Leah na Manjit walipanda gari jingine na safari ya kwenda kituo cha polisi ilianza, mwili wa Shabir ulipelekwa moja kwa moja hospitali ya Canadian Hospital ambako ulihifadhiwa chumba cha maiti.

Kituoni Leah alitoa maelezo yake na baadaye kuruhusiwa kurudi nyumbani ambako alishindwa kukaa na kuamua kuondoka kwenda hospitalini, alimkuta Victoria bado yupo katika maumivu makali! Alitamani sana kumuuliza juu ya kilichotokea lakini alishindwa, na alishindwa pia hata kumweleza juu ya kifo cha Shabir! Manjit alikuwepo pamoja nao, alikuwa bado akiendelea kumlilia baba yake mzazi Shabir! Hakuwahi pamoja na umri wake mdogo kuwaza kuwa siku moja mwisho wa baba yake ungekuwa huo.

Manjit na mama yake hawakulala mpaka asubuhi, mioyo yao ilikuwa bado iko katika majonzi makubwa, Leah alitamani sana kujua nini kilichotokea kati ya Victoria na mumewe mpaka akaamua kujinyonga, moyo wake ulimwambia amuulize Victoria lakini upande mwingine alisita, aliona angeweza kumsababishia maumivu makali zaidi. Lakini asubuhi ya siku hiyo hali ya Victoria ilikuwa nzuri kidogo, dawa za Avelox alizoandikiwa zilionekana kumsadia kidogo.

“Dada Leah kwanini Manjit analia tangu jana?” Victoria aliuliza.

“Hakuna kitu anakuhurumia tu!”

“Ahsante sana kwa kuja maana usingekuja kwa hakika ningekufa! Mambo aliyonifanyia baba ni mabaya mno na sikutegemea angeweza kunifanyia hivyo!”

“Mambo gani?” Ingawa Leah hakutaka kuuliza alijikuta swali hilo likimtoka mdomoni, badala ya Victoria kutoa jibu alibanwa na kwikwi na kuanza kulia, kitendo hicho kilisababisha nyuzi zilizoshonwa tumboni mwake zote zifumuke na utumbo kuanza kuonekana nje!

“Nesi! Nesi!” Leah aliita

“Nini! Nini dada?”

“Njoo uone utumbo unataka kutoka!”

Manesi wote waliokuwa ofisini walitimua mbio hadi kitandani alikolala Victoria, walishangazwa na hali waliyoikuta! Victoria alikuwa bado akilia kwa nguvu, walielewa hiyo ndiyo sababu iliyofanya nzuri zifumuke kwa sababu alilia kwa nguvu na kukaza misuli ya tumbo wakati kidonda kilikuwa bado hakijapona vizuri.

“Call the doctor immediately!”(Mwiteni daktari haraka!) Alisema muuguzi mmoja na simu ilipigwa ofisini kwa daktari Martin Cook, bingwa wa upasuaji wa hospitali ya Canadian Fellowship Consultant Hospital! Haikuchukua hata dakika mbili daktari akawa tayari ameshafika, alipoliona tumbo la Victoria lilivyokuwa wazi hakuwa na kingine cha kushauri zaidi ya Victoria kurudishwa chumba cha upasuaji.

“She needs secondary stiching!”(Anahitaji kushonwa kwa mara ya pili!)

Victoria alikimbizwa haraka chumba cha upasuaji na kumwacha Leah akilia na kujilaumu ni kwanini aliliuliza swali lake,chumba cha upasuaji Victoria alishonwa kwa mara ya pili, ilikuwa ni kazi ngumu kwa sababu kidonda kilishakaa muda mrefu, iliwachukua madaktari masaa mawili kuirekebisha hali hiyo walipomaliza alirudishwa wodini, safari hii haikuwa wodi ileile ya mwanzo alipelekwa katika wodi yenye uangalizi maalum (ICU) ambako hakuna ndugu hata mmoja aliyeruhusiwa kumwona mpaka kidonda chake kilipopona vizuri siku kumi na saba baadaye! Katika siku hizo mazishi ya Shabir yalifanyika.

Siku ya ishirini aliruhusiwa kutoka hospitali kwenda nyumbani ambako alimsimulia Leah kila kitu kilichotokea wakati yeye na Manjit wakiwa Bombay, tangu mwanzo hadi mwisho wa habari hiyo Leah na Manjit walilia machozi walishindwa kuamini kama Shabir alikuwa mtu katili kiasi hicho! Walimhurumia sana Victoria kwa yaliyomkuta, habari hiyo ilipunguza maumivu waliyokuwa nayo juu ya Shabir na kifo chake, hata Manjit alijikuta akisema “Kifo cha baba kilikuwa adhabu yake!”

“Nisamehe dada sikupenda kufanya hivyo, nisingeweza kukusaliti kwa sababu wewe ni kila kitu kwangu ila baba alinilazimisha, ni heri ningekuwa na macho ningeweza kupambana naye!” Alisema Victoria akiwa amepiga magoti na kumshika Leah miguuni.

“Hapana usifanye hivyo Victoria, nakupenda wewe ni kama mtoto wangu! Nimekulea tangu utoto wako, ninajua si kosa lako huna haja ya kuniomba msamaha, ninakupenda, nitakupenda siku zote za maisha yangu. Pole sana!”

“Ahsante dada!”

Huo ndio ukawa mwisho wa Shabir, kifo chake kilimaanisha mali zote alizozimiliki kubaki mikononi mwa Leah na Manjit mtoto wake, Manjit wakati huo alikuwa na umri wa miaka kumi na mbili tu hivyo hakuwa na uwezo wakuiendesha biashara ya baba yake, Leah angeweza kufanya hivyo lakini elimu yake ilikuwa ndogo na isitoshe kosa alilolifanya Shabir ni kutomwonyesha jinsi biashara yake ilivyofanyika.

Kiliitishwa kikao cha wafanyakazi wa vituo vyote vya mafuta walivyovimiliki katika nchi ya Canada, ni katika mkutano huo ndiko wahasibu wataalam wa mahesabu wa kampuni walimshauri Leah aiweke mali yote chini ya uangalizi wa kampuni ya Wataalam wa miradi, hao ndio wangemsaidia kuiendesha biashara yake mpaka Manjit afikishe umri wa miaka kumi na nane au ishirini, wakati huo atakuwa akisomeshwa katika shule za mahesabu na uchumi ili akija kukabidhiwa miradi ya baba yake asishindwe kuiendesha, lilikuwa ni wazo zuri lililoungwa mkono karibu na wajumbe wote wa mkutano na bila mvutano wowot lilipitishwa, kampuni ya MULTI LATERAL INVESTIMENT INC. Iliyomilikiwa na wataalam wa mahesabu nchini Canada ilikabidhiwa shughuli zote za kampuni ya Shabir.

Chini ya usimamizi wa kampuni hiyo kazi zote ziliendeshwa vizuri, kiasi kwamba baada ya mwaka mmoja mkutano wa Bodi ulipokaa faida kubwa ilikuwa imepatikana na Bodi kulazimika kuipa MULTI LATERAL INVESTIMENT INC mamlaka ya kuendelea hiyo kwa miaka mingine kumi zaidi, kipindi ambacho Manjit angekuwa ametimiza umri wa miaka ishirini na mbili na angekuwa amemaliza elimu ya Chuo kikuu.

“Mwanangu nataka usome sana ili hii kazi isije kukushinda!”

“Usiwe na wasiwasi mama najitahidi kadri ya uwezo wangu na sitakuangusha!” Hiyo ndiyo ilikuwa ahadi ya Manjit kwa mama yake.


Miaka kumi na mbili haikuwa mingi kama ilivyotegemewa na wengi ghafla ilikatika na kampuni ya MULTI LATERAL INVESTIMENT INC ikakabidhi kazi kwa Manjit ambaye tayari alikuwa na umri wa miaka 22 akiwa na digrii ya uchumi kutoka chuo kikuu cha Ottawa! Kwa mwili wake ulivyokuwa mkubwa ilikuwa si rahisi hata kidogo kuamini kuwa umri wake ulikuwa ni miaka 22, kama mtu angeulizwa ni lazima angetaja hata miaka 35 au zaidi, Manjit alionekana kuwa na umbile kubwa kuliko umri wake.

Wakati huo Victoria alikuwa na umri wa miaka 42! Alikuwa mama mzima, hakuwa na mtoto wala mchumba! Mambo yote aliyofanyiwa na marehemu Shabir alishayasahau lakini jambo moja alishindwa kabisa kulitoa akilini mwake nalo ni kaka yake Nicholaus! Bado alimkumbuka Nicholaus kupita kiasi, kila siku iliyokwenda kwa Mungu ilikuwa ni lazima amfikirie, bado alikitunza kipande cha noti walichogawana miaka mingi kabla, ni hicho ndicho kilichomtia simanzi zaidi lakini aliamini iko siku angekutana na kaka yake. Leah aliishi naye vizuri na alimtunza kama mtoto wake.

“Ipo siku nitakutana na Nicholaus ninaamini yupo hai!”

Baada ya Manjit kukabidhiwa kampuni yake na Multilateral Investiment Inc. kwa haraka alichukua uamuzi wa kuibadilisha kampuni yake jina na kuiita Canada Oils & Gas Inc. Mabadiliko hayo yaliwafanya watu wengi kuamini Manjit angeweza kuiendesha vizuri kampuni yake.

Alipangua ngazi zote za uongozi kuanzia juu hadi chini na aliajiri Mkurugenzi mpya aliyemtoa katika kampuni ya Multilateral. Yeye alibaki kama mwenyekiti wa kampuni hiyo, mama yake pamoja na Victoria wakawa wajumbe wa bodi.

Miaka mitatu iliyofuata kampuni yake ilishuhudia mafanikio makubwa kupita kiasi, vituo vya mafuta viliongezeka katika nchi nzima ya Canada! Canada oil & Gas Inc ilimiliki vituo vitatu hadi vinne vya mafuta katika kila miji mikuu yote nchini humo. Manjit akabadilika na mtu mashuhuri na kijana tajiri kuliko hata alivyokuwa baba yake.

“ Mama! Nitajitahidi kufanya kazi kwa nguvu zote ili tufanikiwe zaidi!”

“Sawa mwanangu, kila utakachofanya ni sawa kwangu!”

Maneno ya mama yake yalimpa moyo sana Manjit, mwaka huo huo ilitangazwa tenda ya kuliuzia mafuta Dizeli na Petroli jeshi la nchi hiyo, ilikuwa ni tenda ya mamilioni ya dola za kimarekani na ilikuwa ni kazi kubwa kuliko kazi zote alizowahi kufanya tangu akabidhiwe kampuni.Wafanyabiashara wengi nchini Canada waliitaka kazi hiyo na kampuni ya Canada Oils& Gas nayo ilikuwa miongoni mwa kampuni zilizoiomba.

“Mama ni lazima tufanye lolote linalowezekana kuhakikisha tunapata tenda hii?”

“Fanya lolote mwanangu, kila kitu ni ruksa!”

“Ni lazima tutumie pesa mama! Sababu wanasema tumia pesa ili upate pesa!”

“Sawa tu mwanangu!”

Hilo ndilo alilofanya Manjit, alitumia pesa nyingi kuwahonga watu wote waliokuwa na mamlaka ya kuitoa tenda mpaka akaibuka mshindi! Ilikuwa ni furaha kubwa mno kwa Manjit, mama yake, Victoria na hata wafanyakazi wengine wa kampuni hiyo! Walijua kupatikana kwa kazi hiyo kungeongeza maslahi yao.

“Mama tumetajirika!”

“Hakika mwanangu! Nimeamini una akili”

“Itabidi nisafiri hadi Iran kwenda kuongea biashara na matajiri wa huko ikiwezekana tuwe tunapata mafuta ya mkopo kutoka kwao na kuwalipa baada ya kupata malipo yetu kutoka serikalini!”

“Fanya uwezalo!”

Wiki moja baada ya kupata tenda hiyo ilibidi Manjit alisafiri hadi Iran ambako aliongea na wafanyabiashara wengi wenye visima vya mafuta lakini hakufanikiwa kupata hata mmoja aliyekuwa tayari kufanya naye biashara, kila aliyemfuata na kumweleza kuwa mahitaji yake ya mafuta yalikuwa mapipa milioni mbili kwa mwezi, aliiona kazi hiyo ni kubwa sana na kukiri asingeweza kukidhi haja yake!

“Nafikiri ungejaribu Iraq kuna kampuni moja inaitwa Gulf Gas Limited hiyo inaweza kukupa mafuta hata zaidi ya hayo!”

“Inamilikiwa na nani?”

“Awali ilimilikiwa na Mohamed Mashreef huyo alikuwa mfanyabiashara wa Kiarabu lakini alifariki na kumrithisha Mwafrika mmoja, ninavyosikia yeye pia ni mgonjwa kazi zote hivi sasa zinaendeshwa na mtoto wake aitwaye Patrick!”

“Patrick?”

“Ndiyo!”

“Mbona jina si la kiarabu?”

“Ni mchanganyiko wa Mwarabu na Mtanzania!”

“Mtanzania?”

“Ndiyo, baba yake alitokea Tanzania miaka mingi iliyopita!”

“Nahitaji kumwona!”

“Basi safiri mpaka Iraq!”

Siku hiyo hiyo jioni Manjit alipanda ndege na kusafiri hadi Baghadad ambako aliingia usiku na kushindwa kumtafuta tajiri Patrick ikabidi alale mpaka siku iliyofuata asubuhi alipokwenda ofisini kwake! Nje ya ofisi hiyo kulikuwa na idadi kubwa sana ya maaskari walionekana kuimarisha ulinzi lakini Manjit alifanikiwa kuingia hadi mapokezi baada ya kujitambulisha, mapokezi alipokelewa na msichana mrembo wa Kiarabu na kukaribishwa aketi kitini!

“Can I see the Director?”

“Sorry the Director is not around! He is admitted in hospital, but his Deputy is around, would you like to see him?” (Mkurugenzi hayupo lakini Naibu wake yupo, je ungependa kumwona yeye?)

“Yeah! Because this is an official matter I think it can be be handled by any authority! (Ndiyo kwa sababu hili ni suala la kikazi na linaweza kushughulikiwa na mtu yeyote!)

Baada ya jibu hilo msichana huyo alinyanyua simu yake na kubonyeza namba fulani kisha akaanza kuongea na mtu wa upande wa pili na kumueleza kuwa palikuwa na mgeni aliyetaka kumuona! Alipoweka simu yake chini alimuashiria Manjit aingie ndani! Alinyanyuka na kuanza kutembea taratibu akiufuata mlango uliokuwa kulia kwake ilikuwa ni ofisi ya kifahari, iliyopambwa na vioo kila upande! Iliashiria kuwa mwenye ofisi hiyo alikuwa na uwezo mkubwa kipesa! Manjit aliingia ndani akiwa na hamu kubwa ya kumuona Patrick, mawazoni kwake alifikiri mtu huyo alikuwa anakwenda kumwona ni mnene na mzee lakini alishangaa kukuta mtu aliyekuwa akimtafuta ni kijana mdogo kuliko hata yeye!

“You are welcome sir!”(Karibu sana bwana!)

“Thank you! I’m Mr. Manjit Shabir!”(Ahsante! Ninaitwa Bwana Manjit Shabir)

“Manjit Shabir? The owner of the Oil company in Canada!”(Manjit Shabir? Mwenye kampuni ya Mafuta Canada?)

“Oh yeah!How did you recognise me?”(Ndiyo umenigunduaje?)

“Nice to meet you Sir, I’m Patrick N. Abdulwakil I have been hearing of your name so many times and really wanted to meet you one day! Today my dream has come true!”(Nimefurahi kukutana na wewe! Ninaitwa Patrick N. Abdulwakil nimekuwa nikisikia jina lako mara nyingi na nilitaka sana kukutana na wewe siku moja! Leo ndoto yangu imetimia!) Alisema Patrick akinyanyuka na kumkumbatia Manjit, walionyesha furaha kubwa sana.

Waliongea mambo mengi kuhusu biashara yao ya mafuta na hatimaye kufikia muafaka wa kufanya biashara kwa ushirikiano! Patrick alikubali kumuuzia Manjit mafuta kwa mkopo kwake kazi yake pekee ingekuwa ni kuyasafirisha mafuta kutoka Baghdad kwenda Montreal Canada na angetakiwa kulipa pesa baada ya kuyauza mafuta kwa jeshi! Kwa Manjit mambo yalikuwa kama alivyopanga, hakutegemea mipango ingekuwa rahisi kiasi kile furaha yake ilizidi kuongezeka.

“Lakini kumbuka kuwa kampuni yangu haitawajibika na hasara yoyote itakayotokea katika usafirishaji wa mafuta, hata kama meli itazama sisi tutakachojua ni kulipwa pesa yetu tu, sijui jambo hilo utaliweza?”

“Haina shida kabisa Patrick! Hilo litafanyika!” Alijibu Manjit na mkataba ulisainiwa siku hiyo hiyo Manjit aliondoka kurudi Canada bila kuelewa undugu na uhusiano uliokuwepo kati yao.


Kwa Manjit kupata tenda ya kuliuzia jeshi mafuta ilikuwa furaha kubwa na dalili ya mafanikio lakini kwa wafanyabiashara wenzake walioikosa tenda hiyo hasira ziliwajaa, hasira zilizojaa chuki dhidi ya Manjit hasa baada ya kugundua kuwa Manjit alitumia pesa kuwahonga viongozi wa jeshi ndio akapata tenda hiyo, walichukia mno na kulazimika kuunda umoja wa kupambana naye, waliahidi kumkwamisha katika biashara zake zote!

“Ni lazima aanze moja, naona hizi mali za kurithi zimempa kiburi anashindwa kuheshimu wazee, huyu ni mtoto mdogo sana hawezi kutusumbua sisi!” Alisema bwana Davids, mmiliki wa kampuni ya kusafisha mafuta machafu nchini Canada, Crude Oils Inc.

“Kweli! Ni lazima tumkomeshe” Wenzake watano waliitikia.

Mipango mingi ilipangwa usiku huo ili kumwangusha Manjit kibiashara, matajiri waliokosa tenda ya kuuza mafuta jeshini waliunganish nguvu zao ili kupambana nae! Miongoni mwa mipango yaliyopanga ni kumuua Manjit mwenyewe na kama si yeye basi mama yake au Victoria! Ili mradi tu kuhakikisha anarudi nyuma na kufilisika kabisa! Hawakuwa tayari hata kidogo kuona mtoto mdogo tena mgeni katika nchi yao akitajirika mbele ya macho yao!

“Nitazilipua meli zote za mafuta zitakazokuwa zikibeba mafuta yake kutoka Iraq kuja hapa Canada! Hilo niachieni mimi” Alisema Alexandria mmiliki wa vituo vya mafuta vya CanadOils

“Nitatuma watu kuivamia nyumba yake na kila mtu atakayekuwemo ndani siku hiyo ni lazima afe hata yeye mwenyewe!” mfanyabiashara mwingine aliahidi.

“Nitatumia watu wa Mamlaka ya kodi ili wayakague mahesabu yake kuona kama analipa kodi, nina uhakika atakuwa na matatizo makubwa! Na hapo ndipo tutakapomaliza! Canadian Revenue Authority watakamata mali zake zote!” Mwingine tena aliongea kwa hasira!

Yote yaliyosemwa katika mkutano huo hayakua utani, wazee hao walidhamiria kumkomesha Manjit! Walidhamiria kumfanya masikini na hata kumuua kabisa yeye na familia yake yote. Manjit hakujua lolote lililoendelea mioyoni mwa wafanyabiashara wenzake na aliamini hakuna aliyeijua siri yake ya kushinda zabuni hiyo ya kuuza mafuta.


Meli tatu za kwanza zilizobeba matenki ya mafuta ya karibu dola milioni 120 ambazo kwa wakati huo zilikuwa sawa na shilingi za Kitanzania Bilioni 84 zilikuwa zikisafiri katika bahari ya Hindi kuelekea Canada, pamoja na kubeba mafuta ndani ya meli hizo kulikuwa na wafanyakazi wasiopungua mia mbili na kumi!

Huo ndio ulikuwa mzigo wa kwanza ambao Manjit alitegemea kuumwaga jeshini Canada na kupata faida ya dola za Kimarekani zisizopungua 200! Ilikuwa ni faida kubwa mno iliyompa uhakika asilimia mia moja kuwa kama angefanya biashara hiyo kwa mwaka mmoja angeweza kutajirika pengine kuliko mtu mwingine yeyote katika nchi hiyo.

Alikuwa nyumbani kwake akipumzika na familia yake ikiwa ni siku mbili tu tangu aongee na tajiri Patrick akipewa taarifa kuwa tayari mzigo ulishaondoka nchini Iraq na ulitegemewa kuingia Canada baada ya wiki tatu! Ghafla simu yake iliita na mama yake aliipokea na kumpa Manjit.

“Hallow! Manjit anaongea nani mwenzangu?”

“Mimi ni Patrick!”

“Ndiyo za tangu juzi?”

“Ni nzuri lakini sio nzuri sana!”

“Unaumwa?”

“Hapana ila nina taarifa mbaya kidogo, meli zote zilizoondoka hapa na mafuta zimelipuliwa! Wafanyakazi wote wamekufa na meli bado zinawaka moto huku matuta yakimwagika baharini, nilipoteza nao mawasiliano tangu jana leo nimepokea simu ya upepo kutoka kwenye meli ya Atlantic Sailors, wamenitaarifu kuwa waliiona meli yetu ikiwaka moto baharini! ”

“Mungu wangu unaniambia kweli?”

“Huo ni ukweli siwezi kukudanganya hata mimi nimechanganyikiwa! Nafikiri kwako itakuwa hasara kubwa sana, kwa kweli biashara umeianza vibaya kwani sisi mafuta yetu itabidi yalipwe kama kawaida!”

Taarifa hiyo ilimfanya Manjit alie machozi kwani zilikuwa ni habari mbaya mno kwake, alijua ni njama lakini alishindwa kuelewa ni nani aliyezifanya hata mama yake pamoja na Victoria nao walishindwa kuvumilia wakajikuta wakibubujikwa na machozi!

Siku iliyofuata ilibidi Manjit asafiri hadi Iraq kuongea na Patrick ambaye aliendelea kusisitiza juu ya makubaliano yao katika mkataba ulioeleza wazi kuwa Manjit alitakiwa kulipa pesa zote alizodaiwa pamoja na kuwa mafuta yalimwagika baharini! Manjit hakuwa na ubishi alikubali kufanya hivyo lakini si kwa wakati huo.

Patrick alikubali na kumpakilia tena meli nyingine nne zenye mafuta ya thamani ya dola milioni 600 ambazo kwa shilingi za Kitanzania zilikuwa ni sawa na bilioni 480 kwa wakati huo, lakini pia meli hizo hazikufanikiwa kufika nchini Canada, zikiwa katika eneo lile lile zilipolipukia meli za mwanzo nazo ziliangushiwa mabomu na kulipuka! Mafuta yote yalimwagika na watu wote waliokuwemo waliteketea kwa moto, Manjit alizidi kuchanganyikiwa na kushindwa kuelewa ni nani aliyekuwa akimfanyia ukatili huo!

Alipoongea na Patrick juu ya tatizo hilo yeye aliendela kusisitiza juu ya malipo yake! Tayari deni lilishafika dola za Kimarekani milioni 720 Zilikuwa ni pesa nyingi mno kwake kuzilipa na kuendelea kufanya biashara, pamoja na matatizo yote hayo Manjit hakukata tamaa alijipa matumaini kuwa angeweza kulipa deni hilo baada ya kufanya biashara na jeshi kwa muda, hivyo aliomba apakiliwe mafuta mengine tena na Patrick alikubali.

Kwa hasira ya kufidia safari hii alipakia katika meli saba zote zikiwa na mafuta ya thamani dola milioni 800, ilikuwachenga waliokuwa wakimhujumu nne kati ya meli hizo zikapita njia ya kawaida na tatu zikapitishwa njia ya mzunguko wa CapeTown, Afrika Kusini kisha kwenda Afrika ya Magharibi na baadaye kuingia Canada, kwa njia hiyo Manjit aliamini angeweza kufikisha mafuta yake hata kidogo.

Meli zote saba hazikufanikiwa kufika Canada, zote zililipuliwa zikiwa njiani! Manjit alichanganyikiwa zaidi, deni alilokuwa nalo kwa Patrick lilimtisha! Aliamini tayari alishakuwa masikini na angeweza hata kufungwa gerezani kama angeshindwa kulipa pesa za Patrick.

Kwa hakika maadui zake tayari walishafanikiwa kumporomosha. Akilia machozi aliamua kurudi nyumbani kutafuta pesa za kumlipa Patrick.


Aliteremka uwanja wa ndege wa Ottawa saa kumi na mbili jioni na kuchukua teksi.

“Nipeleke Carvin Avenue!”

“Sawa mzee!”

Gari liliondoka uwanja wa ndege kwa kasi na kadri lilivyozidi kuyakaribia maeneo ya nyumbani kwake Manjit alizidi kusikia kelele za ving’ora vya magari ya zimamoto! Awali alifikiri yalikuwa ni mambo ya kawaida katika jiji hilo lenye watu na pilikapilika nyingi za maisha, lakini hatua chache kabla ya kufika nyumbani kwake alishangaa kuona moshi mkubwa angani, alipoingalia nyumba yake hakuiona ilikuwa katikati ya moshi. Moto mkubwa ulikuwa ukiiteketeza, zimamoto walikuwa wakijitahidi kuzima lakini walishindwa.

Hakufikiria kitu kingine chochote, mawazo yake yalimpeleka kwa mama yake mzazi pamoja na Victoria aliowaacha ndani ya nyumba yake! Kwa haraka aliruka garini na kuanza kukimbia mbio kuelekea kwenye moto huo mkubwa huku akiliita jina la mama yake! Aliona ni heri kufa kuliko kupambana na matatizo yaliyokuwa yakimfuata, mbele kidogo alisita na kusimama, woga wa kuungua na moto ulimwingia.

Kwa hakika dunia ilikuwa imemgeuka! Deni la mafuta alilokuwa akidaiwa hakuwa na uwezo wa kulilipa na bado nyumba yake ilikuwa ikiwaka moto na hakuwa na uhakika kama mama yake pamoja na Victoria walikuwa hai au walikuwa wakiteketea ndani ya moto huo.

Kwa jinsi umati mkubwa wa watu ulivyokusanyika hakuna mtu aliyegundua kuwa Manjit alikuwepo eneo la tukio, akiwa amesimama wima huku akitetemeka alisikia sauti ya mama yake ikiliita jina lake kutoka katikati ya moshi mkubwa uliotanda eneo hilo, hiyo ilimaanisha mama yake alikuwa bado amekwama ndani ya nyumba iliyokuwa ikiwaka moto!

Moyo wake ulimuuma kupita kiasi na kujikuta akipata ushujaa wa ajabu na kuanza kukimbia mbio kuelekea ndani ya nyumba iliyokuwa ikiwaka moto bila woga kama ilivyokuwa awali.

Manjit alijua yaliyotokea yote yalikuwa ni hujuma lakini hakujua ni nani aliyemfanyia hujuma hiyo mbaya.

Watu waliokuwa eneo hilo walimwona mtu akikimbia kuingia ndani ya moto, kitendo hicho kiliwashangaza sana na kujikuta wakijaribu kukimbia kwa nyuma wakimfuata kwa lengo la kumuokoa lakini tayari Manjit alishapotelea ndani ya moshi mkubwa uliokuwa umetanda! Walijua naye anakwenda kuteketea.

“Huyu sijui mjinga? Sasa kwanini ameingia ndani ya nyumba inayowaka moto kiasi hiki?” Walijiuliza baada ya kushindwa kumpata.

ITAENDELEA

Dimbwi la Damu Sehemu ya Tano

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment