Noti Bandia Sehemu ya Tatu
KIJASUSI

Ep 03: Noti Bandia

SIMULIZI Noti Bandia
Noti Bandia Sehemu ya Tatu

IMEANDIKWA NA: BEN R. MTOBWA

*********************************************************************************

Simulizi: Noti Bandia

Sehemu ya Tatu (3)

Ndio kwanza nilikuwa nimeamka kutoka usingizini, kuchelewa kwangu kuamka si kwamba mimi ni mtu mvivu, la hasha, hali hii ilitokana na mimi kuchelewa kulala usiku kutokana na kazi nilizofanya. Kama wewe ni binadamu mwenye huruma, utaona ni jinsi gani mimi nilistahiri kulala mpaka muda huu.

Ilinilazimu kulala KB Hoteli iliyoko Mabibo ili asubuhi niweze kuonana na shemeji yangu Mama Feka, ambaye pia alifikia katika hoteli hii. Kilichonitoa usingizini ni kelele ya mwito wa simu iliyopigwa na Peter TWite, Vinginevyo ningeendelea kuuchapa usingizi, nilijivuta taratibu na kupokea simu.

“Jambo Mkuu”, sauti ya Peter ilipenya masikioni mwangu.

“Oh Peter, Jambo. Habari ya asubuhi”.

“Habari nzuri mkuu, nakujulisha kazi uliyonituma, vijana wako kwenye pointi kama ulivyoshauri, kuwatambua kila mmoja amevaa fulana na kofia nyeusi za NSSF. Ili kuepusha usumbufu, nimewajulisha wavae kofia ziangalie nyuma, maana anaweza kutokea mtu mwingine amevaa vile ikawa shida”, Peter alieleza.

“Asante Peter, kama nilivyokufahamisha, usishughulike na jambo lolote mpaka nitakapokujulisha, usizime simu, usiwe mbali na eneo lako, kuna kazi moja itabidi uifanye majira ya saa tisa alasiri hivi. Usiniangushe”, nilisisitiza.

“Siwezi, siwezi kabisa kukuangusha mkuu. Utakapokuwa tayari kunituma kazi yoyote utanifahamisha, nafahamu wakati tuliomo bosi, niamini tafadhali”.

“Usijali Peter, wewe endelea mpaka nitakapokujulisha vinginevyo”.

“Tuko pamoja”.

Niliwasiliana na Luteni Fred Libaba nikamjulisha mahali nilipokuwa, niliagiza awachukue Luteni Claud Mwita na Sajenti Julius Nyawamiza, awalete KB Hoteli chumba namba kumi, floo ya pili. Nikamjulisha kuwa wakifika wanipigie simu. Ningia maliwatoni, nikafanya usafi wa mwili wangu, nilikoga, nikanyoa ndevu na kujiweka vizuri, halafu nikashuka chini kwa ajili ya kifungua kinywa.

Sebastian alikuwa mmoja wa rafiki zangu, kazi yake ilikuwa dereva taksi, alifanya kazi zake sehemu mbalimbali za Jiji la Dar es Salaam. Kijana huyu ndiye aliyenileta hapa usiku, nikamfahamisha pia anifuate saa mbili asubuhi na tayari alikuwa amefika kunichua.

“Umelala saa ngapi Seba?”, nilimuuliza.

“Hizi kazi zetu hatuna muda wa kulala, dereva taksi halali kaka, unaposubiri wateja, ndiyo nafasi ya kulala hiyo”, alieleza Sebastian.

“Nitakuwa na wageni, nahitaji kutumia gari yako kwa shughuli zangu binafsi. itakuwa siku ya leo na kesho, nitakulipa”, nilimwambia.

“Hakuna shaka kaka, funguo za gari hizi hapa, ukimaliza mambo yako utanijulisha, iwe siku mbili, wiki au mwezi”.

Baada ya kupata kifungua kinywa, nilisimama, wakati najiandaa kurejea chumbani kwangu, Fred, Claud na Nyawaminza waliingia.

“We Fred, ina maana mlikuwa karibu sana?”, nilimuuliza.

“Hata sisi tumelala Mabibo, niliwaambia wenzangu, Teacher asipolala Sinza, basi atalala Mabibo, utabiri wangu umekuwa sahihi”, alieleza Fred.

Tulipanda ngazi tukaingia chumba namba kumi, “Karibuni, baada ya kutoka nyumbani kwa Carlos usiku, niliona vyema kulala hapa. shemeji yangu Mama Feka yuko chumba namba nane, kwa kuwa tumekutana wote hapa, ngoja nimwite aje mbele yenu, itakuwa vizuri mkimfahamu”, niliwaeleza wote wakatingisha vichwa kukubaliana nami.

Nilisimama kwa sekunde kadhaa nje ya mlango wa chumba namba nane, nilijiuliza maswali kadhaa, ambayo majibu yake yalielekea kunishinda. Nilijiuliza kuhusu kazi ninayotaka kumtuma mwana mama huyu, ni sahihi au namuingia katika matatizo. Hata hivyo nilipiga moyo kinde, nikagonga mlango, akaniruhusu kuingia. Mama Feka alikuwa amevaa kaptula na fulana, zilizomfanya apendeze sana.

Jasho jingi lilikuwa likimtoka mwilini kwa sababu ya mazoezi, aliponiona akasitisha mazoezi na kunisalimia, “Sema shem wangu, umelala salama?”.

“Niko salama kabisa shem, ama kweli wewe ndiye Cnthia Rothrock wa ukweli, nimelala hapa chumba namba kumi, niko na wenzangu, wanahitaji kukuona, ukimaliza mazoezi yako, njoo room namba kumi tuzungumze kidogo”, nilimwambia.

“Dakika moja”, alisema Mama Feka nikatoka nje na kumwacha akijiandae. Maana vitu vingine vya shemeji sina ruhusa ya kuviona.

“Tumsubiri kidogo, anakuja, alikuwa katika mambo ya kujiweka sawa kiafya”, niliwajulisha wenzangu, waliokuwa kimya, wakainua vichwa vyao juu kuonyesha ishara kuwa wamenielewa.

Wakati tunamsubiri Mama Feka, niliona ni vyema nitumie nafasi hii kuwaeleza habari ya usiku. “Fred, niliwahi kukwambia siku zote usiamini maneno ya mtu, wakati tunamsubiri Mama Feka, labda nitumie nafasi hii kukujulisha kuwa Carlos Dimera si binadamu wa kawaida, ni aina ya mnyama tena hatari zaidi ya chui”, akanitolea macho na kunishangaa.

“Ehee, imekuwaje bosi, maana kiasi fulani umenishitua?”, alihoji Fred kwa shauku kubwa.

“Sikiliza Fred, huyu mzungu rafiki yako, au sijui ni nani kwako, anamiliki kikosi kikubwa cha uhalifu hapa jijini, sasa nakwambia tukifanya mchezo tumekwisha, take care”, nilimwambia.

“Si rafiki yangu kabisa, kumbuka nilikwambia habari za huyu mzungu nilielezwa na rafiki yangu mmoja wa polisi, binafsi sijawahi hata kukutanishwa nae”, alijitetea.

“Basi elewa hivyo, mimi nilimtilia shaka mapema kabisa, ndiyo maana nimejiridhisha baada ya kufika nyumbani kwake usiku. Huyu mzungu ndiye chanzo cha mambo yote ya uhalifu hapa jijini, sasa nasema ama zake ama zangu, amejiandaa vizuri sana, lakini sisi pia tuko vizuri, au vipi jamani?”, niliwauliza wenzangu huku wote wakiniunga mkono.

“Sasa ajiandae kukutana na mkono wa sheria, watu kama hawa siku zao ni arobaini, mwisho wake umetimia, kama ulivyosema, ama zake ama zetu, naamini tutashinda”, Julius Nyawaminza alieleza kwa hasira.

Niliwaeleza kila jambo, jinsi nilivyoingia nyumbani kwa Carlos Dimera, hali ya ulinzi ilivyokuwa na mipango yao ya uhalifu waliyokuwa wakipanga. “Walikuwa katika sherehe, eti wakisherehekea kifo changu, cha ajabu hawakuweka ulinzi wa aina kabisa, wameamini nimekufa, siku wakiniona watatamani ardhi ipasuke”.

“Kama ndivyo kwanini tusiwakamate mapema ili kuokoa muda?”, Claud alihoji na kuongeza, “Maana kila kitu kiko wazi, sasa sijui tunasubiri nini mkuu?”.

“Ni kweli kabisa Claud, kama inawezekana wakamatwe wakati ni huu sasa”, Nyawaminza alirukia kuunga mkono maneno ya Claud.

“Hapana, tusikurupuke kufanya jambo ambalo halina tija kwa taifa. Sikilizeni, ingekuwa kazi ni kuwakamata tu, ningewaita hata usiku tukawamata kama kuku, lakini tutakuwa tumefanya kazi ya bure, lazima muelewe kuwa nchi yetu inatawaliwa kwa mjibu wa sheria, huwezi kumtia mtu hatiani bila kuwa na ushahidi. Fred… unadhani inawezekana, haya sawa, tutamfikisha mahakamani kwa kosa lipi?”, niliwauliza.

“Hakika bosi, itakuwa vigumu kumkamata mtu bila ushahidi, nashauri tufanye kila njia wakamatwe na ushahidi”, alishauri Fred, wote tukamuunga mkono.

“Leo tutafanya kazi moja ndogo, lakini yenye faida kubwa kwetu. Fred jiandae tutakwenda kumkamata mtu mmoja anaitwa Raymond Kenoko, huyu jamaa ni Afisa wa Uwanja wa ndege, Claud na Nyawaminza nitawaelekeza cha kufanya, halafu…”, kabla sijaendelea mlango uligongwa, Mama Feka akaingia.

“Habarini za asubuhi”, Mama Feka alisalimia.

“Oh, nzuri, nzuri”, tulimwitikia kwa pamoja. suluali ya blue na fulana ya njano, alizovaa zilimfanya apendeze sana, aliingia na kusimama mfano wa mtu anayesubiri kupandishwa kizimbani.

“Pole na safari shem wangu, pole kwa kukukatisha usingizi wako, pole kwa kila nililokukosesha kulifanya asubuhi ya siku ya leo”, nilimuomba radhi.

“Usijali shem”, Mama Feka alisema kwa mkato huku akitabasamu.

“Jamani, huyu mwana mama ni shemeji yangu kabisa, ametoka Nyamuswa kwa ajili ya kushiriki mahafari ya chuo kikuu huria, lakini kabla hajafika huko chuoni nikamuomba aonane na sisi kwa ajili ya mambo fulani fulani ambayo tutamuomba atusaidie”, niliwaeleza wenzangu wakatingisha vichwa.

“Kazi gani tena shem? Mbona unanitisha jamani”.

“Usiogope molamu, labda nieleze moja kwa moja utanielewa”. Nilitumia nafasi hiyo kuwatambulisha wenzangu kwake ili awafahamu, halafu niliendelea. “Hapa jijini limeibuka kundi moja hatari la wafanyabiashara wa dawa za kulevya, hawa jamaa ndiyo wanauzia watu madini feki kama umewahi kusikia, wanateka watu na kuwapora mali zao mchana na usiku, wanaibia watu kwa mtindo wa noti au dolla bandia, mji umechafuka kwa ajili yao, sasa sisi hatukubaliani nao”, nilimwambia.

“Umenikumbusha mbali, mwanangu aliwahi kuibiwa kwa mtindo wa madini feki, wakachukua ada yote ya shule, hao watu ni wauaji kabisa”, alieleza Mama Feka.

“Pole, sasa kinara wao yuko hapa ni mzungu, huyu mzungu ndiye anafadhili mambo haya, lakini kumkamata imekuwa ngumu kidogo”, nilieleza.

“Kuna ugumu gani shem?, mtu kama huyo si anakamatwa tu jamani, mwanangu alilia sana siku hiyo, alikuja na chupa akidai ameuziwa madini, iliniuma sana jamani, kwa hiyo ulitaka nieleze ilivyokuwa?”, aliuliza.

“Hapana shem, kuna jambo moja la msingi sana ambalo tumelijadili na wenzangu kwa muda mrefu, baada ya kutafajari kwa kina, tukaishia kukuchagua wewe utusaidie kufuatilia mambo fulani, ambayo yatatuwezesha kumtia hatia mtu huyo”, nilimwambia akacheka.

“Ehe, mnataka mimi nifanye nini?”, alihoji.

“Tunataka tukutume ujiingize upande wake iwe rahisi kwetu kumkamata na ushahidi, unasemaje shem?”, nilimuuliza.

“Heeee, shem hivi inawezekana mtu akajipeleka mwenyewe jehanam, si hatari hiyo, kwanza mimi nimekuja Dar kwa kazi nyingine, aaah itakuwa ngumu, hivi nitaanzaje kujiingiza huko?”, alilalama Mama Feka huku akisimama.

Nilishika kichwa, nikainamisha uso wangu chini, nilianza kutafakari hili na lile nikitafuta majibu lakini nikakosa. Wenzangu, Claud Mwita, Julius Nyawaminza na Fred Libaba nao walikuwa kimya wakiniangalia.

“Keti tafadhali shem”. Nilitumia nafasi hiyo kumweleza mambo mengi yanayoweza kumfanya binadamu akaonekana shujaa kwa watu, nilimuomba arejee alipokuwa ameketi. Nikasimama, nilitembea kutoka kona moja ya chumba hiki kwenda upande mwingine.

“Samahani shem, si kusudio langu kukuingiza kwenye moto, kukutuma ujiingize upande ule si kwamba tutakuacha tu, tutakuwekea ulinzi wa hali ya juu, tutakufuatilia wakati wote, kuhusu usalama wako ondoa shaka”, nilieleza.

“Sawa, lakini nitaanzaje kujiingiza upande wao, kwanza wataniamini vipi?”.

“Tunataka kujaribu kitu kimoja, tumepata taarifa kuwa huyu mzungu Carlos Dimera, anapenda sana wasichana wazuri, kila anapowaona hupagawa, ndiyo maana nikasema kwako itakuwa rahisi atanasa, na akinasa hatutakuacha tu, tutakufuatilia kila hatua utakayokuwa”, nilimwambia.

“Mmmm, sasa naanza kukuelewa, unataka nitumie mbinu zangu huyo mzungu Carlos anipende au sivyo?”.

“Ndivyo tunavyotaka”, Nyawaminza aliyekuwa kimya kwa muda mrefu akitafakari aliongeza.

“Majaribu haya, sina jinsi, niko tayari kuwasaidia sasa natakiwa kufanya nini?”.

“Tutakuwezesha kwa pesa na mavazi. Tumepata ratiba kuwa huyu mzungu kila siku lazima afike Msasani Shopaz Plaza kwa ajili ya kununua vitu vidogovidogo vya kula, halafu huenda Seaclif Hoteli, akitoka hapo, hujirusha kwenye muziki, California Dreema. Shem, hakikisha wewe pia unapatikana maeneo hayo, akikuona tu atakushobokea, lakini uwe mwangalifu sana”, nilimuasa.

“Kazi hiyo niachie mimi, nawahakikishia huyu mzungu kwangu atanasa, chezea Cnthia wewe, niko tayari kuanza kazi hiyo”, alisema Mama Feka hofu ikiwa imemtoka.

Niliwasiliana na Peter Twite kumjulisha hatua tuliyokuwa, nilitumia nafasi hiyo kumwelekeza ratiba ya kazi atakapokuwa na Mama Feka. Tulimpangia kazi ya kumpeleka sehemu alizopangiwa, yaani Shopaz Plaza, Seaclif Hoteli na California Dreema.

Wakati vyombo vya ulinzi na usalama nchini vikifuatilia kwa makini na karibu matukio ya kutisha ya uhalifu yaliyokuwa yakiendelea Jijini Dar es Salaam. Watu kadhaa walifika vituo vya polisi kutoa maelezo ya jinsi walivyo tapeliwa.

Mfanyabiashara John Roman, afika Kituo Kikuu cha Polisi, Sokoine Drive, baada ya kuibiwa kwa njia ya mtandao, Shaaban Ismail, baada ya kubaini kuwa ameibiwa, alifika haraka kituo cha polisi Oysterbay, ambapo maofisa wa polisi walichukua maelezo yak.

John Roman ni mmiliki wa klabu ya ‘Toroka Uje’ ambaye aliibiwa pesa nyingi kwa njia ya mtandao. Alifika polisi akionyesha namba za simu za nje zilizotumika kuwasiliana nae na kumfanya atume pesa nyingi, akiwaomba polisi watumie uwezo kuzifuatilia namba hizo.

Akihojiwa na polisi wa zamu waliokuwa kituoni hapo, John Roman alieleza kuwa, awali alipokea ujumbe kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika ADB, ukimweleza kuwa ameteuliwa kuwa mrithi wa Hayati John Bryson wa Uingereza, aliyekuwa na akaunti katika benki hiyo, lakini alifariki dunia na kuacha pesa nyingi..

Maelezo ya John Roman yalimshawishi Afisa wa Polisi kumhamishia chumba maalumu cha mahojiano, afisa huyo alifanya hivyo baada ya kuvutiwa na taarifa hiyo. Alipoingia ndani ya chumba hicho, askari huyo alimtaka bwana John Roman kulielezea vizuri kuhusu tukio hilo.

“Nimekuleta katika chumba hiki ili tuweze kuzungumza kwa uwazi zaidi, tukio hili ni moja ya matukio ya uhalifu yanayotokea karibu kila siku, naomba uanze kueleza toka mwanzo wa tukio hili mpaka sasa, usifiche kitu na usione aibu. Eleza mpaka ulivyofika hapa”, Inspekta Judicate alieleza, akijiweka sawa kuandika maelezo yake.

“Ni hadithi ndefu Afande, lakini nitahitahidi kueleza kama ilivyo, naamini polisi mba mbinu zetu ambazo zitasaidia kuwakamata watu hawa. Maana kichwa changu hakifanyi kazi vizuri, nimevurugwa”, John Roman alieleza.

“Usijali, maji yakimwagika hayazoleki, lakini maelezo yako yataisaidia polisi katika upelelezi wa tukio hili, cha msingi usifiche jambo”, Inspekta Judicate alimhakikishia.

“Asante sana Afande, nakumbuka siku tatu zilizopita nilipokea ujumbe kupitia email yangu, ukiuliza kama mimi ndiye John Roman raia wa Tanzania Bara, nilipojibu ndiyo, nilipokea ujumbe mwingine ukiniuliza nahusika na biashara gani, nilipojibu kuwa namiliki klabu. Hawakutuma ujumbe tena, isipokuwa walinipigia simu wakitumia namba za nje ya nchi”, alinyamaza kidogo ili kumeza mate, baada ya kutafakari aliendelea.

“Afande, watu hawa ni wajuzi wa hali ya juu, aliyenipigia simu alijitambulisha kwa majina ya Roggers Peter, akidai kuwa ndiye Mtendaji Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ambayo Makao Makuu yake ni Ouagadougou nchini Bukinafaso, Afisa huyu alinieleza kuwa benki imenichagua mimi kuwa mrithi wa mali za marehemu John Bryson, raia wa Uingereza aliyekuwa na pesa nyingi katika benki hiyo, nilipohoji inakuwaje niteuliwe kuwa mrithi wa mali za mtu nisiyemjua, Afisa huyo alinieleza kuwa huo ni mpango wa siri wa benki na kwamba watanitumia nyaraka mbalimbali za marehemu John Bryson, ikiwa pamoja na hati ya kifo ili nizitumie kupokea pesa hizo kama urithi alioniachia. Lakini akaniasa kuwa mwaminifu, akidai kuwa kuna dola milioni sita za kimarekani ambazo zitaletwa Tanzania kwa jina langu, nitazipokea uwanja wa ndege, halafu tutagawana”, alieleza.

Inspekta Judicate aliyekuwa akiandika maelezo hayo kwa haraka na kwa umakini, aliuliza “Kumbe Makao Makuu ya Benki hii yako Bukinafaso?”

“Hata mimi ndiyo nafahamu hivyo, maana sikuwa na uhakika”.

“Oke. Kwa jinsi inavyoelekea ni kweli watu hawa ni wajuzi katika kutenda uhalifu, ehee, ikatokea nini sasa?”.

“Nilishawishika kwenda kwenye mtandao, kama unavyojua dunia sasa ni kijiji, sikuchelewa nikaandika neno Mtendaji Mkuu wa ADB, likatokea jina la Roggers Peter, nikaanza kuyaamini maneno ya mtu huyo, baada ya muda nikapokea taarifa na nyaraka mbalimbali za marehemu John Bryson, ikiwa pamoja na hati ya kifo, ikieleza kuwa alifia nchini Uingereza na kuzikwa huko”, alinyamaza kidogo kupisha kama kuna swali.

“Hizo nyaraka ulizipokea kwa njia gani?”, Inspekta Judicate alihoji.

“Documenti zote za tukio hili zilitumwa kwa njia ya mtandao, na kweli zilikuwa zinaendana na tukio lenyewe, ilifika wakati nikaanza kuwaamini, mimi ni mtu makini sana lakini sijui nilipatwa na jinamizi gani?”, alieleza John Roman huku akitoa nyaraka hizo na kuzikabidhi kwa Inspekta Judicate.

Inspekta Judicate alizipitia documenti hizo moja baada ya nyingine, akiziangalia kwa makini, halafu akaziweka kando.

“Ehee, nini kikatokea sasa, maana unanieleza hadithi ambayo hakika ni tamu masikioni mwangu, endelea?”.

“Jana asubuhi, nilijulishwa kuwa benki imewatuma maofisa wake wawaili, Mohamed Mussa na Seif Mtigino kusafirisha pesa hizo hadi Dar es Salaam, nilitakiwa kufika uwanja wa ndege saa sita mchana kwa ajili ya kupokea pesa hizo. Kwa kuwa pesa zina mambo mengi, nilimuomba Afisa wa Jeshi la Ulinzi, Kapteni Masey anisimamie kupokea pesa hizo, lakini alinikatalia, akidai kuwa huo ulikuwa utapeli, kiasi fulani nilimlaumu, lakini sasa nimeamini kuwa alikuwa na nia njema”, alieleza John Roman.

“Afisa huyo wa Jeshi hakukueleza chochote zaidi ya kusema uache ni utapeli, kama wewe mwenyewe ulivyosema hapa?”.

“Afisa huyo yeye alikataa tu, akidai kuwa hao ni matapeli na kwamba hawezi kupoteza muda wake kunipeleka kwa matapeli eti nikatapeliwe, lakini pia alinisihi niachane na mpango huo, lakini sikumwelewa, ndiyo nazinduka usingizini sasa baada ya kuwa tayari nimeibiwa, tena nakumbuka alinieleza kuwa Benki ya Maendeleo ya Afrika ni kwa ajili ya maendeleo ya nchi za Afrika tu, haiwasiliani na mtu mmoja mmoja, pia alieleza kushangazwa na mtindo wa kusafirisha pesa hizo kuja Tanzania, ningemsikiliza hakika nisingekutwa na jambo hili”, alieleza machozi yakimtoka.

Inspekta Judicate alikuna kichwa cheke, huku kalamu yake ikiwa mdomoni kwa mshangao, alimwangalia John Romani kwa macho makali. “Kumbe ulipewa darasa la kutosha na bado ukaendeleza ujinga wako, aisee wewe ni kichwa maji kweli, lazima ufahamu kuwa maofisa wa Jeshi wana mbinu nyingi, kama alivyokushauri ungemsikiliza, au ungetoa taarifa kituo chochote cha polisi”.

“Ni kweli, hata mimi najiuliza sasa, sijui niliingiwa na tamaa au shetani gani, maana wakati wote mimi ni mtu makini sana”, alieleza John Roman.

“Wewe si mtu makini, ungekuwa makini usingekaidi ushauri wa Afisa wa Jeshi”, Inspekta Judicate alieleza kwa sauti ya kukatisha tamaa. Alimwangalia John Roman kwa macho yake makali, macho ya mwanamke Afisa wa polisi, aliyewiva katika utendaji kazi wake.

“Ni kweli Afande, unajua linapotokea jambo kama hili ndiyo mtu unajifunza, kwa kuwa limetokea sina jinsi kujifunza”. alieleza John Roman kwa unyenyekevu.

“Ehee, kwa hiyo hizo dola ndiyo zikaletwa Dar es Salaam au ilitokea nini tena?”, alihoji Inspekta Judicate kwa shauku.

“Ilipofika saa tano jana, nilipokea simu nyingine kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kwa majina ya Mohamed Mussa, akadai kuwa yeye Afisa kutoka ADB, akanijulisha kuwa ndege iliyokuwa ikitoka Bukinafaso kuelekea Dar es Salaam, Nchini Tanzania imepata hitlafu ikiwa angani na kutua kwa dharura katika uwanja wa ndege wa Entebe, Nchini Uganda, hivyo, akashauri nitume haraka dola elfu ishirini za Marekani ili waweze kuondoka Entebe kuja Dar es Salaam, wakidai kuwa visa zao zikiisha kabla ya kufika Dar es Salaam, itabidi warudi tena Bukinafaso, jambo ambalo wao binafsi hawapendi litokee”.

“Ukatuma pesa hizo?”.

“Mdiyo, ikanilazimu kuwatumia hizo pesa”.

“Kwa nini hukuwaambia watumie pesa walizokuwa wakisafirisha kuleta Dar es Salaam. Maana kama ni pesa walikuwa nazo tena nyingi. Dola milioni sita ni pesa nyingi, ni zaidi ya shilingi bilioni kumi za Tanzania, inakuwaje utume pesa?”, Inspekta Judicate alihoji.

“Niliwashauri watumie pesa hizo walizokuwa wakisafirisha, lakini wakadai kuwa taratibu za Benki haziruhusu pesa hizo kufunguliwa mpaka zifike sehemu husika, nikawaeleza kuwa mimi ni mlengwa wa pesa hizo, naruhusu zitumike, lakini hawakunielewa, wakadai kuwa zikifunguliwa itakuwa vigumu kupokelewa na wakala wa Dar es Salaam, atakayethibitisha kama pesa hizo zimefika salama Tanzania, ikanilazimu kutuma kiasi hicho haraka iwezekanavyo”, alieleza.

“Mama yangu, baada ya kutuma pesa hizo ikatokea nini?”, Inspekta Judicate alihoji.

“Baada ya kutuma pesa hizo. Simu zao hazikupatikana, kuanzia ya aliyejiita Mtendaji Mkuu wa ADB, pamoja na maofisa wote waliohusika kunipigia simu, lakini pia nilipotoa taarifa kwa mamlaka zingine ili kuzuia pesa hizo zisichukuliwe, nilikuwa nimechelewa, hali halisi ndiyo hivyo Afande”, alieleza John Roman.

“Mmmm, iko kazi, maana inawezekana watu hawa wako hapa hapa Dar es Salaam, naamini pia wanakufahamu, ndiyo maana wakaweza kupata hata namba zako za simu na majina yako, ok, ngoja tujaribu jinsi ya kukusaidia, pia taarifa hii tutaipeleka kwa wenzatu wa usalama ili nao waifanyie kazi”, Inspekta Judicate alieleza huku akisimama.

“Nitashukru”, John Roman nae alisema huku akimshika mkono wa wakaagana.

Wakati huo, Mama Feka alikuwa amewasili kwenye maegesho ya magari ya Msasani Shopaz Plaza, alifika eneo hili mapema kwa ajili ya kazi moja, kumshawishi Carlos Dimera ampende. Alikuwa ameketi ndani ya gari aina ya Ford Pick Up yenye rangi ya kijani, ambayo vioo vyake vilikuwa vyeusi, hivyo si rahisi kuonekana kwa mtu anayepita nje.

Aliketi kwenye viti vya nyuma vya gari hii Doble Cabine, huku wakiteta mawili matatu na Peter Twite, aliyemleta hapa. “Cha msingi uwe makini sana na watu hawa, naamini Teacher hawezi kumtuma mtu asiyemwamini, amekuamini ndiyo maana amekutuma katika kazi hii”, Peter Twite alimwambia Mama Feka.

“Nitajitahidi sana, naamini siwezi kuwaangusha, sijui kitokee nini, lakini nitajitahidi kupambana, najiamini”, Mama Feka alimwambia Peter. Alichukua picha ya Carlos Dimera iliyokuwa kwenye mkoba wake, akaingalia kwa mara ya mwisho, halafu akairejesha mahali ilipokuwa.

“Baadaye”, Mama Feka aliaga.

“Kila la heri, usiogope, maana kila utakapokuwa tutakuwepo pia”, Peter alieleza, Mama Feka akashuka kwenye gari na kuingia upande wa Supermaket hii kubwa iliyoko Barabara ya Kawe, Dar es Salaam.

Dakika kadhaa baadaye, Carlos Dimera aliwasili eneo hilo, akifuatana na mpambe wake, Jackna, walipoukaribia mlango wa kuingilia ndani, Jackna alikimbia na kuufungua mlango huo, ili Dimera aweze kupita. kama ilivyo kawaida yao, Walipoingia ndani haraka Jackna, alianza kusukuma tololi, akiwa nyuma ya bosi wake, ambaye wakati huo alikuwa akichagua vitu kadhaa anavyopenda kununua katika Supermaket hii.

Mama Feka aliyekuwa upande huo, akitafuta jinsi ya kuwasiliana na watu hawa, alibeba kikapu mkononi, akasogea mpaka kwenye pembe ya mwisho ya Supermaket, mapigo ya moyo yakamwenda mbio, akajiuliza mawili matatu, akapata jibu. Haraka akazunguka upande wa pili, alipofika sehemu ya makutano, hakuchelewa, akamgonga Jackina kama bahati mbaya, vifaa vyake zikamwagika chini.

“Vipi wewe kaka unatembea kama kipofu?”, Mama Feka alihoji.

Jackina alihamaki, haraka akainua mkono wake juu ili aushushe katika mashavu ya Mama Feka, lakini Carlos Dimera alikuwa mwepesi akaudaka mkono wa Jackina na kumzuia.

“Jackina, acha bwana, usipende kuwapiga watoto wazuri kama huyu, Mungu aliwaumba ili waupendezeshe ulimwengu”, Carlos Dimera alisema huku akitembea taratibu kuelekea kwa Mama Feka. “Pole sana, usijali kwa lililotokea”, hakafu akamgeukia Jackina, “Haraka okota vitu vyake, nitamlipia bili”. Jackina aliinama na kuokota vitu vilivyokuwa vimemwagika na kuvirejesha katika kikapu.

“Utaongeza nini malkia ili nikulipie bili?”, Carlso Dimera alimuuliza Mama Feka aliyekuwa amesimama akiwaangalia kwa hasira.

Alichukua kikapu chake, akatembea hatua mbili, halafua akawageukia na kusema, “Sikiliza kaka, mimi sibabaiki na rangi yako, kwetu si masikini kama unavyodhani, sina shida ya kulipiwa bili, tunajiweza ndiyo maana nikaja hapa, kaa na pesa zako, lakini pia mwambie huyu bwege wako avae miwani ili siku nyingine aweze kuona”.

“Shika adabu yako we malaya”, Jackina alifoka.

“Malaya ni wewe unayetembea kama kipofu”,

“Nyamaza Jackina, mbona hunielewi, usipende kugombana na wasichana”, Carlos alimtuliza Jackina huku Mama Feka akiondoka. “Ni msichana mzuri sana”, aliongeza Carlos.

“Lakini, anaonekana kuwa hana adabu bosi”.

Kama ilivyo kawaida yake, Carlos Dimera, aliwasili katika Hoteli ya Seaclif, ambako hukutana na wageni kutoka nje ya nchi, ambao hufika nchini kwa ajili ya biashara haramu ya dawa za kulevya. Mara hii alifika hapa ili kuonana na mtu maarufu sana duniani, mtu ambaye vyombo vya habari vya dunia humtaja karibu kila siku.

Hakuwa mwingine, huyu ni Emilio, mtoto wa Pablo Escoba, aliyekuwa mwanasiasa, mbabe wa dawa za kulevya, raia wa Colombia ambaye historia inaonyesha hakuwa na mfano. Kijana huyu Emilio, alikuwa amewasili nchini kwa ajili ya kuonana na Carlos Dimera. Alimtambua Carlos kama mtu wa karibu, kutokana na historia zao.

Mtoto huyu wa mbabe wa dawa za kulevya, ambaye baba yake alitoka katika familia ya mwalimu na mkulima, aliambatana na msichana mrembo, Serina Wilson.

Jakna hakuruhusiwa kusikiliza mazungumzo ya Carlos na mgeni wake Emilio, hivyo aliketi katika meza nyingine karibu akisubiri. Wakati wote Carlos alikuwa hafanyi kosa, alijua kufanya kosa moja kunaweza kumgharimu. Aliwatumia hawa kupokea na kusambaza dawa, lakini mambo yake ya ndani, hakupenda kuwashirikisha kabisa.

“Karibu sana, hii ndiyo Tanzania”, Carlos alimwambia Emilio, wakasimama na kushikana mikono.

“Asante sana Carlos, vipi hali ya biashara hapa?”, Emilio alihoji.

“Tuko vizuri”, Carlos alijibu kwa mkato.

“Si kweli Carlos, nimelazimika kuja hapa, ili tuzungumze kwa kirefu kidogo, nini tatizo, haiwezekani mzigo ukwame Adis Ababa kwa muda mrefu kiasi hicho, halafu unasema uko vizuri?”, Emilio aliuliza.

“Kuhusu hilo tumelimaliza, ni kweli kulikuwa na tatizo kidogo kwa wenzetu wa uwanja wa ndege, lakini jambo hilo limekwisha, kila kitu kimekaa vizuri, mzigo unaweza kuwasili Dar es Salaam leo, kuhusu hilo, ondoa shaka, tumelimaliza”.

“Nini kilikwamisha huo mzigo kuingia hapa, kama ni pesa mnazo za kutosha, mnaweza kumnunua mtu yeyote, au unasemaje Carlos?”.

“Hilo halina ubishi, ilitokea tatizo ngazi za juu, huko serikalini, mtu mmoja alipewa cheo akajiona tayari amekuwa Mungu, akahamia uwanja wa ndege, baadhi ya watu wamekamatwa, lakini si wa upande wetu, hata hivyo pesa imefanya kazi yake, mtu huyo ameondolewa, mzigo unaingia leo, mamlaka zote zina taarifa kuhusu mzigo huo kuingia”, Carlos alieleza.

“Nilitaka kujua hivyo, haiwezekani nchi ndogo kama Tanzania kuwe na usumbufu wakati wa kuingiza mzigo, wakati nchi kubwa kama Marekani, China, Japan na South Afrika mzigo unaingia haraka na bila shaka. Nimekuelewa Carlos, nitaondoka leo, hakikisha biashara yetu inashamili na kupata watumiaji wengi zaidi, huo ndio msimamo wetu”, alieleza Emilio huku akisimama kwa ajili ya kuaga na kuelekea kwenye helikopita iliyomleta eneo hili.

“Hatutalala, amini hivyo”, alidokeza Carlos huku wakipeana mikono ya kwaheri, akaaga na kuondoka, akiacha maswali mengi kwa Carlos. .

Baada ya Emilio kuondoka, Carlos alimwita Jakina.

“Tukiendelea kucheza ngoma za sindiba, tunaweza kupoteza kazi, unamfahami huyu jamaa?”, Carlos alimuuliza Jakina.

“Hapana”, Jakina alieleza.

“Huyu ni Mkurugenzi wa Shirika la Tuwezeshe, anatoka Marekani, alipenda kuonana na mimi kwa ajili ya mambo fulani, tukimaliza kazi hii salama, nitamuomba twende wote, yaani mimi na wewe tuishi Marekani, ukaishi huko Jakina”, Carlos alidanganya.

“Hakuna kitakachoharibika bosi, tumejipanga vizuri mno, naamini mzigo utaingia usiku huu, Hawa amefanya kila jambo, hakuna wa kuzuia”, Jakina alijinasibu.

Wakati huo, Mama Feka alikuwa ameketi upande wa pili kwenye kona akiwaangalia. Alipoona sasa ni wakati mwafaka, alitoka na kujipitisha mbele yao. Mama Feka alipita mbele ya meza waliyoketi Carlos na jakina, kama hajawaona vile akatafuta meza akaketi.

“Bosi, umemuona yule dada mshenzi wa Supermarket?”, Jakina alimuuliza Carlos.

“Na wewe husahau, kama alikukela msamehe, nenda mwambie aje aketi na sisi hapa”, Carlos aliagiza.

“Achana na huyo mshenzi, atatupotezea muda wetu, mbona wasichana wapo wengi tu bosi”, Jakina alieleza msimamo wake.

“Hapana, nimesema nenda mwambie aje hapa”.

“Mkorofi yule bosi”.

“Jakina, elewa kuwa si ombi, nasema nenda mwambie aje aketi na sisi hapa, ni wakati wa kumuomba msamaha kwa yaliyopita”, Carlos alieleza huku Jakina akisimama,

Huku mapigo yake ya moyo yakimwenda kasi, Jakina alitembea hadi mahali alipoketi Mama Feka. Aliona njia pekee ni utani, hivyo alimtokea kwa nyuma na kumshika bega.

“Helo, hujambo mrembo”, alisema Jakina huku Mama Feka akigeuka. Macho yao yalipokutana, Mama Feka akaonyesha mshangao wa uongo.

“Haaa, wewe ndiye yule kipofu wa Supermarket?”, Mama Feka alihoji.

“Hapana, ilikuwa bahati mbaya”.

“Ilikuwa bahati mbaya, mbona ulikusudia kunipiga?”.

“Ibilisi tu dadangu, bosi amenituma kwako”.

“Bosi amekutuma kwangu, anasemaje?”.

“Anaomba uhamie kwenye meza yake, tupate chakula pamoja”.

“Tupate chakula pamoja, nikikuita kipofu unachukia, hapa unaona nakula, halafu unasema tukapate chakula pamoja na bosi wako, mbona siwaelewi?”.

“Tunaweza kuhama na chakula chako, tafadhali niruhusu nikubebee chakula”, Jakina aliomba.

“Hapana, mwambie bosi wake sina muda huo”, Mama Feka alieleza.

“Sawa, lakini unapoteza bahati yako”, Jakina alimwambia.

“Acha ipotee”, Mama Feka alieleza kwa kujiamini.

Jakina alirejea kwenye meza ya Carlso.

“Yule msichana ni jeuri sana, anasema hana muda wa kuonana na wewe, nimemwambia anapoteza bahati amesema acha ipotee, anajiamini sana, yawezekana ni mtoto wa kigogo”, Jakina alieleza.

“Achana naye, iko siku atanasa”, Carlos alieleza, baada ya kupata vinywaji na chakula, Carlos na mpambe wake Jakina waliondoka. **

Niliendesha gari kwa mwendo wa kasi ili tuwahi kufika. Wakati huo nilikuwa nikiendesha gari aina ya Isuzu Troupe steshen wogan yenye rangi ya kijani, Fred alikaa kimya akiniangalia, bila shaka aliuhofia mwendo wangu. Tulipofika kwenye taa za kuongoza magari zilizoko katikati ya Barabara za Mandela na Uhuru, eneo la Buguruni, nilisimama ili kusubiri ruhusa ya taa hizi.

Kila mmoja alikaa kimya akitafakari nini hatma ya jukumu lililokuwa mbele yetu, magari yalipoanza kuondoka, niliongeza mafuta nikayapita baadhi ya magari yaliyokuwa mbele, tulipofika kwenye taa za Tazara, zinazoruhusu magari yanayotumia Barabara za Nyerere na Mandela, tulisimama tena hadi zilipoturuhusu kuendelea na safari.

Dereva wa gari lililokuwa mbele yetu alinionysha ishara ya taa, nikalipita gari hili kwa mwendo wa kasi, nadhani dereva huyu alitambua haraka tuliyokuwa nayo, akaamua atupishe. Ni madereva wachache sana barabarani wenye uelewa kama huyu, nilipiga honi ya asanye, nikaongeza mwendo.

“Uko vizuri”, nilimwambia Fred aliyekuwa kimya.

“Niko sawa”, alisema huku akiniangalia.

“Lolote laweza kutokea, lazima tukubaliane na hali hiyo”, nilimwambia Fred.

“Najua hivyo bosi, lolote laweza kutupata, lakini naamini kuwa tutashinda, wewe ukisimamia jambo sidhani kama linashindwa”, alinipamba.

“Ni kweli, lakini kila jambo na wakati wake”, nilisema wakati nikiingia kwenye maegesho ya magari ya Uwanja wa Ndege. Nilitafuta mahali pazuri nikaegesha gari.

“Fred… Hapa tumekuja kufanya kazi moja tu, kumkamata Afisa Ukaguzi, tukifanikiwa kumkamata huyu, kazi yetu itakuwa rahisi, vinginevyo itategemea kudra za Mwenyezi Mungu”.

“Atakamatwa tu”, Fred alisema kwa kujiamini.

“Sikiliza Fred, ingia ndani omba kuonana na Mr. Raymond Kenoko, ndiye Afisa Ukaguzi mwandamizi. Utakapomuona, mwambie kuna mgeni wake ndani ya gari, akifika hapa tumemaliza kazi”, nilimwambia Fred. Aliniangalia kwa sekunde kadhaa halafu akavuta shati na kutoa bastola yake ndogo, akaigagua.

“Iweke hapo kwenye droo ya gari, hapa si mahali pake”, niliagiza, akafungua droo ya gari akahifadhi silaha yake, akafungua mlango wa garu na kutoka taratibu kama ilivyo kawaida yake.

Kwa wasiomfahamu Fred, ni mmoja wa vijana watanashati, mtaratibu, hata vitendo vyake huvifanya taratibu, ukimuona ghafla unaweza kudhani ni mtu zoba, lakini ukihitaji undani wake, unaweza kuingia kwenye mto wenye mamba ili asikutie mikononi mwake.

Wakati nikimsubiri Fred, niliwasiliana na Kanali Emilly, kumuomba ajiweke tayari kuonana nasi wakati wowote kuanzia sasa. Niliwasiliana pia na Claud Mwita na Julius Nyawamiza kuwatahadharisha na hali ya sasa pia kuwaandaa kwa kazi.

Nikiwa ndani ya gari niliweza kuona kila mtu aliyekuwa karibu yangu, nikisaidiwa na aina ya vioo ya gari hii, kwani mtu akiwa ndani haonekani kabisa, lakini unaweza kumuona mtu wa nje kwa ufasaha zaidi. Mara Fred alifungua mlango akaingia.

“Huyu jamaa ametoka hapa dakika ishirini zilizopita, wanasema amekwenda kupata chakula pale Transt Motel, tumsubiri hapa au unasemaje bosi?”, Fred alihoji.

“Hapana, hapana twende haraka”, nilisema huku nikitoa shilingi elfu moja ili Fred akalipie ushuru wa maegeshi ya uwanja.

Haraka nikaliweka gari barabarani, nilipoona taa za Barabara ya Nyerere zitatuchelewesha kupita, niliamua kuliingiza gari huku madereva wa magari mengine wakitupigia honi, nikapenya na kuliegesha gari mbele ya Transt Motel, karibu kabisa na Reli ya kati.

Nilitoa picha ndogo ya Raymond Kenoko nikaiangalia kwa mara nyingine, haikuwa rahisi kumfahamu moja kwa moja hivyo ilitulazimu kutumia akili zaidi. Mara nikawaona watu wawili wakitoka ndani ya Transt Motel, walifanana urefu na maumbo yao, akili yangu ikacheza.

“Atakuwa mmoja kati ya hawa. Shuka muite kwa jina, atakayeitika ndiye”, nilimwambia Fred akafungua mlango na kuita, “Habari ya kazi Mr. Ray?”.

“Nzuri kaka, habari yako”, Raymond alisema huku akisogea ili kumshika Fred mkono, mwenzake alitembea hatua chache akasimama kumsubiri. Bahati nzuri alivaa kitambulisho chake shingoni, kikiwa na jina la RH Kenoko.

“Samahani kwa usumbufu, naitwa Jabir Idrisa, nimefika ofisini kwako nikaelezwa kuwa umetoka kwa ajili ya chakula, nikaona nikufuate, kwa ufupi ni kwamba nina mzigo umekwama, lakini nimeelezwa kuwa nikikuona waweza kunisaidia, sasa tunafanyaje kaka?”, Fred alidanganya.

“Nani kakutuma uje kwangu?” Alihoji kwa sauti nzito.

“Carlos”, Fred alidanganya.

“Ahaa, sawa sawa, ni mzigo tofauti na unaoingia leo?”, alihoji.

“Ndiyo, ni aina nyingine, labda tuingie ndani ya gari ili tuelekezane vizuri, uangalie uwezekano”.

“Hakuna shaka”, Raymond Kenono alisema huku akimuelekeza mwenzake atangulie ofisini. Fred alifungua mlango wa gari wakaingia.

“Mnanipeleka wapi jamani?”, Raymond Kenoko alihoji, wakati naingiza gari kwenye Barabara ya Nyerere kuelekea mjini, baada ya kuiacha barabara inayoingia Uwanja wa ndege.

“Uwe mpole kaka, sehemu ambayo utaweza kujibu maswali yetu vizuri”, nilimwambia kwa sauti ya ukali kidogo. Nilifungua droo ya gari nikatoa kitambulisho changu, nikamuonyesha.

“Nimekosa nini jamani?”, alihoji kwa sauti ya kukata tamaa huku mikono yake ikitetemeka.

“Sikiliza kaka, sisi ni watu wema kabisa, watumishi wenzio katika serikali, huna budi kutulia na usijaribu kufanya lolote ambalo linaweza kuyahatarisha maisha yako”, Fred alimwambia.

“Nimekuelewa kaka, sasa napaswa kufanya nini? kama kuna tatizo linahitaji ufafanuzi tuzungumze tu, dunia ya sasa hakuna siri, mnilinde jamani”, Raymond Kenoko alieleza.

“Sikiliza Mzee Ray, tunakuhitaji kwa mazungumzo ya dakika ishirini hivi, halafu tutakuacha utarudi kazini kwako, cha msingi ni ushirikiano, wewe unajua kwa nini tumekukamata, naamini hivyo”, nilimwambia.

“Hapana, hakika sijui lolote”, alisisitiza.

“Sawa, kama hujui tutakusaidia kujua, cha msingi ni wewe kuwa na ushirikiano”, Fred alisema.

Tulipofika kwenye makutano ya barabara za Nyerere na ile inayokwenda Vingunguti, tuliiacha barabara ya Nyerere, nikachepuka na kuingiza gari kwenye barabara ndogo ya dharura, inayopita kushoto, pembeni mwa barabara hii ya Nyerere, nikaliongeza gari mwendo.

“Mtanisaidiaje?”, alihoji.

“Kuhusu nini?”, Fred alimuuliza.

“Kuhusu kusaidiana ili tumalize jambo hili lisifike mbali, maana ukipuuzia upole, kitakuwa kidonda”, alibainisha.

“Ni kweli, lakini ni jambo gani wakati wewe umesema hujui kwa nini tumekukamata?”, nilimwambia.

“Kwa vyovyote vile kutakuwa na sababu, haiwezekani maofisa kama nyie mnikamate tu bila sababu, lazima ipo sababu ndiyo maana nikasema tuzungumze kirafiki, tusiharibiane kazi. Tusaidiane”, alijitetea.

Mara simu yangu ya kiganjani ikaita, Kanali Benny Emilly alitaka kujua tumefikia wapi, maana kabla hatujatoka uwanja wa ndege kuelekea Transt Motel nilimjulisha wapi atusubiri, nilimweleza kila kitu akatuelekeza mahali alipo.

Tulipofika kwenye ofisi za kiwanda cha sigara cha Master Mind, kilichoko kando ya barabara hii, geti la kuingia liliachwa wazi, hivyo niliingiza gari moja kwa moja. Kama unavyojua sheria inaturuhusu kutumia ofisi yoyote ya umma na binafsi mahali popote, wakati wowote kwa ajili ya usalama wa nchi. Kanali Emilly alikuwa amefika mapema sehemu hii na kuandaa ofisi ya muda, kwa ajili ya kazi hii.

Meja Iddi Satara, mmoja wa wasaidizi wa karibu wa Kanali Emiily alinionyesha ishara nikalisogeza gari mahali alipokuwa, wakati haya yanafanyika Raymond Kenoko alibaki ameduwaa asijue la kufanya.

“Mtanisaidiaje?”, alijitetea kwa mara nyingine.

“Amini tutakusaidia, twende kwanza uongee na mkubwa, cha msingi uwe mkweli, vinginevyo utaozea jela, haki ya Mungu”, nilimwambia wakati tunatoka ndani ya gari, tukaelekea kwenye ofisi ya Kanali Emilly ya muda.

Kanali Emilly aliketi mbele ya meza kubwa iliyozungukwa na viti kadhaa vya wageni, ilikuwa ofisi ya kuvutia sana, Meja Satara alimuonyesha Raymond sehemu ya kuketi, bila ajizi akaketi.

“Karibu bwana Raymond Kenoko, Afisa Mkaguzi Mwandamizi wa Uwanja wa ndege. Naitwa Kanali Benny Emilly, kwa ufupi mimi ndiye nimewatuma vijana wangu wakukamate, ili ufike mbele yangu ujibu maswali mawili matatu, halafu tunakuachia, kikubwa hapa ni ushirikiano, tusaidie tukusaidie, bila shaka umenielewa?”, Kanali Emilly alimwambia.

“Ndiyo baba, niko tayari kujibu maswali yako na kutoa ushirikiano unaotakiwa”, alijibu kwa hofu.

“Una muda gani sasa toka umepata ajira serikalini?”, Kanali Emilly alimuuliza.

“Miaka kama ishirini na sita hivi”, alijibu.

“Miaka kama ishirini na sita, unaonyesha kuwa huna hakika”, Kanali Emilly alihoji.

“Ni miaka ishirini na sita, hakika ni ishirini na sita sasa”, alisisitiza.

“Umeoa?”.

“Ndiyo baba, nimeoa”.

“Una watoto?”.

“Yes, nina watoto watatu”.

“Wazazi wako hai?”.

“Hapana, wote ni marehemu”.

“Una nyumba ndogo, namanisha mke mwingine?”.

Akaonekana kubabaika, baada ya kutafakari kwa sekunde kadhaa akasema, “Yupo rafiki wa kike, lakini hayuko karibu sana, unajua hali ya maisha sasa ni ngumu”.

Kanali Emilly aliendelea kumuuliza Raymond maswali mengi ambayo aliyajibu vizuri. Pamoja na maswali hayo ya kirafiki, akili ya Raymond ilikuwa katika dimbwi la mawazo, akijiuliza kimya kimya, hususan swali la Carlos. Fred alipomwita kwenye gari, alijitambulisha kama kijana wa Carlos, ndiyo maana akakubali kupanda gari, sasa alijiuliza kwanini watu hawa walimtaja Carlos lakini baadaye wakamkamata na kumweka chini ya ulinzi.

“Unamfahamu mwana mama mmoja anaitwa Hawa Msimbazi?”, Kanali Emilly alimuuliza Raymond.

“Hapana, simjui”.

“Humjui, na huyu mzungu anayeitwa Carlos?”, swali hili lilimchanganya kidogo, akaweweseka.

“Simjui pia”, alisema huku akitingisha kichwa chake kukataa kwa msisitizo.

“Unamjua”, nilirukia.

“Siwezi kusema kitu ambacho sikijui, haki ya Mungu simjui Hawa wala Carlos”, alisisitiza kwa mara nyingine.

Kanali Emilly alisimama, alitoka mahali alipokuwa ameketi akatembea hadi kwenye mgongo wa Raymond. Mzee huyu alikuwa na huruma kwa kila kiumbe kilichotengenezwa na Mungu, lakini pia alikuwa katili kwa viumbe vilivyokuwa hatari kwa maisha ya viumbe wengine. Alipenda kucheka sana, lakini pia alikuwa mwenye hasira sana.

“Unadhani sisi ni wapumbavu, unadhani hatuna kazi zingine za kufanya mpaka tukulete hapa, nilitegemea utakuwa muungwana, utajibu maswali yangu vizuri kama tulivyoanza, kumbe naongea na mpumbavu. Sikiliza, naomba ujibu swali langu. Unamfahamu Carlos Dimera”, Kanali Emilly alihoji kwa sauti ya kutisha.

Raymond aliinamisha uso wake chini, akabaki kimya. Kanali Emilly aliendelea kusimama nyuma yake, akisubiri jibu.

“Sikiliza, wewe ni raia wa Tanzania, tena mtumishi wa umma, Carlos ni mzungu, ametoka mbali sana, mpaka anafika hapa nchini, taarifa zake zote tunazo, mpaka anawasiliana na wewe kuhusu mzigo uliokwama Adis Ababa, Ethiopia tunajua, nashangaa kwanini unaficha jambo ambalo liko wazi kabisa”, nilimwambia.

“Mr Raymond, unakumbuka kabla hatujapanda gari uliniuliza swali gani, ulisema ni huu mzigo unaoingia leo au mzigo mwingine, sasa unaficha nini inaeleweka hivyo”, Fred alimwambia.

“Raymond, unataka usaidiwe au uishie jela?”, Kanali Emilly alimuuliza.

“Naomba nisaidiwe”, alisema huku machozi mengi yakimtoka.

“Tutakusaidiaje wakati hutaki kufunguka, jaribu kusema ukweli ili tuangalie jinsi ya kukusaidia”, Meja Satara alieleza.

“Kabla sijasema chochote naomba mnihakikishie usalama wangu, huyu Carlos ni mtu hatari sana, anaweza kuniangamiza”, Raymond alieleza.

“Kuhusu hilo ondoa shaka, tutakulinda kwa gharama yoyote”, Fred alimwambia.

“Na vipi kuhusu familia yangu?” alihoji.

“Kuhusu familia yako, wako chini ya uangalizi wa jeshi la polisi kabla hata hatujakukamata, hivi tunavyoongea hapa mkeo na watoto wako mikononi mwa polisi, lakini kwa ajili ya usalama wao tu”, nilimwambia akaonekana kushangaa.

Baada ya maelezo hayo, Raymond alieleza kila kitu kuhusu Carlos, alieleza jinsi alivyotambulishwa kwake na Denis, Afisa Ukaguzi mstaafu, ambaye sasa ni marehemu, alieleza jinsi alivyofahamiana na Hawa Msimbazi na mengine mengi, pia alieleza mbinu wanazotumia kuingiza dawa za kulevya nchini, na mkakati wa kuua yeyote anayeonekana kuingilia biashara yao.

“Asante, kazi yako imekwisha, Meja Satara, hakikisha huyu jamaa anapelekwa mahabusu ya siri mpaka nitakapojulisha vinginevyo”, Kanali Emilly aliagiza.

“Hakuna tatizo mkuu”, Meja Satara alieleza huku akijiandaa kuondoka na Raymond.

“Mlisema mtanisaidia, imekuwaje?”.

“Tulisema tutakusaidia baada ya kazi hii kwisha salama”, nilimwambia. Kiasi fulani nilifurahi kumkamata mtu huyu, maelezo yake yalitufanya tupate mwanga. Niliwapigia simu Claud na Nyawaminza kuwafahamisha kilichotokea wakaeleza furaha yao.


Wakati huo Mama Feka alikuwa kwenye foleni ya kununua tiketi ya kuingia California Dreema. Alivaa vizuri kiasi cha kumfanya mwanaume yeyote kuingiwa na tamaa, baada ya kupata tiketi yake alipenya mlango na kujitosa ndani ya ukumbi huu.

Muziki laini ulikuwa ukipenya masikioni mwa wapenzi wa starehe, kila mmoja alionekana akicheza na mpenzi wake, huku wengine wakiwa wameketi kwenye meza za pembeni wakiupiga mtindi.

Kama ilivyo kawaida yake, Mama Feka alipita akatafuta sehemu nzuri ambayo anaweza kuonekana kwa urahisi, alifanya hivi baada ya kuwa amemuona Carlos Dimera na wapambe wake wakiwa wameizunguka meza iliyojazwa vinywaji vya kila aina.

Ili aweze kuonekana, Mama Feka alianza kulicheza rhumba, alicheza vizuri huku akigeuka kila upande, kijana mmoja aliyekuwa karibu yake alivutiwa na mwana mama huyu, hivyo akajisogeza na kumuomba wacheze. Lakini hilo lingemfanya auhalibu mtego wake, alichofanya Mama Feka ni kumkwepa kijana huyo, akaendelea kucheza peke yake, kijana huyo kwa aibu akajiondoa eneo hilo.

Jakina alifanikiwa kumuona Mama Feka, hakufanya ajizi, haraka alizifikisha habari kwa Carlos, ambaye alikuwa ameketi kwenye meza ya vinywaji na akina dada kadhaa.

“Bosi, unamuona yule mbabe wa Supermarket?”, Jakina alimwambia Carlos Dimera.

“Yuko wapi?” Dimera alihamaki.

“Yule anacheza peke yake pale”.

“Oh, nimemuona, sasa sikiliza, tafuta mbinu ya kuwafanya hawa malaya wengine wasinisogelee, asije akaniona mhuni. Kwa vile wewe na yeye damu zenu zimetofautiana, acha niende mimi mwenyewe, nimuombe tucheze kidogo”, Carlos alimwambia Jakina huku akielekea mahali alipokuwa Mama Feka.

“Helo, habari yako?” Carlos alisalimia baada ya kumshika bega. Haraka Mama Feka aligeuka na macho yao kukutana.

“He, na wewe unakuja huku?” Mama Feka alihoji.

“Mimi ni mtu wa starehe, lazima nifike sehemu kama hizi, nimekuja kukuomba tucheze kidogo”, Carlos aliomba.

“Unataka ucheze na mimi wakati mlitaka kunipiga kule Supermakrt?”.

“Ilikuwa bahati mbaya, waswahili mnasema wanaogombana ndiyo wanaopatana, pole kwa yaliyotokea, msamehe kijana wangu hakuwa na nia mbaya”, Carlos alieleza.

“Sawa, nimekuelewa, karibu tucheze”, Mama Feka alifurahi kupata nafasi hiyo, wakaanza kucheza huku wameshikana.

“Unaitwa nani?” Carlos alihoji.

“Sweety”.

“Oh, jina zuri sana, unafanyakazi gani Sweety?”.

“Niko nyumbani tu, nimemaliza shule, ndiyo natafuta kazi”.

“Umesomea nini?”

“Mambo ya Maabara”, Mama Feka alidanganya.

Oh, very god, umepata kazi, mimi namiliki kiwanda kikubwa cha madawa”.

“Asante, na wewe unaitwa nani?”.

“Carlos, au ukipenda unaweza kuniita Carlos Dimera”.

“Wewe ni Mtaliano?”.

“No, hapana, si kila mzungu Mtaliano. Mimi ni raia wa Colombia”, Carlos alifafanua.

“Unafanya kazi gani?”.

“Yaani mimi nifanye kazi, mimi ni mfanyabiashara, business men”.

“Unafanya biashara gani?”.

“Ohoo, sasa hapa umekuja kustarehe au kunihoji”.

“Hapana, nilitaka tufahamiane tu”.

“Utanifahamu tu, si bado tuko pamoja”.

“Sawa”, wakaendelea kucheza.

Mama Feka akamshukru Mungu kwa kazi aliyoifanya kwa muda mfupi, aliyakumbuka maneno ya Teacher kuwa Carlos ni mtu hatari, lazima awe makini, akaupiga moyo wake konde na kujiweka tayari kwa lolote, akimtanguliza Mungu katika jukumu hilo zito, lililoko mbele yake.

Boing 787, mali ya Shirika la Ndege la Uholanzi, iliwasili na kutuwa taratibu kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius K. Nyerere, Jijini Dar es Salaam, majira ya saa nne na dakika arobaini na tano usiku. Baada ya abiria wa Dar es Salaam kutoka ndani ya ndege hii. Kazi ya kutoa mizigo ilichukuwa masaa kadhaa, hatmaye kila abiria alitoka na mzigo wake, baada ya kutimiza masharti.

ITAENDELEA

Noti Bandia Sehemu ya Nne

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment