Hii ni Dunia au Kuzimu Sehemu ya Pili
KIJASUSI

Ep 02: Hii ni Dunia au Kuzimu?

SIMULIZI Hii ni Dunia au Kuzimu
Hii ni Dunia au Kuzimu Sehemu ya Pili

IMEANDIKWA NA: AHMED JIRIWA

*********************************************************************************

Simulizi: Hii Ni Dunia Au Kuzimu?

Sehemu ya Pili (2)

“kwanini umethubutu kuleta wapelelezi ndani ya Taifa hili?…..si nakuuliza wewe jamaa?….daah! Hutaki kunijibu wewe” alisema kisha alimvuta Ndungai kwa nguvu na kumchama kisu cha kifua, akakichomoa haraka na kuchoma cha tumbo, akachomoa pia na kumuachia. Ndungai alilia kama mtoto. Alipata mateso makubwa.

“ah, ah!, usife kwanza nataka kukuambia kitu” alisema Kijazi kisha akapiga pafu jingine la bange na kukitupa kipisi. Bangi siyo ugali aisee!

“kawape taarifa wasiojua maana ya sheria kama wewe, waambie kuwa Ungamo hakuingii wapelelezi kizembe” aliesema halafu akamkamata tena Ndungai akamshambulia kwa visu vya kutosha, alimkatakata sana kama mnofu wa nyama ya Nguruwe. Ndungai alidondoka chini akiwa kwenye maumivu makali ya kifo. aliuwawa kifo kibaya sana, damu ziliruka kila upande sebule yote ilichafuka, kulikuwa hakutamaniki. Alitoka humo ndani akiwa katika kicheko kikali mno. Alifika mahali alipoiacha gari yake akavua koti ambalo lilikuwa halitamaniki kwa damu akalitupia kwenye buti akabakiwa na nguo zake safi

kabisa. akajitia garini na kuondoka. Alipokuwa barabarani alitoa simu akatuma ujumbe.

‘kazi yangu imekwisha kiongozi’ baada ya muda kidogo ujumbe ukarudi ukisema.

‘kazi njema mambo yatakwenda vizuri’ akairudisha simu mfukoni na kuchenji gia akapotelea mtaani.

Saa 01:15 Adhuhuri, ndege kubwa ya kitanzania ilikanyaga matairi yake juu ya uwanja wa Tao De. Miongoni mwa abiria waliotoka humo ndegeni, walikuwa wapelelezi wa wili kutokea Tanzania. walikuwa wamevaa kawaida sana, mtu hawezi kuwashtukia kirahisi lakini si kwa macho ya kazi ya Bande Sir. Tayari walikuwa wameshatambulika na kwa muda huo walikuwa wakipatiwa muda mdogo tu ili wafe kirahisi. Wakaingia kwenye Tax moja yenye rangi ya kibuluu, Bande Sir akanyanyua simu na kuiweka sikioni.

“nadhani mmewaona wameingia kwenye Tax ya kibuluu. hakikisheni mnapeana taarifa vizuri nahitaji kusikia ripoti nzuri ya kumpa kiongozi” aliongea hivyo Bande Sir kisha akaingia kwenye gari yake ndogo na kusonga kule ilikoelekea ile gari. Hakutaka kuwa mbali sana.

ile gari ilikuwa ikiendeshwa kwa kasi ya kawaida sana ikielekea katikati ya mji wa Muavengero. Ilifika kwenye makutano ya barabara, hapo kulitokea gari kubwa la mizigo lililokuwa likija kwa kasi sana. Yule dereva wa Tax alikuwa hakujiandaa na kitu kama kile, ilikuwa ni ghafla sana. Mzinga mkubwa ukatokea, ile Tax ulibetuliwa juu na kwenda kujipigiza kwenye kingo za barabara. ikapinduka mara tatu na kugeuza matairi juu. Dereva wa ile gari hakuwa ameumia sana alipata kuzuiwa vizuri kutokana alikuwa amejifunga mkanda lakini wale wapelelezi walikuwa wameumia vibaya sana na mmoja kufa hapo hapo. mwengine alikuwa akijitikisa ili kuweza kujinasua lakini alionekana na mtu ambaye hakujulikana alipokaa, risasi moja ikatosha kumnyamazisha. Wapelelezi wote wakapoteza maisha bila hata kufika popote.

Kilio kikali cha maumivu kilimkuta Tamimu. Alikuwa ameukumbatia mwili wa baba yake ulikuwa hauna uhai tena. Aliona kama ni kitu cha ajabu mno kilikuwa kimekwenda kumtokea kwenye maisha yake. Ndungai alikutwa na kifo cha ajabu mno, alikuwa amekatwa masikio yote mawili, nyama ya mdomi wa chini, pua pamoja na jicho moja. Pamoja na hayo pia alikuwa amechomwa na kitu chenye ncha kali si chini ya mara tano au sita. Kilikuwa ni kilio cha kinyama mno. Tamimu aliwapigia polisi simu asubuhi hiyo na muda haukupita sana polisi wakawa wamefika mahali pale.

“Mungu wangu ‘HII NI DUNIA AU KUZIMU?’ afisa mmoja wa polisi alijikuta akiongea maneno hayo mara baada ya kuushuhudia huo mwili wa kutisha. Walifanya vipimo mahali pale kisha wakamuhoji maswali mawili matatu Tamimu ambaye alikuwa hana nguvu kabisa. Wakati wakiwa katika harakati ya kuukusanya mwili wa Ndungai kwa ajili ya kwenda kuupa hifadhi ili kupisha uchunguzi, simu ya upepo ya askari mmoja ambaye alikuwa kiongozi kwa kumtazama mavazi yake tu. Akairuhusu ile simu ilete taarifa.

“afande kwenye makutano ya barabara ya Muavengero na ile ya madukani kutokea uwanja wa ndege, kuna ajali imetokea ambayo si ya kawaida” ilisikika sauti hiyo iliyoleta taarifa.

“ikoje hiyo ajali?” akauliza huyo askari mwenye cheo cha Koplo.

“gari ndogo Mark II, imegongwa kwa nguvu sana na kutupwa mbali, imesababisha vifo vya watu wawili huku mmoja akionekana kujeruhiwa vibaya sana” ikazidi kuleta taarifa hiyo sauti.

“mzuieni huyo dereva wa hiyo gari nakuja sasa hivi hapo…..aaah! haya mambo sasa yanatisha, sielewi kwanini watu wanauwawa hivi!” alisema huyo Koplo kisha akastaajabu baada ya kuambiwa kuwa dereva msababishi wa hilo hakuonekana zaidi ni kwamba gari tu ndilo lililotelekezwa.

“Muso natakiwa huko nako kumetokea mauwaji mengine ya watu wawili waliokuwa wanatokea uwanja wa ndege, Chukua huo mwili vizuri naita gari sasa hivi” akatoka kisha moja kwa moja hadi kwenye gari waliyokuja nayo akamuamuru dereva aiondoe gari hiyo kuelekea makutano ya barabara ya Muavengero. Gari hiyo ikaondoka kwa kasi kubwa. Tamimu alipatwa na mshtuko kidogo baada ya kusikia kuwa kuna ajali imetokea, tena waliopata ajali ni watu waliokuwa wanatoke ‘air port, jambo hilo lilimpa mashaka makubwa sana na hakutaka kulipa nafasi ya kumfikirisha kuwa eti huwenda ni wale wapelelezi kutoka Tanzania, hili hakutaka liwe rafiki ubongoni lakini aliahidi kwenda kupata uhakika kwa Backa pindi atakapotoka kutoa maelezo polisi.

Taarifa ya habari ya saa moja kamili usiku ilitangazwa kutoka kwenye chombo kimoja cha habari ndani ya nchi hiyo na muktasari wa habari ulisema kwamba.

(Watu wawili wafariki dunia na mmoja kujeruhiwa vibaya baada ya gari waliyokuwa wakisafiria kugongwa vibaya sana na roli kuwa la mizigo.) Habari hiyo ilizidi kufafanuliwa kusema kwamba, watu hao ni wageni na walikuwa wakitokea uwanja wa ngege lakini haikujulikana ni raia wa nchi gani. Lakini ilimaliziwa kwa kusema kuwa bado polisi walikuwa wakiendelea na uchunguzi wa tukio hilo. Wakati habari hiyo ilipokuwa ikitolewa tayari kwa muda huo kuna vichwa vilikuwa vikiumiza akili vibaya mno na kichwa kimoja kilichokuwa kimechanganyikiwa zaidi kilikuwa ni cha mheshimiwa Rais Mabandu. Alikuwa hajielewi kabisa hapo alipo baada ya kupokea simu kutoka kwa IGP kuwa watu wale waliopata ajali ni raia wa Tanzania tena wakiwa ni wapelelezi. Hili Halikuwa jambo dogo kwake na tayari kwa majira hayo alisha muhitaji ofisini hapo IGP. Aliijua Tanzania vizuri, alijua kuwa endapo taarifa hizo zikifika Tanzania basi huwenda kukawa na jambo kubwa na baya kwenye Taifa lake dogo ambalo linategemea msaada mkubwa kutoka kwa majirani zao hao je, vipi wakiwa na migongano? Ni hatari kubwa. Kiti kilikuwa hakikaliki japo alishajaribu si chini ya mara tatu kukaa lakini hamu ya kutulia kitini haikuwepo. Mlango ulifunguliwa kwa utaratibu kisha sura ya IGP Liyambo ikajiingiza humo ndani. Mh. Rais alikimbia haraka na kwenda kukaa kwenye kiti kwa lazima hata kama hamu hiyo haikuwepo lakini alikuwa akihitaji kujua ni nani hao waliogusa ndevu za Dubu.

“hivi Liyambo wewe na watu wako mnafikiria……,aaaaah! Kumbe wewe huhusiki kwenye hili” alisema kwa kuchanganyikiwa sana Mh. Mabandu alichukuwa birauli ya maji lakini hakuinywa akairudisha mezani na kumeza mate ambayo yalitosha kabisa kukiondosha kiu alichokuwa nacho. Maji yatanyweka vipi sasa.

“wapelelezi wa Tanzani wameuwawa kwa ajali hivi ni ajali kweli ulisema?” alisema kisha kuuliza.

“ndiyo kiongozi ni ajali lakini pia kuna zaidi ya ajali….!”

“hilo ulitaka kunificha, maana hukuniambia” alikatisha mh. Rais. Liyambo akajitetea

“hapana mkuu, sikuwa na mpango wa kukuficha, uliponipigia simu ya mimi kufika hapa nami nikampigia simu daktari aliyekuwa akiichunguza ile miili ya hao marehemu……!”

“Liyambo unakosea usiwaite marehemu sema wapelelezi” alisema kwa kukata kauli ya IGP Rais Mabandu. kisha baada ya hapo IGP Liyambo akaendelea.

“ndiyo, hao wapelelezi” ilibidi tu IGP aseme hivyo kwani mkuu wake wa nchi alishasahau kuwa hata kama ni wapelelezi lakini walishakufa tayari na hawezi kurudi duniani kwa kuwaita majina yao ya heshima.

“daktari amenipa ripoti kuwa mwili mmoja kati ya ile miwili umekutwa na tundu la risasi kwenye kifua na si tundu la risasi pekee bali risasi hiyo imekutwa kwenye moyo”

“mungu wangu! Wameuwawa!” mh. Mabandu alihamaki kwa mshangao wa aina yake.

“mbona hawa watu wanatoka hadi nje ya mipaka namna hii hawaoni kama wananiingiza mimi na Taifa hili kwenye matatizo” aliwaza Mh. Mabandu kisha akamtazama IGP kwa muda bila kusema jambo lakini kimya kile hakikudumu sana baada ya IGP Liyambo kuuliza kuwa nini kifanyike kuhusiana na hilo.

“mimi ni Rais gani sijui, najuta kuingia kwenye haya madaraka Liyambo, najuta. Ona ninavyoingia kwenye ugomvi na jirani yangu, ona sasa tutakavyogombana” badala ya kujibu alibaki kulalamika. Mabandu alikuwa amechanganyikiwa na kupagawa nadani yake. Liyambo alitulia kimya bila kuzungumza kitu alijua fika kuwa mh. Rais amechanganyikiwa hivyo alikuwa na kazi ya kuhakikisha anamuweka katika hali ya usawa. Muda wote Mabandu alikuwa ni mtu wa kujiuliza wingi wa maswali tu hakuwa na amani kabisa. Alijiona hakustahili kuwa raisi wa Taifa hilo kabisa. Lakini akiwa kwenye kuwaza namna hiyo, alipata wazo, hili kidogo aliona lingefaa zaidi.

“inabidi niite kikao usiku huu akiwemo na raisi Julio Mobande, nataka kuomba ushauri kwao, hili suala limenielemea nadhani kwa kuwa yeye ni Rais wa muda mrefu ndani ya Taifa hili anaweza kunishauri nini cha kufanya, unasemaje kwenye hili?” alitoa wazo lililokuwa lipo kichwani mwake bwana Mbandu lakini lilipokelewa tofauti kidogo na IGP. Aliweka mashaka Inspkta Jenerali. Akasema.

“ni wazo zuri kufanya hivyo lakini kwanini umewaza hilo moja kwa moja?”

“nimeshakupa sababu zangu Liyambo huzioni kama zina mantiki?” alifoka Mheshimiwa.

“hapana” Liyambo akajitetea.

“sikiliza nikuambie mkuu” akasema IGP kisha akamtazama Rais Mabandu usoni.

“kuna siri inalitafuna Taifa hili na siri hii ni mdudu mbaya kuliko unavyodhani, mdudu huyo siri ametengenezwa na viongozi wengi wa zamani. Hivi unajua kwa nini wanamuandama Backa hadi sasa?” Rais akatikisa kichwa pembe na pembe kukataa kuwa hajui.

“sasa ngoja nikupe mwanga mdogo wa nijuavyo mimi kisha utafikiria kikao hicho utakiitaje au utakitengenezaje na utajua mtazungumzia nini maana mimi sitakuwepo na sipendi kuwepo” akaendelea IGP.

“Mh. Bcka alipewa vitisho na mtu asiyemjua sawa, lakini mimi nimepewa vitisho na mtu ambaye hadi leo yupo madarakani, huyu ni waziri wa ulinzi, mimi naita vitisho kwa sababu hawezi kunipa mimi amri ya kusitisha au kuniamrisha kuondoa askari kule. Mimi nadhani huyu ndiye angekuwa mtu wa kwanza kumuitia kikao kisha wengine kufuata kama unataka iwe hivyo” alisema IGP kisha akashusha pumzi nzito sana iliyofuatiwa na Rais pia. Kimya kikatanda rais sura ikabadilika na kuwa nyeusi zaidi kutokana na rangi yake. Kamasi zilikuwa zikitaka kutangeneza njia ili kutoka lakini zikajishtukia baada ya kujua yapo kwenye pua ya mkuu wa nchi, yakarudi mahali pake kwa kujilazimisha,

“nataka kubaki mwenyewe kulifikiria hili kisha nijue nini cha kufanya” alisema mh. Mabandu lakini kabla IGP hajatoka mule ndani akauliza swali.

“mkuu, hivi ni kweli hukupata kitisho chochote kutoka kwa hawa jamaa?” jicho la kuuliza kwanini unaniuliza hivyo likamtazama Liyambo, hili lilikuwa na mashaka kwa mbali sana. Liyambo akamalizia.

“maana hawa jamaa huwa hawogopi binaadamu kabisa” aliishia hapo Liyambo. Mh. Mabandu akataka kukana kuwa hakuwahi kupokea vitisho lakini akafikiri kwa muda na kujikosoa mwenyewe kama kweli hajapata vitisho yeye kama mtu mkubwa na mwenye sauti kwenye nchi hiyo anashindwaje kumbana na maswali mazito waziri Bande Sir juu ya kutoa amri ya kusimamisha kupeleka walinzi kwa Backa huku akidanganya kuwa ni amri kutoka kwake. Akameza mate ya kujiona yeye ni kivuli tu cha raisi lakini bado hajaapishwa kuwa raisi kamili. Alimtazama kijana yule ambaye miezi michache ijayo anaacha na huo ujana na kuingi kwenye utu uzima.

“nimechanganyikiwa Liyambo, nenda nahitaji kuwa mwenyewe kwa muda huu” alisema huku akiwa anaumia sana moyoni kwa kutokuwa na maamuzi ya mwisho.

Si kama alishindwa kutoa maamuzi la! Bali kila anapofikiria kufanya hivyo alimkumbuka kiziwanda chake na kitinda mimba chake hicho kimoja kilichopo masomoni nchini China. Moyo unakuwa mzito sana. Ni kweli aliipenda Ungamo na aligombea nafasi hiyo ya uraisi ili kuja kuwasaidia wana Ungamo lakini tulizo la moyo wake na kipenzi cha moyo wake alikuwa ni ni binti yake aliyopo masomoni. Mara nyingi sana alijikuta akiwaomba msamaha wana ungamo kwa kusena ‘mtanisamehe sana wana Unagamo’ alilia mwenye usiku na mchana, alilia hadi mkewe akawa anamhurumia lakini hakuwa na msaada mkubwa kwa kilio cha Mkuu huyo wa nchi na hakuwa karibu kwa kumshauri chochote kama mke wa Rais.

“natamani kuurudisha muda nyuma ili niitoe nje ya moyo dhamira yangu ya kulikomboa Taifa hili, ona nimekuwa Rais jina, ona nimekuwa Jibwa koko lisilo na sauti mbele ya wanaume wenzangu. Tazama Mh. Backa anavyosononeka moyoni kwa kukosa msaada lakini huku hawa wapelelezi walikuja kufanya nini sasa ndani ya Taifa hili?” aliwaza mengi Mh. Mabandu kisha akajiuliza swali juu ya kuja hapo nchini kwa wapelelezi kutoka Tanzania.

“Backa, inawezekana aliamua kuomba msaada Tanzania maana kwa mtu kama yeye mwenye ukwasi wa kutosha hashindwi kufanya hivyo lakini…….!” alikuwa akizidi kujiuliza pale kwenye kiti chake ndani ya Ofisi yake iliyondani ya Ikulu, mara mlango ukagongwa kisha mgongaji kuingia humo ndani, alikuwa ni ‘first lady mama Salama Mbonde. Alipita moja kwa moja hadi kitini kisha akamtazama mumewe usoni.

“unaonekana uko na msongo wa mawazo sana mume wangu kwani kuna taarifa mbaya kutoka Tanzania?” aliuliza mama Mbonde au waweza kumuita Salama kwa jina lake la kwenye cheti cha kuzaliwa. Macho ya mshangao kutoka kwa mumewe yakamdondokea, Salama akamkazia macho bwana huyo kuonesha kuwa kweli anataka kujua kuhusu hilo. Rais Mabandu akaikunja sura na kuhoji ni kwanini amelifanya swali hilo kuwa la kwanza hapo. Salama akasema anahaki ya kujua kama mke wa Rais. Mabandu akashusha pumzi nzito na kufungua vishikizo viwili vya suti yake vilivyokuwa vikiling’ang’ania koti hilo hadi akahisi linambana. Alihisi joto pia na ilhali mule ofini AC zilikuwa zikifanya kazi kwa ushirikiano mkubwa sana.

“hakuna chochote kutoka Tanzania hadi sasa” akajibu huku akimtazama mama huyo kwa tuo kidogo, mama huyo akatabasamu na kubadili kabisa sauti na muonekano.

“pole sana mume wangu najua unapitia kwenye wakati mgumu lakini hii ni moja ya mitihani inayowakuta wanadamu. Huna budi kupambana na kulipigania Taifa hili natumai kwa uwezo wa mungu utashinda. Niko bega kwa bega pamoja nawe mume wangu” alisema Salama kwa sauti ya upole sana kisha akatulia. Mh. Mabandu alifarijika mno kupokea maneno hayo ya kutia nguvu, alijikuta akiwa na furaha sana kwani ni mara chache sana mkewe kumpa moyo kisha kumtia nguvu. Alitabasamu hadi mwisho wa tabasamu hilo huku akisahau maumivu ya muda mdogo uliopita.

“asnte sana mke wangu, naomba uwe pamoja nami” alisema lakini mkewe akesema.

“nakuahidi mume wangu lakini hakikisha mwenetu anakuwa salama sitapenda kumuona binti yangu wa pekee akiingia kwenye matatizo. Nadhani unajua kuwa ni tabu na shida kiasi gani mimi nawe tumepita hadi kuja kumpata huyu mtoto”

“najua Salama, najua na nakuahidi kuwa hakuna baya litakalompata binti yetu” alisema Mabandu huku akiwa amemkaribia mkewe, sura zao zikitaka kukaribiana. Salama akarudi nyuma ghafla na kuigamia kitini akavuta pumzi nyingi na kusema kwa unyonge kidogo.

“Backa bado yuko kwenye matatizo na wauwaji wanazidi kumuandama”

“kuna jingine limetokea?” alidakia mh. Mabandu huku akimtazama mkewe kwa macho ya mshangao.

“ndiyo, wamemuuwa rafiki yake wa karibu” alisema Salama.

“Mungu wangu, Ndungai ameuwawa?”

“tena kifo kibaya mno?” alisherehesha Mama Mbonde huku akiwa anamtazama mumewe kwa macho ya kumhirumia kinafiki.

“Backa my friend, umemkosea nini Mungu wewe mtu, mbona ulikuwa mwema, mbona uliwapenda wanachi wote wa Taifa hili na kuwasaidia kwa mali na hali? Leo mbona……!” hakumaliza Mabandu, simu yake ya ofisini ikaita. Macho yakamtoka, simu hiyo huwa inapigwa na watu maalumu na wenye mambo ya msingi zaidi. Alijikuta akitaka kupaliwa na mate kwa kihoro kilichomkumba ghafla, ni nani huyu? akajiuliza moyoni huku ubongo ukimsaliti na kugoma kumpa jibu. Moyo kwa ulivyo na kiherehere ukamwambia ‘mheshimiwa pokea simu itakatika’ Mh. Mabandu kweli akavuta mkonga na kuiweka simu sikioni.

“Hallow!” sauti nzito ikamfanya aweke kiganja cha mkono kwenye spika ya simu hiyo kisha kuishusha na kumtaka mkewe atoke humo ndani. Salama hakupinga alitoka. Mh. Mabandu kabla ya kuendelea na maongezi akabofya kitufe kimoja mezani kisha macho yake yakatazama kioo kimoja cha kompyuta kilichopo kwa mbele, akamuona mkewe akipita kwenye ofisi ya katibu muktasi kisha kuelekea nje.

“habari yako muheshimiwa, samahani sana nilikuwa naweka sawa hali ya kiusalama” mh. Mabandu akasalimu na kuomba radhi kwa kuizuia simu hiyo kwa muda.

“pole kwa matukio ya kuogopesha ama kukutisha yanayozidi kuendelea nchini kwako. Lakini Taarifa ziwafikie hao watishi wa nchi yako ama zisiwafikie naapa watajuta. Thamani ya mpelelezi wangu mmoja ni roho ya mkubwa wao ama aingie mikononi mwetu. Sitawaacha na sina muda maalumu kuanzia sasa. Nimekufikishia ujumbe wewe tu na sijampigia simu mwingine siku ya leo hata ndugu yangu wa damu” baada ya sauti hiyo nzito yenye uchungu ndani yake kuongea mahali hapo kwa takribani dakika moja nzima, simu hiyo ilikatwa. Pumzi za asante Mungu zikamtoka Mh. Mabandu Mbonde. akatabasamu kwa mbali sana lakini tabasamu lake likakatika mara tu baada ya kukikumbuka kifo cha Ndungai. Chozi likamtoka, akalifuta likamtoka tena hili akaliacha na kukiendea kioo kikubwa na kujitazama. Akaliona lile chozi lilivyo na kiherehere, eti lilikosa njia ya kupita likawa linakimbilia kwenye papi za midomo yake, akalifuta kwa haraka sana kisha akarudi mezani. Vitufe sita alivyobofya vilitosha kumruhusu kuiweka simu sikioni, hii ilikuwa simu nyingine ya mezani tofauti na ile ya mwanzo.

“nahitaji kuonana na waziri mkuu pamoja na waziri wa ulinzi baada ya saa mbili na nusu usiku kwenye chumba maalumu” akaikata hiyo simu na kubofya namba nyingine kisha kuiweka tena sikioni, hii haikumpa majibu mazuri akairudisha kwenye kikalio chake na kutoa simu yake ya mkononi. Akatafuta jina kisha kulipiga.

“hakuna njia nyingine inabidi uwepo kwenye kikao cha usiku baada ya saa mbili kwenye chumba maalumu” alisema hivyo Mh. Mabandu lakini hakutaka kusikia hata sauti ya mhemo kutoka upande wa pili, akakata simu. Alitoka humo ndani hadi sebuleni kwake ndani ya Ikulu hiyo. akaja binti mmoja mrembo akiwa na jagi la maji kisha akaliweka kwenye meza ya kioo mahali ambapo mh. huyo amekaa. Akaleta gilasi safi na kummiminia maji muheshimiwa huyo.

“karibu!” sauti tamu na yenye unyenyekevu ikakita kwenye masikio ya Mabandu lakini hakukurupuka kuyanywa yale maji, aliyatazama kama vile kulikuwa kuna ramani ya Taifa lake ndani ya yale maji kisha akanyanyuka na kuelekea chumbani. Hakufika mbali akarudi.

“maji ni uhai” akajisemea kisha akakamata ile gilasi na kujimiminia tumboni mwake. Sasa akajificha huko chumbani kimya.

“ha ha ha haaaa! Aha, aha, aha ha haaa!” muheshimiwa Backa alicheka kicheko kikali mno, kilikuwa ni kicheko ambacho hakika kiliumiza. Backa alicheka hadi akaumiza mbavu zake, kicheko hicho kilidumu kwa muda mfupi sana kisha kilio cha kwikwi kumkamata. Kilio kilichoanza taratibu na hatimae kushika hatamu. Kilio kile kilichokuwa kikitoka bila sauti kikafutika, sasa Backa akalia kama mtoto mdogo, alilia kweli tena alilia kwa uchungu mno, yalikuwa ni maumivu yasiyoelezeka. Kwanini sina bahati mimi? aliwaza Backa kisha akaendelea kulia tu. Phili hakuwa na kitu cha kuongea mbele ya bosi wake hadi kuweza kuirejesha furaha, alishabembeleza sana, alishatoa moyo sana na kumtaka awe mvumilivu kwa kuamini msaada ulikuwa unakuja machoni mwake na kumrejeshea ile furaha yake lakini haikuwepo. Aliamua kumuacha alie hadi pale atakapoamua kunyamaza mwenyewe tu. Machozi yalimmwagika bwana huyo hadi akahisi yanaweza yakapungua mwilini mwake. Alisimama katikati ya kile chumba alichokuwamo kisha akapiga hatua za taratibu hadi sebuleni, akaenda hadi ilipo meza ndogo ya chakula mule ndani akaketi kitini.

“Phili!” aliita huku akijitahidi kufuta machozi. Phili hakuwa mbali hivyo ni kwa muda huo huo alikuwa mbele yake.

“nenda jikoni waambie waniandalie chakula kile nikipendacho” alisema Backa. Mshangao mkubwa ukamkumba Phili lakini hakungoja amri nyingine itoke kwa bwana wake. Akaelekea jikoni kutoa hiyo oda. Muda mfupi mbele chakula kilikuwa tayari, kikaletwa mezani. Hakukingoja kipoe alikila vivo hivyo tena kwa pupa kubwa hadi akakimaliza chote, muda wote huo Phili alikuwa akitabasamu baada ya kumuona bosi wake jinsi anavyokula kwa pupa kile chakula. Backa alipohakikisha tumbo lake liko sawa alinyanyuka na kuelekea maliwatoni kujiswafi kisha akarudi chumbani kwake akavaa suti safi kabisa na ya gharama ya rangi ya kijivu, alinyuka na Moka safi akatoka.

“nataka kutoka sasa Phili, niandalie gari nzuri” aliongea baada ya kuwa hapo sebuleni kwa mara nyingine.

“ni hatari sana boss, huoni kama ni usiku wa jana tu rafiki yako kipenzi aliuwawa? wanaweza kukuangamiza na wewe boss!” alitoa wasiwasi wake kijana huyo makini anayekwenda kwa majina Philimoni Kata. Kwa kupenda kupunguza kuulizwa mara mbili mbili akaamua kulifupisha kwa kujiita Phili. Kijana aliyekuwa karibu sana na Backa baada ya mlinzi wake wa kwanza kufa kwa ajali kama miaka miwili nyuma alipokuwa akitokea Haika City kuitazama familia yake. Backa hakusema kitu alimtazama kijana huyo mwenye akili na umakini mkubwa kuliko umri wake kisha akasema.

“hebu weka hii namba kwenye simu yako” alipokwisha kusema hivyo akazitaja hizo namba Phili akaziandika kisha akaamuru azipige. Zikapigwa na simu ya upande wa pili ikaita, Phili akamkabidhi bosi wake hiyo simu.

“tukutane kwenye maporomoko ya mto Zigi ninamaongezi na wewe kijana wangu, Backa hapa naongea” alizungumza hivyo baada ya simu hiyo kupokelewa, upande wa pili wa simu ukajibu vizuri tu. Backa akamtazama kijana wake ambaye hakuwa akimuelewa bosi wake hata kidogo.

“utanisamehe sana kwa kuto kukupa taarifa, hii ni muhimu sana na ni salama pia kuwa na amani, niandalie gari na nitaondoka na wewe” alisema Backa. Kijana huyo hakusubiri aliondoka aliporudi hapo alimwambia bosi wake kuwa gari ipo tayari. Walitoka hadi mahali ilipo gari kisha Phili akalitoa taratibu hadi nje ya uzio na kuipeleka hiyo gari kwenye kifaa cha kuivusha hadi upande mwingine. Wakatoka na hiyo gari taratibu hadi walipoikamata barabara.

“nadhani umenisikia vizuri nilivyokuwa nikiongea pale, natakiwa kwenda huko kwenye maporomoko ya mto zigi halafu hiyo namba utaihifadhi kwenye simu yako nitakuwa nikitumia kuwasiliana na watu wangu muhimu sitaki kuwa na simu tena nahisi kuna mchezo mchafu wananichezea hawa watu” alisema Backa huku gari ikiwa mwendo wa kasi kiasi barabarani, ilikuwa ikipita nyuma ya uwanja wa Mpira wa kikapu kutokea kwenye hospitali ya Taifa ya Pande. Hapa waliiacha Barabara inayoelekea Madukani na kuichukua Barabara inayoelekea kwenye hifadhi ya maji safi na maji taka.

Walipofika kwenye matanki makubwa ya kusafishia maji, walikunja kulia kuifuata barabara inayotokea huko kwenye maporomoko. Gari ilisimama mbali kidogo na yalipoanzia maporomoka hayo kisha wakashuka na kutembea kwa miguu hadi walipofika yalipoanzia hayo maporomoko wakasimama kimya. Muda mfupi mbele, pikipiki kubwa lenye chata kubwa la moto ubavuni likaingia mahali hapo, kijana mdogo akashuka na kulitoa kofia kubwa la kujikinga akalipachika mbele ya lile pikipiki na kupiga hatua kuwafuata watu aliowakuta mahali hapo. Phili akageuka kumtazama huyo kijana akagundua kumbe alikuwa ni mtoto wa marehemu Ndungai.

“pole sana kijana wangu, pole sana Tamimu kwa msiba mzito wa baba yako” alitoa pole Backa kabla ya salamu, ni mara tu ya kijana huyo kufika mahali hapo.

“nimepoa baba japo inaniuma sana kwasababu baba yangu amekufa kipindi ambacho nilitaka ashuhudie mafanikio yangu lakini sina jinsi na siwezi tena kumrudissha duniani” alipokea pole Tamimu kisha akaongea machache.

“kwanini umeamua kuniita mahali hapa baba?” akahoji. Backa pasipo kujibu akageuka na kumtazama kijana huyo kisha akasema.

“ni mimi ndiye chanzo cha kifo cha baba yako, ni mimi Tamimu. Sijui ni kwa nini nilimshirikisha kwenye matatizo yangu, yale ni matatizo ya familia yangu hakustahili kuingizwa yeye lakini ni kwa nini sasa nimemuingiza hadi anapoteza maisha sijui kifo chake kilikuwa na uchungu kiasi gani” alifuta mchozi uliokuwa ukimtoka kisha akameza mate na kuendelea.

“najua unauchungu sana Mwanangu, wewe ni mwanangu Tamimu lakini kilichonifanya nikuite hapa ni mambo mawili tu, mosi likiwa ni kukujulisha kuwa sitakubali baba yako azikwe kesho” kauli hiyo ikamfanya Tamimu kushtuka. kwanini asimzike baba yake kesho. Akajiuliza lakini kabla hajapata jibu, Backa akaendelea kufafanua.

“acha watu wafanye uchunguzi wao kwa hizi siku tatu kwanza najua hata kama nikifa leo my boy lakini nataka wajue pa kuanzia. Pili ni kukufahamisha ya kuwa sitaweza kuhudhuria mazishi ya rafiki yangu kutokana na hali yangu ya kufuatiliwa na watu nisiowajua pia nikikuonya wewe uachane kabisa na kumtafuta Tereza” akanyamaza. Tamimu akaja juu na kuhoji kwanini azuiwe kumtafuta mpenzi wake, hapo aligoma kabisa.

“naogopa kukupoteza Kijana wangu, baki wewe basi hata sisi tukifa wote ili uziendeleze mali zetu au unataka kila kitu kipotee?….hapana siko tayari kijana wangu. Tereza nitamtafuta mimi mwenye kama nikifa basi mzimu wangu utamrudisha mpenzi wako nyumbani”

“hapana baba, yote uliyoyaongea nimeyaelewa na nitayatekeleza lakini kuhusu Tereza sitaacha kumtafuta na niko radhi kufa. Kifo walichomuua baba yangu si kifo ambacho Mungu amekiidhinisha, ni kifo cha kuzimu kile baba, hebu tazama” alisema Tamimu huku akiitoa picha ndogo na kumkabidhi. Backa akaipokea. Aisee! Chozi zito lilimtoka hakutegemea kuja kukutana na mauwaji kama yale duniani, ama kwa hakika aliamini aliyeuwa hakuwa binadamu na kama alikuwa binadamu basi anamatatizo ya akili si bure.

“baba, acha wewe kusumbuka sasa, mimi nitamtafuta Tereza mpenzi wangu na pia nitahakikisha hawa waliofanya huo unyama wanalipa” Alipomaliza kusema hayo aliondoka mahali hapo bila kuaga, Backa alitaka kuongea kitu cha mwisho lakini hakupata hiyo nafasi akabaki kuugandisha mkono wake hewani tu. Hawajui hawa wauwaji huyu kijana? aliwaza kisha akatulia hapo pasi na kuongea kitu.

Ilikuwa Tayari ni jioni, kigiza kikianza kuomba mamlaka ya kuliteka anga, Ndani ya jumba moja tulivu sana huko Tanzania Jijini Dar es salaam, kulikuwa na kikao kizito kilichokuwa kimekaliwa na watu wachache. Kimya kilikuwa kikubwa sana lakini kimya hicho hakikuwa kwa sababu ya kukosa la kuongea la! Kulikuwa na mtu ambaye alionekana kusubiriwa mahali hapo na hiyo ilijidhihirisha baada ya kila mmoja pale kuitazama simu yake. Kweli kulikuwa na mtu kweli aliyekuwa akisubiriwa kwani muda si mrefu, bwana mmoja aliyejificha ndani ya umaridadi alikuwa akiingia humo ndani huku suti yake nyeusi ikimtangazia umaridadi wake huyo bwana.

“samahani kwa kuchelewa kufika nilikuwa nikipokea taarifa muhimu ofisini kwangu” akaomba radhi kwa kuchelewa kwake kufika huku akitoa sababu mubashara iliyomchelewesha. Akakaa kitini kisha akawatazama wajumbe wote pale ambao idadi yao haikuzidi watu watatu.

“mgh! mgh!” akajikohoza ili kuliweka koo lake sawa baada ya kujiridhisha kwa uwepo wa watu wale. Akasema.

“wamegusa penye sumu isiyongoja kuona damu ndiyo ifanye kazi” akatulia huyo mtu nadhifu kisha akasema tena.

“siyo maneno yangu hayo ni maneno ya mkuu wa nchi lakini hakuishia kwenye maneno hayo tu bali anataka kuanzia sasa hadi kesho kutwa kuwe kuna ufumbuzi wa hili na mtatuzi awe amepatikana” akatulia tena mtu huyo nadhifu huku akiwatazama wale wajumbe kana kwamba anataka kuwaomba pesa ya chai kwa mwenye nayo, kimya kidogo kikakita lakini hakikudumu.

“Bwana Hussein Babu!” akaita yule mtu nadhifu kisha akamtazama machoni mtu aliyemuita, huyo bwana aliyetambulika kwa majina yake Hussei Babu, akanyanyua kichwa juu kisha mtu yule nadhifu akasema.

“baada ya kikao hiki nitakuhitaji ofisini kwangu sawa” alipomaliza kutoa hiyo amri, akafunga kile kikao na kuondoka wa kwanza ndani ya chumba hicho tulivu. Baada ya kikao kile kufungwa, watu wale wawili walikutana kwenye ofisi ya yule mtu nadhifu lakini kilichoongelewa hakikuwa bayana. Watu wale wakaagana na kila mmoja akachukua hamsini zake.

ANTANANARIVO MADAGASCAR.

Usiku huo wa saa mbili kulikuwa na pilika pilika za hapa na pale kila mmoja akionekana kuchanganyikiwa baada ya binti Tereza kurudiwa na fahamu baada ya kupewa chakula chenye madini yenye kumpa nguvu baada ya Daktari kugundua kuwa binti huyo alikuwa akisumbuliwa na njaa na si kitu kingine. Pamoja na kurudiwa na fahamu pia kuwa na nguvu za kutosha lakini binti huyo alishajaribu kujiuwa si zaidi ya mara nne au tano huku ari yake ya kugoma kula ikiwa palepale. Hofu ziliwatanda watu hao, madaktari walizidi kukosa amani kila wakati walikuwa wakizunguka kwenye chumba ambacho alikuwa amelazwa huyo binti ili tu kuhakikisha hakuna madhara mengine ambayo yangeweza kumtokea.

“huyu ni Daktari na mtaalamu kuliko nyinyi hivyo anaweza kubuni chochote na kwa wakati wowote kikawa sumu na akajiangamiza, kuweni makini nae sana” ndivyo Dr. Henry Cartiley alivyokuwa akiwapa angalizo wauguzi wa Hospitali hiyo iliyondani ya himaya ya Dr. Lee. Walinzi waliwekwa wa kutosha kuhakikisha binti huyo hafanyi jaribio lolote la kujiuwa. Tereza alikosa namna ya kufanya kweli hakuwa na njia nyingine ya kuweza kujiondoa duniani sasa akawa analia tu muda wote huku kugoma kula ikiwa ni moja ya ratiba yake. Kitu pekee alichokuwa akikihitaji mahali hapo ni maji na si kitu kingine.

“inabidi kumuwekea madini yenye nguvu humu kwenye maji ili asiwe analegea kutokana na kuzidiwa na njaa?” alitoa wazo muuguzi mmoja.

“kweli hiyo itasaidia” alijibu Dr. Henry huku akiwataka wauguzi wake kufanya hivyo. Wakawa wanamuwekea madini hayo ya kumpa nguvu kwa kuyachanganya na maji. Tereza alipokuwa akihitaji maji tu basi alikuwa akipewa kwa haraka sana lakini baada ya kuyanywa maji hayo alijikuta akipata nguvu za ajabu mno. Hali hiyo hakuipenda na aliichukia kupita kiasi. Wauguzi pamoja na Dr. Henry walifurahi sana kwa kuweza kugundua hicho kitu japo walijua kuwa haitaweza kumsaidia kuishi muda mrefu kwa kutegemea kumpa maji lakini hakukuwa na njia nyingine ya kuweza kuitumia zaidi ya hiyo na kama walitaka kumpa chakula basi ilikuwa ni kumchoma sindano ya kumpa usingizi kisha kumlisha kwa kutumia mipira kama ambavyo walikuwa wakifanya mara moja moja. Tereza akayachukia maji pia na kuamua kuyakataa.

“Dokta huyu binti ni mwendawazimu kabisa” alisema muuguzi baada ya kufika kwenye ofisi ya dokta Henry.

“fuck!” alitukana Dr. Henry baada ya kupokea hiyo taarifa. Hakujua njia ambayo angeitumia kuweza kufanya binti huyo asiathiriwe na njaa.

“una kazi kubwa unayotakiwa kufanya mjinga wewe hebu kula usituchanganye” alifoka Dokta huyo mara baada ya kufika mbele ya kitanda alicholazwa Tereza.

“kama baba yangu hataletwa hapa siwezi fanya chochote na nitakufa tu” alijibu binti huyo hali iliyomfanya daktari huyo bingwa na mwenye roho mbaya kushtuka kidogo kisha akamwambia basi ni bora ale maana siku si nyingi baba yake angekuwa mahali hapo. Tereza akatikisa kichwa chake kukataa. Alihitaji kumuona baba yake mahali hapo ili kama ni kuishi wote basi waishi hapo huku wakifanya hicho ambacho watu hao wanataka kufanyiwa.

“sijui nini kifanyike Bencov nimechanganyikiwa vibaya mno, akili imekuwa ndogo kufikiri inamaana huyu binti ataendelea kuwa katika hali ile huku tukizidi kuchelewa kufanikisha yetu?” aliongea Dr. Lee huku kichwa chake kikiwa kimelalia bega la kushoto kama ilivyo ada. Ilihitaji utulivu mkubwa kumsikiliza mzee huyo ambaye sauti yake ilikuwa ikitoka kwenye kimashine maalumu kilichokuwa kimebandikwa kwenye tundu moja dogo sana chini ya kidevu. Huwezi kutambua hilo kutokana na kuzibwa na kitambaa kisafi kila muda huku usoni akiwa na kinyago kilichofunika uso wake.

“kuna njia yoyote labda ambayo mtu anayo kati yetu ili tuweze kuijadili mahali hapa” alisema Bencov baada ya kichwa chake pia kugoma kufanya kazi, hali ya Tereza iliwachanganya sana na hawakujua nini wafanye ili binti yule aweze kuwa sawa kisha kukamilisha kazi yao waliyoikusudia kuifanya. Tereza alikuwa amekonda sana pale kitandani, muda wote alikuwa akilia na kulitaja jina la baba yake hakukuwa na jina jingine, muda mwingine aliijutia hata taaluma yake na kuiyona kuwa hiyo ndiyo sababu ya kila kitu kwenye maisha yake. Kimya kilikuwa kimetanda pale ndani kwenye kile kikao kidogo cha kujadili hali ya binti waliyekuwa wakiuhitaji uhai wake kwa ajili ya vifo vya mamilioni ya watu.

“hakuna mwenye wazo?” aliuliza tena Bencov. Si Merina, Lonto msaidizi wa Merina bwana mwenye sura ngumu iliyojaa ngeu na makunyazi ya kutisha, Dr. Lee pamoja na huyo Benvov ambaye alikuwa tayari kutoa wazo lenye tija. Hiyo ilimaanisha kuwa sasa ngoma ni nzito kwao.

“jamani samahani” ilikuwa ni sauti ya dokta Henry aliyeingia mahali hapo na kuomba samahani kwa kile kilichoitwa kuharibu kikao cha watu. Wote pale wakamgeukia na kumtazama kwa mshangao wenye alama ya kuuliza juu, Benvov alishindwa kabisa kukaa kitini ikabidi kuinuka na kumuuliza dokta nini kibaya kimejiri huko, hawakutaka kusikia kitu kibaya kimemkuta Tereza. Hilo jambo walilipinga sana.

“hakuna kibaya kilichokea” akasema Dr. Henry, pumzi zikashushwa kisha Bencov akauliza nini kimejiri sasa kwa wakati huo akiwa anakaa kitini baada ya kujua kuwa Tereza yuko salama. Dr. Henry akasema.

“kwa kulazimisha binti yule afanye mlichokipanga itashindikana” hilo hawakulitilia maanani sana kwani hata kikao hicho walikaa kwa ajili ya kujadili hilo, walichotaka kusikia ni nini wafanye sasa. ….

Macho yote na masikio manane yakamuelekea daktari kujua ni kipi chenye msaada ambacho wanaweza kukifanya.

“anasema” akaendelea dokta.

“hatofanya chochote hadi kifo chake kama hataletewa baba yake hapa na kuishi nae” akatulia Dr. Henry. Pumzi za matumaini na furaha zikaibuka kila mmoja akabaki na amani ya kuuuona ushindi mnono.

“hilo niachieni mimi, kesho usiku ama mchana Backa anakuwa hapa na huyo mlinzi wake” alisema Bencov.

“mlinzi wake wa nini sasa?” aliuliza Dr. Lee.

“najua akishamuona baba yake anaweza pia kugoma kutufanyia hiyo kazi yetu sasa mimi nataka kumfanya huyo mlinzi ni kama kitisho kwake ili awe muoga” alitamba Bencov kibabe kabisa na kujiamini kwa hali ya juu. Wakakubali hiyo plani lakini walitaka iwe haraka zaidi. Hilo likawa halina shaka mbele ya kijana huyo mdogo mwenye hasira nyingi kwa Backa bila sisi kujua ni kwanini anahasira naye, leo anaachiwa rungu la kumtia Backa mikononi. Hatari kubwa.

Lakini kwa upande mwingine usiku huo huo kwenye mlango mkuu wa Hospitali ya rufaa ya Pande, kuna mtu alikuwa akiingia taratibu huku akiwa hana wasiwasi kabisa. Aliingia ndani ya hiyo hospitali kwa upole mkubwa, alikuwa ndani ya koti la rangi nyekundu chini akiwa amevaa viatu ambavyo vilikuwa havipigi kelele pindi anapotua chini au anapokanyaga mguu wake chini. Aliongoza moja kwa moja hadi mapokezi akachungulia kwenye kidirisha kidogo akamuona dada mmoja mwenye vazi la kiuguzi akiwa amepitiwa na usingizi. Kazi za usiku siyo mchezo. Aliwaza kisha akagonga kidogo ili kumuamsha, yule dada akashtuka

“nini…..mmmmm mm….ni nani?” akaweweseka.

“habari yako?” akasalimia huyo mtu. Yule dada badala ya kutoa salamu, akapiga kite cha hasira na kero ya kushtuliwa kwenye kisima chake cha ndoto za kuuota umasikini na kadhia ya mshahara wake mdogo usiokidhi haja.

“kuna dokta yoyote usiku huu?” akauliza swali yule kijana hakujali kutokujibiwa kwa salamu yake. Yule dada akachungulia kwenye kile kidirisha akakutana na macho mekundu yaliyotangaza kuwa muda si mrefu mtu huyo alitoka kupata pafu kadhaa za msokoto wa bangi.

“mgh!…..pita hapo kwenye hicho kikorido kushoto, tazama kushoto kuna mlango utaona” alijibu kishari shari yule dada kisha akajilaza tena pale kitini huku akipiga kite cha uchovu, hakudhani kama ile ndoto iliyokuwa ikimfariji, ingejirudia tena. Yule kijana hakushughulika na yule muuguzi tena alipita kwenye ile njia aliyolekezwa kushoto akaona huo mlango akagonga kidogo na kutega sikio kwenye tundu la ufunguo, akasikia minong’ono kutokea ndani.

“ngoja kwanza, msikilize huyo mgongaji kisha tutaendelea” kisha neno karibu pita mlango ukowazi likasikika. Yule mtu akanyonga kitasa na kuusukuma huo mlango ukafunguka. Macho ya yule mtu yakamuona mwanaume na mwanamke aliye katika vazi la kiuguzi wakiwa katika macho ya kulegea japo walijaribu kuyakaza.

“hii ndiyo dunia, kumbe zamu za usiku zina mambo” akili ya yule mtu ikasema.

“karibu ukae kiti hicho, tukusaidie tafadhali”

“nahitaji kuongea na daktari pekee tafadhari” akasema yule mtu.

“unaweza kuongea tu kwani…..!”

“wewe upo kazini na mimi nipo kazini, tusichanganye mambo mengine na kazi” akaweka kibesi kidogo yule mtu kisha akamkazia macho yule mwanaume, macho pekee yalionya kuwa hapo hayupo kwa kuomba undugu au urafiki bali yupo kwa kazi maalumu. Yule mwanaume akagwaya kidogo kisha akamtazama yule mwanamke kwa macho ya kumwambia nenda halafu urudi huyu mwehu akishatoka. Yule mwanamke akakunja sura na mdomo kama yale magari ya zamani ya kubebea magogo ‘Masisu’ kisha akatoka kwa maringo yaliyozidiwa na hasira akauvuta mlango kwa nguvu ukapiga kelele Baaa!

“nikusaidie nini sasa?” alisema kwa hasira kidogo.

“unaweza kuniambia daktari aliyefanya uchunguzi wa maiti tatu zilizokuja kwenye hospitali hii siku tatu ama nne zilizopita?” akasema yule mtu na kumfanya yule dokta kushtuka kidogo. Hakusema kitu akazidi kumkazia macho.

“ok, naitwa Inspekta Bogo ni afisa mpelelezi wa Jeshi la polisi kutoka hapa hapa Pande, niko hapa kwa ajili ya kuchunguza sababu ya vifo vya wale marehemu watatu ambao wamehifadhiwa hapa na kuzuiwa kwenu kuwa wasitolewe hadi uchunguzi utakapo kamilika. Kumbuka kuwa hili jambo ni siri kubwa na ndiyo maana hata taarifa ya kuizuia hiyo miili imekuja kwa siri kwenu” akatulia na kumtazama huyo bwana ambaye kwa muda huo aliitoa mawani yake ya macho na kuiweka pembeni kisha akasema.

“hivyo ndivyo waungwana wafanyavyo. Jina langu ni Albert unaweza kuniita dokta Albert.” akaweka kituo kikubwa kisha akatulia kidogo na kumtazama huyo bwana aliyejitambulisha kama Inspekta Bogo kisha akaruhusu maongezi yaendelee baada ya kukubali kuwa yeye ndiye aliyepewa jukumu la siri na serikali ya kuichunguza hiyo miili ya wale wapelelezi kutoka Tanzania waliopata ajali na yule aliyeuwawa kikatili.

“ok, ni vema ukanipa hizo ripoti sasa nizipitie au niondoke nazo” akasema Inspekta Bogo baada ya kutoa vitambulisho vinavyomtambulisha. Dr. Albert akanyanyuka kitini kisha akamwambia yule bwana amfuate, wakatoka wakaongozana hadi kwenye chumba kingine kilichokuwa na taa yenye mwanga hafifu. Hapo akavuta mtoto wa meza moja na kuchomoa karatasi zenye ukubwa wa A4 mbili akachukua na bahasha ya khaki akamkabidhi yule Inspekta. Isp. Bogo alizitazama kwa macho zile karatasi kisha akaahidi kurudi atakapo hitaji msaada zaidi. Alizitumbukiza zile karatasi kwenye bahasha kisha akatoka hadi nje kabisa ya ile hospitali akadandia pikipiki lake na kutitia gizani. Alikuja kutokea kwenye nyumba moja kubwa kiasi mtaa wa Kanisa kuu la KKKT, hapa akapaki pikipiki yake mbali pia na eneo nyumba ile ilipo kisha akabiga hatua za tahadahari hadi karibu kidogo na geti kuu akaona walinzi wakiwa kwenye sare zao za kazi huku wakiwa na silaha kali za moto. Akatafakari kwa muda kisha akachukua hatua moja ndogo kwenda upande wa nyuma wa ile nyumba. Alipofika nyuma, akajivuta kwa kasi na kudandia ule ukuta akaangukia upande wa ndani bila kupiga kelele yoyote. Akapokelewa na mauwa mengi marefu kisha akaambaa na yale mauwa hadi sehemu iliyo na miti iliyostawi majani akapenya na kuingia kwenye kibanda cha makuti kilichomo mule ndani ya ule uzio. Kibanda hicho kilikuwa ni kwa ajili ya kupumzika tu. Insp. Bogo alipofika mule ndani akapokelewa na mtu aliye katika mavazi ya kulalia. IGP Liyambo.

“mkuu, tayari ripoti mikononi mwangu lakini siyo nzito sana kwa sababu haziniweki karibu na muuwaji au wauwaji kama siyo waliotekeleza mauwaji” alisema Bogo kumwambia IGP Liyambo, mkuu wake wa kazi.

“nenda Muavengero kwenye hii nyumba, nyumba hii haina uzio kama unavyoiona ukifika gonga dirisha hili hapa kisha liza funguo zako za pikipiki au kama unacoin zozote zile mara baada ya kama sekunde tatu za kugonga mlango kisha subiri hapo. Mtu huyo akitoka mpe hii picha na yeye atakupa ripoti. Nakuaminia kijana unajua kila unachotakiwa kufanya na ni muelewa na ndiyo maana nakupenda sana. Pitia ripoti atakayokupa halafu mimi na wewe tutakutana mahali tunapokutania kesho mchana” alisema IGP.

“ok, mkuu, Usiku mwema” aliaga Inspekta Bogo kisha Liyambo akamtakia safari njema ya kuitafuta haki. Bogo akatoka mule ndani kwa njia aliyoingilia hakutaka kuonekana hata na walinzi wa ile nyumba ya IGP kwani hawakuwa wakimuamini askari yeyote yule na hata yeye mwenye hakuwapo kazini alipewa likizo ya miezi mitatu ikiwa ni katika kuzifuatilia kesi hizo za kutisha chinichini. Alifika katika nyumba aliyoelekezwa na kufanya kama alivyoagizwa.



Asubuhi ilimkuta Inspekta Bogo nyumbani kwake akiwa mezani, alikuwa akizisoma karatasi zote taratibu sana akagundua machache makubwa kwenye zile karatasi. Kwanza ni kuhusu vifo vya wale wapelelezi, vifo vile pasi na shaka lolote vimetengezwa kwani ripoti ya daktari ilisema kuwa kwenye moyo wa mpelelezi mmoja, kumekutwa risasi, hii ni kwa mwili wa askari mmoja.

Alizisikia hizo taarifa juu na zilikuwa ni taarifa za harakaharaka ambazo Rais alizihitaji, akataka kupata ripoti za uhakika na za kueleweka. IGP Liyambo akaweka watu wa siri ambao walimuendea Dr. Albert na kumtaka aifanyie uchunguzi miili yote kisha akamwambia kuwa kuna mtu wake angekwenda kuyafuata.

Karatasi hizo Bogo akaziweka chini kisha akachukua zile za uchunguzi wa kipolisi ambazo alizifuata usiku kule alikoelekezwa na Mkuu wake wa kazi. Hizi hazikumpa ufunbuzi wowote kwani wauwaji walikuwa makini na hatari mno lakini alipoangalia chunguzi za kifo cha Ndungai, akakuta ugunduzi wa alana za vidole (finger print). Akataka kujua undani wa kile kitu akagundua kuwa alama hizo zilipatikana kwenye kisu alichokiacha muuwaji. Akataka picha ya mtu mwenye alama hizo. Akakuta picha ya kijana wa marehemu, aaama!

“inakuwaje hii? Inamaana mtoto amemuuwa baba yake, si kweli hii ni ngumu sasa aaahgr!” akang’aka Ispekta Bogo lakini hakukata tamaa. Hata kama muuwaji alikuwa na akili kiasi gani lakini ilikuwa ni lazima amtie mikononi. Akajilaza kitini kidogo, usingizi nao ukamwambia jana usiku ulikuwa unanikwepa leo nimekukamata, kijana huyo akakubali hiyo hatia, usingizi ukambeba palepale kitini, akatopea katika kulala.

Baada ya masaa kadha wa kadha kupita, jioni ya siku hiyo ambayo mambo kwa upande wa Inspekta Bogo yalikuwa yanaanza kwa ugumu wa aina yake, hapo hapo kuna watu walikuwa njiani wakiwa wanaelekea ndani ya Backa Island. Hawa hawakuwa wema hata kidogo na walikuwa ni vijana watatu katili mno. Vijana wenye majina yenye maana kubwa kwa kijana Bencov. Alikuwepo Bacon, Benson na Dede ambao walitengeneza herufi tatu za ‘B.B.D’ Bencov baada ya kupokea ile Odar aliyoomba aachiwe yeye, aliwapa taarifa vijana wake ya kuwataka wasipoteze muda waelekee haraka kwenye kisiwa cha Tajiri huyo kisha wahakikishe wanauwa kila kiumbe watakayemkuta kisha wawaweke chini ya ulinzi Backa na mtu wake wa karibu. Wakisha maliza watoe taarifa na ndege ndogo iendayo kasi ingefika hapo muda mfupi. Vijana hao watatu walikuwa chini ya kichaka cha Mikoko wakiwa kwenye mavazi na vifaa vya kuogelea, hawakutaka kutumia njia ya kawaida ya kwenda na Boti kwenye kisiwa kile kwani ulinzi wake ulikuwa macho zaidi na pia kuna baadhi ya sehemu ziliongezewa ulinzi wa kamera. Kila mmoja aliweka mtungi wake wa gesi ya Oxygen mgongoni kisha wakapokea ishara na Bacon mahali ambapo walitakiwa kutokea. Wakajitosa majini na kuomba maji hayo yawafiche. Maji ya bahari hayakujua kinachokwenda kutokea kwa Backa hivyo bila hiyana yakawaficha wale vijana watatu na kuwapoteza kabisa kwenye macho makali ya kamera za ulinzi za Backa zilizojaa kisiwani pale. Bacon, Benson na Dede, walikata maji kwa ufundi mkubwa hadi walipokuja kutokea kwenye kingo moja kubwa hapa kwa haraka na kasi kubwa wakaibuka kwa nguvu na kila mmoja akamdaka mlinzi aliyekuwa akitazama baharini. Ilikuwa ni kasi kubwa na wale wajinga walicheza na akili za kamera zile. Kwani kamera zilipozunguuka tu wao wakaibuka na kufanya yao. Dakika moja kasoro, ile miili ya walinzi wale ilionekana kwa juu ikielea hiyo ilimaanisha kuwa hawakuwa na uhai tena. Ilivutwa pembeni ya maji bila wavutaji kuonekana kisha ikaenda kupachikwa kwenye seng’enge zilizopo pembeni. wale vijana wakatulia tena. Muda si muda wakaibuka tena kwa pamoja na silaha mikoni mwao mithili ya Bastola na kuzilenga zile kamera zote za eneo lile…….

“kamera za upande wa kaskazini zimevamiwa na walinzi wa kule hawaonekani bila shaka watakuwa matatizoni, kuweni makini na mkuu awekwe kwenye usalama” alisema mtu mmoja kutokea kwenye chumba maalumu cha kuongozea kamera za ulinzi. Hakuna jibu alilolipata kutoka kwa aliyempa hizo taarifa zaidi ya mguno na sauti za maumivu, hiyo ilikuwa inamaanisha kuwa alichelewa ikabidi atoke mwenyewe ili kutoa taarifa, ni kweli alifanikiwa kumpa Phili taarifa hizo lakini alipotoka nje, aliwarahisishia kazi wavamizi. Risasi moja iliyopiga upaja ikamrusha umbali mkubwa na kumpigiza kwenye mlango, akaingia nao ndani kisha kutulia kimya. Ilikuwa ni silaha mbaya kutoka kwenye mikono ya Bencov, silaha yenye kukutesa kabla ya kukuuwa na inakuuwa taratibu sana ambayo ni ndani ya masaa thelathini na sita mpaka sabini na mbili hivi ndipo unakufa na kupotea kabisa kisha mifupa yako ndiyo itaokotwa baada ya kuvuja damu nyingi na kupasuka kwa moyo. Watu hao walikuwa na kasi kubwa kuliko kawaida, walikuwa makini mno.

“kusini, mashariki” alisema Bacon. Wale wenzake wakaelewa nini walitakiwa kufanya wakagawana haraka sana, sauti nyingine ikasikika.

“tukikutana hapa tuwe tumesha warudisha viumbe wema wa Mungu njia ya kwenda kuzimu” wakatawanyika. Walinzi wa Backa walimwaga njugu kama hawana akili vizuri lakini hawakujua walikuwa wakimpiga nani kwa wakati huo. Wakipiga mbele, wanashambuliwa nyuma na walikuwa wakipigwa kwa kasi ambayo hawakuwahi kuiona katika maisha yao yote.

“boss, nifuate mimi tuondoke hapa, huko nje hali ni tete na haijulikani kama kuna kijana wetu ambaye atapona hata mmoja” alisema Phili kumwambia mh. Backa lakini Backa hakuthubutu kupiga hata hatua moja mbele, alitulia kimya huku akiwa amefumba macho hapo sebuleni kwake.

“tuondoke mkuu hali ni mbaya na haijulikani hawa maadui wanavamia na nini maana wanapiga kwenye paja ama miguuni au begani lakini huwezi kufurukuta na unarushwa mbali sana, sijawahi ona silaha za namna hiyo mimi boss. Niamini mimi Boss hatuwezi kupona hapa” alizidi kulalamika Phili, alishaiona hali jinsi ilivyo mbaya lakini Backa bado hakutaka kuondoka mahali hapo hata kidogo.

“mpe taarifa IGP, mwambie wamekuja tena na safari hii wameuwa hadi Inzi na wananitaka mimi” aliongea Backa kisha akafumbua macho yake sasa na kumtazama Phili ambaye alikuwa akifanya alichoagizwa. Aliongea kama alivyoelekezwa kisha akaiweka simu mahali ambapo aliamini hakuna mtu atakayeiona kirahisi pasipo kuikata kwa hiyo IGP alikuwa akisikia kila kitu. Akapiga simu kutoa taarifa na kuwataka askari waelekee huko kwenye tukio kisha akatuli pale kitini akiwa amechanganyikiwa huku ile simu ikiendelea kumpa kila kitu kinachojiri huko kwa Backa Island. Akaweka Rekodi kabisa ili uwe ni ushahidi kwake.

“fanya kila juhudi uondoke hili eneo na uniache mimi Phili. Hawa watu wanaweza kukuuwa, hawapo hapa kwa ajili yako wapo kwa ajili ya mimi tu” alisema Backa akimtaka Phili aondoke haraka sana hilo eneo lakini kijana huyo hakuthubutu kufanya hivyo hata kidogo, alichoking’ang’ania ni kuondoka na boss wake tu.

“ondoka kupitia mlango wa siri wewe na uchukue honda ukimbie hapa, niache mimi hapa hata kama nikifa ni sawa tu. Siwezi kuondoka hapa nahitaji kuonana na mwanagu mimi” aliongea Backa akiwa hatanii hata kidogo mahali hapo kisha akafumba macho yake tena kuwasubiri hao watu. Phili aliposikia kuwa Bosi wake alikuwa akihitaji kwenda kuonana na binti yake akajua hapo hakuna safari ya kutoroka, akaona ni bora afanye jaribio la kujaribu kupambana na hao watu kama anaweza kufanikiwa. Akachomoa bastola yake ndogo kisha akatoka kwa kasi kubwa na kurusha risasi kule ambako aliwaona wale watu, mguno wa maumivu ukasikika kutoka kwa mmoja na kudondoka chini lakini macho yake yalipotazama pale walipokuwa wamesimama wale watu, macho yalimtoka baada ya kuona kifusi cha miili ya askari waliokuwa lindo ikiwa inavuja damu kama bomba lililoharibika huku watu hao wakiwa wanagaagaa chini kwa maumivu makali. Bastola ile ilimtoka mikononi na kudondoka chini aliwashuhudia wale wawili waliosimama wakigeuka kila mmoja akiwa amekamata kichwa cha mtu mkononi mwake. Aisee! aliogopa vibaya sana, mwili wote ukawa unamtetemeka. Ujasiri wa kiaskari ndiwo uliokuwa ukimsaidia mahali pale laiti kama isingekuwa hivyo, angekuwa yu chapachapa kwa choo kidogo na kinyesi. Walikuwa wakimfuata wale watu waliokuwa wamevaa mavazi yenye kofia. Matabasamu ya kukera na kuogopesha ndiyo yaliyokuwa yakizidi kumchokolea hofu iliyobaki moyoni. Akamkumbuka boss wake. Akajikuta akipata ujasiri wa kuingia ndani Phili huku akichomoa bastola nyingine huku akiwasubiri waingie tu ili awashughulikie Lakini haikuwa hivyo kwani alichokitegemea sicho kilichotokea, alishangaa kuona vichwa viwili vya binadamu vikija kule aliko yeye, akahamanika na kupoteza ujasiri wa kile alichotaka kukifanya. Akiwa anazidi kubabaika, alishtukia akipokea mateke mawili yaliyotua kifuani yaliyomrudisha nyuma kidogo. Huyo alikuwa ni Dede dada hatari aliyejichafua mwili wake kwa kujichorachora mapicha na mistari ya ajabu ajabu. Alikuwa na hasira za kuzidi sana na hiyo ni baada ya mpenzi wake Benson kujeruhuwa na kijana huyo. Bacon yeye alikuwa amesimama karibu na mlango akitazama mpambano wa watu wale wawili. Phili alijiweka kimapambano huku akimtazama huyo dada kwa macho ya kumsoma. Alipojaribu kumvaa kwa mapigo yake ya karate alijikuta akipokea kipingamizi kutoka kwa dada huyo ambaye alikosa kabisa urafiki na tabasamu. Phili alipokea mapigo ya ajabu ajabu yaliyomnyima nguvu kwa muda mfupi tu. Phili aliamua kubadilisha mapigo alimrukia Dede kwa mtindo wa Snake jump kisha akamzunguka kwa nyuma na kumpa huyo binti kabali kali sana kiasi cha kumkosesha pumzi. Ilikuwa ni kabali ya kuondoka na maisha ya huyo binti kabisa lakini Phili alipigwa Teke zito lililopiga nyuma ya goti na kumfanya ahisi maumivu makali huku mikono ikikosa nguvu ya kuweza kushika vizuri. Dede akageuka na kifuti safi kilichomkuta Phili kidevuni akabweka kama Mbwa na kudondoka chini. Hapo hapo walifunga kamba kisha wakamfunga na Backa. Backa alikuwa akitokwa na machozi huku akimlaumu Phili kwa kitendo chake cha kuwa mkaidi. Walitolewa nje ambako walimkuta Benson akiwa amesimama palepale kwenye kifusi cha ile miili ya watu. Bwawa kubwa la damu lilikuwa limejaa pale. Bado ile miili ilikuwa ikitoa damu si ndogo.

“Mungu wangu hii ni dunia au kuzimu?” alijiuliza Backa kwa sauti ya chini sana baada ya kuishuhudia ile miili pale chini jinsi inavyovuja damu.

“vipi ukosalama Benson?” aliuliza Bacon.

“nikosalama na tayari nimeshawasiliana na jamaa waje kuchukua mizigo yao” alijibu Benson huku akimsogelea Phili akambana mdomo na kumpa konde kubwa la mdomo. Phili aliyumba huku akitokwa na damu kinywani mwake, Backa aliumia sana lakini hakuwa na jinsi mahali hapo.

“mpuuzi wewe ulitaka kuniuwa wewe si ndiyo?” alibwata kisha akamuacha baada ya kusikika mlio wa Ndege ikija mahali hapo. Muda si mrefu Ndege hiyo ndogo ilisimama juu ya ardhi hiyo ya Backa. Wakasukumwa hadi ndani ya hiyo Ndege. Wakaagana na wale vijana waliokuja na Ndege wakaondoka zao kisha Bacon akamtazama Benson na kumuuliza kama ataweza kuogelea akasema yuko fiti kwani risasi ile haikuwa imemdhuru sana. wakapotea pale kwa kurudi kwa njia ile waliyojia. Muda mfupi baada ya wale vijana wa Bencov kuondoka, Helkopta kubwa ya jeshi la polisi ilifika hapo kisha polisi wengi wakashuka wakiwa na silaha mkononi.

“oh! My god!” alisema askari mmoja baada ya kushuhudia miili iliyokuwa ikivuja damu si kawaida.

“jaribuni kuzunguka kila eneo la jumba hili muangalie kama hawa watu wapo” alitoa amri kiongozi wa wale askari. Mtawanyiko ukafuatia huku SMG zikiwa tayari kwa lolote mikononi mwao.

“aisee huu ni unyama mkubwa sana….lakini mbona kama wanahema, hawa ni wazima afande!” alistaajabu yule kiongozi na kuzidi kushangaa zaidi baada ya kuona watu wale wakiwa bado wanapumua.

“aisee! Ni kweli sasa hii nini maana yake, hawa watu ni hatari sana na silaha walizotumia si za dunia hii kabisa” alisema askari mwengine.

“hebu leteni vifaa vya kuwahifadhi hawa tuwawahishe hospitali haraka sana” alitoa amri kiongozi, vijana wakaelekea kwenye Helkopta ile kisha wakarudi wakiwa na nailoni ngumu. Vijana wakavaa Gloves na kisha kuitumbukiza ile miili kwenye zile nailoni wakafunga na zipu wakiacha sehemu za usoni tu kwa ajili ya kuwapatia hewa japo wenyewe walionekana kuitafuta hewa kwa shida sana. wakawaingiza ndani ya Helkopta.

“afande kila kona tumeangalia hatujaona hata kitu chochote” alisema askari mmoja.

“hata muheshimiwa hamjamuona?” akauliza yule kiongozi.

“hakuna mkuu bila shaka wameondoka nae” alijibu. Alihamanika sana yule kiongozi kisha akatoa simu ya upepo na kupiga mahali.

“afande, muheshimiwa ametekwa na askari wote wameshambuliwa kwa silaha ambazo sijui kama mtengenezaji wake anaishi duniani” alisema.

“unamaanisha….hebu ngoja, askari wangu wameuwawa au?” iliuliza sauti ya upande wa pili ikiwa katika taharuki kubwa. Kama Backa ametekwa aliamini kabisa kuwa hata askari wake watakuwa si wazima.

“hapana afande askari ni wazima lakini wanaonekana hawatadumu katika uzima huo, wanavuja damu mwili mzima”

“wawahishe hospitali haraka sana mbona mnawachelewesha sasa” IGP aliishusha simu ya upepo chini na kuiacha ikiwa inakoroma tu, aliishusha chini huku akiwa kagandisha macho kwenye kalenda kubwa iliyopo ukutani. Kalenda hiyo ilikuwa na picha ya mh. Backa pamoja na viongozi mbalimbali wakiwa wapo katika tabasamu kubwa sana. Aliikumbuka picha hiyo kipindi yeye akiwa ni Askari mwenye cheo cha Inspekta tu kabla ya kutunukiwa cheo hicho kibwa kabisa cha Inspekta Jenerali wa polisi IGP. Chozi la uchungu lilimdondoka bwana huyo anayekaribia kuachwa na ujana kwa masika mbili au tatu zijazo. Alishusha pumzi kubwa kisha akaitazama simu ile kwa muda tu, alikuwa amechoka vibaya mno. Nimeshindwa kukulinda muheshimiwa, kwanini sasa nimeshindwa? Kwanini aaah!” aliwaza IGP Liyambo. Mawazo yalikuwa lukuki mno lakini mawazo hayo yalikuja kukatika baada ya taarifa ya habari ya muda huo kurindima akiwa mahali hapo.

‘watu wasiofahamika wavamia Backa Island na kumteka mmiliki wa kisiwa hicho, wavamizi hao inasemekana ni wale wale waliowahi kumteka binti huyo mwenye taaluma kubwa ya utengenezaji wa madawa mbalimbali ya wanyama na binamu kwa kutumia mimea asilia. Hadi sasa Serikali haijatoa tamko lolote kuhusiana na utekaji nyara huo……!’

“aaaaah! shit!” aliizima hiyo luninga IGP baada ya kuona ni jinsi gani Taifa hilo litakavyomuona mzembe.

“binti anatekwa serikali haitoi tamko, vifo vya wapelelezi kutoka Tanzania pia serikali haijatoa tamko lolote kuhusiana na hicho kitu na leo ni mh. Backa mwenyewe. Lazima wataho…..!” hakumaliza alichokuwa akikiongea mahali hapo yeye mwenyewe Liyambo baada ya simu kuingia. Akaitazama kwa tuo kidogo IGP huyo kisha akanyanyua mkonga wa hiyo simu akaiweka sikioni na kusikiliza sauti.

“tulikuonya ukajua tunaongopa. Hebu fanya hima, msimamishe huyo mtu wako wa siri sijui ni mpelelezi sijui ni nani kisha uache tabia za kuwa na dharau. Kwani ni nani amekwambia uweke mpelelezi sijui mtu wa siri wa kufuatilia mambo yetu? Tulikuambia kesi ya Backa tuachie sisi lakini hukusikia. Nenda Gonja Forest utakuta kichwa cha baba yako

na kiwiliwili utakikuta nyuma ya uzio wa nyumba yako. Hilo ni onyo la vitendo ila kama hutasikia basi utakuwa umehalalisha kifo cha mama yako” sauti ile nzito ikakatika baada ya kutoa maelezo yale ya vitisho. IGP alijikuta akikosa pumzi, alihisi kama moyo unataka kutoka mwilini mwake na kutaka kukimbia riadha. Kelele alishindwa kupiga wala kulia pia alishindwa.

“baba…baba jamani, babaaaaaaaaa!” alinyanyuka pale kitini na kupiga kelele mfululizo akiliita jina la baba yake. Akatoka na kuufuata mlango alipougusa tu huo mlango simu ikaita tena kwa fujo.

“atakuwa ni yule yule, mama au?” akajiuliza IGP huku akiwa anaiogopa ile simu. Akataka kutoka na kuiacha ile simu iendelee kuita kama ikipenda kukatika basi ijikatikie yenyewe. Amuzi hilo hakuliona kama litakuwa ni la maana sana, ile ni ofisi ya kiusalama tena yakiwa ni makao makuu ya polisi hivyo simu za muheshimiwa Rai huwa zinaingia moja kwa moja ndani ya ofisi hiyo. Akarudi na kuinyakua.

“halow!” upande wa pili ukaanza, alikuwa ni Mh. Rais Mabandu.

“mkuu baba yangu” akasema Liyambo.

“Backa yuko hospitali pia au?” eti Rais anauliza hilo swali la kijinga kabisa, inamaana ile taarifa ya habari ambayo haijulikani mpelekaji wa taarifa ile ni nani na wakati vijana wake walisema kuwa hakukuwa na muandishi wa habari hata mmoja. Leo anauliza Backa yuko hospitali, laiti kama Liyambo asingelikuwa kachanganyikiwa basi huwenda angejua mkuu wa nchi anakabiliwa na uchizi kama siyo kichaa cha Mbwa.

“hapana ni baba yangu”

“kwaiyo baba yako ndiyo yuko hospitali si ndiyo? Sasa kuhusu Backa?” ailiuliza Rais Mabandu kisha kimya kikakita. mihemo ya kukata tamaa kati ya watu hawa wawili ambao ndiyo wanaoaminiana, ndiyo iliyokuwa ikisikika mahali hapo.

“hapana mkuu muheshimiwa ametekwa lakini nimepokea simu ambayo imenipa taarifa ya kifo cha baba yangu.” alijibu IGP Liyambo baada ya kupata utulivu wa akili.

“Mungu wangu sasa tunafanyaje Liyambo” alihoji mh. Rais.

“mimi sijui mkuu ilaaa, inabidi uite viongozi wote wakuu wa serikali na wahojiwe juu ya hili baada ya kikao kile cha kwanza kushindikana, maana siwaelewi kabisa, mbona wanakuwa kimya hivi lazima waziri wa ulinzi naye atoe majibu juu ya jambo hili” alisema Liyambo kisha simu hiyo ikakatika.

IKULU.

Mh. Rais alikuwa ametulia kama mwanamkiwa kwenye kiti chake kikubwa ofisini kwake. Alikuwa akiumiza sana kichwa juu ya jambo hilo na alitakiwa kufanya jambo gumu ikiwezekana. Yeye ni mtu wa mwisho na wananchi wote wa Ungamo wanamtazama yeye. Hakuona njia ya kupita zaidi ya kufanya maamuzi magumu aliona ni bora kujitoa ufahamu kuliko kufanywa zoba namna hiyo.

“lazima Bande Sir anipe maelezo yaliyoshiba kuhusiana na kupunguza walinzi kwa Backa. Nilivunja kikao kile nilichotaka kuongea nae yeye tu na IGP lakini sasa ni lazima atoe jibu mbele ya jopo la viongozi wakuu wa serikali kuhusiana na hili, hii ni vita hii” alijisemea Rais Mabandu kisha akatulia Mara alarm iliyoashiria kuna mtu mlangoni ikasikika. Akatazama kwenye kompyuta yake akamuona ni mshauri wake, akaruhusu mlango ufunguke.

“mkuu……?” akaitwa.

“ambia mtoa taarifa awataarifu viongozi wote wakuu wa serikali kuhusu kikao cha kesho usiku ndani ya ukumbi wa mikutano hapahapa Ikulu” alisema Mabandu.

“sawa mkuu laki…..!”

“hakuna cha lakini bwanaa, mimi si ndiyo nimesema lakini mbona mnanidharau hivyo?…nenda nje bwana” alifoka Mh. Rais kisha akabonyeza kinobu cha kuufungua mlango ule na kumtazama usoni mshauri wake. yule bwana mwenye sura pana alimeza tu mate bila kuongeza neno akatoka. Ulikuwa ni mkanganyiko mkubwa wa mawazo, si Rais, si Inspekta Jenerali, wote walikuwa kwenye mambo magumu mno.

Jioni hiyo ilimkuta IGP kwenye hoslitali ya rufaa ya Pande akiwa ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti. Alishalia vya kutosha sasa muda huo alibaki kuumia tu juu ya mwili wa baba yake uliolala monchuari, ulimuumiza sana lakini alipohama na kupelekwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi, huko ndiko kilio kilipoanza upya. Miili ile ya vijana wake iliyokuwa ikipitia maumivu makali kwa kutokwa na damu nyingi kwenye miili yao ilimuumiza sana tena sana.

“mkuu inabidi uvumilie hata sisi tumeshangazwa sana na shambulizi la namna hii” alisema askari mmoja akimtia moyo mkuu wake wa kazi.

“mmegundua nini sasa?” aliuliza IGP akiwa mbele ya daktari.

“hii ni sumu mbaya sana ambayo bado tunaifanyia uchunguzi ili tujue ni sumu gani lakini sumu hii inashambulia zaidi mfumo wa damu na moyo mkuu.” akaweka tuo daktari huyo aliyeifanyia vipimo hiyo miili ya hao askari polisi walioshambuliwa hivyo kisha akaendelea na pale alipoishia.

“tumejaribu kuwapiga picha na kugundua kuwa moyo wa mtu aliyeshambuliwa na silaha hii…..!” alikatisha kile alichokuwa akikiongea daktari baada ya daktari mdogo kufika eneo hilo kwa haraka sana.

“dokta wagonjwa wanazima ghafla sana sijui ni nini hii, yaani wanakata roho huku wanamwagika damu nyingi sehemu zote zilizo wazi kama mdomo, puani na masikioni” alisema huyo daktari.

“shiit!” aling’aka dokta Albert baada ya kupokea taarifa hiyo lakini hapo walikuwa mbele ya kitanda cha mgonjwa wa aina hiyohiyo. Wakamtazama huyo mgonjwa kisha wakataka kuondoka hapo. IGP alikuwa akishuhudia kila kitu huku akiwa na mavazi ya kidaktari, ilikuwa ni lazima ashuhudie hali mbaya ya vijana wake ambao walikuwa wakifanya doria kwenye nyumba ya Backa. Walipopiga hatua tu, kukurukakara zikaanza kusikika kwenye kitanda cha huyo mgonjwa. Dr. Albert alikimbilia kuchukua kifaa cha kusaidia upumuaji, kilikuwa ni kifaa kidogo sana ambacho huwa kinasaidia hali hiyo kwa muda mfupi kisha huondolewa na kuwekwa mshine kubwa ya hewa ya Oxygen. Alikishika kile kifaa na kutaka kukiweka puani kwa yule mgonjwa ambaye alikuwa akihangaika mithili ya mtu aliyekabwa na kukosa pumzi kabisa. Alipokaribia tu kugusisha puani, yule mgonjwa akatoa sauti ya kama mtu anayekohoa au kupaliwa na kitu kisha kimya huku damu zikitoka kwa wingi puani na mdomoni. Dr. Albert akabaki kuganda na kile kifaa mkononi mwake kisha kukishusha taratibu hadi puani.

“tayari huyo dokta” alisema daktari msaidizi wa Albert. Dr. Albert hakusema kitu, alibaki kutoa macho huku akizishangaa zile damu zikimwagika kama maji yatokavyo kwenye bomba bovu. Alitoa macho dokta huyo kijana kisha akachukuwa kipimo chake cha kupimia mapigo ya moyo.

“hakuna kitu” alisema huku akizuia mwili huo usifunikwe. Akamgeukia IGP. IGP alikuwa akitokwa na machozi si utani hata kifo cha baba yake alikiona kina afadhali kuliko hicho alichokiona hapo.

“naomba hizo sampuli mlizochukua kwenye miili ya hawa marehemu muzidi kuzifanyia uchunguzi kisha ripoti mnipe, potelea mbali kisha nitakuhitaji ofisini kwako” aliongea IGP. Dr. Albert alimtazama msaidizi wake kisha akaomba asogezewe mtambo wa kupiga picha za X-RAy. Mtambo ukasogezwa akaanza kazi ya kuupiga picha ule mwili pale kitandani alitaka kujua ni madhara gani ambayo amepata zaidi, baada ya hapo alimkabidhi msaidizi wake huo mtambo kisha akamwambia kuwa asimamie zoezi la kuisafisha ile miili kwa ajili ya kuondoa damu halafu waichome sindaono ya Formalin kwa wingi ili miili hiyo isije kuharibika hadi pale taratibu zingine zitakapofanyika. Hilo lilikuwa kosa tena kosa kubwa ni bora tu wangechukua jukumu la kuizika ile miili kabla hayo mengine hayajatokea lakini ama kwa hakika usilolijua ni sawa na usiku wa kiza. IGP alitoka hapo kwenye chumba hicho maalumu akiwa ameongozana na Dr. Albert hadi kwenye ofisi ya Dr. Huyo.

“niambie daktari, hivi unajua ni kwanini baba yangu ameuwawa kinyama vile” swali ambalo alitakiwa kuulizwa yeye Liyambo kama mwana usalama, anamuuliza daktari. Ilikuwa ni vichekesho.

“hapana siwezi jua Afande.” alijibu kwa utulivu mkubwa sana dokta huyo lakini badala ya Liyambo kuendelea, aliuliza swali.

“ni nani alikuwepo wakati Inspekta Bogo amekuja kuchukua ripoti za uchunguzi za ile miili mitatu mikononi mwako?” Dr. Albert akatulia kidogo na kutoa mawani yake ya macho kisha akahema kwa nguvu kidogo.

“kwanini unauliza hivyo mkuu?”

“wewe ukiuliza na mimi nikiuliza, hatutapata ufumbuzi wa ninachokitaka hebu niambie tu” aliwahi Lyliyambo kwa kumzuia huyo Dokta asizidi kuuliza maswali.

“hakukuwa na mtu yeyeyote yule mkuu” alijibu Dokta lakini kichwani mwake alianza kuhisi kitu ambacho si salama.

“nilitaka kazi hii tuifanye kwa siri kubwa lakini siri hiyo umeivunja miiko yake Albert. Tazama baba yangu mzazi anavyoungua na baridi kali ya kwenye Jokofu la kuhifadhia maiti huku akiwa anasitiriwa na zile nyuzi mlizomshona ili aonekane alikuwa na kichwa chake, lakini kiukweli alikufa kifo cha kifisadi kabisa, ndiyo, amefisidiwa kifo…..ni wewe ulikataa kuitunza siri Albert. Sasa nimuamini nani, mbona hili Taifa limejaa ‘Mashilawadu’ eeenh!” alilalama sana IGP, alikuwa akishindana na dukuduku la kutaka hata kuuwa eneo hilo aisee! sema ni busara tu alizokuwa nazo.

“ngoja nimekumbuka kitu”

“eenhee! Hicho ulichokikumbuka ndicho ninachokitaka” alidakia IGP Liyambo kisha kumkazia macho daktari huyo mzalendo na anayemuamini sana japo alishaanza kuvunja imani juu yake.

“wakati Bogo anaingia hapa ofini kwangu nilikuwa na binti ambaye hata wewe umemuona wakati tunaingia humu ndani, alikuwa mkono wa kushoto mapokezi pale, yule ndiye niliyekuwa naye usiku huo”

“basi inatosha” akasimama Liyambo kisha akapiga hatua moja kubwa hadi alipoufikia mlango kisha akageuza shingo yake akasema.

“Taifa ni chafu kwa sasa, umeshaamua kuwa mzalendo chunga sana roho yako wanaweza kuifanya Andazi la shughuli” kisha IGP akatoka humo ndani kwa kuuacha mlango ujirudishe wenyewe. Alipofika lile eneo ambalo wakati anaingia alimuona huyo binti anayeshukiwa kuwa ndiye aliyevujisha siri hiyo, hakumkuta, mh! akagumia kwa ndani na kujenga mashaka zaidi. Alikunja kona ya kumpeleka kwenye mlango mkubwa wa kutokea mule ndani, alipogeuka tu kuutazama ule mlango, macho kwa uso na binti aliyekuwa anaishusha simu yake chini.

“haba…..ri…..yako afande!” alisalimia kwa kujigongagonga kwa aibu ya kukutwa na mtu huyo lakini hakujua kama tayari ameshatiliwa mashaka tayari na kichwa makini cha IGP.

“salama” alijibu kwa ufupi huku akionekana kuwa na haraka sana hakutaka kukurupuka kudili na huyo mtu kwani alihitaji kuweka umakini na utahadhari juu ya kundi la watu hao.

Yalikuwa yamebakia masaa machache sana kuweza kufika muda wa kikao kizito, kikao ambacho kilikuwa maalumu kwa kumbana kwa maswali mazito waziri wa ulinzi ili wajue ni kitu gani kinahusiana na yeye juu ya yale mambo yasiyoeleweka. Ni takribani masaa mawili tu ambayo ndiyo yalisalia kufika muda huo uliokuwa ukihusudiwa. Rais Mabandu alikuwa ametulia kimya kwenye kiti chake, hakutaka kutoka kabisa ndani hadi muda wa kikao hicho kizito ufike. Lakini akiwa hapo ndani, simu yake ya mezani ikaita, akaitazama kwa muda kidogo kisha akanyanyua mkonga wa simu na kuipokea.

“binti yako yupo karibu yetu sana, tupo naye hapa, yupo kwenye mgahawa huu uliopo karibu na hiki chuo anachosoma. Anajipendeleea mwenyewe” sauti ilisikika kutoka simuni tena ilionekana muongeaji alikuwa akiongea kwa maringo makubwa sana.

“hebu nyoosha maneno wewe, binti yangu ana nini?” alifoka muheshimiwa.

“usifoke basi, unajua nilikuwa nataka kukuambia kuwa…..hapana, nilikuwa nataka kukuambia uachane na hicho kikao ulichotaka kukifanya wewe na viongozi wako, ni hilo tu” akasema mtu huyo wa upande wa pili wa simu. Rais Mabandu akakasirika sana kusikia maneno hayo akajikuta anakuja juu kwa sauti kali lakini hakusikia kitu kingine kilichokuwa kikiendelea badala yake kimya kilitanda tena kilitanda haswa. Akaitoa ile simu sikioni na kuitazama kama kuna kitu cha ajabu alichokuwa akikiona juu ya simu hiyo, mara akasikia sauti nyingi zilizokuwa zikisikika, muheshimiwa Rais akairudisha simu ile sikioni. Zilikuwa ni sauti zenye kuumiza masikio sana lakini Rais Mabandu wala hazikumkera ndiyo kwanza alikuwa akizidi kuikandamiza simu ile kwenye sikio lake kisha kimya tena, kimya hicho hakikudumu sana kilikuwa ni cha muda mfupi tu, sauti nzito tofauti na ile ya kwanza ikasikika ikimwambia.

“nadhani umeisikia sauti ya binti yako akiwa na wanafunzi wenzake wakipata chakula cha jioni. Sasa basi kama utakaidi kufanya tulivyokuelekeza. basi utapokea zawadi ya kichwa cha binti yako kwenye ‘pakage’ maalumu” simu hiyo ikakatwa. Mkuu wa nchi ya Ungamo alichoka, machozi mazito yalianza kumtoka kwa kasi kubwa lakini hakutaka yayazamishe macho yake, alijitahidi sana kuyafuta kisha akaingia kwenye dimbwi kubwa la mawazo.

“hili kundi ni kubwa sana inavyoonekana na bila shaka ni taifa zima liko kwenye usaliti huu. Wanataka nini? Mapinduzi?…hapana kwanini iwe mapinduzi halafu iwe hivi? Kwanini wamemteka Backa na binti yake kwanini? Inamaana hawa ndiyo watakao tumika kwenye hili? hapana, hapana, hapana. Hili jambo ni kubwa sana” alijisemea Mh. Rais huku akijisahau kabisa kama muda ule uliokusudiwa ulikuwa ukikaribia na kutaka kumpita kwa kasi. Mawazo yalikuwa mengi mno kichwani mwake na wala hakujua nini kifanyike ili aweze kuliokoa jahazi hilo lililokuwa katika hatua za mwisho za kuzama. Alikaa humo ndani pasipo kutoa taarifa yoyote ile kama kikao kipo au hakipo. Viongozi wakubwa wa ngazi ya juu ya serikali walifika kwenye chumba maalumu cha mikutano. Walikuwa wakimsubiri Mkuu wa nchi tu mahali hapo ili kujua ni nini kilichopelekea wao kuitwa mahali hapo. Ni viongozi wachache tu ndani ya chumba hicho ndiyo waliokuwa hawajui nini kilichofanya waitiwe hapo lakini wengi walikuwa wakijua na walijua kuwa hakuna kitu chochote kitakachofanyika mahali hapo.

“ha ha haaa!” cheko zito la fedha lilisikika humo ndani, viongozi hao walionekana kuwa na furaha sana ndani ya chumba hicho. Tena walikuwa wamekaa kwa makundi mawili, kundi moja lilikuwa si la watu wengi lakini kundi moja hili lilikuwa na watu wengi tena hawa ndiyo walikuwa na furaha kubwa sana.

“hebu ongeza kinywaji kidogo nijazilie, hakijanikolea kabisa” alisema mtu mmoja mwenye mwili wa wastani, huyu alikuwa ni waziri wa mali asili na utalii mh. Kaladi. Kinywaji kikaongezwa, akapiga funda kadhaa na kirudisha gilasi mezani.

“Bande Sir, mbona muheshimiwa anachelewa sana kufika?” aliuliza huyo bwana huku usoni akiwa na tabasamu pana. Bande Sir aligeuza shingo yake akamtazama kila mmoja mahali hapo kisha cheko kubwa sana la watu hao kwa pamoja likaibuka, walicheka kwa sauti kubwa mno hadi ikawa kero kwa lile kundi dogo ambalo alikuwapo IGP Liyambo. Hawa watu walijua kabisa kuwa hakutakuwa na kitu chochote kitakachoendelea mahali hapo kwani kama ni jambia wao walikamata mpini, walikuwa na imani kuwa hakuna kitu chochote kitakacho watisha mabwana hao. Cheko lao lenye kutia maudhi lilikuja kukatika baada ya mshauri wa Rais kuingia mule ndani na tangazo moja kuwa hakutakuwa na kikao hicho kwani kuna mambo hayako sawa.

“kwanini Rais hakuja kutuomba radhi kwa kutuweka hapa muda wote, hajui kuwa sisi tuna mambo yetu muhimu ambayo tulipaswa kuyafanya kwa muda aliotuweka hapa?” alihoji mh. Waziri bwana Bande Sir huku akiwa amesimama tayari kutaka kuondoka mahali hapo. Wenzake nao wakamuiga, wakasimama na kupiga hatua ndogo ndogo kutoka humo ndani wakipita karibu na lile kundi lililobeba viongozi wachache wazalendo. Waliwatazama kwa dharau kubwa kisha wakaondoka eneo hilo kwa tambo kubwa.

“kuna nini hapa Liyambo?” alihoji waziri mmoja asiye na idara maalum akiwa anamtazama IGP usoni moja kwa moja.

“kuna mambo makubwa sana hapa kiongozi na yanahitaji ufumbuzi wa haraka mno?” alijibu Liyambo kwa utulivu mkubwa kisha akapumua kwa nguvu nyingi.

“kwanini mkuu ameshindwa kufika hapa tena bila taarifa?” lilikuwa swali jingine hili.

“ndiyo maana nimesema pana mambo makubwa sana yanayohitaji ufumbuzi wa haraka sana” alirudia jibu lake kwa msisitizo kisha akasema.

“si mimi wala wewe, kila mmoja anamjua mkuu vizuri, siyo mtu wa hivi huyu, Mabandu tunaemjua sisi siye huyu, huyu amebadilika sana, sasa hili ni tatizo kubwa sana na tatizo linalomtafuna yeye ndilo linalonitafuna mimi. Hawa watu wanamtandao mkubwa sana na ndiyo wanao uringia unafikiri tunafanya nini?” alisema IGP kisha akawatazama wale wenzake halafu akasimama na kuwatakia usiku mwema huku akiwaomba wawe makini na wapange siku nzuri waweze kujua njia watakazozitumia. Akaondoka hapo na kuelekea kwa Mh. Rais.

“mkuu amechoka sana hivyo hahitaji kuongea na mtu yeyote muda huu.” aliambiwa hivyo IGP, hakutaka kuhoji sana alimtakia usiku mwema mtu huyo kisha akatoka nje ya ile Ikulu akaingia kwenye gari yake na kuondoka kwa kasi kubwa. Viongozi wale wakorofi walipoondoka ndani ya viunga vya Ikulu, walielekea Muavengero Kasino. Huko walikwenda kula raha tu na madada poa pamoja na starerhe nyingine bila kuwa na mawazo. Ilikuwa ni furaha kwao kwani hawakuwa wakiogopa kitu chochote kile.

Mlango wa hoteli moja kubwa yenye hadhi ya nyota tatu iliyofahamika kwa jina la Bi. Roz Hotel, ulifunguliwa taratibu kisha mfunguaji akajiingiza ndani bila shaka lolote lile. Alikuwa ni mrembo wa haja sana mwenye umbo la kuleta utata machoni mwa wanaume wenye macho juujuu, umbo lililojigawa vema kwenye mapaja yake huku juu akibeba kifua chenye matiti mazuri yaliyojaa kiasi. Macho yake yenye weusi mzuri yalizidi kumpamba binti huyo. Hakuwa mwengine huyu binti, alikuwa ni Petii. Binti asiyeeleweka anampango gani ndani ya nchi hii ya Ungamo. Tangu kuonekana kwake kule barabarani hadi kuja kumsaidia yule kichaa kutoka kwenye mdomo wa kifo, hadi hapo alipo, hakuna aliyejua huyo binti anatoka saa ngapi humo ndani na kurudi muda gani lakini alikuwa anatoka na kuingia kwa muda kama huo aliokuwa anaingia hapo. Alikuwa amewasha taa tayari ndani ya kile chumba chake na muda huo alikuwa amejikalia tu kitandani. Ghafla alinyanyuka na kulielekea kabati safi la humo chumbani. Akatoka na kijitabu kidogo, hiki kilikuwa kidogo sana. Akakipekua kurasa kadhaa kisha akatuliza macho.

“J.M.J! mh! huyu ni nani?” akajiuliza kisha akatulia kidogo kabla ya kulitaja jina jingine.

“M.Y.S” hili ndilo jina lake au, kwanini anitajie jina hili kisha kujirusha kwenye lile korongo?….kichaa, kichaa kweli lakini…..kwanini….huyu kichaa kwanini anajua kupigana vile halafu kwanini ametaja majina haya kwa herufi tu?” alijiuliza mengi Petii kisha akachukua kalamu na kuliongezea lile jina na kuliandika M.Y.S Kichaa, akalizunguushia duara kisha akalitazama lile jina lakini akaguna Mh! Akalichana lile karatasi na kulitia kinywani kisha akaandika upya yaani aliyaandika kama ambavyo aliandika awali. ‘J.M.J na M.Y.S kisha akayazunguushia duara akakifunga kile kijitabu na kuwaza kidogo kabla ya kupembua nguo zake. Umbo lake tamu likaonekana likiwa ndani ya taulo akielekea bafuni.

Usiku huo huo Backa alijikuta akiwa kwenye kiza totoroo! giza lililomficha sana, hakujua ni wapi alipo. Macho yake aliyafumbua lakini bado kulikuwa na giza tu. Akayafumba tena ili kuyafumbua kwa utaratibu. Akafanya hivyo lakini hakubadilisha kitu, bado giza lilikuwa vilevile. Alikaa hivyo kwa muda kidogo kisha akaanza kusikia michakacho ikitokea nyuma yake yaani nyuma ya ukuta ule aliokuwa ameuigamia akajua bila shaka kutakuwa na dirisha tu, akataka kusimama ili kuweza kuchungulia lakini michakacho ile ikasikika upande wa mbele. Akakaa chini akatulia akiwasubiri wasababishi wa michakacho hiyo. Mlango ukafunguliwa kisha taa kufuatia kuwashwa. Backa akafumba macho kutokana na ukali wa mwanga kisha kuyafumbua taratibu ili kuepuka kuyaumiza macho yake kwa ule mwanga mkali wa ile taa.

“ameamka tayari” alisema kijana mmoja kati ya wawili waliongia humo ndani.

“hivi ndivyo ilitakiwa iwe…karibu sana mzee, jisikie huru kufanya chochote chumba kikosafi kama unavyokiona kina kila kitu kuanzia choo hadi huduma nyingine zinazofanana na hizo, kesho ni siku ya kukutana na binti yako yuko salama. Unatakiwa ule usiwe na wasiwasi wowote kwani binti yako yuko salama kabisa” alibwabwaja huyo mtu. Backa akawaangalia wale vijana kisha akawahurumia sana na kutikisa kichwa, walikuwa ni vijana wadogo sana lakini ukatili ndiyo waliouona unafaa na wakajiingiza humo. Backa hakuoga wala kula, alilitazama bafu kisha akakitazama chakula halafu akayahamisha macho yake kitandani, akafikiri mengi sana yaliyopita nyuma, pia hapo akakumbuka jinsi ambavyo alitekwa akiwa nyumbani kwake. Phili, ndiyo, alimkumbuka phili bwana Backa. Alijua fika kwenye ile safari hakuwa peke yake ila alichokiamini ni kwamba watu hao wamefanya hila za kuwabadilisha chumba. Kitanda alikiona lakini hakuthubutu kuuweka mgongo wake hata kidogo. Angelalaje kwenye kitanda kisafi namna hiyo wakati hajui Phili atakuwa katika hali gani. Alidhamiria kuwa ni lazima ajue hali za watu wake muhimu Phili pamoja na binti yake ndipo aweze kujua aishi vipi. Giza lilikwisha bila kuonekana kwa Phili na siku hiyo pia ikafika katikati lakini pia sura ya Phili hakubahatika kuiona. Hadi anakuja kutolewa humo ndani na kuingizwa kwenye jumba kubwa lenye kutisha kwa ukubwa wake, bado sura ya Phili ilikuwa ni kitendawili, alitamani kuuliza mzee huyo lakini haikuwezekana muda huo hakuupata hata kidogo. Alikuja kushangaa akiingizwa kwenye chumba kikubwa chenye thamani kubwa sana. Akakutanishwa na binti yake aliyekuwa amekonda sana. Backa hakujali kule kukonda kwa binti yake bali kilichomgubika hapo ni furaha tu, alifurahi sana Backa kukutana na binti yake baada ya kupotezana kwa majuma kadhaa. Walipewa nafasi ya kuongea mengi, walikula pamoja kwa furaha kubwa huku wakipeana habari za hapa na pale. Hali ilikuja kubadilika na kuwa ya kilio pale Backa aliposema kuwa walinzi wote waliokuwa wakimlinda walikuwa wameuwawa lakini hakuthubutu kumpa habari za kifo cha baba wa Tamimu kwani Backa aliujua upendo wa binti yake kwa familia ile hivyo alijua moja kwa moja endapo angesema basi ingekuwa ni mwendo wa kubembelezana. Hakujua Backa, nasema hakujua kwa sababu kama angelijua kuwa huo ndiyo ulikuwa muda wa pekee wa kuzungumza na Binti yake kwa uhuru ni bora angemuambia. Backa hakuzijua sababu za yeye kuwekwa karibu na binti yake hivyo laiti angejua, aisee! Furaha ilikuwa kubwa hadi giza lilipoingia ndipo watu hao wakatenganishwa kila mmoja kwenda kulala kwenye chumba chake.

USIKU WA GIZA ZITO Tereza akiwa kwenye kijinguo cha kulalia, kuna mtu aliingia ndani ya chumba chake tena akiwa kwenye vazi jeupe tupu kisha mtu huyo akasimama mbele ya kitanda cha binti huyo. Alikuwa akivuja damu kinywani mtu huyo huku usoni akiwa na kinyago kizito kilichoyaficha macho yake. Shingo lake lilikuwa limelala upande mmoja kama alivyo Dr. Lee lakini kitu kilichoshangangaza na kushtua ni mtu huyo kuwa kwenye uwezo wa kusimama na kutembea kwa kutumia miguu yake. Alifanana kila kitu na Dr. Lee, sema huyu alionekana kuwa ni kijana mdogo sana. Chuchu za Tereza zilikuwa zimesimama dede ukilinganisha na lile vazi lake la kulalia kuwa jepesi na jeupe pee! Lilifanya chuchu nyeusi za binti yule kutokeza na kuonekana vema kabisa japo zilikuwa ndani ya lile vazi la kulalia. Yule mtu aliyekuwa akivuja damu alisogea hadi karibu ya kitanda cha binti yule kisha akainama na kuing’ata kidogo ile chuchu ya yule binti pasipo kumsababishia maumivu. Tereza alishtuka na kugaagaa mithili ya mtu aliyekuwa akiota ndoto nyevu kisha akatulia tuli akiwa amejiachia, alikuwa usingizini bado, miguu alikuwa ameitanua huku na kule na kumfanya yule mtu wa ajabu kutoa ulimi. Mungu wangu! Ulimi ulikuwa mweusi wa kutisha kisha akaonekana kujiramba. Hiki kiumbe kilikuwa kikitisha sana hakikujulikana ni kiumbe cha namna gani, hakikuwepo kwa upande wa binadamu kabisa. Mfanano wake ulikuwa ni sawa na binadamu lakini sidhani kama alikuwa na tabia ama nasaba za kibinadamu. Kiumbe kile kilimtazama Tereza kuanzia miguuni hadi kifuani tena. Alikuwa amemuachia Tereza Doa kubwa la damu kwenye ncha ya chuchu yake. Akatabasamu kwa tabasamu baya na la kutisha ambalo lilifanya hadi kile kinyago chake kuendana na lile tabasamu, alitisha vibaya sana kiasi kwamba kama Tereza angeshtuka na kukiona kile kiumbe, angepoteza fahamu. Alipoona ameridhika kumtazama kisha akatoka kwa kutembea taratibu kuufuata mlango huku lile doa la damu pale kwenye chuchu ya Tereza likifutika na kupotea. Alikuja kutokea kwenye maabara kubwa ya mule ndani ya lile jumba kubwa kabisa la Dr. Lee lililosheheni kila aina ya ushetani ndani yake. Hakuwa akitembea kwa kasi na alikuwa akitembea kwa kuburuza miguu yake taratibu kulifuata kabati moja kubwa jeusi. Alilitazama lile kabati kwa muda kidogo, lile kabati likafunguka lenyewe, miili ya binadamu ikaonekana mule kabatini hii ilikuwa bado ikivuja damu na ilionekana ikiwa bado mibichi kabisa. Kile kiumbe kiliuchomoa mwili mmoja kisha akaupakata mikononi. Alinyanyua sura yake kutazama juu kisha akatoa sauti kali na ya ajabu sana, upepo mkali sana ukavuma mule ndani. Vazi lake likawa linapeperushwa kwa mtindo wa kutisha, upepo ule ukajikusanya sehemu moja na kutengengeneza kitu kama shimo mahali alipo yeye kisha akanyanyuliwa taratibu akatolewa mule ndani kupitia dirishani, dirisha la vioo likapasuka, kelele nyingine za kutisha zikasikika hizi zikiwa kali maradufu. Kelele hizo hazikuishia pale maabara tu bali zilifika hadi chumbani kwa Merina na kutikisa chumba kizima cha binti huyo, ngoma zake za masikio ziliumia hadi akakurupuka kutoka kwenye usingizi mzito akasimama katikati ya kile chumba.

“hii ni nini sasa?” alijiuliza lakini kimya kilitanda, hakukuwa tena na zile kelele, akakimbilia dirishani kuchungulia, akakuta giza totoro!

“shiit! Inamaana hili giza watu hawalioni?” alijiuliza tena kisha akatoka mule ndani akakimbilia kwenye sehemu ambayo ndiyo inayotumika kuwashia taa zote za jumba lile, akakuta pako Off. Hakujiuliza sana aliwasha kisha akaelekea kwenye chumba alichokuwapo Dr. Lee. Akamukuta mzee huyo akiwa amekaa kwenye kigodoro chake. Hakumsemesha alitulia mlangoni na kumtazama vizuri mzee huyo ambaye alikuwa na afya mgogoro sana. Alimkuta Dr. Lee akiwa anatokwa na damu shingoni.

“Boss! Nini kimejiri usiku huu mbona sielewi…umesikia chochote labda?” aliongea kwa kuchanganyikiwa sana Merina kisha akauliza kile ambacho yeye alikisikia ili ajue kama ni yeye tu au bosi wake pia amekisikia.

“nimesikia, amekuja na inaonekana hakuja hivihivi amekuja na hasira za aina yake, kagua hii nyumba yote hadi maabara ili tujue ni ujumbe gani ameacha” aliongea kwa upole Dr. Lee kwa sauti yake ileile ya kukoroma. Merina alitoka kwa kasi kubwa mule ndani. Baada ya muda mfupi tu alirudi akiwa anatweta vibaya sana.

“wafanya kazi wetu wanne wamepoteza maisha kwa damu yao kunyonywa huku mwili mmoja wa wale vijana waliokufa kwa kupata ajali ambayo tuliisababisha sisi na kuondoka na miili kadhaa kabla ya msaada kufika kwa ajili ya kafara la kesho ili huyu binti kukaribishwa, umetoweka, yaani haupo kabisa nimetafuka kila chochoro la hii nyumba sijaona” aliongea Merina.

“my lady Devil!” aliita Dr. Lee.

“kwa niaba yako niko hapa Boss” aliitika Merina au Lady Devil kama alivyopenda kuitwa na mzee huyo.

“kafara tuliotaka kuifanya ameifuata mwenyewe, ukumbuke naishi kwa ajili yake, akikasirika inamaana mimi sina maisha mfano ni zile damu ulizoziona zikivuja kutokea shingoni mwangu. Alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kunifanya mimi kuwa mfu leo, tambua kuwa naishi na niko hai kwa nguvu zake, angeongeza idadi ya damu mwilini mwake ningeangamia. Sitakubali kufa kizembe….sijui umenielewa vizuri au namfunga kibwebwe Mbuzi anengue ngoma ya kumnema mwali?”

“nakupata Boss!” alijibu kwa haraka sana Lady Devil.

“Blod master, Blod master…..King Bondo, alisema atakuwa katika kila njia ya malipizi yetu yaani atasimama kila hatua moja tunayopita lakini akatuahidi vifo vya kinyama sana kama tukimchezea michezo ya kitoto. Nani wa kufa leo au kesho? nani kati yetu anayetaka kufa mapema?” aliuliza Dr. Lee, Lady Devil akajibu hakuna. Lee akaendelea tena akiwa na ghadhabu kubwa sana.

“Bencov amekubali kujiunga nasi, atatusamehe sana maana kifo anachotaka raia wa Taifa la Ungamo wafe, siyo vifo tunavyovifanya sisi, sisi tunatumia mauwaji ya kuzimu na ni lazima kila atayeshuhudia mauwaji hayo ajiulize ‘HII NI DUNIA AU KUZIMU?’

my Lady Devil, kesho kazi ya kutengeneza dawa itakayokwenda kukuza mmea hatari sana utakaokwenda kuwa kifo kwa kila raia atakayethubutu kuukaribisha shambani kwake ama bustanini. Iwe ni kwa lazima au hiyari, kesho Tereza ataanza kutengeneza mchanganyo huo hatari sana” alimaliza kuongea Dr. Lee kisha akamtazama huyo binti ambaye ndiye mtu pekee anayesimama badala yake. Merina akatoka mule ndani kisha akaelekea chumbani kwake moja kwa moja.

%%%%%%%%%**


Saa kumi na moja alfajiri ndani ya hospitali ya rufaa ya Pande kunaibuka taharuki kubwa ya kutisha kisha kuwaacha watu katika sintofahamu ya aina yake. Wataalamu wote pamoja na wauguzi wote wa hospitali hiyo walikuwa wamejaa kwenye chumba kimoja cha kulazia wagonjwa. Ilikuwa ni mshikemshike kweli hakuna mgonjwa aliyekubali kuabaki kitandani siku hiyo, na hii ilikuwa ni baada ya kutokea kitu ambacho hakikuwahi kutokea kwenye maisha ya watu wa Taifa hilo dogo. Dr. Albert alismama kijasiri na kutoa amri kuwaondoa hofu wagonjwa na kuwaambia kuwa tatizo hilo lilitokea kwenye majokofu maalumu ya kuhifadhia maiti ambao walikuwa wakitakiwa kufanyiwa uchunguzi maalumu hivyo aliwataka wagonjwa na watu wote waliokuwa hapo kutazama wagonjwa wao wapunguze hofu na watulie. Alikuwa akijaribu kuwakataza watoto wadogo wa chekechea waache kuishangilia kengele ya kuwaita kwenye uji wenye sukari. Hakuna mtu ambaye alikuwa radhi hata mmoja kumuacha ndugu yake mahali hapo, kila mmoja alikuwa tayari amefungasha mabundu na virago vya ndugu yake.

“aaah wapi!, atakwenda ponea nyumbani si hapa” mmoja wa mtu aliyekwenda hospitalini hapo kumtazama nduguye alisema. Kichwa cha Dr. Albert kiliuma sana na kujiuliza ni nani aliyetoa siri hizo za kidaktari, Haikuwapo kwenye kiapo cha utabibu hiyo hata kidogo na kila alipokuwa akijiuliza ni kwamba jibu hakulipata. Watu wakaondoka na wagonjwa wao huku hospitali ikibaki na wagonjwa ambao ni wale walio katika hali mbaya zaidi. Maneno ya kutisha yakazagaa mitaani kuwa majokofu yaliyohifadhia miili ya askari kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi, yazua balaa baada ya miili hiyo kugeuka mifupa na mafuvu ya kichwa tu. Albert akashangaa uvumi wa siri za kidaktari ukizagaa huku akisahau kuwa kulikuwa na msaliti akimfuga pasipokujua.

Mikono ilikuwa ikimtetemeka Rais Mabandu wakati akiwa analishusha gazeti lake chini baada ya kupata kuisoma habari yenye kichwa cha habari ‘HOSPITALI YA RUFAA YAIBUA MAAJABU’ akalitupia macho gazeti jingine la Siri kali lilokuwa limeandikwa kwa wino wa kukoleza ‘UNGAMO YAOGOPESHA’ pumzi nzito zikamtoka asielewe nini afanye au kipi afanye.

“wapi patanifaa ambapo sura yangu haitatambulika” alijisemea hivyo Mh. Mabandu akiwa anayafinya macho yake kwa hasira. Lakini si yeye tu hofu ilikuwa kwa kila mtu japo wachache tu walikuwa wakifurahi kwa jambo hilo. Kila kiongozi alikuwa na hofu kubwa, kikao cha dharura kikaitwa hiki kikiwahusisha wale viongozi wachache wazalendo, watu wakaulizana kabla waandishi wa habari hawajawauliza wao na wasijue cha kujibu. Nini kifanyike likawa swali gumu ambalo hakuna aliyeweza kulijibu mahali hapo. Kikao kikachukua muda mrefu lakini hakikuwa na ufumbumbuzi kila mmoja akawa na jibu lakie kichwani kama kwa bahati mbaya akikutana na muandishi wa habari, na akaulizwa kuhusiana na majibu juu ya hofu hiyo. Kila kiongozi alikuwa amepanga kuificha sura yake anapojua yeye hadi hilo sekeseke litakapokwisha, haikujulikana saa ngapi na ni nani wa kulimaliza hilo kama si wao kutafuta njia mbadala

MOROGORO TANZANIA SAA 01:37 ADHUHURI

KIJANA mmjoa alikuwa akitoka ndani ya gari na kupiga hatua ndogo ndogo kulielekea lango kubwa jeusi. Hakutaka kuliingiza lile gari ndani ya uzio ule hata kidogo kwani alijua fika kufanya vile ingekuwa ni usumbufu, ndiyo, alikuwa ni lazima atoke tena. Alipoingia tu ndani ya ule uzio aliwaona watu awapendao wakiwa kwenye uwanja wakipasha mwili taratibu pasipo kuitoa miili yao jasho. Akawatazama kwa muda kidogo kabla hajachukua uwamuzi wa kuwafuata watu wale.

“Mary, kaka hakuja na zawadi leo?” aliongea yule msichana mkubwa akimwambia binti mdogo wa miaka tisa hivi. Binti yule aligeuka na kumtazama yule msichana mkubwa kisha kutazama upande ambao kijana yule alikuwa akija. Mary alikimbia kumfuata yule kijana kisha akamrukia na kumkumbatia,

“mh! Mary uwe unasema basi jamani, unajua ungedondoka?” alisema yule kijana akiwa anamkumbatia Mary.

“siyo rahisi kaka niko makini, hata kama usingenishika nisingedondoka….zawadi kaka?” aliongea Mary kisha kuhitaji hitaji lake alipendalo sana au nisema ndivyo alivyozoeshwa.

“hakuna Mdogo wangu niko na haraka sana ila dada….!”

“unaharaka unakwenda wapi?” swali lililomkatisha kijana yule likafanya watazamane wote watatu kwa muda kidogo kisha kijana yule akamshusha Mary akasema.

“tuzungumze kidogo” alisema kisha akatangulia mbele kuelelekea ndani, yule msichana akamwambia Mary amsubiri kwenye bwawa la kuogelea atafika muda si mrefu. Mary akaondoka na kumucha yule dada akielekea ndani.

“Catherine, usiku wa leo natakiwa kuwa Ungamo”

“nini Roi?” aliuliza kwa taharuki Catherine hakuamini hicho kitu alichokisikia hapo ……

hata kidogo. Roi alimtazama binti huyo aliyemrembo na anayempenda kuliko kitu chochote kile kisha akasema kwa kurudia.

“kesho natakiwa niwe Ungamo”

“hivi unajua kinachoendelea huko lakini au hiyo roho yako umeichoka?” aliuliza Catherine.

“my love, tambua kuwa kwa sasa mimi haya ndiyo matukio yangu ya kuweza kukabiliana nayo, hakuna tukio jepesi ninalopelekwa mimi. Kila kinachoendelea huko nakijua….!”

“hata kile kilichotapakaa leo kwenye vyombo vya habari?” alikatisha kwa swali Cat. Roi akaendele.

“si hilo tu, hata vingine ambavyo wewe na mimi hatuvijui. Natakiwa kuzirudisha damu za wapelelezi wetu waliokufa kwenye mchanga wa Taifa lile na nitazirudisha.”

“ok, si tuko wote katika hiyo safari?” aliuliza Cat lakini Roi alimkatalia, kitendo hicho kikawa kibaya zaidi kwa binti huyo.

“kwanini?” akauliza huku akiwa mwekundu usoni.

“Catherine kumbuka kuwa hiki kitengo ni cha siri sana na ndiyo maana kiko huku mkoani, haitakiwi mtu yeyote yule ajue kuhusiana na kitengo hiki pia ni kipya, hii ni kazi yangu ya kwanza na ngumu mno, mimi ndimi wa kumaliza kazi hizi. Wewe utabaki na utabaki kwa ajili ya Mary, Hussein Babu hakukupanga kwenye hili hata kidogo. Mary ni mwanafunzi tena wa elimu ya chini anahitaji ukaribu wako na wewe ndiye uliyesema kuwa asisome shule za bweni ili awe karibu nasi, baki naye. Nimeteuliwa mimi tu na msaada wa kila kitu nitaupata kutoka kwenye hiki kitengo nikiuhitaji” aliongea kwa marefu sana Roi ili kuweza kumuweka sawa mpenzi wake. Kimya kikatanda mule ndani, wakatazamana kwa muda kisha Catherine akaanzisha maongezi ya kuuliza kuhusu kula, Roi akaomba kwenda kuoga kwanza kisha ale harakaharaka ili aondoke. Akavua nguo zake zote na kubakiwa na nguo ya ndani akatwaa taulo lakini Cat akalichukua na kumwambia atangulea yeye atampelekea, Roi akazama Bafuni. Cat hakuwa katika furaha kabisa lakini hakuwa na jinsi tena kwani Roi tayari alikuwa ni mtu muhimu sana kwenye Taifa hili la Tanzania japo hakuwa akijulikana na wengi. Alivua nguo zote kisha akajifunga lile taulo akaelekea bafuni ambako Roi alishaanza kujimwagia maji. Wakapokeana kwa kumbatio mwanana na tamu kila mmoja akazituma fikra zizivute hisia karibu kisha wote wakajikuta kwenye uhitaji mkubwa sana wa kupena penzi tamu la muagano. Walinyonyana ndimi zao kwa raha za ajabu hadi kila mmoja akaridhika na kile kilichokuwa kikifanyiaka mahali hapo, wakabadili michezo, wakapeana tunda hatimaye wakahamia kitandani ambako kulikuwa na shughuli pevu si mchezo. Cat alikuwa akimpa Roi vitu adimu huku akilia kwa hisia kubwa na kumtakia mpenzi wake huyo safari njema na yenye kumfanya arudi salama. Lilikuwa ni penzi la pekee sana hadi kila mmoja akawa hoi bin taabani.

“nakutakia safari njema na yenye ushindi mume wangu, urudi na macho yako yote mawili hata kama watachukua nywele ni sawa tu lakini urudi ukiwa salama” alisema kwa uchungu mkubwa sana Catherine.

“usijali mpenzi kwa uwezo wa Mungu, nakuahidi kurudi hapa nikiwa salama kabisa. Nakupenda sana” alirudisha majibu Roi, aisee! Hakujua ni nini anakifuata huko hata kidogo, hakujua na hakujua hata robo. Alijinyanyua kitandani akimuacha Cat akiwa bado anamtamani kijana huyo ambaye alipanga naye mambo mengi ikiwemo kufunga ndoa na kadha wa kadha, akaelekea bafuni kuoga. Muda akawa ametoka akavaa na kurudi mezani. ile anavuta chombo chenye chakula tu, kijana mmoja mwenye mawani ya macho aliingia hapo sebuleni.

“hata kama hujakula harufu inakutosha, Hussein Babu anakuhitaji muda huu na haraka zaidi” alisema kijana huyo anayefahamika kwa jina la Amiri. Roi alikitazama kile chakula kisha akakamata kijiko akapiga vijiko viwili vyenye ujazo kosha akatoka hadi lilipo gari alilokuja nalo huyo kijana, wakaingia huku macho ya Cat yakiwa yanawasindikiza, Roi akatoa ishara ya kuingizwa kwa gari ndani wakapotelea barabarani.

“kila kitu kuhusiana na hii safari yako kiko kwenye bag lako la kusafiria, kumbuka kuwa hii ndiyo kazi yako ya kwanza Taifa inakupa achana na ile iliyokuletea sifa hadi Tanzania ikakujua, hii ni ya tofauti sana na ni kama jaribio pia kwako tangu utoke kwenye mafunzo maalumu ya kijasusi. Nenda kairudishe heshima ya askari wetu wazalendo nenda ukaitoe aibu hii ya kuwa kumbe Tanzania hakuna wapelelezi mahili na hodari. Hakuna kiumbe hata mmoja anayejua uingiaji wako ndani ya nchi ile hata sisimizi wahajui. Wapo watu makini nyuma yako na utakuwa ukipokea taarifa muhimu kila utakapojikuta kwenye wakati mgumu. Kila laheri kijana wangu” alimaliza kuongea Hussein Babu,

huyu ndiye tuliyekuwa tukimfahamu kama D.A kwenye ule mkasa wa SEX MACHINE uliotaka kuondoka na maisha ya kijana Chriss kabla hajajitambua kuwa Roi. Pia ukiwa na uharibifu mkubwa sana ndani ya manispaa ya Morogoro. (Ni vema kama hujapata kuusoma basi fanya hima). Kijana Roi ndiye aliyeweza kuufutilia mbali mpango mbaya wa Mr. Lee Kim, mkorea aliyetaka kuzalisha mashoga wengi ndani ya Taifa hili. Leo mzee huyo D.A anaibuka tena kama Hussein Babu akiwa ni kiongozi wa siri sana ndani ya kitengo cha siri ambacho hakina jina maalumu bado. Roi anaiacha ardhi ya morogoro na kuelekea jiji Dar es salaam, anachukuwa ndege kubwa kutoka kwenye shirika la ndege la Ethiopia kwa ajili ya kumfikisha kweye nchi ndogo sana ya Ungamo. Nchi inayotishia amani ya wananchi wake kwa mambo ya kutisha yanayoendelea.

Saa sita na dakika nyingi usiku, ndege hiyo inashuka kwenye uwanja wa kimataifa TAO DE. Abiria mmoja baada ya mwingine wanashuka ndegeni humo. Abiria wa tano kushuka alikuwa ni kijana Roi ndani ya suti kali sana, ukimtazama kwa woga waweza kusema ni bilionea fulani hivi kutokea nchi Tajiri hapa Afrika. Alikanyaga ndani ya uwanja huo akafanya taratibu za hapo kisha akatoka nje ya uwanja ule ambako alichukua Tax.

“wapi boss?” aliuliza bwana mtu mzima kidogo mwenye ndevu nyingi kiasi akiwa anafungua mlango wa gari yake ili kijana huyo aweze kuingia. Roi aliingia akakaa kisha akasema mahali anapotaka kufikishwa kwa usiku huo.

“Bi. Rozi Hotel” baada ya kusema hivyo, dereva akataja kiasi na kuingiza gari yake barabarani baada ya kuhakikishiwa kuwa pesa haikuwa tatizo. Wakati Roi akiwa ametulia kwenye Hoteli hiyo nzuri yenye mahadhi ya kiafrika, upande mwingine wa mji huo huo, kulionekana mtu akiwa ndani ya nguo kuukuu akiwa anavuka barabara huku akiwa na haraka sana umakini ukiwa juu kuliko kitu kingine lakini kwa mtu wa kawaida usingeweza kujua kama mtu yule alikuwa kwenye umakini. Macho yake yalikuwa hayatulii hata kidogo, mara atazame huku mara kule lakini shingo yake ikiwa imeinamia chini ili kuificha sura yake kidogo asiweze kufahamika kiurahisi bila shaka. Alipovuka barabara akaingia kwenye nyasi kavu na kubana nyuma ya mti mkuwa kulipisha gari kubwa la taka lililokuwa linakuja usiku huo. Ilikuwa ni kawaida sana gari hiyo kuja kutupa taka mahali hapo lakini kwa usiku huu yule mtu alikuwa na mpango wa kujua je, ni taka tu ndizo zinazotupwa hapo au kuna mengine. Mtu huyu hakuwa mwingine bali ni M.Y.S au kichaa kwa jina zoelefu. Alikuwa amekamata kipande cha gazeti mikononi mwake. Alituli kwa muda sana pale kwenye ule mti uliozingirwa na kichaka hadi ile gari ilipotoka pale jaani ndipo na yeye akachoropoka na kuingia kwenye Minyono iliyoshikamana, ambako alipita huko akaja kutokea hapo jaani. Alizitazama zile taka kwa muda sana lakini hakuona kitu cha maana kwenye zile taka, akatulia pale kwa muda mrefu sana ndipo alipotia mkono wake mfukoni na kutoa kurunzi ndogo sana inayoingia bateri ndogo moja kisha akasogea kwa uangalifu mkubwa hadi pale alipoamini ndipo zilipomwagwa taka mpya. Akawasha ile Kurunzi iliyotoa mwanga mkali na mwembamba usiosambaa, hii ilikuwa ni kurunzi ya kazi kweli. Aliuzungusha mwanga taratibu hadi alipokomea kwenye furushi dogo lililofungwa kwenye mfuko wa salfeti ambalo lilikuwa limefukiwa ndani ya taka kwa kiasi kikubwa sana, akaitia ile kurunzi mfukoni kisha akalivuta lile furushi akalitoa na kuingia nalo katikati ya kichaka cha ile minyono. Akatafuta mahali pazuri kisha akalifungua lile furushi ambalo lilikuwa limejaa majimaji ambayo yalikuwa yakimpa mashaka makubwa sana yule kichaa au M.Y.S. Akamulika na ile kurunzi aisee! Ilitisha kutazama tena ilihitaji ujasiri wa hali ya juu mno kukitazama kilichomo ndani ya lile furushi. Vilikuwa ni vichwa vya binadamu ambavyo vilipasuliwa eneo la juu na kutolewa ubongo kisha kukusanywa pamoja. M.Y.S alilitazama kwa muda kisha akakaa chini akiwa hoi, hakuwa na hofu yoyote juu ya lile furushi wala mahali alipo na lile giza. Hali ni mbaya zaidi.

Usiku ulikuwa tayari umekuwa mkubwa sana, ilikuwa yapata saa sita ama saba. Baadhi ya maeneo ya jiji la Pande yalikuwa na ukimya mkubwa sana, kila mtaa ulikuwa umefunikwa na ukimya huo. Baadhi ya majumba ya starehe pekee ndiyo yalikuwa bado yakiburudisha watu waliokwenda huko kwa ajili ya kuzifurahisha nyoyo zao. Katika baa moja kubwa mjini hapo tunamuona Petii akiwa amekaa kwenye kiti kimoja kirefu mbele yake kukiwa na gilasi moja ndefu yenye kiuno, gilasi ile ilikuwa imeongezwa kinywaji si chini ya mara tano au sita na kwa majira hayo ilikuwa haina muda mrefu tangu itoke kinywani mwa dada huyo. Petii alipiga kimya cha muda sana lakini macho yake yote yakiwa yako kwenye meza moja hivi ambayo ilikuwa imekaliwa na kijana mmoja mtanashati mwenye sura ya duara kidogo iliyovutia. Hakuwa mtu mwenye furaha hata kidogo kijana yule, alionekana ni mtu mwenye mawazo mengi sana. Macho ya petii yakawa na kazi mbili, moja ilikuwa ni kumtazama yule kijana, pili yalikuwa yakiitazama meza moja iliyokuwa inezunguukwa na vijana wane waliokuwa wamelewa kiasi. Kitu kilichofanya awatazame wale vijana ni mitapo yao, vijana wale walikuwa wakijitapa sana huku wakiinuka mara kwa mara na kwenda kucheza muziki, walikuwa na fujo sana vijana wale.

Petii ni nani? na kwanini yuko pale usiku ule? Kuna jambo gani huyu dada analifuatilia? Pengine haya ndiyo miongoni mwa maswali mengi unayojiuliza kichwani mwako kuhusu dada huyu asiyeeleweka.

Petii ni mpelelezi kuyoka Malawi na yupo ndani ya nchi ya Ungamo kwa ajili ya kazi moja tu ya kuja kuwapeleleza wauwaji watatu ambao wapo au wamekimbilia nchini hapa baada ya kufanya mauwaji ya binti mkubwa wa waziri mkuu wa nchi hiyo. Aliinyanyua gilasi yake Petii na kupiga kumbo moja tu la kile kinywaji akakimaliza kabisa kisha akanyanyuka akiwa mkavu mno na kutembea kwa mwendo wake wa maringo kuifuata ile meza ya wale vijana wenye majigambo na majisifu makubwa lakini hakuikaribia, alipita sentimita chache sana na ilipo meza ya vijana wale kisha akaelekea kwenye ile meza ya yule kijana akaizunguka ile meza na kumuinamia yule kijana huku akihakikisha macho yake yanawatazama wale vijana wa majigambo.

“habari yako kaka?” alisalimia Petii lakini yule kijana hakujibu alibaki kunyanyua macho tu na kumtazama, binti huyo hakutia neno jingine akakaa kisha akamtazama kijana yule aliyeonekana kuwa maili nyingi sana kwa mawazo kisha akairudia salamu yake ya awali kwa mara nyingine.

“habari yako kaka?”

“salama vipi?” akajibu kisharishari akionesha hakuhitaji usumbufu kabisa maeneo yale.

“samahani kwa kukuingilia kwenye starehe zako ninashida na wale pale” akasema Petii huku akiwa ameyaelekeza macho yake kwenye ile meza ya wale vijana. Kuna maneno yalikuwa yakiongelewa pale na maneno hayo yaliibuka baada ya Petii kupita pale karibu yao, hayo maneno si mengine bali ni mjadala kuhusu urembo wa yule binti aliyepita karibu yao. Petii alilijua hilo kwani kitu kimoja anacho wakamatia wanaume ni umbo lake, alikuwa na umbo zuri lenye mvuto mkubwa sana ambalo si kila mwanaume anaweza kuvumilia kumtazama tu halafu basi ilikuwa ni ngumu mno. Petii alikuwa yupo kazini japo haijulikani kwa mtu hata mmoja kuwa alikuwa ndani ya mji huu kwa maslahi yapi? Maneno yale ya Petii yalimchanganya sana Yule kijana lakini hakupata muda wa kuuliza kwani Petii alikuwa akitabasamu kwa tabasamu la uchokozi kisha akajinyanyua kuelekea mahali vilipo vyoo.

“tafadhali narudi sasa hivi usiondoke” alisema Petii kumwambia yule kijana…..

“tafadhali narudi sasa hivi usiondoke” alisema Petii kumwambia yule kijana kisha akaelekea njia ya maliwatoni. Pale kwenye ile meza alinyanyuka kijana mmoja huku wale wengine wakimtazama yule kijana ambaye alikuwa amekaa na Petii punde, machoni mwao wakiwa na matabasamu ya kifedhuli na ubabe ndani yake mwishoe wakaangua vicheko vyenye kumkebehi yule kijana aliyopo pale. Petii alipofika chooni ile anafungua mlango tu kuingia ndani, aliguswa bega na yule kijana kisha kabla haja geuka akavutiwa ndani ya mlango mmoja uliokuwa wazi.

“huwa sipendi kuwaacha warembo kama nyinyi bila kuwafaidi” alisema yule kijana mwenye meno ya rangi ya kuoza huku akiwa anapiga hatua ndogo ndogo kumsogelea petii ambaye alikuwa na hofu kubwa, ilikuwa ni baada ya kumuacha Petii na kwenda kufunga mlango. Petii alijifanya yu katika woga sana alikuwa akisogea ukutani na kujikunja kuonesha hofu kubwa. Yule kijana mwenye meno ya rangi ya kuoza alikuwa akizidi kumsogelea Petii huku akiwa na tabasamu lenye kukera usoni mwake.

“kidogo tu kwani ukinipa mimi utakuwa umepungua nini,….halafu mimi huwa sina mapenzi ya kulazimisha mara nyingi nakuwa mpole kama ukinipa mwenyewe ila ukileta kujua, hiki hapa” alisema yule kijana huku akimuonesha Petii kisu halafu kaendelea.

“hiki hapa ndiyo kitakunyoosha wewe lakini pia utamu nitaula” alikuwa amemkaribia kabisa na hapo alikuwa akimgusa na kile kisu cha shavuni na maeneo ya shingoni. Kufumba na kufumbua yule kijana alijikuta mikono mitupu. kisu hakujua mahali kilipokimbilia lakini si mshangao pekee uliomkubwa wa kuporwa kisu la! Alitulizwa na pigo baya sana la kwenye korodani. Macho yalikuwa yamemtoka pasipo kupiga kelele yoyote ile. Pigo jingine likatua kifuani halafu Petii aliruka kwa mruko wa aina yake na kusimama nyuma ya yule kijana.

“nisaidie kitu kimoja tu kisha nikuache uende….kuna watu watatu tu nawatafuta, naomba uniambie jinsi ya kuwapata maana wako kwenye udongo wa mji huu” akatulia Petii kisha akamtazama yule kijana ambaye alitoa macho baada ya kukiona kisu kikiwa shingoni.

“kuna huyu mmoja anaitwa Lonto, nilipata habari alikimbilia ndani ya nchi hii lakini akatoka na sasa yuko nchi nyingine. Unaweza kujua ni nchi gani yupo?” akauliza kisha akatulia kimya alipoona yule bwana hakushtuka akajua kuwa huyo hamjui akasema.

“ok, tuachane na huyo je, huyu Phili mpondi na mwengine,….huyu ni lazima umjue, Bande Sir” alipolitamka tu jina la Bande Sir, yule kijana akatoa macho akajua huyu anamjua sasa akakazia hapo ili kuweza kumjua huyo Bande Sir ni nani na atampata vipi maana picha aliyopewa ya mtu huyo hadi muda huo alikuwa hajaitia machoni.

“niambie huyo Bande Sir ni nani basi na nitampataje” alizidi kuuliza Petii. Kijana yule akabaki kimya, hakutaka kusema akataka kuleta ujanja wa Sungura wa kutaka kujitetea, alikosea. Aliguswa tena kwenye mbavu changa akatoa mguno wa maumivu kisha kisu kile kikakita kwenye shingo lake upande wa mshipa mkubwa wa damu.

“utaniuwa lakini sisemi” alisema kwa jeuri sana.

“utasema kwanza kisha ukitaka kufa utakufa” alijibu kwa jeuri pia Petii huku akikichoma zaidi kile kisu kuzama ndani

“ok,….ok, ok, na….nasema”

“sema sasa unajua ninamuda wa kubembelezana na wewe?” alifoka Petii.

“Muavengero Kasino, maeneo haya ndiyo huwa anapatikana” alijibu yule kijana kisha damu nyingi zikaruka baada ya kuushindilia shingoni mwake mkono ule wenye kisu, kisu kikawa kimezama hadi ndani kabisa, alijiuwa mwenyewe. Petii akamuachia yule kijana akadondoka chini kisha akavua gloves zake akazitia mfukoni na kutoka mule chooni akiwa ameuwacha ule mwili palepele. Alipotaka kuingia mule Baa akaona pale kwenye ile meza ya yule kijana aliyemuahidi kuwa atarudi, pako patupu, wale vijana pia hawakuwepo. Machale yakamcheza, akajua kwa vyovyote wale vijana walitaka kumfanyia ubaya kijana wa watu au wamemfanyia tayari, akatoka mbio kwa kuzunguka upande wa nyuma huko akaja kutoke mbele ya ile baa. Kwenye maegesho ya magari akaona gari ikitoka kwa kasi ya ajabu mno, kasi ambayo ilikuwa tofauti na magari ya kawaida hiyo ilikuwa kasi ya gari za mashindano. Akaitazama ile gari haraka haraka akaona picha kubwa la moto ubavuni huku likiwa na maandishi TN RACE Alipofika mahali gari yake ilipo shit! akajisemea moyoni. Wale vijana watatu walikuwa hawana uhai wote. Hakungoja hapo, aliingia garini na kupotea mahali hapo.

Asubuhi ya siku iliyofuata ilikuwa ya aina yake, Jiji hilo kubwa kabisa ndani ya Taifa hilo la Ungamo liliamka na habari tatu tofauti zenye kuwachanganya watu zaidi na kuzidi kuwatia hofu wana Taifa hilo. Moja ilikuwa ni ile iliyotokea kwenye Hospitali ya Rufaa ya Pande ya kukuta mafuvu ya kichwa na mifupa kwenye majokofu maalumu yaliyokuwa yamehifadhiwa Askari waliouwawa lindoni. Vichwa vya raia vikiwa bado vinatafakari hilo, kuna jingine hili lilikuwa ni habari ya Dampo kuu la kutupia taka kugeuka kuwa ni sehemu ya kutupia na mabaki ya viungo vya binadamu. Watu wengi walikuwa kwenye luninga zao wakitazama habari hiyo mbichi iliyopatikana asubuhi baada ya wanahabari kudai kuwa walipewa taarifa na shuhuda mmoja ambaye alificha jina na sura yake kutokutambulika. Habari hiyo ilionesha vifurushi kadhaa vya viungo hivyo vya binadamu vikiwa vimekusanywa pamoja huku furushi moja likiwa limefunguliwa na kuoneshwa vichwa viwili ambavyo vilikuwa havina ubongo kabisa. Hii ilitisha. Habari hii ikaendana na ile ya vifo vya utata kuibuka kwenye baa moja mjini hapo na habari hiyo ilieleza kuwa ni vijana wane wasiofahamika kukutwa wameuwawa na watu au mtu asiyefahamika hivyohivyo. Picha zikaoneshwa, mmoja kakutwa chooni akiwa amechomwa kisu cha shingo na watatu wakutwa kwenye maegesho ya magari. Hofu kubwa ikatanda Pande na viunga vyake, nchi ikazizima. Raia wakalia na uongozi mbaya tena waliingia ndani kabisa na kusema kuwa Rais wala hazungumzi chochote juu ya mambo hayo yaliyokuwa yakitishia amani ya nchi. Hili likawa ni neno baya sana kwa Rais, alikuwa akiumia moyoni mno hakujua afanye nini kuhusiana na lawama hizo za wananchi wake. Rais Mabandu akaiona Dunia ikianza kutupia macho kwake kwa haya yanaayoendelea nchini kwake. Afanye nini sasa na wakati kila hatua anayochukua, kunawaliomtangulia au wanaomtangulia mbele na kumuwekea kizingiti. Akaona ni bora atulie kisha akaamua kuibadilisha ile methali ya bora lawama kuliko fedheha yeye akasema ni bora fedheha zinazoendelea inchini kuliko lawama za mkewe dhidi ya usalama wa binti yake maana wanaomtangulia siku zote wanaelekeza makali ya upanga kwenye roho ya binti yake. Alikuwa na mapenzi makubwa sana kwa binti yake, lakini mapenzi hayo aliamini kabisa na kuona kuwa mkewe hayajui na mwishoe kumpa lawama za kwamba endapo atakataa sauti za wanaomkataza kufanya anachotaka kufanya basi atamtafutia mbeleko ya kumbebea. Hali hii ikadhoofisha fikra zake juu ya kujua kwanini mkewe anajua hadi mambo ya siri, anayapata wapi? Hakuwa akijiuliza haya Mh. Rais, laiti kama angejiuliza angekuwa na mashaka makubwa sana juu ya first Lady huyo. Lakini mbali ya hayo, habari hizi ziliumiza vichwa vingine vingi zaidi na vichwa hivi vilikuwa ni vya akina Julio na watu wake. Hawa ndiyo waliumizwa sana na hizi habari mpya zilizoibuka asubuhi hiyo. Hawa hawakuishia tu kuzisikia na kuziacha ziende hapana, waliitana kabisa na kuweka kikao kikubwa sana cha watu wengi na kujadili kuhusiana na tukio au matukio hayo mawili.

“nani wa kuweza kutoa habari au siri zetu hadharani na ni nani wa kwenda kule kwenye lile Dampo la porini?” aliuliza Julio Mobande lakini hakuna aliye na jibu zuri la kutoa mahali pale wakabaki kukodoleana macho tu, akarudia tena kuuliza swali jingine.

“nani walikwenda kutupa vile vifurushi jana usiku ya mabaki ya vichwa vile ambavyo ubongo wake tuliutoa kwa ajili ya kuupeleka Madagascar?

“sisi hapa mkuu?” vijana watatu wakasimama na kujibu.

“basi sawa nyinyi mnatakiwa kufa muda huu huu huku kikao kikiwa kinaendelea” alisema Raisi huyo wa zamani Mh. Julio M Julio.

“lakini hatukuona mtu pale jaani mkuu, kulikuwa na usalama mkubwa sasa sijui ni nini hiki?” alijitetea mmoja kwa niaba ya wengine huku akiwa na hofu kubwa machoni mwake.

“najua kuwa hakukuwa na watu ila kifo chenu ninyi ni kwa amani tu na kutaka kuwafundisha wengine kuwa umakini ni jambo la mbele kabla hujafanya chochote. Mimi niko chini ya wengine, nimetukanwa kama mama mjamzito mbele ya wakunga wa kwenye mahospitali yenu haya ya kimasikini” alisema Julio huku akichukua bastola kwenye kisahani, yenye mdomo mrefu na kitako cha rangi ya udongo. Zao la kizamani sana hili la wajapani kipindi hicho cha mjapani kutaka kumtawala mchina. Alipoitwaa alitoa usalama na kuinyoosha kwa yule muongeaji akawa wa kwanza, risasi ikafumua kichwa chake na wengine vivo hivyo, wakadondoka chini kama mizigo kisha akairudisha ile silaha kwenye chombo alichokikamata kijana aliyeileta ile silaha.

“ambia vijana watoe hiyo miili naweza kuichemsha mimi na kunywa supu yao, wamenitukanisha sana wajinga hao. Wanadhani kila kitu ni masikhara tu au ninyi mnadhani hapa tunatunga wimbo wa Taifa? Hapa tunacheza mchezo hatari na wenye mafanikio makubwa baadaye, ambaye amechoka kuongozana nasi aseme tu tumzike hai” alifoka Julio mahali hapo kisha kimya kikatanda kwa muda mfupi kisha vikohozi vya kuyaanda makoo yao kuzungumza vikasikika.

“jana kuna watu wamejaribu kutugusa makalio yetu kipumbavu tu, wametuulia vijana wetu wakati wakiwa kwenye burudani….ona sasa, nadhani mmeshaanza kuona uhatari wa hii kitu si ndiyo?” alisema Julio kisha akaacha swali la wote mezani. Wale mabwana walioko pale wakaitikia kwa sauti na wengine wakitikisa vichwa vyao.

“nataka waliofanya matusi ya kugusa makalio yetu jana usiku, watiwe mikononi na nizione sura zao hata kama kwa bahati mbaya mtakuwa mmezibadilisha kwa kuzijanyaga na katapila, muwalete tu” alisema Julio kisha akatazama kila upande wa wale watu walioko pale kisha akasema.

“Kijazi nakupa kazi hii ya kuandaa….hapana sio kuandaa, kutuma vijana wakunusa hizo harufu za waliotutusi jana. Hili liwe haraka na majibu yake niyapate mapema” akaweka tuo hapo kisha akanyanyuka na kutoka mule ndani.

Gazeti la Siri kali lilitoka machoni mwake akaliweka kando kisha akaitazama luninga kubwa iliyokuwa ikirusha habari za kutikisa nchi ambazo zilikuwa zikienda ukingoni. Pumzi nyingi zikamtoka. Alikuwa ndiyo kwanza asubuhi ya siku ya kwanza ilikuwa inamkuta lakini hii ilikuwa ni asubuhi njema sana kwa kazi yake. Alijaribu kuyaunganisha matukio mawili Roi lakini hakuona mambo ya kumuweka karibu na anachokitaka, akafikiri ni kipi cha kuanza kwa muda ule. Akalitwaa gazeti lile lakini si kwa kuirudia ile habari ya kuogopesha, habari iliyotokea kwenye Taifa hilo changa, habari ya hofu iliyoikumba Hospitali ya rufaa ya Pande.

“watu wanageukaje mafuvu sasa, hili mbona tukio baya mno, linaweza kutokea kweli tena kwenye taifa kama hili ambalo teknolojia bado haijatia pua?” alijiuliza lakini hakuwa na jibu la moja kwa moja, akaliahidi hilo gazeti kuwa ifikapo usiku atakwenda kushuhudia kwa macho yake mwenyewe, gazeti likamtazama bila kumjibu. Akauwacha huo ukurasa na kugeukia ukurasa mwingine huu ulikuwa ni wa tukio la Dampo. Hapa alitaka kujua jina la mwandishi, akachoka.

“Na mwandishi wetu….! Ni jina gani hili?” akajiuliza baada ya kusoma sentensi ya mwisho iliyokuwa ikisena Na mwandishi wetu halafu nukta nne kufuatia. Akalijengea jina lile maana nyingi ili lilete maana likakataa akaamua kuliacha lisomeke hivyo hivyo Na mwandishi wetu….! Hakukuwa na namba ya simu wala anuani za barua pepe. Hakutaka kujiumiza kichwa akalitupa mezani lile gazeti kisha akapata habari kutoka tumboni kuwa afanyalo wala si haki, hata kama yuko bize lakini mahitaji ya wengine ni muhimu. Njaa, tumbo lilikuwa likilalamika na ni kweli kwani hata alipokumbuka mara ya mwisho kutia kitu tumboni akagundua ni asubuhi ya siku iliyopita kwani mchana aliishia vijiko viwili tu vya chakula.

Akajikimbiza bafuni kukoga kisha akatoka na kuvaa akakiacha kile chumba kwa ajili ya kutafuta chakula na kujenga mazoea na jiji hilo la Pande.

Kipigo kikali alipokea Tereza mara baada ya kutengua kauli yake ambayo ilikuwa ni ahadi aliyoahidi mbele ya watu wale asiowajua dhumuni lao. Alikuwa akilia lakini akiahidi kuwa hato kwenda kinyume na maamuzi yake. Ulikuwa ni uongo mkubwa, alichezea kitasa kingine cha haja kilichomyumbisha hadi mzee Backa akahisi kitu kama upanga ukipita moyoni mwake kwa uchungu aliokuwa akiupata. Alitaka kusema kitu kwa watu wale ama kwa binti yake lakini hakuweza kwani gundi zito lilikuwa kinywani mwake akaishia kunyanyua mikono juu kama anayeomba dua kila kipigo kilipokuwa kikipita kwa binti yake.

“usitufanye sisi ni watoto wenzako, ulituahidi kuwa baba yako akija hapa unafanya kazi yetu eti, leo unakataa, hivi unajiamini nini wewe malaya?” alisema Lonto kisha konde zito likatua kwa Tereza hadi likamtupa chini kisha Lonto aligeuka nyuma na kuwaambia vijana waliokuwa wamemshika Backa wamtoe gundi. Backa akatolewa gundi lile na kubaki huru.

“ambia mwanao afanye kazi yetu kama mnauhitaji usalama wenu” alisema Lonto bwana mwenye makunyanzi usoni kisha akachukua msokoto mpya wa Bangi akautia moto na kujipa makali kichwani mwake.

“Tereza ni bora tufe sisi mahali hapa lakini usithubutu kufanya hiyo kazi hawa ni mashetani Tereza, wako duniani lakini wanaamini miungu ya kuzimu acha kabisa”

“etiiiiiii!!” aling’aka kwa mshangao mkubwa sana Lonto, hakuamini kama Backa angekuwa na amri nzito ya kudhoofisha kazi yao tena akiwa chini ya himaya yao wenyewe. Aliubana msokoto wake wa bangi vizuri kwenye papi za midomo yake kisha akageuka na kumshushia kipigo cha dakika moja hadi Backa akawa anahema juujuu.

“unajua hawa wapumbavu ni wajinga kweli, eti, hawaogopi kufa. Ha ha haaa! Wanataka kufa kuliko kutengeneza hii sumu, hawa ni wapumbavu kabisa, hawanijui hawa ndiyo maana wanaongea ujinga” alibwata Lonto kijana hatari anayesifika kwa kuuwa vibaya sana kuliko hata Kijazi. Huyu jamaa naye pia inasemekana alihusika na kifo cha mtoto wa waziri mkuu wa nchi ya Malawi kisha kukimbilia Ungamo, Ungamo na leo yupo chini ya himaya hatari sana ya Dr. Lee. Pamoja na kubwata kote kule na kutoa vitisho lakini Backa alizidi kumuasa binti yake kuacha kufanya ule ushetani. Akazidi kuzipandisha hasira za Lonto, akataka kushushiwa kichapo kingine lakini akasita baada ya kusikia sauti ya kufunguliwa kwa mlango mkubwa wa kutokea hapo. Macho ya wote pale yakatazama huko ulikofunguliwa mlango, aisee! Backa hakuamini, Backa alijikuta akisimama imara kabisa huku macho akiwa ameyatoa pima. Alikuwa ni Phili akiwa katika hali mbaya ya kushindwa hata kusimama, alikuwa akiburutwa kutokea ndani ya chumba kimoja hivi na mburutaji akiwa ni Lady Devil/Merina. Alimleta hadi hapo na kumtupa sakafuni kwa kishindo kizito. Phili alikuwa akipumua kwa shida sana lakini hakuweza kuongea chochote, aliyazungusha macho yake kumtazama Backa kisha akafumba na kukilaza kichwa chini sakafuni.

“angelikuwa anaweza kuongea angeliwaambieni amekutana na maswahibu gani, alipoingia huyu ni sawa na mtu aliye katika hatua ya mwisho ya kifo. Anamuona malaika mtoa roho lakini hawezi kuwaambia watu malaika huyo yukoje hadi anakata roho. Uanafikiri hapendi kusema kuwa malaika huyo anatisha kiasi gani? anapenda sema jinsi malaika huyo anavyotisha inasabisha hadi mdomo kupoteza uwezo wa kuongea na badala yake hubaki ukitetemeka kama mdhulumu wa mali za marehemu. Chumba alichoingia huyu ni zaidi ya anavyotisha malaika mtoa roho na ndiyo maana hawezi kuongea. Nataka ufanye kile ulichoahidi wewe binti ili kuokoa maisha ya huyu aliyekuwa katika hali mbaya” alisema Lady Devil huku akiwa amesimama karibu kabisa na kichwa cha Phili. Backa akamtazama binti yake, Tereza naye akamtazama baba yake macho yao yakakutana. Backa akatikisa kichwa kushoto kulia kukataa. Backa alikuwa akiona ni bora Phili afe kuliko akubali kufanya hiyo kazi. Alijua fika kuwa hao watu ni waongo na wanania mbaya na Afrika japo wengi wao humo walikuwa ni wa Afrika. Tereza akamtazama Phili, mlinzi wa karibu kabisa wa baba yake aliyekuwa tayari kufa ili maisha ya baba yake yawe salama leo anashuhudia akiwa katika hali mbaya huku baba yake akiwa ameridhia Phili afe. Tereza alishikwa na huruma sana akatikisa kichwa kumpinga baba yake lakini Backa alijibebesha ujasiri na kuongea kwa sauti kali na nzito.

“Phili yuko tayari kufa yeye lakini Taifa lake libaki salama, kuwa mzalendo kama Phili bi…..!” alishindwa kumalizia Backa baada ya kushudia Phili akihangaika huku damu zikimmwagika baada ya kisigino kirefu cha kiatu cha Merina chenye ncha kali mithili ya ncha ya mkuki, kikizama kwenye sikio la kushoto la Phili. Phili alikuwa akigaagaa pale chini pasipo kutoa sauti yoyote ile, sijui hata walimfanya nini huko ndani hadi kushindwa kuongea. Alionekana akipitia maumivu makali sana lakini alibakia kugumia tu na si kuongea chochote. Alikuwa akipiga miguu huku na huko bila kupata msaada, damu zilimwagika kila baada ya kile kisigino kuzama kwa urefu fulani. Kilizama chote kwenye tundu ya sikio kisha kukandamiza kwa nguvu hadi Phili alipotulia kimya kuonesha kuwa hii dunia si haki yake tena. Alikufa kifo cha kikatili sana lakini cha amani na ushujaa mkubwa. Backa alikuwa akimwagika machozi mengi huku Tereza akikosa ujasiri wa kutazama ule unyama uliokuwa ukiendelea mahali hapo. Aliyaziba macho yake kwa mikono yake, alipokuja kutoa ile mikono, alikuta Phili akiwa tayari ni mfu. Alilia sana masikini Tereza, alishindwa kujua ni kwanini ni familia yake tu ndiyo iliyokuwa ikiandamwa na manyanyaso ya namna ile. Nilikuambia Phili kimbia lakini hukusikia, ona walivyokuuwa kikatili kijana wangu, nenda kwa amani kifo chako na damu iliyopotea ipo siku itakuja kulipwa hata kama ni miaka mia na ushee. aliwaza Backa akiwa anautazama mwili wa kijana wake makini na mzalendo.

“kazi hii inatakiwa kuanza leo hata kama ni kuuwa wanaoweka kizingiti” sauti ya kutengeneza ilisikika ikitoke kwenye mlango mmoja, Backa alipogeuka alimuona mzee aliyejiziba sura kwa kinyago huku kichwa chake kikiwa kimelala kwenye bega la kushoto, nyuma kukiwa na mtu mwingine mrefu wa kirusi. Huyo mrusi kidogo alianza kumjengea mashaka na hofu. Sura yake ni kama ilimkumbusha kitu fulani lakini alipuuzia kwa sababu alipata habari kuwa mmiliki wa sura ile anayoikumbuka alishajiuwa kwa sumu baada ya kutaifishiwa mali zake zote ndani ta Nchi ya Ungamo kipindi hicho yeye akiwa ni waziri mkuu. Macho ya yule kijana wa kirusi yalikuwa yakimtazama Backa tu huku yakionekana kuwa na hasira kuu kwa mzee huyo.

“nilitegemea kazi imenza, nini kimefanya mchelewe namna hii sasa?” alihoji Dr. Lee.

“huyu mzee analeta kipingamizi sana, anajaribu kumzuia binti yake asifanye kazi yetu” alisema Lonto.

“oooh! Wewe binti anza kazi bwana kwa hiyari yako achana na maneno ya hawa watu wanaweza kutugombanisha bure” alisema Dr. Lee kwa sauti ya ubinadamu kama ni mtu vile lakini Backa akapanda juu kwa sauti kali na kusema kuwa binti yake hawezi kufanya kazi yoyote ile. aisee! Ni bora asingethubutu kuongea kitu basi, angekaa kimya tu. Alikuwa amezipandisha hasira za mtu mwingine kabisa aliyeshindwa kuvumilia.

“ni wewe kabisa, ni wewe kweli, baba alifanya vizuri sana kuiacha sauti yako kama ushahidi. Unakumbuka wewe ulifanya nini kwa baba yangu kipindi upo madarakani? uanakumbuka wewe kweli?” aliongea kwa hasira sana Bencov akiwa ameiva macho. Akamtazama Backa kwa karibu sana kisha akasema.

“kama hukumbuki ngoja nikukumbushe.

MWAKA 1989 PANDE.

Gari tatu zilitimua vumbi kali sana, zilikuwa ni gari za kifahari zenye rangi nyeusi, zilipiga break kali mbele ya lango kuu lililokuwa bado linadai kabisa lenye maandishi makubwa BBD MINING COMPANY. Lango hilo lilifunguliwa kisha gari hizo kuingia ndani na kwenda kuegeshwa mahali pa maegesho. Wanaume wawili na mwanamke mmoja walishuka kila mmoja kwenye gari yake wakaelekea ndani ya jingo kubwa. Walikutana ndani ya ofisi moja tulivu sana lakini si kwa idadi ile ya awali, walikuwa si chini ya kumi wote wakiwa na asili ya Kirusi.

” Benson!” aliita mmoja wa wale jamaa waliongia na zile gari. Mwanaume mmoja akaitikia kisha yule aliyeita kuendelea.

“ni kweli hii inayoendelea hapa?” akauliza.

“sikiliza Bacon, mbona sisi tulikamilisha kila kitu na hati zote na mikataba ya uwekezaji tunayo na serikali wanaitambua wanasemaje sasa kuwa tumeghushi mikataba na tunawekeza kinyume na taratibu?” akauliza Benson. Bacon akachoka. Akalitazama jopo lote lililopo pale kisha akasema.

“tupo kwenye hali mbaya sana kwa sasa, kuna hatihati ya kuipoteza kampuni yetu. Serikali inasema kuwa sisi tumewekeza kinyume na taratibu na wanatuhitaji kwa ajili ya kujibu hili” alisema Bacon akiwa ni mwingi wa hasira sana. Watu wote hapo wakabaki kimya kila mmoja akajikuta akiwa hana neno la kusema.

“kaka tunafanya nini sasa mbona mimi sielewi, ujue wanatuchanganya” aliuliza Dede wakiwa kwenye ofisi yao. Bacon akajibu kuwa hata feli ni lazima washinde hili jambo kwani kila kitu wanacho na kipo kisheria, watashindwaje sasa kisha akawagiiza hao ndugu zake kuwa wahakikishe wanasubiri huo wito kisha waelekee huko watakakohitajika yeye anakwenda kuchukua wanasheria wake wanaoijua sheria duniani ili kuweza kuja kuikabili kesi hiyo ambayo kwao ni kubwa sana na kama wakishindwa ni wazi wanaweza kuchanganyikiwa kwani wamewekeza pesa nyingi sana ambazo kama zikipotea ni wazi watajikuta wanafilisika kiuchumi. Bacon akapanda ndege kurudi urusi huku Dede na Benson wakibaki kusubiri wito wa serikali lakini wakati wao wanasubiri upande mwingine kwenye ofisi moja ya serikali mambo yalikuwa hayasemeki. Kulikuwa na kikao ambacho kilimhusisha waziri mkuu Mh. Backa Ramson Backa, Waziri wa wizara husika ya mali asili na utalii sambamba na viongozi wachache lakini akiwepo na Rais pia. Kulikuwa na mjadala mzito ulikuwa ukiendelea tena mjadala huo ulikuwa ukimuelemea Backa pekee.

“kwanini asiende Waziri wa wizara husika, asiende makamo wa Raisi na niende mimi, mimi ningekwenda kama hawa wasingekuwepo” alijitetea Backa.

“kwanini unataka kunipinga” aliongea Rais Julio.

“siyo kukupinga mkuu nilikuwa natoa wazo hilo na ndivyo inavyotakiwa kuwa”

“sasa mimi ndiye mwenye maamuzi na sauti ya mwisho, nikisema utakwenda wewe si kama nakuonea bali ni kukamilisha wajibu wako. Hatuwezi kuwavumilia hawa watu ikiwa wanatunyonya sisi. Kwanza wewe una sauti kubwa ndiyo maana nimekuchagua/nimekuteua uende wewe” alisema Mh. Julio. Backa akawa hana neno la kuongeza akabaki kutulia.

“kuna askari wapo nje hapo wanakusubiri nenda, utaongozana nao hakikisha unawatia nguvuni wamiliki tu wa huo mgodi Backa” alitoa agizo Rais Julio. Backa alitoka humo ndani na alipotoka, aliwakuta kweli askari wakiwa wanamsubiri kisha akaondoka nao kuelekea kwenye kampuni ya uchimbaji wa madini ya BBD. Kampuni inayomilikiwa na watu watatu kutokea nchini Urusi. Walifanikiwa kuwatia nguvuni na kuondoka nao kwa utaratibu kabisa bila shida au shaka yoyote lakini wakati wako njiani wakiwa wanaelekea kituo kikubwa cha polisi, kuna uvamizi mkubwa sana ulitokea ambao ulimchanganya sana Mh. Backa. Askari wakajitahidi kupambana lakini haikusaidia kitu wale wamiliki wawili wa kampuni ya uchimbaji madini ya BBD. wakauwawa. Lilikuwa ni tukio lililomchanganya sana Mh. Backa alichanganyikiwa kupita kiasi. Kwanini hakufa askari hata mmoja, kwanini hakujeruhiwa mtu hata mmoja na wamekufa wao tu? Alijiuliza Backa maswali hayo lakini hakuna jibu lililojitokeza kirahisi. Akazifikisha ripoti hizi kwa mkuu wa nchi lakini bwana Julio alizipokea kama ajali ya kugongwa Mbwa tu, hili halikuwa jambo aliloliwaza sana akamua kuliacha liende na maji kama machozi ya Samaki baharini. Hakujua chochote kile lakini baada ya muda mfupi habari zikavuma mitaani

kuwa mmiliki mwengine mkubwa bwana Bacon amejiuwa kwa sumu kali sana. Hii lilikuwa ni jambo la huzuni kubwa kwa Backa lakini kwa Mh. Julio Mobande halikuwa jambo la kusikitisha. Miaka ikakatika. hakukuwa na uendelezaji wowote wa kuiendeleza ile kampuni. Backa akajiuliza nini sababu ya kuwafukuza watu ambao walikuwa wakilipa kodi japo si kubwa. Lengo la Rais na waziri wa mali asili na utalii yalikuwa ni nini mbona kampuni ile inaoza. Wachimbaji wadogo wakaomba wajipatie kidogo kitu Rais na wizara yake waligoma kabisa na kusema kuwa eti serikali inampango mzuri na mgodi ule na utakuwa na maendeleo makubwa kwa Taifa. Wananchi wa Ungamo wakatulia pasipo kusema kitu kingine. Baada ya muda wa kama mwaka mmoja mbele Backa akatumwa na Rais awatangazie wananchi kuwa sasa muda si mrefu nchi yao inakwenda kuwapa neema ya kuwaruhusu wachimbaji wadogo waweze kujichimbia baada ya kupewa maeneo. Backa akajitengenezea sifa ya kuwa yeye ndiye alijaribu kumshawishi Mh. Rais na kuweza kukubali kufanya jambo hilo. Miaka ikakatika bila jambo hilo kukamilika, miguno na malalamiko mtaani ikazaliwa, waziri mkuu akakutana na lawama za wanachi kwa kuwadanganya akashindwa kuwapa jibu kwani kila alipo mfuata Rais na kumkumbusha juu ya kile alichomtuma kwa wanachi, Rais alijibu kuwa kila kitu kinakwenda kwa mipango, mipango bado haijakamilika hivyo atulie.

Jambo la kushtuka likaibuka baada ya miaka kama minne kupita, ni baada ya kuja wageni wenye asili tofauti. Hawa walikuwa ni watatu pia lakini hakukua na Mrusi hata mmoja. Alikuwepo raia mmoja kutokea Brazil, mwingine muingereza na huyu wa mwisho alikuwa na ngozi nyeusi ya maji ya kunde alionekana kama mmarekani. Kitu kilichowaacha watu hoi ni kwamba watu hawa walikuja kwa lengo la kuwekeza hapo nchini na waliwekeza kwenye ileile kampuni ya BBD. pia walitumia jina lilelile la kampuni ile B.B.D MINING COMPANY. Majina yao pia yalikuwa ni yale yale ya wale wa kwanza ambao wawili waliuwawa kwa kushtukiza na mmoja kusemekana kujiuwa huko kwao Urusi. Hata walipoulizwa ni kwanini wanatumia majina hayo ya wamiliki wa awali, wakijibu kuwa hawakutaka kwenda mbali na jina la Kampuni hiyo pia ikiwa ni kuwarudisha wateja wao. Kimya kikatanda kazi ikafanyika Taifa likafaidika kweli lakini kumbe ndani kwa ndani kulikuwa kuna mambo mazito yaliyokuwa yakisukwa na yalikuwa ni mambo ya kuja kulipiza kisasi cha wale watu waliopotea. Hakuna aliyejua kati ya Backa na wananchi lakini ni wachache tu ndiyo waliokuwa wkilifahamu jambo hilo. Backa anakuja kushtuka haya baada ya kustaafu uwaziri na kuamua kuishi maisha yake. Julio ndiye aliyeusuka mpango huo wa kumgeuka Backa.

“uliniulia wazazi wangu Backa, uliwauwa wote bila kujua kama unaniweka mimi katika wakati mgumu wa kuweza kuishi. Ulimuuwa baba yangu mdogo na shangazi yangu kwa kuwamiminia risasi barabarani baada ya kuwatia nguvuni kinafiki kwa kuwaambia kuwa wanawekeza ndani ya Taifa lile kinyume na taratibu. Ulijitapa sana kuwa wewe kama waziri mkuu mwenye sauti ya juu, unapesa za kuweza kumfanya Rais asikohoe wala kusema ama kupinga kitu chochote kwako. Wewe ndiye mwenye mamlaka na sauti ya mwisho. Baba yangu mzazi alipozipata taarifa za kuuwawa kwa ndugu zake, hakuweza hata kuiagiza miili ya ngugu zake akajiangamiza kwa sumu. Alikufa baba yangu Backa sababu ni wewe lakini aliamiani mimi nitazaliwa tu. Aliniacha tumboni mwa mama yangu nikiwa ni mtoto wa kwanza na wa pekee hivyo akaacha ujumbe wangu kwa mama yangu dhidi ya Taifa lako lile ulilokuwa ukiringa nalo. Akaacha ushahidi wa kutosha kwenye makaratasi, ilikuwa ni pamoja na mikataba ile ya halali ambayo wewe na watu wako wachache mliibadilisha na kusema kuwa baba yangu alighushi aisee! Niliapa kukuuwa kifo kibaya sana lakini kuna Mtu mmoja tu ndiye aliyenifanya niwe mpole. Huyu ni Rais wako Julio. Alinipa maneno mengi sana kuhusu wewe na kikubwa ni kwamba alisema ni ukwasi wako uliokuwa nao ndiyo iliokuwa ukikupa kiburi hivyo ameniahidi kuwa nami bega kwa bega ili kuweza kulipa kisasi cha wazazi wangu. Huyu ndiye aliyeniambia kuwa unaye binti ambaye ni mtaalamu wa masuala ya utengenezaji wa madawa ya mimea na amesoma kwenye vyuo mbalimbali duniani. Nikafanya chunguzi zangu kweli nikagundua kuwa binti yako amebobea kwenye Sayansi ya mimea. Tereza atanisaidia sana kwasababu yeye ni Botanist (ana elimu ya utafiti wa mimea). Pia ni mbobezi wa Fitopatholojia (mtafiti wa magonjwa ya mimea). Alikuwa na mpango mzuri sana huyu na bara lake la Afrika na alishafanya utafiti wa kutosha mwisho akaamua kutengeneza dawaya ya ukuzaji wa mimea kwa muda mfupi huku ikiwa na uwezo wa kupambana na hali ya ukame. Akaamua kujikita maabara kwa miaka kadhaa na kufanikiwa kutengeneza hiyo dawa inayofahamika kwa jina la DIET PILLS. Ilikuwa ni dawa yenye manufaa makubwa sana kwa bara zima la Afrika kama ingeanza kutumika lakini nasikitika kwani dawa hiyo inakwenda kubadilishwa na kuwa sumu mbaya kabisa kwa ajili ya nchi moja tu ya kwako. Diet Pills itachanganywa na michanganyiko mingine kisha kuwa sumu hatari itakayokwenda kuotesha mimea sumu itakayoangamiza Taifa lako kwa kasi kubwa huku Diet Plls ikitangulia kuwahadaa watu wako. Hii itapendeza sana.” alimaliza kutoa simulizi ndefu kabisa Bencov, simulizi iliyomfungua masikio Backa na kumfahamisha mengi ambayo alikuwa hayajui.

“ndiyo maana Julio hakuwa na msaada na mimi kabisa wakati matatizo yote yale yakitokea, kumbe yeye ndiye msababishi. Kipi nilikosea hadi anitengenezee hukumu ya namna hii? Nilijitoa sana kwa mali na hali kipindi cha uongozi wake lakini mbona ananiuwa sasa tena na familia yangu? Mimi niliwauwa wale wawekezaji kweli? Si tulivamiwa barabarani na kisha kuuwawa?” aliwaza Mh. Backa huku akiwa amesimama asijue hatima yake mahali hapo. Bencov akawa ndiye muongeaji mkuu kwa muda huo mahali hapo. Alipiga hatua ndefu hadi pale alipokuwa amesimama Tereza kisha akamtazama usoni akasema.

“utatengeneza dawa kwa kutufuata sisi na siyo kufuata kauli au amri ya baba yako sawa, kwasababu kufanya hivyo ni kuharakisha kifo cha baba yako mapema. Kila kitu kipo kwenye tube maalumu kuanzia kemikali hadi michanganyiko mingine ni wewe tu kuanza kazi kinyume na hapo naanza sasa kukuonesha kuwa mimi ni adui mbaya sana kwa baba yako….nenda kwenye ule mtambo na uanze kazi sawa?” alisema Bencov na kutoa amri kwa Tereza. Binti huyo akaweka ngumu na kuzidi kusimamia msimamo wake kuwa hata wafanye nini hawezi kufanya hiyo kazi. Alisema hivyo akiwa anatetemeka sana kwani alijua fika kuwa hapo wako na viumbe wasio na utu hata kidogo kwani kifo cha Phili alichokishuhudia, kilikuwa ni cha kinyama sana hivyo alikuwa na wasiwasi na uhai wake na wa baba yake pia. Backa alikuwa akimwaga machozi mtindo mmoja mahali hapo kama mtoto mdogo.

“nenda”

“siendi!”

“fanya tunachokuelekeza binti”

“sifanyi!” alizidi kukazia msimo wake Tereza.

“nenda….moja, nenda….mbili” akanyamaza Bencov. Tereza akamgeukia baba yake na kumtazama usoni, Backa akamtazama binti yake na kumwambia kwa ishara kuwa asifanye, alikuwa akitingisha kichwa Backa mtindo mmoja huku alkionesha kuwa kweli alikuwa akimkataza binti yake huyo kwa dhati kabisa.

“nenda….tatuuu!”

“siendiiiii!!” Tereza alijibu huku akilia kabisa kuonekana kuwa hataki na wasimlazimishe afanye wanavyotaka.

“now!!” Bencov alipiga kelele za kutosha sana sauti ikajaa kwenye kile chumba na kutengeneza mwangwi mkubwa mno kisha kimya kizito kikatanda. watu wakawa wanatazamana usoni wasielewe nini kitakachojiri mahali hapo. Kimya kile kizito kikasababisha sauti ya viatu iweze kusikika vema ikitua kwenye sakafu ya humo ndani hii iliashiria kuwa nyuma yao kulikuwa kuna kiumbe kilikuwa kinajongea kuja mahali hapo. Wote wakageuza shingo zao nyuma kutazama kasoro Backa pekee ndiye aliyekuwa hakugeuza shingo, alijua nini kinakwenda kutokea muda mfupi kwake, alijua na ndiyo maana hakutaka kujisumbua kumtazama ajae.

“hata kama nitakufa sasa Tereza, usithubutu kutengeneza hiyo dawa, utakwenda kuangamiza taifa lako mwanangu, utakwenda kuuwa ndugu zako mwangu” aliongea kwa uchungu sana Backa lakini hakukuwa na aliyekuwa akimjibu mahali pale. Macho makali yenye chuki dhidi yake kutoka kwa Bencov, yalikuwa yakimtazama yeye tu muda wote. Bencov alikuwa akiumia sana kila akisikia maneno hayo kutoka kinywani mwa mzee huyo.

“Dr. Henry Cartley, nini unangoja nimesema now!” alifoka Bencov huku macho yake yakizidi kuwa mekundu kwa ghadhabu. Dr. Henry alikuja na kukamata kichwa cha Backa kisha akachoma sindano kwa nguvu sana shingoni kisha akatulia. Backa alipiga kelele kali mno, kali mno, siwezi hata kuelezea. Zilikuwa ni kelele zilizokimeza chumba hicho pamoja na jumba lote la himaya hiyo kisha Dr. Henry, Dr. mwenye roho mbaya, alilikamata bomba lile la sindano vizuri na kumimina dawa nyekundu iliyokuwa imejaa kwenye lile bomba, ilikuwa ni mfano wa damu. Aliimimina yote mwilini mwa Backa. Backa akaanza kutetemeka kama kuku aliyechinjwa na kuachiwa, alitikisika mwili mzima mzee huyo kisha akaachiwa chini kwa kishindo kikubwa. Akapapatika kwa dakika chache kisha kimya kikafuatia, Tereza alilia sana, alilia kupita kiasi lakini hakuna aliyemhurumia maeneo hayo. Backa alinyanyuliwa kisha akasimamishwa, alikuwa ni zezeta tayari, anatazama lakini haoni au anaona lakini hajui anaona nini au hata kama anajua lakini hawezi kusema kitu. Macho yake yote yalikuwa yamejaa wekumbu hadi mboni nyeusi ikawa imebadilika rangi na kuwa ya kijani.

“baba yako ataishi katika hali hii maisha yake yote kama utakuwa mkaidi, atakula kwa mashine na atapitia maumivu makali mno ambayo binaadamu yoyote yule hakuwahi kuyapitia, maumivu hayo yatakuwa yakimrudia kila baada ya masaa nane. Fanya yetu tuliokuagiza kisha tukupe Ant brynaptic poison kwa ajili ya kumponya baba yako kinyume na hapo ataishi hivi milele au tumuongeze Brynaptic poison nyingine ili afe kabisa” yalikuwa ni maneno ya Dr. Henry hayo akimwambia Tereza ambaye alikuwa kimya kama aliyekuwa akinyolewa, kinywa chake kilikuwa wazi na kujikuta akiangusha kilio kizito kila akimtazama baba yake jinsi alivyokuwa zoba kwa muda mfupi tu. Muda huo huo Backa akaanza kukakamaa kama nyoka aliyemwagiwa mafuta ya taa alikuwa akipiga kelele za maumivu makali. Mishipa ya damu ilitutumka kila kona ya mwili wake, mwili wa Backa ulitisha kwa muda huo mfupi sana. Dr. Henry alimvua Backa shati na kumbakiza kifua wazi. Mwili wake ulikuwa hautamani kuuangali, ulikiwa umetengeneza kitu kama mizizi midogo midogo mwilini mwake. Alikuwa akikakamaa hadi watu waliomzuia wakawa wanashindwa kuhimili uzito alionao. Mwili ulijaa kijani tupu na ramani ya mishipa ya damu iliyokuwa ikitisha mno. Dr. Henry akasema.

“hii sumu ni hatari sana na makazi yake ni kwenye mfumo wa usukumaji damu, inaishi kwenye moyo hii sumu na kila baada ya muda inatutumua misuli na kusababisha mwili wa huyu mtu kukakamaa kutokana na sumu hiyo. Haya ndiyo maumivu atakayopitia baba yako kila baada ya masaa nane hadi mungu atakapomuonea huruma na kumchukua au wewe kukamilisha kazi yetu haraka na kuweza kumponya.”

Ile hali ilimtisha sana Tereza, moyo ulimuuma kupita kawaida hakuwahi kuona unyama wa namna ile kwenye maisha yake yote hapa duniani. Alipokuwa akipokea yale maneno ya dokta Henry, pumzi zilimbana na kumfanya kushindwa kupumua sawasawa hatimae akadondoka na kupiga kichwa chini, Tereza akapoteza fahamu. Taharuki nyingine ikazuka, hofu na mashaka. Ilikuwa ni lazima binti huyo apone haraka ili atengeneze hiyo dawa. Akakimbizwa kwenye chumba cha matibabu huku Backa akipelekwa kwenye chumba ambacho ataishi humo hadi watakapomzawadia kifo.



Harakati za watu hufanywa na watu wenyewe hivyo hupatwi na mshangao pale kweye harakati hizo unapokutana na watu wakiwa kwenye harakati pia. Pengine mwanzo wa kitu huleta mwisho wa jambo jingine je, vipi kuhusu hili neno la mwisho wa kitu kimoja ndiyo mwanzo wa kitu kipya? Maswali kama haya si wengi sana wanaojiuliza mimi naamini hivyo lakini likiija swali jingine la ni nani wanaojiuliza maswali haya pengine jibu laweza kuwa sijui. Maswali haya huwa hayana mwanzo wa kujiandaa, haya huja tu yenyewe na kukufanya ujiulize juu ya kujiuliza na mwisho wa siku hata jibu la maswali uliojiuliza ukajikuta unajiuliza ni wapi utayapata……

“yule binti ni nani aliyekuwa akiniimbia ngonjera zake zisizoeleweka usiku wa jana” yalikuwa ni miongoni mwa maswali machache kati ya mengi aliyokuwa akijiuliza Tamimu. Harakati zake zimeingiliana na harakati za mtu mwingine au ni vipi?

“habari yako kaka……naweza kuka…..samahani kwa kukuingilia kwenye…….sina shida na wewe ninashida na wale pale……!” alizidi kukumbuka maneno ya huyo binti aliyekutana nae usiku uliopita.

“ameuwa mtu mmoja na ni yule aliyemfuata kule maliwatoni, ni yeye aliyeuwa hakuna mwingine kwasababu alisema hana shida na mimi bali alikuwa na shida na wale vijana walevi” alijisemea kwa sauti ya kichoyo kisha akachukua gilasi ya maji akanywa kidogo na kuishikilia mkononi, akapiga hatua ndogondogo hadi dirshani akiwa na ile gilasi ya maji.

“huyu ni nani sasa? hawezi kunifaa kwenye kazi yangu? Hawezi kunifaa kweli huyu kwenye harakati zangu za kumtafuta mpenzi wangu? Atanifaa huyu lakini….hapana atanifaa kwasababu hawezi kunilenga halafu asiwe na kitu cha ziada cha kunifaa kwenye harakati zangu” alizidi kuwaza Tamimu akiwa ndani ya jumba lake kubwa la kifahari. Aliitazama ile gilasi kisha akanywa maji yote yaliyokuwa yamesalia kisha akarudi mezani akaiacha ile gilasi akatoa simu yake ya kisasa mfukoni akapiga mahali.

“kikao ni muda gani na lini hao wageni wanakuja?” aliuliza baada ya upande wa pili kupokea, akatulia kidogo na kusema.

“ok, nakuja sasa hivi mwambie Martan watu wake wasikose kwani kikao hicho kinawahusu sana” akasema na kukata simu baada ya kujibiwa vema na upande wa pili kisha akatoka mule ndani.

“kaka natoka ila sijui nitarudi muda gani kwasababu ninakikao leo halafu kesho ninawageni watakao kuja kwa ajili ya kufanya makubaliano ya kuingia kwenye mkataba wa kibiashara” alisema Tamimu.

“sawa Boss hakuna kitakacho haribika” alijibu huyo mtu anayefahamika kwa jina la kaka. Tamimu alielekea maegeshoni akabonyeza rimoti yake ndogo kisha akaingia kwenye hiyo gari iliyoitika akaondoka kwa kasi kama kawaida yake. Kwa upande mwingine hata Petii alikuwa na maswali juu ya kijana wa jana kuweza kuuwa wale watu waliokuwa na majigambo, alijiuliza sana lakini hakuwa na jibu la kuweza kumuweka katika hali nzuri. Yeye akaweka nadhiri kuwa ipo siku atakutana nae na atajua ni nani kijana huyo wakati mwenzake amepanga kumtafuta ili amjue. Hawa wakawa wanacheza mchezo wa kuigiza huyu akiwa hana haraka na mwenzake kwa kauli ya kusema muda wowote akikutana nae ni sawa tu, huyu mwingine akiwa na hamu ya kumtafuta ili amjue. Petii wakati anamawazo hayo alikuwa ndani ya hoteli aliyofikia na hakupenda kutoka nyakati za mchana mara nyingi alikuwa akitoka usiku tu kwa ajili ya kazi yake huku kwa wengine wakiwa ndiyo muda wao wa kufanya unyama na ushetani.

“tunazo gari thelathini (30) kwa sasa ambazo ni za kisasa na zilizotengenezwa kwa mfumo mpya na wa kipekee sana, zina nguvu kubwa na zina pawa ya Horse 800 hadi 900 ni nguvu ambayo haijawahi kutokea duniani” alisema kijana mmoja mbele ya watu wengi ambao walikuwa ni wafanyakazi wa Tamimu. Hawa wote ndiyo waliounda kampuni kubwa ya magari yaendayo kasi ya T.N RACE.

“mfumo uliotumika ni ule nilioutaka si ndiyo?”

“gari kumi na tano tumetumia mfumo ule lakini gari kumi na tano nyingine, tumetumia mfumo mwingine kabisa ambao uko juu zaidi ya ule ambao umependa tuutumie” alijibu kijana yule msemaji.

“Morde unauhakika na hili ulisemalo? Unajua hii kampuni yetu bado ni changa sana na inahitaji kuingia kwenye mashindano na kampuni kubwa duniani?” alionesha mashaka Tamimu juu ya mfumo mpya alioutumia Morde katika uundaji wa magari.

“nadhani baada ya hapa ningependa kuongozana nawe hadi kwenye hizo gari mkuu” alisema Morde. Kikao kikaendelea, kilikuwa ni kikao kihusucho ‘competition’ ya magari ambayo itakuja kufanywa na wageni watakao kuja ili kuweza kuitangaza kampuni hiyo ya TN. RACE.

“nimefarijika sana hivyo basi, Martan utakuwa na mimi kwenye kazi hiyo ya kuonesha uwezo wa gari zetu nadhani tutakuwa sambamba na vijana wako wawili, ninahitaji gari nne tu kuweza kuingia kwenye mashindano hayo” alisema Tamimu kisha akaamka kutoka kwenye kiti alichokuwa amekalia akapiga hatua mbili tatu hadi mahali ulipo mlango wa kutokea kwenye banda kubwa lililokuwa likitumika kuhifadhia hizo gari akasema.

“jamani hakuna mashindano rahisi, hawa watu ni lazima watakuja na watu wao kwa ajili ya kutupima, sasa sitopenda kuiabudu ile kauli ya kwenye miti hakuna wajenzi. Mazoezi ya nguvu na jioni nitahitaji kuona uwezo wa hao vijana watakaopambana nami hapo kesho” alipomaliza kusema hivyo akatoka mule ndani. Morde alimzunguusha kijana huyo kwenye gari zote hadi mwisho. Tamimu alifurahi sana kuziona zile gari hata hizo zilizotumia mfumo mpya kabisa katika utengenezaji wake pia aliziona na akazipenda.

“zipo gari ishirini na tisa tu pale Morde hiyo moja iko wapi?” aliuliza Tamimu baada ya kuwa amekaa mahali na kijana huyo mtundu.

“nilijua tu hilo utakuwa umeling’amua, hiyo moja sikuiweka pale na haitakuwepo kwa ajili ya majaribio. Ni gari ya tofauti sana na inaumbo dogo mno na ina kasi ya pekee sana. Ni gari ambayo kiukweli nimeibuni mimi mwenyewe na hakuna mtu ambaye nilitaka ahusike kwenye ubunifu wa gari hiyo. Baada ya kutoka kwenye kutazama vijana wakifanya mazoezi tutakwenda huko nilikoihifadhi hiyo gari kiongozi ili ukaishuhudie” aliongea Morde mahali hapo na kumfanya Tamimu asiwe na maswali tena kwa kijana huyo waliagana kisha Tamimu akatoka humo ndani akapanda gari yake hadi Hospitali kwenda kuutazama mwili wa baba yake uliokuwa bado hauja zikwa hadi muda huo.

Wakati hayo yote yakiwa yanaendelea huko uraiani Roi alikuwa chumbani kwake akitazama luninga iliyokuwa ikirusha matangazo kuhusiana na tukio la siku inayofuata ya mashindano ya magari ambayo si ya mbio ndefu wala nini bali yalikuwa ni mashindano maalumu ya kibiashara na ikiwa ni kama kuingia majaribioni kwa gari mpya kabisa kutoka kwenye kampuni mpya inayomilikiwa na kijana mdogo Tamimu.

“napenda watu wengi waje washuhudie mashindano hayo ya aina yake ambayo hayakuwahi kutokea hata siku moja kwenye Taifa hili la Ungamo, ni mashindano ya kwanza hivyo nategemea kupata sapoti kubwa sana kutoka kwa wananchi wenzangu” alikuwa akiongea Tamimu mara baada ya kukutana na waandishi wa habari na hapo alikuwa akijibu maswali machache kutoka kwa waandishi hao.

“vipi kuhusu barabara, utatumia barabara gani labda?” lilikuwa swali jingine kutoka kwa mwandishi wa habari. Tamimu akajibu.

“aaah! Kiukweli kabisa sina shaka na barabara kwani eneo nililonalo ni kubwa sana na mashindano hayo kwa kuwa ni ya kibiashara na kutokana kuwa kampuni zote mbili ni zao la nchi hii ya Ungamo, tumefanya maongezi na serikali tukaomba waturuhusu tutumie barabara ya K2 hadi Muavengero juu kwa muda mfupi tu kisha mengine yote yatamalizikia kwenye uwanja wangu mkubwa kabisa ambao unauwezo wa kuingiza watu wengi sana nafikiri ni zaidi ya watu elfu tano kwa makisio”

“vipi kuhusu usalama sasa, unawahakikishia usalama watazamaji watakao kuja kutazama mashindano hayo?” aliuliza mtangazaji mwingine kwenye mahojiano hayo mubashara.

“usala upo, wasijali kuhusu usalama, usalama upo tena upo usalama wa kutosha kabisa” alijibu kwa kujiamini sana Tamimu.

“lakini nadhani hadi sasa mwili wa baba yako haukufanyiwa mazishi, unawezaje sasa kufunya haya mambo wakati baba yako bado yuko kwenye chumba cha kuhifadhia maiti?” swali hili kiukweli lilimfanya Tamimu kuwa mpole sana hakutaka kusikia habari za baba yake kwani zilikuwa zikimpa uchungu sana, alitaka kumzika mapema tu ili haya yote yasije kujitokeza lakini imeshindikana kutokana na Backa kumzuia na kumwambia kuwa kuna mtu maalumu ambaye angetokea na kufanya uchunguzi wa kina kwenye mwili wa baba yake pamoja na wale askari wawili hivyo auwache na atauzika tu muda ukifika. Hakupenda kuulizwa hilo na mara nyingi anapoulizwa swali hilo huwa anapoteza kabisa nguvu hata ya kuongea. Alijibu kwa unyonge sana.

“nafanya haya yote kwa ajili ya baba yangu na ninaimani hata yeye atafurahi, namuahidi kuwa nikimaliza haya basi na yeye nitampeleka kwenye nyumba yake ya milele” alijibu hivyo kisha akanyanyuka hakuwa tayari kujibu swali jingine lolote, machozi yalikuwa yakimdondoka kama maji, hakujua kama kufanya vile ni kutoa mwanya kwa wapinzani wake ambao nao wanahitaji kuingiza kampuni yao kwenye ubora wa dunia.

“huyu kijana baba yake naye aliuwawa?” alijiuliza Roi akiwa pale ndani baada ya kuzima luninga.

“kwa hali ile hawezi kushinda hata kidogo na ni lazima kampuni yake ianguke vibaya sana sasa kama kampuni yake itaanguka, ni wazi kuna watu lazima watamfilisi huyu mtu au aingie kwenye matatizo na serikali yake. Kuna kitu hapa nahitaji kukifanya ili niweze kuianza hii kazi kupitia yeye, nataka kujua ni nani walihusika kwenye mauwaji ya wale askari ikiwezekana. Kuna kitu natakiwa kukifanya na hicho kitu ni vema kama kikianza sasa” alikuwa akizidi kujiuliza na kujishauri kijana huyo alikuwa na mengi ya kufanya ili kuweza kuingia katika uchunguzi wa kujua ni nani aliyethubutu kuwauwa askari wale wa Tanzania.

“Hah hah haaa! Hili ni pigo baya sana” alisema mtu mmoja mweusi huko Sami Ado. Mji ulio mbali kabisa. Huu ulikuwa ni mji ulio ndani ya Taifa hilo la Ungamo lakini Mji huu ulijitenga sana kiasi kwamba watu wa Sami Ado wakajiona wao sio wa nchi hiyo.

“hili litakuwa ni jambo jema kweli Mike?” aliuliza mtu mwingine mfupi na mnene aliyekuwa amevaa nguo ya moja kwa moja kama wale watu wa Nigeria.

“kabisa na hili litakuwa ni ushindi kwetu, subiri nimfikishie Don dou uone atakavyo farijika” alisema Mike kisha kuondoka hilo eneo.

“Dooon”! aliita kwa sauti kubwa Mike kisha mtu mnene sana mwenye ndevu nyingi nyeupe akaitikia kwa sauti kubwa iliyoshiba fedha na jeuri ndani yake.

” Don dou” kisha akageuka kumtazama kijana huyo mweusi aliyekuwa akimuamini sana kwenye masuala ya chunguzi mbali mbali kisha akaweka ulizo kwa kijana huyo.

“nini Mike?”

“nilikuambia Don, hakuna kampuni inayoweza kuishinda kampuni ya Don dou iwe kwa kumwaga daumu ama kwa nini. T.N. RACE. tu, alikuwa ndiyo kampuni inayotusumbua vichwa vyetu kati ya kampuni zote tulizowahi kushindana nazo, hii ilikuwa ndiyo pekee yenye gari imara sana…..!”

“sasa vipi, mmeharibu uimara wake na unataka kuniambia haina haja ya kumuua huyo mmiliki wa TN. RACE. tena na THE BLACK SKELETON DON DOU itabaki juu?” alikatisha Don kwa maswali kadhaa…..

“hakuna haja ya kumpiga au kumuuwa huyo mtoto mdogo bali tutatumia pigo la baba yake” alisema Mike.

“pigo la baba yake? Baba yake amefanya nini?” aliuliza kwa mshangao Don na kuiona hoja hiyo ni ya kitoto sana lakini Mike akamtoa hofu Don na kumwabia kuwa, kijana huyo baba yake aliuwawa hivi karibuni na hadi muda huo mwili wake haujazikwa kwa madai ya kusubiri uchunguzi. Sasa wakati akiwa anafuatilia matangazo ya majigambo ya Mmiliki wa TN RACE, ndipo akagundua kuwa udhaifu wa kijana huyo mara baada ya kuulizwa swali lihusianalo na baba yake.

“ukimgusia baba yake kwa namna yoyote ile lazima akose nguvu ya kuweza kushindana na atashindwa tu. Kwa wale vijana wake hakuna atakayefua dafu kwangu” alikazia Mike. Don dou alishusha pumzi kisha akatazama pembeni kabla ya kuangusha cheko kubwa sana, cheko lililokuja kukatishwa mara baada ya yeye kukaa kitini akasema.

“nilikuwa sina hata hamu ya kula ujue, nilikuwa namuwazia huyo mtoto, kumbe ni mtoto yatima tu asiye na baba wala mama ni mtoto wa malaya tu huyo, sasa nadhani ndege iko tayari ingiza gari zote zitakazotumika kesho kisha ambia vijana watatu wawe tayari kwa safari, ni usiku huu tunatakiwa tuwe Pande” alisema bwana huyo mnene halafu akamimina mvinyo na kulijaza tumbo lake.

Saa moja usiku Roi alikuwa kwenye Barabara ya K2 akitembea taratibu na gari ya kukodi akazunguuka hadi Muavengero juu kisha akaingia zake mjini na kuja kuegesha gari kwenye Clabu kubwa ya Savana. Akatulia garini pasipo kufanya jitihada zozote za kushuka. Alitulia hapo kwa muda mrefu sana hadi ilipofika mida ya saa tano usiku ndipo akashtuka tena ni baada ya kushtuliwa na honi za gari, alikuwa amepitiwa na usingizi kidogo. Akatazama vizuri na kuona gari ndogo iliyokuwa ikiegeshwa hapo maegeshoni na vijana watatu wakashuka. Kuna kitu alitaka kukifanya Roi na huo ndio muda pekee aliouna unafaa. Wale vijana wakaingia kwenye ile Clabu wakiwa wanaongozana, aliwajua kuwa ni vijana wa Tamimu baada ya kuwa amewaona kwenye matangazo mbalimbali, yeye hakuwafuata bali alitumia funguo zake za kazi kuifungua milango ya ile gari ya wale vijana na kujiingiza ndani akaanza kupekua hapa na pale. Hakukuwa na kitu cha maana lakini alipata picha moja ndogo sana iliyokuwa imehifadhiwa mahali. Picha ile ikiwa imebea sura ya mtu aliyekwenye mavazi ya mashindano lakini hakuwa amevaa kofia ya kujikinga bali alikuwa ameishika mkononi. Akajiuliza huyo atampatia wapi, je, yupo kwenye wale watatu walioingia clabu ama?” Aliyekuwa akimhitaji hasa ni mtu ambaye siku inayofuata atahusika kwenye mashindano tu na si vinginevyo. Akatazama juu akaona kuna picha ilikuwa ikining’inia alipoitazama vizuri akagundua kuwa mtu huyo wa kwenye picha hiyo ndiye huyo aliye kwenye picha aliyoishika.

“huyu ndiye mmiliki wa hii gari, vizuri sana” akajisemea kisha akarudisha kila kitu kama ambavyo alikikuta kisha akajirudisha kwenye gari yake akatulia. Muda si mwingi, wale vijana wakatoka lakini hawakuwa watatu tena walikuwa ni wawili ikabidi Roi awe makini kuwatazama vizuri ili kuweza kujua kama kati ya wale vijana yupo yule aliyemuona kwenye ile picha.

“Bingo!” akasema kisha akatulia. Wale vijana wakaingia kwenye gari wakaitoa kwa mbwembwe kubwa sana wakapotea gizani. Roi akarudisha gari yake nyuma kisha akaigeuza kwa mbwembwe nyingi na kuunga tela. Aliwavukuzia kimya kimya bila wao wenyewe kujua. Alizidi kuwafuata hadi mjini huko gari ile ikasimama akashuka kijana mmoja kisha ikaondoka, Roi akaachana na yule aliyeshuka na kumfuata yule wa kwenye ile gari. Safari yao iliishia kwenye nyumba moja tulivu sana, ile gari ikaegeshwa mahali, Roi nae akasimama mbali kidogo na pale ilipo ile nyumba aliyosimama yule kijana. Yule kijana alifunga mlango wa gari yake akaeleke kwenye mlango wa kuingia ndani ya ile nyumba. Roi aliruka akatulia kwenye maua yaliyopo eneo hilo kisha akapiga hatua ndefu kuukabili ule mlango baada ya Yule kijana kuingia ndani, alipotaka kuufunga tu, akasukumiwa ndani huku aliyeusukuma huo mlango akiwa na bastola mkononi. Yule kijana alishtuka sana kuona jambo hilo la kushtukiza limemtokea.

“kuwa mpole kijana” alisema Roi huku akimuelekeza huyo kijana kwenye meza ya hapo Sebuleni.

“shida nini kwani?” aliuliza huyo kijana.

“nahitaji kushiriki mashindano kesho na nahitaji kutumia nafasi yako ikiwezekana” aliongea Roi yule kijana akazidi kushangaa lakini hakuacha kuuliza kuwa itawezekanaje sasa yeye kuchukua nafasi yake. Roi ikabidi amuelekeze na amueleze kile ambacho amekisikia, akaingia kwenye mtandao wa yutube, akamuonesha mahojiano yote yaliyokuwa yakifanyika mchana uliopita kisha akamueleza dhamira ya kushiriki kwake mashindano hayo kwani aliamini asilimia mia Tamimu hawezi kuibuka mshindi na kampuni yake itakufa haitotoka kimataifa. Yule kijana akagoma na kusema kuwa hawezi kumuamini mtu hata kidogo labda kama akitaka awe mtazamaji tu na ataona jinsi kampuni yao itakavyoibuka na ushindi mnono. Roi akauliza muda ambao mashindano hayo yatatakiwa kuanza na muda ambao madereva wote watatakiwa kuwa tayari. Yule kijana pasipokujua dhamira ya Roi, akaeleza kila kitu.

“ok, sasa kwa kuwa umekataa mimi na wewe kushirikiana basi wewe hutayaona kabisa mashindano hayo na badala yake utakuja kuhadithiwa” aliongea Roi, hakutaka kungoja kauli yoyote kutoka kwa yule kijana, alimgeuza na kumzawadia pigo moja murua kabisa kisha akambeba na kwenda kumfungia mahali ambapo aliamini hakuna mtu atakayemuona kisha akarudi zake hotelini kuisubiri siku inayofuata. Tamimu yeye hakutaka kulala hata kidogo alikuwa anahamu sana ya kuiona kampuni yake ikiwa juu. kila akikumbuka jinsi ambavyo aliona vijana wake walivyo imara aliamini kabisa kuwa hakuna mahali ushindi utaenda zaidi ya kuuleta mikononi mwake. Kila akifumba macho aliiona gari ndogo ya kisasa kabisa aliyoitengeneza Morde. Na alikumbuka jinsi alivyowahiidi vijana wake kuwa yeyote atayeibuka mshindi na kumzidi yeye pamoja na wapinzani basi atamkabidhi gari ile ya aina yake. Tamimu alikuja kupitiwa na usingizi muda ambao hata yeye mwenyewe hakujua, alilala kwa muda mfupi sana na kuja kushtuka saa kumi na moja za alfajiri. Matangazo yalikuwa tayari yameanza, vipaza sauti vilisikika vikirindima kila kona ya eneo hilo. Alijiandaa akatoka akaelekea ulipo uwanja mkubwa kabisa akakuta vijana wake wakiwa na kazi ya kukaribisha wageni. Watu walizidi kumiminika sana kila baada ya sekunde kadhaa. Macho yake yalishuhudia gari za ajabu zikiiangia hapo ndani ya huo uwanja zilikuwa ni gari nyekundu tupu zenye picha kubwa la Skeleton nyeusi ubavuni.

“BLACK SKELETON. DON DOU” alisoma maandishi hayo Tamimu kisha akatoka hapo ndani ya huo uwanja. Yalikuwa yamesalia masaa mawili tu ili kuweza kuingia kwenye mashindano hayo ya aina yake. Wafanya biashara wakubwa wa magari walikuwa wamefika kwenye huo uwanja ili kuweza kushuhudia kwa macho yao ni kampuni gani inafaa kuingia nayo mkataba wa kibiashara wa kuweza kuwatengenezea magari mazuri na yaendayo kasi. Watu walikuwa tayari wamefikia idadi ile iliyotakiwa kuingia, wengi walikuwa wamekosa hiyo nafasi ya kushuhudia mtanange huo lakini hawakutaka kupitwa kirahisi walikaa kwenye barabara ambazo gari hizo zingepita. Walikuwa na hamu kubwa sana ya kuona kampuni yao ya nyumbani itafanya nini. Don dou alikuwa yuko kwenye kiti cha peke yake akiwa anatoa maelekezo kwa vijana wake. Kila raia alikuwamo humo ndani, kwa wale waliobahatika hata Petii siku hiyo hakubaki hotelini alikuwa hapo uwanjani akishuhudia mashindano hayo yenye majigambo makubwa kwa kila pande iliyoshiriki.

“zimesalia dakika ishirini na tano hivyo kila dereva ataelekea kwenye gari yake sasa” sauti kutoka kwenye kipaza sauti ilisikika. Vijana wa Don dou waliingia kibabe uwanjani hapo wakiwa kwenye sare zao za kazi huku wakiwa na makofia makubwa ya kujikinga vichwani mwao. Vijana wa Tamimu akiwemo na Tamimu mwenyewe walielekea kwenye gari zao zilizokuwa zipo kwenye pointi ya kuanzia mashindano hayo. Walinyanyua mkono kuona kama wanachi wenzao wako pamoja nao. Shangwe kubwa likainuka mahali hapo kiukweli ilitia raha sana. Ngurumo za gari za Don dou zilisikika na kuondoka mahali zilipopakiwa hadi mahali ambapo pointi ya kuanzia mashindano hayo ipo. Kila mmoja pale alikuwa na hofu kubwa baada ya kuona gari zile jinsi zilivyoundwa. Hawakutaka kuamini kama kampuni ya nyumbani ingeweza kuibuka na ushindi mahali hapo japo kila mmoja alimtumainia Tamimu.

“wakati wowote kuanzia sasa mashindano haya yanaanza” ilisikika sauti kwenye kipaza sauti kwa mara nyingine. Vijana wa Tamimu walikutana pamoja kisha wakatengeneza duara na kuomba dua kwa ajili ya kuhitaji ushindi eneo hilo. Muda ulikuwa umekwisha tayari, madereva wote walikuwa kwenye gari zao mtu wa mwisho kuingia kwenye gari alikuwa ni Roi ambaye hakuna aliyegundua mahali hapo kama mmoja wa wale waliokusudiwa na mmiliki wa T.N Race hakuwepo. Gari ziliungurumishwa injini zake kisha kibao kilichokuwa kikihesabu kikaruhusu. Walitakiwa kuzunguuka huo uwanja kwa round moja kisha watoke na kufuata barabara walizoelekezwa kila gari ilikuwa na dira maalumu sambamba na ramani husika hivyo haikuwa tabu kufahamu ni wapi walitakiwa kupita. Kila dereva alijitahidi kuonesha mbwembwe zake lakini Roi yeye hakuwa na haraka ya hivyo na alikuwa akiendesha kawaida tu. Gari hizo zikatoka zikaingia barabarani. Zilikuwa ni mbio za aina yake kila mmoja alikuwa anahitaji kuwa mshindi mahali hapo. Hapo palikuwa na awamu mbili tu za kuweza kuzunguuka kisha mashindano hayo kufungwa na kutajwa mshindi. Mike alikuwa mbishi sana huyu pekee ndiye aliyeweza kuleta upinzani mkubwa sana kwa Tamimu. Walikuwa wawili tu, Roi yeye alikuwa nyuma ya hizo gari ambazo muda wote zilikuwa sawa. Walipokuwa wanakaribia kufika uwanjani, wakajikuta wako watu watatu kwenye line moja hii ilimchanganya Mike kwa kiasi kikubwa sana na hadi wanaingia kwenye uwanja huo na kufanya mbwembwe za hapa na pale, gari tatu zilikuwa zimeingia kwa pamoja. Mike aliangalia gari hii ya tatu akajua udhaifu wa huyo mtu ni kukimbia kwa kasi na mmoja hawezi hivyo hapo alikuwa na mtu mmoja tu hatari ambaye alitakiwa kukomaa nae. Huyo hatari hakuwa mwingine bali ni Tamimu. Alisimama ubavuni mwa Tamimu kisha akapandisha kofia lake juu na kuanza kumpa madongo kwa kutumia kisafirisha sauti maalumu huku akimtazama.

“wewe yatima, unajitahidi sana, ongeza juhudi baba yako aliyelala kwenye baridi afurahi” ilikuwa ni misumari ya moto iliyokuwa inakita kwenye moyo wa Tamimu, yalikuwa ni maneno yenye kuumiza sana, alijitahidi kutabasamu lakini alijiona si wakushinda lile shindano. Maneno yalizidi kumwagwa na Mike kama mvua hadi Taminu akawa anamwaga machozi ya uchungu sana. Alibadili muelekeo wa kifaa cha mawasiliano Tamimu na kuzungumza na kijana aliyeingia nae sawa uwanjani hapo.

“siyaoni matumaini ya kushinda shindano hili, jitume kwa kadiri uwezavyo Martan. Pamoja na kuongea kote lakini hakujibiwa kitu, hii ilizidi kumchanganya zaidi. Pia aliamini kama watu hao wamejua kuwa baba yake amefariki na yupo kwenye jokofu la kuhifadhia maiti, huwenda hata huyo anayemuita Martan ni miongoni mwa watu wao, pengine martan amebadilishwa ndivyo alivyoamini Tamimu kutokana na kutokujibiwa kila akipaza sauti.

“baba yako anakuona wewe huko alikolala komaa” alisema Mike. Tamimu alizidi kuumia kiasi kwamba hata gari hizo zilipokuwa zikimpita kwa kasi, yeye alikuwa hajui. Aliondoka kwa kujilazimisha lakini ulikuwa ni mwendo ambao sio wa kumpa ushindi. Watu wengi walikata tamaa baada ya kuona gari aliyokuwa akiitumia mmiliki wa kampuni ya T.N, akiwa anaendesha mwendo ule. Don dou alikuwa akicheka kwa furaha kubwa sana, alikuwa anajua kuwa amemuweza mpinzani wake. Alitoka wa mwisho Tamimu. Barabarani kuulibuka shangwe ya kutosha sana Roi alikuwa akimfunza mtu adabu kwa kumuonesha huyo kijana kuwa kabla yake kulikuwa na watu hatari na makini zaidi. Mike kila alipokimbiza ilikuwa patupu. Ilifikia hatua akaamua kutumia kifaa ambacho kinauwezo wa kuongeza kasi maradufu zaidi, alifanikiwa kumfikia Roi sasa akawa na lengo la kumuangusha kwa kumgonga na kumpindua, hilo mwenzake alijua. Mike alipojaribu kupeleka kikumbo, akakuta gari ya mpinzani wake imehama na kuwa mbele zaidi. Alikasirika kupita kawaida lakini kadiri alivyokuwa akikasirika ndivyo alivyokuwa akiachwa kwa kasi na hatua kubwa zaidi. Hadi wanafika mwisho Mike alikuwa ameachwa hatua kubwa sana. Don dou alikuwa anaona kama utani kwa jinsi gari yake ilivyoachwa na kuingia hapo baada ya sekunde kadhaa. Tamimu alikuwa akilia njia nzima lakini shangwe alilokuwa akilipokea njiani ndilo llililokuwa likimpa hofu na maswali ya kujiuliza….

ni nini kimetokea lakini alipoingia uwanjani ndipo alipoongeza kilio baada ya kusikia kuwa kampuni yake imeibuka na ushindi mnono. Aliona ni kama utani hivi, kitendo cha kuambiwa kuwa kampuni yake imeibuka na ushindi lilikuwa ni jambo ambalo hakuliamini abadani, aliamini hakuna bingwa wa kukimbiza gari kwenye kampuni yake zaidi ya yeye mwenyewe. Huyo aliyeibeba kampuni na kuipa sifa kubwa ni nani? Hilo likawa ni swali alilokuwa akijiuliza. Tamimu alitoka kwenye gari yake akiwa ameshikwa na vijana wake akielekea mahali gari aliyoamini yupo Martan lakini alipofika alimuona kijana akitoka humo ndani akiwa ni tofauti kabisa na Martan. Akashtuka sana na kujiuliza mara nyingi, Martan au siye na kama siye ni nani na Martan yuko wapi? Roi alivua kofia lake na kulishika mkononi watu wakapiga shangwe kubwa lakini kwa upande wa Tamimu akabaki mdomo wazi asijue ni kitu gani kinamtokea mahali hapo. Roi alimfuata na kumkumbatia Tamimu kisha akamng’ata sikio na kumwambia.

“natokea nchi ya amani nimekuja kubeba damu za ndugu zangu zilizomwagika na kupotea ndani ta udongo huu, huu ni mwanzo tu, hivyo kuwa na amani” alipomnong’oneza hayo akamuachia, Tamimu alijikuta akikaa chini pasipokutegemea. Mwili wote ulichoka nguvu zilimwisha, mtu kutoka nchi ya amani? amekuja kuchukua damu za ndugu zake? aliwaza kisha akajiuliza.

“Damu! Damu hiyo vipi?” Wakati akiwa anajiuliza hayo, Roi alikuwa amesimama mahali machoni akiwa na mawani yake matata sana inayoona mbali. Alipokuwa akizunguka pale alipo, alitazama juu kwenye jukwaa la watu maalumu. Macho yake yakamuona Bosi wa ile kampuni ya BLACK SKELETON. DON DOU akiwa anaongea jambo haraka sana akamvuta karibu kisha akaikazia macho midomo ya bosi yule akajua si salama. Akatazama kila upande wa lile eneo akamuona Mike akiwa na bastola mkononi na ilikuwa imemlenga Tamimu pale chini alipokuwa amekaa.

“Tamiiiim!” alipiga kelele Roi huku akitoka lile eneo na kukimbia kumfuta mlengaji. Mike akabadili shabaha baada ya Tamimu kuhama lile eneo baada ya kupigiwa kelele ambazo zilimgutusha. Mike akawa anapiga risasi hovyo kumuelekea Roi lakini hazikuwa zikizaa matunda kwani Roi alikuwa akikimbia mtindo wa Zig zag kitendo ambacho kilikuwa kikimkosesha shabaha Mike. Roi alikimbia kwa kasi kubwa hadi alipolifikia gari moja jeusi la Don dou, akadanda kisha akajigeuza hewani kwa ustadi mkubwa, mateke mawili yaliyoshiba yakatua kifuani mwa kijana Mike. Aliyumba huku bastola ile ikimtoka mikononi. Kila mtu mule ndani alibaki mdomo wazi asiamini kitu kilichotokea mahali pale amani ilikuwa inakwenda kuchafuliwa lakini yule aliyetoa ushindi kwa kampuni ile changa, ndiye aliyeokoa maisha ya mmiliki wa kampuni hiyo. Mike aliyumba lakini hakutaka kudondoka chini likawa kosa. Roi alimpiga ngumi nzito ya kifua yule kijana kisha akashusha na pigo jingine zito la shingo akamaliza na kuinyongelea mbali shingo lake. Mike akajibwaga chini akiwa hajitanbui tena. Hakusubiri Roi, alitoka nje ya ule uwanja kupitia mlango mdogo akaona gari ikiwa inatoka mlangoni kwa kasi kubwa. Akapima shabaha moja kali sana akiwa na bastola mkononi, risasi mbili zikapiga Gurudumu moja ya mbele na moja ya nyuma, gari ile ikapiga mwereka mbaya sana na kubingilia mara mbili kisha kujipigiza kwenye mti wa hilo eneo kimya kikatanda. Roi akanyanyua simu na kupiga polisi kisha akatokomea na asionekane.

“Yule ni nani kwani?” aliuliza Tamimu lakini si yeye wala vijana wake hakuna aliyekuwa anamjua yule bwana.

“Hakuna anayejua boss” alijibu Morde.

“Wapi alipo Martan?” akauliza tena tamimu huku akiamini kuwa Martan ndiye aliyechonga huo mchongo.

“Hayupo na gari yake ndiyo ilitumiwa na yuke mtu…hii picha siielewi bosi” alijibu Morde. Kichwa kikabaki kumuuma kila akikumbuka utambulisho wa yule mtu kisha akaondoka hapo mbele ya vijana wake akaelekea ilipo ofisi yake. Alipofika Tamimu alitulia kimya huku akiitafakari ile hali na maneno ya utambulisho wa yule mtu ambaye kama si yeye eidha angeshindwa vibaya sana ama kupoteza maisha kabisa. Aliyarudia yale maneno kichwani mwake kama anaangalia filamu kisha akahisi kitu, kitu hicho alichohisi, kikamfanya atulie maradufu na kuyatamka yale maneno kwa sauti ndogo tena.

“Nimetokea nchi ya amani na nimekuja kuzichukua damu za ndugu zangu zilizomwagika na kupotea ndani ya udongo wa Taifa hili……oooh! God!” akang’aka.

“Siyo wale wapelelezi kutoka Tanzania?…..watakuwa ndiyo na kama ndiwo, basi huyu ni mpelelezi kutoka Tanzania” alijipa imani na alijiaminisha kwelikweli akatoka mule ofisini kisha akaelekea pale alipowaacha vijana wake. Akatazama muda, ilikuwa imetimu saa moja kasoro usiku.

“Morde gari inamafuta ya kutosha?” akauliza.

“Yapo ya kutosha kiongozi” alijibu Morde kisha akawatazama wenzake ni kama alikuwa akiwauliza jambo kisha akayarudisha kwa Tamimu, alipotaka kuuliza kitu, akawahiwa.

“nakwenda chumba cha kuhifadhia maiti nataka kujua hatima ya kumuhifadhi baba yangu sasa” hakuna aliyejibu tena mahali hapo zaidi ya kumtakia safari njema na uangalifu awapo barabarani. Tamimu akaondoka hadi garini. Akaitoa gari nje ya uzio kisha akaingiiza barabarani na kulitoa kwa mwendo wa kawaida akionekana ni mtu mwenye mawazo mengi sana. Alipofika hospitali, aliegesha gari yake vema maegeshoni akashuka na kupiga hatua ndogo ndogo kuelekea mlango wa kuingilia ndani ya ile hospitali. Wakati anazipanda ngazi mbili tatu za kuingia pale hospitali, kuna mtu aliyekuwa amevaa Kofia ya chepeo alipishana nae lakini hakuwa amemtilia maanani.

“Sasa unaweza kumzika baba yako na pole sana kwa kifo alichokutana nacho baba yako” alisema huyo mtu mwenye Kapelo. Tamimu hakugeuka lakini sauti ya mtu huyo ilimshtua, akataka kugeuka akazuiwa kwa sauti.

“Hapana, nilikuwa nakupa taarifa tu kwani kila kitu kimeshakamilika tayari”

“wewe ni nani?” akauliza Tamimu, sauti aliikumbuka kuwa ni ya yule jamaa aliyempa msaada lakini alitaka kumjua zaidi.

“Bi. Rozi Hotel saa tano usiku chumba namba ishirini na tano (25).” alisema huyo mtu kisha akashuka ngazi na kuondoka zake, Tamimu aligeuka na kumuona bwana huyo akiwa amevaa koti Jeusi na kapelo nyekundu. Akaendelea na safari yake. Aliingia hadi chumba cha kuhifadhia maiti akaomba kutolewa mwili wa baba yake, mwili ukatolewa akautazama kwa muda sana machozi mazito ya uchungu yakamtoka.

“baba kwanini haukuwepo leo? Ungekuwepo baba ushuhudie kijana wako nikipata ushindi mnono wa kunifanya niwe mtu mwenye amani kubwa moyoni mwangu. Nimekuwa namba moja baba, Kampuni yangu ya T.N RACE imekuwa namba moja na nimemshinda yule mshenzi mliyekuwa mkiumiza kichwa kwa ajili yake nadhani sasa mji wa Sami Ado, ule mji uliojitenga leo umekuwa ni mji huru sasa kwani mnyama Don dou ameshindwa vibaya sana na kutokana na unyama wake akataka kufanya ushenzi wake wa kujaribu kuniuwa, ameingia pabaya na hivi sasa yuko chini ya mikono ya polisi pia anahali mbaya sana sijui kama atapona. Nimeirudisha heshima yako baba ya kuwa mwema napenda Taifa lako, watu wengi wanapenda mafanikio yangu na harakati zangu za kuhakikisha Ungamo linakuwa Taifa lenye sifa kubwa ya kutambulika duniani. Lakini…Lakini baba naapa mbele ya Mungu wangu muumba wa ardhi na mbingu, sitakubali aliyekutenda haya abaki hai lazima nitalipa” alisema kwa sauti ndogo maneno hayo yenye uchungu kutoka moyoni. Alilia sana Tamimu, machozi alishindwa kuyazuia hata kidogo aliyaacha yatoke kama bomba la maji bovu kisha akaomba mwili huo urudishwe huku akiutazama kwa mara ya mwisho. Aliliona tabasamu la maumivu la baba yake, ilionesha dhahiri alikuwa amepitia maumivu makali sana kabla ya kifo kumkuta. Alimuaga na kumwambia kuwa huo ulikuwa ni usiku wa mwisho kuishi ndani ya baridi hiyo ya kwenye Jokofu kwani siku inayofuata ndiyo ambayo alipanga kuuhifadhi mwili wa Mr. Ndungai.

Saa 09:30 Usiku. Petii ilimkuta akiwa kwenye mgahawa mdogo ulio pembeni kidogo mwa hoteli aliyofikia, alikuwa akipata chakula cha usiku mgahawani hapo ili aweze kuupitisha usiku huo vema. Aliposhiba vya kutosha, alitoka humo mgahawani na kuelekea chumbani kwake. Moja kwa moja akawasha kompyuta yake na kwenda upande wa barua pepe ili kuona kama kuna ujumbe umeingia. Alikutana na maneno makali sana kutoka kwa Mkuu wake wa kazi na ujumbe huo ulikuwa ukimtaka atoe maelezo ya kutosha mahali alipofikia na pia atoe sababu za kuchelewa kuimaliza kazi aliyotumwa hadi muda huo. Haukuishia hapo huo ujumbe bali ulimtaka pia arudi nchini Malawi haraka iwezekanavyo kama ameshindwa hiyo kazi maana tangu aondoke hajatoa ripoti yoyote ya mahali alipofikia na haijulikani ni wapi adui yao alipo. Petii alichoka sana hakujua jibu la kutoa kuweza kujibu huo ujumbe. Alishaanza kuona ugumu wa kazi hiyo, japo alishapata pa kuanzia lakini hakujua ni kwanini alikuwa akipoteza muda kwenda kulivamia hilo Kasino aliloambiwa kuwa Bande Sir ndipo anapopatikana. Aliutazama huo ujumbe kisha akaivuta kompyuta yake na kuanza kuandika barua ndefu ambayo aliamini itakuwa imejaa sababu za kutosha za kuweza kumuelewesha mkuu wake wa kazi. Alipoona barua hiyo imekamilika, aliituma kwa mkuu wake kisha akaizima kabisa kompyuta yake akajilaza kitandani. Wakati yeye akiwa anajilaza na kutafakari hili na lile, muda huo ndiyo Tamimu alikuwa akiingia ndani ya Bi. Rozi Hotel, akazipanda ngazi moja kwa moja kuelekea chumba namba elekezi. Aligonga mlango mara moja tu baada ya kuwa mbele ya mlango kisha akatulia, baada ya sekunde kadhaa, mlango huo ukafunguliwa akakaribishwa ndani. Alimkuta mwenyeji wake akiwa ametulia kwenye kochi moja lililomo humo ndani yeye akapewa kiti akakaa.

“Karibu sana kijana na pole kwa matatizo yaliyokuwa yakikukabili” alikaribisha kwa mara ya pili Roi kisha kutoa pole kwa kijana huyo.

“Asanate sana kaka, nawe nikushukuru sana kwa kuweza kunisaidia japo sijajua wewe ni nani na kwanini ujue kuwa yatatokea yale” alishukuru Tamimu kisha akapeleka swali lililokuwa likimchanganya kipekee kabisa. Roi alitabasamu kisha akasema

“utambulisho hakuna mwingine zaidi ya ule niliokupa pale na naomba ujue tu kuwa mimi ni Mtu kutoka nchi ya amani kinyume na hapo nitakuwa sina utambulisho mwingine. Kuhusu nimejuaje, nilijua hilo kuwa linaweza kutokea siku moja nilipokuwa ninatazama mahojiano yako na waandishi wa habari. Matangazo yale yalikuwa ni ya mtego sana na ninamashaka sana na yule mwandishi wa habari aliyekuwa akikuhoji siku ile, sina imani nae kuanzia uvaaji, maswali hadi maswali aliyokuwa akikuuliza. Inaonekana dhahiri kuna jambo alikuwa akilifahamu au kuna jambo analifahamu. Maswali yake yamenipa mashaka makubwa sana hivyo nikafanya kila jitihada ili nishiriki yale mashindano ili nijue njia watakazozitumia wapinzani wako” alisema Roi kwa urefu kidogo lakini Tamimu hakuelewa hata kidogo maneno ya huyp bwana.

“Ni kwanini uliamua kushiriki sasa? Wewe ni nani kwangu au unashida gani na mimi ya kuweza kunisaidia? Unahitaji malipo sasa au?” aliuliza Tamimu. Roi akacheka kidogo huku akitazama dirishani aliporudisha sura yake kumtazama Kijana huyo akasema.

“Tamimu, Tamimu, Tamimu, unaoneka ni msahaulifu sana. Inamaana hukumbuki utambulisho wangu kwako? Basi sawa kama hukumbuki acha nisikuchanganye sana.” akatulia kidogo Roi kisha akaendelea.

“kuna kazi ndogo sana nataka unisaidie, kazi hiyo ni kuhusiana na vifo vilivyowakuta wale wapelelezi kutoka Tanzania” akaweka tuo na kumtazama huyo kijana. Tamimu akaguna mh! Akajua hapo mbele yake hakuna mtu mdogo bali yupo na mtu hatari sana kutokea Tanzania, kama siyo mpelelezi basi ni Jasusi.

“kwakweli sijui” akajibu Tamimu na kweli alikuwa hajui kabisa kwani hata Roi alipoyatazama macho ya kijana huyo, yalionesha kuto kujua chochote kitu. Roi akabadili swali ili kuweza kupata mwanga wa kuanzia.

“Muuwaji wa baba yako je, unamjua labda au kitu chochote kama utambulisho wa muuwaji?”

Tamimu akajibu pia hajui.

“ok, basi unaweza kunielekeza nyumba ya Mh. Backa labda?” Roi akauliza swali la mtego ili kumpima kijana huyo. Alitaka kujua kama anachokijibu ni kweli hajui au anamdanganya.

“kwa Backaaa…..sawa naweza kukuelekeza lakini siyo kukupeleka kwasababu ulinzi uliopo ni mkubwa sana” alijibu Tamimu. Roi akajua kuwa hakuwa akidanganywa kitu hapo lakini akauliza swali jingine huku akiomba asidanganywe kitu kwasababu alikuwa na mpango mzuri tu. Tamimu akaruhusu.

“wewe ndiye uliyewauwa wale vijana kule baa usiku wa kama siku tatu zilizopita?”

Mh! Swali hilo likamfanya Tamimu kupata mshtuko mkubwa sana na hata alipojaribu kuuficha alichelewa Roi alishajua kuwa huyo ndiye aliyeuwa.

“Naweza kujenga mashaka na wewe kama hautokuwa mkweli kwangu, niko ndani ya nchi hii kujua waliohusika na mauwaji ya wale wapelelezi sasa kama huta kuwa mkweli utanifanya nianze na wewe, najua ni wewe ndiye ulihusika na mauwaji ya wale vijana watatu” akaweka vitisho Roi.

“hapana sio watatu, mimi nimeuwa wawili tu na ni baada ya kunivamia nilipokuwa natoka ndani ya baa ile” alijibu kwa hofu kidogo Tamimu.

“yule mmoja ameuwawa na nani? Nani ni muuwaji wa yule mmoja?” akauliza tena.

“yule mmoja ameuwawa na binti mmoja mrembo sana lakini simjui jina lake”

“yukoje labda kimtazamo?”

“maji ya kunde, mrefu kidogo, anaumbo la kuvutia sana ni mrembo kwakweli”

“anapendelea sana kwenda maeneo yale?” aliuliza Roi.

“Mmmmh! Sina uhakika lakini huenda akawa anapenda sana kufika yale maeneo kila siku usiku” alijibu Tamimu.

“Asante kwa kuweza kuwa rafiki mzuri nikutakie mazishi mema ya baba yako na nitakuja kesho mazishini….ni wapi utafanyia mazishi ya baba yako?” alishukuru Roi kisha kuuliza.

“Mazishi yatafanyika nyumbani kwa marehemu mtaa wa Majumba mengi karibu sana kaka” alijibu Tamimu. Roi akajibu Asante kisha akamruhusu kijana huyo kuweza kuondoka. Kichwani mwake akawa na maswali machache tu ya kujiuliza, ni wapi anatakiwa kuanzia, alikuwa na sehemu tatu muhimu za kuanza nazo moja ikiwa ni makao makuu ya polisi. Alitakiwa kuisafirisha miili ya wale wapelelezi kurudi Tanzania lakini pia ni kupata majibu kamili ya kiuchunguzi, kutoka kwenye mwili wa marehemu Ndungai kama ni alama za vidole zilizopatikana kwenye kisu kilichosababisha mauwaji yake au vinginevyo, maana aliambiwa kuwa majibu yote yapo kwa IGP. Pili ni nyumbani kwa Mh. Backa, waziri wa zamani aliyetekwa nyumbani kwake huku serikali ikishindwa kufanya kitu juu yake na Tatu ni kumjua huyo binti kuanzia anapokanyaga hadi anapo lala. Kote huku kulikuwa kuna maana kubwa sana kwake kwani aliamini ndiko ambako kungeweza kumuweka karibu na muuwaji au wauwaji wa wapelelezi. Wapi panafaa kuanza? Alijiwazia lakini akaonelea kitu cha kwanza ni kwenda kwa Mh. Backa, huku alijuwa huwenda kungemuweka karibu na watu anaowataka zaidi. Pamoja na hayo yote Lakini Tamimu alifanikisha kuondoa nyaraka na vitu vyote muhimu vya Backa kwani alijua kuwa huwenda kukawa na watu wanaouwinda zaidi utajiri wa bwana huyo.



Hali ilikuwa tete vibaya mno, kila mmoja alikuwa kwenye mawazo makubwa juu ya kile kilichotokea. Tayari yalikuwa yameshakatika masaa kibao tangu kuanguka kwa Tereza na kupoteza fahamu. Muda huo alikuwa ndiyo anatolewa kutoka chumba cha upasuaji. Alishaingizwa humo si chini ya mara moja. Ubongo wake ulionekana kupata matatizo baada ya kuanguka na kupiga kisogo chini. Hali hiyo ilikuwa ni mpya na ya kipekee sana kuwahi kutokea kwa Dr. Henry Cartley.

“Sijawahi hata siku moja kufanya ‘oparesheni’ ngumu kama hii, hii ni ‘Oparesheni yangu ya kwanza tangu kuwa Dr. Bingwa wa magonjwa mbalimbali” alisema Dr. Cartley alipokuwa mbele ya wakubwa wake wa kazi. Alikuwepo Bencov, Merina au Lady Devil pamoja na Dr. Lee.

“nini kilichomtokea huyu mtu sasa?” aliuliza Dr. Lee akiwa amechanganyikiwa sana, Dr. Henry akajibu.

ITAENDELEA

Hii ni Dunia au Kuzimu Sehemu ya Tatu

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment