SIMULIZI Anti Ezekiel – Ep 2
SIMULIZI

Ep 2: Anti Ezekiel

SIMULIZI Anti Ezekiel – Ep 2
SIMULIZI Anti Ezekiel – Ep 2

IMEANDIKWA NA : GEORGE IRON MOSENYA

*********************************************************************************

Simulizi : Anti Ezekiel
Sehemu Ya Pili (2)

ASUBUHI sana nilidamka, kitu cha kwanza nikapanga mipango ya kuhamia nyumba nyingine ya kulala wageni. Nilijiwekea tahadhari kabla ya hatari, ingewezekana kabisa namba yangu ya simu kutumika katika kunisaka na hii ingekuwa hatari sana kwangu. Isitoshe Anitha hakuwa akijua lolote juu ya Ezekiel, hakumjua hata sura. Hivyo kama ningekubali kukamatwa hata kama kweli alikuwa na nia ya kunisaidia ndo basi tena mwisho wa jeuri yake.
Na nilivyoijua sheria ya Tanzania mwenye haki hana haki tena akiwa nyuma ya vyuma vya mahabusu ama gereza. Nani angenielewa na kunisikiliza nimweleze juu ya hadithi za bunuasi kuhusu Ezekiel wa Ubungo na yule maiti wa Temeke.
Hakuna sheria ambayo ingenilinda hata kidogo!! Huenda hata Anitha naye angebadili misimamo yake juu ya jambo hilo!!
Nilitambua kuwa sijaswaki baada ya kuzungumza kwa sauti bila kujua na hapo nikatambua kuwa kinywa hakikuwa katika usafi. Lakini nani angejali hali ile!!
Hakuna hata mmoja!! Nikaendelea kutembea nikiangalia chini, mara mbele na wakati mwingine kushoto na kulia.
Sikuwa na amani!!!
Nikakatisha mitaa zaidi na zaidi na jua lilianza kuchomoza nisijue wapi naelekea.
Umati wa watu ukanivuta katika eneo la wazi, nikajisogeza kwa tahadhari nisijue ni nini nafuata huko.
Magazeti!!! Kundi lile lilikuwa likipepesa macho katika vichwa vya magazeti.
Na mimi nikajiunga huku nikiwa makini kabisa nisiweze kumtazama yeyote machoni, kofia yangu ya pama nayo ilinifunika vyema.

“ALVIN ALILAWITIWA KABLA HAJAUWAWA!!” kichwa cha habari katika gazeti mojawapo kilisomeka hivyo, pembeni yake ilipambwa picha yangu ikisheheni maneno machache “ANATAFUTWA”
Nikajikaza na kuendelea kutazama habari nyingine.
“MUUAJI ANASAKWA AUWAWE” pembeni yake kulikuwa na picha ya kitanzi.
“MIAKA THELATHINI JELA INAMNGOJA SAMSON” kichwa kingine cha habari.
“ALVIN AFA NA SIRI NZITO!!” hili lilikuwa gazeti la udaku nikasonya.
“MANENO YA MWISHO YA ALVIN KABLA HAJAUWAWA. ALIMUACHIA SAMSON UJUMBE MZITO.” Kichwa hiki cha habari kikanivuta zaidi. Na hapo nikapata jibu langu huku utatat ukizidi.
Kumbe aliyekufa anaitwa Alvin, sasa hili jina la Ezekiel limetoka wapi? Nikajipekua na kutoa pesa kiasi na kumpatia muuza magazeti, kisha nikaondoka nikiwa nimeinama chini vilevile.
Mawazo lukuki yakinikabili, nilitarajia nitakuta habari juu ya kuonekana kwangu maeneo ya Shekilango labda hata nguo nilizokuwa nimevaa zingeweza kuandikwa pale. Ajabu hakuna kitu kama hicho kilichoandikwa!!
Nikajikongoja hadi katika mgahawa mmoja, nikapata chain a chapati mbili.
Baada ya hapo nikahama tena, safari hii nikajichimbia maeneo ya Kimara Suka. Mbezi nikatoweka bila taarifa.
Majira ya saa sita nikaiwasha simu yangu!!! Ukaingia ujumbe kutoka kwa Anitha, alikuwa anahitaji kuzungumza name.
Nikambipu palepale!!
Baada ya dakika tano simu ikaingia!! Anitha alizungumza kwa sauti yenye tumaini kiasi fulani.
Nikamwachia ukumbi Anitha akiwa msimuliaji name msikilizaji.

ANITHA

KUTOKA saa kumi na moja alfajiri katika nyumba ya mzee Matata si jambo jepesi hata kidogo, lakini yawezekana ikiwa tu ukiwa jasiri. Nami niliuvaa ujasiri nikatoweka nikidanganya kuwa kuna jambo la msingi la kufanya chuoni asubuhi hiyo. Mzee wangu na shule nadhani unafahamu, hakunioinga hata kidogo. Lakini hasira zake tangu usiku uliopita zilikuwa bado zimemtawala, nadhani hakulala hata kidogo maana tangu akaripie sebuleni usiku ule nilimkuta hapo hapo. Baba ametamka kuwa anakuchukia sana huenda kupita wanadamu wote duniani, eti kisa tu wewe ni mlawiti. Dhambi kubwa kupita zote, analalamika kuwa umemnlawiti kijana wa kuitwa jina la Alvin na ukaona hiyo haitoshi ukamuua ili asikufichulie siri, aliyazungumza haya akiwa na bastola yake ile ya tangu miaka ile. Akakulaani huku akimlaumu mama kwa kushindwa kukufyatua ulipojileta wewe mwenyewe nyumbani. Akatukanya sana nkuwa kwa lolote lile tukiwasiliana nawe tumpe taarifa, hakika amechukia mzee yule. Kila mmoja alimuunga mkono, dada Jenipher akamtukana mama aliyekuzaa na mjomba Yakobo naye akakilaani kizazi chako, mama akatoa ushauri kuwa wakuendee kwa mganga ili wakufanye kichaa milele. Baba akasema akikuona atakuua kwanza nd’o mengine yafuate. Sasa nikajiuliza kuwa kishakuua ni kipi kinafuata zaidi yaw ewe kuzikwa!!!
Niliumia moyoni lakini maneno yao hayakunifanya niwe upande wao, nakufahamu zaidi ya wao wanavyokufahamu. Kama ulikuwa mkweli kwangu ni vipi ufanye yote haya nyuma yangu???
Nikaamua kuutafuta ukweli kama kweli upo…nikatoweka alfajiri.
Sinza Kijiweni ilikuwa kimya!! Kama pangekuwa kijijini basi lazima kuku wangekuwa wanawika lakini huku palikuwa kimya, ni magari kadhaa tu yaliyokuwa yakipita na kupiga kelele.
Nilinyata hadi nikalifikia eneo ambalo nilimkuta Kindo usiku ule uliopita, nikaangaza huku na kule nikajikuta katika ugumu. Huu nd’o ubaya wa jiji la Dar es salaam, watu wengi hawana makazi ya kudumu, vijana wanasota na jua mchana na bado usiku wanalala nje.
Nikashindwa kuelewa yupi ni Kindo na yupi si Kindo. Hofu ya kubakwa ikaniandana iwapo vijana wale wataamka pamoja na kutambua kuwa nilikuwa sina uelekeo maalum. Nilijikabidhi kwa Mungu asubuhi ile kama nifanyavyo siku zote hivyo ni yeye tu alikuwa tegemezi langu!!
Moshi mweupe hewani ukanivuta kutazama unatoka wapi, nikasogea huku nikiwa tayari kwa hatari yoyote iwapo itatokea nitimue mbio!!
Si unanijua tena mimi kwa riadha!!
Sura ya Kindo ilikuwa imara sasa. Haikuwa imemwagika hovyo kama usiku ule, nikamsogelea huku nikihofia lolote ambalo lingeweza kutokea. Sura yake ya kigaidi ilinitisha.
“Kaka…..” nilimwita mara moja na yeye akageuka. Nikamsabahi kwa heshima zote naye akanijibu kwa upole.
Sikutegemea kabisa!! Nikakosa pa kuanzia akanikaribisha katika gogo la mti nikaketi!!
“Naitwa Sarah” nilimlaghai jina ili kwa lolote lile la mbele ushahidi usiwepo. Akatikisa kichwa akingoja nimuulize zaidi, nikamuuliza iwapo yeye ndiye kindo akanijibu8 kwa kirefu kuwa jina loake sahihi zaidi ni Kindole Emmanuel. Mwenyeji wa Iringa!!
Nikastaajabu, hakufanania hata kidogo na maneno yake ukifananisha na ugumu wa sura yake.
Nikamuuliza kuwa kama miezi tisa iliyopita aliwahi kumjua Ezekiel, alijaribu kuvuta miezi nyuma lakini kabla ya kujibu akaniuliza mimi ni nani. Nikakosa cha kujibu nikadanganya kuwa ni rafiki yake Ezekiel na nimepotezana naye siku nyingi lakini katika kumbumbukumbu zangu aliwahi kuniambia ana ndugu ama jamaa aitwaye Kindo na ni mwenyeji wa Sinza. Nikaendelkea kulaghai kuwa nina siku chache sana jijini Dar es salaam na nimekuwa nikipatafuta Sinza na nikimtafuta yeye.
Baada ya kunisikiliza kwa makini alionekana kustaajabu mno, lakini alikana kabisa kumjua Ezekiel. Hakika uso wake ulimaanisha alichokuwa anakisema.
Baadaye akanieleza kuwa miezi tisa iliyopita wala hakuwa jinni Dar es salaam alikuwa zake huko Iringa. Akaniamini na kunieleza kuwa hata yeye si mwenyeji sana jijini Dar es salaam na maisha magumu nd’o yanamfanya alivyo!!
Nikamuuliza huko Iringa akumbuke kwa makini, akakataa katakata kumjua Ezekiel.
Nilijaribu kukupigia simu labda walau uelezee muonekano wa Ezekiel huenda anaweza kukumbuka lakini kama ulivyopanga kutoniamini ulikuwa hupatikani hewani!!
Na asubuhi ikatukuta tukiwa katika mgahawa, Kindo si katili kama nilivyodhani, Kindo si mkorofi hata kidogo!! Na Kindo ni kama alikuwa anafahamika maana watu walitutania sana walipotuona na yeye aliishia kucheka tu na wakati mwingine wakirushiana matusi ya nguoni ambayo hayakumwathiri Kindo.
“Wapiga debe wenzangu hao wakorofi sana…” aliniambia Kindo na hapo nikaijua kazi inayomuweka mjini, nisiite kazi bali kibarua kisichokuwa rasmi.
Kindo alinishukuru kwa ukarimu wangu!! Na baadaye nikamuachia namba za simu iwapo atakumbuka lolote juu ya Ezekiel. Nikampatia na kiasi cha pesa.
Nikaondoka na kwenda kituoni!!!
Hata kabla sijapanda gari nikasikia kilio kikuu kutoka upande niliomuacha Kindo. Nikachungulia na kugundua kuwa anayelia ni Kindo!!
Nikarejea upande ule kutazama kulikoni, alikuwa analia akisema wamemuua kaka yangu, wamemuua kaka yangu!! Sikuelewa ana maana gani bado. Hakutaka kuguswa na mtu hata mimi hakutaka kunisikia.
Watu walibaki kuduwaa wasijue analia nini. Akakimbia na kuvamia meza ya magazeti, akajipekua na kutoa pesa niliyompa akanunua gazeti. Watu wakabaki kuduwaa hakuomba chenji yake, sasa akawa amelikumbatia gazeti.

Na hata alipoliachia alikuwa akiililia picha ya mtu aitwaye Alvin, ambaye amekufa ama ameuliwa na muuaji unasadikika kuwa wewe Sam. Kindo analia akisema ni kaka yake, kwa maana hiyo yawezekana Alvin ndo Ezekiel!!! Nikaishiwa nguvu nikakaa chini. Na hilo nd’o jibu!!!
Kindo akiwa katika kuruka ruka huku na kule mara wakatokea watu wawili waliojazia miili yao wakamchukua na kuondoka kwenda naye wanapojua wenyewe!!!
Hakuna aliyejali, Kindo hakuwa na ndugu!! Nami nikaogopa kujipeleka kimbelembele kwa sababu tayari alikuwa amenikataa na mimi baada ya kuona habari ile katika gazeti!!!
Majira ya saa tano asubuhi!! Nikapanda gari Sam na muda huu naongea na wewe nipo chuoni mpendwa wangu!!
Sijui hata ni kipi kinafuata, labda nitaenda kuonana na Kindo tena akishapoa nimweleze kuwa Alvin nd’o Ezekiel nimsikie ataniambia nini japo ameonekana kuumia sana.
ANITHA AKAMALIZA………

UPANDE WANGU
Kijasho chembamaba kilikuwa kinanitoka, habari ile ilinisisimua sana, ni kama mwanafunzi anayekaribia kulipata jibu lakini mwisho analisahau tena, nd’o kilichotokea Kindo alikuwa mtu sahihi wa kuweza kutupa mwanga juu ya Alvin ama Ezekiel kama nilivyomtambua lakini mkanganyiko wa majina ulituzuzua na sasa yule mtu sahihi akashindwa kutueleza juu ya jambo tunalohitaji.
Nilijilaumu kwa kutokuwa hewani, labda kweli Anitha alikuwa sawa kuweka hisia za mimi kutomwamini. Nilifadhaika lakini ni kweli sikuwa nimejitoa kwa asilimia mia kwake, na nisingeweza kufanyanhivyo kwa sababu.
Aumwae na nyoka akiguswa na ujani hushtuka!!!
Kama baba yake ananichukia vipi kuhusu yeye!!! Na wahenga walisema damu ni nzito kuliko maji???

Majira ya saa kumi jioni nilikuwa katika pikipiki, sasa nilijipanga kwa ajili ya kuonana na Kindo mimi mwenyewe, maelekezo ya Anitha jinsia alivyokutana na kijana huyu yalinisaidia na hatimaye nikajikuta eneo lile. Nikajiweka kijiwe cha kahawa nikaanza kunywa kikombe kimoja baada ya kingine. Wazee walikichangamsha kijiwe kwa hadithi zao za uongo na kweli huku mimi nikiwa msikilizaji.
Laiti kama ningekuwa huru kama zamani basi kijiwe kingepata wateja wengi sana siku hiyo kwani zile zilikuwa hadithi nilizozipenda, hadithi za uongo na kweli kutoka kwa wazee.
Nilichangia mada mara moja moja sana huku saa zote nikijifanya kukolewa na utamu wa kashata!!
“Samahani mzee hivi bwana Kindo leo wapi?” nilimuuliza mzee mmoja aliyevalia kibalaghashia. Aliangaza huku na kule kisha akanieleza kuwa labda ameenda kwa daktari, nikamchimba zaidi akanieleza kuwa daktari ni yule anayewadunga madawa ya kulevya!!
Nikakubaliana naye!!!
Majira ya saa moja usiku kijiwe cha hadithi za sungura na paka kikageuka kuwa cha hadithi ya kutatanisha.
Bwana mmoja akaketi na kunyamazisha wote kisha akaelezea kuwa Kindo amekutwa ufukweni mwa bahari akiwa amekufa!!!
Labda mimi ndiye nilishtuka zaidi, jina Kindo lilikuwa jina nililofuata pale. Lakini kabla sijaiona hata sura yake naambiwa kuwa amekutwa amekufa!!
Nikatahamaki!!
Lakini kabla sijakaa sawa mara nikashtushwa na kauli iliyotolewa na mzee mwenye kibalaghashia ambaye awali nilimuuliza juu ya Kindo.
“Huyu kijana ni mgeni hapa na amekuwa akimuulizia kindo katika namna ya kipekee, kwanza usiku huu na amefunika kichwa chake, macho pia yana mawani namna gani yakhee!! Kwani huyo Kindo ulimtakia nini weye!!” aliwaka kwa sauti ya juu, umati ukjnigeukia, wote wakawa kimya wakisubiri niseme neno.
Sikutarajia shambulio hilo, nikabaki kutetemeka. Hali yangu ya hofu ikawafanya wateja wa kahawa wavutike zaidi kujua ni kwa nini nilimtaka Kindo!!
Wakaanza kunizongazonga, wengine walikuwa mateja na wengine makondakta na wapiga debe, muuza kahawa akaanza kukusanya vilivyo vyake. Hali ilikuwa tata!!
Mara mmoja akanikwapua kofia kichwani na mwingine akanitoa mawani nyeusi usoni!!
Hawakuwa na utani wale watu!!
“Mlete kwnye mwanga huku…mlete huyoo, hawa ndo tunawatafuta hawa hata Rama walimuua hivihivi….” Alikoroma kijana mmoja. Wenzake wakatii wakaanza kunighasi huku na kule!! Wakinivuta kuelekea kwenye mwanga, yule mzee mwenye kibandiko alikuwa jirani na mimi akinitukana sana huku akisisitiza kuwa najua kinachoendelea.
Nilijaribu kujitetea kuwa hata sura ya Kindo siifahamu lakini hakuna aliyeisikia sauti yangu!!!
Sam mimi nilikuwa nimepatikana!! Tukazidi kuuelekea mwanga, na lazima ntungeufikia tu!!! Sura yangu ilikuwa katika magazeti ya siku hiyo!!
Lazima watakuwa waliiona!! Isitoshe sakata alilonisimulia Anitha la Sam kulilia picha katika gazeti. Basi wengi watakuwa waliliangalia gazeti lile!
Gazeti lenye sura yangu!!

**JIFUNZE: KATIKA maisha vikwazo ni sehemu ya mapito!! Hakuna mapito nyoofu mpaka mwisho, jiandae kukabiliana na makwazo maana hayo tuliumbiwa sisi wanadamu ili kupimwa imani yetu!!!

Lile kundi lilizidi kunighasi bila kunipa nafasi ya kunisikiliza. Mwanzoni walisema wanaufuata mwanga ili wanitambue vizuri lakini sasa waliupita ule mwanga na kukifuata kichochoro walichokijua wao. Kuna lugha zao waliambiana na sikuweza kuzikumbuka wala kuambulia chochote!!
Baada ya kukifikia kichochoro kile mara ghafla mimi na yule mzee mwenye kibalaghashia tukajikuta tumewekwa katikati. Harufu kali ya moshi wa bangi ilitawala eneo lile na palikuwa kimya.
“Toa kila kitu ulichonacho bazazi wewe!!!” aliamrisha bwana mmoja, nikashuhudia kisu kikubwa mkononi mwake!! Mzee mwenye kibalaghashia akatumbua macho, hakutarajia kama tukio linaweza kubadilika namna ile!! Yeye alitarajia labda nikishatambuliwa basi atapongezwa lakini mambo yaliharibika wale waliotuzunguka neno kifo cha Kindo lilikuwa la kawaida sana kwao.
Wote tukajikuta tunatetemeka, lakini kwangu ilikuwa nafuu zaidi kutekwa na wale watu ambao niliamini kuwa ni vibaka tu wa kawaida kuliko kuingia katika mikono ya wale watu wabaya ama serikali ambayo ilikuwa imehadaika na sasa ikinisaka kama muuaji na mbakaji!!
Niliangusha simu yangu wakaikwapua!! Nikajipekua na kutoka na kiasi cha pesa na hiki pia wakachukua. Wakatoa vitisho kadha wa kadha
Yule mzee alikuwa na kanzu tu hakuwa na kitu cha ziada, wakamweka kando!!
Si kwamba walimwachia la!!
Nilishangaa ghafla alikuwa hewani na mara akatua chini, alikuwa amepigwa ngwala ya ghafla, yule mpigaji akajikausha kana kwamba si yeye aliyetoka kufanya tukio lile lililoipasua kanzu ya yule mzee na kukirusha kibalaghashia chake kando!! Hawakumwambia lolote.
Wakanirudia mimi tena, hawakuwa na utani hata kidogo na nyuso zao zilijawa chuki tupu!!
Kujifanya wananizongazonga waweze kunitambua mimi ni nani hiyo ilikuwa hila tu hakuna lolote walilotaka zaidi ya kuniibia \, na hilo walikuwa wamefanikiwa!!
Ajabu ni kwamba kuna watu walilishuhudia tukio hili lakini hata kujihusisha kutusaidia hawakujisumbua, na ilikuwa heri hawakujihusisha nasi maana wangeweza kutokea ambao aidha wangeweza kunitambua ama wangeyafanya mambo kuwa magumu zaidi!!
Hakika jiji la Dar es salaam lilikuwa limeoza na maovu kama haya yalikuwa kama kitu cha kawaida mbele ya macho ya watu!!
“Kindo umemfahamia wapi we bwege?” mara aliniuliza yule bwana aliyezungumza kama kiongozi na wenzake kumsikiliza.
“Ni jamaa yangu tu….mimi ni mtu wa Iringa nd’o nilikuwa namuulizia jamani” nilijitetea. Mara bwana mmoja akadakia hoja.
“Na wewe ndo wahanga wa ridandansi ya Michigani ama?” aliniuliza, akili ikafyatuka hilo neno Michigani halikuwa geni hata kidogo masikioni mwangu.
“Hapana, ni ndugu tu jamani!!” niliendelea kujitetea.
Ile kusema neno Michigani basi kila mmoja akacheka kati ya wale vibaka. Bila shaka halikuwa neno geni kwao. Ajabu ni kwamba neno lile hata kwangu pia halikuwa geni kuna mahali niliwahi kuliona kisha nikalipuuzia na sasa nalisikia tena.
“Yaani kila mtu wa Iringa huwa anadanganya kuwa alikuwa Michigani amefukuzwa kazi aisee sijui huko Michigani nd’o kampuni pekee kubwa??….haya dakika moja potea hapa urudi Michigani kwenu huko!!! Moja mbili…..” aliamuru na hakuwa na utani, kabla hajafika tatu nikatimua mbio kali huku nyuma nikimsikia yule mzee mwenye kibalaghashia akilalamika kwa maumivu, bila shaka alikuwa akipokea kipigo kingine kwa kutembea bila pesa.

Sikusimama maana nilikuwa nimeponea katika tundu la sindano, nilikimbia bila kukoma hadi maeneo ya Tandale, nikachepuka na kona kadhaa kabla sijairuhusu akili yangu kufanya kazi tena.
Uzuri ni kwamba nilikuwa nimechukua tahadhari mapema sana, pesa zangu niliziweka katika mafungu mbalimbali kwenye nguo nilizokuwa nimevaa. Hivyo hata nilipowapa wale wakora zile pesa na simu bado nilibakiwa na fedha nyingine ambazo zilinitosha kufanya safari ya kurejea kule nilipofikia kwa kutumia usafiri wa pikipiki tena!!!
Badala ya kusikitikia suala la kukaribia kukamatwa nilitamani tufike upesi Kimara niweze kuwa huru na kisha kujipanga tena upya kujitafutia haki yangu bila uhai wa Kindo!!
Maeneo ya Tandale sokoni, kabla sijachukua pikipiki, kwa tahadhari kubwa nilifanikiwa kununua kofia nyingine, na pia nikavutika kununua fulana kubwa na suruali nyingine.
Ile kofia nikaivaa muda uleule na kisha kutoweka, nikiwa kama mzuka aliyefufuka kutoka katika wafu nisiamini kama na hatua ile nimepona pia.
Majira ya saa mbili nilikuwa chumbani!! Upesi nikachukua bahasha yangu ambayo nilikuwa nimeificha chini ya godoro, nikamwaga makaratasi yote chini na hapo nikaiona ile picha ambayo jengo lake dogo limeandikwa Michigan. Ni hapa nilipokuwa nikisumbua akili yangu kupatambua!!
Niliitazama kwa makini sana, na hapo nikaanza kuunganisha matukio, nikayakumbuka mazungumzo baina yangu na Anitha aliponambia kuwa Kindo ambaye anasadikika kuwa marehemu tayari alikuwa mwenyeji wa Iringa, kama hii haitoshi wale vibaka waliposikia kuwa mimi ni jamaa yake Kindo mara moja wakadakia kuwa na mimi ni wa Michigan!!
Huko Michigan ni wapi?

Na je panahusika nini ni mauaji ya Ezekiel ambaye kwa jina halisi ama vyovyote vile ni Alvin.
Kwa maana hiyo Kindo aliwahi kuwaambia vibaka hao kuwa yeye alikuwa muajiriwa huko Michigan? Baadaye akapewa ridandansi!!!
Hapa kuna tatizo lazima!! Kindo amekufa na siri kubwa sana!!

Nikatamani sana kuzungumza na Anitha usiku huo lakini tatizo sikuwa na simu tena wale mabazazi huenda walishaiuza kwa bei ya kutupa tayari!!
Nikatoka nje na kumkabili muhudumu aliyekuwa mapokezi, nilimkuta akiwa ametingwa katika kusikiliza muziki na ilinilazimu kumuita mara tatu hata akanisikia, nikamsihi aniazime simu yake kuna simu ya muhimu sana nahitaji kupiga!!!
Akalalamika kuwa simu yake huwa haibadilishwi kadi, nikamweleza kuwa sitabadili. Bado akalalamika mengi na klusema simu yake haina muda wa maongezi, nikatoa shilingi elfu tano mfukoni. Uzuri huduma ya vocha ilikuwa pale, hapo akakosa ujanja na kufikia hatua ya kuniazima!!
Nikatoweka na ile simu na kuelekea chumbani kwangu!!
Nikajisifu kwa uwezo wangu mkubwa wa kukariri. Nikaziandika namba za Anitha katika simu ile na kungojea simu ile iiite.
Ikaanza kuita na baada ya dakika kadhaa ikapokelewa!!
Kama mimi nilivyotegea upande wa pili uanze kuzungumza na upande wa pili nao ukangoja mimi nianze kuzungumza!!
Mtego!! Nikajiwazia huku nikiendelea kukaa kimya!!
“Halo!” hatimaye sauti kutoka upande wa pili ilinong’ona. Alikuwa Anitha!!
Hapo nikapata ujasiri wa kujitambulisha upesiupesi!!
Anitha akasikika akikurupuka kwa fujo kutoka alipokuwa na nikasikia vishindo na baada ya hapo aliniuliza kama nilikuwa salama!! Nikajibu kuwa nipo salama kabisa, akaniuliza tena na tena kama nina uhakika na usalama wangu nami nikasisitiza kuwa hakuna baya lolote upande wangu!!
“Kindo amekufa….” Aliniambia binti huyu kitu ambacho nilikuwa nakitambua tayari.
“Nini kivipi?” nilimuuliza kana kwamba hakuna nijualo!!
Alinielezea kuwa na yeye hajui lolote lakini katika mapito yake pale kuhakikisha kuwa anazungumza tena na Kindo alipewa taarifa hiyo.
“Mbona unaulizia mara mbilimbili juu ya usalama wangu lakini!!” nilimuuliza kutaka kujua.

ANITHA akachukua nafasi kusimulia!!

SAM naomba nikiri kuwa naipongeza nafsi yangu kwa kuendelea kukuamini kila kukicha. Sikuwahi kukatishwa tamaa na habari za kwenye magazeti. Kashfa na tuhuma zote ulizozushiwa hazikuwahi kuniteteresha kamwe! Baada ya kifo cha Kindo, nimeamini kuwa kuna watu wabaya wengi wamelizunguka tukio hili na hakika u katika wakati mgumu sana.
Sam najua hujipiganii peke yako na labda unaona haya kunieleza kuwa unao uchungu sana kuwa hujui mkeo alipo na usalama wa mtoto wako. Ni kweli ninao wivu kwa sababu nakupenda lakini amini haya ninayokuambia. Sam naumia sana ten asana, juu ya mama Eva na Eva mwenyewe. Mama Eva ni mwanamke mwenzangu, hana kosa alilowahi kunitendea zaidi tu ya kujikuta katika penzi lako.
Eva ni mtoto mdogo hajui lolote kuhusu hisia zangu kwako!! Hastahili kuchukiwa!! Na sijawahi kumchukia unalitambua hilo.
Sam kwa hali ya amani ilivyo juu yako, kwa jinsi watu wabaya wanavyoisaka roho yako. Nipo radhi niambie unahitaji kitu gani kingine naweza kufanya kwa ajili yako wewe, Eva na mama Eva. Niambie chochote hata kama ni kigumu nami nitakujibu kuwa naweza ama kipo nje ya uwezp wangu!!!” alinieleza kwa hisia kali huku akizungumza kwa sauti ya chini, kila neno likawa na maana kwangu nami nikajibu.

“Anitha, kama nilivyosema awali kuwa hata nikikushukuru namna gani bado sitafikia kiwango unachostahili.
Anitha naomba niwe muwazi kuwa hakika baada ya usaliti alioufanya mzee Matata ambaye ni baba yako imani yangu kwa wanadamu imekuwa hafifu sana. Yaani namuogopa kila mtu!!
Laiti kama ningekuwa sina familia nisingeogopa lolote lakini Eva ndo ananiumiza zaidi huku mama yake akinipagawisha kabisa, sijui alipo huenda hata wamemuua naye tutasikia kama hivyo kwa Kindo!! Anitha nimeamua kitu kimoja, nimeamua kujikabidhi kwako Anitha. Kujikabidhi kwa asilimia zote mia moja.
Kama sitakuwa sahihi basi chozi la Eva na damu ya mama Eva iwe juu yangu kwa upumbavu wangu!! Kilio cha Eva na kinisulubu iwapo sitakuwa sahihi kukuamini wewe kama mtu wa mwisho pekee ninayeamini upo upande wangu!!
Sina lolote la kufanya ikiwa sura yangu haitakikani mtaani na sasa Tanzania nzima wanaijua sura na jina langu popote pale nitakamatwa tu! Anitha narudia tena na samahani kama nitakuwa nakukera, tambua kuwa mimi Sam sijaua mtu wala kulawiti!! Iwapo baba yako ama familia kwa ujumla zimekumezesha sumu na kuamua kunikamata mimi sasa nipo radhi, lakini nikiwekewa kitanzi shingoni, neno nitakalosema juu yako ni kwamba lawama za Eva na mama yake ziwe juu yangu lakini damu yangu na uhai nitakaoupoteza kwa hila na hujuma ya hali ya juu, vyote vitakuwa juu yako Anitha. Namkabidhi Mungu uaminifu huu wa mwisho mkubwa ninaoamua kuuleta kwako. Yeye pekee ndiye ajuaye ni kiasi gani nipo upande wa haki na sijui lolote kuhusu kuua. Na ni yeye huyuhuyu aliyeniambia kuwa kesho nikutane na wewe ana kwa ana!!” nilimaliza huku nikishindwa kuyazuia machozi yangu nilipomkumbuka mke wangu asiyejulikana mahali alipo na Eva anayesadikika kutunzwa na jeshi la polisi Tanzania.
Upande wa pili nilimsikia Anitha naye akililia kilio cha kwikwi, na hata alipozungumza alitoa kauli fupi tu.
“Na kilaaniwe kizazi changu chote milele na milele iwapo siku moja nitasimama na kutetea maovu…Sam tukutane kesho saa tatu usiku. Utaniambia muda huo nije wapi??” kisha akakata simu!!
Sikutaka kumpigia simu kwa sababu nilijua hataweza kuzungumza tena, maneno yangu huenda yamemuumiza moyoni ama yamemtia aibu kwa mpango aliokuwanao na sasa anajutia kwa machozi!!
Nikamtumia ujumbe mfupi. Nikamuelezea wapi nitakuwepo, sitakuwa na simu lakini nitafika kwa wakati!! Pia nikamsisitiza asitumie namba ile tena!!
Nikamaliza nikaifuta namba yake katika simu ile na kumrejeshea muhudumu, salio lililobaki mle lilimfanya atokwe na tabasamu, meno yake ya njano yakaonekana.
Sikurudi kulala, nikaondoka na kujipatia mkate na soda dukani, nikarejea chumbani kwangu kupooza njaa huku nikitafakari Michigani ni kitu gani na kwanini Kindo ahusike nayo na kisha Alvin.
Michigan Michigan!!!
Nililala nikiwaza hayo!!

SIKU iliyofuata kama ilivyoutaratibu wangu nilihama nyumba ile na kuhamia kwingine kabisa maeneo ya Ubungo. Baada ya kuwa nimepata supu ya maana nilijifungia ndani mara nilale mara niamke huku nikitafakari mambo mengi yasiyokuwa na ufumbuzi, kisha nikamtafakari Anitha na uamuzi wangu wa kukutana naye!!
Roho ilinidunda sana na kujiona kuwa najikabidhi kwa muuaji kirahisi, lakini ni kipi ningefanya iwapo hakuna anayeniamini na ushahidi wangu wenyewe ulikuwa utata mkubwa kuliko utata uliokuwepo. Picha na maandishi yaliyoandikwa na msichana ama mvulana asiyejua kuandika vizuri yangeisaidia nini mahakama zaidi ya kubambikiwa kesi nyingine ya kudanganya mahakama.
Eva na mama yake hawa ndio waliniumiza zaidi!!
Hawakuwa na kosa na huenda wangekuwa wameaminishwa kuwa mimi ni mtu mbaya, mwanangu Eva anaambiwa baba yako ni gaidi,.
Nikazichanga karata na kisha nikaitupa kete moja tu kubwa nay a mwisho kwa Anitha!! Kama ana mnapenzi ya kweli ama anatumiwa!!
Nikasinzia tena!!

Majira ya saa mbili nilitoka nyumbani na kwenda eneo la miadi ambalo nilimtumia Anitha katika ujumbe mfupi wa maneno.
Niliwahi maksudi ili niweze kusoma mchezo kama utakuwepo japo hiyo ilikuwa mbinu hafifu tu ya kujihami, kama wamejipanga tayari nisingeweza kuchomoka tena!!
Saa mbili na nusu kwa mujibu wa saa iliyokuwa katika mnara nilimuona Anitha akitembea kwa madaha kuelekea katika eneo nililomwelekeza.
Baada ya kutingwa na mawazo siku kadhaa sasa nilikumbuka kuwa kumbe Anitha ni msichana mrembo kiasi kile. Nalivalia vazi refu jeusi lililozichora nyonga zake vyema, vazi lile halikuishia kiunoni bali lilipanda hadi usawa wa kifua chake na kuzistiri embe sindano ndogo zilizong’ang’ania kukomalia pale kifuani na si mahali pengine, mgongo ulikuwa wazi lakini si wazi kiasi cha kuitwa uchi la! Ulifunikwa na nywele ndefu ambazo alijitambia kila leo!!
Macho yake yalizibwa na miwani yenye mahadhi ya kuvaliwa usiku, mkononi alibeba kipochi kilichofanana na miwani.
Hakika aliwaka!!!
Niliwahi kuwa naye katika mahusiano lakini sasa alipendeza zaidi!! Alichukua nafasi na kuagiza maji ya matunda!!

Akiwa anakunywa kinywaji kile hakuonyesha hofu yoyote machoni mwake.
Nikatazama juu mbinguni na kusema na Mungu!!
“Wajua kuwa sikuua, wajua kuwa mimi ni mja wako!! Nitazame baba huku ninapoelekea, kama ni sahihi nyanyua mguu wangu sasa lakini kama si sahihi baba nitegue nisiweze kuifikia meza ile” nilimaliza ile dua na kisha hatua moja hadi nyingine hadi nikaifikia ile meza.
Nilikuwa nimevaa zile nguo nilizonunua Tandale usiku uliopita!!
Anitha aligeuka na kunbitambua akasimama na kunikumbatia.
Marashi yake yakamfanya azidi kuwa mrembo, joto lake tulivu likanikumbusha mengi yaliyopita!!
Nikavuta kiti na kuketi mkabala naye sasa tukawa tunatazamana. Alipotoa miwani uso wake ulikuwa umechafuliwa na michirizi ya machozi.
Anitha alikuwa analia, na hapa akanyanyua mdomo na kuniambia jambo ambalo sikuwahi kuliwaza.
“Sam umekonda hivi jamanii!!”
Nikashangaa!! Akasema tena, “Yaani umepauka kabisa si wewe Sam. Pole sana.” Alinibembeleza, nikajisikia vibaya badala ya kupata ahueni!!
Robo saa baadaye tukiwa tumeagiza vyakula, nilikuwa nikimuelezea juu ya Michigan na utata niliokutana nao nikiwa namtafuta Kindo.
“Kwa hiyo hukuniamini hata kidogo Sam ukaamua kwenda mwenyewe!! Ni lini utaamini kuwa Anitha yu upande wako.” Alilalamika, nikajifanya sikumsikia nikaendelea kumweleza mambo kadha wa kadha!! Yote haya nilimsimulia nikiwa sijaifungua bahasha mkononi mwangu!!
Ukafika wakati wa kuifungua bahasha, hapa akalazimika kuja kuketi katika ubavu wangu ili nimwelekeze kitu kimoja baada ya kingine ili atambue ni kitu gani namaanisha.
Picha moja baada ya nyingine, andishi moja baada ya nyingine…
MARA tukakatishwa na sauti ya mwanamke, “Heloow!!” tukadhani ni muhudumu wa ile sehemu tukapuuzia na kuendelea na mambo yetu!!
Niliponyanyua macho kwa mbali niliona kitu kama ninacho kifananisha na mzimu usiotakikana machoni kwangu!! Lakini wakati naendelea kuduwaa mara mbele yetu akaketi mwanamama akiwa anatabasamu. Tabasamu la kinafiki.
Nikamtambua upesi yeye na kisha nikapata jibu la yule niliyemfananisha alikuwa ni nani!!
Mbele yangu alikuwa ni mama yake Anitha na yule mzee aliyekuwa anakaribia kufika pale alikuwa ni mzee MATATA…..baba yake mzazi Anitha…….
Bahasha yangu mezani, najilazimisha kufumbua macho lakini hayafumbuki zaidi ili iwe ndoto!!
Nilikuwa maeneo ya Saveyi karibu na chuo kikuu cha Ardhi na mbele yangu alikuwapo mama Anitha na huyu anayemalizia hatua afike nilipokaa alikuwa ni mzee Matata.
Mapigo ya moyo badala ya kwenda kasi yakaanza kushuka kwa fujo!!
Jasho halikutoka lakini mwili ukawa wa baridi sana. Ganzi ikanishika.
NAKUFA!!!! Nikajiwazia…………..

***JIFUNZE!!! DUNIA inapokugeuka mwamini Mungu pekee, yeye hadanganyi, yeye si mnafiki wala si msaliti!! Ukimwambia baba tenda miujiza anasikia palepale!! Sema naye kwa imani naye atatenda!!!

Mzee Matata hakuwa akikosea uelekeo alimaanisha kufika katika meza ambayo nilikuwa nimeketi na Anitha. Usoni alionyesha tabasamu lililojawa karaha tele, na alitembea kama asiyetaka kufika upesi eneo lile lakini alikuwa makini.
Nikajikuta nipo nje ya ujasiri na suruali yangu ikajikuta ikijitahidi kuumeza mkojo uliokuwa ukinitoka bila kuzuiliwa, kwa sekunde kadhaa nikafanikiwa kuuona uso wa Anitha….
Ajabu!! Alikuwa anayo hofu kubwa kuliko mimi, jsho lilikuwa likimtiririka na midomo ikimchezacheza.
Anaigiza!! Niliwaza huku nikiwa sijajua kipi cha kufanya, nisingeweza kukurupuka na kukimbia bila kutambua iwapo mzee Matata anayo silaha yoyote kwa wakati ule, maana bunduki yake ndogo alikuwa akiimiliki kihalali na angeweza kuitumia kunishambulia. Hata akiniua ataishia kupewa pongezi kwa kumuua muuaji na mbakaji, asingelaumiwa na mtu yeyote.
Nilibaki katika hali ileiloe ya kuinama nisijue wala kuamini iwapo, Anitha amenisaliti ama naota!! Kama kweli alikuwa amenisaliti nikajikuta lawama zangu nikizigeuzia kwa Mungu!! Mbona nilimsihi sana kabla sijajikabidhi kwa binti yule!!

“Si nilikwambia…..haya hii nd’o diskasheni…ooh Anitha hawezi kulaghai hawezi sijui nini haya hapa ndo mpo katika kudiskasi?” mama Anitha alihoji swali ambalo liliniduwaza.
Mwanga mwekundu wa taa haukunizuia mimi kuwatambua wazazi hawa lakini ajabu wao waliuliza kitu kingine kama vile hawanitambui!!!
Mzee Matata alishusha pumzi za nguvu sana, sikuwa nimemtazama machoni bado moja kwa moja, niliendelea kuinama huku kofia yangu ikinifunika.
“Mama!! Hivi mnataka kunichunga hadi lini?” alijibu Anitha kisharishari!!
Nikazidi kupagawa.
Ina maana wote wawili wananiigizia Mungu wangu weee!!
“Johnson!! Johnson, nisamehe bure kwakweli halikuwa dhumuni langu, naomba uniachie nafasi nizungumze nao hawa ni wazazi wangu!! Samahani tena Johnson!!” alinisisitiza Anitha, nikapagawa, inamaana yale mavazi yangu niliyonunua Tandale na hilo kofia vimenibadilisha kiasi kile?? Ilistaajabisha sana.
Sasa naitwa Johnson!! Nikashindwa kuelewa kama nisimame ama nisisimame, Anitha akaugundua udhaifu ule akanikanyaga mguu upesiupesi, bado sikuelewa nifanye nini. Akaniinamia na kuninong’oneza.
“Baba haoni usiku ana ‘night blindness’ hajui lolote na mama bado anajiuliza. Ondoka upesi ondoka tutawasiliana.” Kwa kauli hiyo sasa nikatambua nini kinaendelea.
Nikasimama na kuondoka nikiwa na uoga mkubwa na kichwa nikiwa nimekiinamisha. Bahasha yangu mkononi!! Mapigo ya moyo yakiwa katika hali ya kufifia na miguu ikitetemeka kwa fujo.
Anitha!!! Anitha steringi!! Ndo kitu nilichobahatika kukitamka kwa midomo yangu baada ya kujikuta nipo peke yangu mahali bahasha yangu mkononi na hakuna wa kunighasi.
Suruali ilikuwa imelowana bado, sikuamini hata kidogo kama tulikaa meza moja na mzee Matata na mkewe na sasa nilikuwa nimeondoka tena.

Nikaikumbuka kauli ya mzee Matata tangu akiwa bosi wangu aliponieleza kuwa Anitha ndo binti yake kipenzi, hana la kusema juu yake na hataki baya lolote limtokee.
Naam!! Mtoto wa baba alikuwa ametumia nafasi kuniokoa!!
Nikazitazama mbingu na kumwomba msamaha Anitha kwa lolote lile baya nililowahi kumuwazia!!
Anitha alikuwa upande wangu kwa asilimia mia!!
Sikupotezaq muda zaidi nikatokomea!! Si kuelekea katika nyumba ya wageni niliyofikia bali kwingine kabisa ambapo nilifahamu mimi na akili yangu!! Zile nguo nilizopewa na Enock yule rafiki msaliti nikaamua kuachana nazo. Cha muhimu kilikuwa mimi na bahasha yangu!!

*****

Majira ya saa nne usiku nilikuwa nikiusaka usingizi kwa juhudi zote, suruali yangu nilikuwa nimeifua na kuinika chini ya feni ili kufikia asubuhi iwe imekauka.
Niliwaza mengi na kisha kukumbuka kuwa pesa ilikuwa inayoyoma hatimaye. Hili likanitia wasiwasi maana pasi na pesa bila shaka njaa ingeniumbua na kujikuta naomba msaada, msaada kutoka kwa mtu yeyote yule pasi na kujua kama ni mtu hatari ama salama!!
Asubuhi kama nilivyopanga wakati usingizi unabisha hodi nikamkumba muhudumu wa nyumba ile ya kulala, huyu hakuniletea ugumu katika kuniazima simu yake. Nilimwambia kuwa kuna mtu nataka kumbipu!!
Nilipopigiwa simu nikakimbilia chumbani kwangu na kisha kwa tahadhari kubwa nikaipokea simu!!
“Nilijua tu ni wewe na hakika nilisubiri sana kuzungumza nawe!!” Anitha kutoka upande wa pili alizungumza. Sauti yake ilikuwa inaunguruma kiasi na nhakika hakuwa sawa na siku nyingine. Kabla sijamuuliza lolote akaendelea.

ANITHA.

HUWA ni jambo gumu sana kuupina ama kuubatilisha usemi wa damu nzito kuliko maji!! Lakini hubidi kuwa hivyo pale upendo unapochukua nafasi!!
Tukio la jana ni kama ndoto na hata muda huu naamini ni ndoto labda ni wewe wa kuibatilisha ndoto hii, ndoto ya mwanamke kujikuta katika maamuzi ya kuachana na usemi wa damu nzito na hatimaye kuubadili kuwa penzi zito kuliko damu!!
Sijui nilitoa wapi ujasiri ule wa kujitetea mbele ya baba na mama yangu!! Na wala sikutarajia ujio wao usiku ule tena wakinifumania mimi na wewe. Ambaye wanakuita mtu hatari.
Sam, nafsi yangu ilijawa na baridi, lile barafu la ubaridi likazidi kuvimbiana na nikajihisi kukosa amani kwa zana kuwa waweza kuniita msaliti!!! Naam!! Ni mwanadamu gani awezaye kuamini eti mama alishika simu yangu nikiwa nimeenda kuoga akausoma ujumbe uliokuwa umenitumia kunielekeza mahali tulipotakiwa kukutana. Yule mama akawa mjuaji zaidi akaangalia huduma za kipesa katika namba hiyo na kugundua kuwa ulikuwa ukijiita Gabriel Madaraka. Kwa hili naomba nikupongeze sana Sam, yaani laiti kama ungekuwa umetumia namba ambayo umeisajili kwa jina lako basi nadhani ule ujio wa wazazi wangu usingekuwa wa kupooza namna ile.
Mama akamshirikisha baba yangu juu ya mimi kutaka kukutana na mwanaume majira ya saa tatu usiku maeneo yale tuliyokutana. Nadhani wajua ni jinsi gani baba yangu ananipenda kwa dhati, hili kwako si jipya hata kidogo kuwa hataki baya lolote linitokee, akasikia natarajia kukutana na mwanaume ilhali nimewalaghai nyumbani kuwa naenda katika majadiliano ya kimasomo na rafiki zangu. Wazazi wakaitegea mida na hatimaye wakatufuma katika hali ile.
Najua kuwa usingepatikana muda wa mimi kusimulia haya na unielewe iwapo wazazi wangu wangekugundua na kukukamata, na jambo hili lingenifanya niwe adui yako namba moja maisha yako yote!! Sikuwa tayari nikaamua nkuwakosea heshima, nikakutetea na hatimaye ukaondoka.

Sam!! Nilibebwa mzega mzega nikaingizwa katika gari na kuendeshwa moja kwa moja hadi nyumbani!!
Hakuna jambo baya kama kupingwa na wazazi wote wawili katika jambo unalojaribu kulifanya, katika utetezi hakuwepo aliyesimama upande wangu!! Nilipigwa sana na utu uzima wangu huu, baba alinipiga kwa kutumia mkanda huku mama akinipiga vibao na makofi!! Hasira za baba zilikuwa juu zaidi, baada ya kunipiga sana hakutaka kulala nyumbani. Akatoweka na mama naye akaondoka kwenda kumtafuta.
Nadhani waisikia sauti yangu ilivyo mbaya, hii ni kwa sababu nina vidonda mdomoni, walinipiga sana Sam. Lakini niliamua kubeba maumivu haya kwa ajili yako!! Nikateseka lakini uwe na imani kuwa sijawahi kukukana hata siku moja!!

Kosa walilofanya wazazi wangu ni kujiridhisha kuwa Anitha mimi sijakomaa kiakili, wakadhani siyajui mapenzi na sina uamuzi wangu wangu wa mimi kama mimi!!!
Nilitarajia utanipigia simu Sam usiku ule niweze kukushirikisha katika jambo nilililokuwa nimefikiria lakini sikupokea simu yako na nililazimika kuchukua maamuzi ili tu haki ipatikane, Sam mimi nasome sheria na haki za binadamu. Lazima kuna kitu katika mlolongo huu, nami nataka nitambue kuna nini hapa katikati, hii ni nchi yetu Sam na sis indo vijana kama kuna uvundo wowote unaendelea na vijana tunafumbia macho, amini umri na elimu zetu hazitusaidii kitu chochote na ni watumwa wa elimu ya mkoloni huku tukiwa vibaraka wa ukoloni mamboleo. Maumivu hayakunizuia kukivamia chumba cha wazazi wangu ambacho haikuwa mara ya kwanza kuingia. Ile imani ya baba yangu kwangu na kuonyesha mapenzi waziwazi sasa ulikuwa wakati muafaka wa kuitumia. Nikafungua sanduku ambalo nilizijua namba zake za siri, naam!! Nilichokitarajia nikakikuta!!
Unadhani ni kitu gani ki9nachokwamisha mkakati huu zaidi ya pesa!! Unadhani kwa nini Eva na mama yake wapo mahali usipopajua zaidi ya pesa? Sam Pesa haina mdomo lakini ikipaza sauti basi itasikika dunia nzima na wanyonge watatetemeka!!
Pesa inaficha maovu na pesa hii inatibua haya maovu!!
Pesa nyingi inaweza kuficha maovu milele lakini akili nyingi na pesa kidogo hutibua mipango hii!! Sijielewi mimi lakini natambua kuwa Sam wewe unao uwezo mkubwa sana wa kufikiri, naam!! Kwa pesa hizi kidogo nilizochota naamini harakati za kuirejesha amani, kutibua fumbo hili gumu na kumrudisha mama Eva na Eva katika himaya yako basi zote zitawezekana!!
Michigani, Kindo, Ezekiel, Alvin vyote hivi vitajulikana!!
Sam! Baada ya kuiba pesa hizo kutoka kwa wazazi wasiofungamana nami!! Nilitoweka mlinzi akiwa amelala!!
Sasa nane usiku, kila kiungo kikiwa kinauma kutokana na kipigo, macho yakikosa nuru kutokana na uchovu, bado niliweza kuzurula mitaani.
Nakukumbusha kuwa Mungu ni muweza wa yote haogopi usiku wala mchana maana vyote alivibuni yeye!!
Mungu alinisimamia na hadi muda huu unanipigia simu nipo Royal Hotel Temeke chumba namba 18, Anitha huru katika fikra na maamuzi huru!!! Simu yangu iliingoja simu yako tu ili niweze kuizima na rasmi nakutambulishia namba yangu mpya isiyojulikana na yeyote zaidi yako ni 07…675493. nimeamua kuungana na wewe Sam, kama ni batili wazo hili na niadhibiwe nikiwa hai. Na kama nikifa kabla ya kupewa adhabu basi nifanyiwe alichofanyiwa yule dada katika simulizi uliyoiandika na ikavuta maelfu ya watu..”NIKIFA MAITI YANGU IPEWE ADHABU!!”

ANITHA AKAMALIZA!!!!

UPANDE WANGU

Nilibaki kuduwaa nisiamini nilichokisikia, sauti kakamavu japo inayokoroma kutoka kwa Anitha ilibeba ujumbe mzito sana. Harakati nilizokuwa nasisitiza kila siku katika makala zangu, ule uzalendo uliopotea kwa vijana wengi na hali ya kuthubutu sasa niliionja tena kwa Anitha. Na kubwa zaidi yale mapenzi wanayodai kuwa yamelogwa na kuwa ya kudanganyana sasa niliyashuhudia katika upande wa mapenzi ya kweli.
Anitha alikuwa mwanaharakati!! Nilizungumza naye kwa kina akanielekeza juu ya hiyo hoteli ilipo.
Sikupoteza muda nikaivaa ile nguo yangu ambayo siku iliyopita ililowana mikojo ya kiutu uzima. Moja kwa moja nikaenda Temeke kukutana na anitha.
Wakati huu sikumtilia mashaka tena!!
Nilifika hadi chumbani baada ya kuruhusiwa kuingia. Anitha hakuwa akidanganya jambo lolote lile, uso wake mweupe ulikuwa mwekundu, midomo ilivimba sana na yale macho yaliyowahangaisha wanaume wengi sasa hayakuwa na mvuto wowote. Alijaribu kutabasamu lakini akaishia njiani ni kama alipatwa na maumivu kinywani. Nikajisikia huruma nikamkaribia, nilimpooza kwa maneno ya hapa na pale na kisha nikakiri mbele yake kuwa yeye alikuwa ‘steringi wa kike’ katika filamu asiyehofia chochote.
“Anitha sasa vipi kuhusu shule….” Nilimuuliza, badala ya kujibu akalazimisha tena tabasamu.

“Sam!! Tunasoma ili kupambanua mambo katika jamii inayotuzunguka, na si kupata shahada ya makaratasi huku tukishindwa kutatua matatizo katika jamii yetu. Huku nilipoamua kuingia ni shule kubwa zaidi ya hiyo ya makaratasi bila uwezo wa kuchanganua na kupambanua mambo!!!
Unamfahamu Nelson Mandela?? Alifungwa akiwa na miaka mingapi? Alifungwa gerezani miaka mingapi?? Je alipotoka alitumia makaratasi ya shuleni kulipigania taifa lake alilolipenda?? La!! Ile shule ya kunyanyaswa ilikuwa kubwa kabisa katika maisha yake!! Ama labda nikuulize ni wanafunzi wangapi wanaopata daraja la kwanza vyuoni na nchi haiwatambui kwa lolote lile zaidi ya sifa wapatayo siku ya matokeo?? Lakini ni nani awezaye kumsahau yule mwanafunzi kijana kabisa kutoka chuo cha Havard Marekani aliyebuni mtandao wa kijamii wenye nguvu kupita yote duniani?? Nani wa kumsahau Mark Zuckerberg na facebook yake.? Unadhani Mark alitumia makaratasi yake ya kufaulu!! Tuutumie muda uliopo vyema ili tusijutie wakati ujao!!” alijibu kwa kujiamini Anitha hadio akanishangaza, nikaamini kwa kile alichokisema kuwa elimu ya darasani bila uwezo wa kutatua tatizo ni buree!!

Tulizungumza mengi!! Majira ya saa kumi na mbili jioni tukawa na maamuzi, nikaondoka na kwenda kukata tiketi kwa ajiri ya safari ya kwenda Iringa. Kwa lengo moja tu kuitambua Michigani ambayo hadi wakati huo hatukujua kama ni hoteli, casino ama mgahawa!! Lakini tulitaka kuijua Michigan.
Tuliamua iwe siku inayofuata ili kuokoa maisha ya Eva na mama yake ambao lazima sumu za kwenye magazeti kuwa mimi kibaka tena muuaji na mlawiti zilikuwa zimeathiri akili yao kupindukia!!
Nilifanikiwa kupata tiketi mbili za kukaa katika siti moja. Nikiwa nimeandika majina ya bandia!!
Tulilala kimya kila mmoja na tafakari yake, nilikuwa na amani kuwa nipo na mtu sahihi kabisa katika harakati hizi za kunirejeshea amani iliyotoweka na pia kunirejeshea familia yangu!!!
Alfajiri tulikuwa tayari kwa safari ile, safari matata kabisa kila mmoja akiwa mgeni katika mkoa wa Iringa!
Safari ya kwenda kutafuta kitu tusichokijua, lakini kitu tulichoamini kuwa kitatuletea majibu ya maswali yetu ambayo yalikuwa gizani nasi tukiwa gizani huku tukilazimika kuyajibu ili utokee mwanga!!!
Badala ya kupata siti mbili zilizoungana kwa ajili yetu tulijikuta tukiwekwa katika siti ya watu watatu!! Hatukulalamika kwa sababu tulikuwa na shida ya kusafiri!!
Pembeni yetu alikuwepo msichana machachali ambaye alizoeana na kila abiria kana kwamba ni ndugu yake!! Na sisi tuliokuwanaye siti moja alitulazimisha hadi tukamzoea, hadi kufikia Mikumi Morogoro ni kama alikuwa ndugu yetu wa karibu!!
Hapo nikatumia nafasi ya mazoea hayo nikauliza swali.
“Hivi Michigani huwa ni Iringa ama Mbeya maana niliisikia nikiwa Dar es salaam enzi hizo.” Swali lile lilimfanya acheke na kisha kwa kutuonyesha ukomavu wake alitoa majibu yake!!
“Yaani Michigani zimebakia picha tu, aisee paliteketea moto mbona!! Miezi tisa iliyopita mbona ilikuwa mshikemshike, sema uzuri hakuna mtu aliyekufa!! Kwa hiyo Michigani imebakia stori tu hakuna kitu kama hicho kule kama hukubahatika kupaona basi tena watafute akina sisi malijendari wa miji tukuonyeshe picha!!” alijibu kwa kirefu kisha akatoa cheko refu!!
Anitha akanibinya kuniondoa katika mshangao ule!! Lakini na yeye alikuwa ameduwaa!!
Michigani iliteketea miezi tisa iliyopita, katika karatasi lililoandikwa jina la kindo limendikwa miezi tisa iliyopita. Kuna picha ya mahali panaitwa Michigani!!!
Mkasa ukaingia ugumu mwingine!!
Tunatafuta mahali ambapo pamebakia historia!!!!
Nikalegea kwa uchovu na kukata tamaa!!

***JIFUNZE!!…UZALENDO ni hali ya kuwa tayari kupigania kitu kwa manufaa ya wengi. Lakini Uzalendo huja hata katika mazingira ya kawaida, je wewe ni mzalendo kwa familia yako? Je una uzalendo kwa umpendaye ama ndo akiwa katika ugumu unajiepusha naye!! Taifa lako ni kubwa sana kulifanyia uzalendo, lakini vipi kuhusu jamii ndogo inayokuzunguka, vipi kwa watu wema kwako???

Safari iliendelea huku dada msema mengi akiwa anazidi kutuburudisha kwa tuo. Mara alete simulizi hii mara ahamie hii, Anitha alikuwa wa kwanza kuyachoka maongezi na uchovu wa safari. Akasinzia!!
Kisha Yule dada naye baada ya porojo za muda mrefu na yeye akasinzia!!
Binafsi sikuwa na hamu hata kidogo ya kulala, na macho yalikuwa angavu kutazama hapa na pale ndani na nje ya basi lile.
Ninakumbuka jina lake ni Super Feo!!

Tulipofika Mikumi basi lilisimama katika hoteli fulani, kusimama huku kukamzindua tena yule dada msema sana. Akaanza kusimulia juu ya hoteli ili kuonyesha kuwa anaijua sana. Sote tulitelemka na kujipatia mahitaji yetu, kisha tukarejea ndani ya basi tena kuendelea na safari ya masaa kadhaa, tukaupita mlima Kitonga na hatimaye Iringa ikaanza kunukia.
Nikamnong’oneza Anitha kuwa tusishukie Iringa bali twende mbele kidogo aidha Mafinga ama Makambako kabisa.
Aliniuliza kwa nini lakini sikutaka kumweleza kwa kirefu, kichwani mwangu niliamua kuishi kwa hofu tena bila kumwamini kiumbe aitwaye mwanadamu.
Dada msema mengi alikuwa ameahidi kuwa mwenyeji wetu mjini Iringa na kama ikifaa atatuonyesha picha za Michigani na eneo lenyewe.
Lilikuwa jambo ambalo tulikuwa tunalihitaji sana, lakini hapakuwa na haja ya kuingia katika hatari usiyojua kama ni hatari na kushindwa kujihadhari na mwishowe kuambulia mabaya!!!
Tulipofika Iringa yule dada alijikuta akishuka yeye pekee nasi tukiunganisha hadi Mafinga!!
Huko tukatelemka, bila kupumzika tukachukua gari ndogo ikatusafirisha kurejea Iringa tena!!
Hatimaye majira ya saa kumi na mbili unusu jioni tulikuwa Iringa mjini.
Hoteli inayokwenda kwa jina la MR ndo ilituhifadhi usiku ule katika mji ule ambao una baridi haswa.
Ilikuwa hoteli yenye hadhi yake na tuliamua kujihifadhi katika hoteli ya hadhi ile kwa sababu ilitulazima kwanza kuupata usalama kabla ya kuendelea na jambo lolote lile.
Hakika tulikuwa salama!!! Lakini hatukulala kabla ya kuamua jinsi ya kuianza safari yetu!!
Nilimweleza Anitha kuwa ule ulikuwa usiku wetu pekee wa kuwa pamoja kabla hatujatengana na kisha kuwa tunaonana mara moja moja iwapo inabidi!!
“Anitha, unajua fika kuwa mimi natangwaza magazetini nikishushiwa kesi lukuki ambazo sihusiki nazo. Najua hata wewe utatangazwa kupotea labda kutokana na kutoweka nyumbani ghafla lakini taarifa zako haziwezi kuwa nzito kama zangu. Hivyo kwa upande wako ukiamua kufanya jambo moja tu la kuubadilisha mwonekano wako hakuna ambaye atakuwa na shida na wewe. Na ninakwambia kuwa inatulazimu kuwa mbalimbali ilimradi tu mkakati usije kukomea njiani. Kesho nitakuwa nawe katika kuitazama Michigan kwa jicho la tatu lakini baada ya hapo Anitha utalazimika kuwa pekee nami kuwa mtu wa kupewa taarifa na kutoa ushauri!!” nilimweleza kwa kirefu zaidi na hakuonyesha kushtuka hata kidogo.
“Niliamua kuja huku kwa hiari yangu mwenyewe!! Sikulazimishwa na litakalotokea huku ni juu yangu!! Usijali Sam mimi nitasimama imara kukabiliana na lolote.” Hiyo ilikuwa kauli kuu ya mwisho kabla kila mmoja hajapitiwa na usingizi!!!

MKAKATI WA UKOMBOZI

MAJIRA ya saa nne asubuhi tulikuwa eneo ambalo lilijulikana kama Michigan miezi kadhaa nyuma, sasa liliitwa Semtema na katika eneo hilo kilikuwepo chuo kikuu cha Tumaini.
Hapakufanania hata kidogo na hali ya hatari, kila mmoja alikuwa na mambo yake eneo lile.
Semtema!! Tulilazimika kujaribu kuuliza kwanini paliitwa hivyo, wenyeji wakadai kuwa kwa kihehe jina linaloanzia se linamaanisha mwanamke, hivyo kama pangeitwa Mwamtema, hii ingesimama badala ya mwanaume!!
Ilistaajabisha. Hiyo Michigan mbona haipo sasa. Wenyeji wakakana kujua kuhusu Michigan na wengine wakasema walisikia tu uvumi.
Yule dada msema mengi alitudanganya ama!!! Nilijiuliza huku nikizidi kustaajabu.
Majira ya saa sita tuliamua kuzurura zaidi na kutafuta chakula. Bila kujua wapi tunaelekea tulijikuta katika eneo ambalo lilifahamika kwa jina la Isoka. Wenyeji hawakuwa na haja ya kutueleza lolote mtaa huu ungeweza kuuita uswahilini.
Kona hii bangi, mara gongo na kona kona nyingi bila kukutana na mtu anayejali ya mwenzake!!
Tuliamua kutumia eneo lile ili kufaidika na ushushushu wa watu wa uswahilini. Baada ya chakula ilikuwa zamu ya Anitha. Akamuuliza mama muuza chakula juu ya Michigani.
Uzuri wa wahehe, wabena na wakinga ambao ndo wengi katika mkoa wa Iringa, ni wakarimu sana na wanapenda kuzungumza.
Huyu mama hapo tukawa tumemfikisha!!
Na yeye kama yule mama wa kwenye basi aliyetusimulia juu ya Michigani huyu naye aliielezea kadri awezavyo. Hapo sasa tukapata jibu kuwa huenda kule Semtema tulikuwa tunapata majibu kutoka kwa wanachuo ambao wengi si wenyeji wa Iringa na hawaujui mkoa ule.
Maelezo ya huyu mama yakaambatana na ucheshi kidogo. Ni kweli alisisitiza kuwa Michigani haikuwepo tena Iringa, lakini kicheko kilikuja alipomfananisha Masawe kama mshamba!!
“Masawe nd’o nani tena?” Anitha alimuuliza.
“Yupo mchaga mmoja hivi ambaye amekimbia uchagani huko si unajua walivyo wale kwa maduka!! Amefungua duka huku eti akaliita Michigani, kiduka chenyewe kibovu!! Sijaona wachaga wasiojua kufanya biashara kama Masawe yaani!! Ukienda leo mara mafuta hakuna, kesho kiberiti hakuna!! Hovyo kabisa nimemuhama. Michigani ilikuwa enzi hizo, ye analeta leo khaaaa” Alijibu kwa sauti ya juu yule mama na kuyapuuzia yote aliyokuwa anayasema kama hayana maana!!
Tulimdadisi huku tukimuunga mkono kila alipotaka kucheka nasi tulicheka!!
Tulipomaliza tukamlipa pesa yake na kuondoka.
“Mh!! Mama mcheshi yule.” Anitha alinisemesha. Badala ya kumjibu nilimtazama na kuhisi mwenzangu hajang’amua kitu fulani, kuwa yule mama ni zaidi ya ucheshi aliotupatia!! Lipo neno la ziada!!
Michigani!! Michigani ya Masawe!! Huyu Masawe lazima tu atakuwa anajua jambo kuhusiana na Michigani, huwezi tu kuita Michigani bila kujua kwanini unaita.
Anitha akagutuka na kusawazika usoni katika namna ya kustaajabu!!!
Tukapitia kibanda cha kutengeneza nywele.
Anitha akaingia mimi nikabaki nje kungoja!!
Alipotoka hakuna na nywele hata kidogo na hakutisha wala kuchekesha kwa muonekano ule lakini alikuwa amebadilika na asiyemjua asingeweza kuamini kuwa ni Anitha!!

Akiwa katika hali ile ile tulifanikiwa kukifikia kibanda cha Michigani. Kilikuwa kibanda kidogo tena pa kichovu sana. Tulikata tamaa huku tukijiaminisha kuwa maneno ya yule mama ni kweli kabisa.
Katika ya wachaga waliochoka kimawazo huyu alikuwa mmoja wao!!!
Anitha akanipa moyo kuwa tukae mahali na kungoja lakini sikuwa nahitaji la ziada tayari nilikata tamaa. Masawe anauza pipi kifua, ubuyu, na keki ndogondogo!! Wa nini sasa huyu!!
Hana maana Anitha!! Nilimwambia!!
“Sasa unadhani Sam ni wapi tutampata huyo mwenye maana?”
“Anitha ujue tunapigwa baridi saa mbili usiku hii, sikia kwani ile pesa tuliyoiacha ndani ni shilingi ngapi? Na je una pesa ya dharula tuachane hadi kesho tena nitakaponunua simu nd’o tuwasiliane!!”
“Ni milioni nne ile….”
“Weee Anitha umemfilisi mzee Matata we mtoto.”
Hakujibu na badala yake tukakubaliana kuwasiliana siku inayofuata!!
Nikamsindikiza hadi katika hoteli nyingine ya hadhi ya kawaida nami nikarejea MR Hoteli huku matumaini yakianza kufifia.
Matumaini ya kumrejesha Eva na mama yake katika himaya yangu!!
Matumaini ya kuwaaminisha watanzania kuwa sikufanya yote yali yaliyoandikwa gazetini.

****
Saa nne asubuhi tayari nilikuwa na simu, nikaandika namba za simu za Anitha alizokuwa amenipatia!! Upesi akapokea.
“Sam!! Sam!! Mvumilivu hula mbivu!!” alianza hivyo na hapo akaanza kutiririka.

ANITHA…….

“Kuwa wamoja haimaanishi hata mioyo yenu itaegemea upande mmoja, iwapo itakuwa hivyo basi mmoja akianguka nyote mnaanguka, mmoja akikata tamaa wote mnakata tamaa.
Ningeweza kuwa kama wewe Sam, ulivyokata tamaa nami nikate tamaa, lakini kama ulidhani kuwa nililala, mimi sikuwa tayari kulala huku moyo wangu ukinisukuma kufanya jambo fulani. Nilirejea kule uswahilini Isoka. Nilirejea na kuitazama hiyo inayoitwa Michigani Sam, nilikuwa makini sana kutazama huyu mchaga wa kuitwa Masawe anafunga duka saa ngapi, anaishi wapi kama ikibidi na muonekano wake maana jana alikuwa kwenye kidirisha hatukumuona vizuri.
Sam. Kwa duka ama niite kiduka kama kile unaweza kufuatwa na magari mawili!! Kwa hatari ipi iliyopo hadi iwe hivyo, sijaiona sura yake kutokana na giza lakini sam. Hapana mi nakataa yule Masawe yule…sijui lakini huenda anajua juu ya Michigani. Ama la anazo biashara za magendo anafanya na hicho kiduka ameweka kama gelesha tu!!” alinieleza kwa hisia huku akiahidi kuwa analivalia njuga suala hilo hadi ajue la ziada kuhusiana na kiduka kile.
Sikujua Anitha ataweza vipi kumchimba Masawe ambaye anaonekana kujikita katika hiyo biashara yake ya duka!!
Nilitamani kumuuliza lakini nikaona huu ni ukatishaji tamaa.
Nikampa hongera kisha nikakata simu na kujipanga vyema kitandani!!!
Bado nikiwa siamini kama kuna lolote linaweza kutokea katika kile kibanda walichokiita Michigani.
Nikiwa nimekubaliana na Anitha kuwa mimi nitaweza kuwa natoka mida ya usiku tu si vinginevyo kulingana na usala wangu!! Basi niliendelea kuwasiliana naye mara kwa mara kila palivyokuwa na tatizo lolote.

SAA NANE MCHANA. SIMU KUTOKA KWA ANITHA.

Wakati huu alizungumza kwa tahadhari kubwa sana. Sauti yake ni kama ilikuwa inanong’oneza.
“Sam, nimefanikiwa kumfuatilia Masawe na gari ile iliyomchukua usiku. Sam yule wa dukani si Masawe, Sam niamini ninachokwambia, Masawe si yule wa dukani, kuna mtu ameniambia kidogo juu ya uhusiano wao lakini hatuwezi kuzungumza katika simu nitakueleza nilichofanikiwa kujua juu ya Masawe. Sam kuna kitu kinazunguka hapa hata wana Iringa hawakijui!! Nipo mitaa ya huku wapi, sipajui ni wapi Sam lakini ndo huku anapokaa Masawe mwenye lile banda wanaloliita Michigani. Muonekano wake hauendani hata kidogo na kile kiuchafu….kuna picha nimefanikiwa kuipiga japo pamewekwa onyo kuhusu kupiga picha eneo hili. Nimekutumia katika barua pepe!!!…….
(Mara anitha akanyamaza…nikamuita hakunijibu!!! Kama sekunde kumi zikapita Anitha akaanza kuongea huku akitetemeka.
“Sam….Sam..kuna wanaume wanne, yeah wanne wamevaa suti nyeusi wawili nyuma yangu na wawili mbele yangu….Sam wanakuja kwangu hawa…macho yao wameziba kwa miwani…Sama nakamatwa….Sam Sam……Sam weeeee nakamatwa mimi Sam!!…….”
Ghafla nikasikia Anitha akipiga kelele, na pale simu ikakatika.
Nilipojaribu kupiga hakuwa akipatikana tena!!!
Maajabu haya!! Nilijaribu tena na tena kumpigia Anitha lakini simu haikupatikana.
Mungu wangu weee!! Mtoto wa watu nitajibu nini kama si kizaazaa kingine tena kikubwa zaidi.

Nilikaa, nikasimama, nikaingia bafuni na kutoka bila kufanya lolote.
Wanaume wamevaa suti nyeusi mbele na nyuma wakamzunguka!! Mungu wangu, sasa walijuaje kuwa anawafuatilia.
Nilitoka haraka katika hoteli ile na mimi nikaizima simu yangu kwa hofu ya kusomwa mtandao wa mahali nilipokuwa!!
Moja kwa moja nikaingia mitaani, nikazama katika kibanda kinachotoa huduma za Internet, upesi nikafungua barua pepe yangu!!
Nikakuta kweli Anitha alituma picha.
Picha ikafunguka!!
Hamad!!! Ilikuwa picha ya mtoto fulani ambaye niliwahi kumuona tena katika picha!!
Picha zilizokuwa katika fundo la makaratasi niliyochukua kwa Ezekiel!!
Palepale nikajipekua na kutoka na ile picha.
Naam!! Ilikuwa yenyewe na ilifanana kwa kila kitu.
Kuna nini hapo Iringa? Iringa kubwa sijui hata ni wapi alikuwepo Anitha hadi akafanikiwa kuchukua picha ile!!
Baada ya malipo nilikuwa kama nakaribia kupandwa na wazimu!! Nikajilaumu kwa kumwacha Anitha peke yake lakini kwa upande mwingine nikaona ni sawa kwa sababu kama tungeambatana tungekamatwa wote na huo ungekuwa wakati mbaya pengine kuliko yote katika maisha yangu!!!
Nilijaribu kwa mara nyingine kuwasha simu!! Nikajaribu kupiga simu ya Anitha lakini tatizo likawa lilelile. Nilipokata nikakumbana na ujumbe katika simu yangu.
“UTAKUJA KUMCHUKUA MWENYEWE!!” ujumbe uleule kama nilioachiwa wakati wakimchukua mama wa watoto wangu!!
Mama Eva!!….
Ilistaajabisha sana, hawa watu walikuwa wametambaa kiasi kikubwa hivyo????
Sasa nafanya nini? Hilo likawa swali ambalo sikuweza kupata jibu mara moja!!!

Nikaumiza kichwa zaidi na kufikiria ni nani anaweza kunisaidia.
Kwa mara ya kwanza tangu niingie katika kshkash hilo nikakumbuka kumpigia simu. Mama Samson!!
Mama yangu mzazi!!!
Nilikuwa nimeegemea chini ya mti simu ikiwa inaita……..
Kwa mara ya kwanza haikupokelewa!!!
Nikapiga tena, safari hii ikapokelewa.
Nikasikia kelele nyingi sana zinazofanana na vilio. Hatukuwa tukielewana, ikabidi mama akate simu.
Nikapiga tena, sasa alipokea na tulijitahidi kusikiana vyema.
“Nipigie baadaye nipo msibani!!!”
“Mama….” Nilimuita.
“Nani wewe mbona kama eeeh ni nani?” nilimsikia mama akibabaika, ni kama alikuwa amenigundua lakini hakuweza kusema moja kwa moja nami sikutaka kumhadaa.
“Sam hapa mama mwanao Sam.”
“Koma koma….ukome kuchezea akili yangu we mtoto…..ni nyie mmemuua mnanitania sivyo!!!” mama alinistaajabisha kwa majibu yake!!
“Mama mimi ni Sam mama, mama ni mimi.” Nilibaki kusisitiza tu. Mama hakujibu kitu nikalazimika kufanya jambo moja kuu la mwisho la kumsisitiza kuwa mimi ni Sam.
“Mama mimi ni Mwikwabe..” nikamtajia jina ambalo alinitungia utotoni. Hapa nikamsikia mama akihema kwa nguvu.
“Sam…..ni wewe mwanangu!! Mbona mnanichanganya, na huyu wanayemleta kwenye jeneza ni nani sasa.” Alitokwa na kauli ambayo ilinitoa machozi, mama alikuwa amechanganyikiwa kweli na nilijua jinsi gani akili yake imeghafirika.
“Mama sauti hii unayoisikia ni ya mtoto wako wa kumzaa, nipo hai mama. Kama utaletewa mwili hakikisha unautazama kwa makini mama utaamini kuwa nani ni mwanao.” Nilijieleza.
“Sam si wanasema mwili hauna kichwa sijui kimefanyanini huko na huku siwaelewi ujue, yaani Sam nimechanganyikiwa mwanangu!! Mdogo wako amepoteza fahamu hadi leo, baba yako ananiita mimi mchawi eti nimekutoa kafara Sam wangu!! Kweli nilivyoteseka na wewe Sam miezi na miaka leo hii nikutoa kafara Sam. Nilivyobangaiza pesa uende shule na ukapata lazi bado nikutoa kafara. Kweli baba yako ni wa kusema haya mbele ya watu kabisa ananitukana kiasi hicho na watu wanaamini kuwa nimekuua. Sasa wameweka kikao wananidai kichwa chako, eti kama sikitoa kichwa chako basi wananikata changu!! Si uje Sam uniokoe mama yako huku!! Ni wewe sam ujuaye mimi nina nafasi gani kwako Sam. Kama kweli upo hai Sam nakuomba ufanye jambo hili dogo kabisa kwangu!!! Njoo uwaumbue wazee hawa wanaoniita mimi mwanga tena mchawi niliyeshindikana!!” mama alimaliza kuzungumza huku akijizuia kulia, mimi kwa upande wangu sikuweza kujizuia, nilikuwa nalia. Sauti ya mama iliniumiza, waliomwita mama yangu mchawi waliniumiza zaidi nafsi.
Hadi mama yangu anakata simu nilikuwa katika mgagagiko wa aina yako!!
Mpalanganyiko usio kifani.
Anitha amekamatwa na niliisikia sauti yake ikiomba huruma yangu katika simu.
Mama yangu mzazi naye anazushiwa kuwa ameniua angali nipo hai!! Nilijua ni hila za watu wale wabaya kunifedhehesha na kuisababisha jamii nzima inilaani!!
Lakini kwanini sasa wamemgusa hadi mama yangu!! Kwanini uchungu wangu nichangie na mke wangu, mwanangu Eva, Anitha na sasa mama yangu mzazi.
Mwanamke mwenye thamani kwangu kuliko wanawake wote!!!

**JIFUNZE!! Wakati wa malalamiko yako uyatoayo kila siku na kujifanya wewe unaonewa kupita watu wote, kujifanya kuwa ni wewe umetendwa kupita watu wote duniani. Wapo wengine ambao kilio chao ni kikubwa zaidi na hawana amtu wa kuwasikiliza kama ilivyo kwako wewe!! Hawana msaada wowote na badala yake wanalia na nafsi zao!!
Wakati unajifikiria wewe kumbuka kumfikiria na jirani yako.
Huo nd’o UPENDO!!!

**SAM amebaki pekee tena, lakini licha ya kubaki pekee tatizo halijapungua na badala yake limeongezeka.
Mama analia na Anitha analia!!!

ITAENDELEA!!!!
TOA MAONI YAKO, SHARE na LIKES ndo kuichangamsha hadithi yetu
The Legend ” Aunty Ezekiel.
Songwriter: George Iron
Page Whatsapp number: 0683 241717

Point of ten

” I don’t know the only picture of the picture, I don’t know that it is a fire, what is the old months, what is the one who was to be mshikemshike, say that it is not a person of the story. That is the one who don’t Cities in the picture!!” respond and might get so long.
Anitha akanibinya kuniondoa in the surprise!! But he was a ameduwaa!!
Michigani Iliteketea Miezi Tisa Iliyopita, katika karatasi lililoandikwa jina la kindo limendikwa miezi tisa iliyopita. There is a picture called the michigani!!!
The tragedy is the other difficulty!!
We are looking at where you are in history!!!!
Nikalegea for tired and giving up!!

*** LEARN!!… patriotism is the situation for being ready for the benefits of many. But patriotism comes even in the usual environment, are you a patriot of your family? Are you patriotism for your love or when it is in the hardships. Your Nation is very big. How about the small community surrounding you, how are you to your good people?

Continue

Safari iliendelea huku dada msema mengi akiwa anazidi kutuburudisha kwa tuo. Mara alete simulizi hii mara ahamie hii, Anitha alikuwa wa kwanza kuyachoka maongezi na uchovu wa safari. Akasinzia!!
Then the sister with her people of a long time and he is akasinzia!!
Personally I was not afraid to sleep, and eyes was a bright way to watch here and there is outside and outside.
I remember his name is a super.

Tulipofika Mikumi basi lilisimama katika hoteli fulani, kusimama huku kukamzindua tena yule dada msema sana. Akaanza kusimulia juu ya hoteli ili kuonyesha kuwa anaijua sana. Sote tulitelemka na kujipatia mahitaji yetu, kisha tukarejea ndani ya basi tena kuendelea na safari ya masaa kadhaa, tukaupita mlima Kitonga na hatimaye Iringa ikaanza kunukia.
Nikamnong ‘ oneza anitha to be tusishukie iringa but let us go forward a bit either mafinga or makambako.
She asked me why I really wanted to tell him in my head, I decided to live to fear again without trusting the human being.
Sister who says that the one he has promised to be in our host in iringa, and if you have a ikifaa to be atatuonyesha with the picture
It was something that we were really tunalihitaji, but there was a need to get in the risk, if it is very dangerous and losing you don’t pay evil.
He has arrived at iringa, sister, you are alijikuta to be akishuka. with us, we are
There is a tukatelemka, without resting, the small car is to return iringa again.
Finally season
Hoteli inayokwenda kwa jina la MR ndo ilituhifadhi usiku ule katika mji ule ambao una baridi haswa.
It was full of his status and we decided to be kujihifadhi in the status of the status of the status of the status. It will come to come to be security before you
Surely we were well!!! But you will be hatukulala before deciding for the way you start our journey.
Nilimweleza Anitha kuwa ule ulikuwa usiku wetu pekee wa kuwa pamoja kabla hatujatengana na kisha kuwa tunaonana mara moja moja iwapo inabidi!!
“Anitha, unajua fika kuwa mimi natangwaza magazetini nikishushiwa kesi lukuki ambazo sihusiki nazo. Najua hata wewe utatangazwa kupotea labda kutokana na kutoweka nyumbani ghafla lakini taarifa zako haziwezi kuwa nzito kama zangu. Hivyo kwa upande wako ukiamua kufanya jambo moja tu la kuubadilisha mwonekano wako hakuna ambaye atakuwa na shida na wewe. Na ninakwambia kuwa inatulazimu kuwa mbalimbali ilimradi tu mkakati usije kukomea njiani. Kesho nitakuwa nawe katika kuitazama Michigan kwa jicho la tatu lakini baada ya hapo Anitha utalazimika kuwa pekee nami kuwa mtu wa kupewa taarifa na kutoa ushauri!!” nilimweleza kwa kirefu zaidi na hakuonyesha kushtuka hata kidogo.
“Niliamua kuja huku kwa hiari yangu mwenyewe!! Sikulazimishwa na litakalotokea huku ni juu yangu!! Usijali Sam mimi nitasimama imara kukabiliana na lolote.” Hiyo ilikuwa kauli kuu ya mwisho kabla kila mmoja hajapitiwa na usingizi!!!

Strategies of deliverance

At the time at the morning we were in the area that we will be lilijulikana like Michigan several months. Now you will be semtema with the area of the university.
You are hapakufanania even a little and dangerous situation, everyone was with their own area.
Semtema!! Tulilazimika kujaribu kuuliza kwanini paliitwa hivyo, wenyeji wakadai kuwa kwa kihehe jina linaloanzia se linamaanisha mwanamke, hivyo kama pangeitwa mwamtema, hii ingesimama badala ya mwanaume!!
Ilistaajabisha That Michigan why is not now The locals are to know about Michigan and others said just the rumors.
That sister who says the lot of a lot is to be alitudanganya or!!!
At midnight we decided to wander more and looking for food Without knowing where we are going to be tulijikuta in the area that is lilifahamika in the name of the name The locals didn’t have a need of the kutueleza, this area would be in swahili.
The corner of marijuana, when the cudgels, the corner of the corner. Without to meet the person who cares about the one
Tuliamua kutumia eneo lile ili kufaidika na ushushushu wa watu wa uswahilini. Baada ya chakula ilikuwa zamu ya Anitha. Akamuuliza mama muuza chakula juu ya Michigani.
The goodness of poor people, we are wabena and people who are many in iringa province, it is very kind and love to talk.
This mother we were tumemfikisha!!
Na yeye kama yule mama wa kwenye basi aliyetusimulia juu ya Michigani huyu naye aliielezea kadri awezavyo. Hapo sasa tukapata jibu kuwa huenda kule Semtema tulikuwa tunapata majibu kutoka kwa wanachuo ambao wengi si wenyeji wa Iringa na hawaujui mkoa ule.
The information of this mother is to be yakaambatana with a little humor. It is true that you are to be a michigani, we will be haikuwepo again, but I came to alipomfananisha masawe like
“Masawe nd’o nani tena?” Anitha alimuuliza.
“Yupo mchaga mmoja hivi ambaye amekimbia uchagani huko si unajua walivyo wale kwa maduka!! Amefungua duka huku eti akaliita Michigani, kiduka chenyewe kibovu!! Sijaona wachaga wasiojua kufanya biashara kama Masawe yaani!! Ukienda leo mara mafuta hakuna, kesho kiberiti hakuna!! Hovyo kabisa nimemuhama. Michigani ilikuwa enzi hizo, ye analeta leo khaaaa” Alijibu kwa sauti ya juu yule mama na kuyapuuzia yote aliyokuwa anayasema kama hayana maana!!
Tulimdadisi huku tukimuunga mkono kila alipotaka kucheka nasi tulicheka!!
Tulipomaliza to be tukamlipa his money and leave.
” MH!! The funny mother.” anitha alinisemesha. What the way you don’t think and feeling my friend, don’t decide something. to be the mother is more than humor, there is a additional word!!
Michigani!!
Anitha Akagutuka and kusawazika the face in the wonder!!!
Tukapitia the shop to making hair
Anitha Akaingia I was left out on waiting!!
They have been with a hair even a little and you are hakutisha and funny and it’s change it’s change to it.

When it is in the situation that you are tulifanikiwa to kukifikia the the. It was a little booth to kichovu. I will be tulikata up here, you will be tukijiaminisha to be the words of the mother.
In the chaga, the thoughts of the mind was one!!!
Anitha her my heart as we stay in the place and waiting but I haven’t need a extra more. Masawe is selling a candy chest, squash, and the small cake!! What is this!!
Hana maana Anitha!! Nilimwambia!!
“Sasa unadhani Sam ni wapi tutampata huyo mwenye maana?”
“Anitha ujue tunapigwa baridi saa mbili usiku hii, sikia kwani ile pesa tuliyoiacha ndani ni shilingi ngapi? Na je una pesa ya dharula tuachane hadi kesho tena nitakaponunua simu nd’o tuwasiliane!!”
” its four million….”
” weee anitha the trouble old man, you are a child.”
He does not answer and instead of you, you are tukakubaliana in the next
You will be nikamsindikiza until the other hotel of the normal status and I will be nikarejea Mr. The Hotel, hope you will be
The hopes of the kumrejesha eve and his mother in my empire!!
The hopes of the tanzanians who does not make everything.

****
I have already been a good morning, I came out. I came. The of phone.
” Sam!! Sam!! Patience pays. He started that and start from the kutiririka.

ANITHA…….

“Kuwa wamoja haimaanishi hata mioyo yenu itaegemea upande mmoja, iwapo itakuwa hivyo basi mmoja akianguka nyote mnaanguka, mmoja akikata tamaa wote mnakata tamaa.
Ningeweza kuwa kama wewe Sam, ulivyokata tamaa nami nikate tamaa, lakini kama ulidhani kuwa nililala, mimi sikuwa tayari kulala huku moyo wangu ukinisukuma kufanya jambo fulani. Nilirejea kule uswahilini Isoka. Nilirejea na kuitazama hiyo inayoitwa Michigani Sam, nilikuwa makini sana kutazama huyu mchaga wa kuitwa Masawe anafunga duka saa ngapi, anaishi wapi kama ikibidi na muonekano wake maana jana alikuwa kwenye kidirisha hatukumuona vizuri.
Sam. Kwa duka ama niite kiduka kama kile unaweza kufuatwa na magari mawili!! Kwa hatari ipi iliyopo hadi iwe hivyo, sijaiona sura yake kutokana na giza lakini sam. Hapana mi nakataa yule Masawe yule…sijui lakini huenda anajua juu ya Michigani. Ama la anazo biashara za magendo anafanya na hicho kiduka ameweka kama gelesha tu!!” alinieleza kwa hisia huku akiahidi kuwa analivalia njuga suala hilo hadi ajue la ziada kuhusiana na kiduka kile.
I didn’t know anitha what is what you will be kumchimba masawe who looks to be kujikita in the shop business!!
I wanted to ask but I saw this is a ukatishaji.
I are nikampa congratulations then you will be a phone and get prepared to bed.
I am still when I don’t believe if there is anything can happen in the kiosk.
Nikiwa nimekubaliana na Anitha kuwa mimi nitaweza kuwa natoka mida ya usiku tu si vinginevyo kulingana na usala wangu!! Basi niliendelea kuwasiliana naye mara kwa mara kila palivyokuwa na tatizo lolote.

SAA NANE MCHANA. SIMU KUTOKA KWA ANITHA.

This time is alizungumza for big risks. His voice is like it is the inanong.
“Sam, nimefanikiwa kumfuatilia Masawe na gari ile iliyomchukua usiku. Sam yule wa dukani si Masawe, Sam niamini ninachokwambia, Masawe si yule wa dukani, kuna mtu ameniambia kidogo juu ya uhusiano wao lakini hatuwezi kuzungumza katika simu nitakueleza nilichofanikiwa kujua juu ya Masawe. Sam kuna kitu kinazunguka hapa hata wana Iringa hawakijui!! Nipo mitaa ya huku wapi, sipajui ni wapi Sam lakini ndo huku anapokaa Masawe mwenye lile banda wanaloliita Michigani. Muonekano wake hauendani hata kidogo na kile kiuchafu….kuna picha nimefanikiwa kuipiga japo pamewekwa onyo kuhusu kupiga picha eneo hili. Nimekutumia katika barua pepe!!!…….
(Mara anitha akanyamaza…nikamuita hakunijibu!!! Kama sekunde kumi zikapita Anitha akaanza kuongea huku akitetemeka.
“Sam….Sam..kuna wanaume wanne, yeah wanne wamevaa suti nyeusi wawili nyuma yangu na wawili mbele yangu….Sam wanakuja kwangu hawa…macho yao wameziba kwa miwani…Sama nakamatwa….Sam Sam……Sam weeeee nakamatwa mimi Sam!!…….”
Suddenly nikasikia anitha she calls their noise, and when the phone is ikakatika.
The nilipojaribu he was not to be akipatikana again!!!
This wonders!! I tried again and he knelt for anitha but phone was not found.
Mungu wangu weee!! Mtoto wa watu nitajibu nini kama si kizaazaa kingine tena kikubwa zaidi.

I lived and and stopped, I bumped to bathroom in a bathroom and without anything.
Men have worn a black suit before the back. My God, now you will be to be a anawafuatilia.
Nilitoka haraka katika hoteli ile na mimi nikaizima simu yangu kwa hofu ya kusomwa mtandao wa mahali nilipokuwa!!
One of one I bumped in the streets, nikazama in the kiosk making the internet services, in the email.
Nikakuta kweli Anitha alituma picha.
Picha ikafunguka!!
Hamad!!! was a picture of a certain child who ever see this photo!!
Picha zilizokuwa katika fundo la makaratasi niliyochukua kwa Ezekiel!!
Palepale nikajipekua na kutoka na ile picha.
Well!! was itself and ilifanana in everything!!
What is there in iringa? A big iringa, I don’t know where is in the anitha until the akafanikiwa to take the picture!!
Baada ya malipo nilikuwa kama nakaribia kupandwa na wazimu!! Nikajilaumu kwa kumwacha Anitha peke yake lakini kwa upande mwingine nikaona ni sawa kwa sababu kama tungeambatana tungekamatwa wote na huo ungekuwa wakati mbaya pengine kuliko yote katika maisha yangu!!!
Nilijaribu kwa mara nyingine kuwasha simu!! Nikajaribu kupiga simu ya Anitha lakini tatizo likawa lilelile. Nilipokata nikakumbana na ujumbe katika simu yangu.
” you will come to pick up!!” the same message if you are to be nilioachiwa when you are a mother of
Mama Eva!!….
I don’t have a lot, these people were to be wametambaa so much.
What is I doing That is a question that couldn’t have an answer once!!!

I have nikaumiza more head and thinking who can help me.
For the first time since I went to the kshkash that I have, I have not asked him. Mama Samson!!
My biological mother!!!
Nilikuwa nimeegemea chini ya mti simu ikiwa inaita……..
Kwa mara ya kwanza haikupokelewa!!!
Nikapiga tena, safari hii ikapokelewa.
I do not have many noise so much the resembled ones and tears. We were not the tukielewana, I was forced mother he will still call
I got again, now the new and tulijitahidi.
” call me after I am at a funeral!!!”
” mother….”
“Nani wewe mbona kama eeeh ni nani?” nilimsikia mama akibabaika, ni kama alikuwa amenigundua lakini hakuweza kusema moja kwa moja nami sikutaka kumhadaa.
“Sam hapa mama mwanao Sam.”
“Koma koma….ukome kuchezea akili yangu we mtoto…..ni nyie mmemuua mnanitania sivyo!!!” mama alinistaajabisha kwa majibu yake!!
“Mama mimi ni Sam mama, mama ni mimi.” Nilibaki kusisitiza tu. Mama hakujibu kitu nikalazimika kufanya jambo moja kuu la mwisho la kumsisitiza kuwa mimi ni Sam.
“Mama mimi ni Mwikwabe..” nikamtajia jina ambalo alinitungia utotoni. Hapa nikamsikia mama akihema kwa nguvu.
“Sam…..ni wewe mwanangu!! Mbona mnanichanganya, na huyu wanayemleta kwenye jeneza ni nani sasa.” Alitokwa na kauli ambayo ilinitoa machozi, mama alikuwa amechanganyikiwa kweli na nilijua jinsi gani akili yake imeghafirika.
“Mama sauti hii unayoisikia ni ya mtoto wako wa kumzaa, nipo hai mama. Kama utaletewa mwili hakikisha unautazama kwa makini mama utaamini kuwa nani ni mwanao.” Nilijieleza.
“Sam si wanasema mwili hauna kichwa sijui kimefanyanini huko na huku siwaelewi ujue, yaani Sam nimechanganyikiwa mwanangu!! Mdogo wako amepoteza fahamu hadi leo, baba yako ananiita mimi mchawi eti nimekutoa kafara Sam wangu!! Kweli nilivyoteseka na wewe Sam miezi na miaka leo hii nikutoa kafara Sam. Nilivyobangaiza pesa uende shule na ukapata lazi bado nikutoa kafara. Kweli baba yako ni wa kusema haya mbele ya watu kabisa ananitukana kiasi hicho na watu wanaamini kuwa nimekuua. Sasa wameweka kikao wananidai kichwa chako, eti kama sikitoa kichwa chako basi wananikata changu!! Si uje Sam uniokoe mama yako huku!! Ni wewe sam ujuaye mimi nina nafasi gani kwako Sam. Kama kweli upo hai Sam nakuomba ufanye jambo hili dogo kabisa kwangu!!! Njoo uwaumbue wazee hawa wanaoniita mimi mwanga tena mchawi niliyeshindikana!!” mama alimaliza kuzungumza huku akijizuia kulia, mimi kwa upande wangu sikuweza kujizuia, nilikuwa nalia. Sauti ya mama iliniumiza, waliomwita mama yangu mchawi waliniumiza zaidi nafsi.
Until my mother is breaking his phone was in the mgagagiko of your type!!
Mpalanganyiko usio kifani.
Anitha amekamatwa na niliisikia sauti yake ikiomba huruma yangu katika simu.
Mama yangu mzazi naye anazushiwa kuwa ameniua angali nipo hai!! Nilijua ni hila za watu wale wabaya kunifedhehesha na kuisababisha jamii nzima inilaani!!
Lakini kwanini sasa wamemgusa hadi mama yangu!! Kwanini uchungu wangu nichangie na mke wangu, mwanangu Eva, Anitha na sasa mama yangu mzazi.
Mwanamke mwenye thamani kwangu kuliko wanawake wote!!!

**JIFUNZE!! Wakati wa malalamiko yako uyatoayo kila siku na kujifanya wewe unaonewa kupita watu wote, kujifanya kuwa ni wewe umetendwa kupita watu wote duniani. Wapo wengine ambao kilio chao ni kikubwa zaidi na hawana mtu wa kuwasikiliza kama ilivyo kwako wewe!! Hawana msaada wowote na badala yake wanalia na nafsi zao!!
Wakati unajifikiria wewe kumbuka kumfikiria na jirani yako.
Huo nd’o UPENDO!!!

KITENDO cha kujikuta namweka mama yangu mzazi na Anitha katikia mzani mmoja ili nijue nini cha kufanya na nani wa kuanzia kilinivuruga akili akili. Kuna mda nililazimika kusema kwa sauti ilhali hakuna yeyote aliyekuwa akinisikiliza. Nilihaha huku na kule katika mkoa ule wa Iringa nab ado hali ilikuwa tete.
Sikuwa na ndugu, rafiki na hata jamaa wa karibu wa kuweza kumshirikisha lolote lile. Niliketi chini ya ule mti na pasipokutarajia nikapitiwa na usingizi. Bila shaka kutokana na mawazo yaliyokuwa yanazidi badala ya kupungua.
Mimi naitwa marehemu!! Ni nani huyu anasimama nyuma ya haya mambo yote? Niliwaza baada ya kurejewa tena na uhai baada ya kifo cha usingizi!!
Mkononi nilikuwa na bahasha yangu ambayo thamani yake ilizidi kushuka badala ya kuongezeka. Bahasha ambayo badala ya kunipa tumaini iliishia kunipa dalili tu ya matumaini kisha yakatoweka pasipo kutimia. Bahasha ambayo sasa imenionyesha picha ya mtoto ambaye ameketi na ni picha hiyohiyo kutoka katika barua pepe aliyonitumia Anitha.
Anitha ambaye sasa sipo naye tena na sijui ni kitu gani kimemsibu!!
Mbaya zaidi nimetumiwa ujumbe kuwa NITAMFUATA…sasa namfuata wapi mimi eeh!!
Na huku mama anatishiwa kukatwa kichwa iwapo tu kichwa change hakitaonekana!! Mimi ambaye nipo hai.

Washenzi wameamua kuigusa familia yangu ili nijitokeze waniue!!! Ni hili nililitambua kichwani mwangu. Mbaya zaidi sikuwa tayari kujitokeza kwa mtu yeyote yule kabla sijajiweka salama.
Kilichonipa faraja ni maneno ya Anitha usiku ule tuliokutana kwa mara ya kwanza tangu atoroke nyumbani kwao.
“Pesa ni kila kitu!!” nikafanya tabasamu na kisha nikautazama ule mfuko wenye pesa zilizohifadhiwa katika usalama wa hali ya juu!!
Asante sana Anitha!!! Sijui kama zisingekuwepo pesa hizi ningekuwa katika mawazo gani mengine!! Nilijisemea. Na hapo nikanyanyuka na kupiga hatua nyingi kuelekea popote pale na sikuwa nikitambua majina ya mitaa mingi!!
Kufikia hapo nikaamini kuwa nilikuwa nahitaji kwa namna yoyote ile mwenyeji wa mkoa huo aweze kuwa mwanga wangu. Lakini kigumu zaidi nililazimika kupata mwenyeji asiyenifahamu!!
Jambo gumu kabisa, utajuaje mtu hakufahamu!!!
Nikaghairi.
Maamuzi ya pili yakawa ‘jino kwa jino’.
Nikapanga safari ya kwenda Morogoro. Kwanza niwakabili jino kwa jino hao watu wanaotishia amani ya mama yangu halafu kitakachofuata hapo na lolote liwe lakini walau nimpiganie mama yangu!!!
Kwa Anitha sikujua wapi naanzia hivyo huenda ni vyema kupata moja kuliko kukosa yote, isitoshe Anitha alikuwa ni askari aliye tayari kufia vitani akitetea haki!!
Nikalala bila kula chochote, asubuhi sana nikadamkia katika stendi ya Iringa.
Baridi ilikuwa kali sana!! Na basi lilikuwa halijafika, hali ile ya hewa ikanikumbusha jijini Dar es salaam, siku ambayo nakutana na mauzauza ya Ezekiel wawili mmoja mzima na mwingine maiti.
Kisha baada ya masaa kadhaa nakumbwa na kashfa ya kulawiti hadi kuua!!
Uchachu ukanikumba mdomo baada ya kuwaza siku hiyo. Nikatafuta sigara nikawasha na kuanza kupuliza kama siku ile!!!
Nilipopiga funda nne, basi likawasili. Nikaionea huruma ile sigara lakini nikalazimika kuizima kisha kuisagia chini!!
Nikaelekea garini!! Nikapata siti ya dirishani. Nilikuwa sijielewi hata kidogo lakini nilijua naikaribia shari.
Kelele za vijana wauza maji, soda na vinywaji vingine hazikunifurahisha bali kunibughuzi. Mara huyu apige mayowe haya mwingine alalamike vile ilimradi tu bughudha.
“Pata Bajia, Sambusa za leoleo, sambusa za moto mtoto anapoozewa, sambusa za nyama achana na zile za Singida mwawekewa nyama ya punda, usisikie ya watu wahehe wala mbwa…uzushi mtupu kula mwenyewe ujionee kisha ukahadithie. Ukinunua moja nakupa na picha ya huyo ng’ombe aliyechinjwa!! Usiwasikilize wazushi, niulize mimi mama lao!!” hizi zilikuwa porojo nyingine tena, sauti hii ilipangilia maneno hasa na ilikuwa ikirudia mara kwa mara bila kukosea hata kidogo!! Abiria waliokuwa garini wakajikuta wanacheka, lakini katika kucheka huko wengine wakataka kununua kweli. Mimi nikajituliza huku nikijilazimisha kusahau kama nimesikia porojo zile sikuwa na hamu ya bajia wala sambusa za nyama ambazo yule mama alipinga kabisa kuwa sio nyama ya mbwa!!!

Baada ya muda kidogo sauti ile ilihamia katika gari ndani! Mama aliendelea kutuliwaza abiria na maneno yake. Nikavutiwa kunyanyua kichwa nimtazame vyema anafanania vipi huyu mama mwenye uwezo wa ajabu vile wa kukariri.
Lahaula!! Sura haikuwa ngeni machoni mwangu!! Alikuwa ni mama ama niite mwanamke ambaye siku kadhaa nyuma tulisafiri naye wakati tunatoka jijini Dar es saalam, porojo zake zikatufanya tuijue kiasi Michigani.
Sasa alikuwa katika basi letu!!
Nikataka kumpuuzia lakini imani ikanivuta kumuamini kiasi, nikaisshusha vyema kofia yangu ikaniziba sura yangu. Na mimi nikaomba huduma ya sambusa.
Akajongea nilipokuwa huku akiendelea kuhamasisha juu ya sambusa zake.
“Anti samahani naweza kuuliza?” nilianza kujenga hoja.
“Wahehe, Wabena, Wakinga asili yetu ustaarabu na ukarimu, ukitukera hatulipi kisasi siye twajinyonga tu!! Niambie bila shida baba yangu!!” alinijibu huku akinifungia sambusa tatu kama nilivyomwagiza.

“Hivi ni wewe tumesafiri wote majuzi kutoka Dar tuka….”
Kabla sijamalizia tayari alikwisha nitambua.
“Wa Michigani nyieeee ni wewe looh, yukwapi bibi yako yule mbona ana wivu sana yule.” Alinieleza kwa sauti ya chini nikasikia peke yangu.
“Hayupo leo mamangu kuna matatizo yamemkumba…”
“Alienda Michigani ama?” aliniuliza kwa sauti tulivu, sasa hakuwa katika utani wowote ule. Uso wake ulionyesha wasiwasi na ni kama kuna kitu hakupenda kiwe kama anavyodhani. Hakutaka jibu langu liwe kweli.
“Hapana ni matatizo mengine tu, kwanini umewazia Michigan?” nilihoji huku nikiuficha wasiwasi wangu.
“Mh…..afadhali kama sio huko maana….ehee we nawe tena mbona unarudi mwenyewe Dar es salaam” alihoji na sasa alikuwa anatabasamu.
“Hata sirudi Dar ujue, hivi tunaweza kuongea kidogo.” Niliamua kutumia nafasi.
“Lakini bado dakika mbili gari linaondoka hapa.” Alinitahadharisha. Nikamweleza haikuwa muhimu kusafiri wakati sijazungumza naye.
Akakubaliana nami, tukatelemka chini huku akisifia sambusa zake.
Mwanga ulikuwa umeanza kuonekana na giza likaipisha nuru! Tukajiweka mbali na umati wa watu. Nikamweleza shida yangu.
Nikamweleza juu ya Anitha na kupotea kwake katika namna ya utata. Sikumuamini kiundani na kumweleza juu ya hatia inayonikabili jijini dare s saalam juu ya mauaji. Nilimuacha yeye awe msemaji mkuu.
“Kaka Sambusa zangu zitaniozea lakini ujue.” Alinitahadharisha.
“Kwani kapu moja bei gani kwa ujumla.” Akanitajia bei, nikamweleza kuwa nitamlipa mara mbili. Na kama hakuamini vile nikajipekua na kutoka na kiasi alichotaja na ziada yake.
Macho yakamtoka pima na bado hakuonekana kunitambua!!

Mazungumzo yakaanzia pale, yule mwanamke akanieleza machache ayajuayo juu ya mkoa ule. Akapinga kabisa kuwa Anitha amechukuliwa kishirikina. Akapinga kuwa mkoa ule hauna mambo hayo ya kurogana.
“Tena basi bora angekuwa mwenyeji wa huku!! Yaani mgeni hana hata siku nne!! Mi nakataa kwa kweli labda tu kuna mwanaume amemuweka ndani wewe hujui.” Alinijibu kiuhakika zaidi. Nikatamani kumweleza japo kwa ufupi kuwa mimi ni nani lakini niliingiwa hofu.
Nikamuona kama anafikiria jambo kidogo na kasha akasema kwa sauti ya chini kama anayejisemea mwenyewe.
“Auuu labda mambo ya Anti Ezekiel yameanza tena…lakini hamna wala haiwezekani.”
Maneno yake yakanishtua, alikuwa ametaja jambo zito katika sauti ndogo!!
Anti Ezekiel!! Jina hili lilihusiana na mkasa wangu moja kwa moja. Nikakosa ustahimilivu nikahoji.
“Anti Ezekiel ndo nani kwani?”
“Jamaa aliyeleta uzushi huo na yeye ukimuuliza anakwambia jibu hili moja tu UKIJUA NA WEWE UNAPOTEA” alinijibu kwa utaratibu na hakutaka kulizungumzia zaidi.
“Nani anayesema habari hizo kwani?’ sikutaka jambo hili liishie juu ya juu. Nikambana.
“Simfahamu lakini wanasema ni kichaa mmoja hivi. Hakuna atakaye kuamini kuhusu hilo. Si unajua maneno ya vichaa, kwa jinsi nilivyosimuliwa ni kwamba watu walikuwa wakipotea, waganga wa jadi wakishinda kupata majibu yeye anasema ni upepo wa Anti Ezekiel. Mbona huu mwaka wa nne unafika sasa tangu zivume hizi habari.” Alinieleza kwa utulivu huku akiyatuliza macho yake usoni kwangu.
Maelezo yake yakazidi kunichanganya, sasa yule Ezekiel nd’o anafanya nini sasa, mara amekufa mara akaonekana Ubungo, sasa huku Iringa tena kuna Anti Ezekiel wao. Upuuzi huu. Nilihisi kuchanganyikiwa.
“Kwani kaka, Anitha yeye kapoteaje ghafla hivyo!! Tatizo lako ni moja tu wewe unanificha siri huku ukisahau kuwa mficha uchi hazai. Na mficha jipu usaha utamuumbua….” Alinipiga na maneno yale makali, nikajisikia aibu sana maana alikuwa amesema kweli.

“Sio kama nakuficha mama…hapana nimechanganyikiwa kabisa!!!”
“Unadhani suluhu n’do kukaa kimya kaka!!” alizidi kunibana.
Kabla sijasema lolote akachukua uwanja zaidi.
“Sam..” akaniita. Moyo ukapiga kwa nguvu kubwa!! Amenijuaje jina langu huyu mwanamke ilhali siku ya safari sikujitambulisha kwa lolote lile.
“Unajiuliza nimekujuaje?” alisema kilichokuwa katika akili yangu!!
“Sam mdogo wangu! Ama kaka yangu vyovyote vile, katika mawazo yako unadhani mimi ni mtu mbaya ama ninayeweza kuhatarisha amani yako ambayo tayari ipo hatarini. Sam mimi sipo hivyo, nd’o maana hata kwenye basi tulilopanda nilikutambua kuwa unasakwa kwa udi na uvumba lakini je nilisema neon lolote mie! Nilishakoma tabia ya kujifanya najua mambo, biashara yangu ya bajia na sambusa inanitosha sana.
Sihitaji kupata mamilioni kwa kumsukumiza kijana mwenzangu katika moto. Baba yangu amefia jela kwa kosa la kusingiziwa, nitajuaje kama na wewe wanakusingizia, ujue polisi watu wa ajabu sana, wanapenda sana kusaidiwa upelelezi lakini wewe sasa uwe na shida uwaombe msaada nd’o utakoma na kiherehere chako. kama walishindwa kuniruhusu tu kuongea na baba yangu!! Wakanitishia kunifunga, niwapendee nini mimi sasa!!
Mzeewangu akahusishwa na wanaume wengine wanane eti wamehusika kuteketeza Michigani?? Mimi nilikuwa mfanyakazi pale ndani, Michigani haikuwa ya kuteketezwa na watu masikini kama wale. Haya masikini ana haki, Michigani ikateketea na baba naye akafungwa!! Nd’o mimi unayeniona hapa sasa Iringa nd’o mama lao. Yaani sina ndugu wala shoga, napiga kazi tu kupata mkate wangu wa kila siku. Kama wewe usivyomwamini mtu kwa mkasa wako huu na mimi simwamini mtu.
Nilipokuona nikakutambua, machoni hukufanania na mlawiti na muuaji. Tena juzi niliposoma gazetini kuwa umekufa nd’o nikajua kabisa kuwa kuna mpango hapa si bure!! Kama kweli umekufa mbona upo hapa muda huu? “ sasa aliniuliza na kasha kunitazama usoni.
Sikuwa na nguvu za kukimbia, ganzi ilishika mwili mzima. Huyu mwanamke alikuwa ananijua vyema kuliko nilivyodhani!! Na ilikuwa kama bahati tu hakuweza kunichoma popote pale.
“Naiwa Jojina usiniite mama lao!!” akajitambulisha jina lake hatimaye.
Nisingekuwa na lolote la kujitetea, nisingeweza kulaghai tena. Jojina alikuwa ananitambua vyema!!
Nikajaribu kumwomba radhi, akanielewa huku akinisisitiza ni vyema niishi kwa tahadhari kubwa.
“Sasa huyu Anitha, sina hata la kukusaidia lakini kama maneno ya yule chizi yapo sahihi basi kile kitabia cha Anti Ezekiel kinaweza kuwa kimeondoka naye.” Alinieleza huku akijaribu kutabasamu.
“Chizi mwenyewe anayesema hivyo yupo wapi…..” nikaamua kuuliza.
“Mh!! Kwa kweli ni miezi mingi sana imepita tangu nimwone. Nitakudanganya nikikwambia kuwa yupo Iringa hii. Kuna watu wanadai alionekana Dar es salaam, sasa sijui kama ni kweli ama la!!” alinijibu baada ya kufikiria kwa sekunde kadhaa.
“Na uliwahi kumtambua hata jina lake kwani?”
“Alikuwa na majina mengi sana mara wengine wamwite mganga wa jadi mstaafu, wengine walimuita Zuzu…lakini kuna waliodai kumfahamu na wakasema jina lake halisi ni Kindole, wakamfupisha na kumwita Kindo!!!”
“Nini?” nilihamanika nisiamini kile ninachokisikia. Yaani Kindo nimjuaye ama Kindo mwingine, Kindo alikuwa kichaa? Mbona alikuwa timamu jijini Dar es salaam. Nilijiuliza katika nafsi yangu!!
“Na kama ni kweli alikufa basi ndo yaleyale ya Anti Ezekiel labda maana maneno huumba!!!” aligandamiza tena yule mama na kuzidi kunichanganya!!!

**JIFUNZE!! SIRI ni siri iwapo ni ya kwako wewe na moyo wako!! Usijidanganye kumshirikisha rafiki yako na kumwambia akutunzie siri hiyo. Wanadamu hubadilika, leo wamuona mwema na kumkabidhi siri zako kesho anazifanya siri hizo fimbo ya kukuchapia!!!

Nilishangazwa na majibu ya Jojina yaani ni kama alikuwa akijaribu kuniimbia mashairi ambayo yameunganika vyema yakijali uzani wa vina na masivina lakini yakikosa mstari wa mwisho kila mara.
Mara anieleze juu ya michigani, lakini mwishowe hiyo Michigani yenyewe haipo tena.
Anazungumzia mkasa wa Anti Ezekiel ikiwa hamjui wala hana uhakika juu ya kiumbe cha kuitwa jina hilo.
Huyohoyo anadai kuwa Kindo ambaye ana wazimu alikuwa akisema sana juu ya Anti Ezekiel lakini mwishowe huyo Kindo hayupo tena Iringa na mbaya zaidi hajulikani alipo nan i tetesi tu kuwa alioneka Dar mara ya mwisho.

Kama kweli ni huyo kindo Aliyeonekana dar basi kwa namna yoyote tunahangaisha vichwa kumzungumzia mtu aliyeuwawa siku kadhaa nyuma baada ya kuchukuliwa na watu wasiojulikana.
Hawa watu wasiojulikana nd’o hao hao waliomuua Ezekiel, ndo haohao waliomchukua mke wangu na hawa hawa wamenizushia kuwa nimekufa na wamemweka mama yangu katika wakati mgumu kupindukia.
Hawa watu nd’o wanadai kuwa nitamfuata Anitha, na nitamfuata mama Eva.
Hawa watu ni akina nani!!!
Swali hilo likanitia kati kati ya hasira na mtafaruku wa kimawazo. Hawa watu walikuwa wamenizidi ujanja na tayari walishacheza na akili ya watu wa kuaminika serikalini ili nisiaminiwe popote pale!!

“Kwa hiyo dada Jojina….huyo Kindo wewe uliwahi kumuona ama!!”
“Nd’o maanake, hapa Iringa nani ambaye hakumjua na wazimu wake yule bwana. Zaidi lilikuwa skendo lake la Michigan…….”
“Skendo la Michigani?? Kiaje skendo la Michigani, yaani unanichanganya kweli dadangu hujui tu!!”
“Nakuchanganya na kipi tena, nakujibu kila unachouliza kadri ya uwezo wangu!!….na ninajitahidi zaidi ili ikiwezekana leo nyumba yangu iwe na mgeni.” Akazungumza kwa madaha kisha akanitazama kwa jicho fulani nikaelewa maana yake…sikutaka kuyakuza mambo zaidi nikamuuliza kwa utulivu nini kilijiri huko Michigani.
“Wanaomfahamu huyo wa kuitwa Kindo wanadai kuwa alichanganyikiwa baada tu ya kutoka Michigani.”
Akanitazama kisha aakaendelea, “Kindo alikuwa muajiriwa huko Michigani, kilichomtoa huko hakijulikani lakini baada tu ya kutoka huko siku kadhaa mbele Kindo ana wazimu!! Lakini usiniulize maswali mengi maana mimi sijui lolote nazisikia simulizi hizi nikiwa nauza bajia zangu na sambusa za nyama.” Alinijibu kizembe, ni kama alikuwa amechoshwa na maswali.

Majira ya mchahna tulikuwa tukitembea kwa tahadhari, tukakipita chuo cha Tumaini na hapo akanieleza kuwa mahali niliposimama ndipo Michigani.
Nilikata tamaa kwa sababu hapakuwa na sehemu ya kuanzia, ni kama makumbusho tu ya kale ambayo yamevunjwa na kusahaulika zamani sana. Hapakuwa na ulinzi wala mtu yeyote aliyekuwa akijihangaisha na eneo lile. Na hakuna aliyehangaika kutuuliza ni kitu gani tulikuwa tunatafuta.
Sikuwa na la zaidi, nikaondoka na mama yule hadi nyumbani kwake, huko nia ikiwa moja tu kujua zaidi kuhusu Michigani.
Tulipofika alinionyesha picha za Michigani hiyo ya zamani ambayo iliteketea yote miezi mingi nyuma!!
Ilikuwa sehemu ya kuvutia, palikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, hoteli ya kifahari iliyoitwa Michigani na bustani ya kisasa.
“Siku za sikukuu palikuwa panajaa sana hapa, sio unajua mambo ya watoto na wazazi wao??” aliniambia wakati tukiingalia picha ya Michigani.
“Ungeweza kuona maeneo mengi lakini si kila eneo tuliruhusiwa kupiga picha kirahisi, hata hii yenyewe ni basi tu niliipata kibahati. Watu wana mambo, visheria vya ajabu ajabu kama nini!!!” alilalamika. Lakini akiona ufahari na kisha kujisifu kuwa yeye ni mama wa mjini alifanikiwa ajuavyo.
“Wewe uliipataje sasa.”
Kabla ya kujibu swali hili akacheka.
Kama nilivyokueleza awali juu yam zee wangu kuchukuliwa na skendo hili la kuichoma Michigani jambo ambalo hata naenda kaburini nitalikana kwa nguvu zote. Kweli nilibahatika kuingia katika mahusiano na bwana mmoja mtu mkubwa kidogo pale Michigani, basi nikawa nahudumiwa kila kitu kwa bili yake, hakuwahi kunieleza kwa nini picha hazipigwi hata zile za kumbukumbu!! Mzee wangu akazinasa hizi habari, akaniweka kitako kunikanya kuwa Michigani kuna mazingaombwe yanayofanana na ushirikina. Kwani kila sikukuu ifikapo basi kuna watoto zaidi ya watano wanapotea na wasionekane tena. Baba alisisitiza kuwa anaifahamu vyema michigani kuwa watu wake si wazuri, akanisihi nijiweke mbali nisije kupoteza mtoto wangu kwa hila za wanadamu, mtoto huyo alikuwa akiitwa Justin na nilimzaa bahati mbaya tuseme. Baba yake alikimbia, maneno ya baba yakaja na ukweli ndani yake lakini nilikuwa nimechelewa na wala sikutaka kuamini hata kidogo kuwa mwanangu amepotea eti kisa Michigani, japo alipotea siku ya sikukuu pia.
Tulizunguka kwa waganga wa kienyeji lakini hakuna hata mmoja aliyesema ukweli wote walitulaghai. Baba alibaki kusema kichinichini kuwa Michigani hiyo Michigani!! Hakuwa na maelezo ya kutosha labda na yeye hakujua vyema kama mimi nilivyobisha bila kujua neon lolote hadi leo nipo ndotoni.
Nikiwa na mapenzi tele na Dulla huyo mtu mzito wa Michigani nikafikia hatua ya kumweleza hisia za mzee wangu juu ya mtoto wangu kupotea. Dulla akapinga na kusema kuwa baba anazeeka vibaya. Name nikamuunga mkono. Hiyo siku tulifurahi sana, akiwa kama mpenzi akanitembeza maeneo kadha wa kadha akiahidi pia kuwa atakuja nyumbani kujitambulisha kwa baba ili anioe moja kwa moja!! Kwa kuhitimisha furaha yetu akanipa picha hii inayoonyesha maeneo kadhaa ya Michigani.
Baada ya juma moja Michigani ikaungua moto!!!
Siku tatu baadaye baba yangu akaanza kusakwa, akapatikana na alivyopotezwa……alivyopotezwa!!!! Basi tu Mungu anajua” kufikia hapa Jojina akaanza kutokwa na machozi, ilikuwa ni kumbukumbu mbaya sana kwake, lakini ikiwa ni kumbukumbu yenye mafumbo makali ndani yake bila yeye wala mimi kujua majibu!!
“Kwa nini sasa Dulla hakukusaidia katika kumsaidia mzee wako asiende jela.” Nilimuuliza.
“Dulla…Dulla hakuonekana tena, masikini yaani wanadai kuwa hakuna hata mtu mmoja aliyekufa lakini nina mashaka kuwa huenda Dulla alikufa.”
“Kwanini una mashaka hayo sasa!!!”
“Kwa sababu sijawahi kumuona tena na kuna jamaa zake wa karibu walinihakikishai kuwa Dulla alikufa. Na hapo nikaamua kubadilika na kuwa mama lao. Kila biashara nafanya.” Alimaliza kwa mbwembwe huku akilazimisha tabasamu.
Maneno ya mama lao Jojina yalizidi kunivuruga, badala ya mwanga likawa giza tena. Mkasa mmoja haujaisha inaongezeka mikasa mingine lukuki.
Mtoto wa Jojina kupotea, kisha Michigani kuteketea, baba yake Jojina kupotezwa katika uso wa dunia katika namna ya kustaajabisha!!
Michigani ya kwenye picha haikuwepo tena duniani!!!
Kuna nini Michigani?
Swali halikupata jibu!!

“Dulla wangu jamani eeeh!!” alianza kulia chinichini huku akiwa ameikumbatia picha fulani ambayo hakuwa amenionyesha kabla. Nilimbembeleza taratibu, hadi alipoitua ile picha kisha tukahamia katika mazungumzo ya hapa na pale, akanichombeza name nikamchombeza lakini hapakuwa na muda wa kuendelea mbele zaidi. Akasikika muuza magazeti.
“Wacha wee hebu ngoja nikakwapua gazeti, halafu leo kachelewesha huyo. Kuna hadithi nafuatilia magazetini, nakuja Sam usiwe mpweke.” Alinisihi kisha akatoka nje.
Alipotoka nikaupangusa mdomo wangu, sikuwa nimefurahia kumbusu mdomoni, lakini ilinilazimu kufanya vile maana nilihitaji kujua mengi sana kutoka kwa mama lao. Nilikubali kumbusu lakini moyoni nikijiapiza kuwa sitaendelea zaidi japokuwa baridi la Iringa lilitia hamasa kuendelea zaidi.
Nikajiandaa kumkabili akirejea kwa maneno ya kumhadaa ili niondoke pale kwake, nikaupanga uongo nao ukapangika.
Alipoingia badala ya kuniparamia pale kitandani, akanitazama huku akistaajabu.
“Sam!!” aliniita, nikageuka kumtazama, hakuwa kimahaba tena.
“Mkeo….mh!! mkeo anajua ulipo?” aliniuliza, nikaketi kitako niweze kujua nini kinaendelea.
“Kwanini?” nilimuuliza kwa kiherehere nikitaka kujua kulikoni.
“Si ndio huyu Edna ama …mama Eva si nd’o hivyo!!” alizidi kunivuruga.
Uvumilivu ukanishinda nikasimama na kuangalia anachokisoma.
Ilikuwa picha ya mke wangu Edna ama mama Eva kama nilivyomzoea. Sura yake kama niijuavyo ilikuwa inatabasamu!!!
Chini ya ile picha iliandikwa kitu ambacho nilitumia sekunde nyingi kurudia kukisoma.
MAREHEMU EDNA KIMARO!!
Nguvu zikaniishia, nikajitahidi kujizuia lakini ikashindikana na hapo nikaanza kuona giza ..
Kisha…..kisha …..nikaona kitu cha ajabu sana nikatami kukitazama zaidi lakini sikuweza kiza kikazidi kutanda kisha kimyaaa!!!!

Baadaye nilijikuta katika mikono ya uvuguvugu kiza kinene, nikajigeuza huku na huku nikaisikia sauti ikikwaruzakwaruza huku ikiliita jina langu!!
Nilijaribu kuvuta kumbukumbu zaidi kuwa ni wapi nipo.
“Sam!!” sauti iliita tena!! Sasa haikuwa ikikwaruza, ilikuwa sauti ya mama lao. Name nilikuwa nimekumbatiwa vyema na ule uvuguvugu ulitoka kwake.
Feni ilikuwa ikinipuliza!!
Mama lao akanyanyuka na kuwasha taa.
Akanieleza kuwa nilipoteza fahamu!! Kisha bila kunipa nafasi ya kusema chochote akanisihi kuwa sitakiwi kuamini kila ninachokiona wakati wa matatizo.
“Sam sidhani kama mkeo anaweza kulemazwa akili kiasi hicho, yaani hapana kabisa..” alishindwa kuendelea akanirushia gazeti.
Nikaisoma ile habari.
Eti mke wangu alikuwa katika msafara wa kusafirisha maiti yangu kuelekea mjini Morogoro, walipofika chalinze wakapata ajali mbaya ambapo maiti ilipotelea katika korongo na mke wangu akiumia vibaya kabla ya kupoteza uhai!!
Mimi ni mwandishi, nikamshangaa mwandishi mwenzangu aliyelishwa sumu na watu wabaya hadi akafikia kuunda makala ile mbovu inayoenda kupotosha akili za watanzania wote.
Nilitamani walau kumfahamu jina lakini nikakuta makala ile imeitwa MAKALA MAALUMU ikiwa imeandikwa na MWANDISHI WETU
Upuuzi kabisa!!!

Picha ya mke wangu ikanifanya niingiwe hasira maradufu nan i wapi pa kuzishusha hasira hizi.
Nikaamua kumpigia simu mama yangu mzazi ili nijue ni nini kinatokea. Niliomba sana awe peke yake ili aweze kuzungumza name vyema.
Hakika alikuwa peke yake!!
“Sam weee!! Sam mwanangu, nilipokuzaa sikukuzaa uende kuyafanya haya wanayokuandikia. Najua kuwa wanajaribu tu kukuchafua.
Nitakuwa upande wako!! Si nilikuzaa kwa upasuaji na fomu ikasainiwa kufa ama kupona. Basi ni hivyo hivyo nipo nawe katika kufa ama kupona.
Eti watu wa dar es saalam wanadai waliuaga mwili wako, wafanyakazi wenzako waliuaga mwili wako. Tena wananipigia simu kwa kasi kweli wakinipa pole juu ya kifo chako.
Nasemaje Sam, watakukana wote lakini mimi nitakusimamia hadi mwisho..” hapa mama akasita kisha akacheka kidogo!! Na akamalizia na kauli moja ya kishujaa lakini kama anayesanifu.
“Eti maiti imepoteaaaa, walijua tu kuwa mama nd’o pekee awezaye kumtambua mwanaye hata asipokuwa na kichwa!! Kama wamemkamata akili huyo Edna wako ni huyo huyo, kama na baba yako ulevi wake unamsahaulisha magumu tuliyopitia ni yeye si mimi (kisha Akatukana kwa kikabila chetu)” nikajua kuwa mama amakasirika katika kiwango cha mwisho!!! Haikuwa kawaida yake kutokwa na matusi.
Nilishusha pumzi zangu na kupata ahueni, kuwa mama yangu habadilishwi mawazo hata kidogo.
Jojina alikuwa amejikita katika jiko la gesi akiandaa chai, na nilipomaliza kuzungumza na mama na yeye alikuwa ameketi kitandani akiwa na kikombe cha chai.
“Sam, umezungukwa na watu wabaya tena wenye nguvu sana. Yaani mtu anaunda ajali kama hii maksudi anaharibu gari, anachonga jeneza ilimradi tu kukuchafua na kuunda ukweli usiokuwepo!! Wanadamu wabaya sana, na ili ufanikiwe lazima haya mambo yaende hatua kwa hatua vinginevyoo!!!!!” aliishia hapo akanipatia chai, nikachemsha tumbo!!

Nikiwa katika kunywa chai na kumkumbuka mke wangu kipenzi, nikakumbwa na kumbukumbu juu yay ale mazingira ambayo alipotea!! Nilipokumbuka kule dar es salaam nikakumbuka kuwa wakati naona giza kuna kitu niliona….hakika kuna kitu nilikiona.
“Mama lao, kuna kitu nilikiona wakati nazimia kama usemavyo…yaani kuna kitu niliona jamanii..” nilimweleza huku nikikifinyafinya kichwa changu kutafuta kumbukumbu.
Aliniambia kuwa huenda ni katika usingizi mzito tu wa kuzimia lakini nilikana, kipo kitu cha msingi niliona waziwazi!!!
Nikatoka kitandani na kumwomba Mama lao anisimamishe sehemu niliyokuwa mara ya mwisho kabla ya kuzimia. Akafanya vile huku akicheka kimadaha, kanga yake moja maungoni.
Nilipokuwa pale nikamwomba anielekeze pia namna ambavyo nilianguka!! Alifanya kila nilichotaka.
Nikaenda hadi chini na hapo nikajikuta nikionana na kitu cha kustaajabisha na kutisha kwa wakati ule.

Japokuwa ilikuwa picha lakini ilitisha kuitazama, niliisogelea huku nikitetemeka.
Nikaiona picha ile inayotabasamu kama ambayo inanikebehi. Nikaishika huku nikitetemeka.
“Jojina huyu ni nani kwa jina?” nilimuuliza huku nikiwa nimeipakata ile picha katika viganja vya mikono yangu!!
Badala ya kunijibu alicheka kidogo. Nikashangaa maana picha ile ilinitisha mimi lakini yeye hakuiogopa.
“Jojina usicheke huyu ni nani huyu?”
“Anaitwa Dulla, nimwite hayati Dulla, mwanaume wangu nimpendaye akafa kabla…”
Sikumwacha amalize nikayaingilia maongezi.
”Jojina huyu hajafa, huyu na mwenzake mzungu walimteka mke wangu…niamini mama lao..huyu hajafa. Dulla si mtu mzuri niamini sijamfananisha hata kidogo. Dulaa kama ni kweli anaitwa hivyo, kwa jicho langu nilimwona akimchukua mke wangu! Kuna kitu Mama lao..” sasa ikawa zamu yake kuchanganyikiwa. Macho yalimtoka pima ……….
Tukabaki kutazamana.

**JIFUNZE. Mwenye pesa si mwenzako, haki haipo katika dunia hii. Mwenye pesa anayumbisha sheria, na jela anaenda maskini. Wanasema mwenye nguvu MPISHE……usiisake haki dhidi ya mwenye pesa maana haki yako itageuzwa HARAMU.
FUNIKA KOMBE MWANAHARAMU APITE!! Ile kanuni ya mnyonge mnyongeni ila haki yake mpeni!! Haina nguvu tena mbele ya pesa!!

**SAM ndani ya Iringa, picha ya mtekaji wa mkewe anaikuta kwa mama lao. Inasadikika kuwa DULLA amekufa kitambo lakini Sam anauhakika amemuona siku kadhaa nyuma.
**BADO NI UTATA!!!

ITAENDELEA

Leave a Comment