Najisikia Kuua Tena Sehemu ya Pili
NEW AUDIO

Ep 02: Najisikia Kuua Tena

Najisikia Kuua Tena Sehemu ya Pili

IMEANDIKWA NA : BEN R. MTOBWA


Simulizi : Najisikia Kuua Tena

Sehemu ya Pili (2)

KOMBORA hakujibu mara moja. Yeye alimshakia zaidi huyu mtunzi, Bazile. Sauti katika simu ile haikuwa ya kike. Wala hakuona kama mwanamke huyu mlevi wa gongo angekuwa na haja ya kumwandaa na kumpigia simu polisi kama hadithi ile ya Simu ya Kifo.

Hata hivyo, bado aliona umuhimu wa kuwapata wote wawili mapema iwezekanavyo. Yawezekana kuwa mtunzi yule hahusiki. Yawezekana vilevile kuwa yeyote kati yao hahusiki! Aliwaza ghafla kwa hofu. Jambo ambalo litaongeza uzito katika jukumu hili.

Kwa kawaida kesi hii isingemjia yeye Kombora au kikosi chake moja kwa moja. Ingekuwa kesi ya kushughulikiwa na vituo vya kawaida vya polisi. Kikosi hiki cha kumi na mbili kilikuwa chini ya idara maalumu inayoshughulikia masuala makubwa ya mauaji katika jiji hili. Kesi ambayo ilielekea kuwashinda polisi wa kawaida au yenye masuala yanayokanganya au hujuma za kiuchumi na kisiasa ndiyo iliyokuwa ikiletwa hapa.

Hii haikuwa kubwa kiasi hicho. Lakini alikuwa ameipokea na kuiomba toka majuzi alipopata simu ile inayodai mauaji. Alihisi muuaji huyo anamhitaji yeye. Ndipo akawaarifu polisi kumletea kesi yoyote ya mauaji ambayo ingetokea katika saa ishirini na nne.

Hata hivyo, hakuwa amemgusia yeyote juu ya simu ile. Wala hakuwa tayari kumgusia Sajini Abdala suala hilo. Hivyo alimwambia kwa sauti ya amri akisema, “Vizuri sajini. Nawahitaji haraka hawa wawili. Machozi na huyu Bazile. Nafahamu wajua lipi utafanya ili wapatikane kabla ya kesho.”

“Bila shaka afande.”


ULIKUWA ni usiku mbaya mno kwa walevi wa pombe haramu, hasa wanawake. Kote kulikofahamika au kushukiwa kuwa maskani ya walevi hao kulizingirwa na vijana wa polisi na JKT wenye kiu kubwa ya kuupima ujana wao. Wengi walikamatwa na kusukwasukwa kwa makofi na mabuti ya vijana wa polisi. Waliochukuliwa moja kwa moja walichukuliwa, walionusurika walinusurika. Mamia waliyosalia walichujwa hata wakasalia kina Machozi arobaini. Ni hao waliofikishwa kituo cha polisi. Huko pia walichekechwa hadi waliposalia watatu waliofanana kwa sura na tabia. Ni katika watatu hao alipopatikana Machozi aliyetakiwa.

“Wewe unasema umekamatwa Luhanga sio?”

“Ndiyo.”

“Ulikuwa ukifanya nini?”

“Kwani vijana wako walikwambia nini bwana askari? Nilikuwa nikinywa na kustarehe. Sina jambo lingine la kufanya.”

“Hujui kwamba gongo ni haramu kidini na kisheria?”

“Mangapi ni haramu na yanafanywa? Siachi gongo kwa taarifa yako! Bia haitengenezwi kwa ajili yangu wala watu wa aina yangu!”
Sajini Abdala akamkazia macho. Pamoja na uzoefu wake wa kutazamana na wahalifu wa kila aina, lakini macho ya huyu yalimtisha. Yalikuwa ya kila hali ya ulevi na wazimu. Yalitangaza waziwazi kuwa ‘lolote laweza kutokea’. Baada ya misukosuko yote ya vijana wa polisi ambayo iliacha ushahidi wa jeraha dogo katika mdomo wa mama huyo na ngeu katika paji lake la uso, macho hayo hayakuonyesha athari yoyote. Yalikuwa imara yakimtazama sajini huyo na askari wote kwa dharau, kebehi na kutojali.

“Unamfahamu Kondokondo Kitenge?” Abdala alifoka ghafla.

“Mara ngapi nikwambie kwamba namfahamu?” Machozi alirudisha.

“Ni nani wako?”

“Mara ngapi nikwambie kwamba ni baba watoto wangu?”

Ni majibu hayo aliyokuwa kayatoa tangu aanze kuhojiwa suala hilo. Kilichomshangaza Abdala ni jinsi mama huyo alivyozungumza kwa uhakika kama aliyeamini anachokizungumza.

“Sikia wewe mwanamke,” alinguruma Abdala. “Uko hapa si kwa mzaha ila ni suala gumu mno kwako. Hivyo nataka uache majibu ya kilevi. Unijibu kikamilifu. Sawa? Kwa taarifa yako, Kondokondo Kitenge amekufa. Ameuawa usiku wa jana!” Abdala alisita akiutazama uso wa Machozi kuona vipi ujumbe huo ungemwingia.

Kama alitarajia kuona mshangao au hofu katika uso huo, lolote kati ya hayo halikutokea. Machozi alikuwa vilevile kama mama aliyearifiwa kifo cha panya au kifaranga. “Umesema kweli askari?” Alihoji polepole. “Amekufa kweli?”

“Amekufa. Ameuawa usiku wa jana. Waweza kutuambia ni nani kamuua?”

Ndipo kitu cha kutisha kikatokea katika uso wa Machozi. Tabasamu. Lilikuwa la kutisha kuliko tabasamu lolte la mwanadamu. Abdala alililinganisha na lile la sokwe alilowahi kuliona katika hifadhi za wanyama. Baada ya tabasamu hilo Machozi aliropoka kwa sauti ya juu.

“Amekufa sio! Ameuawa….sikupata kupokea habari njema kuliko hiyo katika maisha yangu bwana polisi. .. ndiyo, namjua aliyemuua. Ni mimi mwenyewe. Nimemuua kwa mkono huu!” Akaupunga mkono wake wa kulia angani.

Sajini Abdala akaduwaa. Akawageukia wenzake ambao walikuwa katika mshangao pia. Hakuna aliyetarajia jibu rahisi kama hilo. Hivyo, badala ya kulikubali kama walivyotaka, wakajikuta wakilitilia shaka.

“Nadhani dada yangu hujui unalosema. Huna habari kuwa suala hili linaweza kukufanya ule kitanzi?” alisema askari mmoja.

“Najua! Na nitaingia kitanzini kwa furaha maadamu nimemuua!”

“Ulimuua lini?”

“Jana usiku.”

“Saa ngapi?”

“Sikumbuki vizuri, sijawahi kuwa na saa.”

“Ulitumia silaha gani?”

“Kisu!”

Askari wakatazamana tena. Kisha walibadili mtindo na kuanza kumuuliza mfululizo. Walishangaa kukuta mama huyo akisimama imara akiendelea kudai: “Nimemuua… Nimemuua.”

Taarifa hiyo ilipopelekwa kwa Inspekta Kombora nusura imtie wazimu. Alimsikiliza Sajini Abdala kwa makini kisha akakuna kichwa huku kainamia meza. Kisha alikuna macho akitazama dari. Aliporudisha macho hayo mbele yake yalikuwa yamejaa maswali.

“Unadhani anasema ukweli sajini?”

“Nani, mwanamke huyo sio? Hilo ndilo tatizo lenyewe afande. Ni vigumu kukataa au kukubali kuwa anasema ukweli. Mwenyewe kang’ang’ania hivyo.”

“Achana na maneno ya mlevi,” alidai Kombora. “Kinachotakiwa ni ukweli. Waruhusu vijana maalumu kwa shughuli za aina hiyo wafanye kazi yao hadi watakapohakikisha kuwa kama hasemi, anautapika ukweli huo. Sawa?”

“Sawa, afande.”

Kilichomfanya Kombora achanganyikiwe ni hiyo taarifa nyingine aliyoipata kwa sajini aliyepewa jukumu la kumpata Bazile Ramadhani, mtunzi ambaye Kombora alimshuku zaidi katika mauaji haya. Sajini huyo alirejesha majibu kwa ‘radio call’ ambayo yalimtisha Kombora.

Kwamba alipoenda Barabara ya Pugu kwenye kiwanda cha TEGRY ambako Bazile alikuwa akifanya kazi, aliarifiwa na wakubwa wake kuwa alikuwa hajafika kazini hapo siku mbili nzima. Baada ya kuhangaika sana, walimpata msichana mmoja ambaye alisemekana kuwa alikuwa rafiki wa Bazile.

Ni huyo aliyewaongoza hadi Kigamboni ambako Bazile alipanga chumba. Huko pia walikuta chumba kitupu. Jirani zake walidai kuwa ‘ametoweka ‘ tangu majuzi. Hakuna aliyefahamu alikoenda. Hakuna aliyeagwa.

Ni hilo lililomtia Kombora mashaka zaidi. Aweza kuwa popote. Aweza kuua tena wakati wowote. Hivyo, alimwamuru sajini huyo kuendelea na upelelezi juu ya tabia na mwenendo wa mtu huyo.
Maongezi hayo Kombora aliyasikiza moja kwa moja katika ‘radio call’ hiyo.

“Bi nani sijui mwenzangu.”

“Mimi sio? Naitwa Ashura.”

“Ndiyo, bi Ashura. Waweza kutusaidiaje ili kumpata mapema huyu rafiki yako? Aweza kuwa kaenda wapi?”

“Kwanza ningeomba nisieleweke moja kwa moja mimi ni mpenzi wake Bazile, bwana askari. Niwie radhi kwa hilo lakini ndio ukweli wenyewe. Niliondokea kumpenda lakini hapendeki. Hana muda wa mapenzi. Na hata maongezi hajui. Ukitaka kumsikia akizungumza lazima uongelee vitabu. Mimi mambo ya vitabu siyajui. Hivyo nilikuwa kama najilazimisha kwake tu. Mara kwa mara muwapo pamoja utamkuta kakusahau kabisa yuko maili elfu moja katika dunia ya peke yake. Hivyo kuhusu swali lako siwezi kulijibu. Hakuwahi kuniamini katika masuala yoyote ya maisha yake isipokuwa ya vitabu tu.”

“Ahsante sana. sasa dada Ashura, unadhani Bazile aweza kuua mtu?” kicheko laini cha msichana yule kikamfikia Kombora.

“Kuua! Bazile! Siamini. Kwa kuwa anaandika vitabu vya mauaji siyo? Kwa kweli sijapata kuona mtu mwoga au mstaarabu kama yeye. Hajapata kumtukana mtu, hajapata kumpiga mtu kofi, ataanzaje kuua? Ebu bwana askari, kweli mnamtafuta kwa nini? Eti mnamshuku kaua mtu?
“Kuua au kuuawa. Hajaonekana siku mbili. Unadhani habari hiyo ni njema? Chumbani kwake kila kitu kimo, isipokuwa yeye tu.”

“Kweli kabisa!”

Baba mwenye nyumba naye alikuwa na yake.

“Kuua siyo? Japo ni mtulivu, mimi nadhani anaweza kabisa. Mtoto hakai nje na wenzake kuongea. Kutwa nzima chumbani. Ukimuuliza nini anafanya atadai anasoma. Ukichungulia utamwona kainamia meza anaandika. Hachoki kuandika. Nadhani alikuwa na aina fulani ya wazimu. Yaweza kumtuma kufanya lolote.”

Hayo ndiyo yaliyokisumbua kichwa cha Kombora. Kafa mtu mmoja. Washukiwa wawili ambao hawafahamiani wala kuishi pamoja. Mmoja anadai kuwa kaua, wa pili haonekani aliko. Angewezaje kulipeleka mbele suala hilo likiwa katika utatanishi mzito kama huo?

La muhimu lilikua kupatikana huyo Bazile. Akiwa katika milki ya polisi, Kombora angeweza kufarijika zaidi na kufahamu namna ya kutatua msongamano huo. Hakujua vipi na lini Bazile angeingia mkononi.

Simu ikalia. Kombora akainyakua na kuiweka sikioni akinguruma. “Inspekta Kombora hapa.”

“Kombora! Rafiki yangu Kombora siyo?”

Haikuwa sauti ngeni masikioni mwa Kombora. Ilikuwa ileile ambayo alihitaji kumpata mwenyewe. Naam, sauti ileile ambayo sasa, Kombora hakuitarajia, akishuku mwenyewe tayari yu ahera. Hakujua kama ilimpasa kuisikiliza au la. Hakujua ajibu nini zaidi.

Maadamu chombo cha kusikilizia bado kilikuwa sikioni, aliendelea kumsikiliza.

“Mbona kimya rafiki yangu Inspekta? Upo? Sikia ndugu yangu najisikia kuua mtu mwingine. Waweza kunisaidia?”

“Wewe! Ni wewe Bazile Ramadhani?” aliuliza Kombora kiasi akitetemeka.

“Umelipataje jina langu mapema hivyo Inspekta? Kumbe u hodari kiasi hicho? Ndiyo ni mimi. Kwa heri Inspekta.”

“Sikiliza….” Tayari simu ilikatwa.

Kombora aliduwaa nusu dakika. Katika nusu nyingine alikuwa alikuwa akimngurumia opereta kuchunguza ilikotoka simu hiyo.

Jibu halikumfariji. Simu ilipigwa kutoka katika vibanda vya simu vilivyoko huko Forodhani. Simu ya wazi ambayo mtu yeyote wakati wowote anaweza kupiga.

Hata hivyo hakusita kutuma makachero hao. Hakutokea yeyote aliyekuwa tayari kueleza sura na umbile la mtu au watu walomtangulia kutumia simu. Pamoja na watu wote waliokuwa hapo kuonyeshwa picha ya Bazile, jibu la haja halikupatikana.


IWAPO Kombora alikuwa akisubiri habari za kifo kimoja, basi alikosea sana. Usiku huo walikufa watu wawili. Wa kwanza alikuwa Fambo Wamangi.

Kama ilivyo kawaida ya kifo, kilimtokea bila kutarajia. Kutwa nzima alikuwa ameshinda katika ofisi yake alikuwa akiendelea na shughl zake za kila siku. Alikuwa meneja-masilahi katika kampuni ya Enterprise.

Kampuni hii ilishughulikia biashara za aina zote na mataifa mbalimbali. Wote waliomwona siku hiyo walishangazwa na jinsi alivyokuwa mchangamfu na mcheshi zaidi ya kawaida yake.

Baada ya kazi, alirejea nyumbani kwake ambapo alicheza na wanawe, akacheka na mkewe na kutaniana sana na jirani zake. Saa mbili za usiku alitoka na mmoja wa jirani hao kwenda baa ya jirani ambapo walipata chupa mbili mbili zilizomfanya Wamangi azidi kuchangamka. Kisha walirejea nyumbani. Wamangi akakiendea kitanda ambako alikuwa ‘mtundu’ kama siku zile za ujana wao, jambo ambalo lilimfurahisha sana mama watoto wake. Usingizi uliwakuta katika hali hiyo ukawachukua na kuwahamisha hadi katika milki nyingine, ya ndoto na starehe.

“Nilipoamka nilijikuta bafuni,” yalikuwa maelezo ya mama huyo kesho yake. “Nilikuwa nimefungwa kamba mkononi na kitambaa mdomoni. Nikajitahidi hata kamba hizo zikafunguka. Nikarejea chumbani ambako niliyoyakuta yalikuwa hayatazamiki. Mume wangu mpenzi alikuwa kalala chali kitandani, uchi kama alivyolala usiku wa jana, mwili wake mzima ukiwa umelowa damu nzito ambayo ilikuwa ikiendelea kutiririka kutoka katika jeraha baya mno la kisu au sime lililokuwa wazi kifuani. Sikuweza kutazama mara mbili. Sikuweza kupiga kelele. Nadhani nilianguka na kuzirai kwani nilipopata fahamu tena nyumba nzima ilijaa watu, askari na jirani ambao walikuwa wakinihudumia.”

Kifo hicho ni katika Mtaa wa India, jengo la Abdulkar lenye ghorofa nne. Marehemu alikuwa akiishi katika ghorofa hiyo ya nne pamoja na jirani ambao ni familia mbili za Kiafrika na tano za Kihindi. Ni mmoja kati ya jirani hao aliyeipigia simu polisi alfajiri baada ya kusikia watoto watatu wa marehemu wakilia kwa nguvu bila msaada wowote wa wazazi wao. Alipochungulia na kuwaona wazazi katika hali hiyo, alidhani wote walikuwa wamekufa, hivyo aliiambia polisi, “Bana na bibi ake yote kafa.”

Kifo cha pili kilikuwa kimetokea kilomita kadha wa kadhaa nje ya wilaya hii ya Ilala. Hicho kilitokea huko Kinondoni Mkwajuni. Marehemu kama bwana Jugeni Kawamba, kama Wamangi kutwa nzima ilikuwa ya kawaida kwake.

Kwa muda wa miezi kadhaa, Kawamba hakuwa na kazi. Hivi alikuwa kamrejesha mama watoto wake pamoja na wanawe wote kwao katika vijiji vya Wilaya ya Mbulu mkoani Arusha, ili aweze kuyakabili maisha pindi akiendelea na msako wa kutafuta kazi.

Akiwa mtu aliyepitia madaraka makubwa, yenye marupurupu ya kutosha, maisha ya kuishiwa yalimtatiza mno. Ingawa hakuwa kaishiwa kiasi cha kukosa pesa ya matumizi, lakini kule kuona akiba yake ya benki ikielekea kumezwa kabisa bila matumaini ya kuongeza chochote juu ya akiba hiyo siku za usoni kulimtia hofu.

Hivyo alikata makundi ya urafiki wa matumizi na kuwa mtu wa kutulia nyumbani akijisomea.

Usiku huo usingizi ulimtoka kabisa. Japo alijituliza kitandani macho kayafunga na kujaribu kubembeleza usingizi, haukukubali kabisa. Mawazo yalikuwa yakimrejesha kuitazama hali yake kiuchumi inakoelekea. Haikuridhisha. Mara akaanza kuijutia safari yake ya majuzi aliposafiri kwa ndege kwenda na kurudi Zanzibar ambako aliitwa kwenda kufanya mahojiano ya ijara. Labda asingesafiri kwa ndege, meli ingetosha! Aliwaza.
Mara alihisi kuinamiwa na dude refu jeusi na alipojaribu kufumbua macho yalizibwa kwa mkono wenye nguvu kama chuma. Juhudi zake zote za kuutoa mkono huo hazikufua dafu. Alipojaribu kurusha teke lilidakwa kwa mkono mwingine. Dakka hiyohiyo jisu kali lilipenya kifuani kwake kwa maumivu makali. Hakuwahi kupiga kelele, kwani mkono uliokuwa usoni ulihamia mdomoni kuuziba. Pigo la pili lilimmaliza. La tatu hakulisikia kabisa.

Akiwa mtu anayeishi peke yake katika nyumba hiyo ambayo hata alikuwa hajamaliza mkopo wake aliopewa na THB, ilichukua muda kabla maiti yake haijagunduliwa. Ni kijana muuza magazeti ambaye aliigundua. Kijana huyo akiwa na mkataba wa kumletea magazeti kila siku, asubuhi hiyo pia alimfikia.

Akashangaa kuona mlango ukiwa wazi alfajiri yote hiyo jambo ambalo halikuwa la kawaida katika nyumba hiyo. Hivyo aliamua kuchungulia. Mlango wa chumbani pia ulikuwa wazi.

Macho yalipofika chumbani humo yalivutwa na damu kavu ambayo ilitapakaa sakafuni, kitandani akiwa kalala mzee Kawamba, jeraha kubwa likicheka kifuani mwake. Akitetemeka, kijana huyo aliwaita jirani ambao walijua la kufanya.


“HAIWEZEKANI. Hawezi kuvumiliwa zaidi. Lazima yeye au maiti yake ipatikane katika muda wa saa ishirini na nne zijazo.
“Unasikia Sajini Abdala?” alifoka Inspekta Kombora, macho kayatoa kwa ukali na hasira.

Mbele yake kulikuwa na majalada lukuki. Jalada la Machozi ambalo lilikusanya habari zake zote na kutokuacha mwanya wowote unaomuunga na kifo cha Kitenge japo mwenyewe aliendelea kudai hivyo licha ya mateso ili aseme ukweli.

Jalada la marehemu Wamangi na Kawamba lilionyesha mienendo yao ya kutwa nzima pamoja na shughuli zao za nyuma. Hayo pamoja na maandishi mengine, yalifurika mbele ya Kombora yakimdai atulie na kuyasoma. Hakujisikia kusoma chochote.

Hakujisikia kutulia. Alitamani apate uwezo wa kupaa, aruke hadi mbele ya Bazile popote alipo ammiminie risasi zote zilizokuwepo katika bastola yake. Ni hilo tu alilohitaji.

“Lazima afe,” akaongeza.

“Ni kweli afande. Ni mtu hatari mno kuendelea kuishi nje ya kuta za magereza. Tatizo ni jinsi alivyoondokea kuwa hodari mno pamoja na mitego yote ya polisi usiku na mchana, bado anawakwepa na kutimiza nia yake,” alijibu Sajini Abdala aliyekuwa kaketi mbele ya Kombora.

“Mimi pia hilo linanishangaza,” Kombora alimuunga mkono.
“Nilivyoichunguza historia yake ya nyuma inaonyesha kuwa aliwahi kupitia JKT. Pengine ni hilo linalompa uwezo wa kutushinda ujanja. Bila hivyo, ningeweza kupendekeza kuwa anasaidiwa na mtu au watu.”

“Kweli mzee, kwa mfano alivyoua siku ya leo. Ameweza kuua hapa mjini kisha akasafiri hadi Kinondoni ambako ameua tena. Utadhani kuna mtu anayemsaidia kwa usafiri.”

“Aweza kuwa anatumia mabasi ya abiria. Akiwa kakificha kisu chake vyema, kondakta na abiria wanamwona kama mtu wa kawaida tu. Nimejaribu kutazama uwezekano wa mtu yeyote kumsaidia sikuona. Yeye ni kichaa aliyepata kichaa hicho baada ya utunzi kuiathiri akili yake na vitabu vyake visivyoeleweka kudharauliwa na watoaji. Amepata wazimu. Nani atakayemsaidia mwendawazimu kama huyo? Angeweza kusaidiwa na mwehu mwenzake Machozi, lakini katika uchunguzi inaonyesha kuwa hawafahamiani kabisa. Na bado Machozi tunaye ndani. Hapana sajini, tusisumbue vichwa vyetu kutafuta mambo yasiyo ya muhimu. La muhimu ni kumpata huyu Bazilw kwanza. Endapo baada ya kupatikana kwake vifo vitaendelea, ndipo tutaanza msako mpya.”

“Ndiyo afande.”

“Na kuhusu picha yake, peleka katika magazeti yote. Tangaza kuwa yeye ni mtu hatari ambaye anatakiwa hai au maiti mapema mno. Yeyote atakayemwona aiarifu polisi mara moja. Sawa?”

“Lakini afande…” Abdala akasita tena kidogo kabla ya kuendelea. “Suala hili naona unalipa uzito mno. Ni rahisi sana kutoa maelekezo yasiyoridhisha endapo utakuwa katika hali uliyonayo siku hizi. Tangu kisa hiki kilipoanza sijakuona ukivuta; jana nzima hukunywa hata chai; leo pia naona huna wazo la kutia chochote. Licha ya hayo, uso wako umegeuka kabisa utadhani mtu anayefuata katika orodha ya vifo hivi ni wewe. Kwa nini afande? Huoni kuwa ni hatari kwako? Nadhani hii ni kesi ya kawaida kama nyingine nyingi ambazo tumezitatua kwa njia ya kawaida. Isikutishe sana…”

“Isinitishe!” Kombora alifoka. Kisha alijirudi na kujaribu kutabasamu, lakini tabasamu halikutokea. Akamtazama Abdala kwa huzuni huku akiwaza: Huyu hajui. Hafahamu kuwa napata simu za muuaji kila kabla ya mauaji hayo. Naweza kustarehe vipi, mimi kama kiongozi wa polisi, hali muuaji ananikebehi kwa siku kabla ya kumwaga damu isiyo na hatia?

“Hapana sajini,” akajibu. “Kama ni mzaha tutaufanya baada ya kumtia Bazile katika mikono yetu. Kwa sasa jambo muhimu ni kumpata tu. Sawa?”

“Bila shaka atapatikana afande.”

“Sawa.”


“…ATAPATIKANA afande….sawa…” Brown Kwame akafunga chombo chake na kumgeukia mwenzake aliyeketi upande wa pili wa meza. Wakaangua kicheko.

“Umeona Chenja?” alimuuliza mwenzake. “Hakuna lolote watakalozungumza hapo kituoni kwao ambalo linapita bila kulisikia. Nafahamu kila mpango wao kabla hawajaanza kuutekeleza. Kwa hiyo, kaa ukijua kuwa hakula chochote wala lolote litakalotukwamisha. Moto tuliouwasha umeshashika mbuga nzima. Hawawezi kuuzima. Acha waendelee kujua adui yao ni yule bwana mdogo Bazile. Napenda waendelee kuamini hivyo. Watakapogutuka itakuwa ‘too late’ kwao. Sisi tutakuwa tumemaliza kazi yetu.”

“Kwa kweli watu hawa ni wazembe kuliko nilivyotegemea,” Chenja alisema. Kama ilivyo kawaida yake, alisema huku akipapasa tumbo lake ambalo lilichomoza nje ya kifua chake. “Hadi sasa wanaamini kuwa adui yao ni Bazile?”
“Na bado nitawafanya wazidi kuamini hivyo,” Kwame alijibu kwa majivuno. “Huu ni mpango wa kimataifa bwana Chenja. Mbinu zilizotumika ni za kitaalamu ambazo mtu yeyote mwenye akili za kawaida lazima ahadaike tu. Leo nitawaonyesha adui yao. Bazile atawatembelea. Nataka kumfurahisha zaidi rafiki yangu Kombora.”

“Angalia usi-over do.”

“Hakuna litakalotokea. Bado kifo kimoja tu, baada ya hapo amri iko mikononi mwetu, nchi miguuni mwetu. Utaona bwana Chenja. Subiri kidogo tu.”

“Sawa, sasa nadhani niende zangu. Ni hatari kukawia hapa.”

“Hakuna mahala penye usalama kama hapa. Mtu yeyote anayevuka geti hapa ndani namwona vizuri. Silaha zilizotegwa katika chumba hiki zimepangwa kwa namna ambayo mtu kwa kawaida haoni na zaweza kumteketeza wakati wowote nitakapo. Zaidi ya hayo, vyumba vya jirani wapo walinzi waliohitimu kuua na kuadhibu endapo nitatoa amri hiyo. Licha ya yote hayo, ulikoingia wewe watu wanadhani uko maliwatoni. Hakuna anayejua siri ya mlango huo. Hatufanyi mzaha hata kidogo bwana Chenja. Tumedhamiria. Na kwa kuwa tuko ukingoni hatuna lolote la kuhofia. Hata hivyo bora uende zako.”

“Kwaheri.”

Kwame alibonyeza dude fulani, sakafu ya chini ya meza ikafunuka na kuachia mwanya wenye ngazi inayoingia ardhini. Chenja aliaga tena na kisha kuifuata ngazi hiyo. Alitokea katika nyumba moja upande wa pili wa mtaa. Nyumba hiyo siku zote ikiwa haina watu wengi, isipokuwa wachache ambao walijua wanachokifanya, ilikuwa rahisi kwa Chenja kutoka nje ya mlango huo ulioandikwa GUEST LAVATORY bila kuonekana na kuingia katika gari lake ambalo lilimrejesha kazini kwake.

Kwame aliendelea kutulia juu ya meza yake akitabasamu. Kila kitu kilikuwa kikimwendea kama ilivyokusudiwa. Furaha ilioje!

Machoni mwa serikali na mbele ya kila mtu, Brown Kwame alikuwa yuleyule, mtu mfupi, mnene, kidevu kilichofunikwa na ndevu nyingi zilizozunguka uso mpana wenye macho maangavu, mtu ambaye siku zote alionekana mtanashati kwa suti za nje na viatu ambavyo vilitengenezwa kwa matakwa yake binafsi katika viwanda mashuhuri.

Mtu huyu kikazi alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni mashuhuri iliyoitwa Snow Fund ambayo ilishughulikia mambo mengi yakiwa pamoja na huduma za usafiri kwa watalii, uuzaji wa vinyago nchi za nje, uwakala wa uingizaji na usafirishaji wa bidhaa na kadhalika. Ofisi hii ilikuwa ikifanya kazi vyema na wafanyakazi wake walikuwa wakiridhika kabisa kimshahara.

Ni hiyo picha ya nje iliyokuwa wazi machoni mwa wengi. Hata wafanyakazi wote wa matawini na hapa makao makuu walikuwa na picha hiyohiyo. Kwame alipenda iendelee kuwa katika hali hiyo. Hakupenda upande wa pili uonekane, hadi hapo baadaye kidogo.

Katika upande huu wa pili, Kwame hakuwa Kwame, bali alikuwa
Joe Kileo, mwakilishi wa kampuni moja kubwa ya kijasusi kutoka nchi za Magharibi. Kampuni ambayo ilikuwa ikiendesha shughuli nyingi za hatari katika nchi kubwa na ndogo kuhujumu tawala na uchumi ili zielekee upande wautakao kwa manufaa yao na nchi zao.

Shirika hilo la ujasusi, licha ya kumlipa Kwame fedha nyingi za kigeni, ndilo lililompa mtaji mnene ambao aliutumia kufungua kampuni hii. Haja yao haikuwa faida wala huduma kwa jamii, bali ilikuwa kupata fursa nzuri ambayo iliwawezesha kukutana na watu wao waliojifanya watalii kuingiza silaha, dawa hatari na vitu vingine ambavyo vilikusudiwa kutumiwa siku za usoni.

Tayari walikuwa wamefanya mengi maovu. Bado walikusudia kufanya mengi. Wakiwa katika kuyaandaa hayo ambayo walikusudia kuyafanya ‘pigo la mwisho’, ndipo Kwame alipomwona kijana yule Bazile Ramadhani akimjia ofisini kwa mwendo wa haya haya na miswada mitatu mikononi, akiomba msaada wa kusaidiwa kuchapishiwa vitabu.

Kwame akajitia huruma, akampa ushauri wa kuwaona wachapishaji. Kijana huyo akamweleza jinsi alivyokata tamaa kwa wachapishaji hao. Kwame akazidi kumhurumia. Kumbe Joe Kileo, kama alivyojulikana kwa washiriki wake, alikuwa amepata. Alifurahia sana kimo cha kijana huyu, hasa urefu wake ulivyosadifu na kupatana na matakwa yake.

Njama alizokuwa ameinjika zilikuwa kwenye hatari ya kuvuja-sasa eti Muumba kamwonyesha njia. Hivyo aliwaamuru makachero wake ambao walimfuata Bazile kwa siri hadi kwake ambako walitekeleza jukumu walilopewa la kufanya waamini kwamba kaibiwa muswada kwa kumlaza kwa dawa zao za kitaalamu na kuanza maongezi hayo yaliyomfanya aamini. Kisha waliingia ofisi ya Kitenge usiku na kuiba muswada huo; ndipo yakafuata yote ambayo yalikuwa yakiendelea kutukia. Yote ambayo yalikuwa yakizungusha kichwa au ubongo wa Inspekta Kombora na wenzake wote kwa namna alivyokusudia kabisa Kwame.

Jambo lingine la kutia moyo ambalo lilizuka bila kutarajiwa katika wakati unaostahili ni lile la kujitokeza yule mwanamke malaya, Machozi na madai yake ya ‘kumuua’ Kitenge. Hayo Kwame alikuwa ameyasikiliza katika chombo chake kilichonasa kila maongezi yanayofanyika katika ofisi ya Kombora.

Kwanza yalimshangaza kisha yakamfanya acheke kwa furaha. Ilikuwa nyongeza nyingine juu ya mtafaruku uliokuwa umepangwa kumsumbua Kombora na polisi wote wasiweze kupata walao wazo ambalo lingewaelekeza kulikokuwa na ukweli.

Lingine ni jinsi Kitenge alivyolewa usiku ule hata wasipate haja ya kutumia dawa zao za kulevya. Bahati ilioje. Polisi wangeendelea kumsaka muuaji wa bandia katika sehemu ambazo hayupo hali yeye Kwame na kikosi chake wakiwacheka na kuendelea na harakati zao pasi ya aina yoyote ya hofu.

Kwame alitabasamu tena, alijipongeza kwa jinsi mambo yalivyokuwa yakimwendea kwa utaratibu na bahati kubwa. Kisha aliitazama saa yake ya mkono, akainuka na kumpitia katibu wake ambaye alikuwa kainamia mashine ya chapa akichapa barua.

“Natoka kidogo,” alisema na kuendelea na safari yake bila kusubiri jibu. Je, alielekea Kituo cha Polisi namba kumi na mbili.

Kituoni aliomba kumwona Kombora. Alimkuta akiwa kachakaa uso kwa mikunjo ya hasira na mshughuliko. Nusura Kwame acheke au kumpa pole. Lakini alijifanya hajui lolote linalotokea. Badala yake alimsalimu Kombora kirafiki na kujikaribisha juu ya kiti kilichomwelekea.

Hawakuwa wageni kwa kila mmoja, ingawa kazi zao zilikuwa zikiwanyima fursa ya kufahamiana zaidi. Mara mbili, tatu wamekutana katika baa au tafrija fulani, mara kadhaa wameonana kikazi Kwame akileta malalamiko au matakwa fulani fulani ya kampuni yake.

Kwa Kombora, Kwame alikuwa mtu wa kuheshimiwa, ambaye ‘amebahatika’ kupata wadhifa mnono wenye nafasi zote za kutumia. Wadhifa ambao ulimruhusu kusafiri kokote kule nje ya nchi bila hofu ya wanawe kulala njaa. Kinyume na yeye ambaye kazi yake ilikuwa kulinda masilahi ya nchi na watu wengine usiku na mchana sehemu za hatari ambazo dakika yoyote waweza kupoteza maisha. Kazi ambayo malipo hayakuwa ya kuridhisha sana kulingana na uzito wa jukumu.

Hata hivyo, Kombora aliipenda sana kazi yake. Aliona furaha mno kuona matajiri wa matajiri na maskini maisha yao yakiwa mikononi mwake na kuutegemea msaada wake. Ilikuwa tamu zaidi ya utajiri kuona baba mzima mwenye umri zaidi ya baba yake akikulilia ili umwokoe kutokana na ‘mtu’ au ‘jambazi’ ambalo linakusudia kumuua. Wadhifa ulioje!

“Ndiyo bwana Kwame, unaendeleaje huko Snow Fund?”
“Vizuri tu.”

Kwame alipoona Kombora akimtazama kwa macho yanayomuuliza shida yake aliongeza, “Nilichofuata ni kukueleza juu ya lile suala lililonileta majuzi.”

“Suala la?”

“Wizi wa shilingi elfu moja.”

“Alaa!” Kombora akakumbuka. Lilikuwa moja kati ya masuala madogo ambayo kwa kawaida hayashughulikiwi na ofisi hii. Zaidi ilimshangaza kuona Kwame na ukurugenzi wake aking’oka toka ofisini na kuja kutoa ripoti juu ya wizi mdogo kama huo. Kwa nini asipige walao simu? Alikuwa amejiuliza siku hiyo.

Hakujua kuwa ni siku hiyo ndiyo Kwame alipoleta chombo chake kidogo chenye ukubwa wa gololi na kukipachika kwa hila sehemu fulani kwenye meza ya Kombora. Chombo ambacho kilikuwa kikinasa na kupeperusha maongezi yote yaliyokuwa yakifanyika katika ofisi hii.

“Kwa kweli ndugu Kwame, suala lako bado…”

“Ndiyo, ndiyo Inspekta,” Kwame alikatiza. “Nilichofuata ni kukuomba ufute kesi hiyo. Nilikosea kuileta mbele yako. Ulikuwa wizi mdogo mno. Kuufanya ufahamike itakuwa kuwatangazia wafanyakazi wote wenye nia ya wizi kuthubutu kufanya hivyo. Watakuwa wameona kuwa Snow Fund si imara kama wanavyodhani.”

“Siyo vibaya ndugu Kwame. Hata hivyo endapo tutampata mwizi hatutasita kumfungulia mashtaka.”

“Vizuri,” Kwame alijibu akiinuka. “Kwa heri Inspekta.”

“Karibu tena bwana Kwame.”

Nje ya kituo kicheko kingine kilimtoka Kwame. Hata hivyo, hakukiruhusu kitoke nje. Alichekea tumboni.


USIKU huo, kama mwingine wowote, tangu mauaji yalipoanza kutokea, jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake lilifurika askari polisi na JKT ambao walikuwa makini wakilinda doria. Kila mlinzi alikuwa na picha ya Bazile akilini na rohoni. Picha ambayo ilikuwa imetangazwa na kusambazwa kote kwa juhudi kubwa. Walevi, wachawi, wazinzi na wote wenye maradhi ya kutembea usiku walitaabika sana usiku huo.

Kila mmoja alihojiwa na kutazamwa sana akilinganishwa na picha ya Bazile. Wale ambao waliondokea kufanana naye walao kidogo walitaabika zaidi kwa maswali ya mdomo na vitendo. Baadhi waliendelea na safari zao baada ya kupitia vituo vya polisi.

Mtu aliyehitajika hakuonekana. Polisi mmoja alikuwa kajibanza kwenye uchochoro wa Mtaa wa Nkurumah. Hakuwa usingizini wala hakusikia kusinzia. Hata hivyo, alitahamaki akipatwa na kitu kama kizunguzungu au usingizi wa ghafla. Alipojaribu kupambana na hali hiyo alisikia kishindo kutoka kwa nyuma yake. Pindi akigeuka alikutana na pigo la judo ambalo lilitua shingoni mwake na kumlainisha. Akaanguka chali, silaha ikimtoka mkononi na kudakwa na jitu lenye mavazi meusi. Jitu hilo lilimwinua na kumsogezea askari huyo uso wake likisema:

“Natumaini wanifahamu.”

Askari huyo hakujua ajibu nini. Uso huo haukuwa mwingine zaidi ya ule wa Bazile Ramadhani. Uso wa mtu katili ambaye alikuwa tayari kuua wakati wowote. Huku akitetemeka, askari huyo alijaribu kujitetea, lakini aliambulia pigo jingine ambalo lilizidi kumlegeza viungo.

“Naona wanifahamu,” liliongeza jitu hilo likiutia mkono wake mfukoni na kuuchomoa ukiwa umeshikilia jisu refu ambalo licha ya kiza kilichotanda katika uchochoro huo, lilimeremeta. “Hiki ni kisu kilichowaua wote. Kingeweza kukuua wewe pia endapo kingehitaji. Hata hivyo nitakuacha hai, nakuhitaji. Nataka upeleke salamu kwa rafiki yang mpendwa Mkwaju Kombora.”

Polisi huyo hakuwahi kusikia yote. Alikuwa hajifai kwa kutetemeka, kutetemeka ambako kulikoma na nafsi yake kuchukuliwa na mshtuko mkubwa pindi kisu hicho kilipopita ghafla kifuani na kuacha jeraha kubwa kwa alama ya msalaba. Maumivu hayo makali pamoja na mshtuko vilimfanya aruke na kuanguka sakafuni ambako alitulia kwa dakika nzima kama anayesikiliza ili afahamu kama yungali duniani au tayari kawasili kuzimu. Akiwa katika hali hiyo alisikia kwa dhiki kubwa sauti ya jitu hilo iliyosikika ikicheka na kisha kusema, “Mpe Kombora salamu tafadhali.”

Fahamu zilipomrudia vyema, askari huyo alijikuta yu peke yake, damu zikimvuja na kuiharibu sare yake. Silaha yake ilikuwa imetupwa hatua chache kando yake. Akajitahidi kuinuka na kuiokota silaha hiyo. Kisha alikumbuka kupuliza kipenga ambacho kiliwaleta askari wote karibu na alipokuwa. Baada ya kuona mkasa huo, askari walijitoma mbio huku na huko wakisaka na kusakanya kila pande ya eneo hilo. Hawakuona chochote.

Wakati huohuo, Inspekta alikuwa akiamshwa kutoka katika usimgizi ambao ulikuwa ndiyo kwanza anaupata baada ya saa sita za kufanya doria jijini na baadaye kuduwaa chali kitandani akifikiri kwa nguvu. Simu ilikuwa imemfuata nyumbani baada ya kupigwa kituoni baada ya kuunganishwa.

“Kombora hapa, nani mwenzangu?”

“Inspekta Kombora? Ni mimi rafiki yako kipenzi…”

Kombora asingeweza kuisahau sauti hii. Ilikuwa ya yuleyule adui yake mkubwa katika orodha ya maadui zake wote walioko hai. Hakupenda kuisikia sauti hii. Lakini bado pia alipenda kuisikia ili ajue lipi mwendawazimu huyu alikusudia kutenda.

“…wako. Nimeona nikufahamishe mwenyewe kuwa nimekutumia salamu za upendo kwa mkono kwa mmoja wa askari zako. Utafurahi sana kumwona Inspekta. Anavutia kwa rangi nyekundu na kidani cha aina yake alichovaa kifuani.”

Kombora hakuwa na hamu ya kuendelea kusikiliza sauti hiyo. Sauti ambayo sasa ilikuwa ikisikika masikioni mwake kama mwito wa mauti yenyewe utokao kuzimu moja kwa moja. Hata hivyo, aliendelea kusikiliza. Haja haikuwa kumsikia bali kuwapa fursa makachero wake ili waifuate simu. Alikwishatoa siri ya simu baina yake na muuaji huyo na kuweka wataalamu tayari kujua simu inatoka wapi na kuwaashiria vijana ambao waliandaliwa kutoa ishara kwa askari wa doria katika eneo hilo ambao waliruhusiwa kuua chochote watakachokikuta kikipiga simu hiyo. Uzoefu wake kikazi ulimfanya Kombora ajue kwamba vijana hao walikuwa kazini wakisikiliza simu hiyo a kutimiza wajibu wao.
“Inspekta?”

“Nipo.”

“Mbona kimya rafiki yangu?”

“Hujajibu chochote.”

“Juu ya nini?”

“Salamu zangu. Zaidi ya salamu ni kwamba najisikia kuua mtu mwingine. Unasemaje?”

“Unataka nisemeje? Nikupigie magoti kukusihi usiue? Niwezalo kusema ni ukae ukijua kuwa nitakutia mbaroni. Na utajuta kuzaliwa. Pamoja na hayo, bado nakushauri kuwa ujitokeze mwenyewe. Upo uwezekano wa kukusamehe,” Kombora alimaliza huku akijiuliza kama hajavuka kiwango kiasi cha kumtoa mtu huyo kwenye simu mapema kabla watu wake hawajamfikia.

“Inspekta! Mbona maelezo mengi mno?”

“Siyo mengi, ningeweza kueleza mengi zaidi…”

“Inspekta. Uko peke yako kwenye simu?” alidakia mtu huyo.

“Ndiyo. Nitakuwa na nani tena?”

“Uongo. Unajaribu kupata nilipo kwa simu. Hongera kwa juhudi zako na pole kwa kazi yako isiyo na matunda.”

“Sivyo…sikia…” ilikuwa kazi bure. Kicheko kilisikika upande wa pili kikifuatwa na kukatwa simu. Kilichobaki katika masikio ya Kombora ni kicheko ambacho kilitisha na kuchukiza mfano wa kicheko cha mauti yenyewe.


HABARI mbaya husafiri haraka sana kuliko habari njema. Hii ya mauaji ilienea haraka mara mbili zaidi ya kawaida. Licha ya picha ile ambayo ilitokea magazetini na maandishi ya waandishi ambayo yalieleza kwa ufupi chini ya vichwa vya habari: “MUUAJI HATARI AZUKA JIJINI” na la Kiingereza lililodai “THE MURDERER STILL AT LARGE”, bado kuna mengi yaliyosemwa baina ya mtu na mtu mitaani. Huyu alisema hivi na yule akaongezea lake ikawa habari pana ya kutisha kuliko ilivyokuwa.

Kama watu wengine, Joram Kiango akiwa mkazi wa jijini Dar es Salaam, alipokea habari hiyo kwa njia zote. Aliwasikiliza wambeya wa mitaani, akayasoma magazeti yote na kisha kuulizia vizuri kwa miongoni mwa rafiki zake walioko katika Jeshi la Polisi. Baada ya kuipata kikamilifu na kuona jinsi polisi walivyokuwa wakitapatapa katika hali ya kukata tamaa, alitabasamu.

Kwa Joram, tabasamu hili halikuwa la furaha ya kusikia watu wasio na hatia wanateketea pasi sababu, hasha. Kwake, tabasamu hili huwa dalili ya shauku. Shauku kubwa ambayo humjia na kumteka kikamilifu kila litokeapo tukio la kutisha na kusikitisha kama hili ambalo huhitaji mtu shujaa kulitatua. Moja kwa moja Joram hujihisi kama mtu huyo na kujitupa katika duru la mapambano kwa mbinu zake ambazo humfanya aponee chupuchupu, huku katatua au kuweka hadharani siri za hatari ambazo polisi huwa wamefikia hatua ya kukata tamaa.

Hakuna asiyemjua Joram Kiango. Ni yule kijana mrefu, mwenye maungo yenye nguvu na sura nzuri ambaye wakati wote huwa mchangamfu. Yule kijana mwenye ofisi yake inayoitwa Private Investigator ambayo hushughulikia upelelezi wa aina mbalimbali toka kwa wateja ambao huwa kampuni au mashirika yenye haja ya kujua jambo fulani, watu binafsi wanaohitaji kutatuliwa hili na lile na yeye anapojisikia haja au njaa ya kusaidia polisi katika shughuli zao za kila siku.

Kijana huyu mwenye umri usiozidi miaka ishirini na sita ni juzi tu aliporejea kutoka Marekani ambako alikuwa akiishi na wazazi wake wanaoishi huko. Ni huko ambako Joram alipata moyo wa kishujaa baada ya kukua miongoni mwa watoto weusi na kuona walivyokuwa wakinyanyaswa na wenzao weupe.

Ingawa alipata elimu nzuri lakini mara baada ya elimu hiyo alijiunga na vikundi vya wahuni weusi waliokuwa wakisumbua sana Jeshi la Polisi. Waliiba na kupigana wakiharibu na kusumbua katika maduka na benki. Baada ya hapo Joram alijiunga na CID na kufanya kazi nzuri, lakini ghafla akaacha kazi baada ya kujiona kakamilika kimwili, kifikra na kimtazamo.

Ndipo akaja Dar es Salaam ambako alifanya mengi, yaliyoipendeza polisi kabla hajapatiwa kibali cha kufungua ofisi hii.
Machache kati ya aliyoyafanya yaliwavuta waandishi hata wakayaandikia vitabu na kuviita DIMBWI LA DAMU na LAZIMA UFE…

Alitabasamu tena akalitupa gazeti na kumtazama Neema Idd katibu wake ambaye pia alikuwa akimtazama.

“Unajua Neema…”

“Usiniambie. Najua kila kitu. Macho yako yanaonyesha kuwa unataka kujiingiza katika mambo haya. Sijui umelogwa mwenzangu. Labda hukusikia juu ya yule polisi aliyepewa salamu za kumpa Kombora?” Neema alimaliza.

“Yule bwege? Mtu una bunduki mkononi kama siyo uzembe ni nini hata mtu mwenye kisu akuchanje kifuani?” Joram alijibu akicheka.

“Siyo kuchanjwa Joram! Amejeruhiwa vibaya sana.”

“Pamoja na hayo,” kisha sauti ya Joram ikabadilika na mzaha ukatoweka kabisa. “Jambo linalonishangaza katika suala hili ni huyu mwandishi Bazile! Imekuwaje akawa hodari ghafla kiasi hiki?

Vipi awe mjanja wa kuepuka mitego yote ya polisi, shujaa kiasi cha kumkabili polisi mwenye silaha na kumpa salamu za jeraha kifuani na wakati huohuo akimdhihaki mkuu wa polisi kwa simu za kashfa mara kwa mara? Hamu yangu ni kujua alivyopata uwezo huo kwanza, kisha nitajua namna ya kumtia mikononi.”

“Yaani umeshaanza kazi?”

“Bila shaka. Sina haki ya kustarehe hali mtu yuko hai na ameahidi kumwaga damu nyingine zisizo na hatia. La, Joram Kiango si mvivu kiasi hicho mama.”

Neema hakuwa na la zaidi. Kwa kadri anavyomfahamu, Joram kamwe hatastarehe tena, tayari kazama kichwa na miguu katika dimbwi la mkasa huo. Kumshauri kusingesaidia. Hata hivyo alimwambia neno lilelile ambalo amemwambia mara nyingi:

“Angalia Joram. Jihadhari.”

“Hakuna anayemfahamu Joram Kiango zaidi yako Neema. Ninayo nafasi nzuri ya kumtia muuaji mkononi kwani kama ujuavyo, adui huyo kajizatiti kukabiliana na jeshi la polisi, hana habari ya mtu mmoja anayejiita Joram. Huoni kama hiyo ni nafasi nzuri ya kumfumania?” alimalizia akiwasha sigara na kuanza kuivuta kwa utulivu.

Katika utulivu huo, alikuwa akipambana vikali na tamaa ambayo ilikuwa ikimshawishi ainuke na kuanza uchunguzi juu ya mkasa huo. Tamaa ambayo aliishinda nguvu baada ya kujikumbusha tena na tena kuwa alikuwa hajajiandaa kikamilifu kuweza kusimama kiume dhidi ya muuaji au mauaji mazito kama hayo, mauaji ambayo sasa yalikuwa yamewashinda polisi kuyakabili.

Kujitumbukiza kiholela ingekuwa sawa na kumwalika muuaji ampe yeye Joram salamu ambazo safari hii zingeelekezwa si kwa Kombora bali ahera. Naye Joram hakuwa tayari kwenda huko mapema kiasi hiki.

Hivyo alijituliza akiwaza yapi ameyafahamu tayari dhidi ya muuaji huyo, mangapi polisi imefanya katika juhudi zao za kumtia mbaroni, kiasi gani wamefanikiwa na vipi wamefeli. Kadhalika alihitaji kujua mangapi yanafahamika juu ya marehemu, mangapi hayafahamiki na yapi yalistahili kufahamika.

Baada ya kuyafahamu hayo, yeye kama Joram Kiango angekuwa tayari kufuata njia zake ambazo zingemfikisha hadi kisogoni au usoni pa muuaji huyo. Joram, angependa zaidi kukutana naye uso kwa uso, aupime na kuushuhudia kwa macho yake ujabali wa mtu huyo aliyeondokea kuwa jitu kwa muda mfupi tu.

Akiwa na uhakika na mbinu zake, pamoja na matumaini juu ya njia atakazopitia ambazo ni kinyume na zile za polisi, alijisikia furaha kana kwamba tayari kamtia adui huyo mikononi mwa sheria. Akaitupa sigara yake katika kasha la taka na kutoka nje akipiga mluzi.

*JORAM KAAMUA KUINGIA KAZINI KUMSAKA HUYU ANAYETUMA SALAMU ZA MAUAJI. NI KIPI KITAFUATA? FUATILIA RIWAYA HII KALI

ITAENDELEA

Najisikia Kuua Tena Sehemu ya Tatu

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment