Heka Heka Sehemu ya Tano
KIJASUSI

Ep 05: Heka Heka

SIMULIZI Heka Heka
Heka Heka Sehemu ya Tano

IMEANDIKWA NA: JAPHET NYANG’ORO SUDI

*********************************************************************************

Simulizi: Heka Heka

Sehemu ya Tano (5)

Asubuhi hii wakati mpelelezi Jacob Matata akiwa ndani ya gari lake akisubiri kuvuka na kivuko cha Kigamboni kuelekea ng’ambo ya pili, hawa watu watatu walikuwa na mipango yao mingine. Herkan Kalm yeye alikuwa ndani ya gari yake aina ya Mercediz SLS-Class Coupe ndani ya kivuko cha Kigamboni lakini tofauti na Jacob yeye alikuwa anatokea Kigamboni kuelekea mjini. Hakuwa na mengi ya kufanya mjini bali alikuwa anakwenda uwanja wa ndege Dar es salaam kwa ajili ya kupokea mzigo wake uliokuwa umetumwa toka kwa washikirika wenzake walioko ng’ambo.

Toka siku ile nyumba kambi yake ilipoteketezwa na vijana wa ofisi fukuzi, hakuona sababu ya kwenda kwenye nyumba yake iliyoko Mbezi, hiyo ilikuwa ni kwa sababu za kiusalama zaidi. Hivyo alikwenda kwenye jumba lake jingine ambalo lilikuwa Kigamboni ufukweni mwa bahari ya Hindi jirani na hotel moja maarufu eneo hilo. Hakuwahi kutoka huko, leo ilimlazimu kwenda kuuchukua ule mzigo kwa vile hakutaka makampuni ya kusafirisha vifurushi kwenda nyumbani kwake.

Kama zingekuwa ni sumaku zingevutana, gari la Herken Kalm lilipita jirani na lile la Jacob ambalo safari hii lilikuwa katika msululu wa kungoja kuingia kwenye kivuko.

Wakati Jacob Matata na Herken Kalm wakiwa wanapishana kwenye kivuko cha Kigamboni, John Kificho yeye alikuwa ndiyo anaondoka uwanja wa ndege wa kimataifa KIA baada ya kuwa amewasili hapo akitokea Dar es salaam asubuhi hiyo, sasa alikuwa anelekea Arusha mjini. Taarifa kuwa yale magari ya mizigo yalikuwa yamefika salama aliona mpango ulikuwa unaelekea kukamilika. Taarifa alizokuwa amepewa na Frank alitakiwa aende Arusha kwa ajili ya kupokea mzigo maalumu na pindi akiupata tu, ataondoka kwa ndege ya kukodi toka Arusha hadi Dar es salaam. Hakuambiwa ni mzigo gani ila aliambiwa ahakikishe usalama wa yale magari ya mizigo. Japo yalikuwa yamebeba mali ya serikali lakini yalikuwa na umuhimu kwao kuliko hata serikali yenyewe. Saa nne na robo, John Kificho alikuwa ameshaingia ndani ya sehemu ya mapokezi ya hotel ya Kibo Palace.

Magari yenyewe ambayo John Kificho na Harken Kalm walikuwa wakiyawazia kwa pamoja bila kujua, ndiyo yalikuwa yameingia eneo la Njiro mkoani Arusha. Yaliendeshwa taratiibu yalipokuwa yanakaribia kizuizi cha kwanza kuelekea yalipo maghala maalumu ya kuhifadhia chakula maeneo ya njiro Arusha. Japo watu wengi walijua na kuamini kuwa maghala hayo yalikuwa yakihifahi chakula tu, lakini ukweli haukuwa hivyo. Maghala hayo yalihifadhi nyara muhimu za umma. Ndiyo maana kama ungejaaliwa kuyajua yalipo, usingadhani ni maghala ya chakula tu kutokana na yalivyojengwa na ulinzi ulivyokuwa mkali maeneo hayo. Kwanza yalikuwa yamejengwa jirani na kituo cha wale jamaa wa fanya fujo uone pale Njiro. Pili kulikuwa na ulinzi wa mitambo sambamba na askari waliovaa sare na ambao hawakuwa wamevaa sare.

Magari hayo ambayo ndo kwanza yalikuwa yanawasili toka Dar es salaam ambapo yalikuwa yamepakia shehena ya magunia ya chakula katika soko la kariakoo yalianza kukaguliwa hatua hamsini kabla ya kulifikia lango kuu la maghala hayo. Moja ya magunia hayo lilikuwepo gunia ambalo lilikuwa limepakiwa na kijana Mud kwa malipo maalumu ya shilingi milioni moja.

Mud alishangaa sana siku hiyo akiwa anapakia magunia, alipoliona gunia lenye alama aliyoambiwa, alienda haraka kulibeba maana hayo ndiyo maelezo aliyokuwa amepewa na mpigaji wa simu, kuwa ahakikishe analiona gunia hilo na kulibeba. Hivyo alilibeba na kushangaa kwa lilikuwa jepesi tofauti na magunia mengine. Pia alishangaa kuona amebeba vitu kama vyuma na siyo nafaka kama yalivyokuwa magunia mengine. Alijiuliza mengi na kushangazwa, lakini ajizi nyumba ya njaa alijiambia. Hakuwa na muda wa kupata majibu ya maswali yake hayo, alihitaji hela kwa ajili ya mama yake ambaye alikuwa nahitaji nauli ya kuja Dar es saklaam kwa matibabu. Alibeba gunia hilo na kulipakia ndani ya gari. Kazi yake ikawa imeisha akawa amepata ujira wake. Baada ya wiki moja alipata milioni kumi zake lakini na kitu cha ziada, alipelekwa kigamboni akakabidhiwa nyumba kwa ajili ya kuitunza kwa malipo ya shilingi laki tano kila mwezi. Kwa mtu aliyekuwa anabeba magunia Sokoni Kariakoo asingeweza kukataa kazi kama hiyo. Huo ni mshahara ambao watumishi wengi nchi hii huusikia tu. Hivyo juzi alishangaa kumwona mtu ambaye wamekuwa wakiwasiliana tu kwenye simu akiwasili eneo hilo huku akiwa anavuja jasho. Ni siku ambayo himaya ya Herkan Kalm ilikuwa imeteketezwa huku yeye akipone chupu chupu kunaswa na vijana machachari wa ofisi fukuzi. Alipowasili Harken wala hakuongea sana na Mud. Mud aliendelea na shughuli zake na Herken aliendelea na mipango yake.

Hivyo moja kati ya magari hayo lilikuwa limebeba lile gunia maalum. Huo ulikuwa mpango kamili na halisi ambao ulikuwa umehaririwa na kuratibiwa vyema na jasusi la kijerumani liitwalo Frank. Kwa njia tofauti na namna tofauti Frank alikuwa amewashirikisha John Kificho na Herkan Kalm kwa vile kwa nia tofauti walikuwa jirani na vyombo husika katika umma kutokana na umaarufu wao na nguvu yao ya kifedha. Frank alikabidhiwa kazi ya kuhakikisha shehena ya meno ya tembo iliyokuwa imekamatwa inapatikana na kusafirishwa nje ya Tanzania.

Mpango huo ulibuniwa na kundi la mtajiri wachache ambao walikuwa nyumba ya shunguli nzima ya kukusanya na kusafirisha nje meno ya tembo nchini. Baada ya mpango wao kukwama na kontena mbili za meno ya tembo kukamatwa ndipo matajiri hao walipokuja na mpango mbadala wa kuhakikisha wanayapata tena men ohayo kablwa ya kuteketezwa kama ambavyo serikali ilikuwa imepanga kufanya. Meno 34,000 ya tembo ambayo kwa biashara ya magendo nchini China yanagharimu Pauni 150 milioni za Kiingereza (Sh403.5 bilioni) yalikuwa yamehifadhiwa kwenye ghala la nafaka njiro, ni viongozi wachache sana wa ngazi za juu ndiyo waliokuwa wakijua men ohayo yalikuwa yakihifadhiwa wapi. Kati ya viongozi waliokuwa wakijua mpango huo ni mheshimiwa Mondia ambaye tayari alishakuwa marehemu, na waheshimiwa wengine wane ambapo kati yao walikuwa wanashikiliwa na Harken Kalm kwa msaada mkubwa wa Kiroboto, huku wakiliacha polisi wakiwa wanahangaika kujua ni kwa nini kila kiongozi aliyetoweka kulionekana “Amazon Cat”.

Magari yale yalivuka vizuizi vyote na kuruhusiwa kuingia ndani. Tofauti na John Kificho aliyekuwa aumeingia asubuhi, Kiroboto yeye aliingia Arusha jioni ya siku hiyo hiyo. Yeye alipofika Arusha wala hakwenda kupumzika, akiwa na briefcase yake, alikwenda hotel ya Kibo Palace.

“Kuna mgeni wangu yuko hapa nahitaji kuonana naye” Alisema alipokuwa mapokezi.

“Unaitwa nani kaka? Mhudumu aliuliza huku kijana mwingine akitaka kupoke mzigo wa Kiroboto.

“Nitwa Ben. Usijali nitabeba mwenye” Alisema Kiroboto huku akiumba tabasamu usoni kwake.

“Nayetaka kumwona anitwa John Kificho” Alisema huku akiyaruhusu macho yake yaangalie jinsi sehemu ya mapokezi ya hoteli hiyo ilivyokuwa imepangiliwa vema.

“Yuko namba 21G anakusubiri” Mhudumu alisema, kabla hata hajamaliza, Kiroboto aliparamia ngazi, huku akiacha muhudumu yule akimsindikiza kwa macho. Alijikuta moyo wake umemkinai huyo mtu, jinsi alivyokuwa akiongea, jinsi alivyokuwa akiangalia, mhudumu hakupenda Kiroboto aendeleea kuwa pale.

Baada ya dakika chache Kirobot alishuka ngazi taratibu, alipita sehemu ya mapokezi bila hata ya kuaga wala kushukuru. Alipofika mlangoni ambapo alinyanyua macho yake na kuweza kuona kibao cha hospitali ya AICC, alitoa simu yake ya kiganjani.

“Vipi Mwita umeshafika Arusha? Okay vizuri sana, basi tukutane pale Njiro sinema ili unipe paka wangu, bila shaka umemuhudumia vema njiani!! Kiroboto alisema huku akiingia kwenye gari ambayo alikuwa ameshafanyiwa mpango na Herkan Kalm kuitumia hata kabla hajafika Arusha.

Saa mbili kasoro usiku wakati kibaridi cha Arusha kikiwa kinapuliza na kumfanya mtu kweli ahisi kuwa yuko jirani na mlima meru na Kilimanjaro, Kiroboto alikuwa amejituliza kwenye viti vya abiria kwenye uwanja wa ndege wa Arusha ambao uko eneo la Kisongo. Si uwanja mkubwa kama jina la Arusha lilivyo. Alifika hapo dakika ishirini zilizopita huku akiwa na paka wake. Hata wakati John Kificho akiwasili kiwanjani hapo akiwa amebeba ile briefcase aliyokuwa amempa jioni ile, Kiroboto alimwona na akamwangalia kwa macho ya kebehi. John alipofika hakukaa alipokewa na rubani wa ndege ya kukodi ambayo ilikuwa aikimsubiri tayari kwa kuondoka kama ambavyo alikuwa ameelekezwa na Frank, jasusi la kijerumani ambalo lilikuwa katika hatua za mwisho kukamilisha oparesheni ya kutorosha meno ya Tembo. Maelekezo ilikuw akishapewa briefcase na mtu aitwaye Ben, basi aondoke Arusha kwa ndege ya kukodi.

Ndege iliyokuwa imemchukua John Kificho ilichanganya injini na kuondoka kwenye uwanja wa ndege Arusha. Kiroboto aliingalia ile ndege ikijigeuza na kurudi upande huu walipokuwa wamekaa na kufanya kelele kiasi kwa vile ndege yenyewe ilikuwa ndogo. Ilipopita usawa aliokuwa amekaa Kiroboto, alisimama na kuelekea sehemu aliyokuwa ameegesha gari yake. Aliingia ndani, akamrusha Paka wake kiti cha nyuma, kasha Akaka kwenie kiti cha dereva ilihali mlango wa gari ukiwa bado wazi, alichukua kitu kama remote ya tv, alielekezea upande ilipokuwa ile ndege ikiambaa ambaa na mawingu. Kilichofuata hapo ni mlipuko mkubwa na kuacha enaga lote la eneo la kisongo likingaa kwa mwanga wa mlipuko ule. Ndege aliyokuwa amepanda John Kificho ilikuwa vipande vipande. Kiroboto alitabasamu huku akiliondoa gari lake. Sehemu hiyo ilikuwa imejaa taharuki watu wakikimbia ovyo ovyo. Hakuwa na muda wa kuangalia hayo, usiku huo alikuwa na kazi kubwa mbele yake. Aliposhika bara bara ya Munduli ndipo akapishana na gari ya polisi na Jeshi zikiwa zinaelekea uwanja wa ndege ambako yeye alikuwa anatokea.

Saa nne kasoro dakika mbili Kiroboto alikuwa miongoni mwa vijana kumi waliokuwa wakisubiri kuruhusiwa kuingia ndani ya ghala la nafaka Njiro kwa ajili ya kushusha mzigo uliokuwa umeingia usiku huo. Walikaguliwa kwa mitambo maalumu an wakaguzi walipojiridhisha waliwaruhusu hao vijana kuanza kazi ya kupakua magunia toka ndani ya magari. Kiroboto hakuwa na kasi sana kama wengine ambao walitaka kubeba magunia mengi kwa vile malipo yao yalitegemea maguni ambayo wangebeba. Alishaambiwa gari ambayo ilikuwa na lile gunia maana Mud alishamwambia Herkan Kalm namba ya hilo gari. Hivyo kiroboto akawa anangoja tu alione lile gunia ambalo lilikuwa na zana zake za kazi, alichukuwa halafu aanze kazi. Wakati akiwa anaangalia vijana wakiwa wamechachamaa kubeba, mara akaja dereva mmoja wa hayo magari, macho ya Kiroboto na yake yalipokuta yule dereva akaminya jicho kuonyesha kuwa wametambuana.


Siku iliyofuata Jacob alikuwa alikuwa kwenye harakati kubwa. Kwanza safari yake ya Kigamboni kwenda kuonana na Mud ilimdhirishia kuwa Harken Kalm alikuwa na mpango mkubwa zaidi ya alivyokuwa akidhani mwanzo. Asubuhi ile alipopishana na Herkan Kalm, kwa msaada wa wataalamu wa masula ya mawasiliano wa ofisi fukuzi alifanikiwa kujua Mud alipo kwa kufuatili namba ya simu ambayo Mud alikuwa akiitumia. Katika namba za simu ambazo Jacob Matata alikuwa amefanikiwa kuipata katika simu ya mheshimiwa Mondia moja wapo ilikuwa ya Mud. Alipofika enea alilokuwa akiishi Mud alikutana na habari za jinsi kijana huyo maisha yake yalivyobadirika ndani ya siku moja, toka kuwa masikini na kuwa milionea wa kufunga baa na watu wakanywa bure. Kasha siku mbili baadae kuhamia kwenye jumba la kifahari kigamboni. Ni jumba hilo ambalo Jacob alikuwa nakwenda kuliangalia na kumhoji Mud wakati alipopishana na Harken Kalm.

Alipofika kwenye jumba hilo la Herkan Kalm wala hakupata upizani wowote toka kwa Mud. Hiyo ikamdhihirishia kuwa kijana huyo alikuwa ni kondoo aliyekosea njia.

“Haya nakubaliana na wewe kuwa humjui vizuri huyu mzee wa kizungu, lakini hebu niambie kwa nini alikulipa hela zote zile? Jacob alimhoji Mud.

“Brother, miye kama nilivyokuambia kuwa ni mbeba mizigo sokoni Kariakoo. Sijui huyu mzee alipataje simu yangu, akanbipigia na akaniambia kuwa kuna kitu anataka nimfanyie. Nilipomuuliza ni kitu gani, kabla ya kujibu akaniambia tanipa hela nzuri sana….” Mud alijieleza huku akitetemeka.

“Shilingi ngapi?

“Milioni kumi brother, nadhani hata ungekuwa wewe usingekataa, tena nyie maaskari mnavyopenda hela” aliongea Mud

“Ennnhe akakwambia umfanyie kazi gani?

“Aliniambia siku iliyofuata kuna gari ingekuja kupakia mzigo, alinitaka kuhakikisha nalitambua gunia moja maalumu na kulipakia kwenye gari” Mud alisema huku akiusoma uso wa Jacob

“Hivyo tu?

“Ndiyo afande”

“Miye siyo afande, naitwa Jacob”

“Jacob yupi, au ndiyo yule nayesikiaga habari zake kuwa anatisha katika kuupanga mkono? Mud alisema kishabiki

“Jacob Matata” Jacob alisema jina lake lote

“Daaah hata siamini brother, ina maan hapa kuna ishu kubwa sana, hadi wewe unafuatilia!!! Ukweli brother nilipobeba lile gunia halikuwa na nafaka bali kulikuwa na vitu kama vyuma vyuma hiv….” Mud aliposema hivyo akili yake ikacheza

“Kwa nini hukudhani kuwa ni hatari kufanya vile?

“Brother mama yangu alikuwa amepata ajali siku moja nyuma, na ilihitajika hela ya kumsafirisha kumleta Dar kwa ajili ya matibabu. Hata kama ningejua kwamba ni uharifu bado ningefanya kaka, kuokoa maisha ya mama yangu” Mud alisema huku akijaribu kumwonyesha Jacob uso wa huruma.

“Sikiliza Mud, hivi sasa uko katika mkasa mkubwa sana. Nina hakika huyu mtu unayekaa naye hapa ndiye aliyepanga ajali ya mama yako ili kukushinikiza wewe kukubaliana na mpango wake wa kiharifu. Sasa sikiliza, unaweza kukumbuka namba za gari zilizokuwa zinachukua mzigo siku ile?

“Ndiyo hizi hapa” Mud alifungua pocha yake ya kuhifadhia hela akamwonyesha Jacob.

“Kwa nini uliiandika hii namba ya gari? Jacob alihoji

“Kwa sababu ndiyo iliyoyabadiri maisha yangu, mwanzoni nilikuwa nayo kishwani lakini bahada ya haya yote kutokea nikaona niiandike kama historia ya maisha yangu” Mud alisema huku akiwa anairudisha mfukoni pochi yake.

“Sikiliza Mud, unatakiwa uendelee kukaa hapahapa ili huyu mzungu asishitukie lolote. Hakikisha unakuwa kama ulivyokuwa siku zote. Hii hapa ni namba yangu, kama kuna jambo lolote la ajabu ajabu unaona au unahisi linafanywa na mzungu huyu nipigie au nitumie meseji…” Jacob hakumaliza kuongea akasikia mlio wa gari likija upande huo.

“Swali la mwisho, je kuna msichana yeyote umeshamwona hapa tangu umekuja?

“Hapana hapa tuko wawili tu” Mud alijibu. Jacob alimwangalia Mud kisha akampa mkono na kutoweka kwa staili ya jabu. Mud alitaka kushangilia maana vitu hivyo huviona kwenye sinema tu.

Hivyo siku hii Jacob alikuwa katika harakati nyingi sana. Alianzia kwenye lile shirika la usafirishaji la umma kuulizia gari yenye ile namba ilikuwa na safari ya wapi.

“Hiyo gari imeondoka juzi kwenda Arusha, jana asubuhi imefika Arusha” Alieleza huyo afisa amabaye Jacob aliambiwa kuwa ndiye anayehusika kupanga safari za magari

“Mzigo ulipakiwa karibuni wiki nzima iliyopita inakuwaje gari ikaondoka juzi? Hapo sikuelewi!!! Jacob alihoji.

“Ni kweli ilitakiwa iondoke kama wiki moja iliyopita, lakini dereva wa gari hiyo aliuawa usiku wa kuamkia siku ya safari. Hivyo safari ikasitishwa na kuruhusu madereva wengine kwenda kumzika mwenzao. Juzi ndiyo safari na shughuli nyingine zikawa zimeanza. Maana wiki yote ilikuwa ni shughuli za msiba na purukushani ya kujibu maswali ya polisi na vitisho vyao vingi. Hapa nilipo mwili na akili yangu vyote vimechoka. Hivi napanga hata niombe likizo, maana nimesumbuliwa sana na Polisi kama wewe” Alisema huyo jamaa katika hali ya kulalamika.

Alipotoka hapo Jacob alikwenda nyumbani kwa dereva aliyekuwa ameuawa. Hapo akaomba kuongea na mke wa marehemu.

“Kwani wewe nani? Alihoji mtu huyu aliyeonekana kuwa ndiye msemaji wa familia

“Mtu wa usalama” Jacob alijibu

“Aaaaaah nyie watu wa usalam tangu mmeanza kuhoji hadi leo hamjapata maelezo ya kutosha tu. Kila siku mnakuja kuhoji na bado muuji wa ndugu yetu wala hamumpati” Alisema huyo mzee kwa sauti ya kukereka na kulalamika.

“Mzee mtuwie radhi, ndiyo sehemu ya kazi yetu. Miye sitamchosha” Jacob alisema. Baada ya dakika tatu hivi, alikuwa ameingizwa kwenye chumba cha mjane wa marehemu.

“Dada wala sikusumbui sana, miye nataka kujua kama kuna kitu cha tofauti ulisikia au kuona kabla muuaji hajaingia ndani na kumuua mumeo? Jacob alisema baada ya kuwa amesalimia nakumpa pole mama mjane.

“Mmmmmh hapana kitu chochote…”

“Kweli? Hakuna kabisa? Jacob alihoji huku akimkazia macho mjane huyo ambaye alioneka kuwa katika fikira za kukumbuka

“Mmmmmmh sijui kama hili lina uhusiano wowote, nilisikia mlio wa Paka dirishani kwetu. Si kawaida kusikia Paka akilia kwa sauti kama ile dirishani” Alisema yule mjane huku akimwangalia Jacob.

“Amazon Cat” Jacob alisema hku akishusha pumzi. Hakukaa zaidi, alimpa mfiwa mkono wa shilingi laki moja na kumfanya yule mjane aangue kilio tena.

“Asante sana kaka yangu, askari wengine huja na kunisumbua tu na maswali kasha huondoka wakiniacha na machungu tu” Alisema huyo mama wakati Jacob akiwa anainuka na kuondoka.

**

Regina alikuwa anasubiri muda wake wa kufa. Kila dakika iliyokuwa ikikatika ilikuwa ikimaanisha kitu kwake, alitamani azisimamishe zile sekunde zilizokuwa zikitiririka kwenye saa iliyokuwa mezani kwake. Bomu lililokuwa linakwenda kumuua lilikuwa limewekwa mbele yake huku yeye akiwa amekaa kwenye kiti, kamba imara sana zikiwa zimeukaza mwili wa binti huyo usiweze kuachana na kiti. Alijaribu kutafakari maisha yake jinsi yalivyoanza na ambavyo sasa yalikuwa yanaelekea kwisha. Hakuona kitu ambacho kilikuwa kimewahi kumvutia katika maisha yake. Aliendelea kutafakari akiwa amechoka kwa sababu ya njaa na mateso aliyokuwa Napata kwenye hicho kiti. Kumbu kumbu zake zilipofika kwa Jacob Matata walipokutana kwa mara ya kwanza pale Miami Hotel, Regina hapo akatabasamu. Hiyo ndiyo ilikuwa kumbukumbu pekee iliyomfanya atabasamu. Moyo wake ulikuwa umekufa kwa Jacob Matata, lakini hakuwahi kupata muda wa kuonyesha kwa vitendo. Kumbu kumbu zake zikamnong’oneza kuwa alishawahi kumwambia Jacob kuwa anampenda, hapo tena Regina akatabasamu zaidi. Mara mlango wa chumba alichokuwa amefungiwa ulifunguliwa. Aliangalia dakika zilizokuwa zimebaki ili lile bomu kulipuka, zilikuwa zimebaki dakika tano. Mlango ukabaki wazi kwa sekunde kadhaa kasha paka mkubwa kiasi mwenye macho makali akaingia akitemea kwa maringo. Regina alimwangalia yule paka, hakutaka kuamini kuwa yule paka ndiye aliyekuwa amefungua ule mlango. Akiwa bado anamshangaa yule paka, mara wakaingia watu wane, wakiwa na wasiwasi mkubwa. Walionekana kuwa wamedhoofika japo kwa mtu anayeweza kuangalia vema angeweza kutambua kuwa kuchoka kwao kulikuwa kumekuja ndani ya muda mfupi. Macho yao, nywele zao, na jinsi ngozi zao zilivyokuwa ilikuwa ni dhahiri kuwa siku chache zilizopita walikuwa ni watu katika jamii. Watu wenye nafasi zao, ila sasa waionekana kufifia. Macho ya Regina yalimwangalia kila mmoja wao kwa zamu. Kasha yakarudi kwa yule paka, hapo akashindwa kuoanisha habari, watu hawa walikuwa wamefungwa mikono yao huku midomo yao ilikuwa imefunikwa na kitu kama ile gundi ya kufungia maboksi. Kama ambavyo hakutaka kuamini kuwa yule paka alikuwa amefungua mlango, pia hakutaka kuamini kuwa watu hao walikuwa peke yao. Alitaka kuwaambia kuwa sehemu hiyo ni hatari na kuna bomu ambalo lingelipuka wakati wowote. Lakini hakuweza kufanya hivyo kwani yeye naye pia mdomo wake ulikuwa umezibwa hivyo asingeweza kuongea. Akiwa anatafakari hayo, ndipo akaingia yule mtu ambaye Regina aliamini kuwa ana moyo wa shetani akiwa ndani ya mwili wa binadamu. Kiroboto aliingia akitembea taratiibu, mkono mmoja ndani ya mfuko wa koti lake na mwingine ukiwa umeshikilia kipande cha Karoti huku akiwa anajitafuna. Macho yake yalipokutana na yale ya Regina alitabasamu. Alienda hadi alipokuwa Regina, akamtolea kile kitu kilichokuwa kimemziba mdomo. Akafanya hivyo kwa wale wanaume wengine wane.

“Huna haja ya kuogopa mrembo, Jacob Matata yuko kwenye harakati za kukuokoa!! Kiroboto aliongea huku akivuta kiti na kuanza kufunga vitu Fulani ambavyo hata hivyo

“We kaka hivi unapata raha gani kuwateza watu kiasi hiki tena bila kosa lolote? Regina alisema kitakatifu.

“Wewe unaweza kuwa huna makosa lakini hawa hata nikiwaachia sasa hivi bado mwisho wao unaweza kuwa kitanzi. Watu hawa ni viongozi wakubwa, lakini kwa tamaa zao. Fikiria watu amabao wamepewa dhamana ya kuongoza vichwa zaidi ya milioni arobaini, wamepewa kulinda na kutetea mali zao, wao ndiyo wanakuwa wa kwanza kuiba na kuwatendea hao watu vitu ambavyo ndivyo sivyo…” Alisema Kiroboto huku akiwa anasimama na kuwaendea wale waheshimiwa wanne.

Waheshimiwa hawa ndiyo wale ambao walikuwa wametoweka kama wiki moja ailiyopita. Wakati Jasus la kijerumani, Frank linatafuta namna ya kufanikisha mpango wa kuiba yale meno ya Tembo, ndipo lilipopitia kwa Herkan Kalm na John Kificho ili waweze kutafuta watu ambao ni viongozi dhaifu na wenye uchu wa madaraka. Ni katika harakati hizo, waheshimiwa hawa wakaingia katika mpango mzima. Kazi yao ilikuwa ni kutoa taarifa muhimu za kuwezesha uibwaji wa pembe hizo. Kundi la viongozi hawa lilikuwa chini ya Mndia ambaye hata hivyo aliuawa na Kiroboto.

“Hwa hawafai kuishi, na kama wanaishi basi hawafai kuwa uraiani” Kiroboto alisema kasha akaanza kuwashushia kipigo kikali wale waheshimiwa.

“Sasa si uwapeleke mbele ya vyombo vya sharia, kuliko kujichukulia sharia mknoni?!!! Regina alipiga kelele baada ya kuona kipigo walichokuwa wakipata wale jamaa kilikuwa kikali sana.

“Vyombo vya sharia ndiyo wao, na wanaofanya dhambi ndiyo wao, sasa unategemea nini mrembo? Kiroboto alisema huku akiendelea kushusha kipigo kwa wale jamaa.

“Hebu angalia saa ya kwenye bomu hapo bado inatembea au imesimama? Kiroboto alisema huku bado akiendelea kutoa kipigo. Kwake ilikuwa kama sehemu ya mazoezi lakini kwa waheshimiwa wale ilikwa ni nusu kifo, katika maisha yao hawakuwahi kukutana na mtu anajua kupiga kama huyu aliyekuwa mbele yao. Wawili kati ya waheshimiwa hao waliwahi kuwa wanajeshi, lakini katika mafunzo yote waliyowahi pitia hawakuwa kuona stahili za huyo jamaa.

“Imesimama! Regina alijibu kwa mshangao

“Jacob Matata, kwa hiyo ameshampata Herkan Kalm na ameshatumia remote control kutegua hili bomu. Niltegemea hivyo baada ya kutokumpata Herkan Kalm kwenye simu na kuambiwa kuwa meli imepata hitilafu ya kiufundi. Mpango wote umeshavurugika, si mbaya sana nitamsubiri hapa hapa nimmalize kwa mkono wangu mwenyewe, shenzi sana huyu na…..” Kabla Kiroboto hajaenedelea kujiapiza sauti nyingine ilisikia. Ilikuwa ni sauti ya kizungu kwa vile muongeaji wake alikuwa mzungu.

“Mambo bado hayajaharibika Ben, we need to eliminate Jacob and then we move on with our plans” Sauti ilisema na kumfanya Kiroboto kusitisha kipigo ili kumwangalia msemaji. Macho ya kiroboto yalitua kwa mzungu mmoja mwenye kipara, mwili uliojengeka, mrefu mpana, alikuwa amevaa miwani nyeusi. Kiroboto hakusubiri kuambiwa kuwa huyu ni mtu wa kazi. Macho yao yalipokutana walitambuana kuwa wote walikuwa wahitimu.

“Bila shaka ni bwana Frank? Kiroboto alisema kwa kusahili

“Bila shaka wewe ndiye Ben au Kiroboto kama inavyojulikana Duniani kote kwa watu walioko kwenye fani hii! Frank alisema. Kasha wote wakainama kwa ile salamu ya kininja.

“Nahitaji kuongea na wewe” Frank alisema. Bila kujibu lolote Kiroboto alitembea kuelekea mlangoni ambapo Frank alikuwa amesimama. Wakatoka nje.

“Jacob ndiye anayejua mpango huu kwa sasa, tukimmaliza yeye tutaendea na mpango huu bila kubughuziwa. Najua kwa sasa hivi, Jacob anamshikiria Herkan Kalm, tulishajiandaa kama hilo litatokea. Hivyo najua wapi Herkan Kalm atampeleka Jacob Matata. Nataka uende ukamsubiri pale, akishakuja muhifandi, napenda kuona kuwa risasi itakoyoingia kichwa cha Jacob iwe inatoka kwenye bastola yangu. Miye nitaendelea na mipango mingine ikiwa ni pamoja na kuwahifadhi hawa hayawani walioko humo ndani” Frank aliongea na wote wakakubaliana na mpango mzima.

Kama Jasusi Frank lilivyokuwa limekisia, Jacob na Herkan Kalm walikuwa wanaingia kwenye nyumba moja iliyoko Mbagala mwisho. Baada ya kuhojiwa kwa muda, hatimaye Herkan Kalm alikubali kwenda kumwonyesha sehemu ambayo wenzie kwenye mpango huo wangekuwepo.

“Haya tangulia ndani, ukifanya ujanja wowote, kichwa chako halali yangu” Jacob alisema wakati wakiingia ndani. Alishapewa ramani ya jinsi nyumba hiyo ilivyokuwa.

Waliingia ndani, nyumba ilionekana kuwa kimya kabisa, walipoingia upande mwingine wa jingo ndipo alipoweza kusikia sauti za watu wakiwa waongea na kucheka kwa sauti kubwa.

“Wewe ndiyo una bibi miye nasubiri harusi tu”

“Kwa ni queen ya jembe ameshatoka? Sauti zilisiki, ilikuwa wazi kuwa walikuwa wanacheza karata.

“Utagonga kama mnavyogonga siku zote, wakishituka na kufanya fujo yoyote, risasi ya kwanza toka kwangu itaingia kwenye kichwa chako kwanza ndipo nitashughulikia wengine baadaye wakati wewe tayari ukiwa maiti. Sijui kama uko tayari kuwaokoa hawa wakati wewe ni maiti? Jacob alionya huku akimpa nafasi Herkan Kalm agone mlango. Wakati Herkan Kalm akiwa ananyanyua mkono wake kugonga, huku Jacob Matata akiwa tayari na bastola zake mbili mkononi, mara Jacob akahisi kitu cha baridi kiligusa shingo yake, akataka kufanya kitu, lakini alipomwona paka alipita kuelekea upande aliokuwa amesimama Herkan Kalm mara moja akajua ni nani alikuwa nyuma yake.

“Dondosha bastola zako friend, Herkan gonga mlango ili tuingie huko ndani nasi tukajiunge kusheherekea kama hao huko wanavyofanya” Kiroboto alisema kwa sauti tulivu nzito. Harken Kalm aligeuka, alipomwona Kiroboto, ndipo uso wake ukageuka kuwa mwekundu na macho yake yakang’aa kwa hasira.

“Shenzi sana huyu, kanipotezea muda wangu, sijui kama nitawahi ndege. Hebu shughulikeni naye miye sina muda wa kuendelea kukaa ndani ya nchi hii nitaelekea uwanja wa ndege, mambo mengine tutawasiliana na muda wowote nenda kaangaliea akaunti yako” Harken Kalm alisema. Aliomba kijana mmoja kati ya wale waliokuwa wanacheza karata mule ndani ampeleke airport.

Jacob aliingizwa ndani akafungwa sawasawa.

“Ndiyo, Frank, niko na Jacob Matata hapa, anangoja zawadi yake ya risasi kama ulivyokuwa umemwahidi” Kiroboto alisema kwa furaha, kasha akasikiliza maelezo kwa muda toka kwa Frank kabla ya kusema.

“Hamna shida nitachukua vijana kadhaa hapa tutaelekea bandarini sasa hivi. Ndani ya saa moja tutakuwa tumehamisha mzigo na kuweka kwenye hiyo meli nyingine na kuondoka” Kiroboto alipomaliza kusema hivyo aliweka simu yake mfukoni. Akachukua vijana sita na kuacha wanne waendlee kumlinda Jacob Matata wakati yeye akielekea Bandarini kama alivyokuwa amesema. Jacob alijua mambo yameshaharibika, kidogo alijilaumu kwa kutokutoa taarifa kwa wenzi juu ya pale alipokuwa amefikia katika kisa hiki hadi dakika hiyo. Alijua kifo chake kingemaanisha kuendelea kufichika kwa yote aliyokuwa amegundua hadi sasa na ingekuwa aibu kwa taifa kama viongozi na wageni mbalimbali ambao kwa muda huo alijua wameshaanza kukusanyika viwanja vya Jangwani tayari kwa shughuli ya uteketezaji wa pembe za Tembo, kama wangeambiwa kuwa men ohayo yametoweka. Alifikiria hasira zikamjaa kifuani. Alimfikiria msichana Regina, alijua bado yuko hai, hasa baada ya kutegua lile bomu alilokuwa amewekewa mara tu alipompata Herkan Kalm, lakini hakuwa anajua yuko wapi kwa sasa nan a hali gani uko aliko.


Ni kweli umati wa watu ulikuwa umeanza kutililika katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam. Ulinzi ulikuwa mkali sana, maana vyombo vya usalama visingeweza kuukwepa ukweli kuwa kitu walichokuwa wanakwenda kukiteketeza hapo kilikuwa na thamani kuwa hivyo si ajabu kufikiria kuwa kuna mtu au kundi la watu mahali Fulani ambao wangetaka kujaribu bahati yao. Hivyo huyu alikuwa na redio ya upepo akiongea, huyu yeye alibeba kamera yake kubwa tayari kuchukua tukio moja kwa moja kwa niaba ya kituo chake cha televisheni, yule yeye alikuwa na bendera yake ya chama na nguo zilizoonyesha chama chake, lengo ni kuonyesha kuwa chama chake kinaunga mkono suala hilo. Watangazaji wa redio nao walikuwepo wakijaribu kuelezea kwa undani ili mradi kuhakikisha kuwa yeyote ambaye hakuwepo kwenye viwanja vya Jangwani aweze kupata nini kilikuwa kikiendelea japo kwa kupitia matangazo ya redio au televisheni.

Huyu yeye alikuwa amevaa sare zake za polisi, alikuwa amechoka kiasi kuwa hata radio yake ya upepo ilipokuwa ikiongea ktaka maelekezo toka kwake hakuwa na muda wala hamu ya kutoa hayo maelekezo. Wiki ilikuwa imekatika tangu pale alipokuwa amekabishiwa kazi ya kuongoza kikosi maalumu cha cha kufuatilia tukio la kutoweka kwa viongozi waandamizi wanne huku wawili wakiwa wameuawa katika mazingira yanayoonyesha kuwa muuaji na mteka alikuwa ni yule yule. Kifo cha mheshimiwa Mondia kilikuwa kimeongeza uzito wa kazi yake, hivyo wakati watu wengine wakiwa katika hati hati ya kuhakikisha usalama wakati wa zoezi la uchomaji wa meno ya Tembo, kamanda Tiko naye alikuwepo eneo hilo, ila akili yake ilikuwa imekufa ganzi na matendo yake yote yalikuwa yameshikwa na kigugumizi. Nyota zake begani ndizo zilizomtofautisha na raia wa kawaida lakini matendo yake hayakuwa na tofauti yoyote na raia wa kawaida. Hakuwa na mpango, hakuwa na lengo na wala hakuwa na wajibu wowote uliokuwa unamsumbua. Haikuwahi kutokea hapo kabla yeye kupewa kazi maalumu halafu ndani ya wiki nzima akawa hana fununu wala chochote cha kuonyesha kuwa kuna maendeleo kwenye upelelezi wake. Kifo cha Mondia ndicho kilichomfanya atake hata kujiuzulu kazi yake. Hivyo alikuwepo tu pale jangwani akiwa kama mtu aliyeshindwa, japo vijana wake wa kazi walikuwa hakomi kumpigia simu ya rediao ya upepo kumwomga ushauri kwa hili na lile na kumshirikisha mambo kadhaa, lakini ndani yake alikuwa ameshakufa moyo.

Kadiri muda ulivyokuwa ukiyoyoma ndivyo watu walivyozidi kufurika katika viwanja vya Jangwani. Hatimaye gari za wakubwa mbali mbali zilianza kuwasili. Wawakilishi wan chi marafiki na mashirika marafiki nao wakaanza kuingia. Uwanja ukanona na kila mmoja sasa akawa anangoja muda muafaka ili tukio lifanyike.

Mjadala mkali ulikuwa unaendelea kati ya viongozi hawa.

“Tukisema tunahairisha bila kutoa sababu tutaonekana wababaishaji sana” Huyu alisema.

“Sasa unadhani katika mazingira kama haya tutatumia rugha gani, kwa vile hata mkuu mwenyewe anajua tuseme amepata dharula kwa hivyo itafanyika siku nyingine itakayo pangwa” Huyu naye alitoa maoni yake

“Jamani lazima mjue kuwa dunia ya sasa hamna siri, kesho tu mtakuta kwenye vyombo vya habari duniani kote kuwa meno ya Tembo yalikuwa yameibwa. Hivyo ni bora huo ukweli tukautoa siye kuliko kusubiri utolewe na watu wengine, jambo ambalo litaoneka kuwa tunaficha jambo. Watu wenye nia mbaya na siye wataitumia hiyo kutupaka matope zaidi, hivyo bora kusema kweli wakati huo huo tukiongeza juhudi za kutafuta zilipo hizo pembe” Huyu alisema huku akiwa anafuta jasho japo chumba walichokuwa wakitumiwa kilikuwa na mashine kali ya kupoozea hewa.

“Duuuh miye kwa kweli nashindwa hata nitoe ushauri gani, haya ni mambo ya aibu sana. Najua hata mkuu hatuelewi kabisa, na najua lazima kuwa watu miongoni mwetu wanahusika na hili jambo. Inauma sana kuona jambo hili linatokea katika mazingira kama haya. Hii ni sawa na taulo kuanguka mbele ya mama mkwe” Alisema huyu mheshimiwa mwingine.


Wakati wakubwa hao wakiwa katika wakati mgumu wa kutafuta namna ya kuuleza umma kile kilichokuwa kimetokea, kwa hawa mambo yalionekana kuwanyookea. Kiroboto alikuwa kwenye moja ya vyumba vya meli hii. Hii ni meli ya dharula ambayo Frank alikuwa ameitafuta baada ya kugundua kuwa Jacob Matata alikuwa imeihujumu ,meli ambayo tayari walikuwa wameshapakia makontena mawili yaliyokuwa na meno za Tembo. Hivyo alikuwa akisimamia zoezi la kuhamisha makontena toka kwenye meli ya awali na kuweka kwenye meli nyingine.

Herkan Kalm yeye alikuwa anaelekea uwanja wa ndege, alikuwa ameshaazimi kusafiri kwenda nchi yoyote ile kama takuta ndage aliyokuwa amekusudia kusafiri nayo imeondoka. Hakutaka kukaa tena Tanzania. Kwa sababu ya kile kilichokuwa kinakwenda kufanyika viwana vya Jangwani, magari yaliyokuwa yanatoka Mbagala, yalishindwa kuingia huku Tazara kwa vile kulikuwa na msongamano wa magari mengi yaliyokuwa yakiitafuta ubongo kwa ajili ya kwenda Jangwani. Herkan Kalm pia akajikuta amekwama kwenye huo msongamano.


Jacob aliinua macho yake, akatazama saa iliyokuwa ukutani, ilikuwa ni saa saba kasoro dakika tatu. Alijua ilikuwa imebaki takribani saa moja ili shughuli ya pale Jangwani ianze, ilikuwa wazi kuwa muda huo hakutakiwa kuwa amefungwa na kutulia kama ambavyo alikuwa ndani ya chumba hicho. Alifikiria kila mbinu kuona kama angeweza namna ya kujiokoa lakini hakuweza kuambulia chochote. Wale vijana wanne waliokuwa wameachwa hapo ndani walikuwa wamesimama kwenye kona nne za kile chumba wakiwa wameshikilia Bunduki zao aina ya SMG zenye kiwambo cha kuzuia sauti, hawakuwa wakiongea wala kujitingisha. Hata pale Jacob alipojaribu kuongea hili na lile, wao walimwangalia tu.

Saa Saba na dakika kumi na sita kulisikika kama kishindo mlangoni. Wale walinzi walisikia pia, mmoja wao akatembea hadi mlangoni, alifungua mlango wa chumba walichokuwepo, akatoka nje kuangalia nini kilikuwa kinaendelea. Zilipita dakika kadhaa yule jamaa aliyekwenda nje hakurudi. Wa pili akaamua kwenda, baada ya dakika tatu alirejea. Aliporejea macho yake yaligongana na Jacob, Jacob akatabasamu. Badala ya kwenda kwenye kona aliyokuwa amesiama, jamaa alimimina risasi na kuwamaliza wale walinzi wawili waliokuwa wamesalia mule chumbani.

“Asante Kefa, ulijuaje niko huku? Jacob Matata alishukuru huku akiuliza. Pindi mtu huyu alipoingia tu na macho yao kugongana Jacob alishamtambua kuwa ni Kefa mmoja wa wafanya kazi wenzie toka ofisi fukuzi.

“Usinishukuru miye, mshukuru Mud maana ndiye aliyetuelekeza hapa na pia kutusaidia kumkamata Herkan Kalm amgaye alikuwa anaelekea uwanje wa ndege kwa ajili ya kukimbilia nje ya nchi” Kefa alisema huku akiwa anamalizia kumfungua Jacob Matata. Alimkabidhi Jacob silaha. Kidogo Mud akaingia huku akiwa anatembea kishabiki shabiki. Alikuwa najisikia raha kuona hatimaye ameweza kufanya jambo la maana.

“Hatuna muda wa kupoteza, mutanisimulia baadaye ni jinsi gani Mud aliweza kupajua hapa na kujua kuwa Herkan Kalm alikuwa anatoroka. Kwa sasa tujiandae kumsubiri Frank ambaye atakuwa hapa muda wowote toka sasa” Jacob alisema huku akiwanza kuzikusanya maiti zilizokuwa humo ndani.

“Kwa hiyo kila mlinzi aliyetoka kuja kuangali kunani, ulimdungua siyo? Jacob alihoji

“Yeah, kila aliyetokezea nilivunja shingo lake, baadaye nikaona yule mwingine angeingiwa na wasiwasi na kukusababishia matatizo hivyo nikaivua nguo maiti moja nikavaa miye ndipo nikaingia na kuwamaliza wale wawili waliokuwa wamesalia ndani” Kefa alisema huku wakiwa wameshamaliza kuzirundika maiti katika chumba kimoja.

“Frank atakuja hapa muda si mrefu toka sasa, bila shaka hivi tunavyoongea atakuwa amekaribia hapa. Miye nitakuwa upande wan je wewe utakuwa upande wa ndani. Kwa vyovyote vile wakati wa kuingia ndani atawatanguliza mateka, mateka wote wakishavuka mlango kuingia ndani, miye nitamshitua kwa hivyo tutaanza mchezo. Wewe utawachukua mateka wowote atakaokuwa amekuja nao na kuwaruhusu kutokea mlango wa nyuma. Mud aliniambia anajua kuendesha. Mud utalisogeza gari upande ule wa nyuma, mateka wakishakuja tu wewe utaondoka nao hadi ofisini kwetu. Bila shaka kwa sasa unapafahamu ofisini kwetu?

“Ndiyo Bro” Mud alijibu huku akivuta vuta vindevu vyake kwenye kidevu. Mara wakasikia mlio wa gari likija upande ule.

“Haya kila mmoja nafasi yake!!! Mud pitia mlango wa nyuma usiwepo kabisa maeneo haya!! Jacob alipiga kelele. Wote wakatawanyika. Dakika chache baadae wakasikia gari hiyo ikiwa inapiga breki mbele ya jumba hilo. Jacob alikuwa amejibanza seemu ya upenuni jirani kabisa na ulipokuwa mlango wa kuingia ndani ya nyumba. Mwanzoni alipata wasiwasi kama lango kuu lingekuwa limefungwa maana bila shaka Frank kwa wadhifa wake angesubiri kufunguliwa lango na hapo ndipo kasheshe ingeanza. Hofu ya Jacob Matata ilikuwa ni kuhatarisha maisha ya mateka yeyote ambapo aliamini mmoja wao angekuwa Regina wake. Alipoona kuwa lango lilikuwa wazi moyo wake ulitulia. Wa kwanza kushuka kwenye gari alikuwa Regina, baadae akafuatiwa na wanaume wengine wanne, ambao Jacob aliwatambua mara moja kuwa ni waheshimiwa ambao wamekuwa wakitafutwa na polisi usiku na mchana. Jacob alimwangalia Regina ambaye alionekana kudhoofu na kukata tamaa. Moyo wake uliingiwa na uchungu mkuu kuona kiumbe anachokipenda kama kile kikiwa katika mikono ya watu wale katili. Baada ya dakika chache Frank alishuka akiwa hana silaha yoyote. Kwa kudadilia Jacob aliona kuwa Frank anaweza kuwa kati ya miaka atobaini hadi arobaini na tano, alikuwa ni mtu aliyejengeka kimazoezi, tembea yake na tazama yake ilionyesha fika kuwa alikuwa mtu wa kazi. Walitembea kuelekea mlango ambao Jacob alikuwa jirani nao, kama alivyokuwa amesema Jacob Matata, mateka walikuwa mbele halafu yeye Frank alikuwa nyuma yao. Wakati mtu wa mwisho akiwa anaingia ndani Jacob alikuwa ameshanyata hadi jirani kabisa na alipokuwa Frank, huku mkononi akiwa ameshikilia kopo moja bovu bovu. Mtu wa mwisho alipokuwa amepotelea ndani, Jacob alirusha lile kopo upande wa kushoto wa alipokuwa amesimama Frank wakati yeye Jacob alikuwa yuko sehemu iliyoko upande wa kulia. Kwa kasi sana Frank aligeuka upande lilikokuwa limetua lile kopo wakati huo huo Jacob akaachia teke kali la mguu wa kushoto, lakini Frank alikuwa mwepesi zaidi alikwepa, kasha yeye akaachia teke kwa kutumia mguu wa kulia, Jacob aliinama likapita na kuukumba mlango, mlango ule wa mbao ngumu ukavunjuka. Frank ariruka hewana na kujisogeza nyuma ili kujipa nafasi ya kukabiliana vema na Jacob Matata.

“Nilikuwa na hamu sana ya kupambana na wewe, maana nadhani mara nyingine wamekuwa wakikupa sifa kwa vile umekuwa ukipambana na wapinzani dhaifu” Frank alisema hukua kiwa amejipanga tayari kwa mpambano. Jacob hakujibu kitu. Frak alikuja kwa kung fu mbili na alipokuwa kuwa karibu zaidi na Jacob aliachilia karete moja safi sana, Jacob akayumba. Frank akamufuata kwa pupa, likawa kosa, Jacob alijifungua na kumnyoosha Frank kwa Teke la tumbo, Frank akaenda chini. Jacob hakumfuata, alimsubiri anyanyuke, kuona hivyo Frank akajua anapambana na mtu aliyeiva, akabadili mbinu, akaachia mapiko matatu ya kama ya ndege tai, moja likamwingia Jacob, kuona hivyo nay eye akaachia ngumi – shoka, ikampata Frank shingoni. Wakati hajaamua bado Jacob alikuwa ameshamparamia kwa vifuti vitatu vya nguvu ambayo viliuchana uso wa Frank na kuacha damu zikiwa zinamtoka puani na mdomoni. Hasira zikampanda Frank, akamparamia Jacob, ambaye tayari alishagundua kuwa mpinzani wake alikuwa amepandwa na jazba. Hivyo alimsubiri tu afanye kosa kama hiro, Jacob alimkwepa Frank, halafu akamtandika teke kali la usoni ambalo halikuubakiza uhai wa Frank, alikoroma kisha akakauka.

“Mchezo mzuri bosi” Kefa alisema

“Ala kwa hiyo ulikuwa unaangali sinema siyo? Jacob alisema huku akiingia ndani.

“Mateka waliookolewa wako wapi? Jacob aliuliza

“Wako huko nyuma” Kefa alijibu kasha wakaelekea huko nyuma

“Jacoooooooob!!!!!!!!!!!!!!! Regina aliruka kwa furaha alipomwona Jacob akija kwenye gari walilokuwepo.

“Reginaaaaa! Jacob alisema wakati Regina akiwa anatua mwilini mwake kwa kujirusha. Alimdaka na kumzungusha juu juu. Wakati huo huo Regina akawa analia kwa Sauti.

“Usilie Regina, hatimaye niko hapa, tuko salama”

“Jamani Jacob nilikuwa nimeshakata tamaa ya kukuona tena!!!! Regina alisema kwa furaha kasha wakabadilishana ndimi. Wengine wakabaki kuwa mashuhuda tu. Mud alivyoona hali hiyo akaweka mikono kichwani.

“Kefa, hawa waheshimiwa wakabidhiwe kwa polisi, wasihojiwe wala kufanywa jambo lolote hadi pale watakapopata maelekezo ya ziada toka kwangu. Huyu binti atunzwe sehemu salama na apatiwe huduma zote muhimu za kwanza. Chakula, nguo, mapumziko. Nadhani unanielewa Kefa, sina haja ya kusema zaidi. Jacob alisema huku akimkonyeza Kefa.

“Tutakutana bandari ya Dar es salaam, maana mchezo ndiyo unakwenda kuishia pale. Mwambie Bi. Anita amtaarifu mkuu kuwa wasihairishe shughuli za uteketezaji wa meno ya Temo. Asimwambie zaidi na wala hatuhitaji polisi eneo lile” Jacob alisema huku akiwa natembea kuondoka eneo hilo na kwacha Kefa, Mud, Regina na wale waheshimiwa wanne wakiwa wanamwangali.

“Nooo Jacob, kama unakwenda kupambana na Kiroboto, name nataka twende wote, kama kufa tufe wote!!!!! Regina alisema huku akichomoka mbio kuelekea kule alikokuwa akielekea Jacob.


Saa saba kasoro dakika kumi na nne, mplelezi Jacob Matata aliwasili kwenye geti kuu la kuingilia Bandarini. Kwanza alitaka kupitia lango kuu kuingia dani, lakini sauti nyingine ikamwambia hiyo isingekuwa busara. Mara nyingi Jacob Matata anaposikia sauti kama hiyo hutii na kuifuata. Akatembea kurudi nyuma upande huu ziliko ofisi za Sea express na Azam express. Hapo alijigfanya kama anayetaka kusafiri, huku macho yake yakiwa yameelekezwa baharini zilikokuwa meli nyingi kubwa za mizigo. Hakuchelewa kuiona meli iliyokuwa na makontena mawili, ilikuwa imeegeshwa sehemu ya nje kidogo toka kwenye msongamano wa meli nyingine. Hakuwa na njia nyingine salama ya kuweza kufika mahali ile meli ilikuwepo zaidi ya kuogelea. Hiyo haikuwa shida kwake, maana alikuwa na uwezo wa kuogelea toka ksiwa kwenda kisiwa kingine, ndiyo maana huitwa makomandoo.

Dakika tano baadaye alikuwa ameshaifikia ile meli, kwa vile alikuwa ameihujumu meli ya kwanza Jacob alitegemea kukutana na ulinzi mkali zaidi. Alijishikiza pembezoni mwa meli hiyo huku akijaribu kutafuta sehemu ya kuibukia na kuingia ndani. Alizunguka ile meli akiwa ndani maji bado, hakuwa anaogelea bali alikuwa ameshi upido wa meli kwa chini na hivyo alisogea upande atakao kwa kujivuta. Ajivuta hivyo hadi alipofika sehemu ambayo kulikuwa na Kamba inaning’inia. Jacob alijaribu kuivuta ile Kamba, ilikuwa ngumu, akahisi itakuwa imefungwa kwenye moja ya vyuma vya juu. Alipotaka kuitumia ili kupanda apande wa juu wa meli, wazo jingine likamkataza. Hakutaka kuamini kuwa ile Kamba iliachwa kwa bahati mbaya. Hakuitumia, akaendelea kuzunguka ile meli akiwa ndani ya maji. Alipofika sehemu ambayo ile meli ilikuwa imepakana sana na meli nyingine hapo akachomoa mfuko wa karatasi toka kwenye moja ya mifuko iliyokuwa kwenye koti lake. Alitoa gloves maalumu akazivaa mikononi, kasha akagusa chuma mkono ukanata. Gloves hizo huwezesha kiganja cha mvaaji kunasa kwenye chuma, mbao au sehemu ya ardhi ngumu kama jiwe na ukuta wa simenti.

Aliibuka juu, aliangaza macho ile sehemu ya juu ya meli hakuona mtu. Kwa hadhari kubwa akanyata hadi upande mwingine wa kontena. Hapo akatulia na kusikilizia, hakukuwa na ishara za kuwepo mtu yeyote. Alitembea hadi upande ambao kungekuwa na mlango wa kuingilia upande wa ndani wa meli toka upande huu wa sehemu wazi ya kuweka mizigo. Ndyo hakuchelewa kuuona mlango, alinyata hadi penye mlango. Alinyoosha mkono ili aujaribu mlango, kabla hata hajafanya hivyo akasikia sauti nyuma yake.

“Fungua mlango na utembee mbele kuingia ndani, ujanja wowote wala hatuna haja na wewe! Ilikuwa sauti isyo na hata chembe ya masihala. Hakubisha akafungua mlango na kupiga hatua kuingia ndani, hata hivyo alihitaji kuingia ndani, alitembea taratibu huku kwa makini sana akiwa anahesabu hatua za mtu aliyekuwa nyuma yake. Alipomaliza kushusha ngazi za kuingia upande wa vyumbani wa meli hiyo yule jamaa bado likuwa anashuka, Jacob akajiangusha chini, jamaa kuona hivyo akaona aruke ili ambane Jacob pale chini, akakuta patupu, alipotaka kusimama, Jacob tayari alikuwa nyuma yake, risasi tatu zikakifumua kichwa chake. Kutokana na vile vishindo vilivyotokea wakati anakamuana na huyo jamaa, aliweza kusikia wengine wakikimbia kuja upande aliokuwepo. Jacob alipanua miguu akajibana kwenye dari ya juu ya kile kijinjia alichokuwepo. Hivyo walipopita watu wanne yeye alikuwa juu yao ila hawakuweza kugundua. Walipokuwa wameshampa mgongo, alijiachia toka pale juu, kishindo cha kutua chini kiliwafanya wageuke, lakini walikuwa wameshachelewa risasi zilizokuwa zimetoka kwenye midomo miwili ya bastola za Jacob Matata ziliwaacha wakianguka chini kama mchicha. Kabla hata hajageuka alishitukia anapokea teke kali la mgongoni, akaanugia upande wa mbele na kujibamiza kwenye chuma. Kabla hajainuka akaona Paka akipita mbio kuelekea upande mwingine, mara moja akajua anpambana na nani. Aliruka kwa kujipindua huku teeke la mauti lililokuwa limelenga paji lake la uso likimosa na kutua chini. Alijigeuza hewani na kumkumba Kirobot wote wakaenda chini! Haikuchukua hata sekunde kila mmoja akawa ameshaamka toka pale chini kwa staili ya aina yake.

Hakuna aliyemuongelesha mwenzie, Jacob akajari kwa shoto lake, Kiroboto akaridaka na kulinyonga kwa lengo la kumwaga chini Jacob, Jacob akajikunja kama anayekwenda chini halafu akajipindua kwa kifuti cha mguu wa kushoto kilichompata sawasawa Kiroboto kidevuni. Kiroboto aliachia ngumi mbili ambazo zote zilimpata Jacob tumboni, ambaye akaenda chini kwa maumivu. Kuona hivyo, Kiroboto akaruka upande wa pili na kumpa Jacob mgongo ili ajigeuze na kumpa Jacob ile stahili mbaya zaidi ya judo iitwayo kitaalamu Kano Jigoro’s Kodokan. Hilo lilikuwa kosa, kwani kasi yake haikuweza kuzidi kasi ya macho ya Jacob, ambaye kwa haraka sana aliweza kuuona mgongo wa Kiroboto, hakutaka kupoteza nafasi hiyo ya pekee, alijipindua na kupiga teke aina ya tick tack lililotua sawasawa kwenye uti wa mgongo wa Kiroboto na kuuvunja. Kiroboto alitoa mguno wa maumivu. Jacob alisimama kwa kasi akamtandika Kiroboto viganja vingine viwiwili kwenye paji la uso Kiroboto akalegea. Mara yole Paka wa Kiroboto “Amazon Cat” akatokea na kutaka kupita eneo hilo, Jacob Matata akamdaka shingo lake kwa mkono wa kushoto, kasha akaanza kuliminya koo la huyo paka taratibu kama mtu anayekamua Limao. Paka alitoa mlio wa ajabu huku macho yakiwa yamemtoka. Kiroboto hakuwa na la kufanya, kuvunjwa uti wa mgongo na vile vipigo vya mwisho vya viganja viwili vilimmaliza kabisa.

“Niiue tu Jacob Matata, hata hivyo kitendo cha kupigwa kiasi hiki na mwanaume mwenzangu ni kama nimeshakufa tayari. Kama unaona shida nipe bastola nijitie risasi mwenyewe” Alisema Kiroboto amabye alikuwa hoi baada ya kipigo kile kizito.

“Sikiliza Kiroboto, Mbao hata uichonge vipi haiwezi kukata nyama. Kuna njia nyingi za kupata utakacho lakini njia ya uovu kamwe haimpi mtu atakacho, zaidi sana huchukua hata kile alichonacho. Uliyokuwa umeyapata kule Sierra Lione yalikuwa yanatosha, lakini hukutosheaka ukaona bora uisaliti hata nchi yako mwenyewe, ona sasa hata kile kidogo ulichokuwa nacho hakitokuwepo tena. Masaa machache yajayo fedha zote zilizo katika akaunti zenu za benki zitachukuliwa na kupewa maskini na nyingine kupelekwa kwenye shughuli mbali mbali za kimaendele” Jacob alisema hayo huku akimsogerea Kiroboto. Alipofika pale alipokuwa amelala, aliweka bastola yake kando.

“Herkan Kalm tayari yuko kwenye mikono ya dola ila wewe sitokupeleka huko na wala sitakuua kwa risasi, wewe nitakuua kwa mkono wangu mwenyewe” Jacob alisema kasha akakishika kichwa cha Kiroboto, akakizungusha na kuivunja shingo yake. Kabla hata hajakiachia kile kichwa mlango wa chumba alichokuwepo ulifunguliwa, alijirusha pembeni huku akiwa ameinyakua bastola aliyokuwa ameiweka chini wakati. Mara akamwona Kefa akiwa kasimama mlangoni bastola mbili zikiwa mikononi kwake tayari kwa lolote.

“Kazi nzuri Bosi” Kefa alisema huku akifutika bastola zake kiunoni.

“Kefa hatuna muda wa kupoteza, bila shaka umeshafanya utaratibu wa gari mbili za kubeba hizi kontena na kuzipeleka jangwani? Jacob alisema huku akiwa ameshasimama.

“Ndiyo bosi, gari ziko tayari na madereva tutakuwa mimi na wewe” Kefa alijibu

“Nadhani tuondoke, maana zimebakia dakika arobaini shughuli ya uteketezaji wa meno ya Tembo uanze. Nilimwambia Bi Anita amwambia Mkuu wan chi kuwa waendelee na taratibu na mzigo utakuwa pale kwa wakati. Hivyo najua macho ya viongozi wote yako barabarani yakitarajia kuona mzigo ukiingia.


Na kweli japo muendesha tukio alikuwa akipamba kwa maneno ya mbwembwe na kejeli nyingi zilizoonyesha kuwa nchi ilikuw imedhamiria kukomesha vitendo vya ujangili wa vipusa lakini viongozi wote waliokuwa pale walikuwa kama waliokalia kaa la moto wakiwa juani. Muda wote walikuwa wakiangaza macho yao kuona kama kuna jipya lingetokea. Mkurugenzi wa ofisi fukuzi, Bi Anita pia alikuwa kwenye wakati mgumu sana, alikuwa ameshamwambia Rais kuwa kontena za meno ya Tembo zingekuwa pale muda wowote, lakini kadri dakika zilivyokuwa zikiyoyoma ndivyo mshaka yake yalivyokuwa yakiongezeka. Hakuna mtu aliyekuwa akimuamini katika ofisi yake kama Jacob Matata, kama ingekuwa ni kumuangusha hii ingekuwa mara ya kwanza. Wakati akiwa anafikiri hayo, mara gari mbiligubwa za mizigo zipiga kona na kuanza kuingia ndani ya eneo la viwanja vya Jangwani. Polisi, Viongozi, wanajeshi wote waliokuwepo mahali hapo walisimama, kuona hivyo umati wa watu waliokuwa hapo nao walisimama. Magari hayo yaliendeshwa taratibu kuelekea sehemu ambayo shughuli ya uchomaji meno ya tembo ilikusudiwa kufanyika.

Gari hizo zilipofika lile eneo ambalo kulikuwa na kuni nyingi na maguduria ya mafuta, zilisimama na mara zikawa zimezungukwa na wanajeshi wenye silaha nzito nzito. Zilipita sekunde kadhaa hukugari hizo zikiwa zimezungukwa namna hiyo na hakuna yeyote aliyeshuka toka ndani ya hizo gari. Baadaye alishuka kijana mmoja mkakamavu, mrefu kiasi, mweusi japo si ule weusi wa giza, alikuwa na mwili wa mazoezi, ukimwangalia tu kama wewe unajua kusoma miili ya watu utatambua kuwa alikuwa na umri kati ya miaka thelathini na tano hadi arobaini. Nguo zake zilikuwa zimechanika chani na kutapakaa damu, huku akiwa na majeraha na michubuko kadhaa iliyoonekana dhahiri mbele ya wanajeshi hawa ambao sasa walikuwa wakimshangaa.

“Jacob Matata” Bibi Anita alinong’ona.

Jacob alimama hivyo kwa sekunde kadhaa, alipoanza kutembea kuelekea lilipokuwa gari jingine ambalo lilikuwa limeendeshwa na kefa, ndipo wanajeshi wale walipokumbuka kupiga saluti na hiyo ilifanyika baada ya kuona mkuu wao wa kazi anampigia saluti Jacob Matata. Jacob hakuwa na muda wa kujibu saluti zao, alifika pale ilipokuwa imeegesha gari iliyokuwa ikiendeshwa na Kefa. Alifanya ishara Fulani, Kefa akateremka. Wote wawili wakafanya ishara ya kuinama kasha wakaanza kuetembea kuelekea upande waliokuwa wamekaa raia wa kawaida.

“Tumemaliza kazi comrade, yaliyobaki hayatuhusu, tuwaachie wenyewe waendelee! Jacob alisema, huku wakiwa wanatokomea kwenye umati wa watu. Waandihi wa habari waliwakimbilia ili kuwahoji, lakini si Jacob wala Kefa aliyejibu lolote.


Huku mwili wake ukiwa umelowa jasho, Jacob alielekea kwenye gari aliyokuwa ameelekezwa na mkuu wa Ofisi Fukuzi kuitumia pindi akitaka kuondoka eneoo hilo. Mara akatokea Mud, akiwa na tabasamu lake la kishabiki.

“Ooooh Mud mambo? Jacob Matata alimsalimia Mud baada ya kukaribiana

“Nzuri kaka Jacob! Mud alijibu kwa mkato kama aliyekuwa akisubiri swali toka kwa Jacob

“Ennnhe Mud hebu niambie ulijuaje kuwa nilikuwa nimeshikwa mateka kule Mbagala? Jacob aliuliza huku akimvutia pembeni kupisha gari la askari wa fanya fujo uone waliokuwa wakiingia hapo kwa fujo.

“Angalia wasije kukuvunja hao bwana mdogo, maana wao ndiyo wababe hapa” Jacob alimwambia Mud kisha wote wakacheka.

“Uliponipigia simu muda ule kuulizia kama Herken Kalm alikuwa ametoka au la, na nikakujibu kuwa alikuwa ametoka kama dakika tano nyuma, nilipata hisia kuwa nifuatilie wapi alikuwa akielekea. Nilikodi bodaboda na kuelekea kivukoni, nilikuwa na hakika kuwa lazima angetumia hapo kama alikuwa anaelekea mjini. Kulikuwa na kila dalili kuwa alikuwa anaelekea mjini na alikuwa na safari maalum. Nilipofika kivukoni niliiona gari yake ikiwa miongoni mwa gari zilizokuwa kwenye foleni zikingojea kuvuka. Basi name kwa kujificha fiche nikakata tiketi na kungoja kuvuka. Kivuko kilipofika, gari ya Herkan Kalm ilikuwa miongoni mwa gari zilizoingia kivukoni. Name nikaingia kivuko ila nikiwa katika hali ya kuhakikisha kuwa Herkan Kalm hanioni. Wakati tukiwa tunasubiri kivuko kuanza safari, nikiwa naangaza angaza macho, nikakuona ukiwa umebana upande wa nyuma. Nikajua hapa kuna mchezo, unajua miye napenda kufuatilia visa na mikasa. Basi nikakuona pindi unakwenda kwenye gari ya Herkan Kalm. Sikujua nini kiliendelea mule ndani ya gari. Kivuko kilipofika upande wa pili, nikakodi bodaboda na kumwomba awafuatilie mliko kuwa mnakwenda, nilikuwa na hamu ya kjua mwisho wa sinema yenu. Hadi mnafika Mbagala na kuingia kwenye lile jumba miye nilikuwa nimebana kwenye miti naangalia sinema nzima. Dakika chache tu baada yaw ewe kuingia aliingia mtu mwingine aliyekuwa na bastola huku akiwa kabeba paka mkononi. Nikahisi wenda ulikuwa umezungukwa na Herkan Kalm alikuwa amekupeleka mtegoni. Basi, nikachukua zile namba ambazo ulinipa na kuniambia kuwa kama nina jambo nataka kukuambia na ukawa hupatikani kwenye simu nipige kwenye hiyo namba nitawapata watu wa ofisini kwako. Nikapiga hiyo namba na kuwaeleza tukio zima na wapi nilikuwa wakati huo. Haikuchukua muda mrefu watu wa ofisini kwenu wakawa wamekuja. Muda mchache tu mara baada ya yule mwenye Paka kuingia kwenye ile nyumba ambayo wewe na Herkan Kalm mlikuwa mmeingia, nilimwona Herkan Kalm akitoka kwa haraka na kuondoka na ile gari yake mliyokuwa mmeitumia kwenda pale. Hilo nalo nikawataarifu watu wa ofisini kwako. Wakaniomba namba za gari na aina ya gari, nikawaambia. Baada kama ya dakika kumi, nikamwona yule mtu aliyekuwa ameingia na Paka naye akiwa anaondoka huku amefuatana na vijana wengine sita.

Watu wa ofisini kwako walifika na mpango wa kuingia ndani ukafanyika na ndiyo tukawa tumeweza kukuokoa” Mud alisimulia huku akonyesha kufurahia jambo alilokuwa amelifanya.

“Sikiliza Mud, najua Herkan Kalm alikuwa amekuachia nyumba na hati yake, gari mbili na kadi zake, na umesema kuwa alikupa hela za dola na shilingi nyingi. Nenda kaanze maisha yako, miye nitahakikisha haupati matatizo yoyote na vitu ulivyopewa havitaguswa na kuhusishwa katika mkasa huu, hiyo itakuwa kama kifuta jasho chako. Kumbuka mara baada ya hapa usimsimulie mtu yeyote mkasa huu wala usijihusishe na uhalifu wa aina yoyote. Usipofanya kama navyokuambia lazima utaishia matatizoni. Asante sana kwa ushirikiano wako katika kazi hii, miye nakwenda, Regina ananisubiri mahali” Jacob alisema halafu wakakumbatiana na Mud kwa sekunde kadhaa. Baada ya hapo alipiga hatua kama tano kabla ya kugeuka na kumwangalia Mud ambaye bado alikuwa amesimama akimwangalia Jacob Matata alivyokuwa akitembea kikomandoo.

“Kefa ataleta ile gari ambayo Herkan Kalm alikuwa akiitumia kwa mara ya mwisho, nayo ni halali yako Mud” Jacob alisema kasha aminya jicho moja. Mud hakujibu ila akaonyesha ishara ya dole gumba. “Kweli kinachodondokea kwenye tope hakidundi na Mshkaki hauchomwi kwa jiko a gesi” Mud alijisemea wakati macho yake yakiwa yanalisindikiza gari alilokuwa akiendesha Jacob Matata.


Hata kabla hajagonga mlango wa chumba ulishafunguliwa, Regina alisimama mlangoni akiwa amevaa gauni yake ya chumbani ambayo ilikuwa nyepesi kiasi cha kuweza kuonyesha maungo yake ya ndani. Waliangaliana kwa sekunde bila kuongea neno, Jacob Matata aliutalii mwili wa Regina, kisha akashitukia tu Regina ameshamvaa maungoni na kumkumbatia kwa nguvu.

“Ingia ndani Jacob, nimekuwa nikikusubiri wewe mpenzi, kwa vile nimekuona najua mambo yote yamekwisha isipokuwa hatujamaliza yale ya baina yetu, na muda uliobaki najua ni wangu na wako”Walivutana hata hawakutambua jinsi walivyofika kitandani.

“Ama kweli, ndiyo wajue kuwa japo jogoo anawahi kumka na kuwika hawezi fungua mlango. Wenye nyumba ndiyo tunafungua sasa na jogoo wameishia kuwahi kuamka na kuwika tu! Jacob Matata alisema wakati akiisukuma suruali yake kwa mguu wa kushoto na kuiacha idondoke chini. Hakuwa anaihitaji saa hiyo. Ilikuwa ni kwenye moja ya vyumba vya hoteli moja ya kifahari iliyoko kando kando ya bahari ya Hindi, ambapo Regina alikuwa amehifadhiwa tangu alipookolewa toka kwenye mikono ya Frank. Jacob alimwagiza Kefa kuhakikisha binti huyo anapata mambo safi. Dakika chache baadaye wote walizama katika ulimwengu mwingine ambao Regina alikuwa akiuota kila siku. Ulimwengu usiokuwa na Kificho, Kiroboto, Kipipa, Frank wala Herkan Kalm, ulimwengu wa kufanya na kufanyiwa utakacho.


MWISHO

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment