Jiue Mwenyewe Sehemu ya Nne
KIJASUSI

Ep 04: Jiue Mwenyewe

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Nne

IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE


Simulizi : Jiue Mwenyewe

Sehemu Ya Nne (4)

ONTARIO CANADA

ROBINSON QUEBEC alikuwa kimya katika bustani yake kubwa iliyoizunguka nyumba yake kati jiji la Ontario nchini Canada, sura yake ilikuwa imekunjana kwa hasira. Akashusha sigara yake anayovuta na kukung’uta jivu lake katika kibweta kilichoandaliwa kwa kazi hiyo, kisha akamtazama aliyekuwa mbele yake.

“Tracy!” akaita.

“Yes, Boss!”

“Nilikuwa nikikuandaa kwa miaka yote kwa kazi ngumu na za hatari kama hizi, na zote umenifanyia vizuri kabisa zikapelekea hata ukapata kazi na mashirika makubwa kama KGB na wengine, sasa nataka nikupe kazi moja, hii naweza kuiita ngumu lakini wewe utaipima,” Robinson alimwambia Tracy Tasha aliyekuwa ameketi pembeni yake akisikiliza kwa utulivu sana kila kitu.

“Nakusikiliza,” alisema.

“Nakutuma tena Afrika Mashariki,” Bwana Robinson akatulia akimwangalia Tracy usoni.

“Kazi ileile au?” Tracy akauliza.

“Ndiyo, sasa ukaimalizie,” akavuta tena pafu moja, “mara hii nataka ukaondoe Roho ya rais wa Tanzania, kwani amekiuka makubalino yetu, nasi hatuna budi kutekeleza mkataba wetu,” akarudisha sigara kinywani, “sikia, iwe kwa sumu, kwa ajali au njia yoyote ile wewe ndiye ujuaye la kufanya, hakikisha ndani ya siku chache tu uwe umemaliza kazi na hapo watakaposhtuka juu ya kifo hicho ndipo tutapita nyuma kukusanya tunachotaka,” akamaliza.

“Ok, na vipi juu ya usalama wake? Yaani vikwazo vya kiusalama,” Tracy akauliza.

“Hivi kuna nchi ya Kiafrika ambayo ina usalama wa kukushinda wewe? Tanzania! Ah wapi, wala usiogope, hawana lolote ni kelele za ubahatishaji tu mbona mpaka leo hawajagundua kuwa dereva aliyemwendesha Rais siku ya tukio lililopita alikuwa Breyman?” Robinson akamwuliza Tracy.

“Ok, kesho nitaondoka,” akajibu.

“Sawa, uwende Kesho na ukafanye kazi kikamilifu, George Mc Field yuko pale kukusaidia kwa lolote, usihofu tumejipanga,” Robinson akamweleza.

“Sawa, hilo limepita,” Tarcy akanyanyuka na kubaki wima. Ni mwanamke mzuri kuwa mpenzi au mke wa mtu lakini dunia imembadili kimaisha amekuwa mnyama mbaya kuliko mnyama mwenyewe.

“Sikia Tracy, ulinzi wa Rais umebadilishwa saa chache zilizopita, nimepata hiyo taarifa kutoka vyanzo vyangu. Ameongeza watu wanaomzunguka na kuimarisha maeneo nyeti, hivyo nahitaji utumie weledi wako wa juu kabisa kuifanya kazi hiyo. Ukikamilisha, utajiri wako utaongezeka mara nne,” Robinson akamaliza huku akimshika makalio mwanadada huyo katili, alisahau kabisa kama anaweza kumgeuka na kumtoa roho.

UWANJA WA NDEGE WA

J.K NYERERE-DAR ES SALAAM

NDEGE KUBWA YA LUFTHANSA ilitua katika ardhi ya Dar es salaam, Rubani wa ndege hiyo na wasaidizi wake hawakujua kabisa kuwa wameiletea Tanzania maafa, maafa makubwa.

Tracy Tasha alikuwa wa mwisho kushuka katika ndege hiyo kubwa ya kisasa, hakuwa mgeni na nchi hii, kwa kuwa alishafika mara moja na hii ilikuwa ni mara ya pili. Alikuwa na kijibegi kidogo na mkoba mkononi mwake, akapita eneo la ukaguzi wa hati za usafiri bila tabu akitambulika kwa jina la Naomi Schubety, raia wa Venezuela, mwanafunzi wa chuo kimoja cha afya huko Marekani, John Hopkins.

“Karibu sana!” George Mc Field alimlaki mwanamke huyu, hawakuwahi kukutana, ilikuwa ni mara ya kwanza, Tracy akabaki kimya akimwangalia mtu huyu ambaye sasa alionekana katika mavazi nadhifu, mwenye mwenye ndevu nyingi.

Tracy akatoa noti ya Paundi 100 akamwonesha, na Mc Field akatoa noti ya Shilingi 10000 akamwonesha, hiyo ilikuwa ni ishara ya utambulisho wao ambayo kila mmoja aliambiwa kwa wakati wake. Wakaingia garini na kuondoka kuelekea mjini.

“Umekuja kufanya kazi, siyo?” Mc Field akamwuliza Tracy.

“Ndiyo, ni hilo tu,” akajibu.

“Unapenda kufikia hoteli gani?”

“Aaa yoyote lakini nafikiri ya hali ya kati ingenifaa zaidi,” Tracy akaeleza.

“Ok,” Mc Field akaiacha barabara ya Nyerere na kuichukua ile ya Mandela kuelekea Ubungo.

“Land Mark Hotel, hapa patakufaa siyo?” akamwuliza.

“Yap, pako poa,” akajibu hukua akishuka katika gari. Akaagana na Mc Field kwa miadi ya kuonana usiku wa siku hiyo kwa mipango ya mwisho.

08

CANADA

      ROBINSON QUEBEC alikutana na washirika wake kama kawaida, hii ilikuwa mara tu baada ya kuondoka Tracy kuelekea Tanzania.

“Tumemaliza kazi! Tusubiri matokeo,” Robinson akawaeleza swahiba zake wawili.

“Safi sana, kama Tracy amekwenda, hilo ni amuzi sahihi, mwanamke yule huwa hashindiwi, na wala haogopi kitu, kuua ni starehe yake,” akajibu yule mjumbe mweusi.

“Ndiyo, na wameshakutana na Mc Field, kila kitu kiko sawa, tusihesabu hasara basi tuhesabu faida katika hili,” Robinson akaeleza.

“Sir. Robinson Quebec, uishi milele!” wakamtukuza. Baada ya hapo wakatawanyika wakisubiri kazi ya Tracy ikamilike ili nao wasonge mbele.


REJEA – SHAMBA

“Sasa ipo hivi, almasi za Mwadui hazikuibwa na waziri kama ilivyojulikana mwanzo,” Madam S alikuwa akifanya hitimisho la uchunguzi wa taasisi hiyo, akaendelea “sasa ni nani aliyeiba almasi hizo? Mpaka sasa tuna mtu huyu George Mc Field na nina uhakika hajaondoka nchini, na yeye atakuwa ndiye aliyejigeuza kuwa kama waziri, Amata anamjua huyu jamaa, huyu ni Jasusi mwenye uwezo wa kujigeuza hata akawa mjusi,” akatulia na kuwatazama vijana wake, “sasa tunaingia kazini, asakwe George Mc Field apatikane akiwa anapumua au hapumui, na swahiba zake, wakati huo ufanyike uchunguzi juu ya chanzo cha wizi wa almasi hizi, sote tunaingia kazini, na tutajipanga kama ifuatavyo…”

Kila mtu alibaki kimya, kila mmoja moyoni mwake aliona wazi kuwa haya ni maji mazito mpaka Madam S anahusisha watu wake wote kikazi kwa wakati mmoja, haikuwa kawaida kwa mwanamama huyo, yeye daima alimpa mtu mmoja kazi moja labda itokee inahitaji msaada wa karibu ndipo mngekuwa wawili, hata hivyo bado aligawa kazi pasi na wao kujua kama nani ana kazi ipi. Lakini mara hii wote watano na yeye mwenyewe wa sita, kila mmoja aliona kazi ni kubwa na nzito. Baada ya kushusha bilauri yake iliyojaa sharubati ya embe akafungua kabrasha lake na kuliacha wazi mezani.

“Hali ya Mheshimiwa Rais ni mbaya, amepatwa na presha ya kushuka, sasa dawa yake tunayo sisi kuhakikisha utatuzi wa hili umepatikana, nimeongea naye kasema mabadiliko aliyoyazungumza kayakamilisha katika sekta ya ulinzi wa nchi hivyo msishangae. Sasa nataka tufanye kazi hii kwa kasi ya ajabu kidogo. Kamanda Amata utakuwa mstari wa mbele kabisa ukisaidiwa karibu na Gina katika mapambano, kila anayenukia harufu ya almasi za wizi, awe mkubwa awe mdogo, toa taarifa tumkamate mara moja, na atakayekataa kutii sheria bila shuruti basi we unajua jinsi ya kumtuliza. Scoba kama kawaida, utakuwa makini katika kuokoa na kukamata anayetakiwa kufanyiwa hivyo. Chiba utahakikisha unawaunganisha wote bila kuwapoteza katika mtandao, kunasa mawasiliano ya kila unayemhisi na kuto mwongozo kwao, nikiwa na maana kuwa ofisi yako sasa itaamia hapa au ndani ya gari yako maalumu kwa kazi hiyo wakati mimi na Jasmine tutakuwa hapa kwa msaada wa haraka…” akiwa hajammializa kusema hayo, mara sauti ya simu ya Chiba ikawashtua, akaitoa mfukoni na kuitazama, akawapa ishara ya kutulia.

“Terminal Two,” akawaambia na wote wakatega sikio kwa kuwa aliweka sauti kubwa.

“…Hello…” akaita

“Hello, Terminal Two hapa…”

“Nakusoma, endelea,”

“Kuna mzigo hapa umeingia, nina wasiwasi nao kwa picha ulizonipatia…”

“Ok tuma taarifa zote hapa haraka…” akamwamuru mtu huyo ambaye daima humtumia kunasa watu anaowahitaji. Mtu huyu ana kifuniko ‘undercover’ cha Idara ya Uhamiaji lakini kitengo cha usalama wa Taifa kinachofanya maswala ya utambuzi.

“Copy!”

Chiba akakata simu na kutulia.

“Kumekucha…. Kwa umakini wa huyu kijana lazima aliyeingia ana jambo,” Chiba akasema.

Wakati wakiendelea na mzungumzo, kompyuta ya Chiba ilikuwa imekwishapokea taarifa kutoka uwanja wa ndege, akazifungua na kuprint nakala kadhaa na picha zilizotumwa pamoja nazo.

Picha kumi na mbili za mnato zilizomuonesha mwanamke katika ‘engo’ mbalimbali, mbele nyuma, kutoka juu, usoni kwa karibu kifuani, mgongoni na mazingira mengine, kisha kulikuwa na picha ya mjongeo ambayo Chiba aliicheza kwenye kompyuta kubwa ya ofisini kwa Madam S na wote wakaishuhudia. Mwanamke huyo akipita katika ukaguzi, akitoka mlango wa ‘wanaowasili’ akisalimiana na mwenyeji wake, kisha wakiondoka lakini picha hiyo haikuweza kuonesha mtu huyo kaondoka na gari gani.

Kamanda Amata akazitazama zile picha kisha akampatia Chiba. Chiba akaziweka kwenye kifaa chake. Pamoja na zile ambazo Kamanda alizileta kutoka Afrika Kusini, na zile zilizotoka Ufaransa na zilizochorwa katika tukio la Bunju, kisha kwa kutumia kompyuta, softiwea maalumu akazioanisha ‘crossmatching’ kama ni mtu mmoja au ni watu tofauti. Ndani ya dakika kumi walipata jibu alikuwa ni mtu mmoja hata kama alijibadili namna gani. Softiwea hii iliyotengenezwa na Chiba akishirikiana na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam ilikuwa ikifanya kazi kwa ufanisi wa hali ya juu sana, ikikufananisha pua, macho au maziwa kama we ni mwanamke au ndevu kama we ni mwanaume kwa kuwa waliiaminisha kuwa hata mtu ajibadili vipi kuna sehemu hatoweza kujibadili, hivyo ilitafuta sehemu ambayo ilikuwa na unasaba kisha ikaoanisha kutoka hapo.

Baada ya kupata picha kamili ya mwanmke huyo, akaiingiza katika mtandao wa usalama unaowatambua watu hatari duniani, kwanza alianza na ule wa CIA ambao ulimpa jibu lenye utata, akaingiza kwenye mtandao wa MOSSAD kama unamtambua mtu huyo nao ukaleta majibu kama yale yale baada ya kupitisha kwenye kioo picha zaidi ya 250.

“Shiit!” Kamanda Akang’aka.

Mtandao mwingine wa kijasusi wa KGB nao ukaleta majibu yanayofanana.

Tracy Tasha, raia wa Marekani, mzaliwa wa Jimbo la Arizona, mwenye miaka thelathini na moja, maelezo yaliendelea kumweleza kama muuaji hatari asiyekamatika, anayetafutwa kila kona ya dunia na kila kitengo kiwe cha kipolisi, kijasusi au mashirika binafsi. Ulimweleza kuwa hakamatiki, mitandao mingine ikampa jina la The Devil, wengi walieleza wazi kuwa wamekamata nyayo zake tu lakini mwenyewe hawakumkamata. Mtandao mwingine uliwafanya Madam S na jopo lake kucheka maana ulijitamba kuwa kamera zake za CCTV ndizo zenye uwezo wa kumkamata kila apitapo eneo fulani.

Taarifa zile zilimfanya Madam kushusha pumzi ndefu, akavua miwani yake na kujifikicha jicho la kushoto.

“Tutoe taarifa kwa wadau wanaomtafuta? Maana sisi huyu sio wa kwetu,” Madam S akauliza.

“Hapana, usitoe taarifa kabisa, kwani itakuwa vurugu kubwa hapa, na sisi lazima tumchunguze kwanza kaja kufanya nini, kisha tumuoneshe kuwa sasa kafika mwisho wa maisha yake…” kabla Kamanda hajamaliza kusema hayo Gina akadakia.

“Ningemshauri aandike urithi kama ana watoto,” wote wakacheka.

Waliona baadae kuwa Mwanamke huyo na kama kuna wengine wasakwe kimyakimya bila kelele ili kutowagutusha, hali ya tahadhari ikatolewa kwa watu wa idara ya Usalama wa Taifa kuwa makini na kila wanayekuwa na wasiwasi naye, ulinzi mpya ukaanza kazi mara moja, safu zikapangwa upya, mkuu wa kitengo kile akaondolewa akawekwa mwingine, akatolewa huyu kule akapelekwa kule, huyu na yule wakapelekwa mikoani, yule wa mkoa ule akaletwa huku ilimradi tu kuiweka safu mpya.


Kamanda Amata alikuwa na Chiba wakijadili hili na lile, “enhe nambie Jenny anasemaje?” akauliza.

“Oh, nilisahau, alileta kitu muhimu sana, alileta kadi inayotumiwa kubadili sauti ya mtu, na tumeichunguza ndipo tukapitisha moja kwa moja kwamba waziri hakuusika na ule wizi kwani alibanwa akalazimisha kusema maneno fulani wakati ile kadi ikirekodi na kisha aliyejifanya waziri ndiye akaitumia sauti hiyo,” Chiba akaeleza.

“Lazima tujivunie kuwa na wewe Chiba, ni mtu wa juu sana kwenye hii midude unajua wewe ndiyo huwa unanifanyia mi mambo kuwa mepesi,” wakacheka pamoja.

“Acha Bwana, sasa unataka kumwona Jenny?” Chiba akaanza.

“Mmmm hajaondoka?”

“Hapana, nilimwambia asiondoke mpaka utakaporudi, nimempangia chumba pale Rombo Green View, Sinza, naye amefurahi sana kusikia aonane nawe,” Chiba akaeleza.

“Aaa, wakati mbaya sana huu, unaweza kuwa kitandani na wenzako wanaiangamiza nchi,” Kamnda akajibu.

“Aaaa kaka! Kamanda leo wa kusema hivi! Hivi hivi! Siamini itakuwa umeokoka labda,” Chiba akatania.

JINIA – saa 3:25 asubuhi.

KAMANDA Amata alikuwa katika ofisi ya uhamiaji ndani ya Uwanja wa Ndege wa Dar es salaam sambasamba na Gina.

“Unasema ulimwona,” akauliza.

“Ndiyo nilimwona, akapokelewa na kasisi wa kanisa,” akajibu kijana wa uhamiaji aliyetuma taarifa za Tracy kwa Chiba.

Kasisi wa kanisa, akawaza Kamanda, “haya makanisa nayo yana mambo! Utakuta wanahifadhi majasusi humu humu si’ tumekaa tu,” akaeleza Kamanda, “hukuwaona hata wamepanda taksi gani au gari gani?” akauliza.

“Waliondoka na gari binafsi, Peugeot 404, TX 768 M,” akajibu yule kijana.

“Ok. Asante sana, nitafanyia kazi, tujue kaja hapa kwa nini,”

Kamanda na Gina walitoka eneo la Uwanja wa Ndege na kuliendea gari lao, wakaingia na kuketi, nyuma ya usukani alikuwa Gina. Kamanda akawasha simu na kupiga mamlaka ya mapato Tanzania na kuuliza namba za gari hilo TX 768 M ni mali ya nani. Baada ya dakika kumi hivi akapewa jibu kuwa ni mali ya kampuni moja ya kijerumani inayofanya kazi za kijamii huko vijijini, lakini ofisi yao ipo Dar es salaam, wakatajiwa anwani na mahali ilipo.

“Gina, twende Mtaa wa Mkwepu, plot namba 45C, “ Kamanda akamwamuru na Gina akaondoa gari kama alivyoelekezwa.

Walipofika walipandisha ngazi moja kwa moja mpaka ghorofa ya tatu ya jengo hilo, wakakuta kuna duka kubwa la kuuza vifaa vya maofisini, walipouliza wakaambiwa hao Wajerumani waliamisha ofisi kuelekea mtaa wa Ali Khan Upanga. Bila kusita Gina na Kamanda wakaongoza njia kuelekea huko, haikuwa tabu kuipata ofisi hiyo kwani walipopita tu shule ya Zanaki wakaiona kwa mbele wakaegesha gari, wakateremka kuingia katika nyumba hiyo yenye uzio mkubwa wa miba. Mlangoni palikuwa na mlinzi wa kampuni binafsi.

“Hawa jamaa waliondoka kwa likizo, ila watarudi, kwa sasa hawapo,” alieleza yule mlinzi.

“Ok, ni muda gani ambao hawapo hapa,” akauliza Gina.

“Ni kama wiki moja sasa,” akajibiwa.

“Sawa asante basi tutakuja wakati mwingine,” Gina akashukuru, wakaondoka na Amata kurudi garini.

Kamanda Amata alipoketi tena na Gina garini, akamtazama mwanadada huyo mrembo wa sura na ngozi nyeusi inayong’azwa kwa lishe bora na virutubisho makini, “sasa naongea na wewe kama mshirika wa kiofisi na sio wa kikazi, unafikiri kwa nini hawa watu wameenda likizo ndani ya wiki moja ambayo hiyo hiyo imetukia tukio hili?” akamwuliza.

“Hata mimi hapo moyo wangu unapiga chogo chemba, nashindwa kupata jibu, nahisi kuna jambo kati yake, any way, tunafanya nini sasa?” Gina akajibu na kuuliza.

“Hapa hatuna budi kulisaka gari lenye namba hizo, kwa kuwa mpaka sasa ni ufunguo pekee wa kazi yetu, hebu twende leo tukamtembelee rafiki yetu wa muda mrefu, nafikiri huyu anaweza kutusaidia kwa namna moja au nyingine,” Kamanda akamwambia Gina.

“Nani huyo?”

“We endesha gari mpaka kituo cha polisi kati,” Kamanda akaamuru.

“Aaaaa ok, nimeshamjua, na kweli ni wa siku nyingi sana,” Gina akaitikia.

Dakika nyingine ishirini na tano ziliwafikisha katika kituo cha polisi kati, walipoegesha gari wakashuka moja kwa moja na kuifuata kaunta kabla hawajapandisha ngazi ghorofa ya kwanza ambako walimkuta yule wanayemhitaji, Inspekta Simbeye.

“Karibu kijana, naona leo umefuatana na mrembo wako!” akakebehi.

“Ee Bwana si unajua tena lazima alinde,”

“Kabisa; hongera bibiye nasikia umeteuliwa katika idara nyeti ambayo wenzako wanaililikutwa kucha hadi wanagongana kwa waganga, lakini wewe aaaaa kiulaini umeikwaa,” Inspekta Simbeye kama kawaida yake akawa akimwaga utani, akawakaribisha na kuketi nao, “ndiyo Bwana Amata , najua tu kuwa ukija hapa basi huko yamekushinda,” akamwambia.

“Hapana, nikija hapa basi nataka usaidizi wa mapana na marefu, kuna hii namba hapa ya gari, naihitaji hii gari ama nijue sasa hivi iko wapi au imepita mtaa gani,” akamwambia Simbeye, akampa kijikaratasi kilichoandikwa hiyo namba. Inspekata Simbeye akakitazama kwa udadisi sana kile kijikaratasi, akafinya macho akafinyua, kisha akawatazama Gina na Amata, “ ok kwa hiyo mnataka vijana waingie kazini?” akauliza.

“Ndiyo maana tukaja kwako kwa maana wao vijana wako wanajua kunusa vitu kama hivi kwa haraka kutokana na mtandao walio nao,” Kamanda akeleza.

“Ok, nipe dakika kadhaa,” akainua simu ya mezani na kuzungurusha namba fulani kisha akamwita kijana mmoja. Dakika mbili yule kijana alikuwa kasimama kwa ukakamavu kabisa mbele ya Inspekata wake akiwa katika sare yake nadhifu nyeupe katika mkono wake wa kushoto akining’iniza ‘V’ tatu yaani alikuwa Sajini.

“Nataka upeleke taarifa kila point huko barabarani wakiiona hii gari leo wanipe taarifa haraka iwezekanavyo,” akatoa amri.

“Sawa Afande!” akajibu yule kijana na kutoa saluti ya utii kisha akaondoka zake.


Siku hiyo askari wa usalama barabarani waliongezeka mpaka kila mtu alishangaa, gari nyingi zilisimamishwa hii ikakuguliwa pale na ile kule ili mradi tu wajaribu kuipata ile wanayoitaka. Haikuwa kazi rahisi bali ilikuwa ngumu, madereva walikasirika sana maana walisimamishwa hata zaidi ya mara tano lakini hawakujua ni nini ambacho wenzao wanakitafuta. Siku ilienda kasi hakuna jibulolote lililoleta maatumaini. Kamanda Amata akiwa katika mgahawa wa Steers alianza kukata tamaa, maana alitegemea taarifa hiyo ingeweza kumpa njia ya kupenyea katika kulikabili swala hilo.

Akiwa anaweka weka vitu vyake vizuri tayari kuondoka katika mgahawa huo mara simu yake ikapata uhai mpya, namba iliyosomeka kiooni ilikuwa ni ile ya Simbeye. Kumekucha, akawaza, kisha akaibonyeza kile kidubwasha cha kusikilizia na kuiweka sikioni.

“Windo lako limeonekana, limetoka barabara ya Mandela na kuingia barabara ya Morogoro…” Sauti ya Simbeye ilieleza.

“Ok, nimekupata, naomba taarifa kila point anapopita mpaka atakaponikaribia, nipo mjini kati na sasa naelekea barabar ya Morogoro kutokea Mtaa wa Samora,” Kamanda akaeleza.

“Wrong, pita barabara ya Ohio ukatokee ile ya Bibi Titi kisha kunja kurudi Maktaba nafikiri atatumia njia hiyo,” Simbeye alieleza kana kwamba anajua mtu huyo anakwenda wapi. Kamanda Amata akatia gia na kuondoka pale Steers, moja kwa moja akaiacha Ohio na kuikamata ile ya Bibi Titi kuelekea Maktaba akiwa makini kabisa kutazama gari zinazokuja mbele yake, akafyatua nobu ya simu ya upepo yenye uwezo wa kunasa mawimbi ya simu zote za mtindo huo zinazopita ndani ya mita mia tano za mraba, akaweka vizuri signali za redio ya polisi akazipata na kusikiliza wanavyoelekezana juu ya gari hiyo.

“…Imepita hapa mataa ya Magomeni ova….”

“….Imeelekea Kinondoni, point ya Kinondoni tafadhali, ova!…”

Kamanda Amata alipiga U – turn pale maktaba na kurudi haraka akakunja kushoto kwenye makutano ya barabara ya Bibi Titi, Ohio na ile ya Ally Hassan Mwinyi, akaifuata hiyo kwa kasi akiwa na malengo mawili, ama kukutana nalo kwenye makutano ya Barabara ya Ally Hassan Mwinyi na Ile inayotoka Kinondoni.

“… imepita mataa ya Mwananyamala. Imenyoosha kuelekea Morocco, Ova…”

“….Endelea kunipa ripoti Ova!…”

Kamanda Amata akakaza mguu na kuongeza kasi kuwahi katika makutano ya Morroco maana kutoka hapo hakujua hasa ni wapi anaweza kuwaona tena.

“…imeelekea barabara ya Hali Hassan Mwinyi, ova…”

Kamanda Amata aliposikia taarifa ya mwisho alikuwa tayari amefika karibu na Mbuyuni njia ya kwenda Kanisa la Sant Peter, akakunja kulia na kuifanya kama inataka kuingia barabara ya pili kuelekea mjini, akasimaman katikati akisubiri, wakati huo taa ziliwaka nyekundu, gari zikasimama. Kamanda Amata akatazama kwa haraka haraka, akaiona ile gari ikiwa imesimama ikisubiri foleni, akatazama kwa umakini ndani yake, alimuona mtu mmoja tu, mwanaume aliyekuwa ameketi nyuma ya usukani. Gari zilizpoanza kutembea, akavizia nyuma ya hiyo gari zikapita gari mbili kisha yeye akaingia hapo na kuifuatilia taratibu. Ile gari ilikwenda na kuingia katika maegesho ya Motel ya Agip katikati ya mji, mtu aliyekuwa humo akashuka, mwanaume mwenye tambo la haja, kwa harakaharaka Kamanda alimuona mpiganaji huyo akivuta hatua fupifupi na mguu wake akiwa akichechemea kwa mbali, akamkumbuka, George Mc Field, akatikisa kichwa, kisha akacheka, baada ya kugundua kuwa mtu huyo miaka kumi ilopita hakuwa akichechemea lakini kwa kipigo alichokipata kwa Kamanda Amata mara ya mwisho katika sakata la Mwanamke Mwenye Juba Jeusi kumbe lilimuacha na mguu mbovu. Akamtazama mpaka alipoingia ndani, akateremka garini na yeye kuiendea kaunta ya moteli hiyo.

Moustache alioubandika juu ya mdomo wake ulimbadili kiasi, na kofia kubwa aliyovaa ilimfanya aonekane mmoja wa ‘watumia pesa’. Amata akasimama jirani kabisa na Mc Field ambaye alikuwa amejibadili kiasi ila kwa Amata alimtambua kwa alama zake alizokuwa akizikumbuka. Kabla hajaongea na mhudumu wa kaunta jicho lake kali lilikuwa likitazama katika kaitabu ambacho Mc Field alikuwa akiweka saini, akaona namba ya chumba 206. Akajifanya anaulizia mtu fulani ambaye hayupo kabisa katika hoteli hiyo. Kisha akatoka mara baada ya kujibiwa kuwa mtu huyo hayupo. Akarudi garini na kuiondoa gari yake kisha akenda kuiegesha upande wa pili. Alijua wazi upande gani ambako kile chumba kilitazama, akaiacha gari yake na kurudi upande wa pili.

Chumba alichokitegemea, kikafunguliwa pazia, Amata hakuwa na haja ya kujua nini kinaendelea ndani ya chumba hicho, akatulia akisubiri. Ilichukua dakika arobaini na tano, pazia likafungwa tena. Kamanda akawa makini kuona nini kinatokea, mara gari ile ikawashwa na kuondoka maegeshoni.

Kama kawaida, akasubiri dakika kumi na tano akaingia ndani ya hoteli ile na kukwea ngazi mpaka chumba namba 206 akautazama mlango kwa makini kama kuna alama yoyote iliyoachwa ambayo mtu huyo itamfanya agundue kuwa alitembelewa. Hakuona, akachukua funguo yake inayoweza kufungua vitaza 999, akaipachika na kucheza nayo sekunde nne tu mlango ukatii, akausukuma taratibu lakini alikumbuka lililompata Madam S, akatanguliza mkono wake huku akikubali kitakachotokea, alitegemea kutobolewa na misumari mibaya inayotegwa na Jasusi huyo mara nyingi, hakukuwa na kitu.

Akaingia kwa hatua mbili ndani, hakuwasha taa ijapokuwa giza lilikwishakijaza chumba hicho, akaichukuwa miwani yake na kuivaa, chumba chote kwake kikaangazwa na mwanga usioonekana na mtu mwingine, akatazama kwa macho, akakagua chumba hicho kwa macho, hakutaka kugusa chochote kile, kisha akachukua kijitufe kidogo mfano wa big G, akakiendea kitanda akakitazama na kupachika kile kidubwasha uvunguni kwenye chaga, kisha akatoka taratibu na kukiacha chumba hicho, akarudi kwenye gari yake, akafungua saraka ya gari na kutoa kidubwasha kingine kama redio ndogo sana ukubwa wa kiberiti, akakiwasha ili kurekodi kila sauti itakayotokea ndani ya chumba hicho kisha yeye akaondoka zake kwa usafiri, mwingine huku ile gari akiiacha pale pae.

“Las Vegas Cassino!” akamwambia dereva aliyekuwa kimwendesha. Dakika chache baadae alikuwa katika Cassino hiyo kubwa iliyopo kwenye njia panda ya kuelekea Agha Khan kutokea Barabara ya Ally Hassan Mwinyi.

“Yes Kamanda,” Madam S akaiita kutoka nyuma yake wakati Amata akiwasha sigara kana kwamba yeye ni mvutaji.

“Agip Motel namba 206,”

“Maelekezo mengine,” akahoji Madam.

“Baada ya saa kadhaa, watoto wanacheza,” akajibu.

“Ok,” Madam akamalizia kwa kuitikia, akampita Kamanda na kuondoka zake, akaiendea gari yake, kukamata kitasa.

“Subiri!,” Kamanda akamshtua Madam S, kisha akampa ishara ya kurudi kwake, Madam akataii. Wakati Madam S alipokuwa anataka kufungua mlango wa gari, Kamanda Amata alimuona mmoja wa walinzi wa Cassino hiyo akichomoa kitu kama remote mfukoni mwake. Hiyo ilimpa ishara Kamanda kuwa kuna hatari inakaribia kutokea, Madam alaiporudi kwa Kamnda yule mtu akarudisha ile remote mfukoni mwake, na kupotea eneo lile mara moja.

“Hakuna usalama,” akamwambia Madam S

“Umeona nini?” Madam akauliza

“Gari yako lazima ina mlipuko, ngoja kidogo,” akajibu na kuifuata gari ya Madam S, akawasha saa yake na kuisogeza jirani, ikapiga kelele na kuwaka taa nyekundu, akamtazama Madam S.

“Wamejuaje kama niko hapa mpaka waniwekee bomu?” Madam S akauliza.

“Muwinda huwindwa mama! Acha hiyo gari tumia usafiri mwingine, tuonane kesho asubuhi,” Kamanda akamuaga mwanamama huyo na kutoka eneo lile. Kwa mwendo wa miguu akarudi kuifuata barabara ya Ally Hassan Mwinyi, akiwa taratibu njiani, nyuma yake kulikuwa na watu wawili wakija nao wakiwa wametokea katika casino ileile. Aliporudisha uso mbele akaona mtu mmoja akija upande huo, hakuonesha kugwaya, alitembea kwa mwendo uleule. Alipofika katikati, wa nyuma na wa mbele wakiwa umbali sawa, akasimama na kugeukia katika maua yaliyo mbele yake, akafungua zipu ya suruali na kujifanya anakojoa, akisubiri aone watu hao watachukua hatua gani. Alijua kama watasita basi ni wabaya kwake lakini kama si wabaya watapita na Hamsini zao.

Wale wawili wakasita kidogo, wakawa kama wanajiuliza jambo, yule mmoja akajifanya anafunga kamba za viatu, kwa vitendo hivyo Kamnda Amata akajua wazi kuwa anawindwa na amekwishwekwa katikati, akageuza na kurudi alikotoka kule kwenye wale wawili, akaona wakiwa na woga Fulani, akaongeza mwendo kuwaendea, akachanganya miguu kama anatroti.

“Simama!” wakamwamuru.

“Mna amri gani ya kunisimamisha mimi? Ninyi ni nani?” akauliza huku akiwapita.

Wale jamaa walimpa hatua mbili tu za kupita, wakageuka na mmoja wao akatoa kitu kama mpira akauzungusha katika viganja vyake, mwisho huu huku na huu kule tayari kwa kumkaba. Kwa haraka akaupachika shingoni mwa Amata, hilo alilitegemea tangu mwanzo, na aliigundua hiyo mbinu. Akanyosa juu mikono kwa kuikunja mikono yake na ule mpira ukaivaa mikono, akaisukuma mbele na yule jamaa akajigonga kisogoni mwa Amata. Akajivua ule mpira na kugeuka haraka, konde moja alilolitupa, lilipiga shavuni mwa Yule mjing akaenda chini, yule wa pili akarusha ngumi akadakwa mkono, akauzungusha na kuuweka begani akauvunja, yowe la uchungu likamtoka yule jamaa. Wakati huo yule mmoja aliyekuwa akitokea mbele akawa amefika, mkononi alikuwa amekamata kitu kama bastola. Amata akamwacha yule jamaa na kuchumpa kuingia kwenye maua, lo! Hakuangalia vizuri, kwenye yale maua kulikuwa na seng’enge yenye ncha kali sana, zikamchoma, kabla hajajinusuru yule jamaa akafyatua ile bastola yake, kitu kama msumari kikamchoma shingoni. Amata akajisikia ganzi, miguu akahisi ikipata ubaridi, taratibu akaanza kupoteza nuru. Kila alipojaribu kujitutumua hakuweza, akatulia na kukumbwa na giza nene.

“Mmemkamata?” sauti hiyo aliisikia kwa mbali sana.

“Aaa nimempata lakini Shebby kavunjwa mkono msaidieni,” akaendelea kuwasikia kwa taabu na mwisho masikio yake hayakuwa na nguvu tena za kusikia chochote.

SIKU ILIYOFUATA saa 3:30 asubuhi

MADAM S ALIINGIA OFISINI kwa kuchelewa kidogo, akamkuta Chiba akiwa anamsubiri.

“Vipi Chiba?” akuliza.

“Nimekuwa nakusubiri sana maana kila simu nikikupigia sikupati, nikaanza kuwa na wasiwasi,” Chiba akajibu.

“Ah, mbona simu zangu zilikuwa on zote? Kwa nini ulikuwa hunipati?” Madam S akatoa simu zake na kuziangalia zote zilikuwa sawa.

“Shida za mitandao hizi,” akamwambia kisha akaingia ofisini.

“Nipe jipya,” Madam S akamwambia huku akivuta kiti chake na kukaa.

“Hakuna jipya, ila sina taarifa yoyote ya Kamanda tangu jana nilipokuwa nawasikia mara ya mwisho pale Cassino ya Las Vegas,” akamweleza Madam.

“Aaaa Kamanda tuliachana kama saa nne hivi, na tangu hapo hata mimi sikumtafuta,” Madam S akajibu, akafikiri jambo kisha akaendelea kusema, “jana aliacha gari pale Motel Agip mtaa wa pili hivi, kuna information alikuwa anainasa, nafikiri atakuwa ameiendea, hebu mtafute kwa simu yake ya kwenye gari”.

Chiba akajaribu lakini simu iliishia kuita tu.

“Hayupo garini!”

“Jaribu nyumbani”.

Chiba akajaribu simu za nyumbani, zote hazikupatikana kabisa, “hakuna connection kabisa,” akamwambia Madam S.

“Mpigie Gina,” akatoa maelekezo. Chiba akampigia Gina akampata, akamwulizia juu ya Kamanda Amata, Gina hakuwa na jibu sawasawa, akamwambia atapita nyumbani kwake Kinondoni akamwone.


Kamanda Amata alikuwa kwenye kiti cha chuma, hakuwa na fahamu, mikono yake ilifungwa nyuma ya kiti hicho ilhali miguu yake ilikuwa imefungwa pamoja kwa kuzungushwa nyuma ya miguu ya mbele ya kiti hicho. Alikuwa amelala usingizi, shingo yake imeeinamia chini, udenda ukimtoka. Ndani ya chumba hicho cha wastani kulikuwa na vijana watatu wenye Sub Machine Gun kila mmoja iliyoshiba vizuri. Hawakuwa wakiongea, kila mmoja alisimama kona yake akiweka ulinzi madhubuti. Waliambiwa watoe taarifa pindi tu atakapoamka. Ilikuwa zimekwishapita saa kumi na mbili tangu adungwe dawa ile mbaya kabisa mwilini mwake ambayo huenda na kuudhoofisha milango yote ya fahamu.

Amata alianza kuhisi baridi kwa mbali sana, fahamu zilianza kumrudia, kidole chake cha kalulu kilianza kuchezacheza.

“Anaamka huyu! Oya waite jamaa!” mlinzi mmoja alitoa amri kwa walio nje. Ijapokuwa alikuwa kamanda peke yake katika chumba hicho kama mateka lakini walinzi wa ndani walikuwa watatu waliobeba SMG zilzizoshiba risasi, nje ya mlango kulikuwa na walinzi wengine wapatao watano nao walikuwa na silaha kama zizohizo. Kwa ujumla walimwogopa, labda kutokana na habari walizopewa juu ya uhatari wa mtu huyo.


Peugeot 404 iliegeshwa nje ya nyumba fulani katika eneo la Upanga, mtaa wa Ali Khan. George Mc Field ambaye tangu ameingia nchini alikuwa ameuvaa Uafrika-butu, alionekana Mwafrika lakini aliyepauka kidogo, hiyo ilitokana na kujibadilisha kwa ngozi yake kwa madawa maalumu na kuupoteza uhalisia wa uraia wake. Alikuwa Jasusi aliyetafutwa kila kona, alitekeleza mengi sana ya kuua, kuiba, kuteka, kutesa na mambo yanayofanana na hayo. Alijishauri mara kadhaa siku alipoapewa kazi ya kuja kufanya wizi wa almasi katika mgodi wa Mwadui, lakini kutokana na donge aliloahidiwa alikubali.

Akachagua watu watatu makini kati ya vijana wake, akawafundisha Kiswahili, mapigano, jinsi ya kutembea kama Watanzania, akaandaa mkakati makini wa kuiba almasi kwa kujifanya yeye ni Waziri wa Nishati na Madini. Kazi hii kwa Mc Field haikuwa ngumu sana, kwa kuwa yeye alikwishapitia kozi mbalimbali za Kijasusi na Ukomandoo aliiona kazi ndogo ila aliipenda kwa kuwa ilihusisha pia kuwapoteza watu uhalisia wa wanachokiona.

WIKI MOJA NYUMA

FORKER FRIENDSHIP, ndege ya serikali, iliondoka katika uwanja wa ndege mdogo wa mgodi wa North Mara kuelekea Mwadui. Wageni waliotumwa na makampuni kutoka nje kuja kwa ajili ya kutazama fursa za uwekezaji, walitulia vitini, walikuwa watatu, wazungu. Ndege ilipokaa sawa hewani na kuruhusiwa kufungua mikanda, mmoja wao alinyanyuka na kuelekea maliwato.


        “Vipi, kuko sawa huko?” Mc Field aliuliza akiwa katika eneo la mizigo, amekaa akisubiri wakati, yeye aliingia ndegeni bila mtu yeyote kujua, alijifanya mmoja wa wafanyakazi wa ndege hiyo pale North Mara, akajificha katika behewa ya mizigo, akijibadiliasha hapa na pale mpaka akafanana kabisa na Mheshimiwa Waziri. Utaalamu wa hali ya juu unaotumiwa na Majasusi au wapelelezi mbalimbali huko nchi zilizoendelea. Mission ilishapangwa, kila kitu kilitengenezwa, ilibaki kuvaa tu.

“Yeah, tuko level nzuri kutoka usawa wa bahari,” akajibu yule mtu.

“Ok, zima pale, kisha pachika hako kamtungi katika hiyo pipe,” akamwelekeza, yule kijana akafanya hivyo, “subiri kidogo, dakika tano hivi, nitakujulisha,” akamwambia, kisha ukimya ukawakabili kati yao.


Ndani ya chumba cha rubani, mashine za kuonesha vipimo vya hewa, presha, kani mvuto, mwendo kasi na kadhalika, vilionesha hitilafu hasa katika upande wa presha na hewa safi. Rubani alijitahidi kurekebisha hapa na pale lakini ilikuwa ngumu, akainua kidubwasha cha kuongelea na kuwatangazia abiria kutumia hewa ya ziada inayotoka katika mitungi maalumu ndani ya ndege hiyo. Juu ya kila kiti, kwenye saraka kubwa za mizigo ya ndani zikachomoka barakoa za kuvaa puani kuweza kuvuta hewa safi.

Wakati huohuo kule chini kwenye mizigo, Mc Field na mwenzake wakaondoa mtungi wa oxygen kwenye ‘Chemical Oxygen Generator System’ na kupachika mtungi wao wenye dawa kali ya kulevya katika njia za kupitisha hewa safi. Haikuchukua dakika moja wote walikumbwa na usingizi mzito isipokuwa wale Wazungu tu ambao hawakugusa kabisa barakoa zile.

“Tayari, waambie wenzako mulete waziri huku chini. Yule kijana akafanya hivyo. Waziri akaletwa chini kwenye mizigo akiwa anapumua kwa tabu, Mc Field akachomoa kijikadi kidogo kilichounganishwa vizuri kwenye kompyuta ndogo.

“Soma hapa,” Mc Field akamwambia waziri. Mheshimiwa akabaki kakodoa macho tu, hakujua la kufanya, “soma hapa!” akamlazimisha na kumchapa kofi la usoni.

“Tu-na-hitaji -makasha ma-ta-no ya almasi sa-sa ni amri ku-to-ka I-ku-lu ba-ru-a hii – ha-pa”.

Kisha mmoja wa wale vijana akamdunga sindano na waziri akalala usingizi wa maana. Wanaume wakafanya walichotumwa.


Rejea sasa: Tracy Tasha…

TRACY TASHA ALIVIRIGA nywele zake na kuzifunga kwa nyuma, akaiweka miwani yake usoni, akachukua kitu kama kalamu iliyokuwa na rangi inayofanana na ngozi yake akakiendea kioo kikubwa na kuanza kujitengeneza uso wake vizuri kwa namna anayoijua yeye, alipohakikisha kajiweka tofauti, akafungua mkoba wake na kutoa stika moja ambayo aliibandika kwenye shavu lake. Stika ile ilitengenezwa taswira ya mtu aliyeshonwa jeraha kwa nyuzi saba. Akatoka nje ya hoteli na kuingia katika tax iliyokuwa ikimsubiri, “mtaa wa Ally Khan mkabala na Zanaki Sekondari,” almwambia dereva kisha yeye akaketi kiti cha nyuma bila kuongea zaidi hata pale alipoulizwa maswali kadhaa na dereva huyo hakujibu zaidi ya kutikisa kichwa tu.

Dakika arobaini na tano ziliwatosha kupambana na foleni na kuingia katika eneo husika. Tracy alilipa na kuachana na dereva huyo, alipopotea, akavuka barabara na kuingia kwenye geti dogo katika nyumba aliyihitaji. Ilikuwa nyumba kubwa ambayo nyuma yake kulikuwa na banda kubwa lililojengwa kwa matofali ya kupangwa, ndani yake kulikuwa na kitu kama handaki ambacho watu wengi hawakujua hilo.

“Karibu sana, this way please,” George Mc Field alimkaribisha Tracy na kisha wote wakashuka handakini.


Kamanda Amata alikuwa ameendelea kuketi palepale alipofungwa, akili yake ilisharudiwa na fahamu kamili, lakini bado alijifanya hajaamka sawasawa, aliweza kusikia kila kitu kilichoendelea, alijuwa wazi kuwa ni nani anayesubiriwa na alisubiri kuona kama hao wanaokuja ndio wale anaowahitaji, alihitaji kuwajua. Kwa mara kadhaa alijaribu kujitikisa na kuona kama kamba zile zimemfunga sawasawa, mikononi alishindwa hata kujitikisa lakini miguuni nako ilikuwa hivyo hivyo, akatulia na kufumbua jicho moja kwa mbali, akawahesabu wote waliokuwa ndani, ni watatu tu na bunduki zao.

Nikileta makeke tu natobolewa kwa risasi zenye hasira, akawaza. Mara akasikia lango likifunguliwa upande wa juu na watu waliokuwa wakiongea kwa lugha ya Kiingereza wakaingia ndani ya eneo hilo.

Sekunde chache tu watu wawili walikuwa mbele yake, yule mgeni wa kiume akatikisa kichwa chake na kijana mmoja akaweka pembeni bunduki yake, akakunja mikono ya shati lake. Kamanda Amata akajua sasa kumekucha. Yule bwana alimsogelea, akamatazama Amata. Akamwinua uso wake, Kamanda akafumbua macho yote mawili akamwangalia, yule jamaa akasita kidogo maana alishaambiwa uhatari wa kiumbe huyo. Akaita wenzake wamuweke sawa. Amata akafunguliwa kamba na kuondolewa kitini, kamba za miguuni zikarudishhiwa kisha zile za mikononi zikafungwa kwa nyuma lakini wale vijana wakamkamata huku na huku upande wa nyuma na yule mwingine akaanza kumshindilia makonde ya tumboni, makonde ya nguvu. Amata alivumilia lakini nguvu za mikono za yule Bwana zilikuwa zikimwingia kisawasawa, damu zikaanza kumtoka kinywani.

“Ha! Ha! Ha! Haaaaaa! Mwacheni! Kamanda Amata, leo au niseme sasa, umefika mwisho wako, na lazima ufe sambamba na yule tunayemtaka au tuliyetumwa kumtoa roho yake,” Mc Field akamwambia Kamanda huku akimgeuza uso wake uliowiva kuwa mwekundu. Alihema kwa taabu sana, “Mc Fi-e-ld, uta-lipa, utalipa, na-kwa-mbia utalipa,” akamwambia kwa sauti ya taabu. George Mc Field akastuka kidogo baada ya kusikia jina lake likitajwa, akajiuliza pamoja na kujibadili inawezekanaje kuwa kajulikana kirahisi namna hii, akajikaza.

“Nani anayekudanganya hayo? Sikia mpumbavu wewe, kabla hujafa nitataka kukupa siri moja nzito ambayo utakufa na hautaweza kuifikisha popote pale, na siri hiyo ni kuwa kesho tunaondoa roho ya mtu mkubwa sana hapa katika Taifa lenu,” Mc Field alizidi kutamba wakati Tracy akiwa kasimama kando mikono yake kaifungamanisha kifuani mwake, akitafuna pipi mpira isiyokwisha.

Konde moja zito la Mc Field lilitua katika shavu la Kamanda Amata, akahisi taya lake limevunjika, kabla hajatulia akapata lingine la upande wa pili.

“Sikia we Bwege, nimekuja tena nikiwa na hasira mbili, na kazi moja! Nadhani umenielewa, leo hutoona jua la nje, kibibi chako kinahaha huko duniani kukutafuta na hakitakuona tena,” Mc Field alimweleza Amata.

“Utalipa, ha-ta mimi ukiniua, yu-po nyu-ma atakayekuua kwa kwa niaba yangu, atakutenganisha kichwa na kiwiliwili chako,” Kamanda akaeleza.

“Ha! Ha! Ha! Ha! Haaaaaa!!!!” Mc Field akacheka sana, “nani unayemtegemea, huyu hapa au mwingine?” Mara mlango mwingine ukafunguliwa, Gina akasukumiwa ndani na kuanguka sakafuni. Kamanda Amata alitamani aruke kumdaka Gina ambaye alijibwaga vibaya sakafuni.

“Tunapotaka kufanya kazi, huwa tumejipanga, wewe na huyu malaya wako wote leo mnaenda kuzimu,” Mc Field alijigamba. Kamanda Amata alikuwa amefura kwa hasira kali, akimtazama Gina aliyekuwa chini hajiwezi, ilionekana amepata kipigo kisicho cha kawaida.

Tracy Tasha alivuta hatua na kumsogelea Gina, alivuta mguu wake na kumtandika Gina teke kali la usoni. Gina akatupwa upande wa pili, akabaki chali damu zikimvuja puani na kinywani. Mguu wa Tracy ulienda juu na kubaki hewani kwa sekunde kadhaa kabla hajaushusha chini kwa maringo, kisha akatembea kama Miss kumwendea Amata.

“Huyu ndiye ulienipa vitisho juu yake? Eti Kamanda, kamanda? Makamanda wametulizwa kwa mkono huu,” akaupunga mkono wake hewani, akamtazama Mc Field, “hakuna mwanaume wa chuma wala nini, hapa ni utepetevu tu,” akamalizia kisha akarudi alipokuwa. Mc Field alitabasamu huku akitikisa kichwa chake juu chini, akimwangalia mwanamke huyu anayetembea kwa madaha, mrembo wa sura na mzuri wa shepu, lakini mwenye roho iliyojaa kutu.

“Kamanda Amata una la kusema? Sasa ni saa saba inaenda saa nane, muda wetu unayoyoma, huyu mwanamke ndiye atakayekuua wewe usiku wa leo kwa kukukata kichwa chako,” Mac Field alimwambia Kamanda.

“Hata kama, La- la-ki-ni, kwa-nza nitaku-ua we-we,” akimaanisha Mc Field, “pili we-we mwana-m-ke uta-ji-ua –mwenye- we,” aliongea kwa tabu. Mc Field na Tracy wakaondoka ndani ya chumba kile wakiacha maagizo kuwa watu hao washughulikiwe ipasavyo.


Ilikuwa ni vigumu sana kwa Madam S kuamini kuwa Kamanda na Gina wametekwa, haikuingia akilini. Wamempataje kirahisi hivyo? Alijiuliza bila ya kupata jibu. kila mara alikuwa akimwita Chiba ofisini na kumwambia hili au lile, alionekana wazi amechanganyikiwa. Chiba alijaribu kumtafuta Kamanda kwa simu zake lakini ilikuwa ni ngumu sana kwake kupata jibu kuwa wapi yupo kwani simu zake zilikuwa zikisoma eneo la mwisho la Upanga, Las Vegas Cassino.

“ Wameniweza!” alijiambia moyoni, “Scoba!” akaita.

Scoba akageuka kumtazama Chiba.

“Harakati lazima ziendelee kaka, hatujui Gina na Kamanda wako wapi mpaka sasa, na wala wako katika hali gani, hivyo tufanye juu chini kupata jibu,” Chiba, TSA 2, ilikuwa ni nafasi yake sasa kutoa majukumu.

“Iendee gari ya Kamanda pale Motel Agip kuna information inayoweza kutusaidia,” akaamuru na Scoba akawasha gari yake na kuondoka. Kama alivyoeelekezwa. Gari ya Amata ilikuwa palepale, Scoba kwa tahadhari ya hali ya juu sana akiendea ile gari, hakuhitaji kuiendesha, moja kwa moja aliifungua droo iliyokuwa imefungwa kwa lock maalum, akachukua anchotaka, alipogeuka tu kuondoka kuiacha ile gari, nyuma yake mlipuko mkubwa ukatokea, ile gari ikanyanyuliwa juu na kuvingirishwa mara kadhaa kabla haijatua juu ya gari nyingine ambazo nazo zilidaka moto, kizaazaa.

Scoba, alitupwa na ule msukumo uliotokana na mlipuko, akatua katika mlango wa vioo wa duka moja la madawa, akaanguka nao mpaka ndani. Mtaa mzima ulikuwa ni hekaheka kila mtu akitaka kunusuru gari yake na kusahau uhai, wapo waliofanikiwa lakini pia wapo ambao gari zao ziliteketea kabisa.

Tukio hilo lilivuta wengi sana mahala hapo, hii ilimsaidia Scoba kuondoka taratibu na kuielekea taksi iliyokuwa jirani. Ulikuwa ni mlipuko ambao mtu yeyote hakuutegemea hasa kwa jiji kama la Dar es salaam ambalo utulivu na amani zimekuwa ni desturi kwa wakazi wake.


“Pole Scoba, lakini haujaumia sana,” Dkt. Jasmine alimpa pole Scoba huku akimpa huduma ya kwanza katika chumba cha siri kilicho ndani ya ofisi ya Madam S. Damu kiasi zilikuwa zikimvuja katika upande mmoja wa kichwa chake baada ya kujikata vibaya kwa kioo pale alipoangukia, akaufungua mkono wake na kumpa Madam S kile kidubwasha.

“Mpe Chiba,” akamwambia.

Ilikuwa ni kinasa sauti kidogo kilichofichwa katika gari ya Kamanda Amata, Chiba alikichukua na kukiunganisha na mitambo yake, kisha akafuatilia mazungumzo yaliyokuwa humo kwa makini. Ndipo alipogundua kuwa Kamanda Amata ametekwa kadiri ya mazungumzo ya mtu aliyekuwa akiongea na simu katika chumba cha Motel hiyo. Aliendelea kufuatilia mazunguzmao hayo lakini hakujua kabisa ni wapi watakuwa wamemficha Amata. Chiba na wengine vichwa vilianza kuwazunguka.

“Tutapajuaje? Kumbuka Mc Field anamjua vizuri sana Amata, hawezi kumpa nafasi zaidi ya kumuua tu. Ndiyo, Amata anaweza kujiokoa lakini ni kazi ngumu sana kwa mtu kama Mc Field ambaye anauju uwezo wa kamanda, mtu kama yule hawezi kurudia kosa,” Madam S alimwambia Chiba huku akijifuta machozi.

“Ok, Madam, najua cha kufanya ila sasa tuandae Kikosi cha Ukombozi,” Chiba alitoa ushauri.

“Sawa, ni wewe mwenyewe na Scoba mtafanya kazi hiyo, hakikisheni inazaa matunda,” akampa maagizo, kisha akamsogelea Chiba, “ukikutana na Mc Field usijipime kupambana naye, tumia silaha, mmalize,” akamnong’oneza kisha akarudi kitini.

Chiba akairekodi ile sauti kwenye kompyuta yake na kuwasiliana na rafiki yake wa karibu sana katika moja mitandao maarufu ya simu, akampa kazi ya kutafuta watu hao walikuwa wakiongea wapi na wapi.

Dakika tano baadae alipewa taarifa kuwa mmoja alikuwa eneo la Mjini Kati maana mnara uliosoma ulikuwa ni ule wa jirani na jengo la Kitega Uchumi la Bima na mtu wa pili alionekana kuwa mitaa ya Zanaki Sekondari kwani mnara uliomsoma ni ule wa jirani na chuo cha ufundi cha Dar – Tech, upande wa nyuma. Chiba alijiridhisha na maelezo hayo na akamuomba mtu huyo amwambie namba hizo kwa sasa zinasoma wapi ili waweze kuwafuatilia watu hao. Jibu alilopata ni kuwa moja ya namba hizo ilikuwa imezimwa lakini nyingine bado ilionekana ipo mitaa hiyo ya Upanga, Mtaa wa Aly Khan.

“Scoba, upo poa? Tunaweza kuingia kazini?” Chiba alimwuliza. Scoba akaitikia kwa kichwa kushiria kuwa yuko fiti na anaweza mapambano, wakatoka katika chumba hicho na kufungua kijistoo kidogo, wakachagua silaha zinazofaa kwa kazi hiyo.

“Vipi mbona mnapakaua?” Madam akauliza.

“Tunaenda kupambana na jeshi, so lazima tujiweke kamili,” Chiba akajibu. Scoba akachagua Short Gun double barell, akaijaza risasi, bastola mbili aina ya PK 380 akazitia kibindon. Chiba akatazama huku na kule akainua silaha inayoitwa Heckler and Koch UMP , akaitia begani na nyingine ndogo ndogo kama visu, kamba za plastic, wakatoka wakavitia kwenye buti la gari na wao wakabaki na bastola mbilimbili zilizosheheni risasi. Wakaondoka na kuelekea Upanga.

10

AMATA ALIKUWA MDHOOFU sana baada ya kipigo alichokipata kutoka kwa wale jamaa mara baada ya Mc Field na Tasha kuondoka katika eneo lile, walikuwa wakimpiga huku wakimcheka sana na kila mmoja alijiona mshindi katika hilo, damu zilikuwa zikimvuja, wakati huo Gina hakuwa na nguvu hata ya kusimama.

“Sasa kinachofuata ni kufanya mapenzi na huyu malaya wako huku wewe ukiangalia,” mmoja wale jamaa akamwambia Amata.

Yule jamaa akamwendea Gina na kuanza kumfungua suruali aliyokuwa amevaa, huku wenzake wakishangilia na kupiga picha za video. Kitendo kile kilimuuzi sana Amata, kikampa hasira, hasira ambayo ilirudisha nguvu za ziada mwilini mwake. Mmoja wa wale vijana akamsogele Amata.

“Usijifanye huoni, angalia huku tunachomfanya malaya wako kisha picha zote tunapeleka kwa wakubwa zako,” akamwambia Kamanda huku akimshika kidevu kumgeuzia sura kule alikokuwa Gina. Ni dakika au nukta hiyo ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu sana na Amata, aligeuka ghafla na kudaka kidole cha yule jamaa kwa meno, akamuuma na kukikata kisha akakitema chini.

“Aiiiiiigggggghhhhhh!!!!! Ananing’ata mjinga huyuuu!” yule bwana akalia kwa uchungu sana, wenzake wakagutuka na kusogea kumsaidia. Kamanda Amata aliruka akiwa na kamba miguuni na mikononi, akajikunja kisha miguu yake akaipitisha katikati ya mikono yake na kutua nyuma huku mikono sasa ikiwa mbele. Akaanguka kwa kuwa hakuwa na uwezo wa kusimama sawasawa, akabiringita na kuifikia nguzo iliyosimikwa kushikia jengo hilo, akajiinua na kuketi, harakaharaka akashika ile kamba ya miguuni na kuifungua haikumpa tabu aliivuta tu ikalegea.

Kabla hajamaliza, alipata teke la mgongoni, mtu mwingine akaja kwa mbele na kurusha teke ambalo lingetua usoni au kifuani lakini Amata akalizuia kwa mikono yake iliyofungwa, akaunasa ule mguu na kuubana vizuri.

Kamba ya miguuni ikawa imekwishauacha mguu wake, akazungusha mguu na kumtia ngwala yule aliyemdaka mguu, jamaa akajibwaga chini akifikia kisogo, akatoa ukelele wa kifo. Mara hii alijikuta amezungukwa, akajiinua haraka na kuruka samasoti, risasi zikachimba chini na nyingine kwenye nguzo. Wakati yeye akitua chini alitua na wawili, mmoja alimshindilia vipepsi viwili vya pamoja na mwingine, akamshushia mateke makali, wote wakaenda chini, akabiringita na kujificha nyuma ya kasha kubwa la bati gumu, likamkinga dhidi ya adui zake.

“Oya, akitoroka huyo, tumekwisha!” Sauti ya mmoja ikasikika.

“Hatoki mtu hapa! Mzungukeni,” mwingine akatoa amri.

“We Chulubi, hakikisha huyo mwanamke umemfungia ndani, tushughulike na huyu mbwa koko,” sauti hii na maneno hayo yalimtia hasira Amata. Akiwa tayari ameiondoa kamba mikononi mwake kwa meno, alilisukuma lile kasha na kisha akajitumbukiza na kuseleleka nalo, risasi zikapiga juu yake lakini hazikuweza kuliathiri kwa lolote. Liliposimama akaruka nje na alipotua akambamiza mmoja mwenye bunduki, akaenda chini na bunduki ikitoka mikononi, akaruka samasoti akatua na kuiokota ile AK 47, akaitekenya na wawili walikuwa chini wakitupwa hewani na kugalagala wakigombania roho zao.

“Uwiiiiii! Mi nilisema, nilisema mimi!” mmoja akapiga kelele huku akikimbia kupanda ngazi za kutokea juu, lakini mara naye akarudishwa ndani kwa risasi, akajibwaga chali katika sakafu isiyokwisha.

Kamanda Amata akashangaa, alipotazama juu akaona vivuli vya watu vikiteremka katika ile ngazi, akajibana nyuma ya nguzo akiwa anatweta.

“Kamanda Amata!” ile sauti ikaita, mara moja aliitambua sauti ya Chiba.

“Chiba!” Naye akajibu huku akishusha bunduki yake na kutoka nyuma ya nguzo, hakumaliza hata hatua mbili, alihisi kitu cha moto kikipita katika mkono wake, ilikuwa ni risasi iliyopigwa kutoka nyuma na mtu mmoja aliyebwagwa hapo kwa kipigo. Kamanda aligeuka akiwa na maumivu lakini kabla hajafanya lolote risasi ilipenya katikati ya paji la uso la yule kijana huyo na kufumua sehemu ya nyuma ya kichwa chake.

Kamanda alipogeuka mbele alikuta bastola ya Scoba ikiwa bado imekamatwa barabara mkononi mwake.

“Asante Scoba, Gina hali yake ni mbaya, tumsaidie,” akawaambia na mara wakaweka silaha zao vyema lakini Scoba alibaki kasimama na bunduki mkononi kuhakikisha ulinzi.

“Tufanye haraka kabla polisi hawajafika,” Chiba alieleza. Pamoja na jeraha mkononi mwa Kamanda Amata lakini alijitahidi kusaidia na Chiba akambeba Gina mabegani mwake.

Scoba alikuwa wa mwisho kutoka katika ile nyumba pale Upanga, wakaliendea gari na kuingia kisha Scoba akabonyeza kitufe fulani na mlipuko mkubwa ukatokea kwenye ile nyumba, akaiondoa gari eneo hilo na kuacha kelele za wafanya biashara zikiita ‘Majambazi, Majambazi’


“Haujaumia sana Kamanda, risasi haijagonga mfupa, imejeruhi nyama tu,” Jasmine alimtia moyo Kamanda huku akiendelea kumshona jeraha lake.

“Ndani ya saa 24 lazima watu hawa wawe mikononi mwetu ama marehemu au wazima,” kamanda alikuwa akiongea huku akionekana kuwa na hasira sana juu ya adui zake.

Gina alikuwa amelazwa juu ya kitanda, chupa ya maji ikiwa juu ya linga, alikuwa na bendeji kiasi usoni na nyingine mkononi, alikuwa macho na alikuwa anaelewa kila kitu.

“Kamanda upumzike, tutafanya kazi ya kuwanasa sisi tuliobaki,” Chiba alimwambia Amata.

“Hapana, nasema hapana, nichome ganzi tafadhali, nataka kuingia katika mapambano, mpaka nijue mwisho wao au mwisho wangu,” Kamanda aliongea kwa hasira.

Madam S alisimama mbele ya Amata aliyekuwa sasa ameketi, akijaribu kuvuta akili na kuyapitia matukio.

“Kamanda,” akaita kwa upole, “unajisikiaje sasa?”

“Najisikia hasira Madam,” akajibu huku akigeuka, alionekana wazi mwili wake umejeruhiwa.

“Upumzike,” Madama akamsihi.

“No! hiyo haipo kwenye kamusi yangu, kumbuka adui ataona kambi yake imefumuliwa je atakaa hapa? Nikipumzika mpaka nipate nguvu tayari atakua London,” Kamanda akaeleza. Madam S akajifuta uso wake kwa viganja vya mikono, “Gina, anaendeleaje?” akauliza.

“Kaondolewa kapelekwa Shamba kwa matibabu zaidi, Gina amepigwa sana, ameumia sana,” Kamanda akajibu huku akiinuka, akasimama sambamba na Madam S, “sikia Madam, naongea kwa sauti ya chini, kuna mkakati mzito unaoendelea, hawa jamaa wametumwa kuondoa roho ya Mkuu wan chi, that is it!” akamtazama Madam.

“Ndiyo, lakini hatujajua kwa nini mpaka sasa wanataka kutekeleza hilo,” Madam akaongeze huku akimpita Kamanda na kukivuta kiti chake, akaketi na kuegemea meza, “Keti Kamanda!” akamwambia.

“Hii ni kitu nzito Kamanda, ni ya siri na ni nzito, sana lazima ishughulikiwe kikamilifu. Kwanza tushughulike na hawa waliokuja, tukiwatia mkononi wao sasa watatuambia nani aliyewatuma, hao sasa tutawafanyia kazi baadae kwa siri,” Madam akamwambia Kamanda.

“Ndio, lazima tukate mpaka shina sio matawi tu,” Kamanda akaongeza, “Mheshimiwa Rais anaendeleaje na afya yake?”

“Alipata mshtuko, sasa yuko sawa, na kesho ataongea na waandishi wa habari asubuhi saa nne palepale Ikulu, kuhusu hali halisi ya yaliyotokea, moja la kudunguliwa msafara wake na pili la kuibwa kwa almasi,” Madam akajibu.

“Hapana, sio wakati sahihi wa kufanya hivyo, Mheshimiwa hasijitokeze hadharani, akijitokeza anaweza kuwa amejianika wazi mbele ya muuaji,” kamanda akamwambia Madam.

“Amata, nimemwambia hayo, lakini inaonekana kuna kitu anaficha, sasa hii ni hatari kwa usalama wa nchi, sisi tunamlinda wakati mwingine inabidi atusikilize, ila safari hii amelazimisha kuongea na waandishi,” Madam akaeleza huku akipigapiga meza.

“Nimekuelewa, wacha iwe!”

Akanyanyuka kitini na kujitazama huku na huku, “naondoka Madam,” akarudisha mlango na kushuka ngazi taratibu, akaingia kwenye gari moja wapo ya ofisi na kutoka eneo hilo.

Simu ya kwenye gari ikaanza kuita, akainyakua na kuiweka sikioni.

“…Uwe mwangalifu we mtoto bado nakuhitaji,” Madam akamwambia. Kamanda Amata akaongeza kasi ya gari akaiacha barabara ya Ohio na kukamata ile ya Ally Hassna Mwinyi, akapita daraja la Surrender na kupinda kushoto mpaka nyumbani kwake Kinondoni. Akaegesha gari karibu na baa ya jirani. Akateremka na kuiendea nyumba yake. Alipoufikia mlango tu, akasita kidogo, kwa akili ya harakaharaka akajua nyumba yake imeingiliwa, akaichomoa bastola yake kutoka kwenye soksi, akaiweka tayari, akafungua mlango taratibu akaingia ndani kwa kunyata, kila alipotazama palipekuliwa, lakini hakukuwa na dalili yoyote ya mtu, akafungua chumba chake na kukuta hali ni hiyohiyo, kila kitu shaghalabaghala, akajua kwa vyovyote kulikuwa na purukushani. Akaenda mahali anapoficha zana zake za kazi na kabrasha za muhimu. Ni picha kubwa ya ukutani, akaibofya upande mmoja, ikaachia na kuteremka, akabonyeza tarakimu fulani na mahala hapo pakafunguka, akatazama kila kitu kipo sawa. Akapaacha na kwenda kwenye chumba chake cha siri ambako huficha kompyuta yake inayoweza kuona kila kitu kinachotukia umo ndani ikisaidiwa na vijikamera vidogo vidogo zilivyofungwa katika kona tofauti. Akafungua mlango na kujifungia ndani.

Ni chumba kidogo ambacho mlango wake kwa upande wa nje ni kabati lililoja viatu na makorokoro yasiyo na maana. Akawasha kompyuta hiyo iliyo mezani. Akarudisha nyuma matukio mpaka alipoona tukio lililotukia, akaanza kutazama.

Kwanza aliona mlango ukifunguliwa, Gina akaingia na kuita, kisha akaingia katika chumba cha Kamanda, akiendelea kuita. Hapo Kamanda akajua bila shaka Gina alikamatiwa hapo nyumbani kwake. Mara akaona kwenye ile picha mlango ukifunguliwa na watu watatu wakiingia, wakamvamia Gina kule chumbani. Gina akapigana nao kwa nguvu zote, akawaumiza vibaya mpaka ikabidi watumia kitu kizito kumpiga kichwani akazimia, wakambeba na kuondoka naye.

Kamanda Amata akashusha pumzi ndefu. Akainuka na kutoka ndani ya kile chumba, akaingia chumbani mwake na kuoga kisha akajilaza kwa dakika kadhaa akisubiri muda muafaka wa msako, lakini kichwani alijiuliza aanzie wapi, hakupata pengine zaidi ya Motel Agip.

Muda ulipotimu, akajianda kwa mavazi ya kazi, akachukua silaha zake muhimu na kuzitia kwenye kona mbalimbali za nguo yake, kisha bastola moja akaitupa kitandani na kuilalia kwa mgongo, yeye akiwa chali. Kichwa chake kilikuwa kikipanga na kupangua.


Mc Field aliikusanya mikono yake kifuani, kichwa kilikuwa kikimzunguka, hakujua nini anapaswa kufanya. Hata alichokuwa anakiangalia hapo dirishani hakukielewa, ndipo alipokumbuka kuwa hata hajarudi hotelini kwake. Akashusha mikono yake na kugeuka kumtazama Tracy aliyekuwa katingwa na kompyuta yake ndogo.

“Tracy,” akaita, Tracy akainua uso, “umeona kazi ilivyo nzito ee? Yule ndiyo Kamanda Amata, katorokaje pale, hawa ndio TSA, wanatisha,” akamwambia.

“Na sasa tunafanyaje, maana tumeambiwa tuwadhibiti hawa ndio tutimize lengo letu,” Tracy akajibu, “Lazima wameokolewa, uwezo wa huyo Kamanda sijui Amata ni mdogo sana, hawezi kunitisha mimi,” akajigamba.

“Ok sasa tunabadilisha program,” Mc Field akamwambia Tracy.

“Enhe, tunafanyaje, maana mimi haya mengine siyajui, mi nataka kumaliza kazi yangu tu niondoke,” Tracy akadakia na kuifunga kompyuta yake. Mc Field akachomoa kipande cha gazeti moja la kiingereza, akamtupia mezani. ‘Rais kulihutubia Taifa’, ilikuwa ni habari iliyopewa uzito wa juu mbele ya gazeti hilo, akaisoma habari hiyo na kukiweka mezani.

“Asante Mc Field, kesho naenda kumaliza kazi yangu, naomba niandalie usafiri wa kuondokea tafadhali, maana hiyo ndiyo kazi yako,” Tracy akasema huku akijifunga nywele zake vizuri.

“Hilo lisikuumize kichwa, nitanunua tiketi usiku huu huu, nafikiri kutoka hapa tuondoke na ndege ya kukodi mpaka Nairobi kisha pale wewe utachukua ndege na mimi nitarudi kwa kutumia usafiri wa barabara. Uzuri wa ndege ya kukodi unachagua muda wa wewe kuondoka, kwa hiyo, ukimaliza kazi, mara moja nitakutorosha, hilo niachie mimi,” Mc Field akamtoa hofu Tracy.

“Sawa, kama mambo yakienda sawa basi kesho saa tatu hivi tayari bendera zao zitakuwa nusu mlingoti, huwa sibahatishi kabisa,” Tracy alisimama na kuagana na Mc Field.

“Sasa mpango wote mimi nitaupabga usiku huu, wewe relax maliza kazi na mi nitakuwa pale tayari kukuondoa salama,” MC Field alipokwisha kusema hayo akatoka katika hotel ya Land Mark na kuchukua gari ileile anayoitumia ,TX, akaondoka zake.

Tracy alisogelea kabati la nguo katika chumba cha hoteli hiyo, akavuta kijibegi chake na kukitupia mezani, akakifungua katika mfuko wa pembeni kabisa kuangali kama zana zake zipo, naam zote zilikuwepo, zimetulia tuli kama alivyoziweka.

“You have got a job,” akazinong’oneza. Kisha akaufunga na kuurudisha mahala pake. Akaitazama saa yake mkononi ikamwambia ni saa nne za usiku.


ITAENDELEA

Jiue Mwenyewe Sehemu ya Tano

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment