Msako wa Mwanaharamu Sehemu ya Tatu
KIJASUSI

Ep 03: Msako wa Mwanaharamu

Msako wa Mwanaharamu Sehemu ya Tatu

IMEANDIKWA NA : RICHARD MWAMBE

*********************************************************************************

Silimulizi : Msako Wa Mwanaharamu

Sehemu Ya Tatu (3)

“Ulijiandaa sana kijana!” Amata akamsifia.

“Ndiyo, maana maelekezo mengi tayari nilipewa na Madam S nimwone Yule mzee ndiye akanipa ramani ya mji huu na lile kasri la Pancho,” Chiba akaeleza.

“Amekwisha, Gabacholi yule!” Amata akasema huku akifungua chupa ndogo ya Grants na kuigugumia kinywani.

“Aaaaaaakkhhhh!” akashusha pumzi iliyoashiria ukali wa kinywaji hiko.

  • * *

Chiba alizima mlio wa injini ya boti na kuiacha iseleleke taratibu mpaka ilipo karibia umbali kama wa mita mia tano hivi. Wakati huo Amata alikuwa tayari amekwishavaa nguo zake za kupigia mbizi, mitungi yake mgongoni na begi dogo lilisiloingia maji mbele ya tumbo lake.

“Chiba, hapa kazi tu, mi naingia kwa njia ya maji nafikiri ni njia rahisi kama ulivyonambia, na wewe pitia hii hii lakini upande wa pili sote tukaibukie ndani na kutafuta njia ya kumnasa mtu huyo, tukishamtia mkononi kila mtu aangalie ustaarabu wa kuitoka hiyo himaya lakini tukutane Bahrain,” Kamanda Amata alimweleza mkakati mzima Chiba kisha akajitupa majini na kupotelea humo.

Chiba akaendele kupiga kasia kuisogeza ile boti mpaka kwenye mimea ya baharini iliyojazana upande mmoja wa peninsula hiyo. Akaegesha naye akavaa vifaa vyake na kujitupa majini kwa uelekeo mwingine.

  • * *

Ndani ya hekalu hilo sherehe za mwanga ‘Diwali’ zilikuwa zikiendelea, watu walikuwa wakiimba na kucheza, kwa ujumla palichangamka. Premji Kanoon au Pancho Panchilio alikuwa ameketi sehemu ya juu kabisa akifuatilia michezo na burudani zote zilizokuwa zikiendelea katika ukumbi huo. Kando yake alikaa na watu wengine kadhaa huku wanawake kama nane hivi warembo wa kuvutia walikuwa wakimpepea, wengine wakileta vinywaji na kadhalika. Nyuma yake alisimama mtu mmoja, mwanaume mwenye tambo kubwa, aliyefuga sharubu zake na kuzichanua huku na kule kama askari wa Kijerumani enzi za mkoloni. Mikono yake aliifungamanisha nyuma. Macho yake yalionekana kutopepeswa upande wowote ule. Na katika kila upande au kona ya jengo lile walionekana vijana waliovalia sare na vitambaa vyao vichwani mwao wakirandaranda huku na kule.

Kamanda Amata aliibuka majini na kujikuta kwenye chumba ambacho ndani yake kuna boti kubwa la kifahari lililoegeshwa.

‘Nimekuja wakati mzuri, ningekuja mchana kusingekuwa na maji hivi,’ akawaza huku akivua ule mtungi na kuuweka kando, akatoa na yale mavazi yake kisha akafungua begi lake na kujipachika kila silaha aliyoihitaji mwilini mwake. Sauti ya viatu vya mtu aliyekuwa akija upande huo vilimfanya atulie tuli huku kisu chake kikiwa ngangari kiganjani.

“Inabidi tuiwashe kwanza ili injini ipate moto. Mkuu anasema hana budi kwenda Punjawar usiku huu,” Sauti ya kwanza iliongea.

“Mbona ghafla hivi wakati sherehe hii yote kaandaa kwa ajili ya watu wake?” Sauti ya pili ikauliza.

“Mi mwenyewe sielewi aisee, ngoja tuwashe kabisa yeye akifika ni kuondoka tu,” ile sauti ya kwanza ikarudia.

‘Nimsubiri kwenye boti?’ Amata akajiuliza moyoni.

‘Uamuzi mbaya utakuwa’ akajijibu mwenyewe na nukta hiyohiyo yule jamaa akaibukia kwenye mlango mmoja wa chumba hicho. Amata akaruka kwa wepesi na kumvamia huku akiwa tayari kamdidimiza kisu moyoni. Akamshusha chini taratibu na kumsukumia kwenye maji. Kisha akatulia kwani bado mwingine alikuwa akija upande huo.

“Kumar! Kumar!” Yule wa pili akaita. Lakini hakukuwa na jibu kutoka kwa swahiba wake, akaendelea kwenda na alipofika kwenye kile chumba hakuamini anachokiona. Mwili wa Kumar ulikuwa ukielea kifudifudi majini. Mshtuko wake ulikuwa zahiri shahiri, akainua redio yake na kuomba msaada.

“Kumar mara cuka hai! Kumar mara cuka hai!” (Kumar amekufa! Kumar amekufa), Amata akajibana kimya nyuma ya pipa kubwa lililojaa vipuli mbalimbali. Dakika hiyohiyo watu kama saba wenye silaha wakaingia katika kile chumba.

‘Nimecheza blanda’ akajiambia, akachomoa bastola yake iliyofungwa kifaa cha kuzuia sauti na kuiweka tayari. Risasi ya kwanza akapiga mtungi wa kuzimia moto na poda iliyokuwa ndani yake ikatoka kwa kasi na kuwachanganya wale jamaa. Kamanda Amata akapita kwa kasi huku watatu waliokuwa mbele yake wakiwa chali kwa risasi kutoka kwenye bastola yake, sekunde mbili tu alikuwa keshafika mlangoni na kuufunga kwa nje akiwaachia kizaazaa. Ujia mrefu ulimkaribisha. Ving’ora vya hatari vikalia kila kona, mvurugano ukaanza kila kona, burudani zikasimama na kelele za vilio nzikaanza huku na kule.

  • * *

Chiba aligundua hali ile baada ya kusikia kelele za watu, akapachika head set yake masikioni tayari kwa kazi.

“Amata vaa barakoa yako kazi inaanza,” Chiba akaongea kwenye kile kifaa na kisha akavaa kinyago chake cha kuzuia gesi ya machozi na kinachoweza kumfanya aone gizani bila tabu. Akatazama huku na kule akaona sensor ya moshi ambayo ikipata moshi basi huruhusu maji kumwagika, akatazama huku na kule akaona ua jirani, akavuta karatasi la urembo lilikuwa hapo akawasha moto na kisha akasogeza karibu na ile sensa, nukta hiyohiyo jengo zima likaanza kutiririsha maji, Chiba akaifuata swichi kubwa ya umeme na kuizima kisha akaondoa fyuzi na kuzitupa mbali. Sasa jengo lote lilikuwa giza na jenereta liligoma kuwaka, tayari kijana huyo wa TSA alishapita na kuondoa betri. Yale maji yaliyokuwa yakimwagika nayo yakakatika ghafla.

  • * *

UKUMBI wote ulishikwa na kimuhemuhe, Amata alichomoa bastola yake yenye mabomu ya machozi na kutawanya huku na kule. Moshi huo mzito uliwafanya watu kukohoa bila kikomo, wakiishiwa nguvu na wengine kuanguka chini hawajiwezi.

Pancho Panchilio, aliinuliwa pale alipoketi na vijana wake kama saba hivi wakawa wamemzunguka kwa kumlinda wakiwa na silaha zisizojua huruma. Kutokana na gia lile walishindwa kumwona sawasawa Amata hivyo ilikuwa ni rahisi kwake kuwatawanya kwa risasi. Zilipomwishia akaruka sarakasi na kutua karibu kabisa na Pancho Panchilio huku miguu yake ikiwatandika mateke walinzi wawili waliobaki. Pancho alitaka kukimbia kuingia kwenye mlango mmoja lakini hakufanikiwa, ngwala moja maridadi ilimbwaga chini vibaya, wale vijana walipojaribu kunyanyuka, risasi za Chiba ziliwarudisha chini na Amata akapata nafasi ya kuinuka na kukutana uso kwa uso na Pancho.

“Twende nyumbani mwanaharamu wewe!” kamwambia huku akimtandika konde moja kali lililomfanya ayumbe na kupoteza mwelekeo. Konde la pili likamrudisha chini akiwa hoi, pamoja na ule moshi kumlegeza. Amata alijikuta akishikwa na hasira akikumbuka mtu huyo alichowafanyia yeye na wenzake kule Kerege katika mkasa uliopewa jina la Kitisho.

Kabla hajafanya lolote, akajikuta akipigwa na kitu kizito kisogoni, lakini mpigaji hakulenga sawasawa, Amata akageuka na kupeleka mashambulizi makali yaliyolifanya lile jitu lipoteane lenyewe kwa lenyewe. Lilipotulia likajikuta likitandikwa risasi mbili za kifua.

“Hatuna muda wa kupoteza, nasikia ving’ora vya wanoko huko nje,” Chiba alimwambia Amata, na wakati huo huo, Amata akamkamata mkono Pancho na kumkokota kwa nguvu. Mirindimo ya risasi bado ilikuwa ikiendelea, moshi wa machozi ulikuwa umechanganyika na ule wa baruti na kulete harufu ya tatu.

“Ondoka naye Amata, mi nalinda mkia wako,” Chiba alimwambia tena braza ‘ake na Kamanda Amata akatoka na Pancho, alipoona upinzani umekuwa mkali akambeba Pancho na kuruka naye ghorofa ya chini yake wakafika hoi. Amata akawahi kunyayuka na kutumia bastola yake nyingine kupambana na wawili watatu waliokuiwa mahali hapo na kujaribu kumletea zengwe.

Haraka akaiwahi gari iliyokuwa imeegeshwa hapo na kufungua mlango.

‘Asante sana’ akashukuru baada ya kukuta funguo ikining’inia, akafungua buti.

“Ingia!” akamwamuru Pancho huku akiwa amekiinua kile kinyago chake na kukiweka kwa juu, Pancho akapigwa butwaa kumwona kiumbe huyo matata.

“Unashangaa nini? Ingia unanipotezea muda,” kamanda akang’aka lakini Pancho hakutaka kufanya hivyo. Konde moja la tumbo likamfanya Pancho ajiinamie huku amejishika tumbo lake, teke la kusukuma lilipeleka mpaka kwenye buti na Kamanda Amata akamalizia kufunga buti hilo kwa mguu kisha akaingia kwenye usukani, akaiwasha gari hiyo na kutoka kwa kasi huku akigonga geti na kukunja kushoto. Mfukuzano na gari za polisi ulichukua nafasi katika barabara za Bombay. Amata aliwapeleka nje ya mji kwenye barabara ya hatari kabisa, yenye mteremko mkali na wenye kona za ajabu, ambapo wengine waligwaya na waliojaribu walijikuta wakiishia shimoni.

Baada ya kuhakikisha wote kawaacha mbali Amata alichukua uelekeo wa Bahrain house na kuliacha jiji hilo. Saa tisa za usiku akaegesha gari ndani ya jengo hilo kuukuu, akateremka akiwa hafai kwa vumbi lililomkaa mwilini. Akafungua buti na kumtoa Pancho aliyekuwa kajikunyata ndani yake.

“Shuka!” akamwamuru naye akashuka. Akamkokota mpaka ndani ya chumba kimoja kikubwa.

“Pancho Panchilio au Premji Kanoon, karibu katika himaya yangu, mara hii ni zamu yako,” Sauti ya Madam S ikasikisa na taa yenye nuru hafifu ikawaka. Madam S akainuka alipoketi na kumjongelea mtu huyo. Kofi moja kali lilitua shavuni mwa Pancho na kumwacha akitetemeka.

“Ulifikiri utafanikiwa kunikimbia? Twende nyumbani nikakuoneshe kama mimi ni Head of T.S.A,” Madam akaunguruma na kumpa pingu Amata naye akamfunga mikono yake na mnyororo akautia miguuni mwake. Akamkokota mpaka kwenye ile gari waliokuja nayo na Chiba mara ya kwanza.

“Nafasi yako ni kwenye buti tu, akamwingiza na kulifunga kisha akatulia nyuma ya usukani huku kushoto akimwacha Madam S.

“Chiba, Chiba, wapi?” Kamanda akauliza kwenye kile chombo chake.

“Naegesha boti nimefika,” akajibu.

“Weka kiberiti,” akampa agizo. Baada ya sekunde chache Chiba aliungana na wenzake na kuingia siti ya nyuma.

“Mzigo uko wapi?” akauliza Chiba.

“Upo mahala pake,” akajibu huku akiondoka eneo lile na kupita njia za vichochoroni.

“Kilomita ishirini na mbili kijiji cha Malve” Madam S alimwambia Amata na moja kwa moja akaelekea huko nje kabisa ya mji.

Hali ya utulivu ilitawala kijiji kile watu wote walikuwa wamelala ndani ya nyumba zao, ni miti tu iliyokuwa ikitikiswa na upepo wakati Amata akiegesha ile gari katika moja ya kichaka karibu na barabara kubwa inayoelekea baharini, barabara ya vumbi. Dakika mbili tu Scoba akatua na ndege ndogo aina ya Boeing yenye uwezo wa kubeba watu watano lakini yenye nguvu na kasi ya kutosha. Ndege hii ilinunuliwa na serikali ya Tanzania kwa kazi maalumu kama hizi na pia kwa ulinzi wa haraka wa Rais wa nchi inapobidi. Nje ya kumhudumia Rais, ni TSA pekee waliweza kuitumia ndege hii na ni kwa kibali cha Rais tu.

Scoba, akatumia barabara hiyo kutua kwa kutumia mwanga wa tochi alizowasha Madam S akiwa chini kwa ishara aliyompatia. Hakuna kusubiri, walimkokota mtu wao na kumpakia ndegeni, huku kwa mbali wakisikia ving’ora vya polisi vikielekea upande wao.

“Haraka, haraka, haraka,” Madam alihimiza na mlango ukafungwa, Scoba moja kwa moja aliiongeza nguvu ile ndege na kuodoka kwa kasi huku akiwaacha wale polisi wakijaribu kufyatua risasi bila mafanikio. Dakika moja ndege ile ikawa angani ikikata bahari na kuelekea katika anga ya kimataifa ambako huna ruhusa kuifanya lolote.

  • * *

“Na leo hii utatakiwa kusema siri zote ulizozificha mwanaharamu wewe!” Madam S alimwambia Pancho kwa ukali mara baada ya ndege ile kukaa sawa angani na kila mtu kuweza kufanya shughuli yoyote. Pancho Panchilio alitulia kimya akiangalia kwa jicho la kukata tamaa huku mwili wake ukionekana bado kukosa nguvu kwa kipigo cha rasha rasha alichokipata kutoka kwa Amata.

“Kamanda mwondoe hapa mpeleke kwenye chumba cha mwisho,”

Kamanda Amata akanyanyuka na kumchukua Pancho kwa kuushika ukosi wa shati lake, akamkokota mpaka katika chumba hicho na kumtupia humo. Mlango ukafungwa na ukimya ukatawala.

“Najua hauko peke yako kwenye mtandao huu, Mahmoud na mwenzake tulishawakamata wewe ukatutoroka kijanja. Na wale vibaraka wako wengine kule Kerege tumewakamata na wengine wamekufa wenyewe lakini wewe bado umetukimbia. Hukutukimbia tulikuwa tunaendelea kukuchunguza na sasa arobaini zako zimefika, haya nitajie mmoja baada ya mwingine kabla hatujatua Dar es salaam,” Madam S alionekana kuwa na hasira kali juu ya mtu huyo. Pacho alibaki kimya hakuzungumza lolote.

“Jeuri!” Amata akasema, kisha ghafla akapiga teke kwenye korodani lililomfanya Pancho apige kelele za maumivu na kuikusanya mikono yake yenye pingu katika eneo hilo.

“Utasema?” Kamanda akauliza. Lakini Pancho bado alibaki kimya huku akigugumia kwa maumivu makali. Amata akachukua kiberiti cha gesi na kukiwasha kisha moto wake akauweka chini ya kidevu cha Pancho. Maumivu aliyoyapata kwa moto ule uliokuwa ukiichoma ngozi akashindwa uvumilivu.

“Aaaaaaiiigghhh! niache! niache! nasema! nasema!” akapiga kelele.

“Sema, upo na nani kwenye mtandao?” Amata akauliza.

“Kamba Sebule, Kamba Sebule,” akataja jina la mtu mkubwa ambaye ni balozi wa nchi wa Tanzania katika nchi fulani.

“Na mna misheni gani hapa?”

“Mapinduzi ase aaaaiyyayayay aaaaiiiggghh! We muuaji wewe,” akalia kwa uchungu.

“Mwingine nani?”

“Alibaki huyo huyo, aaaaaaghhh!”

“Hutaki kusema ee? Sasa nakutupa nje kwa huna faida wewe,” Kamanda akamwambia Pancho kisha akamtazama Madam S.

“Madam! Jishike vyema namtupa nje huyu mshenzi,”

Akabonyeza kitufe fulani na mlango ukafunguka taratibu, upepo mkali ukaingia ndani na kuleta ufumbufu mkubwa huku ndege ile ikiwa juu futi 40000.

“Utasemaaa au husemiii?” Kamanda aliuliza kwa kelele huku akimtazama Pancho. Akabaki kimya bila jibu. Amata akamsukuma na kumtanguliza kichwa nje, akamsukuma nje. Pancho akatoka mlangoni na kuning’inia vibaya.

“Aaaaaiihhhh, weweeeeeee! Niache nasema kila kituuu, ohhhhh! Nooooo!” Pancho akapiga kelele.

“Sema, mna misheni gani?”

“Mapinduzi, mapinduzi asee,” kutokana na upepo mkali Pancho aliyumba na kujigonga kwenye ubavu wa ndege. Kamanda Amata akatumia nguvu zake zote na kumvuta ndani akambwaga kando huku ule mlango ukijifunga taratibu. Pancho alipoteza fahamu na kutulia kimya.

“Kamba Sebule,” madam S akarudia jina hilo.

“Vipi?” Amata akauliza.

“Inabidi achunguliwe mara kwa mara asije kutupotea kuanzia sasa,” akajibu.

Madam S na Amata wakatoka katika chumba kile na kumwacha Pancho akiwa hajitambui damu ikitiririka usoni huku pingu na mnyororo vikiwa vimemdhibiti.

“Vipi?” Chiba akauliza.

“Poa, yupo huko kapumzika,”

“Yuko down?” (amekufa?)

“Hapana anaelea tu,” (hapana amezimia tu)

“Kinachoendelea?” Chiba akauliza.

“Kamba Sebule, yupo kwenye mtandao,” Amata akajibu huku akiketi sawia kitini. Chiba alibaki kakodoa macho kwa taarifa hiyo, hakutegemea mtu kama Kamba Sebule kuhusika kwenye mtandao wa maovu kama huo.

DAR ES SALAAM – saa 2:30 asubuhi

Saa tano ziliwaweka hewani na asubuhi ya saa mbili na nusu waliwasili uwanja wa ndege wa jeshi, Dar es salaam. Gari jeusi lenye boksi kubwa nyuma lilisogea taratibu mpaka kwenye ile ndege na kusimama jirani kabisa. Pancho Panchilio aliteremshwa na kuingizwa kwenye hiyo gari haraka na kufungiwa humo, askari wawili wenye silaha wakaingia pia sehemu ya nyuma, milango ikafungwa na safari ikaanza.

“Asanteni sana kwa kazi vijana,” Madam S aliwashukuru Amata na Chiba.

“Ndiyo wajibu wetu,” Chiba akaitikia.

“Sasa mpumzike kisha kesho jioni tuonane ili tuweke mambo sawa juu ya mtu huyu,” Madam akamaliza kusema na kuingia garini, Scoba akaondosha gari iliyombeba Madam S. Chiba na Amata waliingia kwenye gari jingine alilokuja nalo Gina wote wakaondoka uwanjani hapo.

Siku hiyohiyo …

BAGAMOYO

VIJANA KAMA SABA hivi walikuwa katika chumba kimoja cha jengo lililochini ya ardhi katika kisiwa kimojawapo kati ya visiwa vinne katika bahari ya Bagamoyo. Vijana hao wote walivalia mavazi meusi na kofia zao zilificha hadi nyuso na kuruhusu macho tu kuonekana. Mikono yao waliifutika kifuani na kufanya wote wawe katika mtindo mmoja wa kupendeza. Kati yao mmoja ndiye alikuwa na mkanda mpana mwekundu katika kiuno chake.

Vijana hawa walikuwa ni jeshi la siri sana la Pancho Panchilio, walikuwa wamefuzu mafunzo Ninjutsu huko Uchina kwa nyakati tafauti. Gabacholi huyu aliwaajiri na kuwaweka katika himaya yake, maalum kwa kazi maalum.

“Komredi ametekwa,” akawaambia wale vijana wengine.

“Usiku wa kuamkia leo pale Bombay, washenzi wamemchukua komredi na mpaka tunavyoongea sasa ameshafikisha hapa nchini,” akaendelea kusema; “hii inaonesha dharau kubwa sana kwetu, kwa kuwa wale jamaa tulifanikiwa kuwateka wote wakatutoka kwa namna ya kibabe sasa naona wametugeukia sisi. Hatuwezi kuwaacha, sasa ni vita na vita hii ninaitangaza sasa. Komredi lazima akombole ndani ya saa sabini na mbili hata kama atakuwa amefichwa Ikulu, ohi?”

“Oha!” wakajibu kwa pamoja kumaanisha kuwa wanajua na wanaelewa kile walichoambiwa, wakaiondoa mikono yao kifuani na kukutanisha viganja kisha wakainama. Baada ya mazungumzo mafupi wakatawanyika na wawili kati yao wakabaki pamoja na Yule aliyevaa vazi lenye mkanda mwekundu wakaketi katika meza hiyo ya duara pamoja wakijadiliana jambo.

“Tutatumia gharama yoyote tumpate,” mmoja wao akasema.

“Hilo ndilo hasa nalitaka tuzungumze, mambo waliyoyafanya Bombay kule si madogo, wamedhalilisha hekalu la Hanuman,” mwingine akadakia.

“Yote tuyaache, mpango wao ukoje mpaka sasa na wapi amehifadhiwa?” Yule wa kwanza akavunja mazungumzo.

“Kutoka chanzo chetu cha habari wanasema jamaa kahifadhiwa Keko, lakini kesho kutwa atafikishwa Kisutu mahakamani,” Yule kiongozi akajibu.

“Baaasi mpaka hapo kazi imekwisha, lazima atekwe ama anavyokwenda au anavyotoka,” mwingine akajibu huku akipiga ngumi mezani.

“Nani wa kulainisha mipango? Si unajua wote wapo lupango,” Kiongozi akauliza.

“Aaaaa Mkuu hilo ni dogo, Kamba Sebule na Maliapopo si wapo? Watafanya kazi,”

“Na hata hizi habari ni Maliapopo aliyenipatia na yuko sambamba na kila linaloendelea atatujulisha,” akamaliza na kuwaomba vijana wakae tayari kwa lolote watakaloambiwa.

GEREZA LA KEKO

PANCHO PANCHILIO aliketi sehemu ya peke yake, mikono yake ikiwa na pingu kama alivyoletwa siku iliyotangulia. Chumba chenye mtindo wa duara kilichojengwa kwa vyuma imara pande zote, ndimo alimohifadhiwa mtu huyo. Taa yenye mwanga mkali wa watts 750 ikawashwa na kummulika mtu huyo muda wote, joto kali likamtesa, mwili ukatota kama aliyemwagiwa maji.

“Aaaaaigh Shit!” aling’aka baada ya taa ile kummulika usoni moja kwa moja kila ajigeuzapo.

“Acha kupiga makelele ya kitoto bwege we!” Madam S alimwambia huku akisogea taratibu na vijana wake Chiba na Amata wakiwa nyuma yake.

“Kesho mahakamani,” akamwambia.

“Afadhali haki ikatendeke maana hapa mnanionea tu,” Pancho akajibu.

“Haki? Unaijua haki wewe? Ungeijua haki ungefanya yote uliyoyafanya? Pancho au nikuite Premji Kanoon, nchi iliyokulea unaweza kuifanyia haya? Kudhulumu haki, haki ya mwananchi mdogo anayevuja jasho la chumvi na kulilamba kwa kukosa maji safi ya kunywa lakini wewe na mabwanyenye wenzio wenye matumbo makubwa yasiyo na shukrani mnahamisha fedha na kuzificha ughaibuni,” akameza mate, na kuendelea, “Pancho! Kweli kabisa unadiriki kukifutilia mbali kikosi hiki unachokiona ili tu uendeleze biashara yako haramu, unaniteka mimi wewe, unateka vijana hawa uwaue halafu ufanye nini kwenye nchi hii? Kila anayekaribia kung’amua madhambi yako unataka ummalize. Siku yako imefika, nimekufuata India kwa gharama ili nikuoneshe kama mimi ndiye Madam Selina, mwanamke wa chuma tena chuma cha pua, kama kukuua ningeshakuua long time ila nilitaka kwanza nikuoneshe jeuri yangu kisha nikusweke jela maisha yako yote …”

“Kamwe, Pancho Panchilio hawezi kuingia jela, ha! Ha! Ha! hiyo sahau we mwanamke, utaiona miujiza yangu kabla ya kufika jela au hata mahakamani, mtatafutana ninyi nakwambia na hapo ndipo mtashuhudia mmoja mmoja wenu akianguka na kufa wakati mi narudi kuishi maisha yangu ya anasa. Ikitokea wewe ukabaki hai basi nitakualika kwenye tafrija kubwa pale Kilimanjaro Hoteli kisha utaona nani na nani wamealikwa, ndipo utakapojiona upumbavu wako we mwanamke ni mwanamke tu…”

Madam S alijikuta akishikwa na hasira akachomoa bastola yake.

“Rudia maneno yako nikupasue fuvu hilo,” aliongea kwa hasira.

“Ha! ha! ha! ha! Muoneni bibi yenu huyu, hana akili kabisa,” aliwaambia kina Chiba na Amata. Kama alifikiri anamuuzi mwanamama huyo pekee, basi alikosea sana, kitendo cha ghafla, Pancho alijikuta akipoke teke moja la kilo nyingi usoni, akajipiga kisogo ukutani kisha akaanguka sakafuni, kimya!

“Funga domo lako! Punguani wewe,” Amata akaunguruma. Sekunde chache Gabacholi huyo akajiweka sawa tena mara hii sura yote ilikuwa nyekundu.

“Tena wewe! Wewe! Wewe! Ipo siku yako. Nitakutoa huo utumbo niuanikie nguo,” Pancho alimwambia Amata.

“Utafanya hayo kabla bastola yangu haijafumua ubongo wako,” Amata akamaliza na kumtazama Madam S aliyekuwa amekunja sura kwa uchungu.

“Kesho Mahakamani,” Madam akamwambia Pacho na kugeuka kuanza kutoka ndani ya chumba kile maalum.

  • * *

SIKU ILIYOFUATA

Asubuhi ya siku iliyofuata, Pancho Panchilio aliandaliwa tayari na kupelekwa mahakamni ili kusikiliza shitaka lake. Magari ya magereza na lile la FFU yalikuwa tayari mbele ya gereza hilo la Keko. Ulinzi mkali uliimarishwa kuzunguka ngome hiyo kwani taarifa kwa vyombo vya usalama ilikwishatolewa kuwa mtuhumiwa huyo ni mtu hatari sana. Vijana wa kazi walikuwa tayari kwa lolote.

Akiwa chini ya ulinzi mkali, Mhindi jeuri huyo alitembezwa taratibu huku miguu yake ikiwa imefungwa kwa minyororo na kisha mnyororo huo huo kuunganishwa na kuishika pingu iliyoifunga mikono yake. Msafari ulianzia Keko kuelekea Kisutu ambako shauri lake lilitakiwa kusikilizwa. Kwa kuwa barabara zote yaani ya Chang’ombe, Nyerere, Bibi Titi zilizuiwa magari kupita kwa dakika kadhaa, iliwachukua dakika kama kumi na tano tu kuwasili katika mahakama hiyo huku Pancho akiwa ndani ya gari maalumu iliyozibwa pande zote.

Mahakama ilifurika watu, kama kawaida, waandishi wa magazeti na wale wa televisheni walikuwa bize kutafuta habari lakini zaidi kuipata picha ya mtu huyo. Baada ya yote kukamilika na shauri hilo kuahirishwa, Pancho alitakiwa kurudishwa rumande mpaka baada ya mwezi mmoja ambapo ushahidi utakuwa umekamilika. Gari lile lililomchukua kutoka Gereza la Keko, ndiyo iliyokuja gerezani hapo kumbeba kwa mara nyingine na sasa ilikuwa na kazi ya kumrudisha mahabusu. Alitolewa akiwa chini ya ulinzi mkali mnyororo wake miguuni na pingu mkononi, moja kwa moja akaingizwa ndani ya gari hiyo isiyo na dirisha hata moja katika eneo la kuifadhi wahalifu. Baada ya kufungwa mlango wake askari wawili wenye silaha walikaa katika kijichumba kidogo wakiwa na bunduki zilizoshiba vyema.

Msafara ukaanza kutoka katika gereza hilo, gari la polisi likatangulia mbele likipiga ving’ora vya kuomba njia, kisha likafuatia hilo lililombeba mhalifu na mwisho kulikuwa na gari jingine la askari magereza wenye silaha, safari kuelekea Gereza la Ukonga na sio Keko tena ikaanza kwa kasi huku gari nyingine zikiacha njia na kuupisha ule msafara uende. Kasi iliyokuwa kwa gari zile haikuwa ya kawaida, kila mtu alishangaa na kujiuliza ‘kuna nini?’

Wakati huohuo…

Barabara ya Shaurimoyo na Nyerere

Ndani ya gari moja lililoegeshwa muda mrefu katika Barabara ya Shaurimoyo, watu sita walikuwa kimya kwa muda mrefu, na mara ukimya ule ukakatishwa kwa biip moja ya simu ya kiongozi wao. Kutoka kiti cha mbele alichoketi akageuka nyuma na kuwatazama viajan wake.

“Mko tayari? Tunafanya kazi sasa, dakika tatu kila kitu kiwe kimekamilika, kwa kuwa wao hawajajiandaa kwa hilo basi itakuwa ushindi ni upande wetu, ohi?”

“Oha!” wakaitikia vijana wa kazi waliovalia nguo za khaki, na bunduki zenye risasi tele migongoni mwao, nyuso zao zilikuwa tayari kufunikwa na barakoa za kukinga gesi ya machozi, walikamilika.

Kiongozi wa operesheni hiyo aliinua redio yake ya upepo na kuiweka karibu na kinywa chake.

“Namba one, namba one, stand by!” akaongea.

“Umesomeka, namba one stand by,” akajibiwa.

“Namba one on your marks… Get set… go!” Yule kiongozi alitumia mtindo unaotumika na wanariaadha kutimua mbio.

Kutoka upande wa Keko, karibu kabisa na eneo la daraja la leri pembezoni mwa Kiwanda cha Uchapaji cha Taifa, liliwashwa tingatinga na kuchomoka kwa kasi kuelekea barabara ya Nyerere. Hamad! Wakati ule msafara unafika na lile tingatinga linafika, ajali mbaya isiyosemeka ikatokea. Lile tingatinga likaigonga gari ya mbele ya polisi na kuharibu vibaya, haikuishia hapo, iliigonga ile gari ya kubeba mhalifu na kuikunga njia, ikaibana karibu na gema la daraja. Mtafutano wa watu ukaanza asubuhi hiyo katika eneo lile.

Kutoka kwenye lile gari la askari maalum wa magereza, waliruka na kutua nje kila mmoja akachukua sehemu yake kwa kuangalia nini kinatokea. Kabla hawajakaa sawa, gari aina ya Range Rover ikaingia kwa kasi na vijana kama sita hivi wakateremka haraka na kulizunguka eneo lile, mabomu saba ya machozi yakatua ardhini na wao wakavaa barakoa zao tayari kuzuia adha ya gesi ile ya machozi. Wawili kati yao haraka wakaenda kuufungua ule mlango wa lile gari, risasi zikaanza kulindima kutoka kwa wale vijana wa magereza na polisi, wakashambuliana na wale majambazi. Jambazi mmoja akapigwa risasi na kudondoka lakini hakufa bali alijeruhiwa vibaya.

Mlango ukafunguka, mmoja wa askari bado alikuwa ana nguvu zake, alimpiga yule jambazi kwa kitako cha SMG kichwani, akapepesuka na kushindwa kustahimili akaaguka chini, Yule mwenzake akatumia risasi ya moto na kupiga askari wote wa ndani kisha akaingia na kumfungua bosi wake. Mabomu ya machozi yaliongezwa na mosi ukatapakaa eneo lote.

Yule jambazi aliyetoka na Pancho akapiga aina Fulani ya mluzi na wale wenzake wote wakakimbili garini, lakini jambazi mmoja aliyekuwa mwisho ambaye kiutaratibu lazima apande mwisho, akamchapa risasi yule jambazi mwenzake aliyekuwa na hali mbaya pale chini ili kuzuia asije ongea lolote, nukta hiyo hiyo ukasikika mlio wa helkopta eneo lile, nalo likazidisha vumbi, wale majambazi na mtu wao wakajitupa ndani yake na lile dege likapotelea angani.

“Upo Salama Mkuu,” Kiongozi akamwambia Pancho.

“Yeah, hongereni kwa kazi,” akawapongeza wakati huo wakimwondoa ile minyororo na pingu mikononi mwake.

“Ha! Ha! Ha! Ha! mmewapiga chenga ya mwili,” Pancho aliwasifu vijana wake kwa lugha ambayo Yule dereva hakuielewa.

“Ijapokuwa tunasikitika tumepoteza wawili,”

“Usijali, hiyo ni najali kazini,”

“Sawa Boss”.

Ilikuwa kama filamu hivi, kwa ughafla wa tukio lile ambalo halikuchukua hata dakika tatu, askari waliokuwa wakisindikiza mhalifu huyo walijikuta hoi. Wamezidiwa ujanja, ijapokuwa waliwapiga risasi wawili lakini wao walipoteza wawili pia. Utulivu ukarudi, kilichobaki kilikuwa na mtapakao wa moshi na harufu ya baruti inayoishia kwa upepo. Watu walikuwa wakisogea taratibu kuona kulikoni. Polisi nao walifika na kuweka ulinzi eneo hilo ikiwa pamoja na kufunga barabara.

Mkuu wa polisi mkoa wa Dar es salaam alikuwa hapo akiangalia hali halisi, sura yake ikikunja ndita sehemu ya juu ya macho yake, hasira isiyojificha ilionekana wazi wazi.

“Washenzi hawa,” akang’aka kwa hasira.

Wakati polisi wengine wakiendelea kupima hapa na pale yeye bado alikuwa akiendelea kuwasiliana kwa redio yake.

“Nipo eneo la tukio, mmeona helkopta yoyote ikipita maeneo hayo?” akawauliza polisi wa anga ambao daima kazi yao ni kuvichungulia vya juu.

“Vipi Mkuu?” sauti ya Inspekta Simbeye ilimfanya yule RPC kushtuka na kumwangali mtu huyo. Wakapigiana saluti za kijeshi kisha mazungumzo yakaendelea.

“Kwa hiyo wamekuja na helkopta mpaka hapa na kumchukua mtu wao?”

“Ndiyo, lilikuwa ni shambulizi la ghafla na la ufundi wa hali ya juu ijapokuwa hata vijana wetu wamefanya kazi kubwa mpaka kuwalaza hawa wawili, sema tu ndiyo hivi wameshakufa, laiti wangekuwa hai pangechimbika,” akamaliza kusema RPC na kumwacha Simbeye akikagua hapa na pale kuona kama kuna lolote la ajabu katika ajali hiyo, alitazama hiki akagusa kile, alipindua hiki na kusimamisha kile kule arimuradi tu afanye kitu.

SHAMBA

Mchana huohuo

Simu ya mkononi ya Madam S iliita kwa fujo, alipotupa jicho mezani akaona simu inayowakawaka ni ile ya taarifa nyeti.

“Shiit, nini tena?” akaongea kwa sauti ya kuonesha kuwa hajafurahia simu hiyo, akainyakuwa na kuitega sikioni kwanza.

“Hello Sellina!” mara moja akaitambua sauti hiyo.

“Ndiyo Simbeye vipi (…) what! Unasema, (…) acha masihara katika kazi asee,”

“…Madam habari ndiyo hiyo, Pancho Panchilio kaokolewa na jamaa zake kwa njia za kikomandoo”.

Madam S akakata simu na kuitupia mezani kisha yeye mwenye akajitupa kitini na kushusha pumzi ndefu. Akawaita vijana wake wote na kuwapa taarifa hiyo ambayo iliwachanganya mpaka wakachanganyikiwa. Lakini la kutokea tayari lilikuwa limetokea.

04

KIJIJI CHA MINDE – BAGAMOYO

“Babu! Babu!” kijana wa makamo alimwita babu yake huku akiwa anahema kama aliyefukuzwa na mbwa.

“We, nini?” babu yake aliyekuwa ameketi chini na wavuvi wenzake wakiwa wanasuka nyavu zao alimjibu kwa kumwuliza.

“Ame- ameam- amemka, yule mtu ameamka…”

Yule mzee akawatazama wale wavuvi wenzake na wote wakakurupuka na kukimbimbilia kwenye ile nyumba walimomlaza huyo mtu. Walipofika waliingia taratibu bila kufanya kelele na kumtazama.

“Oooh! Ameamka, asante binti kwa dawa ulizompatia,” yule babu alimshukuru binti aliyekuwa kando na chungu chake kikubwa kilichojaa maji ya kijani.

“Bila asante, ni wajibu wangu kumsaidia,” akajibu.

Wale wazee wakasogelea kitanda na kumzunguka wakimtazama, naye pia alizidi kuwatazama kwa kuwashangaa.

“Niko wapi? Niko wapi hapa?” akauliza kwa ukali na kumkunja kanzu mzee mmoja aliyekuwa jirani na yeye.

“Aaah a a a! kijana tulia kwanza, hapa upo mahali salama kabisa,” mzee mwingine alimsihi mtu huyo kwa lugha ya pwani.

“Wewe ni nani kijana?” Yule mzee akauliza.

Yule mtu akawashangaa tena, akawatazama na kuwakazia macho, kisha akajitahidi kukaa na kuegemea ukutani.

“Naitwa Amata,” akajibu kwa kifupi.

“Amata! Pole sana Amata, tumekuokota baharini ukisukwasukwa na mawimbi makali. Mungu mkubwa kwani yalikupeleka mpaka kwenye mikoko nasi tumekuona huko, nini kilikupata kijana,”

Amata akanyamaza kimya akifikiria jambo, akijaribu kuvuta kumbukumbu kwa lile lililotokea.

Saa 20 Zilizopita…

Ajali ya ndege.

Mara tu baada ya kiti cha Amata kufyatuka na kutoka nje wakiwa angani, parachute alilokuwa akitumia Amata likagoma kufyatuka, akahangaika nalo huku msukosuko ukiendelea. Kutoka kwenye ile ndege akaanza kuanguka kwa kasi huku akielekea baharini.

“Scobaaaaaa!!!!” aliita kwa nguvu lakini mwito wake haukuwa na nguvu kwani Scoba naye alikumbwa na maswahiba yake. Kutokana na lile parachute kushindwa kufunguka, Amata alitua baharini kwa kishindo na kuzama kwa sekunde kadhaa kabla ya kuibuka juu. Kwa mbali aliiona kitu kama boti ikija kwa kasi na kupunga mikono kuomba msaada lakini badala ya msaada wale jamaa wakafyatua risasi kumshambulia, Amata akapiga mbizi na risasi mbili zikampata eneo la mbavu. Maumivu yake yalimweka kwenye hali mbaya kiasi kwamba alijikuta akipoteza nguvu. Jua lilififia machoni pake, kiza kikayafumba macho, akajikuta anapoteza nguvu na ukimya mkuu ukamchukua.

“Nimekwisha!” akajitahidi kutamka kwa taabu.

“Ma-da-m S” akajitahidi kuita kwa nguvu lakini bado aliona giza likimzidi nguvu.

  • * *

“Shabash, nimempata kwisha habari yake,” kijana mmoja alikuwa akishangilia kwenye ile boti. Huku akipiga risasi nyingine hewani.

“Una uhakika?” Mwenzake akauliza.

“We sogeza mashine pale uone, maiti tu ile,”

Ile boti ikasogea mpaka pale na kuukuta mwili wa Amata ukiwa kifudifudi juu ya maji baada ya kuibuka. Wakautazama na kuondoka zao.

“Buriani, hatuna historia ya kubeba maiti,” yule nahodha wa chombo akageuza na kuondoka zao mpaka katika kambi yao iliyojengwa katika moja ya visiwa vilivyozunguka eneo hilo huku bado wakipiga risasi hewani kuoneshya.

  • * *

Mawimbi ya bahari yakausukasuka mwili wa Amata na kuutupia kwenye mikoko iliyofungana katika pwani ya eneo hilo, na kunasa huko. Jioni ya saa kumi na mbili hivi wavuvi kutoka kijiji cha Minde walikuwa wakipita kuelekea katika shughuli zao huko katikati ya bahari, wakiwa na karabai zao wakipita pembezoni kabisa karibu na ile mimea ndipo walipouaona mwili huo.

“We hebu mulika pale,” mzee mmoja akamwambia nahodha wa chombo hicho.

“Nini?”

“Yule siyo mtu Yule?” wakatazama kwa makini na kugundua ni mwili wa binadamu, wakashuka na kutumbukia majini mpaka eneo lile.

“Oh Shit, si ajabu akawa hai huyu, mtazame!” wakamgeuza geuza na kuamua kumbeba. Safari ya kwenda uvuvini ikaghairishwa na wazee wale wakaamua kurudi kijijini. Walifika na kumshusha Amata kisha wakamlaza chini mkekani huku wakisogeza moto jirani ili kumpa joto. Mzee mmoja alikwenda kumwita binti anayesifika kujua dawa za asili, akaja na kuanza kumfukizia Amata moshi wa mchanganyiko wa majani na magome makavu ya miti.

“Hajafa bado huyu?” mzee mmoja akauliza.

“Hapana hajafa huyu, ila amezimia na yuko mbali sana katika mzimio wake, ninamwita polepole ataamka tu,” yule binti akajibu.

Matibabu hayo ya kienyeji yaliendelea mpaka asubuhi yake na mchana wa siku hiyo Amata alirudiwa na fahamu

Siku ilofuata

Amata alitoka nje ya nyumba hiyo majira ya saa nne asubuhi, akasimama nje na kuangalia upande wa baharini, akiwa hajui ni wapi alipo mpaka dakika hiyo. Akiwa bado hajisikii vyema sana hasa sehemu fulani za mwili wake ambako kulikuwa na kitu kama jeraha aliendelea kutembea hapa na pale pale kijijini akiangalia hiki na kile. Kila hatua chache alisimama kutokana na maumivu aliyokuwa akiyasikia katika maeneo ya mbavu. Kila alkisjidhika aligundua kuwa kulikuwa na majeraha. Nyuma yake akahisi mchakacho wa nyayo za binadamu, akasimama na kusubiri.

“Naona una nguvu sasa,” sauti nyororo ya kike ikasikika nyuma yake, akageuka na kugongana macho na mwanadada mrembo aliyekuwa ndani ya mavazi ya kawaida kabisa ya kijijini.

“Ndiyo, sasa najisikia nafuu zaidi, ila maumivu tu eneo hili,” akamjibu na kumwonesha eneo lenye maumivu.

“Pole, unywe ile dawa niliyokupa, ndani ya saa sita mpaka kumi zijazo utajisikia sawa kabisa, ni dawa nzuri kwa majeraha kama hayo,” Yule mwanadada akamweleza.

“Unaitwa nani?” Amata akauliza.

“Minde!” akajibu huku wakiwa wanatazamana na Amata.

“Asante Minde, umeokoa maisha yangu, unastahili zawadi, zawadi kubwa kabisa. Niambie hapa ni wapi?”

“Hapa ni Minde,”

“Minde tena?” Amata akauliza kwa kupata uhakika.

“Ndiyo, usishangae, kijiji hiki kinaitwa Minde na mimi naitwa Minde,” yule mwanadada akamweleza Amata kisha akauchomoa mfuko wa plastiki ndani ya kanga yake kuukuu na kumpa Amata. Alipoupokea alihisi wazi uzito wa kiasi wa mfuko huo, akaufungua ndani na kuangalia, akatabasamu kisha akamwangalia binti yule kwa kumkazia macho.

“Minde!” akaita kwa sauti tulivu.

“Umevipata wapi hivi?” akauliza.

“Nimevitoa kwenye nguo zako ulizovaa,” akajibiwa. Kamanda Amata akavimwaga juu ya jiwe lililokuwa jirani. Kwanza akachukua bastola iliyokuwa hapo, akaivuta slider yake na kuirudisha, akaifyatua kitako na kuchomoa magazine iliyojaa risasi, akazipachua moja moja na baadae akazirudishia tena. Akamtazama Minde akamwona jinsi alivyojawa na woga.

“Mbona unaogopa?” akamwuliza.

“Mmm umejuaje kama naogopa?”

“Nikimwangalia mtu usoni huwa najua kila kinachofanyika ndani ya ubongo wake,” wote wakacheka.

“Basi we unafaa kuwa mtabiri!”

Amata akachukua waleti iliyokuwa pamoja na hivyo, akaifungua na kukuta kila kitu chake kipo salama, ndani yake licha ya vitambulisho kulikuwa na fuba la pesa za kitanzania kama shilingi laki tatu hivi, akachomoa noti kadhaa zilizofungwa vyema. Akazihesabu harakaharaka zilikuwa shilingi laki moja.

“Hii zawadi yako Minde,” akamkabidhi, binti yule akamtazama Amata kwa jicho la uchu na kumshukuru kwa kibantu. Amata alimkumbatia Minde mikononi mwake huku akimwangalia usoni na kuyaona macho yanayojaa machozi.

ITAENDELEA

Msako wa Mwanaharamu Sehemu ya Nne

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment