Noti Bandia Sehemu ya Pili
KIJASUSI

Ep 02: Noti Bandia

SIMULIZI Noti Bandia
Noti Bandia Sehemu ya Pili

IMEANDIKWA NA: BEN R. MTOBWA

*********************************************************************************

Simulizi: Noti Bandia

Sehemu ya Pili (2)

Baada ya mpango huu kuwekwa sawa, mjadala mwingine ulianza, walibuni mbinu nyingi za kuchukua pesa kwa wafanyabiashara matajiri na baadhi ya wastaafu walioorodheshwa bila kusababisha madhara. Mbinu hii ilipangwa na Carlos mwenyewe, mzungu huyu alikuwa na mbinu nyingi na kuwafanya washiriki wa mtandao huu kutegemea zaidi mawazo yake.

Pamoja na kumiliki pesa nyingi, ambazo walifanikiwa kuziiba kwenye mabenki kadhaa ya Dar es Salaam. Pia waliweza kusafiri ndani na nje ya nchi wakitumia hati bandia na mbinu hizi na zile kujipatia pesa.

Carlos Dimera alikuwa karibu na baadhi ya viongozi wa serikali. Nchini Tanzania, alikuja nchini kwa mgongo wa mwekezaji aliyekuja kujenga kiwanda cha kutengeneza tembe maalumu za kope za urembo wa akina dada. Kutokana na ukarimu wake alifahamiana na kila mtu. Machoni mzungu huyu alionekana kama rafiki wa kila mtu, lakini moyoni alikuwa adui mkubwa wa maendeleo ya taifa.

Kumbukumbu zilionyesha kuwa mzungu Carlos Dimera alikuwa amefukuzwa kutoka katika baadhi nchi za Afrika ambako alibainika kufadhili vikundi vya wahalifu. Nchi ya mwisho kutimuliwa ilikuwa Rwanda, ambako aliishi kwa zaidi ya miaka mitatu, akitokea Kampala, nchini Uganda baada ya kutiliwa shaka. Alipoingia Dar es Salaam Tanzania hakuwa mgeni katika nchi ya Afrika Mashariki, kwani alimudu kuongea kwa ufasaha lugha ya kiswahili hivyo haraka aliweza kuunda mtandao wake na kuanza kazi rasmi.

Maofisa kadhaa wa idara za serikali, waliokuwa na dhamana ya kusimamia pesa za umma waliibiwa kwa mbinu hizi na zile, baadhi waliona aibu kuripoti taarifa hizo polisi wakihofia kufukuzwa kazi wengine wakijipeleka polisi wenyewe wakidanganya wamevamiwa na majambazi.

Baada ya kuingia Jijini Dar es Salaam, haraka Carlos aliweza kujenga hekalu au jumba kubwa la kisasa kando ya bahari na kuiomba serikali imruhusu kuweka walinzi wake binafsi, baada ya kupata kibali, aliweka ulinzi mkali kuzunguka jumba hili, akiwatumia askari wa kukodi kutoka kitengo maalum cha ujasusi cha Havana, nchini Cuba.

Vinywaji na vyakula vya aina mbalimbali vililetwa, wajumbe walikula, wakanywa na kusaza, wakiifurahia faida ya kazi yao, kila mmoja alionekana mwenye furaha kupita kiasi, wakimuomba mungu awasaidie kufanikisha jukumu lililokuwa mbele yao.

Pamoja na wajumbe hawa, Carlos Dimera, alikuwa na vijana wengine watatu ambao huonekana kwa nadra sana. hawa waliokuwa wamehitimu vizuri mafunzo ya ujasusi sehemu mbalimbali duniani, vijana hawa pia aliwatumia kwa nadra sana, hususan pale Simba, Chui na Nyati wanapokuwa wameshindwa kutimiza moja ya majukumu yao. Simba, Chui na Nyati walikuwa mfano wa mbwa mwitu, kazi yao kubwa ilikuwa kuteka au kuua watu pale wanapoagizwa kufanya vile.

Kufukuzwa kwa Carlos katika baadhi ya nchi hizo haikumfanya kuvunja mitandao yake huko, kazi ziliendelea kama kawaida kwani ndiye aliyeanzisha utapeli wa noti za bandia, pia ndiye muasisi wa kutegesha vyura, mijusi na wadudu kwenye baadhi ya ofisi za serikali na hivyo kuwafanya watumishi wa ofisi hizo, Mawaziri, Makatibu Wakuu wa Wizara na Wakurugenzi kuzikimbia ofisi zao wakiamini kurogwa na wakati huo huo vijana wa Carlos Dimera wanageuka kuwa waganga hodari wa tiba na kufanikiwa kujipatia mapesa mengi kutoka kwa vigogo hao.

“Bosi, nakuhakikishia vijana wako tayari kwa kazi, tumefanya mengi kupitia ubunifu wa kichwa chako, ili tusonge mbele lazima mtu afe, mtu huyo anajiita Kapteni Teacher, kama alipona katika shambulizi la jana, leo hawezi kuchomoka, vijana wameapa”, alisema Hawa kwa kujiamini.

Mwana mama huyu alikuwa katili na kipenzi cha Carlos Dimera, alikuwa na sifa kadhaa za kumfanya awe kipenzi cha mzungu huyu, moja ya sifa hizo ni ukatili pia alikuwa na uwezo wa kubadili jambo, akalisimamia kwa nguvu zake zote hata likawa sheria au kanuni.

“Sikilizeni, nimepata ujumbe wa maandishi kutoka kwa wanaspoti wetu, kama mtakumbuka wiki iliyopita tuliweza kuchukua kiasi kikubwa cha pesa kwa watu wawili, mmoja ni Waziri mstaafu huko Mikocheni, mwingine ni mfanyabiashara wa Sinza”. Carlos Dimera aliwaeleza.

“Naam bosi, kilikuwa kibarua kigumu mno, lakini tuliweza kufanikiwa, kuna nini bosi?” alihoji Jackina aliyekuwa kiongozi wa operesheni hiyo.

“Wahusika wametoa taarifa polisi. Lakini sina tatizo na jeshi la polisi, hawa ni watu wetu wanachukua mshahara hapa, mbaya ni kwamba malalamiko yamepelekwa idara ya usalama inayosimamiwa na wanajeshi, Hawa amesema tuna watu wetu huko lakini haitoshi, wanajeshi ni kigeugeu. Jaribio la jana lilikusudia kumuua Teacher na kutoa onyo, baada ya jaribio hilo kushindwa naamini adui yetu atajipanga vizuri zaidi, akionekana popote ua kwanza”, alisema Carlos Dimera.

Baada ya kutafakari kwa sekunde kadhaa, Jakina akasimama, “Taarifa kutoka kwa wana mtandao wetu ni kwamba idara hii inawategemea sana maofisa wake wawili. Huyu Kapteni Teacher na mwingine anaitwa Fred, huyu ni afisa wa cheo cha Luteni.

“Safi sana Jackina, ndiyo sababu nakuamini sana, naamini kazi yako itafanyika vizuri, ukitoka hapa pita kwa mhasibu akuongezee nguvu, ikiwezekana Teacher na huyu Fred wasilione jua la kesho. Lakini jitahidi kuwahadharisha vijana wako wasiende kichwa kichwa kwa watu kama hawa”, Carlos Dimera alishauri.

“Kuhusu hilo ondoa shaka bosi, hivi tunavyoongea vijana wako nyuma yake, tumewahadharisha wasiwe na papara, kazi hizi hazitaki papara, subiri wakati ufike, utasikia”, alisema Jackina kwa kujiamini.

“Naamini kuwa wote mmeinjoy vizuri, haya ndiyo maisha, nani kati yenu atapenda kurudi kijijini, aanze maisha ya kijijini, unaamka alfajiri na jembe mkononi, mazao baada ya miezi sita, unavuna, bado kuna usumbufu kibao, ikiwemo kukopwa mazao na usilipwe kwa wakati au hata usilipwe kabisa”, alihoji Nombo.

Baada ya kupanga mipango ikapangika, kikao kilivunjwa, huku Carlos akisisitiza kupewa taarifa ya kifo cha Teacher mapema iwezekanavyo.

Ofisi zetu ziko ghorofa ya juu katika jengo la Benjamin Wiliam Mkapa. Baada ya kuegesha gari kwenye maegesho ya Hotel JB Belmont, nilikwea ngazi mbili tatu nikaitafuta lifti iliyonipeleka juu kabisa. Shambulizi la usiku lilinifanya niliweka ulinzi wa kutosha kuzunguka eneo la ofisi zetu.

Kazi yangu ya kwanza niliyofanya usiku baada ya kutuliza akili yangu ni kuwasiliana na Sajenti Julius Nyawaminza, huyu ni Komandoo aliyebobea, akilitumikia jeshi katika vikosi vya Zanzibar. Nilimwagiza kufika haraka Dar es Salaam, kwa vile Unguja ni karibu alifika Jijini asubuhi na kujiweka kwenye pointi niliyompangia awe.

Kwa kuwa vijana wetu wa Dar es Salaam wanafahamika kwa kiasi fulani, nilipanga kuwatumia kwa kazi zingine, hivyo niliwasiliana pia na Luteni, Claud Mwita kutoka vikosi vya Komandoo mkoani Morogoro, ambaye pia aliweza kufika kwa wakati, akafanya kile alichoelekezwa kufanya.

Nilichelewa kwa dakika kadhaa kufika ofisini kwa Kanali Emilly kama ambavyo tulikuwa tumeafikiana, kuchelewa kwangu kulitokana na mipango ya hapa na pale, maana mtu akikuanza utani lazima ujiandae kutaniana naye, lakini pia akikuanza uchokozi muonyeshe kuwa amepita njia mbaya.

Mapokezi nilipokelewa na Linnah David, Katibu Muhtasi wa Kanali Emilly, “Ulikuwa wapi Teacher? Mzee anakusubiri kwa shauku kubwa, amesema ukitia pua tu, usisimame, moja kwa moja ingia ofisini kwake”, Linnah alitania.

“Vipi hali yako Linnah, sikukuacha ofisini, nilisikia wewe pia umepata likizo kulikoni? Au ndiyo umeitwa haraka kama mimi?”, nilimuuliza akatabasamu.

“Nitakwambia ukitoka kwa bosi”, alisema Linnah huku akinihimiza kuingia ndani ya ofisi ya Kanali Emilly.

Mapigo ya moyo wangu yalianza kunienda mbio, sikujua kilichotokea hata nikaitwa haraka kiasi hiki, taratibu niligonga mlango wa ofisi ya bosi, baada ya kusubiri kwa sekunde kadhaa nilitasua kitasa cha mlango na kuingia ndani. Kanali Emilly aliponiona haraka alisimama na kunielekeza sehemu ya kuketi. Nilishangazwa na hatua hii, kunielekeza mahali pa kukaa karibu kabisa na yeye tofauti kabisa na kawaida yake.

Kanali Emilly alikuwa mzee wa makamo, lakini mwenye busara na nguvu nyingi, hakuwa mwepesi wa kushindwa jambo. Baada ya kupeana mikono na mimi kuketi mahali aliponielekeza, aliinua simu yake ya mezani akamwagiza Linnah atuletee vinywaji. Kabla ya kukata simu, Kanali Emilly alimtaka Linnah kuongeza vinywaji kwa ajili ya wageni wanaokuja. Mimi nikabaki kimya.

“Karibu sana Teacher, pole kwa kukatisha likizo yako fupi, nimekuita kwa sababu kuna tatizo limetusibu, tutakuwa na wageni hapa ofisini muda si mrefu, wanakuja kuongea na sisi, tutawasikiliza, tutashauriana nini cha kufanya”, alisema Kanali Emilly, aliinua tena simu yake ya mezani akaongea na watu ambao mimi sikuwajua, akawajulisha kuwa mimi nimefika hivyo waje ofisini kwake.

“Kuna tatizo gani bosi, maana sielewi kinachoendelea?” nilimuuliza Kanali Emilly.

“Kuna tatizo kidogo limetoke. Nikaitwa haraka nyumba kubwa, kutakiwa kurudi kwako haraka ni agizo la Rais. Wakati tunawasubiri hawa ndugu zetu, nitakudokeza kidogo kilichotokea”, alifungua droo ya meza yake, akatoa bahasha kubwa iliyojaa mapesa, pia akatoa kiboksi kilichojaa makaratasi yaliyoandaliwa kama pesa, akanipatia.

“Hizi ni pesa zangu?”, nilimuuliza Kanali Emilly akache

“Ziangalie kwanza Teacher, halafu nitakueleza sababu”.

Zilikuwa pesa nyingi zinazotumika katika mataifa mbalimbali duniani. Zilikuwepo noti za shilingi elfu kumi za kitanzania, nilizipitia noti hizi moja baada ya nyingine, sikuona tofauti. Niliendelea kuziangalia noti hizi kwa umakini mkubwa, zilikuwepo noti za Saandaang Piso zinazotumika Jamhuri ya watu wa Philipines, Diez ya Uruguay, Paundi ya Misri, Birr ya Ethiopia, Yen ya Japan na Won ya Korea Kusini.

Niliendelea kuzipitia pesa hizi kwa umakini sana, Kanali Emilly alikaa kimya akiniangalia, sikufahamu lengo la mzee huyu kunipatia pesa hizi niziangalie tu. Niliendelea na zoezi la kuzikagua noti hizi, Rupiah ya Indonesia, Rupee ya Pakistan, Rand ya South Afrika, Afghan ya Afghanistan, Rouble ya Belerus na Peso ya Cuba.

Kulikuwa na idadi kubwa ya noti, ni vizuri nikutajie aina zote za noti zilizoko mbele yetu ili uweze kunielewa vizuri, kabla mzee hajasema jambo.

Aina nyingine ya pesa sikuwahi kuziona kabisa, kama Rouble ya Russia, Litu ya Luthuania, shilingi ya Kenya, Franc ya Afrika ya Kati, Real ya Brazil, Drams ya Armenia, Lira ya Uturuki, Krone ya Denmark na Riyal ya Saudi Arabia. Zingine ni Paund ya Sudan, Lei ya Romani, Dong ya Vietnam, Dollah ya New Zealand, Peso ya Argentina, Dinar ya Libya, Hryvmy ya Ukraine, Sum ya Uzbekistan, Kwacha ya Zambia, Franc ya Kongo, Franc ya Chad, Dinar ya Algeria, Rouble ya India, Franc ya Cameroun, Mark ya Ujeruman na Dollar ya Marekani.

Baada ya kuzipitia pesa hizi, nikazirejesha mikononi mwa Kanali Emilly, ambaye alizijaza kwenye bahasha kubwa, akaniangalia kwa sekunde mbili tatu, alipoona nimekaa kimya nikimwangalia akatoa bahasha nyingine iliyojazwa makaratasi yaliyokatwa kwa mpangilio mzuri mfano wa pesa. Karatasi hizi zilifungwa kwa mafungu sawa na noti, zikitofautiana kwa ukubwa wa aina ya pesa husika.

Niliendelea kuumiza kichwa changu, nilijiuliza sababu ya Kanali Emilly kuleta pesa hizi mbele yangu, kilichoanza kunizindua ni haya makaratasi yaliyokatwa mfano wa pesa, mawazo yangu hayakunipeleka mbali, nikahisi kuwa huenda karatasi hizi zimekamatwa kwa matapeli waliotapakaa kila kono ya miji ya Afrika Mashariki na duniani, wakiwaibia watu kila siku.

“Naam kamanda wangu, nifahamishe sasa. Kuna habari gani mkuu?”, nilimuuliza baada ya kumaliza kazi ya kuzipitia karatasi alizokuwa amenipatia. “Hizi noti na karatasi nahisi zimekamatwa kwa matapeli”, niliongeza.

“Afadhali tungekuwa tumewakamata, Teacher hili ni tukio linalotia huruma sana, huwezi kuamini nikikueleza kile kilichofanyika, watu wameuza majumba, magari na wengine wamefirisika kabisa kutokana na pesa na karatasi hizi ulizoziona”, Kanali Emilly alieleza.

“Ehee?”, nilihoji huku nikikiweka tayari kumsikiliza. Mara simu ikaita, akainua mkonga wa simu na kuiweka katika sikio lake la kushoto, baada ya muda alisema, “Waruhusu wapite tafadhali”, akaweka simu chini.

“Teacher, kabla sijakueleza hali halisi ya tukio hili, bahati nzuri wahusika wamefika, utawasikiliza kwa makini, wataeleza kilichowasibu, sidhani kama tutashindwa kuwasaidia katika hili”, alisema Kanali Emilly.

“Itategemea na kazi yenyewe bosi, kama ujuavyo hii ni dunia, hata uwe mjuzi wa kuogelea kiasi gani, iko siku maji yatakuzidi ujanja, unaweza kuingia mpaka kimo fulani ukashindwa kuendelea, lolote laweza kutokea”, nilimwambia. Sikuona vizuri kumsimulia kuhusu tukio la usiku, hivyo nilimezea.

Mlango wa ofisi uligongwa, Linnah akaingia akifuatiwa na watu wawili waliotakata vizuri, ukiwaangalia huhitaji kuuliza, moja kwa moja niliamini kuwa watu hawa ni vigogo kutoka serikalini ama matajiri wenye mapesa yao.

Sajenti Julius Nyawaminza aliwasili bandarini, Dar es Salaam kwa Meli ya Kilimanjaro II majira ya saa moja na dakika ishirini asubuhi akitokea Visiwani Zanzibar. Baada ya kuwasili Dar es Salaam, kutoka bandarini, Nyawaminza alitembea kwa miguu yake hadi eneo la Posta mpya kama alivyokuwa ameelekezwa.

Kijana huyu alikuwa na shauku ya kufanya kazi aliyokuja kuifanya Dar es Salaam, alifikiria mambo mengi aliyozungumza na Teacher usiku, akajiona mwenye bahati kipindi hiki kuitwa kufanya kazi katika mazingira aliyokuwa akiyasubiri kwa siku nyingi.

Baada ya kuhitimu kozi mbalimbali za kijeshi ndani na nje ya nchi, Sajenti Julius Nyawaminza alipangiwa kazi katika vikosi vya Zanzibar. Akiwa Visiwani Zanzibar, alifanya mazoezi yake ya kawaida kila siku akisubiri hali mbaya itokee. Yeyote angemuona barabarani kwa bahati mbaya asingeamini kuwa kijana huyu ni moto wa kuotea mbali, kama huamini mtafute umchokoze ili uamini haya niyasemayo..

Begani, Nyawaminza alining’iniza mkoba wake mdogo wenye vifaa vyake kadhaa vya kazi. Alipofika eneo la Posta mpya alinunua gazeti la michezo, akaketi kwenye mojawapo wa vibanda vya abiria wanaosubiri usafiri vilivyoko mbele ya jengo la Benjamini Wiliam Mkapa na Benki ya CRDB.

Luteni Claud Mwita, kutoka mkoani Morogoro, naye pia alikuwa amewasili katika eneo hilo, yeye alitumia usafiri wa bodaboda kutoka Ubungo, alifanya hivyo kutokana na hali ya barabara za Dar es Salaam asubuhi kuwa na msongamano wa magari mengi, hususan wakati wa kuelekea katikati ya Jiji.

Kama alivyofanya Sajenti Julius Nyawaminza, Claud Mwita alitafuta gazeti ya michezo, baada ya kupitia vichwa vya habari vya gazeti hili, akatafuta uelekeo akaweka makazi yake ya muda akisubiri taarifa kutoka kwa Teacher.

Pamoja na kusoma magazeti, vijana hawa walifika hapa kwa kazi maalum, kuangalia aina ya watu wanaofika eneo hilo na muda wa kukaa kusubiri usafiri wa daladala ama taksi zilizoegeshwa katika eneo hilo. Kila mmoja kwa wakati wake alituma ujumbe mfupi wa maneno kumfahamisha Teacher kuwa tayari amefika na yuko kwenye pointi ya kazi.

Nao Simba, Nyati na Chui kama wanavyofahamika, walifika eneo hilo mapema zaidi, hawa waligawana njia za kuingia na kutoka katika jengo hilo, Simba akiulinda mlango mkuu wa mbele unaoangalia kituo cha daladala, Nyati akajiweka upande wa kuingia na kutoka magari, Chui akaimalisha ulinzi kwenye mlango mdogo unaotokea sehemu ya maduka kama unatokea barabara ya Jamhuri.

Teacher aliingia ofisini kwa Kanali Emilly na kuonyeshwa karatasi zilizoandaliwa mfano wa noti, lakini zilikuwa bandia.

“Karibuni”, Kanali Beny Emilly alisimama kuwakaribisha wageni hawa. Kwa sheria za kijeshi ilinilazimu mimi pia kusimama ili kumuunga mkono bosi wangu. Baada ya wageni hawa kushikana mikono na mzee huyu, wakanishika mkono.

“Karibuni, karibuni sana, mnaweza kuketi”, Kanali Emilly alirudia kusema huku akiwaonyesha sehemu za kuketi.

“Shukrani sana”, walisema wageni hawa kwa pamoja huku wakiketi taratibu kwenye viti vilivyokuwa mbele yangu. Kutokana na uzoefu wangu wa kazi nikabaini kuwa wageni hawa walikuwa na tatizo zito linalosumbua nafsi zao.

“Karibuni tena ndugu zangu, karibuni sana hapa ofisini kwangu, huyu kijana ndiye Teacher ambaye niliwafahamisha amesafiri, nikaona ni vizuri tumsubiri awepo ili tuzungumze wote kuona namna ya kusaidia jambo hili”, Kanali Emilly alisema akiwaangalia wageni hawa.

Halafu akanigeukia, “Teacher, hawa ni wageni wetu, nimefarijika kukuona umerejea wakati muafaka kabisa, dunia ya sasa hakuna siri, jana niliitwa Ikulu kwa mheshimiwa Rais, nimeulizwa maswali mengi ambayo nimekosa majibu, nikaamini kuwa ukirudi tutajadiliana na majibu yatapatikana, ndivyo ninavyoamini”, alisema huku nikimwangalia kwa makini.

Aliinua simu yake ya mezani akampigia Katibu Mahsusi wake Linnah, akamwambia atuletee vinywaji juisi, soda, maji na sambusa. Haikupita hata dakika tano, vinywaji vililetwa, tukaanza kunywa huku kila mmoja akiliweka tayari koo lake kwa mazungumzo.

“Mko tayari kwa mazungumzo yaliyowaleta, ni muda muafaka sasa kuzungumza?”, Kanali Emilly aliwauliza watu hawa.

“Naam, tunaweza kuanza mazungumzo yetu”, alisema mmoja wa watu hawa huku akimwangalia mwenzake usoni, mfano wa mtu anayeomba ridhaa ama kibali kwa ajili ya kuanza kutoa maelezo.

“Itapendeza kama mtaeleza kuanzia mwanzo ili tuwe pamoja na Teacher katika mazungumzo haya”, Kanali Emilly aliwaeleza watu hawa, halafu akanigeukia mimi”, “Teacher jana nilikutana na watu hawa, walinisimulia kwa undani kuhusu jambo hili lakini itapendeza zaidi wakirudia mbele yako ili upate picha kamili” aliniambia.

“Kijana au Teacher kama mzee wetu anavyokuita. Naamini utaelewa vizuri nikianza kwa kujitambulisha, sisi ni nani tunatoka wapi na tumefika hapa kwa sababu gani?”.

“Naam”, nilijibu kwa mkato.

“Asante. Mimi binafsi naitwa Enock Nyanda, mkaazi wa Msasani ni mfanyabiashara maarufu hapa Jijini Dar es salaam”, alisema huku akiniangalia, nikamuonyesha ishara aendelee.

“Huyu mwenzangu anaitwa mzee Sadik Tagazi, makazi yake pia ni Msasani, ni mfanyabiashara wa siku nyingi… Kijana wangu, naamini nitaeleweka vizuri kwako nikisema wazi kuwa tamaa ya kupata mali nyingi imeniponza mimi, imemponza hata huyu mzee mwenzangu, tumeingizwa mjini, nimeibiwa kiasi kikubwa cha pesa, huyu mzee mwenzangu pia amefanyiwa hivyo hivyo, tumeumizwa”, alisema huku machozi yakianza kumtoka, jambo ambalo kwa kiasi fulani liliushitua sana moyo wangu.

“Ehee, ilikuwaje mpaka mkaibiwa kiasi kikubwa cha pesa kama ulivyosema”, nilihoji huku akili yangu ikibadilika, maana tukio hili ni moja ya matukio ya kawaida ambayo huwatokea watu kila siku, mawazo yangu yakarejea shambulizi la usiku, nikajiuliza ni wizi huu wa pesa uliosababisha nishambuliwe na kuponea chupuchupu.

“Labda, niseme wazi kuwa watu hawa wametumika teknolojia ya kisasa sana, naamini kwa teknolojia hii hata nani angeibiwa, mimi ni mtu makini sana, lakini huwezi amini nimeibiwa kirahisi mno”, anaeleza mzee Sadik ambaye kwa muda mrefu alikuwa kimya.

“Ni teknolojia ipi hiyo, mbona mnazunguka tu hamsemi wazi?”, niliwauliza.

“Nimewapa nafasi ya kuzungumza, ndiyo maana nikasema uwanja ni wenu, tusipoteze muda, cha msingi elezeni nini kilitokea mpaka mkaibiwa, jambo hili ni kweli linaweza kumpata kila mtu, lakini mengine ni uzembe wa mtu”, alisema Kanali Emilly kwa hasira.

“Si kusudi letu kupoteza muda, tunataka kueleza jambo hili kwa kinagaubaga zaidi ili muone jinsi ya kutusaidia pia kuwanusuru ndugu wengine wanaokusudiwa kuibiwa kama sisi, nashauri mwenzangu aanze maana yeye ana taarifa nzuri na muhimu zaidi”, alisema mzee Enock.

“Leo ni tarehe ngapi”, alihoji mzee Sadik.

“Leo… Jumatatu ya Machi 21, unataka kusema nini?”, Kanali Emilly alieleza na kuhoji.

“Ehee ni jambo zito lakini nitafanyaje, Machi 13, mwaka huu watu wawili nadhifu sana walifika ofisini kwangu… Nitaeleza kwa kifupi, utaniuliza maswali itakapobidi”, alisema mzee Sadik. “Baada ya watu hawa kufika ofisini kwangu, tulianzia mbali sana, niliamini ni watu safi, tena waungwana sana, wakajitambulisha kuwa wanafanya kazi katika ubalozi mmoja nchini Tanzania, baada ya kujitambulisha walitoa karatasi fulani kuwa hizo ni dola za Kimarekani ambazo hazijasafishwa”, alinyamaza kidogo ili kumeza mate.

Linnah aliingia ofisini kwa Kanali Emilly akiwa amebeba faili kubwa, aliliweka sehemu ya mafaili yanayoingia halafu akaniangalia na kufinya jicho lake, nikatabasamu akatoka.

“Ehee, leta habari, baada ya kuonyeshwa karatasi hizo ambazo walidai ni dola wewe kama wewe uliamini kuwa ni dola?”, nilimuuliza. Alionekana kupagawa, kiasi fulani alionekana mwenye aibu kiasi.

“Teacher, ukweli ni kwamba hawa jamaa zetu wameibiwa lakini inashangaza jinsi wanavyoona abu kueleza ukweli kuhusu tukio hili, kwa uzoefu wangu, baada ya kukutana nao na kuzungumza nao jana, nimeamini kuwa hawapendi jambo hili litoke nje, yaani kwenye vyombo vya habari, hilo tumelizingatia, sasa watueleze kwa undani jambo hili lilivyotokea”, Kanali Emilly alieleza.

“Kama ulivyosema, itakuwa fedheha iwapo tukio hili litarushwa kwenye vyombo vya habari, vinginevyo hakuna tunachoficha, ndio maana nikasema tumeibiwa, wezi wametumia teknolojia ya kisasa kabisa, hata hivyo mimi na mwenzangu tunakiri kuwa tamaa ya kupata utajiri zaidi imetuponza. Kama ambavyo nilivyotangulia kusema, watu hawa walijitambulisha kuwa wanatoka ubalozi wa Marekani na walifika kwangu wakidai kuwa wanatafuta mtu mwaminifu ili wamkabidhi hizo dola azisimamie wakati wa kusafishwa, na kwamba mtu waliyemuona ni mimi”, alisema mzee Sadik.

“Uliwauliza, walikufahamu vipi?”, nilimuuliza.

“Naam, niliwauliza wamenifahamu vipi, pia niliwauliza wanajuaje kuwa mimi ni mwaminifu katika masuala ya pesa, mmoja wao alisema amepata kusikia sifa zangu na ndiye aliyependekeza waje kwangu, mara moka nikayaamini maneno yake”, alisema mzee Sadik.

Nikajiweka vizuri kwenye kiti ili niweze kusikia habari hii, maana kwa kiasi fulani ilianza kuusisimua mwili wangu, “Baada ya hapo nini kiliendelea?”.

“Baada ya kuongea mambo kadhaa na watu hawa, nikiuliza maswali nao wakijibu, hatmaye walinidokeza kuwa baada ya tukio la wizi wa dola milioni mbili za Kimarekeni, lililotokea Uwanja wa ndege wa Julius Nyerere, usafirishaji wa dola, paundi na pesa zingine zinazoingizwa nchini Tanzania ulibadilishwa, sasa zinaingia kama karatasi halafu zinasafishwa kwa dawa maalumu ili zianze kutumika kama dola”, alinyamaza kidogo ili kupisha swali, alipoona nimekaa kimya akaendelea.

“Nilihoji pia, ili kujuwa kama ni tukio hilo la wizi tu lililopelekea pesa zote zinazoingizwa nchini Tanzania kuchafuliwa, pia nilitaka kujuwa hali hiyo ni kwa Tanzania peke yake, watu hao ambao walikuwa wakiongea taratibu kwa kujiamini sana, walisema uhalifu umeongezeka sana duniani hivyo mamlaka za fedha zimeona hiyo ndiyo njia salama zaidi ya kusafirisha pesa”, alieleza.

Aisee ni stori tamu sana, endelea nakusikiliza”, nilisema huku Kanali Emilly akitabasamu.

“Baada ya majadiliano ya muda mrefu, maofisa hawa waliodai kuwa wanatoka Ubalozi, walitoa mfano wa karatasi kadhaa zikiwa na rangi nyeusi, wakadai kuwa hizo ni dola orijino ambazo huletwa nchini na baadaye kusafishwa kwa dawa maalumu ambayo walisema pamoja na kupatikana kwake kuwa vigumu, wao wanajua mahali pa kuipata na kazi hiyo ikafanyika vizuri. Una swali?”, aliuliza huku akiniangalia usoni, macho yetu yalipokutana, alionekana wazi kuwa mwenye aibu.

“Teacher, karatasi anazoeleza mzee Sadik nimekuonyesha kabla hatujaanza mazungumzo”, alisema Kanali Emilly nikatikisa kichwa kukubaliana naye.

“Sasa ilikuwaje ukaamini kuwa hizi karatasi ni dola?”, nilimuuliza baada ya kusimama, nikazichukua zile karatasi alizonionyesha Kanali Emilly, nikamuonyesha, maana maelezo haya yaliniingia vizuri, nikasahau kama nilikuwa likizo.

“Lo, sijui shetani gani aliniingia, mwanzo sikuwaanini kabisa, nilipanga kupiga simu kuwajulisha polisi kuhusu watu hawa ili wakamatwe, lakini baadaye nilishawishika kuwaomba vitambulisho vyao, hakika vilikuwa vitambulisho vya ubalozi wa Marekani, nikaanza kuyaamini maneno yao, nikaingia kwenye mtego baada ya mmoja wa maofisa hawa kutoa dawa na kusafisha karatasi kadhaa ambazo ziligeuka kuwa dola halali kwa matumizi. Hakika nilianza kusadiki, baada ya kudai kuwa dawa waliyonayo ni kidogo haiwezi kusafisha zaidi ya karatasi ishirini”, alinyamaza kidogo akachukua glasi yake ya juisi akanywa kiasi huku midomo yake ikimcheza mfano wa mtu aliyekutana na baridi kali.

“Teacher, nakuhakikishia kuwa, kazi ya kusafisha karatasi hizo na kuwa dola ilifanyika mbele ya macho yangu, nilifuatilia tukio hilo kwa umakini wa hali ya juu. Karatasi kumi ziliingizwa kwenye dawa nikiona, baada ya sekunde kadhaa zikatolewa zikiwa tayari zimebadilika na kuwa dola mia mia za Kimarekani, wakati huo boksi kadhaa zilikuwa kando zikiwa zimesheheni karatasi hizo, hakika nikauona utajiri mkubwa mbele yangu, nikajua sasa nimeukata”, alisema mzee Sadik, alinyamaza kupisha kama kuna mtu mwenye swali, alipoona kimya akaeleza.

Baada ya karatasi hizo kusafishwa na kila moja ilikuwa dola mia za Kimarekani kuonekana, walinikabidhi, halafu wakaanza kusafisha karatasi ambazo walidai ni paundi za Uingereza ambazo pia zilipotakata zilikuwa paundi mia kila moja. Wakadai dawa hiyo imeisha nguvu, wanatafuta watu wa kusaidia ili karatasi hizo zisafishwe na kuwa dola. Wakanipatia dola zilizosafishwa ili niende sehemu ya kubadilishia pesa kuthibitishe kama ni dola halali, nikafanya hivyo, hakika zilikuwa dola halali kabisa, nikajiona mwenye bahati kuonana na watu hawa”.

“Aisee, kweli hapo hakuna ujanja, lazima utaibiwa tu”, nilimwambia akacheka kidogo huku akisisitiza kuwa huo ni wizi ambao si rahisi mtu kukwepa, labda uwe fukara. Na jamaa hawa hawamfuati mtu asiye na kitu.

“Tamaa ya kupata pesa nyingi imeniponza”, alisema akitoa kitambaa cha jasho mfukoni akafuta machozi yaliyokuwa yakimtoka.

“Karatasi walizokuja nazo ofisini kwako na kudai kuwa ni dola ambazo hazijasafishwa, waliziacha kwako?”. niliuliza.

“Yes, waliziacha karatasi hizo kwangu huku wakisisitiza kuwa nisitoe taarifa hii kwa mtu yeyote, wakadai kuwa wangerudi kesho yake mapema kuangalia kama nimebadili dola, ili tuangalie uwezekano wa kupata pesa za kununua dawa kwa ajili ya kusafisha karatasi zilizobaki, ambazo walidai iwapo zitasafishwa zote ni zaidi ya shilingi bilioni tano za Tanzania, nilifurahi sana”, alisema mzee huyu.

“Kama ndivyo, mbona wewe umefaidika”, nilimwambia.

“Hapana, nimeumia sana Teacher, waliporudi mara ya pili walinieleza kuwa karatasi hizo zina thamani kubwa sana, ni mapesa ya kigeni yanayosubiri kusafishwa, kwa hiyo waliniomba mimi kama mwenyeji wao niwatafutie mtu mwenye pesa ili tununue dawa na kusafisha karatasi hizo, ambazo wao walidai kuwa waliziiba ubalozini”, anabainisha.

“Ndipo wewe ulipotoa pesa?”, nilimuuliza.

“Hapana, kwa vile walinieleza kuwa dawa ya kusafisha karatasi hizi inauzwa kwa bei mbaya, nilimfuata mzee mwenzangu, Enock Nyanda, baada ya kumshawishi alikubali tushirikiane kutoa pesa ili dawa ipatikane, ndipo kazi ya kutafuta dawa ilipoanza”.

“Hapo ndiyo patamu sasa, ehee?”, niliteka masikio.

Baada ya utaratibu wa pesa kupatikana, maofiosa hawa kutoka ubalozi walituambia kuwa, sehemu ambayo tunaweza kupata dawa ni kwenye maabara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Walishauri kuwasiliana na Profesa waliyedai kuwa anahusika na maabara ya chuo, baada ya kuwasiliana naye kwa simu yake ya mkononi, alitupangia muda ya kwenda kumuona”, alitulia kidogo, akaonesha hasira iliyokuwa katika nafsi yake, halafu akacheka.

“”Watu hawa walijipanga vizuri”, nilijisemea.

“Hakika, kwa mchezo huu walijipanga vizuri kuhakikisha wanafanikiwa”, alirukia Kanali Emilly.

“Inaonyesha hivyo. Maana siku iliyofuata tulifika eneo la chuo kikuu, tukakutana na Profesa mmoja anaitwa Davis Magajimbo, kwa vile alikuwa ametuelekeza sehemu ya kumuona, Baada ya kumfahamisha kuwa tunahitaji dawa ya kusafisha dola, alitueleza kuwa dawa hiyo inauzwa bei mbaya na ili kuipata lazima zipatikane shilingi milioni mia moja za kitanzania”, alisema, baada ya kutafakari kidogo akaendelea.

Kutokana na thamani ya dola na wingi wa karatasi zilizokuwa zimeandaliwa kwa ajili ya kusafishwa, tulikubali kutoa kiasi hicho cha pesa kwa Profesa, ambaye alitukabidhi dawa huku akidai kuwa dawa hii ni nyingi sana, akashauri kama ikibaki tutaitumia wakati mwingine. Haraka tuliwasiliana na maofisa wa ubalozi kuwajulisha kuwa dawa imepatikana, nao hawakuchelewa kufika”.

“Walipofika ikawaje?”, niliuliza.

“Kufika kwa maofisa hawa kulitupa faraja, walishauri dawa hiyo ihifadhiwe vizuri kwenye jokofu, ili kazi ya kusafisha dola kwa vile ni nzito ifanyike kesho yake mapema alfajiri, kwa madai kuwa kuna kazi nyingine wanaifanya wakati huo ili kesho yake wasiwe na ratiba nyingine”, alisema mzee Enock ambaye alikuwa kimya kwa muda mrefu.

“Ah, jambo hili lilipangwa kwa ustadi wa hali ya juu, tulihifadhi dawa hii vizuri kama watu hawa walivyoagiza, siku ya pili walifika mapema alfajiri kama walivyoahidi, walinihimiza nitoe dawa ili kazi ya kusafisha dola ianze”, alipofika hapo machozi yakaanza kumwagika.

“Usilie tafadhali, hii ni hali halisi ya dunia, unaweza kulala masikini ukaamka tajiri, ama ukalala tajiri ukaamka masikini, yote ni mipango ya Mungu”, niliwaambia ili kuwatia moyo

“Teacher, sasa tunawasaidiaje wazee hawa?”, lilikuwa swali kutoka kwa Kanali Emilly. Kutokana na swali hili, nilitembea hatua tatu kutoka nilipokuwa nimesimama, halafu nikarejea tena kwenye kiti nilichokuwa nimeketi awali.

“Inategemea…”, nilijibu kwa mkato,

Baada ya kutafakari kwa muda, huku tukiangaliana kama mabubu, nililazimika kumweleza Kanali Emilly kuhusu mkakati wangu wa kazi zilizokuwa mbele yangu.

“Afande…, kabla sikaingia kazini rasmi, naomba utambue kuwa kujiingiza katika jambo hili, ni sawa na kuanzisha vita, nasema hivi kwa sababu watu waliofanya uhalifu huu wana mtandao mkubwa mno. Hawa ndio wahusika wakubwa wa dawa za kulevya, ndio wahusika wa uhalifu wa kila aina. Swali langu ni kwamba, uko tayari kwa mapambano na watu hawa?”, nilimuuliza.

“Potelea mbali, lolote liwe, dunia itatukumbuka kwa hili, tukilimaliza salama tutashukru, tukiishia njiani naamini wapo watakaokuja kuliendeleza”, Kanali Emilly alisema huku akisimama kuonyesha msisitizo. “Niko tayari kabisa”.

Nililazimika kumweleza Kanali Emilly, kuhusu shambulizi la jana usiku uwanja wa ndege wa Julius Nyerere, akaonekana kushangazwa, nami nikatumia nafasi hiyo kumweleza jinsi nilivyojipanga kukabiliana na watu hawa, maana walikuwa wamenianza.

“Afande, kutokana na umuhimu wa jambo hili, nimelazimika kuwaita vijana wetu wawili, Luteni Claud Mwita kutoka Morogoro na Sajenti Julius Nyawaminza kutoka Zanzibar, hawa ni makomandoo wenye uwezo mzuri, bahati nzuri wako karibu na eneo hili. Hapa ofisini nimeamua kuwatumia Luteni Fred Libaba na Sajenti Peter Twite tu, nina sababu za kufanya hivyo”, nilidokeza.

“Sababu gani hiyo Teacher, wakati idara yetu hapa inao vijana wenye uwezo mzuri tu, wangeweza kukusaidia kwa karibu zaidi, jambo hili linahitaji ushirikiano wenu”, alishauri.

“Afande, nimelazimika kufanya hivi kwa sababu, sielewi ilibainika vipi kuwa nimesafiri, ilifahamika vipi kuwa niko kwenye ndege nikirejea Dar es salaam, na sijui nini kilisababisha hata watu hawa wakanishambulia baada ya kutoka kwenye ndege, hilo linanitia shaka”, nilimwambia. “Hawa vijana tutawashirikisha kwa kazi nyingine, kuhusu hii watuache kwanza. Kama utapenda operesheni hii iwe na mafanikio utaniwia radhi kwa hilo”.

“Umesomeka, hakuna ubishi katika hilo. Kuna la ziada?”.

“Hapana”, nilimwambia, baada ya ukimya wa sekunde kadhaa nilimwambia kuhusu ujio wa shemeji yangu Mama Feka. “Afande, kama ulivyosikia nikiongea na simu, shemeji yangu tunayeshibana sana yuko njiani kuja Dar es Salaam, pamoja na kwamba anakuja kwenye mahafari ya chuo kikuu, kwa vyovyote vile atapenda kufikia kwangu, kama unavyojua familia yangu nimeihamisha kabisa ili sasa vita vianze, itakuwa vita ya kufa au kupona”, nilisema kwa hasira.

“Sasa kuhusu huyu shemeji yako utafanyaje, maana nyumbani kwako sasa si sehemu salama kama ulivyosema?”, alihoji Kanali Emilly.

“Nafikiria kumshirikisha katika vita hivi, maana ujio wake unaweza kuwa faida au hasara, lolote laweza kutokea”, nilimwambia Kanali Emilly akaonekana kunishangaa.

“Kwanini umeamua kufanya hivyo Teacher?. Huyu shemeji yako ataweza kumudu hali ngumu ya vita ambavyo hatujui nani adui na rafiki?”.

Nilitumia dakika mbili tatu kumweleza Kanali Emilly, kuhusu uhodari wa Mama Feka. Nilimweleza jinsi mama huyu alivyo na msimamo imara katika kutekeleza majukumu yake, nilieleza historia yake fupi, kuwa kabla ya kujiunga na chuo kikuu huria cha Tanzania, alifanya kazi kama mwalimu wa michezo katika shule kadhaa, lakini kabla ya hapo alikuwa ameshiriki mafunzo mbalimbali ya kijeshi kwa mjibu wa sheria.

“Kuhusu hilo nakuachia utaamua mwenyewe. sasa umepanga kumtumiaje huyo shemeji yako, au ni siri yako?”.

“Hapana, ndiyo maana nikakushirikisha kuhusu jambo hili. Afande, Mama Feka ni mwanamke mrembo sana, ni mwanamke ambaye anaweza kumshawishi mwanaume yeyote akaingia katika himaya yake. Labda nikudokeze jambo moja”.

“Itakuwa vizuri”.

“Hapa Dar es Salaam, kuna mtandao wa uhalifu ukiongozwa na mzungu mmoja aitwae Carlos Dimera, kama unavyojua taratibu na sheria za nchi yetu huwezi kumkamata mtu bila kuwa na ushahidi wa kutosha. Taarifa nilizonazo ni kwamba huyu Carlos anapenda sana wanawake warembo, kwa Mama Feka ataingia, akiingia amekwisha”, nilifafanua.

“Ni mpango mzuri Teacher, tufanye kila iwezekanavyo watu hawa wakamatwe na ushahidi, hii itasaidia kuwafikisha mahakamani, nikutakie kazi njema, tuwasiliane kila hatua utakayofikia, ukihitaji msaada wa aina yoyote usisite kunijulisha, kuanzia sasa ofisi hii itaacha mambo mengine yote ili tushughulikie jambo hili”, Kanali Emilly alisema.

“Nikutakie kazi njema, tuombe mungu ndiye mwenye dhamana ya uhai wetu, lolote likitokea itakuwa kwa mapenzi yake, lakini pia tuko tayari kufa kutetea wengi”, nilisema huku tukisimama. Tukashikana mikono.

Muda ulikuwa umeyoyoma sana, nilitoka ofisini kwa Kanali Emilly, huku mawazo mengi yakiwa yamenizonga juu ya jambo hili, nilijiuliza kuhusu mbinu walizotumia watu hawa, kiasi fulani nilijikuta nikicheka mwenyewe na kuwasifu kwa jinsi walivyoweza kufanikisha mpango wao wa wizi na kuwaacha wazee hao kwenye mataa. Nilifungua mlango nikatokea mapokezi. Linnah aliponiona akasimama.

“Pole sana bosi wangu, naona kikao kilikuwa kirefu kupita maelezo”, alisema, mama huyu askari mwenye cheo cha Staff Sajenti, lakini aliheshimiwa sana kutokana na utendaji kazi wake uliotukuka.

“Ndiyo mambo ya kazi. Sikiliza Linnah, naomba nisaidie kazi moja muhimu sana, niitie Sajenti Peter Twite aje ofisini kwangu haraka, ikiwezekana aingie kwa siri. mtu zaidi yako asijue”, niliagiza halafu nikaingia ofisini kwangu.

Nilipanga kumtumia Peter kufanya kazi maalumu, kazi ya kimafia, ambayo ingetusaidia kumaliza jambo hili haraka. Baada ya muda mfupi Peter aliingia ofisini kwangu.

“Jambo Afande?” alinisalimia.

“Jambo. Habari ya toka usiku wa jana, Peter ujumbe wako ulinisaidia sana, maana sikujua lolote litatokea, sijui ingekuwaje?”, nilimuuliza.

Peter akatumia muda huo kueleza mambo yalivyokuwa uwanja wa ndege, akaeleza jinsi alifika uwanja wa Julius Nyerere kwa ajili ya kunipokea, uwanja wa ndege alikutana na watu ambao aliwatilia shaka, kutokana na uzoefu wake wa kazi baada ya kuwawafanyia utafiti alibaini kuwa walikuwa katika mpango wa kumsubiri mtu.

“Ilikuwa vigumu saba kuwabaini, baada ya kutulia na kusoma mazingira ya uwanja wa ndege, nilibaini magari mawili aina ya BMW, moja likiwa limeegeshwa karibu kabisa na sehemu ya kutokea abiria na lingine liliegeshwa sehemu ya kutokea magari. Ulipoanza kutoka wewe watu wawili walilikimbilia gari la mbele, ambalo lilianza kuondoka, lingine likasuri gari ulilopanda liondoke ndipo wao walifuate gari hilo kwa nyuma. Haraka nikakutumia ujumbe wa tahadhari”.

“Ama kweli ulifanya kazi ya ziada, sikuwa na mashaka kabisa, bila wewe pengine siku ya leo ingekuwa ya maombolezo kwangu, asante Peter”, nilimshika mkono.

“Usijali mkuu, haya ni matunda yako, kumbuka wewe ndiye uliyenifundisha haya, ulinifundisha jinsi ya kunusa harufu mfano wa mbwa, Nikushukuru kwa kunifikisha hapa”, alisema Pete.

“Tuachene na hilo, sasa nataka ufanye kazi moja ya muhimu sana, nimemwambia Mzee Emilly kuwa mapambano yameanza, ni mapambano makali ambayo yafaa tuyapigane sasa, hakuna jinsi, kazi yako tafuta vijana watano, wawe raia wa kawaida tu, lakini waendesha bodaboda jijini, ingia nao mkataba, lakini wapatie pamit na alama ili wasisumbuliwe na migambo. Pikipiki zao waziegeshe kwenye barabara kubwa tano za jiji. Yaani Morogoro road, Ali Hassan Mwinyi, Nyerere road, Kilwa road na Bibi Titi Mohamed, ukimaliza hilo tuwasiliane nitakuelekeza kazi nyingine”, niliagiza.

“Nitalifanya hilo haraka sana bosi”, alisema Peter.

“Ok, usikose kunijulisha, kumbuka kuwafahamisha kuhusu matumizi ya pikipiki hizo, maana tumepanga kuwatumia wao katika kazi fulani, isifike wakati wakatushangaa, kazi kwako”.

Niliwasiliana na Luteni Claud Mwita kumuuliza kama uwepo wake eneo hilo umebaini nini akanidokeza kuwa watu ni wengi, pamoja na kufanikiwa kufahamiana na Sajenti Julius Nyawaminza, wameimalisha ulinzi katika eneo hilo.

Simba, Nyati na Chui, wao walikuwa eneo hilo wakitembea hatua kadhaa kwenda upande mwingine na kurejea kwenye pointi huku silaha zao ndogo, zikiwa tayari zimeondolewa usalama. Risasi zikiwa chemba tayari kwa lolote.

Baada ya kupanga mipango yangu, niliyoofanya kimya kimya, nilifungua mkoba wangu mdogo, nikatoa kamba niliyoinunua Kariakoo. Ilikaribia kuwa saa moja ya usiku, giza lilianza kuifukuza nuru, niliwasiliana na wenzangu. Claud Mwita, Julius Nyawaminza na Fred Libaba nikawaomba tuonane kwenye Mghahawa wa YWCA uliopo hapo Posta Mpya kwa ajili ya chakula cha jioni.

Pamoja na kwamba Mghahawa huu uko karibu kabisa na kituo cha Daladala cha Posta Mpya, wengi hawakupajua, lakini pia niliwahadharisha wenzangu kuwa makini. Nilishauri kila mmoja achukua chakula na atumie meza tofauti, baada ya hapo tutakuwa na mazungumzo yetu binafsi nje ya eneo hilo.

Taratibu nilifungua mlango wa ofisi yangu nikachungulia kwa nje, nilitafuta sehemu ya siri nikazificha funguo za gari, halafu nikawasiliana na David, mmoja wa vijana wanaofanya kazi karibu yangu, nikamfahamisha mahali nilikohifadhi funguo hizo ili azichukue na kuipeleka gari kwa aliyeniazima, rafiki yangu Edgar.

Hapakuwa na dalili yoyote ya kuwa na mtu, hata Linnah alikuwa ametoka na kufunga ofisi yake, nilitoka haraka na kuivamia lifti iliyonishusha ghorofa ya kwanza. Nilitembea haraka hadi kwenye maegesho ya magari, sikutaka kupoteza muda, nilichungulia upande wa pili lilipo jengo la ofisi za benki ya CRDB. Baada ya kujiridhisha kuwa hakukuwa na mlinzi eneo hilo wakati huo, nikairejesha kamba yangu kwenye mkoba, baada ya kujiridhisha kuwa hakuna kikwazo cha kunisumbua.

Niliangalia nyuma na upande wangu wa kulia na kushoto, sikumuona mtu, lakini kwa vile jengo hili linalindwa kwa kamera maalumu za usalama, nililazimika kufanya jambo moja ili kamera hizo zisinione. Nilisogea kwenye kivuli, nyuma ya magari kadhaa yaliyoegeshwa hapa, nikatumia nafasi hiyo kujirusha chini, upande wa jengo la CRDB. Haikuwa shida kwangu kuruka sehemu kama hiyo.

Lango la kutokea bado lilikuwa wazi na kwa vile kuna ofisi zingine juu ya ghorofa hili, nilitoka na kuwapita walinzi na baadhi ya askari polisi waliokuwa kwenye kibanda chao cha ulinzi. Nielekea shell ya Gapco, nikakavuka barabara na kuingia YWCA, Wenzangu wote walikuwa wamefika na tayari walikuwa wamepata chakula.

Tulisalimiana na kupeana ishara, kwa vile Mghahawa huu ni wa kujihudumia mwenyewe, na njaa ilikuwa karibu iniue nilielekea kwenye dirisha la huduma, nikaagiza chakula, ambacho nilikula haraka haraka, ili kwenda sawa na wenzangu, ambao kila mmoja alikuwa na hamsini zake.

Wakati huo Carlos Dimera alikuwa akiwasiliana na wakala wa kusafirisha mizigo kutoka Bogota, nchini Corombia, wakala akimjulisha kuwa baada ya masaa ishirini na nne mzigo huo ambao ni dawa za kulevya, utakuwa umewasili kwenye uwanja wa ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam.

“Tunahitaji maelezo kutoka kwenu, hivi tunavyoongea hapa shehena ya dawa za kulevya imetua salama katika uwanja wa ndege Addis Ababa, nchini Ethiopia. Tumelazimika kupitishia mzigo nchini Ethiopia badala ya Ouagadougou, nchini Burkina Faso kama ilivyokuwa awali kwa sababu za usalama, taratibu zote za mzigo kuondoka Ethiopia kesho zimekamilika, kazi kwenu, vipi hali ya usalama huko?”, Carlos Dimera aliulizwa.

“Dar es Salaam, Tanzania hali si mbaya sana, japokuwa kuna mawingu na mvua za hapa na pale, lakini haziwezi kutuzuia kuendelea na majukumu yetu. Kuna wingu moja limetanda angani kuashiria mvua, lakini wataalamu wa hali ya hewa hapa Tanzania wanasema wingu hilo halina madhara, waganga wako kazini kuhakikisha wingu hilo halidondoshi hata tone moja la maji, kuhusu hali ya uwanja wa ndege wa Dar es Salaam ni nzuri sana, tunausubiri”, alieleza Carlos Dimera kwa simu ya mkononi.

“Oke, lakini kuweni makini sana katika jambo hili, nasikia serikali ya Tanzania sasa hailali?.”

“Kuhusu hilo ondoa shaka kaka, niko na mtandao unaoeleweka, mtandao wa vijana wa mjini ambao nimewafundisha mbinu za kila aina, hata hili wingu lililotanda angani mwisho wake wa kutanda na kuleta hofu ni leo, wingu hili halitakuwepo tena”, alisisitiza Carlos.

Baada ya Carlos Dimera kumaliza kuongea na simu hiyo, aliingiwa na hofu kidogo, alisimama akatembea hatua mbili, halafu akajiuliza maswali kadhaa, akainua simu yake ya mkononi na kuongea na Nombo.

“Uko wapi Mr. Nombo?”, alihoji Carlos Dimera.

“Niko katikati ya mji bosi, nimelazimika kuja huku kuongeza nguvu kwa vijana, kazi hii lazima iishe leo bosi, kuna habari mpya?”, Nombo alihoji.

“Hakuna habari mpya, isipokuwa wakala wa kusafirisha mizigo anauliza, hatua gani tumefikia, mzigo umewasili salama Addis Ababa, Ethiopia, yamebaki masaa ishirini na nne tu mzigo uwasili Dar es Salaam, na wingu bado limetanda angani, unadhani kuna uwezekano wa kuliondoa?”, Carlos Dimera aliuliza.

“Tulia bosi, tumuombe Mungu atasaidia, maana uwezekano ni mkubwa mno, kwa vile hujafika kwenye uwanja wa mapambano, ungeshuhudia adui alivyowekwa kati, hakika jengo lote la Benjamin Mkapa liko chini ya usalama wetu, kila anayetoka na kuingia anaonekana, kuhusu hilo usijali, leo ndiyo mwisho wa wingu hili, labda utokee muujiza gani”.

“Niwatakie kazi njema, jitahidini bwana jambo hili liishe mapema leo, vinginevyo nitume kikosi kazi?, hawa jamaa zetu wapo tu wanasubiri kazi kama hizi, mkishindwa semeni”, aliuliza Carlos.

“Hakuna sababu, mapambano ya mchana yangeleta shida kidogo, maana watu walikuwa wengi eneo hili, lakini sasa hali iko shwari, hili giza litatusaidia pia. Kunywa, kula ukiamini kuwa kazi hii imekwisha”, Nombo alieleza, Carlos akapata faraja na matumaini.

Baada ya sisi wote kupata chakula cha jioni kwenye Mghahawa huu wa YWCA, tulitoka mmoja baada ya mwingine kama tulivyoingia, lakini tukiwa nimewapa ishara ya kukutana sehemu nyingine ambayo tutafanya mazungumzo na kupanga mipango yetu kwa siri.

Kabla ya kutoka ndani, niliwasiliana na Mama Feka, ili kujua wapi amefika, akanifahamisha kuwa amefika salama Jijini Dar es Salaam. Nilimfahamisha kuwa nitamtafuta kesho, hivyo atafute hoteli itakayomfaa apumzike kwani alikuwa amesafiri kwa muda mrefu.

Wakati tunatoka ndani ya Mghahawa huu wa YWCA, nilisikia kelele za risasi, zilizosikika kutoka upande wa pili, zikafuatiwa na harufu ya baruti. Kwa sisi wazoefu wa mambo ya silaha, mara moja nikahisi jambo. Watu walikimbia kuelekea upande tuliokuwa, ghafla kwa muda mfupi hali ya usalama ilikuwa imetoweka katika eneo la Posta Mpya.

Tuliangaliana na wenzangu, moyo wangu ukaingiwa na hofu, nikahisi jambo la hatari limemtokea David. Tulianza kusogea taratibu eneo la tukio. Nilifungua mkoba wangu nikatoa moja ya kofia zangu za kuficha sura, nikaivaa ili kuficha sehemu ya uso wangu.

“Tukimbie, majambazi yamevamia na kuua watu, mwenyezi mola tusaidie”, mama mmoja wa makamo alisikika huku akikimbia kuyanusuru maisha yake.

“Sijawahi kuona unyama kama huu, binadamu kumuua binadamu mwenzao tena mbele ya watu utadhani wanaua mnyama”, alieleza mzee mmoja aliyekuwa amelala kwenye mfereji wa barabara ya Azikiwe.

Toyota Carina TI, ambayo David alikuwa akiendesha kutoka kwenye maegesho ya magari ghorofa ya kwanza, ishambuliwa na kuteketezwa vibaya kwa kombora ambalo halikujulikana, David aliuawa katika shambulizi hilo. Waliofanya shambulizi hilo hawakufanya makosa. Nilisikitishwa sana, lakini kwa kiasi fulani nilijiona mwenye bahati, maana kazi yangu sasa ingekuwa rahisi au ngumu zaidi.

Polisi hawakuchelewa kufika eneo la tukio, waandishi wa habari pia waliwasili na kamera zao, mimi na wenzangu Claud Mwita, Julius NYawamizna na Fred Libaba tuliangalia tukio hilo kwa dakika kadhaa tukiwa mbali kiasi, halafu tukapeana ishara ya kuondoka eneo hilo. Hata kama ungekuwa mtaalamu wa hisia kiasi gani hakika usingeweza kubaini ishara zetu, labda uwe mmoja kati yetu.

Kutokana na uzito wa tukio hilo, niliwasiliana na Peter Twite, nikamfahamisha klichotokea, nikamwelekeza mambo ya matatu ya kufanya, afike haraka eneo la tukio na kutoa taarifa kwa Kanali Emilly, ahakikishe majina ya marehemu hayaripotiwi kwenye vyombo vya habari, ofisi anayotoka marehemu iwe siri na mwili wake uhifadhiwe mahali salama mpaka tutakapomaliza kazi.

Baada ya kutoa agizo hilo kwa Twite, tulikubaliana kuonana kwenye Mghahawa wa Chief Pride, uliopo mtaa mdogo wa Chaga, katikati kabisa na barabara za Jamhuri, upande wa kushoto na Libya, upande wa kulia. Tulipanda ngazi hadi ghorofa ya kwanza, hapakuwa na wateja zaidi ya meza na viti. Wakati tunapanda ngazi, muhudumu alitufuata kwa nyuma, tulipoketi akawa tayari kutusikiliza. Tuliagiza vinywaji kila mmoja alichoona kinamfaa.

“Nadhani hapa patatufaa kwa mazungumzo, au mnasemaje bosi?”, Fred alihoji baada ya muhudumu wa Mghahawa huu kuondoka.

“Pamoja na kwamba sijaelewa lolote kuhusu kilicho mbele yetu, lakini kwa utulivu huu, nashauri tuifanye sehemu hii iwe kwa ajili ya kukutana tukiwa na dharura. Naamini kazi tuliyoitwa kuifanya itakuwa ngumu, lakini tutashinda”, alieleza Claud.

“Sikilizeni, naamini mpaka sasa adui zetu wanasherehekea ushindi wakidhani nimekufa, David ameuawa kinyama, wamemuua wakidhani ni mimi, sasa kabla jua la kesho halizachomoza, yatupasa kufanya kazi ya ziada, kujua wauaji wanapatikana wapi, wanafanya nini? Sababu zilizowasukuma kutushambulia, tukilijua hilo, kazi yetu itakuwa rahisi, tofauti na hapo tutakuwa tunajisumbua kutwanga maji ndani ya kinu”, niliwaeleza.

Vinywaji vililetwa mezani, tukaanza kunywa huku kila mmoja akieleza mpango kazi wake. Baada ya kila mmoja kutoa mchango wake huku Fred akijaribu kuweka kumbukumbu ya maandishi, nikakumbuka kuhusu, Carlos Dimera.

“Wakati mwingine linapotokea tukio la kushitua kwa aina hii, akili yangu hulazimika kufanya kazi ya ziada. Fred…, unaweza kumfahamu mzungu mmoja anaitwa, Carlos Dimera?”.

“Yaa. Ndiyo, Carlos Dimera namjua, huyu jamaa ndiye tajiri mwenye kile kiwanda cha kutengeneza tembe za malaria, Huyu jamaa anatajwa kuwa mtu safi na mwaminifu kwa serikali, pia anatajwa kuwa mstari wa mbele katika kusaidia jamii, ana nini?”, Fred alihoji.

“Yatupasa kumchunguza haraka iwezekanavyo. Nimewahi kusikia minong’ono kuhusu yeye, lakini nisimchumie dhambi, nataka kujua anaishi wapi, anapendelea mambo gani?”, nilimuuliza Fred.

“Huyu Carlos, anaishi Mikocheni A, ukiziacha taa za usalama barabarani za Morocco, barabara ya kwanza kabisa ingia kulia, nimewahi kuonyeshwa na rafiki yangu mmoja Inspekta wa polisi. Anasema walikwenda kupokea msaada wa Pikipiki kumi za kuwasaidia polisi kufanya doria, ndipo nilipobaini kuwa ni mtu safi. Ni matajiri wachache sana wenye moyo wa kusaidia suala la usalama wa raia”, alifafanua Fred.

“Siyo sababu, yafaa achunguzwe, na kazi hii lazima tuifanye usiku huu, huyu jamaa kwa nyakati fulani, binafsi nilijaribu kufuatilia nyendo zake, sikupata mambo makubwa sana, lakini nilipata mashaka kidogo, sasa nitamfuatilia kwa undani zaidi ili nijiridhishe”, nilisema.

“Inspekta Judith, aliyenionyesha nyumbani kwake alinidokeza kuwa wakati anawakabidhi Pikipiki hizo, Carlos mwenyewe aliwaeleza polisi kuwa binafsi anachukia sana vitendo vya uhalifu, akaahidi kutoa magari mawili maalumu kusaidia doria, ndiyo maana najiuliza”, Fred alieleza.

“Siyo sababu, wahalifu wana mbinu nyingi, hujaona wachawi walivyo wakarimu, anakufanyia vitendo vya ushirikiana huku akikuonyesha wema. Hata ukielezwa kuwa huyu ndiye mchawi wako huwezi kuamini, kutoa msaada haitoshi kukufanya uwe mwaminifu”, Nyawaminza alieleza.

“Hakika”, Claud alisapoti.

“Ndugu zangu, Claud na Julius, kwanza poleni kwa safari, niwaombe radhi kwa safari ya kushitukiza, nimelazimika kuwaita ili tusaidiane kupigana vita iliyoko mbele yetu”, nilitumia nafasi hiyo kuwaeleza kila jambo, kuanzia wazee walioibiwa kwa mtindo wa noti bandia na jinsi dawa za kulevya zinavyoingizwa nchini na kuchangia kuharibu maisha ya ambani ni nguvu kazi ya taifa na kizazi cha sasa.

“Tuko pamoja”.

“Kuanzia sasa, mtaziacha kazi zenu zote, mtayaacha majukumu yenu yote, tukabiliane na jambo hili, si kazi rahisi kama tunavyodhani, kuwakabiri watu hawa ni sawa na kuwa mkononi na tiketi ya kwenda ahera, kwa vile tuliapa kuilinda Jamhuri yetu, hatuna budi kuifanya kazi hii”, niliwaambia huku wote wakiniangalia kwa macho makavu.

“Hakuna shaka kuhusu hilo Kamanda”, alieleza Claud, Julius akatikisa kichwa kuunga mkono.

Nikatumia nafasi hiyo pia kuwaeleza wenzangu kuhusu ujio wa shemeji yangu Mama Feka, nikawaeleza nilivyopanga kumtumia mwana mama huyu.

“Ataweza?”, alihoji Nyawaminza huku akicheka.

“Naamini ataweza, Mama Feka ni mmoja kati ya wanamke jasiri sana”, niliwahakikishia, halafu nikamgeukia Fred, “Sikiliza Fred, hawa jamaa watafutie mahali pa kulala leo, kuanzia kesho hatutakuwa na muda wa kulala, lakini iwe maeneo ya Sinza, Kinondoni au hata Kijitonyama, mimi nitakwenda nyumbani kwangu wakati huu, kuna vifaa vyangu vya kazi nitachukua halafu nitamtafuta Carlos, hata wewe pumzika maana kesho utakuwa na kazi nyingi zaidi”.

“Asante”, Fred alishukuru.

“Angalizo, jambo hili bado ni siri, pale ofisini hakuna anayejua mpango huu zaidi ya Mzee Emilly, Twite na wewe Fred, hatuna sababu ya mtu mwingine kujua, ndiyo sababu ya kuwaita hawa jamaa, Claud na Nyawaminza. Of rekodi”, nilionya.

“Nimekusoma”, alieleza Fred.

“Fred, wakati unakwenda kulala, hakikisha unapata ratiba ya huyu Carlos, ujuwe ni mtu wa aina gani, anapenda nini, ana msimamo gani, nani rafiki zake wa karibu na hiki kiwanda chake kinakidhi haja? tumia akili zaidi kuliko nguvu”.

Wakati huo kulikuwa na sherehe kubwa nyumbani kwa Carlos Dimera, vinywaji vya kila aina vilikuwa mezani, nyama za kila aina zilitafunwa, muziki laini ukipenya katika masikio ya watu hawa, kila mmoja akiyatafakari maisha baada ya kazi nzito.

“Umefanya kazi nzuri sana Nombo, kuanzia sasa mshahara wako unaongezwa mara mbili zaidi, lakini hata, Simba, Nyati na Chui pia posho zenu zimeongezwa, mmefanya kazi nzuri sana. Kumfuatilia adui kuanzia usiku wa jana, leo asubuhi, mpaka jioni mnamaliza kazi ni jambo kubwa mmefanya. Kuondoka kwa mbwa huyo ni ushindi kwetu”, Carlos Dimera alieleza.

“Wakati mwingine lazima ujifanye kama mwendawazimu ili kazi yako iwe nzuri. Nguvu ya Nombo kwenye uwanja wa mapambano imesaidia sana, milango yote ya kuingia na kutoka ilikuwa chini yetu, tulisubiri mpaka mwisho, alipotoka tu akakutana na kifo, wakati ndugu zake wakiomboleza sisi tunakula raha”, Nyati alieleza.

“Sasa ni wakati wa kula na kunywa, kazi yenu imenifurahisha sana, sina budi kuwaambia nawapenda sana, shehena kubwa ya dawa za kulevya yenye utajiri, itaingia Dar es Salaam, kesho alasiri, taratibu zote za kupokea mzigo huo zimefanyika, kunyweni lakini msilewe”, Carlos alishauri. Wakaendelea kunywa huku wengine wakicheza muziki.

Wakaendelea kula, kunywa na kucheza muziki

Ilikaribia kuwa saa sita na nusu za usiku, niliposhuka kwenye taksi iliyonitoa katikati ya mji, nilipenya uchochoroni, nikapita nyuma ya Kanisa la KKKT, lililopo Kijitonyama, nikaambaa na ukuta wa kanisa hili nikaibukia kwenye barabara ya vumbi inayoelekea nyumbani kwangu. Nilitembea haraka haraka, nilipoufikia mti ulio karibu na nyumba yangu nikasimama na kuufanya kuwa ngao yangu.

Eneo hili lilikuwa kimya kabisa, ni nyumba yangu pekee iliyokuwa katika hali ya giza. Hii ilitokana na familia yangu kutokuwepo. Baada ya kujiridhisha kuwa hali ilikuwa shwari, nilinyata mfano wa paka, nilipoufikia ukuta wa nyumba, nilitoa funguo za mlango wa siri ulioko nyuma ya ya nyumba, nikaufungua taratibu, nikaurejesha kama ulivyokuwa, nikasubiri kwa sekunde kadhaa halafu nikasogea na kuingia.

Kwa vile hali ya usalama haikuwa nzuri, familia yangu niliihamishia sehemu nyingine, nilitumia nafasi hiyo kukagua usalama wa eneo la nyumba yangu, nilipohakikisha kuwa hakuna dalili zozote za hatari, nikauendea mlango wa nyumba, nikaufungua kwa tahadhari nkajitosa ndani.

Ndani ya Nyumba hii kulikuwa kumepekuliwa sana, kabati ya nguo iliyoko chumbani kwangu ilikuwa imepekuliwa na baadhi ya nguo na vitu vyangu vingine kuachwa bila kuvirejesha mahali pake. Nadhani waliamua kuviacha hivi baada ya kujiridhisha kuwa waliniua katika shambulizi la Posta kwa hiyo waliamini kuwa siko tena duniani. Lakini walikosea jambo moja. Hakuhakikisha nani alikuwa akiendesha gari lile walilolishambulia.

Kiasi fulani nilicheka mwenyewe, maana nilijua sasa kazi imeanza, niliyakumbuka maneno ya Rais wa kwanza wa Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, alipokuwa akitangaza vita dhidi ya majeshi dhalimu ya Ndul Iddi Amin Dada wa Uganda. Kilichonisisimua zaidi ni pale Mwalimu aliposema, ‘RAFIKI ZETU WALIOKUWA WANASEMA MWALIMU ACHA, SASA WAKAE PEMBENI, WATUPISHE, MAANA HATUTAWASIKILIZA TENA, ILI SASA UBISHI UISHE’.

Maneno haya ya Mwalimu Nyerere yaliniongezea hamasa, nililiendea kabati langu maalumu lenye dhana zangu muhimu za kazi, kabati hili lilikuwa sehemu ya siri, nikalifungua kabati hilo lililoko ukutani, nikatoa fulana mbili maalumu zisizopenya risasi (bletproof), nikazihifadhi vizuri kwenye mkoba wangu, halafu nikatoa bastola mbili aina ya M9 zisizotoa sauti, zote zikiwa zimejazwa risasi kumi na mbili kila moja kwenye magazini zake, nikazifutika kwenye mapaja yangu, moja kulia na nyingine kushoto. Nikatoa magazini zingine nne zenye risasi za ziada, mkasi wa kukata vyuma na kisu kidogo nikaviweka kwenye mkoba wangu.

Kichwa changu kilijawa na mambo mengi, nilijiuliza hili na lile, nikishika hili na lile. Niliwakumbuka wenzangu, Luteni Claud Mwita, Fred Libaba na Julius Nyawaminza, moyo wangu ukajawa na matumaini ya ushindi. Maana kila mmoja alikuwa na hamasa ya kuingia kwenye uwanja wa mapambano.

Baada ya kutoa vifaa hivyo, nilirudi hatua moja nyuma, nikasimama nikitafakari nini kingine kitanisaidia zaidi katika mapambano na watu hawa, nikaikumbuka ngazi yangu ambayo mimi huitumia kupanda au kushuka kwenye majengo makubwa. Pamoja na kwamba nilikuwa na kamba maalumu niliyoinunua Kariakoo kwa ajili ya kazi hiyo, nikalazimika pia kuichukua ngazi. Usidhani ni mzigo mkubwa, ilikuwa ngazi ya kisasa kabisa, unaweza kuiweka hata kwenye mkoba wako na mtu asijuwe ulichobeba.

Sasa nilikuwa tayari kwa mapambano na watu hawa, nilipiga magoti chini nikamuomba mungu wangu, nikawaomba bibi na babu zangu ili wanisaidie. Nikayakumbuka maneno mazuri ya waswahili, ‘AKUANZAE MMALIZE’ nikaapa kufa au kupona. Ama zangu ama zao.

Baada ya kupiga maombi, nilitoka ndani ya nyumba yangu na kuacha kila kitu kama nilivyokikuta, Hasira na woga vyote vilikuwa ndani ya nafsi yangu, nikajiuliza iwapo nitaishia njiani katika vita hivi nani atakuja kuviendeleza. Imani ikanijia kuwa iko siku atapatikana kijana mkeleketwa wa atakayewasha moto na kuendeleza mapambano hadi kieleweke.

Saa yangu ya mkononi ilinieleza kuwa ni saa nane kasoro dakika chache usiku, nilipenya kwenye uchochoro nikatokea Chuo cha Ustawi wa Jamii, eneo hili lilikuwa na wasichana kadhaa wanaouza miili yao, waliponiona walinigombea, lakini mimi sikuwajali, niliwapita kimya kimya nikatafuta taksi iliyonishusha karbu na taa za usalama barabarani za Morocco.

Muda huu magari yalikuwa machache barabarani, baada ya kushuka kwenye taksi iliyonileta, nilitembea haraka kurudi nyuma, kama Fred alivyokuwa amenielekeza, nilianza kuhesabu nyumba moja baada ya nyingine, nikiitafuta nyumba ya Carlos Dimera, hatmaye nikaiona.

Eneo hili lilikuwa limezungukwa na miti mingi, kwa vile nilikuwa nimevaa nguo nyeusi, nililipita geti kuu la kuingilia ndani. Nilifanya hivi ili kuona kama kulikuwa na mtu yeyote eneo hilo. Baada ya kujiridhisha nilirudi nikinyata taratibu na kwa tahadhari kubwa, nikauparamia mti uliokuwa karibu na ukuta, nikatulia juu kwa sekunde kadhaa, nikiangalia ndani ya ngome hii. Nilipoona hali ni shwari niliifungua ngazi yangu, nikaifunga juu, halafu nikashuka taratibu kwa hadhari, hatimaye nikajitosa ndani.

Mwanga mkali wa taa ulilifanya eneo hili kuwa la usalama wa kutosha, muziki laini ulisikika ndani ya jengo lililokuwa mbele yangu. Nililala kifudifudi, nikakuloo hadi nyuma ya dirisha lililokuwa na kelele ya muziki, nikautumia mti mkubwa uliokuwa eneo hili kujikinga ili nisionekane.

Chumba hiki kilikuwa kimejaa watu, Carlos Dimera alikuwa ameketi juu ya kiti kikubwa, huku wasichana wawili warembo wakifanya kazi ya kumpepea asipate jasho, vijana kadhaa walikuwa wakicheza muziki, huku wengine wakipata vinywaji.

“Jamani, makamanda wangu, mmeinjoi hamjainjoi?” Carlos aliwauliza vijana wake.

“Tumeinjoi sana bosi, tumekunywa, tumekula, tunacheza muziki”, walisema.

“Kama nilivyosema, mzigo unaingia usiku, sasa sitaki mlewe, tuna jukumu kubwa mbele yetu, Teacher amekufa sawa, lakini hatujui nani atafanya nini, au siyo jamani?”, Carlos Dimera alieleza.

“Hakika, lakini nikutoe hofu bosi, kifo cha Teacher kitasababisha wengine waogope kabisa, ni mtu mwendawazimu ambaye ameona kilichompata mwenzake, halafu aingie kichwa kichwa, itawachukua muda”, Nombo alidakia.

“Ndiyo, lakini mnajua wanaweza kujiuliza kwanini Teacher ameshambuliwa na kuuawa kinyama namna ile?”, Carlos Dimera aliuliza.

“Maswali lazima yawepo, nakuhakikishia mzigo utaingia na kusambazwa kwa amani kama ilivyokuwa, huyu mshenzi alikuwa kikwazo kikubwa kwetu, kifo chake ni faraja kubwa katika familia yetu”, Hawa Msimbazi alieleza.

Nilikaa kimya nikiwasiliza washenzi hawa, nilijiuliza kwanini hawakuweka ulinzi wa aina yoyote katika eneo hili, lakini nikabaini kuwa hofu ya kuvamiwa na mimi ilikuwa imewatoka baada ya kubaini kuwa niliuawa katika shambulizi lile.

“Kanali Emilly ameagiza lazima wwatu hawa akamatwe wakiwa na ushahidi, vinginevyo tutakuwa tumefanya kazi ya bure”, nilijisemea mwenyewe, maana bila hivyo walikuwa katika himaya yangu, ningewaita wenzangu tukawatia mikononi, lakini tutakuwa tumefanya kazi ya bure.

“Wakala anasubiri taarifa kutoka kwangu ili mzigo uondoke Addis Ababa, Ethiopia. Hatutaki kufanya makosa, shehena iliyopo stoo ni ndogo, mzigo unaotarajiwa kuingia ni mkubwa kiasi cha matumizi ya miezi sita, kazi kwenu, kuingia kwa mzigo huu kutawafanya wote kuuaga umasikini”, aliwaeleza Dimera.

“Bosi, tumejipanga vizuri mno, waswahili wanasema kila anayetaka cha uvunguni sharti ainame, maana yangu ni kwamba, kila atakayeonekana kuingilia anga zetu, mauti yatamkuta, Teacher ni mfano wa kuigwa na wenzake”, Jakna alifafanua.

“Basi, maneno yenu yamenitia nguvu, Jakna, unajua utaratibu wa kupokea mzigo, panga halafu utanijulisha, nitawasiliana na wakala ili kuwajulisha hali halisi ya Dar es Salaam. Kama ilivyo kawaida yetu, Hawa Msimbazi, utasimamia taratibu za kupokea mzigo. Sitaki mpango wetu huu uferi”, alisisitiza.

Walizungumza na kujadili mambo mengi huku nikiwasikiliza, nilimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika hapa na kusikia upuuzi wao, ilionekana kuwa hofu yao ilikwisha kabisa baada ya kufanya shambulizi lililomuua kijana wetu David.

Dakika kumi zilikuwa zimenitosha kabisa, baada ya kudaka baadhi ya maneno ambayo niliamini yatanisaidia katika kazi yangu, nilijitoa taratibu, nikapita sehemu ile ile ya awali, nikatoa ngazi yangu na kuondoka eneo hili salama usalimini. Nikiamini kuwa habari hizi zitamshangaza sana Fred.

Baadhi ya maofisa walikuwa wameugeuza uwanja wa ndege kuwa njia ya kupitisha dawa za kulevya. Raymond Keneko, alikuwa Afisa Mwandamizi Kitengo cha Ukaguzi wa mizigo. Kiutendaji ukimuona utaamini kuwa ni mtu makini, mwenye msimamo wa kati, asiyeyumbishwa katika kazi zake. Lakini alikuwa mmoja wa watu hatari, dhaifu waliopenda kupokea zawadi kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa, bila kujua kuwa zawadi hizo ni kishawishi.

Ndiyo kwanza Kenoko alikuwa amefikisha umri wa miaka arobaini na saba. Akiwa mmoja wa watumishi wachache wa uwanja wa ndege waliokuwa wakipokea pesa nyingi kutoka kwa mzungu Carlos Dimera, kila wakati mzigo wa dawa za kulevya unapokuwa njiani kuletwa Jijini Dar es Salaam.

Asubuhi hii wakati Kenoko akipata kifungua kinywa nyumbani kwake, alipokea ujumbe kutoka Hawa Msimbazi, ukimjulisha kuwa malighafi za kiwanda cha kutengeneza vidonge vya malaria zilizokuwa zimekwama nchini Ethiopia baada ya kukosa usafiri sasa tayari kuletwa Tanzania. Kutokana na uzito wa ujumbe huo, Raymond Kenoko alilazimika kuacha kila kitu mezani, akafanya maandalizi yake na kuondoka haraka kuelekea kazini.

Mkewe na watoto waliyajua vizuri majukumu yake, hivyo hawakushangazwa na kitendo cha kuacha chakula mezani. Alipofika ofisini, aliwapanga vizuri watu wake, aliweka kila jambo katika mstari, akipita kila idara inayohusika na ukaguzi wa mizigo akiweka mambo sawa. Baada ya kila jambo kuwa limefanikiwa, aliwasiliana na Hawa Msimbazi.

“Nakujulisha kuwa kazi yangu imekwisha, kazi imebaki kwenu dadangu, njia zote za kuingia na kutoka ziko wazi. Mwambie Carlos asihofu, kila idara imejulishwa kuhusu kuingia kwa mzigo huo, bahati nzuri ni kwamba wakuu wa idara zote wamepewa amri kuushughulikia mzigo wenu haraka, wanasubiri mgao wao”, Raymond Kenoko alimjulisha Hawa Msimbazi.

“Umesomeka kakangu, Carols mwenyewe amesema malipo yako yataongezwa, kazi unazofanya kwa upande wetu zinastahili nyongeza, mimi kama mwakilishi wake, naahidi kuongeza posho zaidi”, alisema na kukakata simu. Kisha aliwasiliana na Carlos Dimera.

“Habari ya asubuhi bosi?”, Hawa alimsalimia Carlos.

“Niko salama, una habari gani nzuri?”, alihoji Carlos Dimera.

“Habari nzuri ni kwamba Uwanja wa ndege kumeeleweka. Taratibu zimekwenda vizuri, Mr. Raymond anasema kwa upande wao hakuna shaka, kazi imebaki kwetu, tena amenihakikishia kuwa idara zote zinazohusika kupokea mizigo zimejulishwa kuhusu kuingia kwa mzigo huo, hali ni shwari”.

“Nimekupata Condeliza Rise, maana hauna tofauti kabisa na mwana mama wenye jina hilo, kazi alizofanya akiwa Waziri wa Mambo ya Nje Marekani, zilitosha kumfanya awe kivutio kwa wanawake wenzake duniani. Ngoja niwasiliane na wakala ili mzigo usafirishwe kwa ndege ya usiku leo.

“Fanya hivyo bosi, kilichonisisimua zaidi ni kwamba, huyu Raymond ambaye ndiye Afisa mkaguzi, anasema njia ziko wazi”.

“Asante Hawa, wapange watu wako vizuri mkaupokee mzigo huo, sitaki kusikia jambo baya limewakuta”, Carlos alibainisha.

“Tuko tayari kwa mapokezi na kwa lolote, napata faraja kwamba, Raymond amesema hali ni nzuri kuliko wakati wote, hususan baada ya Waziri aliyekuwa akiwafuatilia na kuweka kamera za CCTV uwanjani hapo kuhamishiwa wizara nyingine, hii imetuongezea nguvu na matumaini”, Hawa alisema.

“Oke, niwatakie kazi njema na mapokezi mema, lakini tuwasiliane, kila hatua mtakayokuwa mnijulishe, lolote laweza kutokea”, Carlos alieleza wasiwasi wake.

“Ni kweli bosi. Tutakujulisha”, aliongeza Hawa Msimbazi. Baada ya Carlos kuongea na Hawa. Alifanya mawasiliano ya mwisho na wakala.

“Habari ya asubuhi kaka?”, Carlos Dimera alisalimia.

“Huko Tanzania ni asubuhi, Addis Ababa ni mchana, tunakula chakula, leta taarifa?”.

“Ndio maana nikakupigia. Najulisha kuwa hali ya Dar es Salaam ni shwari kabisa, vijana wako tayari kupokea mzigo, kulikuwa na mvua za rasharasha na mawingu ya hapa na pale, lakini sasa yamedhibitiwa, itakuwa vizuri mzigo ukiingia Dar es Salaam leo usiku. Hali ni nzuri”, Carlos Dimera alieleza.

“Mzigo uko tayari, kilichokuwa kikisubiliwa ni taarifa za awali kutoka kwenu, hata hivyo Mamlaka za usalama nchini hapa Ethiopia zilianza kuhoji kuwepo kwa mzigo huu, lakinimaofisa wetu makao makuu Bogota, Colombia waliwasiliana na mamlaka za hapa na kuzijulisha kuwa mzigo huu unaopita, naamini utaingia leo Dar es Salaam”, alieleza wakala.

“Asante na samahani kwa kuchelewa kutoa taarifa za awali, hii imetokana na hali ya usalama nchini Tanzania kuwa si ya kuaminika wakati huu, kiasi fulani mambo hayaeleweki. Serikali ya sasa haitabiriki, kwa kuwa mipango imekaa vizuri sasa tuko tayari kupokea mzigo, ambao utawafanya vijana wengi wa nchi hii kupoteza mwelekeo baada wakivuta dawa hizi za kulevya”, Carlos alieleza na kukata simu.

ITAENDELEA

Noti Bandia Sehemu ya Tatu

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment