Nyuma ya Machozi Sehemu ya Tano
MAISHA

Ep 05: Nyuma ya Machozi

SIMULIZI Nyuma ya Machozi
Nyuma ya Machozi Sehemu ya Tano

IMEANDIKWA NA: ALLY MBETU

*********************************************************************************

Simulizi: Nyuma ya Machozi

Sehemu ya Tano (5)

ILIPOISHIA:

Wazo la kumuua aliliondoa kwa vile aliamini hakuna mwanaume chini ya jua anayempenda kama Kinape. Ila aliapa kila atakayeonja asali yake itageuka sumu na kuapa kumsaka aliyemtoa usiku mpenzi wake na kuhakikisha anampoteza kama alivyompoteza Happy.

SASA ENDELEA…

Pia alipanga kutomuuliza chochote hata akirudi asubuhi lakini atafanya uchunguzi wa siri na akimjua lazima amuue. Alishindwa kulala na kujikuta akizunguka nyumba huku akilia akiuapia moyo wake kuwa ataendelea kubeba dhambi mpaka hapo Kinape atakapojua thamani ya penzi lake.

Alishinda amekaa sebuleni macho muda wote alilia kwa hasira, alikumbuka Kinape akirudi na kumkuta analia lazima angehoji hapo angekosa la kujitetea. Alifuta machozi na kunawa kisha alipanda kitandani na kujilaza japo usingizi hakuwa nao kifua kilivimba kama kinataka kupasuka kwa hasira.

Kinape alirudi nyumbani alfajiri akioneka amelewa, Kilole alipokea bila kumwambia kitu. Kwa vile alikuwa amechoka baada ya kuoga alipanda kitandani kulala.

Kinape akiwa njiani akirudi nyumbani alifuta meseji zote hata simu alizompigia Happy. Akiwa amelala Kilole alitumia nafasi ile kuipekua simu ya mpenzi wake lakini kila alipofungua hakukuta kitu. Aliamini mtihani wa kwanza ameshindwa lakini hakutaka kuwa mkali kwani aliamini muonja asali haonji mara moja lazima atarudi hapo lazima atamkamata na kufanya alichokipanga.

DEUS GEREZANI

Baada ya Teddy kuondoka gerezani, mkuu gereza alikuwa na mazungumzo na Deus ili kujua kipi kinatakiwa kabla ya kutolewa gerezani.

“Deus kwanza nashukuru kwa mgeni wako, yaani na mimi nitamalizia nyumba yangu na kupata kigari cha kutembelea, si unajua bado miaka miwili nistaafu, mbona kaniokoa.”

“Yote inatokana na wema ulionitendea, na mimi nakuahidi nikirudi safari yangu salama nitakupa zawadi kubwa.”

“Usiwe na wasiwasi, kuna kitu nilitaka kujua kutoka kwako.”

“Kitu gani hicho mzee wangu?”

“Kwa muda huu unataka nikufanyie kitu gani ambacho unaamini kitakuweka katika hali nzuri kwa muda uliobaki.”

“Tena umeniuliza swali zuri ambalo lilikuwa likiniumiza kichwa.”

“Kitu gani? Niambie nipo tayari kukusaidia, unataka ukae nje ya gereza muda huu?”

“Hapana, kupata muda wa mazoezi ya kujiweka sawa kabla ya safari yangu ya Italia.”

“Hayo mazoezi saa ngapi?”

“Usiku.”

“Hakuna tatizo, usiku nitakuchukua mwenyewe kukupeleka kwenye gim na kukurudisha.”

“Nitashukuru.”

Baada ya mazungumzo Deus alirudi gerezani kwa mwendo wake wa kuvuta mguu kuonesha bado ugonjwa unamsumbua. Mkuu wa gereza alipanga mpango ule kuhakikisha Deus anatoka mapema kwa kuhofia yaliyomkuta kama angekaa gerezani kwa muda mrefu lazima atakufa kwa mawazo.

Usiku majira ya saa nne wakati wafungwa wote wamelala Deus alitolewa kwenye chumba alichotengewa na kuongezwa baadhi ya vitu vya kumliwaza toka Teddy alipompa mkuu wa gereza asante la milioni kumi. Deus alipelekwa gim muda ambao watu walikuwa wamemaliza na kufanya mazoezi peke yake kwa saa mbili kisha alirudishwa gerezani na kujipumzisha huku akila chakula kizuri kilichokuwa kikipikwa kwa mkuu wa gereza.

JIJI MWANZA

Penzi la Kinape na Happy alilizidi kuota mizizi kiasi cha Kinape kumuongezea wiki nzima kuwepo jiji Mwanza kuendelea kuwa naye akiamini ndiyo njia pekee ya kumuenzi mpenzi wake marehemu Happy aliyeuawa na Kilole. Mabadiliko ya Kinape yalimfanya Kilole kuendelea kupelelezi bila kuonesha ameshtukia kitu.

Kwa vile ilikuwa ni vigumu kugundua huwa anakwenda wapi, ilibidi amkodi mtu kumfuatilia Kinape kila kona ili ajue anakwenda wapi kila apoondoka nyumbani. Kijana mmoja aliifanya ile kazi kwa kufuatilia nyendo za Kinape na kufanikiwa kumuona akiingia hoteli ya Gorden Crest.

Baada ya kumuona katika hoteli ile zaidi ya mara mbili alimpigia simu Kilole kumjulisha.

“Sister huwa anakuja hoteli ya Gorden Crest.”

“Umemuona hapo mara ngapi?”

“Zaidi ya mara mbili na akiingia huchukua muda mrefu kutoka.”

“Umemuona kaongozana na nani?”

“Kwa kweli mara zote nimemuona peke yake.”

“Na akitoka huwa ameongozana na nani?”

“Hutoka peke yake.”

“Nitakuongeza fedha chunguza huingia wapi na huwa na nani.”

“Hakuna tatizo nitakuwa jibu muda si mrefu.”

Anko Jay Jay kijana aliyepewa kazi ya kumchunguza Kinape alipokata simu aliingia ndani ya hoteli ya Gorden Crest lakini alishindwa aanzie wapi na amuulize nani. Kwa vile ilikuwa vigumu kujua yupo mule kwa ajili ya mazungumzo au chumbani na mwanamke.

Akiwa amesimama kwenye korido akiwaza alimuona Kinape ameongozana na msichana mmoja mzuri. Walimpita wakizungumza na kusimama pembeni yake, aliwasikia wakizungumza:

“Sasa baby wacha nikimbie nyumbani si unajua yule mtu machale yameanza kumcheza ila nikija Arusha utanichoka.”

“Siwezi baby, yaani nitanenepa.”

“Kapumzike basi baby, kesho.”

Anko Jay Jay alishuhudia Kinape akilishana mate mbele yake kisha waliagana na Kinape kutoka nje ya hoteli na yule msichana kurudi chumbani. Anko Jay Jay aliachana na Kinape na kumfuatilia yule mwanamke aliyepanda ngazi kuelekea juu.

Alimfuata mpaka alipomuona akiingia katika chumba ambacho alinakili namba zake kisha aligeuka na kuteremka hadi chini kisha alimpigia simu Kilole.

“Haloo sister itabidi uniongeze mshiko.”

“Ukifanya kazi nzuri sitakuwa na hiyana nitakuongeza nyingine kama niliyokuahidi.”

“Basi sister nimefanya bonge la kazi.”

“Usiniambie!” Kilole alishtuka kusikia vile.

“Nimemaliza kila kitu kazi kwako.”

“Mmh! Niambie umefikia wapi?”

Anko Jay Jay alimweleza yote na kumfanya Kilole afurahie kwa kuruka juu na kusema:

“Anko Jay Jay umefanya kazi nzuri sana.”

“Kwa hiyo?”

“Njoo uchukue chako, nikiwa na shida nitakutafuta ila nakuomba siri hii usimwambie mtu,” Kilole alimuonya Anko Jay Jay.

“Siwezi sister.”


Kinape kutokana na kubadili ratiba yake ya kuwahi kurudi nyumbani pia mpenzi wake kutoonesha wasiwasi wowote aliamini mambo yake yanakwenda vizuri. Ilikuwa lazima aende mchana hotelini na kula chakula cha pamoja na Happy na jioni kuwa pamoja hadi saa nne usiku na kurudi nyumbani huku akimweleza Kilole kuwa na mazungumzo na rafiki zake.

Siku ya pili kama kawaida Kinape majira ya saa sita mchana alikwenda hotelini kwa Happy kwa ajili ya chakula cha mchana. Mlango ulikuwa umerudishwa kama kawaida alifungua mlango huku akiita:

“Sweetiiiii.”

Kama kawaida yao kila alipofika na kumwita vile Happy hukurupuka na kwenda kumrukia kwa furaha. Lakini siku ile alishangaa kutopokewa alipoingia ndani alimkuta Happy akiwa amelala kifudifudi kitandani akiwa katika mavazi ya kulalia.

“Babiiii,” Kinape alimwita huku akimsogelea kitandani.

“Babiii kulala gani huko, amka tukapate lunch.”

Happy hakujigeuza wala kuitikia, ilibidi amtikise huku akimwita.

“Happy..Happy, wake up baby.”

Lakini vilevile hakuonesha kushtuka kitu kilichomshtua Kinape na kumgeuza kwa nguvu ili kumshtua. Happy aligeuka mzimamzima akiwa amelegea kifuani kukiwa na damu na sehemu aliyolala kulikuwa na damu nyingi. Kinape alishtuka na kutaka kupiga kelele za kilio lakini alishika mdomo asitoe sauti.

Alipomchunguza aligundua mpenzi wake mwingine kauawa kwa risasi. Kwa haraka alitoka nje ya chumba na kukimbilia nyumbani huku akiwa katika hali ya kuchanganyikiwa. Kilole alishtuka kumuona yupo katika hali ile alimfuata chumbani na kumkuta Kinape machozi yakimtoka huku mikono ikikosa pa kushika kila alipojishika aliona hapafai.

“Honey vipi?”Kilole alimuuliza.

“Safi.”

“Mbona hivyo?”

“Wee acha tu,” alijibu huku akigeukageuka kitandani kama kuna miba.

“Kuna nini honey? Kilole alimuuliza kwa sauti ya upole.

“Hakuna kitu naomba uniache,” Kinape alijibu kwa hasira mikono ikiwa kichwani.

“Mmh! Haya ukihitaji msaada wangu utanifuata,” Kilole alisema huku akitoka nje.

Kinape alianza kulia kilio cha sauti huku akisema:

“Kwa nini lakini…Ooh! Happy kwa nini lakini? Uuuu aaa..sikubaliii Happy hawezi kufa kirahisi namna hii,” alilia huku akipiga ngumi kifuani kwa nguvu.

Kinape alijua lazima aliyefanya kitendo kile cha ukatili atakuwa Kilole tu hakukuwa na mtu mwingine ambaye angefanya mauaji kama yale.

Alikumbuka kifo cha mpenzi wake wa kwanza hakikuwa na tofauti na kile cha Happy wa pili. Moyoni alijiuliza Kilole ataendelea kuua mpaka lini. Alitoka chumbani kama mbogo na kwenda sebuleni kumfuata Kilole amueleze kwa nini amemuua Happy.

Aliapa bila majibu mazuri angemfia mikononi, alipofika alipokuwa amekaa Kilole akisoma ujumbe kwenye simu wakati huo katika luninga kulikuwa kunaoneshwa tukio la mauaji katika hoteli ya Gorden Crest. Kinape kwanza alitulia kusikiliza nini kinaendelea baada ya kifo cha Happy.

Mtangazaji alielezea tukio la kifo cha msichana aliyefahamika kwa jina la Happy Simoni Mfanyakazi katika kampuni ya Utalii Arusha aliyeuawa kwa risasi majira ya saa nne na saa tano asubuhi katika hoteli ya Gorden Crest. Mtangazaji aliendelea kusema kuwa msichana yule alikuwa amepanga pale siku ya tatu akiwa na mpenzi wake wa kiume ambaye alikuwa halali pale na kukutana mchana na usiku kisha mpenzi wake huondoka.

Taarifa ziliendelea kusema siku ya tukio mpenzi wake alionekana pale hotelini na kwenda kuweka oda ya chakula cha mchana kama kawaida, baada ya wahudumu kuona anachelewa ndipo walipokwenda chumbani na kukutana na tukio lile la kutisha bila kumuona yule mpenzi wake.

Taarifa zilizidi kuelezwa kuwa baada ya hapo walitoa taarifa katika uongozi wa hoteli kisha kuitaarifu polisi waliofika na kuichukua maiti kwa uchunguzi zaidi huku mpenzi wake akiendelea kusakwa na polisi.

Baada ya taarifa ile Kinape alimgeukia na kuuliza kwa sauti kali:

“Nani kamuua Happy?”

“Happy! Ndiye nani?” Kilole alijifanya kushangaa.

“Unajifanya hujui siyo?” Kinape alimtolea macho yaliyokuwa mekundu kwa ajili ya kulia.

“Baby mbona unataka kuniingiza katika matatizo, nimuue Happy mara mbili?” Kilole alizidi kuruka.

“Siyo mpenzi wangu wa Dar huyu aliyekufa leo hii.”

“Kinape…Mimi na sijui huyo Happy wapi na wapi, kwanza nimuue kanifanya nini?” Kilole alijifanya kushangaa.

“Nitajua tu muda si mrefu.”

“Kujua nini, kwanza nataka uniambie huyo Happy ni nani? Kinape ulikuwa na mwanamke wa pembeni?” Kilole naye alikuja juu huku akimfuata Kinape na kumvuta shati.

“Niambie Kinape kumbe ulikuwa na mwanamke unaona Mungu kakuumbua.” Kilole alisema huku akilia kwa uchungu.

“Nitajua tu.”

“Kujua nini mpenzi wangu, anayetafutwa ni wewe?”

Kinape alikaa kwenye kiti na kuanza kulia kwa sauti ya kwikwi huku akisema:

“Nini hatima ya yote.”

Kilole alimfuata na kukaa pembeni yake na kumsemesha kwa sauti ya upole:

“Baba Junior hebu nieleze kifo cha huyu msichana wewe kinakuhusu vipi?”

“Ni rafiki yangu ambaye alikuwa mfanya biashara na nilikuwa nakwenda pale kwa ajili ya mazungumzo ya kufanya biashara Mwanza na Arusha. Leo nilipofika nikakuta ameuawa kwa kupigwa risasi kifuani.”

“Anafanya biashara gani? Kama madini huenda ameuawa na majambazi, hakuibiwa kitu chochote?”

“Hata sijui huoni kama mimi nipo hatarini.”

“Nitakusaidia mpenzi wangu, itabidi uondoke kajifiche Afrika ya Kusini mpaka matatizo yakiisha urudi ukiweezekana tuhamie huko wote.”

“Yaani ikiwezekana hata leo niondoke maana nikishikwa nitanyongwa au kuozea gerezani.”

“Hakuna tatizo mpaka jioni utapata jibu la safari kuna mtu nitampigia simu ili uondoke na ndege ya saa sita usiku.”

Tarehe Tisa Desemba siku ya uhuru mheshimiwa rais alipotangaza msamaha kwa wafungwa wenye vigezo vya kuachiwa, Deus alikuwa mmoja ya watu walionukaika na msamaha huo. Kama kawaida walisomewa majina wafungwa watakao achiwa na kutolewa gerezani kwa msamaha wa rais.

Baada ya kusomewa Deus alitoka katika mwendo wake wa kuvuta mguu wa kushoto kama kweli ni mgonjwa. Wafungwa wenzake walimuaga wakiamini kabisa jamaa yao ni mgonjwa ambaye hakuwa na faida yoyote kuendelea kuwepo gerezani.

Baada ya kutoka gerezani, nje ya gereza alimkuta Teddy akimsubiri na kuondoka naye ndani ya gari lililokuwa na vioo vyeusi mchana ule moja kwa moja mpaka uwanja wa ndege na kwenda naye kwenye maficho yake jijini Mwanza.

Walifika Mwanza majira ya saa tisa alasiri, baada ya kufika tu Mwanza hakutaka kupoteza muda alimuuliza Teddy.

“Ipe information ili kazi ifanyike mara moja.”

“Deus mbona haraka sana kwa nini usipumzike kwa siku mbili tatu, nina wasiwasi ulitakiwa upumzike mwezi mzima kuuandaa mwili. Kifungo si mchezo hasa magereza ya kibongo.”

“Teddy nipo fiti huu mwili unauonaje?” Deus alitoa shati kuonesha mwili uliojengeka kimazoezi.

“Ha! Deus, mwili umejengeka kimazoezi umefanya muda gani? Tena unaonesha upo fiti.”

“Ile mbaya, nimejiandaa kuifanya kazi kwa aina yoyote ya mapigano kwa siraha au mkono mtupu.”

“Kwa hiyo ulitaka twende lini?”

“Kesho.”

“Keshooo?” Teddy alishtuka.

“Teddy hebu tumalize kazi hii mara moja ili nifanye nyingine, una picha ya huyo mshenzi?”

“Sina, labda tuangalie kwenye Facebook.”

Waliwasha Lap top na kuiweka moderm na kumsachi jina la Moses Chris, lakini ilionesha ameondoa picha zake zote na kuacha kivuli tu kwenye jila lake.

“Sasa tutafanyaje?” Deus alimuuliza Teddy.

“Nimekumbuka hebu sachi jina la Jarome Moore.”

Walitafuta jina la Jarome Moore na kufunguka kisha walifungua kwenye picha zake, baada ya kutafuta kwa muda Teddy alisema.

“Huyu hapa,” alimuonesha kwenye picha aliyopiga pamoja na Jarome Moore.

“Okay, tuisevu kwenye desktop.”

Baada ya kuiweka desktop Deus aliikuza na kuitazama kwa muda kisha alisema:

“Okay, nimemuona.”

“Kwa hiyo?”

“Tayari.”

“Ina maana huchukui picha yake?” Teddy alishangazwa na uchukuaji wa picha ya Moses.

“Kazi yetu haitakiwi kutembea na picha ya mtu unaweza kutuweka katika matatizo.”

“Kwa hiyo unataka kuniambia umeisha mtambua hata ukikutana naye?”

“Wee utasikia nimefanya nini, fanya mipango ya hati za kusafiria nianze kazi mara moja ambayo nina imani itachukua siku chache kabla sijaanza msako wa kufa mtu wa wale mashetani.”

“Ukiwashika utafanyaje?”

“Nitajua nikiwashika, ila nitakachowafanya Mungu anajua.”

“Hiyo kazi nitaifanya miye.”

“Nilitaka kusahau nitaondoka peke yangu hii kazi sitaki msaada ni ndogo sana.”

“Kwa nini? Utawaweza peke yako nasikia wapo wengi.”

“Mimi peke yangu sawa na jeshi la watu mia.”

“Mbona unajiamini sana?”

“Kwa vile najiamini.”

“Kwa hiyo unataka ondoke lini?”

“Teddy, huu si muda wa kupoteza, natakiwa niondoke kesho usiku.”

“Visa nitapataje?”

“Mpigie mtu huyu.”

Deus alimpa namba ya rafiki yake kipenzi anayefanya kazi uhamiaji. Baada ya kuita alizunguza naye.

“Haloo.”

“Haloo.”

“Nani mwenzangu?”

“Deus.”

“Deus! Deus gani?”

“Mpolipoli.”

“Wee Acha utani, Deus mpolipoli ni mmoja tu ambaye mpaka sasa sijui yupo hai au amekufa.”

“Hajafa yupo hai na ndiye unayezungumza naye.”

“Wewee, acha utani! Ni wewe kweli?”

“Sasa kiliza Bon ni hivi nitafutie visa ya kusafiri kesho jioni.”

“Lakini mbona kama siamini.”

“Bon, ni hadithi ndefu unayoijua na usiyoijua, kama nikirudi salama safari yangu ya Italy tutazungumza mengi.”

“Unajua siamini.”

“Best camooon.”

“Kweli nimeamini ni wewe, nipe muda upo wapi?”

“Nipo Mwanza, usiku wa leo nitakuwa Dar kwa ajili ya safari ya Italia.”

“Siamini mpaka nikuone.”

“Utaniona la muhimu nifanyie hiyo kazi mara moja.”

Deus alikata simu na kumgeukia Teddy aliyekuwa bado ameshangaa.

“Vipi mbona unanishangaa?”

“Siamini, visa utapata kesho.”

“Kesho ni safari ya kifo.”

“Deus kwa nini tusiende wote? Unajua moyo wangu haunipi kabisa wewe kwenda peke yako.”

“Hapana kazi hii si ya kitoto.”

“Deus unanidharau kwa vile mwanamke?”

“Walaa, kazi hii tukienda wawili tunaweza kumpoteza mtu, sitaki nikuone akifa.”

“Siwezi Deus.”

“Nina uzoefu na safari za aina hii, kama jamaa anakuwinda utakuwa umepata nafasi ya kukupata kwa urahisi. Niache nicheze naye kwa vile hanijui nitamumaliza kama kuzima kibatari.”

“Deus ukifa nami nitakufa nakupenda sana.”

“Asante.”

“Sio siri nilikupenda toka siku ya kwanza na ulichonifanyia ndiyo ulizidi kunimaliza. Naomba nipasue siri yangu ambayo ilinitesa muda mrefu Deus nakupenda sana tena sana.”

“Asante.”

“Deus mbona kila kitu unasema asante au hunipendi?”

“Utajua nikirudi Italia.”

“Hapana Deus naomba uniambie kama kweli nami unanipenda, nina imani nina nafasi kubwa moyoni mwako baada ya mkeo kukutenda.”

“Nami nilikupenda toka nilipokuona lakini sikuweza kusema ningeweza kuharibu kazi.”

“Kweli Deus, nimefurahi sana kusikia kumbe na wewe ulikuwa ukinipenda.”

Walijikuta wamesahau mambo ya safari na kuingia dunia nyingine iliyoandikwa historia mpya kwa siku ile.

“Deus naomba unioe.”

“Hiyo ndiyo itakayofuata kama nikirudi salama.”

“Deus mpenzi utarudi salama nakusubiri kwa hamu kubwa.”

Kila mmoja alimpa uhuru mwenzake mikono yake uzuru pande zote za mwili, ilikuwa raha kwa wote huku Teddy akitimiza ndoto yake ya kumtamkia Deus kuwa anampenda.


Mpango wa Kilole kumtorosha Kunape uligonga mwamba baada mtu waliyekuwa wakimtegemea kufanya mpango wa safari kusafiri kuwa nje ya nchi kwa wiki nzima.

“Sasa itakuwaje mpaka arudi si nitakuwa nimekamatwa?” Kinape aliuliza akiwa amejawa na hofu.

“Kinape usihofu kwa vile hawakujui, we kaa ndani usitoke mpaka soo litakapoisha,” Kilole alimpa moyo.

“Kumbuka wamesema wamechukua mkanda unaochukua matukio yote ya hotalini siku ile huoni nitaonekana?”

“Hata kama utaonekana bado hujaua.”

“Hata kama sijaua huenda wakasema nimeshilikiana na muuaji?”

“Kwanza kamera zile hazina uwezo mkubwa wa kuiona picha kwa ufasaha, pia muuaji ataonekana si wewe hivyo hawatashughulika na wewe zaidi ya kumsaka muuaji.”

“Mmh! Usalama wangu ulikuwa kuondoka hapa tu,” Kinape alihofia kukamatwa na kufunguliwa mashtaka.

“Jamaa anarudi baada ya wiki usiwe na wasi akirudi tu unaondoka.”

“Itabidi nivumilie sina ujanja.”

Wakiwa wamekaa sebuleni wakisikiliza taarifa ya habari, taarifa kutoka polisi zilisema kuwa kamera la hoteli ambazo huonesha mwisho nje ya mlango wa kuingia chumbani. Majira saa saa tano na dakika tano asubuhi alionekana mtu kama mwanamke aliyekuwa amevaa hijabu akiingia katika chumba cha marehemu na kutoka baada ya dakika kumi.

Taarifa ziliendelea kusema muuaji ndiye aliyevaa jazi refu la kumziba mwili mzima. Jeshi la polisi lilikuwa likiomba mpenzi wa mwanamke yule ambaye alikuwa Kinape kwenda kujisamilisha ili kutoa msaada kwa polisi kwa kuonesha muuaji anamjua. Kauli ya mtangazaji ilimfanya Kinape alalamike kwa sauti.

“Jamani mimi nimjue wapi muuaji?” Kinape aliuliza huku akizidi kukata tamaa.

“Hebu acha kujitia presha, usijitokeze tuone watakuona wapi kwa muda huu matembezi yako yatakuwa usiku tu.”

Wakiwa katikati ya mazungumzo mtoto ndani alilia na kumfanya Kilole amfuate ndani na kumkuta amejisaidia, ilibidi amfanyie usafi kwanza. Sauti ya kuonesha katika simu ya Kilole ujumbe umeingia ulilia na kumfanya Kinape kuiona simu ya Kilole aliyoiacha kwenye kochi.

Kwa haraka aliichukua na kuufungua ujumbe ulioingia uliokuwa unasomeka.

“Sawa sister sitamwambia mtu, unatisha lakini kumbe we mafia mbaya.”

Alisoma mwingine uliotangulia ambao ilionesha Kilole aliosoma na kuujibu:

“Sister yule demu anayetembea na mumeo nimesikia ameuawa, vipi umemuua wewe?”

Ulikuwa ujumbe uliotangulia ambao Kilole aliujibu na kutumiwa mwingine ambao nao aliamini angeujibu. Aliichukua namba ya simu ya aliyetuma ujumbe na kuufuta ujumbe ulioingia ili Kilole asijue kama ameshika simu yake na kuirudisha simu juu ya kochi kama ilivyokuwa.

Moyoni alitamani kumuuliza lakini alivuta subira isionekane kama anampekua baada ya kuwekeana mipaka kwenye simu zao. Kilole akiwa chumbani alikumbuka amesahau simu juu ya kochi sebuleni. Alimweka mtoto kitandani na kutoka haraka.

Simu yake aliikuta alipoiacha aliichukua na kurudi nayo chumbani, kabla ya kuingia chumbani Kinape alimwita.

“Kilole.”

“Abee,” aliitika huku akigeuka kumtazama.

“Mbona umefuata simu kwa haraka?”

“Nilisikia ikiita kumbe masikio yangu.”

“Mmh! Haya.”

“Kwani umewaza nina mwanaume wa nje?”

“Basi tu.”

Kilole hakuongeza neno alielekea chumbani kumvisha nguo mtoto kisha alitoka naye na kukaa pembeni ya mpenzi wake ambaye aliamini ana mawazo ya kukamatwa kumbe alikuwa amepata nusu ya ushahidi wa kifo cha mpenzi wake Happy.

Akiwa amekaa akimuangalia Kinape alijikuta akikumbuka jinsi alivyomuua mpenzi wa Kinape. Baada ya kukamilisha uchunguzi wa mabadiliko ya mpenzi wake na kufahamu ana mpenzi aliyempangia Gorden Crest alijipanga kwenda pale.

Majira ya saa nne asubuhi baada ya kumlisha chakula mtoto wake alimlaza kitandani na kuvalia baibui lililouficha mwili na uso na kuchukua bastora aliyoichomeka kwenye suruali na kutoka.

Alitumia gari dogo na kwenda kulipaki pembeni ya ofisi za Tanesco, gari lake lilitazamana na Maktaba kuu. Alikodi bodaboda na kuteremkia karibu na hoteli ya Gorden Crest. Baada ya kumlipa fedha dereva wa bodaboda alimuomba amsubiri.

“Samahani kaka yangu, kunisubiri kwa dakika kumi utanitoza kiasi gani?”

“Baada ya kukusubiri utaelekea wapi?”

“Nitarudi uliponitoa.”

“Ukinipa buku tatu haitakuwa mbaya.”

“Basi mimi nitakupa tano unasemaje?”

“Utakuwa umecheza sister.”

“Poa, wacha niwahi.”

Kilole alichepua mwendo kuingia ndani ya hoteli na kuelekea upande wa vyumba, kutokana na elekezo aliyopewa kuhusu jografia ya hoteli ile haikumpa kazi kufika kwenye ngazi za kupanda juu na kwenda hadi ghorofa la pili. Alipofika kabla ya kuelekea chumbani kwa mbaya wake alitulia kwa muda kuangalia kama kuna mtu anamfuatilia.

Hali ilikuwa ya tulivu hakukuna na watu sehemu ile, kabla ya kuchepua mwendo aliipapasa bastora yake kupata uhakika kuwa ipo. Taratibu alikwenda hadi mlangoni na kuzungusha kitaza kama mlango umefungwa kwa ndani.

Mlango ulitii amri na kufunguka aliingiza mkono ndani ya hijabu na kutoa bastora yake na kuingia nayo kaishikilia mkononi.

Alimkuta Happy amejilaza kwa kulalia tumbo akiwa katika vazi la kulalia, nguo ilivyokuwa ilionesha hakuwa na kitu ndani kumaanisha alikuwa akimsubiri mpenzi wake ampe burudani.

Baada ya kuingia ndani alitulia akimuangalia yule msichana kwa hasira, aliamini muda ulikuwa unakwenda kwa vile kamuona mbaya wake ilitakiwa kazi moja na kuondoka. Alifunga mlango kwa sauti kidogo kitu kilichomshtua Happy kuamini mpenzi wake amefika.

Alipogeuka alikutana na mwanamke aliyekuwa amevaa hijabu bastora mkononi iliyokuwa imemwelekea yeye.

“Vipi dada?” Happy alishtuka.

“Unashtuka nini ulipomchukua mume wangu mbona hukushtuka?”

“Sa..sa..mahani dada mi..mi..si..jachukua mume wa mtu!” Happy alijitetea huku akitetemeka.

“Kinape mumeo?”

“Si..sijajua kama ni mumeo..ni..nisamehe.”

“Sina muda wa kubishana na mwizi wangu.”

“Sasa unataka kunijfanya nini dada yangu?”

“Unataka kujua, Sali sala yako ya mwisho utajua muda si mrefu.”

“Tafadhali dada usiniue.”

“Lazima ufe kwa vile niliapa kila nitakayemkamata na mume wangu lazima nimtangulize mbele na Kinape anajua hivyo si kosa langu aliyekuponza ni huyo aliyekudanganya.”

“Dada yangu nakuapia kwa miungu yote sirudii te…”

Kilole aliona muda unachelewa alifumba macho na kuminya kifyatulio mara mbili kwa haraka, risasi mbili zilitua kwenye kifua cha Happy na kumrusha kwa nyuma.

Baada ya kukata roho, kwa moyo wa ujasiri Kilole aliuchukua mwili ule na kuulaza kitandani kisha alitoka taratibu kuelekea nje ya hoteli. Alimkuta dereva wa bodaboda akimsubiri alipanda hadi alipopaki gari lake, baada ya kumlipa alipanda ndani ya gari lake na kurudi nyumbani kwake.

Alipofika alijikausha kusubiri taarifa ya kifo cha mpenzi wa Kinape na jinsi mpenzi wake atakavyokipokea. Baada ya saa mbili ndipo aliporudi Kinape akiwa amechanganyikiwa na kumuuliza na yeye kukataa kujifanya hajui kitu. Alipanga kumweleza baada ya kila kitu kutulia.

“Kilole,” Kinape alimwita baada ya kumuona mpenzi wake amehama kimawazo.

“A..abee,” Kilole alishtuka kutoka katika dimbwi la mawazo.

“Vipi mbona kama upo mbali?” Kinape alimshtua Kilole.

“Aah! Ni..ni..po sawa kwani vipi?” Kilole alishtuka kama anatoka ndotoni na kubabaika.

“Mbona kama upo mbali?”

“Aah! Nipo sawa.”

“Basi nataka kutoka mara moja,” Kinape alisema akinyanyuka.

“Wewee! Unataka kwenda wapi umesahau unatafutwa?”

“Ooh! Nilijisahau yaani nimechanganyikiwa ile mbaya.”

Kinape alielekea chumbani kulala na kumuacha Kilole akiwa amekaa sebuleni, baada ya Kinape kwenda chumbani Kilole aliipekua simu yake labda kuna ujumbe umeingia lakini hakukuta na ujumbe wowote.

Alimtumia ujumbe yule Jay Jay asimwambie mtu pia asitume tena ujumbe wowote muda ule ili aende ndani akamliwaze mpenzi wake aliyekuwa kwenye lindi la mawazo.


Majira ya saa tatu usiku Kinape alimuaga Kilole kuwa anatoka mara moja.

“Safari ya wapi tena baba?”

“Si unajua leo nimekaa ndani kama utumbo ngoja nikanyooshe mwili.”

“Sawa baba, kuwa makini tu si unajua sasa hivi wewe ni lulu?”

“Hilo nalijua.”

“Unarudi saa ngapi?”

“Sichelewi.”

“Au twende wote?”

“Na mtoto umuachie nani?”

“Tutatoka naye, si hatufiki mbali?”

“Kuna baridi, huu si muda wake wa kumtembeza usiku, akikuwa tutatoka naye.”

“Haya baba, basi uwahi kurudi si unajua bila wewe nyumba inapwaya.”

“Nalijua hilo mpenzi wangu nitawahi, si unajua leo siko vizuri nahitaji kuwa karibu yako.”

“Ni kweli baby wangu.”

“Basi baadaye, nitachukua gari ndogo.”

“Mume wangu lolote ulitakalo.”

“Lazima nikujulishe,” siku ile Kinape alikuwa mpole sana lakini moyoni palifukuta kwa hasira.

Kinape alitoka na gari ndogo hakufika mbali alisimama gari na kuipiga namba iliyomtumia ujumbe Kilole. Kabla ya kupiga alikumbuka kama ataipiga huenda akashtukiwa alijaribu kwanza kutuma ujumbe kama watashindwa kuelewana basi angempigia. Alituma ujumbe unaosema:

“Oya Anko Jay Jay upo anga zipi mida hii?”

Baada ya muda ujumbe alirudi.

“Nipo Kapili Kabana, nani mwenzangu?”

“Unatoka saa ngapi huko?” aliongeza swali badala ya jibu.

“Mmh! Mpaka saa tano vipi una ishu?”

“Ndiyo.”

“Ishu gani?”

Kinape hakumjibu tena aliwasha gari na kuwahi Kapili Kabana, alipofika alipakia kwenye maegesho na kupiga simu huku macho yake yakitazama mlango wa kutokea.

“Oya, nipo nje njoo mara moja nina haraka.”

Anko Jay Jay alitoka nje haraka akiamini kuna ishu ameletewa, kwani mjini yeye alikuwa akiishi kwa misheni tauni kila kazi iliyokuja mbele yake aliifanya ikiwemo ya udalali wa kila kitu mpaka wake na waume za watu kwake ilikuwa kazi ndogo.

Alipotoka alitazama kulia na kushoto labda atamuona mtu aliyekuwa akimwita, kuhangaikakwa Jay Jay kumtafuta aliyempigia simu kumfanya Kinape amuone kwa urahisi. Akiwa na simu mkononi alipiga ili kumuuliza mtu anayemtafuta yupo wapi. Baada ya muda simu iliita na kumuamini ndiye mhusika, alikuwa kijana mmoja aliyeoneka brother men.

Hakuipokea aliteremka na kumfuata alipokuwa amesimama kwa vile alikuwa amevaa kapelo ilikuwa vigumu Anko Jay Jay kumfahamu, alipomkalibia alimpa mkono na kumsalimia.

“Habari Anko Jay Jay.”

“Nzuri, nina imani ni mtu uliyekuwa ukitafuta?”

“Kweli kabisa,” Kinape alijibu huku akitoa kofia kichwani.

‘Ha!” Anko Jay Jay alipomuona alishtuka na kutaka kukimbilia lakini hakuweza kwa vile Kinape alikuwa amemshika mkono kwa nguvu.

“Sasa unataka kukimbia nini?” Kinape alimuuliza kwa sauti ya chini.

“Siyo hivyo brother.”

“Basi sikiliza naomba uwe mtulivu tuzungumze taratibu bila hivyo nitakufanya kitu kibaya.”

“Sawa Brother,” Ako Jay Jay ilibidi awe mpole.

“Naomba twende kwenye gari langu tuzungumze kirafiki.”

“Hakuna tatizo brother.”

Waliongozana hadi kwenye gari na kuingia ndani, muda wote Anko Jay Jay alikuwa na wasiwasi mwingi. Baada ya kutulia Kinape alimuuliza kwa sauti ya chini.

“Unanifahamu?”

“Ha..hapana.”

“Kuwa mkweli, kwa nini ulitaka kunikimbilia?”

“Ulinishtua.”

“Naomba uniambie ukweli la sivyo kifo cha mwanamke aliyefariki leo wewe ndiye utakaye kuwa mtuhumiwa namba moja.”

“Siyo mimi brother, mi nilitumwa nikuchunguze tu kama una mwanamke, zaidi ya hapo sijui lolote, hata mimi nimeshtuka kusikia yule mwanamke ameuawa.”

“Nani alikutuma?”

“Mkeo.”

“Umemjuaje mke wangu mimi usinijue?”

“Nakujua brother.”

“Alikutuma nini?”

“Alinikutuma nikuchunguze kama una mwanamke wa nje, baada ya kazi yangu kwisha nilimpa ripoti na kunipa changu na mimi kuendelea na mambo yangu mengine. Leo mchana nimeshtuka kusikia yule mwanamke ameuawa kwa risasi, kwa kweli sijui lolote zaidi ya kazi ya kukuchunguza tu brother.”

“Kwa hiyo mke wangu ndiye aliyekutuma?”

“Ndiyo brother.”

“Kama yeye alikutuma nani alimuua yule mwanamke?”

“Sijui, labda yeye mwenyewe.”

“Baada ya taarifa ya kifo yeye alikuambiaje?”

“Amesema nisimwambie mtu juu ya kifo kile pia hata mpango wetu wa kuwachunguza.”

“Asante, naomba taarifa hizi usimwambie mke wangu kama tumeonana, sawa?”

“Sawa brother, nitafanya kama nilivyokueleza.”

“Okay endelea na burudani,” Kinape alisema huku akimshikisha noti mbili za elfu kumi.

“Asante brother,” Anko Jay Jay alipokea huku akiwa haamini kama ametoka salama.

Baada ya kuachana na Kinape alimpigia simu Kilole kumweleza kuhusiana na kufuatwa na mumewe usiku ule. Baada ya simu kuita sana ilipokelewa.

“Anko Jay Jay si nimekuambia usinipigia simu mpaka nikupigie mbona unakuwa si mwelewa?”

“Sister kuna jambo la muhimu limenifanya nikupigie simu usiku huu.”

“Jambo gani?”

“Mumeo kanifuata na kunibana juu ya kifo cha yule msichana na kuniomba nisikuambie.”

“ Anko Jay Jay acha utani?” Kilole hakuamini.

“Kweli sister.”

“Amevaaje?”

“Jinsi ya bluu na tishet nyekundu na kofia nyeusi na chini kavaa raba nyeupe.”

“Mmh! Ni kweli,” Kilole alishusha pumzi ndefu.

“Yaani huwezi kuamini nilishtuka kidogo haja ndogo initoke.”

“He, makubwa! Amekuuliza nini?” Kilole alishtuka sana.

”Eti nani kamuua yule mwanamke.”

“Mmh! Kwanza wewe umekujuaje?”

“Nikuulize wewe, kwa vile siri ilikuwa ya watu wawili.”

“Kosa limetendeka wapi?”

“Lazima litakuwa kwako tu.”

“Mmh! Umemjibu nini?”

“Nimwambia sijui lolote.”

“Halafu.”

“Alinibana na kutishia kunipeleka polisi kuwa mimi ndiye muuaji.”

“He! Ikawaje?”

“Nilimchoropoka na kukimbia, sasa usalama wangu utakuwaje?”

“Okay, Jay Jay nimekuelewa nitakujulisha muda si mrefu.”

“Poa sister jambo hili lifanyie kazi naweza kuozea gerezani wakati sijui lolote kuhusiana na kifo hicho.”

“Anko Jay Jay hebu niachie kazi hiyo maana hata mimi suala hilo limenishtua sana, lakini nakuapia huwezi kukamatwa nitamtuliza huyu mshenzi kabla hajafanya lolote.”

“Sawa sister nakutegemea wewe.”

“Usikonde.”

Kilole alikata simu na kukaa kwenye kochi akiwa amechoka na kuamini itakuwa vigumu kwa Kinape kumwelewa akijua yeye ndiye aliyemuua mpenzi wake mwingine. Aliamini kama Anko Jay Jay alikimbia lazima Kinape atamtafute na kumlazimisha kusema ukweli kwa vile ameishaonesha woga lazima angesema kweli. Alijua usiku ule ulitakiwa kila mtu amzidi akili mwenzake kama Kinape aliweza kumzidi akili kwa kumgundua mtu aliyemtumia kumchunguza lazima atataka kujua nani kamuua mpenzi wake.

Baada ya kuwaza na kuwazua alipata jawabu ya kitu kilichokuwa kikimsumbua kuificha siri ile kabla Kinape hajajua ni kumuua Anko Jay Jay usiku uleule. Alichukua simu yake na kumpigia Anko Jay Jay, baada ya kuita ilipokelewa upande wa pili.

“Vipi Sister?”

“Umesema upo wapi sasa hivi?”

“Nakaribia home siku imeishaingia nuksi.”

“Tunaweza kuonana?”

“Wapi?”

“Tukutane daraja la Nyakabungo.”

“Poa nakuja.” Anko Jay Jay alikuwa anakaa jirani na shule ya Mirongo kufika Daraja la Nyakabungo isingechukua dakika tano.

Kilole alikata simu na kwenda ndani kuchukua bastora na kuifunga kiwambo cha kuzuia sauti na kuichomeka kwenye suruali ya jensi na kuvaa vazi lake analolitumia kwenye matukio kama yale.

Alitoka kwa haraka kabla Kinape hajarudi, kwa vile kutoka kwake mpaka kwenye daraja la Nyakabungo hakukuwa mbali hakuitaji kutumia gari alitembea kwa miguu kwa mwendo wa haraka kumuwahi Anko Jay Jay.

Njiani kila gari lililokuja mbele yake na kumuulika na taa aligeuka na kulipa mgongo mpaka lilipopita. Aliliona gari lao dogo na kujua Kinape ndiyo anarudi lazima angemtafuta. Alichepua mwendo hadi karibu ya daraja na kumuona Anko Jay Jay akija kwa mbele akipepesa macho huku simu ikiwa sikioni.

Kilole hakutaka kupoteza muda kwa vile alikuwa kwenye giza alitoa bastora yake na kumlenga kifuani na kuachia risasi mbili zilizomrusha Anko Jay Jay chini ya daraja. Kwa haraka aligeuka na kurudi alipotoka.

Wakati anafanya kitendo kile mlinzi mmoja aliyekuwa kwenye nyumba zilizokuwa upande wa shule ya sekondari ya Lake aliona. Kwa vile alikuwa kwenye kiza aliona tukio lile ambalo lilimshtua lakini alikaa kimya kihofia uhai wake.

Kilole baada ya kutimiza dhamila yake alirudi nyumbani, alipofika alizificha nguo kwa nje na kuelekea kwenye Bar ya karibu na kununua chips mayai kisha alirudi nyumbani. Kinape aliyefika kitambo na kushangaa kutomkuta mpenzi wake. Alipoingia chumbani alimkuta mtoto amelala kitu kile kilimuonesha hayupo mbali.

Alitulia kwenye kochi akiwa na hasira kwa Kilole, alijikuta akipata kigagaziko cha kumuuliza usiku ule. Alipanga kujifanya ametoka kutembea ili asijue chochote. Baada ya nusu saa Kilole alirudi na chipsi kwenye mfuko.

“Vipi baby umerudi zamani?”

“Kiasi, vipi ulifuata chipsi?”

“Ndiyo mpenzi, ulifika mbali?’

“Si sana.”

“Karibu chipsi.”

“Sijisikii kula mpenzi naomba nikapumzike,” Kinape alisema huku akielekea chumbani na kumuacha Kilole akimsindikiza kwa macho.


Baada ya kupewa maelekezo ya awali na taarifa kutoka Dar es salaam kuwa kila kitu kimekwenda vizuri anasubiliwa yeye kusafiri tu. Jioni ya siku ile walipanda ndege mpaka Dar. Waliwasili uwanja wa ndege wa J.K .Nyerere jijini Dar majira ya saa moja usiku akiongozana na Teddy pamoja na mwanaye kipenzi Rose. Walipofika walimkuta mwenyeji wao akiwa na kila kitu, mwenyeji wake alipomuona alifurahi na kumkumbatia kwa furaha asiamini kama rafiki yake yupo hai.

“Siamini…siamini Mungu mkubwa,” Bon alimkumbatia Deus kwa furaha mpaka machozi yakamtoka.

“Deus siamini naona kama ndoto yaani ninachokiona siamini,” Bon alisema huku akibubujikwa na machozi ya mshangao.

“Bon ni mitihani ya maisha ni histori ndefu.”

“Unajua siamini naona kama nimeona mzimu wako, wakati wa matatizo yako nilikuwa nje ya nchi na niliporudi nilikutana na Mr Mabina na kunieleza ukiwa gerezani ulipatwa na tatizo lililosababisha upate stroke lililosababisha ulazwe hospitali kwa muda mrefu na mara ya mwisho alikuja kukutembelea aliambiwa amefariki.

“Niliulimia sana rafiki yangu, uliponipigia simu sikuamini baada ya kunifahamisha nilifanya uliyonituma lakini hamu yangu kubwa kukuona leo. Nimefurahi sana mtu niliyelezwa alipooza sehemu mmoja na kusikia umekufa upo hai katika afya njema kweli Mungu mkubwa. Ilikuwaje maana bado naona kama ngamia kapita kwenye tundu la sindano mbele ya macho yangu.”

“Kabla ya yote kwanza nashukuru kwa kazi nzuri uliyonifanyia, naomba tusizungumze lolote niombee Mungu safari yangu nirudi salama nitakupa picha kamili.”

“Naomba hata unidokeze kidogo kwani utaniacha kama mtu aliyeota usiku alipoamka asubuhi aliyoyaona yakabakia ndotoni na si kweli.”

Deus alimdokeza kidogo lakini safari ya Italia hakumweleza anakwenda kufanya nini. Baada ya mazungumzo ya marafiki wawili waliofanya kazi pamoja kwa muda mrefu kabla Deus hajaingia kwenye matatizo walitafuta sehemu yenye tulivu kuzungumza. Deus alikuwa anaondoka usiku ule na ndege ya British Air ways saa nne usiku.

Muda mwingi walikuwa sehemu yenye mwanga hafifu ambayo ilikuwa vigumu kwa watu kuwatambua kwa urahisi. Hawakupenda kuonekana kwa ajili ya usalama wa Teddy. Majira ya saa tatu Deus kabla aliingia chumba cha wageni kujiandaa kuondoka.

Walimuomba Bon awapishe kidogo wazungumze, baada ya kusogea pembeni wapenzi wawili na mtoto wao walizungumza ya mwisho kabla ya safari.

“Sasa mpenzi naomba nikupe maelekezo ya mwisho,” Teddy alimweleza Deus.

“Sawa.”

“Ukifika katika mji wa Sicily kuna Cassino nyingi katika zote nilizokueleza, anazopenda Mose zipo mbili, ni mpenzi sana wa kucheza kamali anazozipenda ni Piedimonte San Germano na Liola Hotel (Aquino) hii Liola ndiyo yenye gharama sana na hata kamali yake ni kubwa. Kama Mose ana fedha hupendelea hoteli hii ambayo ina cassino ndani lakini akiwa ana fedha kidogo japo biashara yetu inakufanya uwe na fedha mpaka kufa, hupenda kwenda San Germano.”

“Nimekuelewa.”

“Unaweza kutembelea Cassino zingine lakini hizi huwa hakosi.”

“Kwa vile mji wa Sicily si mgeni kwangu haitanipa wakati mgumu, hii kazi ni ndogo sana kwangu.”

“Inaweza kuwa ndogo lakini jamaa wale ni wabaya kuua kwao jambo la kawaida, ukikosea mahesabu wanaweza kukupoteza.”

“Si rahisi.”

“Mpenzi mbona unajiamini sana?”

“Watu sampuli ya huyo mshenzi nimepambana nao sana.”

“Nina imani fedha uliyonayo inatosha sana.”

“Inatosha sana, hii kazi nataka kuifanya ndani ya saa 24 niwe nimemaliza kila kitu.”

“Basi nakutakia kila la heri katika safari yako.”

“Nashukuru sana, ila kama mambo yatakwenda kinyume naomba unitunzie mwanangu.”

“Bila shaka nitamlea kama mwanangu wa kumzaa, lakini sitaki ufe bado nakuhitaji baada ya maisha ya mateso nina imani tunahitaji faraja ya mioyo yetu.”

“Mwanadamu amezaliwa na kufa, hivyo hatuwezi kuepuka kufa kama tumezaliwa.”

“Ni kweli lakini Mungu atakutangulia.”

Walikumbatiana kisha alimbusu Teddy na mwanaye Rose, alimwita Bon.

“Best wacha nikajiandae na safari, shemeji yako anarudi Mwanza kesho asubuhi.”

“Hakuna tatizo nikutakie kazi njema, nakubiri kwa hamu najua una mengi ya kunieleza.”

“Tumuombe Mungu anirudishe salama.”

“Nina imani kwa dua zetu wote atakutangulia.”

“Amina.

Aliagana na wote kisha alielekea kwenye ndege kwa ajili ya safari ya kuelelea Sicily Italia.


Kinape aliamka siku ya pili akiwa mtu mwenye mawazo mengi kutokana na tabia ya Kilole kuwaua watu wake wa karibu kila kukicha. Alijiuliza hali ile itaendelea mpaka lini, kuwaua watu wasio na hatia. Akiwa sebuleni akitazama taarifa ya habari ya saa kumi na mbili asubuhi, katika taarifa ule ya habari alishtushwa na taarifa ya sikitisha ya kifo cha mtu aliyeamini kwake ni muhimu kuhusiana na kifo cha mpenzi wake Happy.

Katika taarifa ile habari moja ilimshtua baada ya mtangazaji kusema: Kijana mmoja anayefahamika kwa jina la Anko Jay Jay mkazi wa maeneo ya Mirongo jiji Mwanza, ameuawa usiku wa kuamkia siku ile kwa kupigwa risasi mbili za kifuani na mtu aliyekuwa amefunika mwili nzima.

Taarifa iliendelea kusema, mlinzi wa nyumba za jirani ndiye aliyeshuhudia mtu aliyekuwa ameuziba mwili mzima mithiri ya ninja, akimpiga risasi kijana aliyekuwa akija kwa mbele huku akiuliza kwa sauti “Uko wapi?” Bila ya kujua alikuwa akimpigia nani yule mwanamke alitoa bastora na kumpiga risasi iliyomrushia darajani kisha kugeuka kurudi alipotoka.

Taarifa iliendelea kusema:

Mlinzi baada ya kuona kitendo kile alikaa kimya kuhofia uhai wake na baada ya kuondoka muuaji alimjulisha bosi wake na kupiga simu polisi, baada ya polisi kufika waliuchukua mwili wa marehemu na kuupeleka hospitali ya Sekou Toure kwa uchunguzi zaidi.

Mkuu wa polisi aliwataadharisha watu wote kuhusiana na mauaji ya kutisha yanayoendelea nchini hasa jiji Mwanza yanayofanywa na mwanamke anayevaa vazi refu la kumficha kama ninja ambaye amekuwa tishio jijini baada ya kufanya mauaji mawili ya kufuruliza. Mkuu wa polisi amewaomba watu kutoa ushirikiano pale anapoonekana mtu wa aina hiyo ili kumtia nguvuni.

Wakati taarifa ya habari ikiendelea Kilole naye alisimama kwa muda kusikiliza taarifa za kifo cha Anko Jay Jay. Baada ya taarifa ili aliondoka kuendelea na shughuli zake. Kinape aliamini aliyefanya vile alikuwa Kilole lakini ushahidi hakuwa nao hivyo ingekuwa vigumu kumtia hatiani moja kwa moja hasa baada ya mtu aliyemtegemea kutoa ushahidi kumuua.

Alijuliza Kilole kamuua Anko Jay Jay kwa ajili gani? Aliamua kutoka nje ya nyumba akiwa na mawazo mengi sana na kujiuliza hali ile itaendelea mpaka lini. Aliamini mwisho wake angekuwa kama Deus ambaye kwake aliamini amekwisha fariki.

Akiwa anatembea taratibu kichwa chini mikono nyuma kuzunguka nyumba yao alishtuka kuona kitu kama furushi jeusi likiwa pembeni ya maua. Aliinama na kulitazama kwa kulipekua na kipande cha mti kwa kukinyanyua. Aliponyanyua alishangaa kuona bastora ukidondoka chini, aliiokota na kuichomeka kwenye bukta aliyokuwa amevaa na kuificha kwa fulana aliyovaa juu.

Alitupa kipande cha mti na kuinyanyua nguo iliyokuwa kimezungushiwa bastora na kugundua lile ni gauni lefu lenye mtandio wake na kutambaa cha kujifunika usoni na kuwa kama ninja. Kwa mara ya kwanza alipata ushahidi wa nani muuaji japo mwanzo alikisia bila kuwa na ushahidi.

Aliviangalia vitu vile na kukumbuka vitu vingi kuanzia kifo cha mchumba wake na mpenzi wake wote wenye majina ya Happy pamoja na Anko Jay Jay ambaye aliuawa muda mfupi baada wa yeye kuzungumza naye kwa mujibu wa shuhuda.

Aliishika bastora mkononi na kuitazama kwa muda hasira zilimpanda mpaka akaanza kutetemeka. Moyoni alijiapiza siku ile ndiyo ungekuwa mwisho wa kumvumilia muuaji mkubwa asiye na chembe ya huruma aliyemkosanisha na rafiki yake kipenzi Deus na kusababisha kifo chake.

Aliamini baada ya Anko Jay Jay anaweza kufuata yeye aliona dawa ni kumuwahi kabla hajawahiwa. Alibeba zile nguo mkono wa kushoto na mkono wa kulia alishikilia bastora na kuingia ndani kama askari aliyetumwa kumkamata mtuhumiwa wa mauaji.

“Kilole,” aliita kwa sauti kubwa.

Kilole aliyekuwa jikoni akiandaa maziwa ya mtoto, alipotoka alishtuka kukutana na mdomo wa bastora ukimtazama huku mkono mwingine ameshilikia nguo zake za kazi.

“Kinape vipi?” alimuuliza macho yamemtoka pima.

“Kilole kwa nini umemuua Happy?”

“Hilo jibu uliza swali,”Kilole alijibu kwa kujiamini.

“Kwa nini umemuua Anko Jay Jay?” alibadili swali.

“Alistahili kufa.”

“Kwa nini?”

“Sina jibu zaidi ya nililokujibu.”

“Kilole, umesababisha Deus kufungwa, umesababisha nimgeuke rafiki yangu umesababisha kifo chake na kumuacha Rose yatima. Umemuua mchumba wangu Happy umemuua mfanya biashara mwenzangu Happy na mwisho umemuua Anko Jay Jay.”

“Kinape kina kitu unajua unataka nikujibu nini?”

“Naomba jibu kwa nini umewaua?”

“Sina jibu, unataka kunifanya nini wakati unajua kila kitu?”

“Nataka na wewe uwafuate wenzako,” Kinape alisema huku akitetemeka na jasho kumtoka bastora kaielekeza kwa Kilole.

“Kwa hiyo unataka kuniua?”

“Lazima ufe Kilole, siwezi kuishi na mwanamke mwenye roho mbaya kama wewe.”

“Haya niue,” Kilole alisema huku akisogea mbele ya mdomo wa bastora.

Baada ya kusimama mbele ya bastora bila kufanywa jambo lolote alishika bastora na kuanza kunyang’anyana. Kila mmoja alitumia nguvu kwa Kilole kutaka kunyanyang’anya na Kinape kuing’ang’ania.

Kwa bahati mbaya katika kugombea kidole cha Kinape kilichokuwa katika kifyatulio kiliminya kifyatulio kilicho fyatuka na kusababisha risasi mbili zitoke na kumuingia mtu chini ya kifua.

“Aah!” ilikuwa sauti iliyoonesha risasi kumuingia.

Taratibu mmoja aliteremka chini huku damu zikimtoka chini ya kifua, mwingine alishtuka na kutaharuki na kumtazama mwenzake aliyekuwa ametoa macho pima huku akisema kwa sauti ya mawimbi. Alimuwahi na kumpakata huku mkono ukijitahidi kuziba sehemu zilipoingia risasi na kuufanya mkono mtote damu.

“U.u..u..me..ni..ua…,” ilikuwa sauti ya mawimbi.

“Nooo…samahani… bahati mbaya.. hu..wezi kufa,” alisema kwa sauti ya kilio ikifuatiwa na machozi.

“Na..na..kufa…ume..ni..ni..,” alisema kwa shida huku damu ikimtoka mdomoni na kuweka michirizi pembeni ya mdomo iliyoteremka mpaka kwenye mapaja ya aliyemkumbatia.

“Huwezi kufa…usife… mpenzi wangu kazi yote niliyofanya imekuwa bure.”

“Naomba Deus a..ni..ni..samehe sana, ni..ni..na imani nina deni zito kwa..kwa..a ke.”

“Jamani huu mkosi gani….Ki..Ki..Ki..,” alishindwa kumalizia jina kwa uchungu ulikuwa mkubwa moyoni.

“N.n.na..na..ku.ku.f..f.,” damu ilijaa mdomoni na sauti ilishindwa kutoka nuru ya macho ilipotea taratibu roho iliachana na mwili. Alimtikisa kwa nguvu huku akimwita jina lake lakini hakuwa na jibu macho yalikuwa yametulia kama alikuwa akimtazama lakini tayari roho iliachana na mwili.


Sauti ya tamu ya kike ya mhudumu wa ndege ya British Air ways ilimshtua Deus aliyekuwa amepitiwa na usingizi:

“Ndugu abiria wa ndege yetu ya British Air ways, ndege yetu ndiyo inakaribia kutua katika uwanja wa Sicily, tafadhali mnaombwa mfunge mikanda, tunawatakia safari njema yenye furaha, asanteni.”

Deus alifumbua macho na kuangalia saa yake ilimuonesha ni saa mbili na nusu za usiku. Alichukua mkanda wake na kujifunga kisha alitulia huku abiria wengine nao wakijifunga mkanda. Baada ya muda ndege iliteremka uwanjani na matairi kugusa rami na kutembea kwa muda kabla ya kusimama.

Deus alikuwa wa mwisho kuteremka kwenye ndege, alitoka taratibu na Brifcase yake mkononi. Baada ya kufanyiwa upekuzi alitoka nje ya uwanja wa ndege na kupokewa na dereva wa teksi.

“Habari ndugu.”

“Nzuri.”

“Karibu Sicily,” Dereva mwenye asili Kichotara alimkaribisha Deus.

“Asante.”

“Unaelekea wapi?”

“Liola Hotel (Aquino).”

“Hakuna tatizo.”

Deus aliingia kwenye gari na kuelekea mjini akilakiwa na mataa yaliyoupendesha mji wa Sicily kwa taa.

“Pole na safari?” dereva alionekana mcheshi alimsemesha Deus aliyekuwa kimya akitafakari safari yake.

“Asante.”

“Kaka wewe ni mgeni mji huu?”

“Kwa nini?” swali lile lilimfanya Deus aache kuangalia mitaa na kumtazama dereva.

“Mbona hapa jijini kuna hotel tulivu zipo pembeni ya mji karibua na upepo wa bahari unakwenda hotel ile.”

“Ni uamuzi tu, shughuli zangu huzifanyia karibu na ninapokwenda.”

“Na kweli, kuwa katika hoteli ya karibu na shughuli zako ni vizuri.”

“Nashuku kwa kulielewa hilo.”

“Umekuja kibiashara?”

“Ndiyo.”

“Biashara gani? Naweza kuwa msaada kwako.”

“Biashara yangu aihitaji msaada wa mtu.”

“Okay, nilidhani utahitaji mwenyeji.”

“Mi mwenyewe ni mwenyeji hivyo sihitaji mwenyeji mwingine.”

Wakati huo teksi ilikuwa ikikata kona kuingia Liola Hotel (Aquino), baada ya kuegesha kwenye maegesho dereva alimwambia mgeni wake.

“Nina imani tumefika salama?”

“Nashukuru.”

“Hata uendeshaji wangu nina imani umeupenda?”

“Ni kweli, wewe ni dereva mzuri.”

“Basi ndugu yangu atakapokuwa ukija hapa kwa shughuli zako usiache kunitafuta ndugu yako, kadi yangu hii hapa, naitwa Abdul.”

“Hakuna tatizo, nitakutafuta,” Deus alisema huku akipokea ile kadi ya biashara ya Dereva Abdul.

“Hakuna tatizo, vipi totoz?”

“Nikihitaji nitakutafuta.”

“Usiwe na wasiwasi sisi ndiyo wenyeji wa mji huu, ukiingia kichwa kichwa unaweza kukombwa kila kitu.”

“Hakuna tatizo.”

Baada ya kumlipa chake aliteremka kwenye gari na kuingia ndani ya hoteli na kwenda moja kwa moja mapokezi na kupokewa na msichana mrembo.

“Karibu kaka.”

“Asante.”

“Unahitaji msaada?”

“Ndiyo, nataka chumba.”

“Unataka cha juu au chini?”

“Nataka ghorofa ya pili.”

“Umepata.”

Baada ya kuandikisha mapokezi alipewa msichana aliyempeleka mpaka chumbani kwake. Baada ya kumfikisha msichana aliyempeleka alimwambia kwa sauti tamu:

“Karibu sana.”

“Asante.”

“Nina imani imeridhishwa na huduma yangu pia vyumba vyetu?”

“Ni kweli, huduma yako ni nzuri pia chumba ni vizuri sana.”

“Utahitaji huduma zaidi?”

“Kama ipi?”

“Najua usiku utakuwa mrefu sana kama ukilala peke yako, ukiniihitaji nikupe kampani nitakuwepo leo kwa ajili yako,” binti mrembo alisema kwa sauti ya wizi.

“Nashukuru, nikuhitaji nitakujulisha.”

“Naitwa Loveness na namba yangu ya simu hii piga muda wote usihofu,” yule msichana alimpa kikaratasi alichokuwa kimeandikwa namba ya simu na kumfanya Deus ajiulize ameandika muda gani ikiwa muda wote walitembea pamoja kupanda juu.

“Nashukuru,” Deus alikipokea kile kikalatasi na kumwacha yule msichana aondoke.

Baada ya kuondoka alifunga mlango na kwenda kujitupa kitandani kama mzigo macho yake yakitazama juu. Aliusikia mwili wake ulivyochoka kutokana na kusafiri saa 24 bila kupumzika. Uchovu aliousikia aliamini akijiegesha lazima atalala na yeye alitaka kazi ile aianze usiku ule. Japokuwa alikuwa amechoka sana hakutaka kupumzika

Alijinyanyua kitandani na kukaa kitako, alipoangalia saa yake ilimuonesha ni saa nne na dakika saba, baada ya kuweka mizigo yake aliteremka upande wa Cassino. Alipofika upande wa Cassino kila mtu alikuwa yupo bize na mambo yake.

Alielekea upande watu wakiokuwa wakicheza kamari huku wakinywa pombe, alizunguka taratibu kila kona bila kumuona mtu aliyemfuata. Alitulia kwa muda wa saa nzima akizunguka kila kona. Saa tano iliingia bila kumuona, alitoka hadi hotelini na kuagiza chakula kutokana na njaa aliyokuwa akiisikia.

Baada ya kula alirudi tena Cassino lakini hakumuona mtu wake, alisubiri mpaka saa sita bila dalili za kuonekana Moses. Aliamua kwenda kuoga ili amtafute Abdul ampeleke hoteli nyingine. Baada ya kuoga alimpigia simu Abdul dereva wa teksi. Baada ya siku kuita ilipokelewa:

“Haloo.” Simu ilipokelewa upande wa pili.

“Haloo mr Abdul.”

“Haloo, nani mwenzangu?” Abdul aliuliza.

“Aah! Bwana Abdul si tumeagana muda si mrefu?” Deus alishangaa kuulizwa jina, lakini alikumbuka alichukua namba ya dereva bila kumpa yake.

“Nimeagana na watu wengi, hebu nikumbushe.”

“Ndugu yangu hata sauti huijui?”

“Ooh! Mgeni wangu wa Liola Hotel (Aquino)?”

“Ndiyo.”

“Okay, unahitaji huduma gani kwa sasa?”

“Kwani una huduma ngapi?”

“Kaka si tulizungumza kama unahitaji mtoto wa kukusaidia kuuvusha usiku na usafiri.”

“Kwa sasa nahitaji usafiri.”

“Unataka kwenda wapi usiku wote huu?”

“Utajua ukifika.”

“Poa, nakuja muda si mrefu.”

Japo mwili wa ulikuwa umechoka Deus aliamini siku ile hakutakiwa kuupitisha bila kufanya kazi iliyompeleka, alikuwa radhi ya siku ile ashinde kama popo kwenye kwenye Cassino zaidi ili tu kumtafuta Moses bila kuwa na uhakika kwa kumpata kwake aliona akicheza pata potea.

Baada ya muda simu yake iliita ilikuwa namba ya Abdul, alichukua bastora yake na kuipachika kiunoni kisha aliteremka chini. Alimkuta Abdul anamsubiri alipomuona alisogeza gari karibu yake na kumfungulia mlango. Deus aliingia na kumueleza:

“Nipeleke Piedimonte San Germano.”

“Hakuna tatizo, inaonekana mzee mtu wa kujirusha, eeh?”

“Hapana kuna mtu namfuata.”

“Hakuna tatizo,” dereva alisema huku akikanyaga mafuta baada ya gari kuingia barabara kuu. Kutokana na uchache wa gari barabarani walitumia dakika kumi kufika Piedimonte San Germano. Abdul alipaki gari kwenye maegesho na kumgeukia Deus aliyeoneka anawaza kitu.

“Mheshimiwa tumefika.”

“Okay nashukuru,” Deus alijibu huku akifungua mkanda na kutoa bochi ili amlipe.

”Kiasi gani?”

“Kwani si nakusubiri au nakuacha?”

“Sijui nitachukua muda gani lakini nahitaji huduma yako kwa muda wote nitakaokuwa hapa.”

“Kwa hiyo nikusubiri?”

“Ndiyo maana yake.”

“Kumbuka kuna chaji ya kukusubiri.”

“Usihofu nitalipa.”

“Nikusibiri hapa au tuingie wote.”

“Siyo mbaya tunaweza kuingia wote.”

Walitoka ndani ya gari na kulifunga gari kwa rimoti kisha waliongozana ndani ya ukumbi. Kwa vile hakuwa mgeni wa sehemu zile alitafuta meza moja na kukaa na Abdul kisha waliagiza vinywaji. Deus alitumia nafasi ile kumuacha Abdul mara moja na kuelekea upande wa cassino.

“Mzee nakuja,” alisema huku akinyanyuka.

“Hakuna tatizo.”

“Suala la malipo usiwe na wasiwasi nitamaliza mimi.”

“Najua nipo na mtu mzito.”

Deus aliachana na Abdul na kuelekea upande cassino ambako kulikuwa kumechangamka kulikuwa na watu wengi kila mtu alikuwa bize na kucheza kamali huku akinywa pombe. Alizunguka kila sehemu bila kuiona sura ya Mose, alirudi alipokuwa amekaa Abdul akiamini sehemu ile ilikuwa ndiyo karibu na njia ya kuelekea upande wa kuchezea kamali hivyo angeweza kumuona kila aliyeingia na kutoka ndani.

Muda ulikatika bila Mose kutokea kitu kilichozidi kumchanganya na kuona njia waliyotumia kumtafuta Mose ilikuwa ya kitoto heri angemuelekeza anapoishi kuliko kumtafutia cassino. Alianza kuiona kazi inaanza kuwa ngumu, lakini hakukata tamaa aliendelea kukaa pale kuangalia waliokuwa wakiingia na kutoka.

“Mzee unaonekana haupo sawa?” Abdul alimuuliza baada ya kumfuatilia kwa muda mrefu.

“Kivipi?”

“Toka timefika unaonekana kuna kitu unakitafuta.”

“Nakuja,” Deus alisema huku akinyanyuka baada ya kumuona mtu mmoja anayefanana na Mose akipita akielekea upande wa kaunta. Kwa vile alikuwa amempa kisogo hakuwa na haraka ya kumfuata. Alimwacha asogee mbele kidogo kisha alimfuata nyuma taratibu ili amuone mtu yule anayefanana Mose anakwenda upande gani.

Alimuona amesimama kaunta na kuagiza kinywaji, hakuwa na haraka naye alimwacha mpaka atulie. Japo mtu yule alimfananisha na Mose kilichomshangaza alikuwa peke yake tofauti na maelezo ya Teddy kuwa Mose alitembea na kampani ya vijana wa kihuni.

Alimuona yule mtu akihama kwenye kaunta na kusogea sehemu ya kuchezea kamali alisogea taratibu hadi alipokuwa na kumtazama usoni kwa chati.

Alipomtaza vizuri aligundua kumbe siye mwenyewe, alijikuta akijifyonza na kurudi sehemu yake. Pamoja kuwa na Abdul mawazo yake yalikuwa mbali kila muda aliangalia saa yake ya mkono na kuuona muda ukizidi kukatika bila mhusika kutokea.

Mpango wa kumtafuta mtu kwenye Cassino aliuona wa kitoto badala ya sehemu anayoishi ambayo ingemfanya aifanye kazi ile kwa uhakika mkubwa, japokuwa Teddy alimweleza Mose ana tabia ya kujesha club kuliko kuwepo nyumbani.

Kila dakika alitupia jicho kwenye saa na kumuonesha muda unazidi kutaradadi, mishale ilimuonesha ni saa nane kasoro usiku. Alijikuta akijifyonza mwenyewe kila dakika kitu kilichomfanya Abdul kumuuliza.

“Kaka vipi mtu aliyemfuata amechelewa nini?”

“Aah! Kuna Cassino ngapi maarufu kwa kamari jijini?”

“Mmh! Zipo nyingi tofauti na ulipopanga na hapa kuna Piazza Marcom, Gari, Forum Palace na nyingine nyingi ila kati ya hizi moja utafurahi.”

“Sasa fanya hivi nirudishe mara moja hotelini ili unipeleke ya karibu.”

“Ya karibu ni Piazza Marcom.”

Walilipa vinywaji na kutoka huku moyoni Deus akianza kuona ugumu wa kazi iliyopo mbele yake, mwili nao ulikuwa umechoka kutokana na safari ya saa 24 angani. Alitamani kurudi hotelini kulala lakini hakukubaliana na hali ile. Abdul alikimbiza gari na kutumia muda mfupi kurudi hotelini.

“Niteremshie hapa wee kageuze,” Deus alimwambia Abdul aliyelisimamisha gari katikati ya barabara.

Gari lililokuwa kija mbele lilisimama na kupiga hodi, Abdul alipotaka kuliondoka gari Deus alimwambia:

“Waache wasubiri,” alisema huku akiteremka kwenye gari.

Waliokuwa kwenye gari la mbele walianza kutukana:

“Wee fala ondoa uchafu wako barabarani.”

Kauli ile ilimfanya Abdul azime gari kabisa na kumfanya Deus amshangae.

“Vipi Abdul,” Deus alimuuliza akiwa bado amesimama pembeni ya gari.

“Hawa watoto hawanijui, kuuza midawa yao ya kulevya haiwezi kuwafanya watudharau wakubwa zao.”

“Unawajua?”

“Nawajua si wazungu wa unga hawa.”

“Oyaa wee fala ondoa kopo lako, “ aliteremka kijana mmoja aliyekuwa amevaa kofia kwa kuigeuza nyuma na kupiga ngumi kwenye boneti ya gari.

“Ondoaa Ondoaaa.”

Kitendo kile kilimfanya Abdul kutoka kwenye gari na kwenda kumbeba mzimamzima na yule kijana na kwenda kumtupa kwenye gari lao. Wenzake walitoka kishari.

“Nyie paka hakuna hata mmoja anaweza kunigusa au mnataka nilipasue gari lenu?” Abdul aliyekuwa amejengeka kimazoezi akitamba mbele ya wale vijana.

“Basi brother unajua mwenzetu amelewa,” jamaa mmoja alisema huku akimvuta mwenzake aliyeoneka amekunywa kidogo.

“Mose waambie wenzako mimi nani?” Abdul aliendelea alijitapa.

Wakati Deus akisogea karibu na Abdul ili kumsaidia kwa lolote macho yake yalipata mshtuko baada ya kumuona mtu aliyekuwa akimtafuta sana. Mose aliwatuliza wenzake na kurudi ndani ya gari lao. Abdul aliingia ndani ya gari lake na kuitoa gari njiani.

Deus alipata wazo la haraka na kurudi kwenye gari na kumfanya Abdul amhoji:

“Vipi mbona umerudi?”

”Naomba tuwafuate hawa popote wanapokwenda.”

“Achana nao watatupotezewa muda.”

“Kuna kitu nataka kujua.”

“Gharama zinaongezeka.”

“Usiwe na wasiwasi wee fanya kazi fedha siyo tatizo.”

“Kama bado unayo yangu achana nao,” Abdul alisema huku akiliacha gari la kina Mose likiingia barabarani na kuondoka kwa kasi.

“Abdul utaniudhi ifuate ile gari hakikisha hulipotezi,” Deus alisema kwa sauti ya amri.

Abdul aliwasha gari na kuliondoa kwa kasi kulifukuza gari la kina Mose lililokuwa likimbizwa kwa kasi ya ajabu na kushindwa kuliona kila walivyokanyaga mafuta hakufanikiwa kuliona.

“Abdul tutawaonaje wale watu?”

“Mmh! Kwa kweli sijui, si unajua uwezo wa gari lao na langu, hata kama tungewafuata nyuma wangetuacha lile gari habari nyingine hata bei yake mbaya wananunua wazungu wa unga tu.”

“Sasa watakuwa wamekwenda wapi?” Deus alianza kuchanganyikiwa.

“Lazima watakuwa wamekwenda Piedimonte San Germano, ndiyo club iliyopo mbele,” Abdul alimtoa wasiwasi.

“Basi twende tuwawahi.”

“Kwani kuna nini? Wewe ni polisi?”

“Hapana, kuna mtu nina shida naye katika wale vijana.”

“Hakuna tatizo.”

“Yule anayeitwa Mose unamfahamu?”

“Ndiyo.”

“Anakaa wapi?”

“Kwa kweli sijui huwa tunakutana sehemu hizi.”

“Unamjua vipi Mose.”

“Mmh! Yule kijana ana historia ndefu kwanza inasadikiwa na fedha sana hata lile gari ni lake, pili ameponea tundu la sindano kwenye kinywa cha mauti. Inasemekana walidhulumiana mshiko na wenzake, si unajua wale wazungu wa unga.”

“Nani aliyemfanya vile?”

“Wengi walijua labda shemeji yake, lakini baadaye alikataa, mpaka sasa haijajulikana nani aliyemfanyia kitu kama kile, Kwa sasa imekuwa kimya hakuna tena habari zile.”

Abdul alipunguza mwendo ili akate kona kuingia Piedimonte San Germano, bahati nzuri lile gari waliliona na kwenda kupaki pembeni yake.

“Imekuwa vizuri tumewakuta,” alisema Abdul huku akizima gari.

“Kazi nzuri,” Deus alijibu huku akiteremka kwenye gari na kuelekea ndani ya Cassino haikupita muda Abdul alikuwa pembeni yake.

Walitembea kwa mwendo wa haraka mpaka ndani ya cassino.

“Abdul nisubiri hapa,” Deus alimuacha Abdul sehemu ya mwanzo na kuelekea kwenye kamali.

Alipofika alimkuta Moses akiwa ameshikilia bunda la dola mkononi akijiandaa kucheza, pembeni alikuwa na rafiki zake ambao walionekana ni wapambe wake. Kwa hali ile aliamini anaweza kukesha bila kufanya jambo lolote, ilibidi atumie akili za kuzaliwa kuweza kumtoa Mose sehemu ile kabla hajaingia kwenye kamali.

Alirudi hadi kwa Abdul aliyekuwa amekaliwa na mwanamke mmoja aliyekuwa sehemu ya mwili wake wazi na kuchezeana. Alisogea mpaka karibu ya Abdul na kuishika siraha yake kwa kuamini muda si mrefu itakuwa ama zao ama zake na damu itamwagika.

Alipoangalia saa yake ilimuonesha ni saa tisa na nusu za usiku ulikuwa umebakia muda mchache kuingia alfajiri ambayo ingemuharibia shughuli yake ya siku ile.

JIJI DAR ES SALAAM

Akiwa bado ameishikili mwili ambao aliamini kabisa ulikuwa umetengana na roho, aliutikisa tena huku akijiona kama amefanya kazi ya bure ya kubeba maji kwenye gunia. Akiwa kama mtu aliyekuwa akizungumza na mtu aliye hai kwa kuutikisa mwili usiokuwa na uhai.

“Mpenzi amka…amka mpenzi wangu…kuna faida gani ya mimi kuendelea kuishi kama wewe niliyekutegemea umekufa….Wewe ndiye aliyefanya nifanye yote haya.”

Aliukumbatia mwili wa mpenzi wake kama amempakata mtoto mdogo, machozi yake yaliangukia kwenye paji la uso wa marehemu.

“Mpenzi…bahati mbaya..Ki..Ki.. samahani… sikukusudia kukuua bahati mbaya…Eeh! Mungu kwa nini umemchukua mtu huyu wakati bado namhitaji sana.”

Wakati huo mtoto ndani alikuwa akilia kwa sauti kwani ndiyo alikuwa akiandaliwa maziwa. Aliuweka mwili chini bila kujifuta damu alikwenda chumbani na kumchukua mtoto na kumbeba akiwa na damu zake mkono. Alitoka naye hadi pembeni ya mwili wa marehemu alipiga magoti na kumweleza mwanaye ambaye alikuwa hajui chochote.

“Gift mwanangu huna tena baba tena… Baba yako amekufa.. Kinape amka umuone mtoto wako ataishije bila baba?” Kilole machozi ya majuto yalimtoka kama maji.

Gift kama alisikia alichoelezwa na mama yake, aliangua kilio kama kauguzwa moto, kila alivyombembeleza hakunyamaza. Kilole alijikuta naye akiangulia kilio akiwa bado amepiga magoti mbele mbele ya mwili wa Kinape aliyekuwa amefariki muda mrefu.

Akiwa hajui afanye nini, sauti ya mlango kugongwa ilimshtua, kwa haraka alikwenda hadi mlangoni na kufunga kwa ndani badala ya kufungua kisha alishusha mapazia yote. Aliuvuta mwili wa Kinape hadi chumbani na kutengeneza michirizi ya damu toka sebuleni hadi chumbani.

Kwa haraka alichukua dekio na ndoo ya maji ya kuanza kuifuta damu, wakati huo mlango uliendelea kugongwa na kuzidi kumuweka Kilole kwenye wakati mgumu na kujiuliza atakuwa nani. Alijikuta akipata wazo baya na kwenda chumbani kuchukua bastora ili kumzimisha anayegonga mlango moyoni aliapa hatakubali kushikwa kirahisi lazima afe na mtu.

Alipotaka kwenda kufungua mlango alisita kwanza alirudi ndani na kusafisha damu iliyokuwa kwenye zuria aliubeba mwili wa Kinape kwa shida na kuulaza kitandani kisha aliufunika shuka na kuhakikisha nguo zote zenye damu anaziweka bafuni.

Baada ya kuhakikisha hakuna damu sehemu zote alipuliza pafyumu ili kuondoa harufu ya damu mbichi. Baada ya kupulizia manukato kila kona alitoka hadi mlangoni na kufungua mlango. Lakini nje hakukuwa na mtu yeyote alizunguka nyumba lakini hakumuona.

Alirudi ndani na kujiuliza atafanya nini baada ya kumuua bila kukusudia mwanaume aliyemfanya afanye yote yale. Moyoni alitamani awatafute wote aliowaua kwa ajili ya Kinape ili awaombe msahama. Alitamani kulijua kaburi la mume wake Deus ili akamuombe msamaa kwani nguvu zote alizotumia ilikuwa kazi bure.

Wazo lililomjia lilikuwa kutafuta vijana wa wamchimbie shimo ili usiku amzike mwili na Kinape, kwa kuhofia kama akikaa sana na mwili unaweza kuharibika na kutoa harufu na kusababisha kutiliwa mashaka. Wazo lile lilimpa ujasiri na kumbeba mtoto wake na kufunga nyumba kisha alielekea kijiweni kutafuta vijana wa kumchimbia shimo ambalo ndilo litakuwa kaburi la Kinape


Nyuma ya meza kubwa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai DCI Karimu Swago aliyekuwa kimya akiisoma ripoti ya mauaji ya kutisha yaliyotokea kwa muda mfupi Jiji Mwanza na muuaji alikuwa mwanamke anayevaa vazi refu jeusi linalouziba mwili wake na kuwapa wakati mgumu jeshi la polisi kumjua ni nani.

Baada ya kuisoma alimgeukia mkuu wa upelelezi Athumani Fukwa.

“Fukwa,” alimwita huku akimkazia macho.

“Mkuu.”

“Mpaka sasa mmefikia wapi mauaji haya?”

“Mkuu kwa kweli bado tunapambana lakini bado hatujajua ni nani anayefanya mauaji haya.”

“Kwa hiyo mnataka kuniambia chombo cha dola tumeshindwa?”

“Hapana mkuu, bado tunaendelea na upelelezi.”

“Hapa naona kuna mtu anaitwa Kinape, mmesisha mtia mikononi?”

“Mkuu simu yake haipatikani.”

“Kama haipatikati mmetumia mbinu gani kumpata?”

“Mkuu bado tunaendelea na upalelezi ikiwa pamoja na kuhoji waliokuwa wapenzi wa marehemu Happy aliyeuawa Gorden Crest.”

“Mmh! Na kuhusu familia ya Anko JayJay inasemaje?”

“Kwa kweli hawajui lolote kutokana na marehemu kufanya mambo yake kivyakevyake bila kumshirikisha mtu yeyote.”

“Alikuwa akifanya kazi gani?”

“Wanamwita martpapas.”

“Wana maana gani?”

“Hakuwa anachagua kazi kila kazi uliyokuja mbele yake aliifanya.”

“Hakuwa na rafiki wa kike?”

“Hilo tuliuliza, tuliambiwa hakuwa na mwanamke mmoja hivyo ilikuwa vigumu kumjua nani aliyekuwa akijua habari zake kwa siku ile.”

“Mliwatafuta na kuwahoji?”

“Ndiyo,tuliwapata wachache, wote walisema walikuwa na muda mrefu bila kumtia machoni.”

“Hana mtu wake wa karibu?”

“Yupo lakini inaonesha aliondoka siku tatu kabla ya kifo cha Anko Jayjay.”

“Alikuwa na umuhimu wa kumuhoji, inawezekana kuna vitu anavijua vinaweza kutusaidia kupata mwanga.”

“Hakuna tatizo mkuu tulimueleza tukiwa na shida naye tutamtafuta.”

“Basi atafutwe mara moja nataka jioni nipate jibu mmefikia wapi, haiwezekani tuchezewe kiasi hiki tumekaa kimya. Hamjui tunaiabisha sifa ya jeshi letu makini lenye nguvu,” DCI Swago alisema kwa sauti ya amri.

“Sawa mkuu.”

“Basi naomba kazi ifanyike mara moja naamini hatujashindwa kama hamuwezi nitaingia mwenyewe mstari wa mbele.”

“Kazi itafanyika mkuu,” Mkuu wa upelelezi Fukwa alimhakikishia mkuu wake kazi itafanyika.

Baada ya kutoka kwenye kikao na mkuu wake wa kazi, Fukwa aliwaita vijana wake wa kikosi maalumu na kutoa amri ya kijeshi.

“Nina imani mmemsikia mkuu, kwa hiyo sitaki kusikia tena muuaji bado anatamba, mpaka kesho jioni nataka tuwe tumemkamata. Sijui mtamkamata vipi, hiyo si juu yangu bali kusikia yupo mikononi mwa polisi, sawa?” Mkuu wa upelelezi Fukwa.

“Sawa mkuu,” vijana aliitikia kikakamavu.

“Nina imani mmepata pa kuanzia?”

“Ndiyo mkuu.”

“Haya tawanyika mkimkosa na ninyi msirudi hapa.”

Ilikuwa kauli iliyowapa wakati mgumu kikosi cha kazi kinachodili na mtukio kama yale. Walikubaliana kutawanyika huku kila mmoja akijipa jukumu lake ili wakikutana wajue wamefika wapi.


Kachero Mzengwa alitembea taratibu maeneo ya Mirongo kwa kupita katika vijiwe vya Anko Jay Jay. Kwa vile alikuwa katika vazi la kawaida alifika kwenye uwanja wa mpira wa shule ya Mirongo na kuwakuta vijana wakicheza kamali huku wakivuta bangi hakufanya kitu na yeye alijichanganya.

Na yeye aligongea sigara ya kawaida na kuvuta huku akifuatilia kamari.

Mara alisikia jamaa mmoja akisema:

“Washikaji tumempoteza mwanetu Jay kama utani,” jamaa aliyekuwa akivuta bangi alisema.

“Mmh! Unajua naye alizidi kila kazi alifanya unakumbuka Tom nilimweleza Jay kwa kazi yake ya ukuwadi ipo siku atakufa. Jamani Jay kufa kwa risasi kama siyo kumkuwadia mume wa mtu ni nini?” mwingine aliongezea huku akilamba lizila unyonge bangi.

“Na kweli jamaa alizidi, mi nilijua mwisho wake mbaya.”

“Tena Side bahati yake alikwenda bushi la sivyo na yeye angekufa.”

Wakiwa katikati ya mazungumzo alitokea jamaa mmoja na wote waligeuka na aliyekuwa akinyonga alisema:

“Sideeee wapi Jay, jichanganye na wewe utamfuata mwenzako, fanya kazi zote lakini ya ukuwadi ni kifo.”

“Mwambie, hivi wewe mkeo akikuwadiwa utajisikiaje?”

“Jamani mbona umekosa ya kuzungumza, naona kijiwe hakinifai nikajichanganye na masela wa Lake sekondary,” Side alisema huku akiondoka taratibu na kuwaacha jamaa wakiendelea kumpaka mbovu.

“Side kuondoka siyo dawa, kama utafanya kazi ya rafiki yako nawe si muda mrefu utamfuata.”

“Ninyi mnajuaje kama kauawa na mke wa mtu?” Side alisimama na kuuliza.

“Side hata kama mimi siyo mpelelezi lakini ukiangalia mauaji yalivyotokea picha nzima inaonesha kauawa mwanamke aliyekuwa nyumba ya wageni. Hata siku mbili hazijapita kauawa Jay tena na mtu wa aina moja mwanamke anayevaa vazi refu la kumziba mwili na uso.

“Huyo mwanamke lazima amegundua yule mwanamke aliyemuua hotelini anatembea na mumewe na mtengeneza mipango ni Jay na yeye kumuua. Sasa nawe jipendekeze moto ukuwakie sisi siyo wajinga kukomaa na kazi za upusha, tunapenda maisha mazuri lakini mwisho wake kufa kama jambazi.” Jamaa mmoja aliyekuwa akisema kwa sauti nzito huku akinyonga ganja.

Machero Mzengwa alijikuta akipata kitu kipya ambacho hakuwahi kukiwaza, alichosema jamaa aliyekuwa akinyonga ganja. Japo alifurahi kumuona Side mtu muhimu kwake lakini pia alipata mwanga mwingine ambao aliamini utamsaidia atakapozungumza na Side. Alimpigia simu dereva wa defenda ili apate usafiri wa kuondoka na Side.

“Poa, lakini mnanionea bure,” Side alizidi kujitetea.

“Tukuonee vipi ikiwa wewe na Jay mlikuwa mnatutenga na kutuona sisi sio kwa vile mnakamata fedha ya ukuwadi.”

Mara ghafla kulizuka ugomvi baada kudhulumiana kwenye kamali, ile ilimpa nafasi kachero kumfuata Side aliyekuwa amesimama pembeni na kumsalimia.

“Side vipi?”

‘Poa mkubwa.”

“Sasa Side tuzungumze kidogo.”

Walisogea pembeni kidogo ili wazungumze, ghafla lilitokea defenda na kuwafanya waliokuwa wakicheza kamali na kuvuta bangi kukimbia. Side naye alitaka kukimbia lakini alishikwa na kachero Mzengwa na kushindwa kukimbia.

“Vipi Brother?” alilalamika ili aachiwe.

“Tulia,” Kachero Mzengwa alisema kwa sauti ya amri.

Baada ya gari kusimama Side alipakiwa na gari lililokwenda moja kwa moja hadi kituo cha makosa ya jinai. Waliteremka na kuingia naye kwenye chumba cha mahojiano. Kwa vile Side alikuwa na wasiwasi sana kachero Mzengwa alimuagizia soda ya baridi kwanza. Baada ya kutulia alianza kumuhoji.

“Side ondoa wasiwasi hutafanywa kosa lolote ila nahitaji msaada wako,” Mzengwa alianza kwa kumtoa wasiwasi.

“Msaada gani?”

“Anko Jay Jay alikuwa nani yako?”

“Rafiki yangu sana.”

“Kabla ya wewe kwenda shamba alikuwa na dili gani?”

“Mmh! Nakumbuka alipewa kazi na dada mmoja ya kumfuatilia mume wake.”

“Mume wake alikuwa na tatizo gani?”

“Alikuwa na wasiwasi anatembea na mwanamke mwingine.”

“Mmh! Baada ya hapo nini kiliendelea?”

“Aliniambia amegundua kweli yule mwanaume alikuwa na mwanamke kampangia hotelini.”

“Baada ya hapo?”

“Alipomaliza kazi yake alilipwa chake na mimi kesho yake nilisafiri, nikiwa bushi nilipopata taarifa za kushtusha kuwa mchizi wangu Jay ameuawa,” Side alisema kwa uchungu.

“Unakumbuka huyo mwanamke alikuwa amepangiwa hoteli gani?”

“Gorden Crest.”

“Na hiyo mwanamke unamjua?”

“Kwa kweli sikuwahi kumuona.”

“Sehemu anapokaa unapajua?”

“Ni Isamilo lakini nyumba siikumbuki vizuri kwa vile tulikwenda usiku ila nakumbuka nilimsubiri sehemu na kuingia kwenye nyumba yenye geti.”

“Hukumbuki hata kidogo?”

“Nikifika nitaijua japo sikuangalia vizuri siku tuliyokwenda.”

“Nafikiri twende muda huu ukatuoneshe hiyo nyumba.”

“Sawa.”

Walikubaliana kwenda kuitafuta nyumba ya mwanamke aliyempa kazi Anko Jay Jay ambayo waliamini anaweza kuhusika kwa asilimia kubwa katika mauaji yale.


Majira ya saa kumi na mbili za jioni Land Cruser ilitembea taratibu katika mitaa ya Isamilo. Walilipaki sehemu na kuteremka kisha kutembea taratibu kufuata mtaa ambao Side alikuja siku moja na marehemu Anko Jay Jay kufuata malipo ya kazi aliyopewa ya kumchunguza mume wa mtu.

Sehemu aliposimama kumsubiri ilimchanganya kidogo kutokana na nyumba zile kufanana kidogo katika nyumba aliyoingia Jay.

“Vipi umeikumbuka?” kachero Mzengwa alimuuliza.

“Kati ya nyumba hizi mbali moja wapo, sikumbuki nilisimama wapi kwa vile ilikuwa usiku.”

“Joe unasemaje?” Mzegwa alimuuliza mwenzake.

Kabla hajamjibu lilikuja gari na kusimama kwenye nyumba moja kati ya zile mbili na kupiga honi. Baada ya muda alitoka mama mmoja mwenye mwili mkubwa kufungua geti huku akisema:

“Mume wangu leo nimekuwa mlinzi.”

“Mlinzi yupo wapi?”

“Nimemtuma mara moja.”

Baada ya kufungua geti gari lilingia ndani na kulifunga, baada ya kufungwa geti Side alisema:

“Itakuwa nyumba hii.” aliionesha nyumba jirani na gari lilipoingia gari.

“Kwa nini?”

“Jay alinieleza yule mwanamke anaishi na mume na mtoto mchanga hii inaonekana wenye nyumba ni watu wazima pia nyumba ile alinieleza haina mlinzi.”

“Una uhakika?”

“Ndiyo ni nyumba hii.”

“Basi tuondokeni tukajiandae kuja usiku nina imani kazi itakuwa si ngumu sana.”

“Na huyu?” Joe aliuliza kuhusu Side.

“Huyu tutakuwa naye mpaka zoezi la leo usiku liishe kisha atarudi kwake.”

Walirudi kwenye gari lao na kurudi ofisini kwa ajili ya operesheni ya kumtia mikono Kilole ambaye waliamini ndiye aliyekuwa akijua kila kitu juu ya kifo cha msichana aliyeuawa Gorden Crest na Anko Jay Jay japokuwa hawakujua muuaji ni nani, lakini waliamini kumtia mikononi yule mwanamke angewasaidia upelezi wao kwa kiasi kikubwa.


Deus baada ya kuikagua siraha yake alisogea mpaka karibu ya dereva teksi Abdul aliyekuwa amezama kwenye penzi na mwanamke wa usiku.

“Mzee vipi?” Deus alimshtua Abdul.

“Poa mkuu.”

“Naona upo kazini?”

“Hapana nimemwita huyu baada ya kuona maboweka.”

“Njoo basi nje mara moja.”

Walitoka mpaka nje pamoja hadi ya cassino.

“Vipi mzee?” Abdul alimuuliza Deus akimtazama usoni.

“Mose unafahamiana naye sana?”

“Kiasi ila tunaelewana sana.”

“Kuna kazi nataka kukupa ukiifanya vizuri nitakupa fedha nzuri.”

“Kazi gani mkubwa?”

“Nina shida Mose ila nataka ukamtoe bila wapambe wake kuja nina mazungumzo naye.”

“Hilo mbona dogo.”

“Lakini usimwambie kama kuna mtu anamwita.”

“Hiyo kazi niachie mimi, akili yangu ukisikia fedha huwa haishindwi na kitu chochote hata kumfukua marehemu.”

“Basi nifanyie hiyo kazi mara moja, ila ukija hakikisha wewe unasimama huku na yeye huku.”

“Hakuna tatizo bosi wangu.”

Abdul aliingia ndani mara moja hadi kwenye meza za kamali na kumkuta Mose bado kashikilia bunda la dola akisubiri kuingia kucheza kamali.

“Mose,” Abdul alimwita alipomkaribia.

“Unasemaje Brother Abby?”

“Samahani nakuomba mara moja.”

“Una shiga gani brother? Zungumza nakusikiliza.”

“Naomba tutoke nje mara moja.”

“Si unajua muda wangu wa kuingia kwenye gemu umekaribia, jana walinila leo nina usongo nao,” Mose alijitetea ili asiende mbali.

“Dakika tano tu, waachie washikaji wakushikie unarudi sasa hivi.”

“Paul shika mkwanja huu narudi.”

“Poa mkubwa.”

Walitoka hadi sehemu ya kupakia magari, Deus alipomuona anakuja alizunguka nyuma ya gari. Walichomoa bastora tayari kwa tukio, walipofika walisimama Mose akiwa amempa mgongo Deus kama alivyomuelekeza Abdul. Aliiweka bastora yake tayari na kumsogelea taratibu hadi waliposimama na kumwekea bastora Mose kisogoni huku akisema kwa sauti ya chini yenye amri.

“Fungua mlango wa mbele wa gari na uingie ndani bila kuleta ujanja la sivyo nitakufumua ubongo.”

“Mheshimiwa vipi?” Abdul alishtuka kuona Deus ameshikilia bastora.

“Sitaki swali nawe ingia upande wako mara moja.”

Abdul hakutaka kubishana alizunguka upande wake na kuingia ndani na Mose naye alifanya kama alivyoelekezwa. Deus aliingia mlango wa nyuma na kusema kwa sauti ya amri.

“Elekea baharini mara moja.”

“Sawa,” Abdul alijibu huku akiwasha gari na kuondoka.

“Kaka mkubwa nimefanya nini?” Mose aliuliza kwa sauti ya upole.

“Utajua muda si mrefu.”

Gari lilitoka hoteli ya Piedimonte San Germano na kuingia barabara kubwa na kuelekea upande wa baharini.

“Abdul nataka gari likimbie kama linapaa,” Deus alitoa amri ya kijeshi.

“Hakuna tatizo mkubwa.”

Abdul alibadili gia na kukanyaga mafuta na kulifanya gari liondoke kwa mwendo wa kasi. Kabla ya kulivuka daraja refu gari la kina Mose lilikuja nyuma kwa kasi na kuwavuka na kusimama mbele yao kwa ghafla na kumfanya Abdul kufunga bleki kwa nguvu zote. Lakini gari lao liliseleleka na kwenda kuligonga gari la kina Mose wakati huo wapambe wa Mose walikuwa wametoka ndani ya gari na bastora mkononi tayari kumsaidia bosi wao.

Deus akili ilimchemka na kuona kafanya makosa ya kutoka naye mbali sana, lakini aliamini atapambana nao mpaka tone la mwisho la damu yake japokuwa alikuwa peke yake akipambana na kundi la zaidi ya watu sita wote wana siraha.

Deus naye kwa wepesi wake alitoka nje na kujificha nyuma ya teksi ya Abdul ambaye alikuwa hajui afanye nini. Wapambe walikuwa amekwisha ivamia gari na kumtoa bosi wao. Jamaa aliyetupwa juu ya gari na Abdul naye aliona ile ndiyo sehemu ya kulipa kisasi kwa Abdul.

Bila kuuliza alimjaza Abdul risasi za kichwa mpaka alipoamini amekata roho na kichwa hakitamaniki.

“Jamani mbaya wetu asikimbie,” Mose alisema kwa sauti ya juu.

“Hatoki lazima tumtie mikononi.”

“Nataka tusimuue tumshike akiwa hai,” Mose alitoa amri wa wapambe wake.

“Huyu hatoki hapa.” Ilikuwa kauli ya kumuunga mkono Mose ambaye alikuwa na hasira na Deus.

Deus aliinama kwa chini ili asionekane, wakati huo risasi zilikuwa zikirindima sehemu aliyojificha naye alijitahidi kujihami kwa kurudisha mashambulizi. Risasi ya bega iliyompata Deus ilimfanya adondoshe bastora chini. Alipotaka kuiokota kwa mkono cha kushoto alikuwa amechelewa teke zito lilitua usoni kwake na kumrudisha nyuma.

Hakutaka kufa kikondoo alipambana kiume kwa kutumia mkono mmoja na mateke. Alijitahidi kuwadhibiti huku Mose akiendelea kuwakataza wenzake kutotumia siraha ili kumkamata akiwa hai.

“Jamani tusimuue lazima tujue nani kamtuma,” Mose alipaza sauti.

“Bosi usiwe na wasi atalegea muda si mrefu.”

Kauli ile ilimpa nguvu Deus ya kuendelea kupambana huku akishangaa ujasiri wa Mose wa kuwakataza wenzake wasitumie siraha na kuendelea kupambana kwa mikono. Kitu kizito kilichompiga Deus kisogoni kilimpoteza fahamu na kuanguka chini kama mzoga.

Mose na vijana wake kwa haraka alimchukua Deus na kumweka kwenye gari lao na kuelekea naye baharini.

“Mkuu wapi hii?” mmoja wa wapambe wake aliuliza.

“Huyu lazima tukamhoji bahari baada ya kupata ukweli tunamuua na kumtupia majini ili kuondoa ushahidi, pia inatakiwa usiku huu tuondoke Sicily twende Torino kwa muda ili sakata ili lipite lazima watatulitilia mashaka kwa vile gari letu linaweza kuonekana kwenye kamera zao.”

“Hakuna tatizo.”

Walimbeba Deus kuelekea ufukweni kwa ajili ya kumhoji na kumuulia mbali.


Kilole baada ya kufanikiwa kuwapata vijana waliomchimbia shimo nyuma ya nyumba. Aliwalipa ujira wao na kusubiri muda wa usiku auzike mwili wa mpenzi wake Kinape aliyemuua kwa bahati mbaya wakati wakigombea bastora.

Akiwa amesimama kwenye uzio kwa ndani aliona watu wakielekezana nyumba yake, ile ilimtisha sana na kuona bwawa linaweza kuingia luba.

Mapigo ya moyo wakiwa yana mwenda mbio alitulia akiwachungulia awaone wanataka kufanya nini.

Baada ya muda aliwaona wakiondoka, alijikuta akijiuliza watu wale walikuwa na shida gani. Baada ya kuondoka alirudi ndani na kutafuta pombe kali na kunywa ili kupunguza maumivu ya moyo baada ya kumuua mtu muhimu maishani mwake.

Majira ya saa tatu na nusu usiku Kilole alitoka mpaka nje ya geti kuangalia hali ya hewa ambayo ilikuwa tulivu. Aliamini hakukuwa na mtu aliyekuwa akimtilia mashaka alirudi hadi ndani na kwenda moja kwa moja chumbani na kuufunga vizuri mwili wa mpenzi wake katika shuka ambao ulikuwa amepoa na kuanza kukauka.

Aliuvilingisha shuka kisha aliuvuta mpaka chini na kuanza kuburuza kuupeleka nje kwenye shimo. Aliuburuza mwili hadi nje na kupumua kidogo kutokana na uzito wa mwili wa mpenzi wake. Alijifuta jasho kwa mkono kisha aliendelea kuuvuta mpaka karibu na shimo ili autumbukize na kuufukia.

“Hapo hapo… Upo chini ya ulinzi,” Sauti kali ya amri ilimshtua Kilole na kumfanya adondoke chini kwa hofu.

Alipoangalia aliwaona watu zaidi ya wanne wakiwa na silaha mkononi.

“Unafanya nini?” sauti kali ilimuuliza.

“Si.si..si..” Kilole aliingiwa kigugumizi huku haja ndogo ikimtoka kwa hofu.

“Unaburuza nini?”

“Jamani bahati mbaya sikukusudia.”

“Hukusudia nini?”

“Jose mbona kama mtu huyu?” Kachero Mzengwa aliuliza baada ya kuuona kilichokuwa kikiburuzwa kilikuwa kama mtu.

Wakitumia tochi kukichunguza kilichokuwa kikiburuzwa na Kilole, askari aliyeimana kuangalia alisema kwa sauti ya juu.

“Ha! Mtu?”

“Eti?” walishtuka.

“Bwana we, mwili wa mtu huu.”

“We mwanamke unaupeleka wapi huu mwili?”

“Samahanini jamani…ba..ba..ha..”

“Huyu nani?”

“Mu.mu..mu..me ..wa..wa..ng…”

Presha ya Kilole alikuwa kubwa sana kiasi cha kumfanya aishiwe nguvu na kupoteza fahamu. Walimpatia huduma ya kwanza lakini haikusaidia waliteuliwa askari wawili kumuwahisha Kilole hospitali ya Seko Toure katika ulinzi mkali.

Kabla ya kuupeleka mwili wa marehemu hospitali walifanya upekuzi kila kona ya nyumba ile. Ndani ya nyumba waligundua vitu vingi vikiwemo vifaa vya Kilole vya kufanyia mauaji. Pia bastora na risasi vyote vilivyokutwa ndani. Baada ya kukamilisha upekuzi walimchukua mtoto wa Kilole aliyekuwa amelala hajui lolote ili kumpeleka kwa mama yake.

Mwili wa marehemu waliupeleka hospitali ya Seko Toure kwa ajili ya uchungu kabla ya kufanya taratibu zote za kuwatafuta ndugu wa marehemu. Baada ya taratibu zote walimpeleka mtoto kwa mama yake wadini, walimkuta Kilole ameamka akiwa amejilaza mkono wake mmoja ukiwa na pingu iliyofungwa kwenye kitanda alicholala.

Aligeuka na kuwangalia askari na mtoto wake na kujikuta akiangua kilio, mtoto wake naye aliamka na kuanza kulia ilibidi anyanyuke na kunyonyesha ili anyamaze.


Deus alipepesa macho kuangalia sehemu aliyokuwepo alishtuka na kujiuliza pale alikuwa akiota au kweli. Alirudisha kumbukumbu kilimtokea mara ya mwisho ni kweli huku akijipapasa, mkono wake ulitua kwenye bega la mkono wa kulia na kukutana bandeji.

Alizidi kushtuka aligeuza shingo taratibu na kukutana na tabasamu pana.

“Pole mpenzi,” sauti tamu ya Teddy ilitua kwenye ngoma za masikio ya Deus.

“Teddy!” Deus alimwita akiwa bado anajipapasa.

“Abee mpenzi.”

“Ninachokiona mbele yangu ni kweli au naota?”

“Huoti mpenzi ni kweli mpenzi.”

“Hapana hii ni ndoto tu,” alisema huku akirudisha mkono kwenye bandeji na kuanza kukandamiza kwa nguvu. Lakini Teddy aliwahi kumshika mkono.

“Deus unataka kufanya nini?”

“Teddy hii ni ndoto tu.”

Alipoangalia pembeni alimuona mwanaye kipenzi Rose akiwa amelala usingizi, alizidi kujishangaa.

“Hapa ni wapi?”

“Ndani ya ndege,” Teddy alimjibu huku akimshika mkono aliouondoa kwenye jereha na kuanza kuupapasa taratibu.

“Ndani ya ndege! Tunatoka wapi na tunakwenda wapi?”

“Tunatoka Italia na tunarudi Tanzania.”

“Hapana…Hapana hii ni ndoto si kweli,” Deus alizidi kukataa.

“Kwa nini mpenzi?”

“Teddy nimekuacha Tanzania umefikaje Italia na umewezaje kuniokoa kwenye kinywa cha mauti?”

“Ni historia ndefu naomba kwanza tufike nyumbani, la muhimu mshukuru bwana Mungu wako kwa kukuwezesha kuendelea kuvuta pumzi yake mpaka muda huu.”

Pamoja na kuelezwa yote bado Deus aliamini ile ni ndoto kutokana na hali aliyokutananayo ya kuwa ndani ya kinywa cha mauti. Pamoja na kuamini ile ni ndoto lakini bado hakujua yupo wapi japokuwa ndoto ilimuonesha yupo sehemu salama.

Teddy aliamini kabisa Deus yupo katika wakati mgumu kuamini kilichomkuta na sehemu aliyokuwepo ilibidi amrudishe katika hali ya kawaida.

“Deus,” alimwita kwa sauti ya chini huku akitembeza mkono yake kichwani kwa Deus aliyekutana na joto la kumsisimua.

Deus hakuitika japo alisikia akiitwa aligeuza shingo na kumtazama Teddy aliyekuwa amekaa pembeni yake akitembeza mikono yake taratibu.

“Deus, najua ni vigumu kuamini hali iliyokutokea na sehemu uliyopo sasa ndiyo inakuchanganya sana.”

“Hapana Teddy si hicho.”

“Nini sasa kinachokufanya usiamini kama ni kweli?”

“Mimi na wewe tumeachana lini?”

“Juzi usiku.”

“Wapi?”

“Dar.”

“Ukijiandaa kwenda wapi?”

“Mwanza.”

“Huoni kuwa mbele yangu ni ndoto usiyokubalika?” Deus alisema akiwa amemkazia macho.

“Deus mpenzi wangu, najua hicho ndicho kinacho kutatiza, ni kweli uliniacha Dar lakini sikwenda Mwanza kama nilivyo kuahidi bali nilikufuata Italy.”

“Muongo!”

“Kweli mpenzi wangu, sema tu tumeomdoka ndege tofauti ya Italy mimi ndiye niliyewahi saa moja kabla yako niliondoka na ndege ya Fly Emirates.”

“Teddy mi si mtoto mdogo wa kudanganywa namna hiyo, Italy si sawa na kutoka Ubungo kwenda Kariakoo, kuna maandalizi yake hasa kutoka nje ya nchi kuna taratibu zake si za saa zaidi siku nzima hata siku mbili.”

“Ndiyo maana nikakueleza ni historia ndefu, moyo wangu haukukubali kukuamini moja kwa moja uende peke yako. Nilichowaza ndicho kilichotokea bila kufanya hivyo lazima ungekufa na mimi kusakwa mpaka kukamatwa kisha kuuawa kifo kibaya sana namjua vizuri sana Mose ana roho mbaya sana.”

“Mmh! Bado siamini.”

“Kweli Deus moyo wangu ulikataa kukuacha peke yako kwa vile namjua vizuri Mose. Nilijua kama ningekueleza tuongozane ungekataa hivyo nilifanya mipango yangu kwa siri bila wewe kujua ulipofika Italy nilikufuatilia kila hatua.”

“Uliwezaje kuniokoa katika kundi la vijana hatari kama wale?” Deus alikubaliana na hali halisi ilibidi awe mpole.

“Kwa vile niliwahi kufika Italy nilisubiri wageni watakaoingia na ndege uliyopanda na kuweza kukuona. Kabla sijaja niliwasiliana na mtu mmoja katika kampuni ya magari ya kukodi aniandalie gari atakalo liweka uwanja wa ndege na kunieleza lipo sehemu gani.

“Nilipofika nililikuta aliponielekeza likiwa katika hali nzuri, nililikagua na kukuta lipo kama nilivyoitaka. Huwezi kuamini nilikuwa tayari kwa lolote niliamini kama sikufa mimi basi Mose.”

“Na Rose?”

“Rose nilimuacha Hotelini.”

“Hoteli gani?”

“Liola Hotel (Aquino.”

“Muongo si ndiyo hoteli niliyopanga mimi?”

“Nilibahatisha kati ya hoteli mbili, niliamini utapumzika lakini sikukuamini bado nilikufuatilia kwa kukaa mapokezi. Ulipotoka nilikufuatilia mpaka

Piedimonte San Germano bila wewe kujua. Hata uliporudi bado nikuwa na wewe mpaka mlipokutana na Mose na kundi lake bila wewe kumjua Mose haraka .

“Ilionekana ulimtambua na baada ya kashikashi ndogo mliachana nao kisha niliona mkiwafuata hapo ndipo nilipojua shughuli imeanza. Mpaka unamteka Mose na kuondoka naye niliamini umefanikiwa lakini kuna mpambe mmoja aliona mchezo ule na kuwafuata wenzake ndani.

“Hapo ndipo nilipojua kazi imeiva, niliwaacha watangulie nami niliwafuata nyuma huku moyoni nikijiapia ama zao ama zangu. Nikiwa kwa mbali niliona mchezo mzima. Lazima nikusifu wewe ni mwanaume wa shoka mpaka kukushinda walitumia nguvu ya ziada.

“Sikuweza kuingilia mapigano yenu baada ya kuanguka moyo uliniuma sana mpaka machozi ya uchungu yalinitoka nikajua wamekumaliza. Walipo kuchukua na kuondoka na wewe sikujua wanakupeleka wapi, niliwafuatilia na kuwaona wanakupeleka ufukweni.

“ Kwa vile sehemu ilikuwa ya uwazi niliwaacha niwaone wanaenda wapi. Nilipowaona wamesimama niliamua kuwafuata kwa kuingia ndani ya maji.

“Namshukuru Mungu nilikuwa mtundu toka nilipoingia kwenye kazi hii ya hatari. Niliogelea hadi karibu yao na kutokeza kwa taratibu na kuwaona wanakumwagia maji uamke. Nilitumia nafasi ile kuwaua wote kwa risasi kisha nilitoka na kukuta hujafa ila una jeraha la risasi begani.

“Nilitumia gari lao kukubeba mpaka nilipopaki langu na kukuhamishia kwenye gari langu. Nilikupeleka kwa daktari wangu ambaye alikushughulikia na kusema huna tatizo kubwa zaidi ya jeraha tu. Nilitaka nisafiri naye mpaka Tanzania lakini alisema hakuna sababu ya yeye kusafiri na sisi kwa vile huna tatizo kubwa sana.

“Kwa vile nilijua kimenuka sikuwa na jinsi ilibidi nikodi ndege kwa gharama kubwa sana ili kuhakikisha usiku uleule tunaondoka Italy. Nilimfuata Rose hotelini na kuondoka mpaka uwanja wa ndege kisha tukaondoka. Hivi ninavyozungumza tuna saa sita tupo angani toka tutoke Italy.”

“Kwa hiyo Mose umemuua?”

“Yeye ndiye wa kwanza nilimpiga risasi tatu za kichwa kisha wenzake. Yaani hakuna siku niliyofurahi kama leo,” Teddy alisema kwa furaha huku akiubusu mkono wa Deus aliyekuwa bado amegandisha macho kwake.

Imauhakika gani kama Moses amekufa?”

“Baada ya kutoka ndani ya maji nilichukua bastora yake iliyokuwa na risasi kumi na kukisambaratisha kichwa chake kama atakuwa mazima tena basi nitajua ni mzimu.”

“Kwa hiyo kazi yangu imekuwa ya kitoto?” Deus aliuliza kiunyonge.

“Hapana mpenzi, kazi uliyofanya wewe ilikuwa kubwa sana mimi nimemalizia tu, nisingeweza kupambana na mijitu kama ile ambayo umeitoa jasho.”

“Unafikiri kwa nini Mose hakutaka kuniua?”

“Nina imani alitaka kujua umetoka wapi na nani kakutuma, anaamini mtu wa pale hawezi kumfanyia kitendo kama kile.”

“Baada ya kunihoji nini kingefuata?”

“Baada ya kupata ukweli wangekuua na kukutupia baharini.”

“Nashukuru sana Teddy kuyaokoa maisha yangu.”

“Nikushukuru wewe mpenzi kwa kuyatoa maisha yako kwa ajili yangu, Deus sijawahi kuona mwanaume mwenye mapenzi mazito na mimi kama wewe umekubali kuyatoa maisha yako kwa ajili yangu, umekubali kupoteza kazi yako kwa ajili yangu. Sina cha kukulipa zaidi ya kukuahidi upendo wa dhati na maisha mazuri mpaka kufa kwako, nife unizike ufe nikuzike.”

“Nashukuru kwa kulitambua hilo, ila nami nina kazi yangu.”

“Ipi?”

“Ya kumsaka Kilole na Kinape.”

“Nitakusaidia mpenzi wangu mpaka tuwatie mkononi na hakuna hukumu nyingine zaidi ya kifo.”

Ndege iliingia Dar es salaam Tanzania majira ya saa tano usiku, Deus alichukuliwa na kupelekwa kwenye moja ya jumba lililokuwa likitumiwa na kikundi cha wauza dawa za kulevya ambalo lilikuwa lipo mikononi mwa Teddy ambalo alilikimbia kumkimbia Mose lakini baada ya kumuua hakuwa na wasiwasi tena na lilikuwa kwenye hali nzuri.

Alimpigia simu daktari wao ambaye alifika kumhudumia Deus aliyekuwa na jeraha ambalo lililonekana lipo katika hali nzuri hakutakiwa kupewa huduma zaidi alitakiwa kupumzika.

Siku ya pili Deus wakiwa sebuleni amejilaza kwenye sofa akiangalia tivii taarifa ya habari ya saa sita mchana. Deus alishtuka kumuona Kilole akiwa anatoka mahakamani chini ya ulinzi. Macho yalimtoka kumuona mbaya wake akiwa mikononi mwa chombo cha dola.

Alijikuta akinyanyuka na kukaa kitako huku macho yakemtoka pima, mtangazaji alisema kesi ile itaendelea tarehe iliyopangwa kufikishwa tena mahakamani kusikizwa kesi yake ya mauaji ya watu wa tatu. Mwanamke mmoja aliyekuwa akifanya kazi katika kampuni za kitalii mkoani Arusha aliyefahamika kwa jina la Happy pia mvulana mmoja aliyekuwa akifanya kazi za misheni tauni aliyefahamika kwa jina maarufu Anko JayJay pia mwanaume mwingine aliyefahamika kwa jina la Kinape ambaye inasadikiwa alikuwa mumewe wote aliwaua kwa risasi.

“Vipi mbona unaoneka umeshtuka na kukaa kitako wakati nimekueleza hutakiwi kuimana kwa mbele?” Teddy alimuuliza Deus baada ya kutoka chumbani na kumkuta amekaa kitako tofauti na alivyomuacha akiwa amejilaza.

“Aisee Kilole,” Deus alijibu kama anatoka usingizini.

“Kafanya nini?”

“Kumbe alikimbilia Mwanza, ameua.”

“Ameua?”

“Ndiyo, yupo mikononi mwa polisi ana kesi ya mauaji ya watu watatu.”

“Mauaji?”

“Ndiyo, ha..ha..rafu kuna jina sijaelewa vizuri sijui nimesikia vibaya.”

“Jina gani?”

“La Kinape.”

“Limefanya nini?”

“Ameuawa na Kilole.”

“Utani huo, si ndiye aliyeondoka naye kamuua kwa kosa gani?”

“Kwa kweli sijui kitu ila katika majina ya watu aliyowaua nimesikia jina kama hilo lazima atakuwa yeye kwa vile wamesema ni mume wake.”

“Kesi ipo wapi?”

“Mwanza.”

“Umesema imeahirishwa mpaka lini?” wakati huo Teddy alikuwa akimlaza Deus kwenye sofa taratibu asimtoneshe jeraha.

“Hata najua baada ya kuiona picha ya Kilole nimechanganyikiwa.”

“Kwa vile umejua yupo Mwanza kazi hiyo niachie mimi.”

“Hapana tusimuue nzi kwa nyundo wakati kajifia mwenyewe.”

“Kwa nini unasema hivyo?”

“Yule yupo chini ya mikono ya dola pia kesi yake ni nzito lazima atanyongwa kwa nini tutumie nguvu tukikosea mahesabu tuanze kukimbia upya.”

“Deus watu wale hawaaminiki anaweza kupona kimaajabu na kuanza kutusumbua. Nitamuua kwa mahesabu makali sana hakuna mtu atakayejua. Japokuwa najua kakuumiza lakini ndiye chanzo cha matatizo yote yako na yangu.”

“Mpenzi hebu kwanza tuiache mahakama ifanye kazi yake kisha tutajua tufanye nini?”

“Kwa hiyo tarehe ya kufikishwa mahakamani huijui?”

“Itabidi uulizie Mwanza.”

“Hakuna tatizo,” Teddy alisema huku akichukua simu na kupiga sehemu aliyokuwa amepanga.

“Haloo.”

“Haloo Juma mambo vipi?”

“Poa sister.”

“Eti Juma kuna mwanamke anashtakiwa kwa makosa ya mauaji hapo jijini?”

“Ndiyo dada, leo alipandishwa kuzimbani kwa mara ya kwanza.”

“Tarehe ya kurudi unaijua?”

“Mmh! Hebu subiri nikuulizie usikate simu.”

“Hakuta natatizo,” Teddy alisubiri baada ya muda sauti upande wa pili ilisema.

“Mpaka tarehe 22 ya mwezi ujao.”

“Asante.”

“Upo wapi dada?”

“Nipo Dar.”

“Utarudi lini?”

“Nitakujulisha.”

Teddy alikata simu na kumueleza Deus tarehe ya Kilole kupandishwa tena kizimbani.

“Nina imani mpaka siku hiyo nitakuwa nimepona.”

“Kwa hiyo tutakuwa mahakamani siku hiyo?”

“Itakuwa vizuri.”


Siku ya kupandishwa tena kizimbani Kilole ilifika, mahakama ilikuwa imejaa kusikiliza kesi ya mauaji yaliyotikisa jiji la Mwanza mwanamke mwenye vazi refu jeusi. Deus, Teddy na mtoto wao Rose walikuwa miongoni mwa watu waliokuwepo mahakamani pale.

Baada ya hakimu kuingia na kukaa kwenye kiti chake na watu wote waliokuwa wamesimama kuelezwa wakae chini mahakama ilianza. Kesi ilianza mara moja kwa kuitwa kesi ya kwanza ilikuwa ya uchomaji wa nyumba na kusababisha mauaji ya mtu mmoja na uhalibifu wa mali.

Mtuhumiwa alisomewa shtaka na kurudishwa rumande bila kujibu kitu. Kesi ya pili kutajwa ilikuwa ya Kilole. Kama kawaida alitoka rumande na kupandishwa kizimbani. Alipanda taratibu akiwa ameinama huku moyoni akijutia kitendo cha kuua mpenzi wake Kinape bila kukusudia.

Baada ya kupanda alisimama na kutulia kusubiri kusomewa mashtaka. Akiwa ameangalia chini kusubiri kusomewa mashtaka yake kwa mara ya pili, kwa vile hakutakiwa kujibu lolote mpaka upelelezi utakapokamilika alitulia kusubiri kusomewa ili arudishwe rumande.

Akiwa ameangalia chini alinyanyua macho yake taratibu na kuwaangalia watu waliokuwa mahakamani. Macho yake yalipogongana na Deus, alishtuka na kuyarudisha tena sura ilikuwa ileile ya Deus mtu anayejua amekwisha kufa.

Aliyatuliza macho yake huku mapigo ya moyo wakienda kwa kasi, alijiuliza anaota au ni kweli.

Akili yake anajua Deus aliisha kufa yule aliyesimama mbele yake ni mzimu wake au nani. Kingine kilichomchanganya zaidi kilikuwa mwanamke aliyekuwa amekaa naye ambaye alikuwa akimkisia ni mpenzi wa Deus, alikuwa pembeni yake na mtoto wake Rose.

Pale ndipo alipoamini yule ni Deus ambaye alidanganywa amekufa kumbe alikuwa hai. Hata alipoanza kusomewa mashtaka akili haikuwa pale yote ilikuwa kwa Deus na kujiuliza ni kweli au yupo ndotoni. Alijaribu kujifinya alihisi maumivu na kugundua si ndoto ni kitu cha kweli.

Moyoni alijiapiza kwa vile alijua kesi ile hawezi kupona lazima atanyongwa kutokana na ushahidi wote aliamini ile ndiyo nafasi ya pekee ya kutimiza azima yake ya kumuua Deus. Alimuangalia askari aliyekuwa pembeni yake ametulia akiangalia watu.

Alipoangalia kiunoni kwake aliiona bastora amekaa kihasarahasara. Alipiga hesabu zake na kuamini ataipata na kufanya mauaji ya mwisho mulemule mahakamani kabla ya hukumu yake ya kunyongwa. Baada hesabu zake kukamilika alichomoka kama mshale na kumpiga kikumbo askari mpaka chini na kuipokonya bastora iliyokuwa kiunoni.

Kwa wepesi wa ajabu aligeukia upande alipokuwa amekaa watu waliokuwa wamekaa watu sehemu yaliyokuwepo wabaya wake. Deus na Teddy kwa pamoja waliliona tukio lile na wote kulala chini, watu wengine nao wamelala chini kuhofia kupigwa risasi. Kuchanganyikana na watu ilimpa Kilole wakati mgumu kuwapiga risasi wabaya wake.

Kwa hasira alipiga risasi mfululiza eneo waliokuwepo na kuua watu ovyo na wengine kuwajeruhi. Askari aliyepigwa kikumbo na kunyang’wa bastora, alinyanyuka kishujaa baada ya Kilole kumpa mgongo. Alimvaa na kuanguka naye chini.

Kwa wepesi wake aligeuza batora na kumpiga yule askari kifuani.

Hali ya mahakamani ikawa tafrani kila mmoja alishikilia roho yake kutokana na milio ya risasi.

Teddy akiwa amejilaza alitoa bastora kwa siri na kumlenga Kilole sehemu ya kichwa ili ammalize kabisa. Wakati huo Deus alikuwa ameisha muona Teddy anataka kufanya nini, kabla hajafyatua alimsukuma kwa miguu na risasi aliyopiga Teddy ilimkosa Kilole na kwenda kupiga ukutani.

Wakati huo askari wa kikosi maalumu walikuwa amefika kwa vile Kilole alikuwa amepagawa askari mwenye shabaha alimpiga risasi ya bega aliloshika bastora na kuidondosha na kuwapa nafasi ya kumvamie. Kilole aliyekuwa akitokwa na damu begani huku akipiga kelele wamuue kabisa aliwekwa chini ya ulinzi mkali.

Askari walisaidia kuondoa maiti za watu watatu na askari mmoja na majeruhi zaidi ya ishirini. Mahakama haikuweza kuendelea ilibidi iahilishwe kutokana na tukio lile zito. Wakiwa nje ya mahakama baada ya kukamatwa Kilole na kuwekwa chini ya ulinzi mkali.

Teddy alimlaumu Deus kumkanyaga wakati alijua ile ndiyo ilikuwa nafasi ya kumuua mbaya wao bila tatizo.

“Deus umefanya nini?”

“Hapana, haikuwa na haja kulipa baya kwa baya.”

“Deusiiii! Angetuua huoni kama alitukusudia?”

“Ni kweli lakini bado siamini natakiwa kumhukumu kifo.”

“Kwa nini Deus?”

“Kesi aliyonayo bado ni hukumu nzito kumbuka kaua watu wengi na leo ameongeza kosa lingine la kuua watu wengine mahakamani.”

“Deus hayo hayaniingii akilini, tulikubaliana tumfanye nini?” Teddy alimuuliza huku machozi yakimtoka.

“Teddy unanipenda?” Deus alimuuliza akiwa akimkazia macho.

“Tena sana mpenzi wangu wewe kwangu ni kila kitu.”

“Basi nakuomba nisikilize mimi, tuachane na Kilole nina imani nisingefurahi kumuona anakufa mbele yangu. Sitakiwi kuwa na roho ya kisasi kwa vile Rose ni mwanangu mtoto wa Kilole.”

“Lakini si alikusudia kuua?”

“Ni kweli, tushukuru Mungu tumepona.”

Kilole alipelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu ya jeraha la bega kisha hospitali ya wagonjwa wa akili ili kupimwa akili. Baada ya matibabu na vipimo vyote Kilole alikutwa akili yake ipo timamu hivyo alipandishwa tena kizimbani baada ya kupona jeraha katika ulinzi mkali. Kesi yake haikuchelewa alihukumiwa jela maisha na kazi ngumu.

Teddy alioana na Deus na kuwa mke na mume Rose alilelewa na Teddy ambaye tayari aliishajua ndiye mama yake wa kumzaa huku akisubiri wa kwake kuongeza familia. Waliamua kuhamishia maisha yao Mwanza na kufungua miradi na Teddy kuachana na biashara ya dawa za kulevya.

MWISHO

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment