Mkono wa Jasusi Sehemu ya Tatu
KIJASUSI

Ep 03: Mkono wa Jasusi

SIMULIZI Mkono wa Jasusi
Mkono wa Jasusi Sehemu ya Tatu

IMEANDIKWA NA: RICHARD MWAMBE


Simulizi: Mkono Wa Jasusi

Sehemu ya Tatu (3)

“Yes!” akatamka kwa sauti ya chini, akachomoa vitu vya kusikilizia na kupachika sikioni, akatikisa kichwa baada ya kuona anapata mazungumzo yao kwa ubora wa hali yajuu, huku wakati mwingine akitumia saa yake kupata picha zao japo kwa mbali, na ile sauti ikijirekodi kwenye chombo maalum ndani ya gari yake aliyoiacha porini.

“Tunataka tujue hasa mazingira yaliyopelekea vifo vya watu hao,” moja ya sauti ya kike iliuliza na Amata aliipata sawia kabisa kupitia kile chombo chake.

“Walikosa hewa, maana mitambo ya kuingiza oksijeni kule chini ilizima ghafla kutokana na hitilafu ya umeme,” sauti ya Yule kiongozi ilisikika ikijibu. Baada mazungumzo mafupi ambayo licha ya kuyasikiliza, Amata alikuwa akiandika kwenye kijitabu kidogo, aliwaona wakiingia kwenye kijichumba ambacho kwake alielewa haraka kuwa ni lifti ambayo ingewapeleka chini. Kutoka pale alipojificha kulikuwa na umbali ambao hasingeweza kuvuka kiurahisi kwani camera za usalama zilitanda kila mahali, alijaribu kutazama jinsi zilivyowekwa na wapi zinaangalia, jinsi walivyozifunga, kwa haraka haraka aligundua ubora wa kamera hizo, infrared camera zinazoweza kuona kwa umbali wa futi 100 kwenye giza nene. Akili ilimzunguka, alitamani Chiba awepo, ‘kwa vyovyote angejua jinsi ya kuzibloku japo kwa sekunde kumi tu, name ningeweza kupita eneo hili,’ alijiwazia na kulaumu kwa kutojiandaa kwa hilo.

Ile lifti ikateremka chini lakini kitu ambacho Kamanda Amata bado alifurahi ni ile hali ya kuendelea kupata majadiliano ijapikuwa kwa mbali lakini aliweza kuelewa kinachoongelewa. Alitamani kama naye pia angekuwa huko chini ili aone mazingira hayo.

“Kwa hiyo hapa ndipo walipofia?” sauti Fulani ikauliza.

“Ndiyo, ni hapa, kama unavyoona kuna mashine maalum ya kuingiza hewa, sasa hii ilizimika ghafla,” Yule kiongozi akajibu.

“Poleni sana, kwa nini mlikuwa hamuitengenezi hii mashine wakati mnajua umuhimu wake kwa maisha ya binadamu? Bi Lereti, mgodi wako umeua mara tatu mfululizo”.

Kamanda Amata akashtuka kusikia jina hilo, Lereti? Akajiuliza huku akishindwa kujua kama ninLereti huyo huyo au kuna mwingine, alikosa jibu. Akaendelea kusikiliza mazungumzo hayo mpaka alipojua kuwa watu hao sasa wanarudi juu, akajitega vyema kuangalia kama yupo Lereti anayemjua yeye. Ile lifti ilijitokeza juu, na ule ujumbe wote uliteremka, Amata akainua darubini yake ndogo ya jicho moja na kumtazama mmoja baada ya mwingine.

Waoooh! Lereti Khumalo, akajiwazia alipomfikia mwanamke huyo aliyeliweka umbo lake vyema katika vazi alilovaa.

§§§§§

Katika msegesho ya magari waligundua mwili wa askari aliyevuliwa nguo, ikawa kizaazaa. Msako dhidi ya Amata ukaanza katika eneo lote la mgodi, askari wenye mbwa walihaha kujua ni wapi alipoenda mtu huyo lakini ilikuwa ngumu kung’amua, kila walipojaribu mbwa alishindwa kujua harufu ya hasa amtakaye.

Taarifa ikafika kwa viongozi wa mgodi, nao wakaamuru mtu huyo asakwe popote alipo ndani ya mgodi huo, ilikuwa kizaazaa.

Kamanda Amata bado akili yake ilikuwa ikimfikiria Lereti baada ya kuhakikisha ni yeye anayemuona, mwanamke aliyekuwa naye miaka mitano nyuma kitandani, na kutomuona tena sasa alikuwa mbele yake. Lereti Khumalo, Ok! Akajiridhisha baada ya kufikiri hili na lile juu ya mwanamke Yule. Akajitoa katika ficho lake na kuambaa na ukuta uleule aliojia ambao alihakikisha kuwa camera za usalama hazimuoni kirahisi, akapita na kutokea kwenye ghala kubwa lililohifadhiwa vitu mbalimbali ikiwamo mitambo ya uchimbaji madini. Akajificha kwenye moja ya kasha kubwa ambalo ndani yake kulikuwa na mkorokoro anuai, akatulia kusikiliza kinachoendelea. Nje yake alisikia mibwako ya mbwa na watu waliokuwa wakiongea Kiingereza, akajua anatafutwa, akatoa kijichupa chake kidogo chenye manukato akajipulizia juu ya nguo alizovaa kisha akatulia. Wale jamaa wenye mbwa walifika hadi kwenye lile kasha lakini mbwa hakuweza kuitambua harufu ngeni isipokuwa alilewa kwa ile harufu ya manukato, wakapita na kuondoka.

CHUMBA CHA MAWASILIANO

“Nahisi kuna mwingiliano wa frikwensia hapa!” kijana mmoja aliyekuwa amevalia headphone kubwa kichwani mwake huku akicheza na kompyuta yake huku na kule alimwambia mwenzake aliyekuwa akinywa kahawa.

“Unasema? Hebu washa hiyo mashine hapo tuyasome hayo mawimbi,”

Wakawasha luninga nyingine ambayo iliweza kuonesha mwendo wa mawimbi ya mawasiliano kutoka katika mitambo yao, hapo wakaona kweli kuna aina mpya ya mawimbi ya mawasiliano ya sauti inayoingilia kati ya mawimbi yao. Wakaendelea kutafuta frekwensia gani mawimbi hayo yanapita wakati huo wakasambaza taarifa kwa vitengo vya usalama na kazi ya kutafuta chanzo cha mawimbi hayo ikaanza ilahali ile ya kutafuta mtu aliyefanya mauaji ya askari mmoja kule nje chini ya lori ikaendelea.

CHUMBA CHA MKUTANO

Baada ya wakaguzi wale kumaliza shughuli yao kule chini na kurudi katika chumba cha mkutano waliketi kufanya majadiliano ya mwisho, ndipo alipoingia kijana mmoja ndani ya huo ukumbi na kumnong’oneza kitu mmoja wa wadau wa juu kabisa wa mgodi huo juu ya taarifa za kuwapo mtu au aina ya mnaso wa mawasiliano yao. Baada ya kuongea kwa sekunde kadhaa aliondoka na kuacha kikao kiendelee.

“Wajumbe mnisamehe, hatuwezi kuongea chochote kwa kuwa inaonekana mazungumzo yetu yananaswa mahala Fulani, hivyo kwanza ukaguzi unaendelea kisha mtapewa taarifa nyingine,” alipowapa ujumbe huo watu waote wakaonekana jutahayari. Lereti nalisimama kitini na kutoka kwenda kuzungumza na Yule mtu alkiyetoa ujumbe huo, kisha wote wakaelekea chumba cha mawasiliano kuangalia hali hiyo, kweli walikuta aina Fulani ya frekwensia mpya katika mtandao wao.

Lereti alimeza mate, akashindwa kuelewa kinachoendelea.

“Nina wasiwasi na wageni wetu, sidhani kama wamekuja kwa mema? Lereti au kuna jambo unalolifanya kwa siri?” Yule wakili wa mbia wake akamwuliza.

“Usitake nikutukane, kwanza kabisa ninyi mnanihujumu sana katika hii biashara halafu unataka kunambia nini!” Lereti akaongea kwa jazba. Wakati wakibishana hivyo mara yale mawimbi ya mnaso wa sauti yakapotea na yakabaki yale ya kawaida tu.

§§§§§

Kikao kilihitimishwa kwa mabishano makali sana ndani ya chumba kile juu ya vifo vile na chanzo chake, Kamanda Amata kutoka pale alipoa aliendelea kunasa mazungumzo hayo kwa kugeuza frekwensia za chombo chake mara kwa mara ili kuwasumbua. Alipojiridhisha na kazi yake akafurahi sana. Mara hiyo hiyo akasikia sauti za watu wakiongea ndani ya ghala hilo, akachungulia kupitia uwazi mdogo aliouacha na kuona wale watu wakiunganisha vitu kama vitoroli na mbele yao kulikuwa na lokomotivu ndogo, akawasubiri wamalize kazi yao, walipokiwasha chombo chao kuondoka, naye akajitoa na kukimbia huku akiwa ameinama mpaka kwenye kile kitoroli cha nyuma akadandia na kuingia ndani yake.

Dakika tano walikuwa nje ya ghala, na kutokea eneo kubwa la kutupa taka taka kulikuwa na kitu kama shimo lililojazwa makorokoro mbalimbali.

Yasiyo na kazi, vile vitiroli vikasimama na kujibinua kumwaga taka na makorokoro mengine mengi, Kamanda Amata akajirusha na kutua pembeni lakini si mbali na lile shimo, akaangalia kila kinachomwagwa na baadae wale jamaa wakaondoka. Amata akabaki peke yake katika lile eneo la taka, harufu iliyokuwa hapo ilikuwa nzito na kali, alilijua hilo baada ya kuona wale jamaa wakiwa wamevaa barakoa katika nyuso zao. Akatoa kifaa maalum cha kumkinga dhidi ya gesi hatarisgi akakivaa usoni mwake, katika kuondoka eneo lile ndipo alipoona kitu ambacho hakukitegemea…

HIKI KILIMVUTIA, KISIMAMISHA AKILI YAKE, taratibu akasogea eneo lile hatarishi akainama na kuihakikisha akionacho, mtungi wa gesi ya Carbon Monoxide uliowekwa nembo tu ya (CO) ambayo kama hujasoma mambo ya Kemia huwezi kujua. Akautazama ukiwa umelala katikati ya takataka, akaupiga picha kutumia saa yake ya mkononi.

“Inaweza kuwa wametumia gesi hii kutekeleza mauaji?” akajiuliza kwa sauti ndogo ya kujisikia peke yake, akaondoka eneo lile taratibu lakini kumbe hakujua kuwa hata kule aliweza kuonekana kwa kamera zenye nguvu zilizofungwa upande huo kwa siri. Akiwa anatoka kwenye lile korongo lililojaa takataka akakutwa amezingirwa na watu kama kumi wenye silaha, hakujua wamefika muda gani.

“Wewe ni nani?” mmoja aliyekuwa hana silaha yoyote aliuliza, “Au nikuulize unatafuta nini huku, hujui hili ni eneo hatarishi?”

Amata hakujibu alibaki akiwaangalia tu.

“Na hizi nguo umezipata wapi? Shiiit, mkamateni twende naye, huyu ndiye aliyeua askari wetu,” yle kiongozi akatoa amri, kamanda Amata akakamatwa akapikiwa kwenye kijigari kidogo kisha wakarudi nae kule mgodini.

HOTELI YA MICHELANGELO – Johannesburg

DON ANGELO akamwangalia Jesca Gen aliyesimama mbele yake akiwa chini ya uangalizi wa vijana wawili wenye miraba mine. Katika hoteli hiyo kubwa ya Michelangelo, Don Angelo alikuwa akimiliki casino kubwa ya kisasa ambayo wateja wake walikuwa ni wazungu tu, hakuruhusiwa mtu mweusi kuingia humo na endapo angethubutu basi kifo kilikuwa dhahiri shahiri kwake. Ndani ya casino hiyo kulikuwa na watu wanaojulikana kwa kunywa damu ya binadamu, watu wenye meno kama ya Chui au Simba, huitwa Vampaya.

Don Angelo alisimama akamsogelea Jesca, akamtazama kwa jicho kali.

“We mwanamke! Jana umefanya nini? Unathubutu kujenga uhusiano na mbwa mweusi?” Don akauliza, Jesca akabaki kimya.

“Hunijibu? Umekuwa jeuri ee! Isitoshe ukalala naye kwenye eneo ambalo mbwa weusi hawaingii, unatutafuta nini Jesca?” Don akaongea kwa ukali huku akimgusa gusa kwa fimbo yake begani,

“Yule ni nani?” akamwuliza.

“Mr. Spark!” Jesca akajibu.

“Mr. Spark …” Don akaongea kwa kubana pua, akirudia jina lile,

“Mr. Spark, ndivyo alivyokudanganya, hukujua kama umelala na jasusi hatari kutoka Tanzania? Na bila shaka umetoa siri zetu nyingi,” akambwagia mapicha mbalimbali ya Kamanda Amata mezani na maelezo juu yake, “Huyu ndiye Mr. Spark wako, ukamvulia na nguo kwenye nyumba yako ukampa kila kitu kisha ukamtorosha, sasa uniambie yuko wapi?” Don akang’aka, kisha akarudi na kuketi kwenye kiti chake huku akivuta kibweta chake chenye madawa ya kulevya, akakiweka puani na kuvuta mfululizo.

Jesca alizitazama zile picha na maelezo yaliyokuwa kwenye karatasi juu ya kamanda Amata, yakimweleza kuwa ni Mpelelezi namba moja kutoka Tanzania anayeongoza idara ya Ujasusi ya nchi hiyo, kazi zake nyingi zimeishangaza Afrika na mashirika ya Kimataifa hasa katika kutatua migogoro mizito kwa siri na kupambana na watu hatari na wengi wao kuwaua. Jesca akashusha pumzi akaanza kutetemeka akimwangalia Don Angelo.

“Huna maisha mwanamke, una saa nne tu za upendeleo kisha maisha yako nitayatwaa kwa jinsi usiyoielewa, uhai wako utabaki tu ukinambia huyo bwana wako unayemwita Spark yuko wapi, ondoka!” akamwambia kwa ukali, Jesca akaondoka katika nyumba hiyo ya kifahari iliyojengwa ndani ya hoteli hiyo kubwa.

“Mumwangalie kila anakokwenda mpaka nitakapowaamuru kumuua, damu yake itakuwa kinywaji chetu leo hii,” Don akazungumza peke yake kwa sauti lakini kundi kubwa la watu wa aina yake walimsikia vyema kutoka kona mbalimbali za jengo lile.

Jesca akatoka nje ya ile casino mpaka nje kabisa ya hoteli na kutoka katika eneo hilo, akavuka barabara kubwa na kuingia kwenye mgahawa wa Kwazulu Natal, akaketi na kuitisha kinywaji, akatulia na kunywa taratibu huku kichwa chake kikijawa na mawazo mengi juu ya ujumbe aliopewa. Jessca alijuta sana kwa mkutano wake na Amata usiku iliyopita lakini kilichomuumiza zaidi ni kuwa hakujua hata mwanaume huyo kaondoka saa ngapi ndani ya nyumba yake na akaelekea wapi, bahati mbaya hata mawasiliano na mtu huyo hakuwa nayo, kashehe. Jesca alimaliza kinywaji chake na kuuacha huo mgahawa, akiwa karibu na kituo cha tax akasita kupanda, ndani ya gari hiyo kulikuwa na mtu mmoja zaidi ya dereva.

“Oh, sorry, nitachukua ya nyuma,” akamwambia Yule dereva, lakini mtu wa nyuma akakenua meno yake ya kutisha na bastola ikiwa mkononi mwake.

“Panda twende!” akamwambia. Jesca akatzama huku na kule akaisogelea ile tax kisha aktimua mbio kutoka pale. Yule mtu akashuka na bastola mkononi, akaanza kumtimua Jesca, Jesca hakuangalia usalama wake, aliingia barabarani kuvuka, ilikuwa ni barabara kubwa inayopita kila aina ya magari, akavuka barabara ya kwanza na kusimama kidogo kwenye mstari kisha akavuka ya pili. Honi za magari zilisikika katika eneo lile, Yule mtu naye akaingia barabarani kumfuata Jesca, akiwa katikati ya barabara kishindo kikubwa kikasikika, lori kubwa likamgonga Yule mtu na kumkanyaga, Jesca hakusimama, alikimbia upande wa pili na kutoweka.

Watu walijaa wakitazama mtu huyo, polisi nao walifika na kuondoa mwili ule haraka baada ya kupima ile ajali, dakika kumi na tano baadae hali ikawa shwari eneo lile.

§§§§§

Kamanda Amata alifikishwa kwenye jingo maalum lililokuwa nyuma kidogo ya yale maghala ya mgodini, akafungiwa humo, kilikuwa chumba kikubwa lakini ndani yake hakikuwa na kitu chochote kile, akatulia na kutazama hapa na pale ili kujua nini cha kufanya, wakati huohuo akasikia ule mlango ukifunguliwa na jopo la watu kama wane hivi wakaingia ndani, kati ya watu hao alikuwamo Lereti Khumalo.

Kamanda Amata akamtazama mwanamke huyo, kwa haraka haraka akaisoma hali yake na kumwona kuwa mtu mwenye mawazo mengi na wasiwasi wa jambo Fulani, akamtazama kijana mwingine mnene aliyekuwa jirani yake, aliyevalia suti safi nyeusi, mzungu mwenye nywele ndefu nyeusi zilizomwagika mabegani, askari watatu, wawili wenye silaha na mmoja hakuwa na silaha yoyote, alimtambua kwani ndiye aliyekuwa akitoa amri ya kukamwatwa kwa kwake kule kwenye takataka.

Amata alisimama kuwatazama, nao wakamtazama, hakuna aliyeongea kati yao. Lereti akamwangalia Amata, hakuweza kumtambua kutokana na jinsi alivyochafuka na mava zi yale aliyovaa ambayo yalikuwa ya palepale.

“Wewe ni nani?” Yule kijana wa kizungu akauliza.

“Mr. Spark,” Amata akajibu. Kutoka aliposimama akauona mshtuko wa wazi wa Yule kijana wa kizungu baada ya kutaja jina hilo.

“Nafikiri tumepata kuonana mahali?” Yule kijana akauliza.

“Labda tulionana kabla sijazaliwa au kuzimu,” Amata akajibu.

“Hivi nani unajua ni nani unayemjibu?” akauliza.

“Kibaraka tu wa bwana wake asiyemjua,” Amata akajibu kijeuri.

“Inaonekana wewe ni kijana jeuri tangu kuzaliwa kwako, sasa dawa ya mtu jeuri mimi ndiyo ninaijua na sasa nitakupatia, huwezi kulete vurugu kwenye mgodi wangu halafu ukajifanya wewe ni jeuri,” akamwambia. Lereti aliposikia sentensi hiyo akageuka na kumtazama Yule kijana ilibaki kidogo amzabe kofi.

“Acha kujisifu, huu ni mgodi wa huyo Madam hapo, na nimekuja kuhakikisha unarudi mikononi mwake ama kwa maji au kwa damu,” Amata akajibu. Lereti akamtazama Amata lakini bado hakumjua, kwa maneno hayo aliyoyasikia, tabasamu likachanua katika uzo wake wa kuvutia. Yule kijana wa kizungu akampiga begani Yule askari kiongozi. Yule askari kiongozi akajua nini anapaswa kutenda akajiweka vizuri na kumsogele Amata.

“Wewe, usiwe kibaraka wa watu weupe, heshimu Uafrika wako, ni upumbavu na utumwa kuwakandamiza weusi wenzako hata kuwaua kwa manufaa ya hao weupe,” Kamanda akamwambia huku akiwa kasimama bila kujitikisa.

“Hata unitukane wewe lazima nikutie adabu, kikaragosi wewe,” akajigamba.

“Kabla hujanitia adabu utaonja raha ya Akhera kwa masaa kadhaa,” wakati Amata akisema hayo Yule jamaa akamjia kama mbogo, Kamanda Amata akamuepa na kumpiga pigo moja la karate lililotua sawia sehemu ya nyuma ya shingo, Yule jamaa alipitiliza kwa pigo lile na kujibamiza uso ukutani, kabla hajatulia, Amata akaruka hewani na kumsindikiza na teke linguine, akawaona wale askari wengeni wakiweka sawa bunduki zao tayari kufyatua, akamdaka Yule jamaa na kumgeuza upande wapili kisha yeye akaruka sarakasi na kuwatawanya wale askari ka mateke ya hewani. Zile risasi zikamraru Yule askari kiongozi akajibwaga chini kwa kishindo kama gunia la mpunga hana uhai. Wale askari walianguka kila mmoja upande wake, Yule mzungu akabaki kakodoa macho, yote hayo yalitukia ndani ya sekunde tano tu na Amata hakuwapo ndani ya kile chumba.

King’ora cha hatari kikapigwa kila kona ikawa mshike mshike wa kumsaka Kamanda Amata, akapita ndani ya ghala linguine na kupanda kwenye makasha mpaka juu kabisa ambako kulikuwa na uwazi wa mtu kuweza kupenya, akachungulia na kuona chini kuna lundo la mchanga, Mungu mkubwa! Akajiseme na kujirusha juu ya uke mchanga, akaseleleka nao mpaka chini. Alipofika chini tu kuna gari kubwa ilikuwa ikipita upande huo, akaiwahi na kuidandia katika mlango wa dereva, akaufyatua na kumvuta nje kisha akaukalia usukani…

Walinzi walijipanga kumzuia kwa kuvurumisha risasi upande wa mbele na kwenye magurudumu ya lile lori lakini Kamanda Amata alikuwa akiliendesha kwa kasi na kuliyumbisha huku na kule. Wale walinzi walijitahidi kuzuia kwa kuingia barabarani lakina Amata hakusimama alipita na wote wakaruka pembeni huku bunduki zao zikianguka kando. King’ola cha hatari kiliendelea na mshikemshike ulikuwa sio mdogo, akalielekea geti kuu la kutokea mahalia pale, bado risasi zilivurumishwa nyuma yake, na baadhi ya magari yalionekana kuingia barabarani ili kumfukuza kumkamata. Walinzi wa geti wakalifunga geti hilo lachuma kwa minajiri ya kumzuia haikuwa rahisi kwani alikuwa akija kasi. Wale walinzi walimlenga kwa bunduki, akaona hakuna namna.

“Sikutaka kuwaua lakini tutaona la kufanya”, akajisemea huku akichomoa bastola yake na kulenga shabaha madhubuti, risasi ya kwanza ilimpiga pajani Yule mlinzi akaanguka kando nay a pili ilimpata wa upande mwingine begani akadondoka juu ya lundo la magunia ya mchanga. Kamanda Amata aliligonga geti na kutoka nje ya wigo wa mgodi huo na kuendelea na safari huku nyuma akifukuzwa na magari makubwa kwa madogo. Bado risasi zililindima naye alikuwa akishuhudia vioo vya gari yake vikitawanyika, akaamua kuwanyia unyama.

“Hawanijui kama mi Kamanda, ngoja sasa,” akatazama huku na kule akaona kitu kama mfuko uliokuwa na vitu ndani akauvuta kwa mkono wake, ulikuwa na uzito wa kama kilo kumi hivi akaunyayua na kuuweka juu ya akseleleta na kuhakikisha sasa lile lori linaweza kwenda peke yake, akafungua mlango na kujirusha nje kwa namna ambayo hasingeweza kuumia, akatua kwenye nyasi na kujibingirisha vichakani, akajificha na kutazama kinachoendelea. Kwa kuwa alifanya kitendo hicho kwenye kona ya tao hawakuweza kumwona kama kawatoroka, waliendelea kumkimbiza, akajificha kuwaangalia mwisho wao. Lile lori likaacha njia na wakati huohuo risasi moja ilipiga tanki la mafuta na kusababisha mlipuko mkubwa na lile gari lakaangukia kolongoni.

§§§§

“Yule mshenzi amefia kolongoni kwa mlipuko mkubwa kama mnavyoona moshi kutoka mbali,” mkuu wa idara ya ulinzi alitoa taarifa kwa wakuu wake wa kazi. Wote wakafurahia na kumpigia makofi ingawa walipenda kama wangempata akiwa mzima.

Kikao na wale wageni kilikwisha lakini mvutano ulikuwa mkubwa sana hasa katika sababu ya vifo vile. Swala la kusema kwamba mitambo ilizimika kwa hitilafu halikuwaingia akilini. Na utata mkubwa ulioibuka upya ni juu ya kifo cha daktari aliyekuwa akichunguza miili ya wale marehemu, ripoti iliyokuja pale na iliyokwenda serikalini baada ya kifo chake ilithibitisha kuwa watu hao walikufa kwa kukosa hewa na saini ya daktari huyo ilionekana pale.

Lereti alibaki kimya hakuwa na la kusema, jopo lile kutoka serikalini lilikuwa tayari kuondoka mahali pale na wabia wake upande wa Robinson Dia-Gold waliona ushindi walioupata, utapeli walioufikiria ulikuwa ukienda kufanikiwa. Kwa ujumla tajiri maarufu muuza madini, mwenyeji wa Canada aliyejulikana kama Robinson Quebec alikua na tabia hiyo kwa kila mtu anayefanya naye biashara, alipanga kumdhulumu Lereti kwa mtindo huo wa kufanya mgodi uonekane hauko salama hasa kwa wafanyakazi wake kisha afanye kuwazunguka. Ndani ya nchi ya Afrika Kusini, Robinson alikuwa na urafiki na genge hatari la wazungu wenye kuua kwa kukusudia, wenye ibada za kunywa damu za watu. Watu hao ambao walikuwa na maeneo yao maalum ya kuendeshea shughuli zao hata serikali ya nchi hiyo haikuwagusa.

§§§§§

Habari za kuvamiwa mgodi huo zilifika kwa Don Angelo, alipopata picha chache za muonekano wa mtu huyo aliyevamia hakuwa na shaka kuwa ni Amata kwa kuwa zilishabihiana kabisa na zile ambazo anazo.

“Nilikuwa namtafuta sana huyu mtu, bora amekufa mwenyewe maana ningemkata mimi angejuta kuzaliwa dume,” akasema huku akizungukazunguka ndani ya sebule yake kubwa.

Alipochoka kuzunguka akaketi kwenye kiti chake na kuendelea na shughuli zake za kawaida, mezani kwake kulikuwa na faili moja kubwa alilokuwa akilifanyia kazi ndani yake kulikuwa na mikataba mbalimbali ya kuifanyia kazi. Mara simu yake ya mezani ikaita. Akainyanyua na kuiweka sikioni.

“Ndiyo, Don hapa,”

“Ile kazi huku imekamilika,” sauti kutoka kwenye simu ikamwambia.

“Oh! Ha ha ha ha safi sana, imekwenda kama tulivyopanga?”

“Ndiyo, kama tulivyopanga ijapokuwa kulikuwa na kutofautiana kidogo lakini tumewaweka sawa,” akajibu huyo aliyekuwa akipiga.

“Ok, kama ni hiyo sasa, inabaki kazi moja tu, na kazi hiyo ni nyepesi kama kuzima mshumaa kwa kuupuliza,” Don akaeleza.

“Kazi ipi?”

“Safi sana, hilo ndilo swali nililokuwa nalihitaji, nata Lereti auawe ndani ya saa arobaini na nane, ili huo mgodi sasa uwe chini yetu na hapo itakuwa rahisi kuutaifisha, kumbuka tayari tuna hati feki, na tumezipata taarifa za uchunguzi kutoka kwa dokta Nkosizulu, ilobaki ni hiyo tu basi,” Don akaeleza. Ukimya ukachukua nafasi kati ya hao wawili kila mmoja alihisi mwenzake anapumua kwa nguvu.

“Sasa Don, kwa sababu sakata la hawa wafanyakazi halijatulia, kwa nini Lereti tusimwache kwanza ili tumuondoa baadae sana?” Yule bwana wa upande wa pili akauliza.

“Usiwe kama motto mdogo wewe, Lereti anatakiwa kuuawa full stop, atakufaje nakuachia kazi hiyo uifanye na kikosi cha assassin haraka, wao watajua watamuuaje, na taarifa ya kikao chako pamoja nao naitaka leo usiku, hakuna wa kutuzuia hapa,” akamaliza na kukata simu. Akachukua mtemba wake na kukunja nne kisha akauvuta taratibu kwa saterehe zake.

§§§§§

LERETI KHUMALO alikuwa nusu kichaa nusu mzima, mara kwa mara alikuwa akiongea mwenyewe, akienda huku na kurudi kule, kila chumba cha nyumba yake aliingia na kutoka akiwa hajui hata ni nini amekifuata. Kila aliporudi chumbani kwake aliinua kitabu chake cha kumbukumbu na kupekuwa namba ya simu ya Kamanda Amata lakini hakuiona isipokuwa kile kipande cha karatasi kilichochanwa. ‘Hivi nani alichana hii anwani?’ alijiuliza huku akipigapiga miguu chini.

Akiwa kajitupa kitandani kwake na kugubikwa na machozi mengi huku akiitazama picha ya baba yake, simu yake ikaita, akaiinua na kutazama kwenye kioo ilikuwa namba tupu haikuwa na jina. ‘Nani huyu mida hii?’ akajiuliza lakini hakukuwapo mtu ndani ya nyumba hiyo isipokuwa yeye na mfanyakazi wa nyumba tu, mbwa upande wan je na walinzi wake wanaolinda kwa zamu.

“Unaongea na Dudumile Mwambakosi,” sauti kutoka kwenye simu ikajitambulisha moja kwa moja.

“Dudumile, habari rafiki?”

“Nzuri uko wapi?”

“Niko nyumbani sasa,” Lereti akajibu.

“Nahitaji kukuona sasa naomba nije kwako,” Debrah anayejiita Dudumile alimwambia Lereti. Ilikuwa mbali kumkubalia kuonana naye kwani alihisi hasije kufanyiwa mchezo mchafu katika hilo kwani mpaka hapo tayari machale yalikuwa yakimcheza kuwa lolote linaweza kutokea.

“Usiogope, naomba tuonane,” akasisitiza Debrah, mwisho Lereti akamkubaalia mwanadada huyo kufika nyumbani kwake.

Saa nne usiku, Debrah aliwasili na gari yake na kufunguliwa lango kisha akajitoma ndani na kukutana na mwenyeji wake, baada ya maamkio na vibywaji vichache ndipo azungumzo yalipoanza.

“Ndio Dudumile, mbona usiku, unanitisha,” Lereti akaanza kwa kusema.

“Hapana sikutishi na wala husiogope, kwanza kabisa mimi sio Dudumile lile lilikuwa ni jina tu la bandia la kufanya nitimize azma yangu, naitwa Debrah Mbongheni, natokea Pretoria, wala sikuwahi kufanya kazi na baba yako, sasa nitakwambia lile ambalo lilikuwa linanileta kwako,” Debrah akaongea, ‘Ila navunja masharti ya kazi, ah! Potelea mabali,’ akapiga moyo konde.

“Sikia Lereti, nilikuja kwako kufanya uchunguzi juu ya chanzo cha kifo cha baba yako, nah ii niliifanya kwa sababu nilipewa kazi ya kufanya uchunguzi wa vifo vya watu kumi na nane ndani ya Mgodi wako vilivyotokea miaezi mitatyu iliyopita, lakini sasa nikiwa katikati ya kazi na nilikuwa naanza kuelewa mengi nikapewa taarifa ya kuachana na hiiyo operesheni. Sasa nimekuja mimi kama mimi, nahitaji unambie kuna nini kinachoendelea ili nijue sakata hili linaishia wapi,” Debrah akajieleza.

Lereti alibaki kimya akisikiliza maneno hayo yaliyoonekana kama uongo ndani yake lakini pia kwa kiasi Fulani yalimkjengea imani.

“Dudumile!” akaita kwa sauti ya chini, “Kiukweli sijui kinachoendelea hata sasa, ila ninachohisi mbia wangu anataka kunizunguka ikiwezekana autaifishe mgodi wa baba yangu,” akaeleza kwa uchungu.

“Je mazingira ya vifo vilivyotokea mfululizo katika miezi michache hii unavionaje ni vya kawaida au vipi? Maana waliouawa wengine ni watu wa karibu wa baba yako,” Debrah akaendelea kudadavua.

“Kiukweli sasa ndio Napata maswali mengi katika hilo, wachunguzi waliokuja kutoka serikalini wamekubaliana na hitilafu ya mitambu ya vipooza hewa kule shimoni, lakini mimi kama mimi sijawahi kupewa taarifa hiyo, hivyo sijui kuna nini hivi sasa nataka nikaonane na waziri wa biashara kwa kuwa yeye huyo anaujua mkataba wa The Great Khumalo na ule wa Robinson Diamond,” Lereti akaeleza kinagaubaga.

“Na unategemea kwenda lini?”

“Baada ya saa ishirini na nne zijazo,” akajibu. Debrah akatulia kimya akifikiri jambo, hakujua hasa nini anatakiwa afanye.

“Debrah, nahitaji msaada wako kama inawezekana,” Lereti akamwambia Debrah kwa sauti ya chini. Debrah hakujibu, aligeuka na kumtazama Lereti.

“Nisaidie nipate kampuni binafsi inayoweza kufanya uchunguzi wa kina katika hili, nataka nibaini ukweli wa jambo hili maana mimi ndiye ninayepata shida, damu za hawa marehemu zinanisumbua zinalilia haki yao,” Lereti akaeleza kwa uchungu huku macho yake yakiwa yamejawa na machozi.

“Najua, usijali nitakuunganisha na kampuni moja nzuri sana kutoka Uingereza, ila kwanza nenda kamuone waziri kisha unipe jibu amesemaje, hapo sasa tutajua tunafanya nini, ila nahisi umezungukwa na watu wabaya sana, jiangalie na maisha yako,” Debrah akamweleza.

“Kuna vitu vinatokea vinanipa utata sana, Yule daktari aliyekuwa akifanya uchunguzi wa ile miili aliuawa kabla ya kukabidhi ripoti yake serikalini, na sina uhakika kama ripoti iliyokuja iko sahihi ijapokuwa imesainiwa na daktari huyohuyo,” Lereti akamwambia Debrah. Hapo moyo wa Debrah ukapiga chogo chemba na macho yake yakatulia kwa dada huyo ambaye machozi yake yalipotiririka mashavuni mwake uzuri wake wa kuzaliwa ulionekana dhahiri shahiri. Debrah akatikisa kichwa na kuanza kuunganisha matukio hayo ili kufanya picha moja yenye ukamilifu.

“Lereti kama ni hivyo unapambana na genge hatari zaidi ya MAFIA, hata mimi nimeshaambiwa kuwa nikijiingiza tena huku nitauwa, lakini siogopi hakuna wa kuniua,” Debrah akasimama mara tu alipomaliza kuzungumza hayo, “Wacha niende,” akaaga. Lereti akasimama na kumshika mabegani.

“Lala tu hapahapa, sasa ni usiku sana,” akambembeleza.

“Acha niende, nisikuletee matatizo bure, tuonane kesho kutwa Pretoria utakapokuja wizarani,” akamwambia na kisha kupotelea kwenye mlango wa mbele.

KAMANDA AMATA aliegesha gari yake maegeshoni mwa Hoteli 77, akateremka na kuingia chumbani mwake, kabla hajafanya lolote kwanza alisimama na kukitazama kona moja mpaka nyingine, ndipo akagundua kuwa chumba hicho kilipekuliwa na mtu mwenye uzoefu wa hali ya juu sana, ni vitu v ichache sana vilivyomfanya ajue kuwa chumba hicho kimekaguliwa. Akachomoa bastola yake na kuanza kuangalia hapa na pale, nyuma ya mlango, uvungu wa kitanda, bafuni, hakuna mtu, akaitupia kitandani bastola yake na kuvua nguo zile alizozivaa, akazitupia bafuni kwenye gudulia la uchafu.

Baada ya kujiswafi kwa dakika kadhaa na kujibadili kabisa mwonekano wake, akatoka nje ya hoteli hiyo. Aliitazama saa yake ilikuwa saa tano za usiku, taratibu akaingia katika gari yake na kuondoka.

Akaiwasha gari yake, ayo ikamwitikia, akatupia gia namba moja alipotaka kuiondoa ikagoma, kumbe alisahau kufunga mkanda, akafanya hivyo na kutoka taratibu. Ndani ya gari hiyo alikuwa akifuatilia upya mazungumzo ya wale wakaguzi na wamiiki wa mgodi huo kule mgodini. ‘Napinga kabisa, hao watu kumi na tano wa mwisho hawajafa kwa hivyo mnavyosema, na ukweli utajulikana tu hata kama mmemuua Dr. Nkosizulu,’ alijikuta akijisemea peke yake wakati akiingia barabara ya Mama Silowane ambapo katika mtaa huo, kitalu namba 79 ndipo nyumba ya marehemu daktari huyo ilikuwapo.

Alipita kwa mwendo wa taratibu na kukuta gari nyingi zikiwa zimejipanga barabarani usiku huo, muziki wa maombolezo ulisikika kutoka katika vipaza sauti. Kamanda Amata alitafuta mahala pazuri na kuiegesha gari yake kisha akateremka na kuiweka suti yake vizuri, hakuvaa tai siku hiyo, akaipachika miwani yake inayoweza kuona vizu vya chuma vilivyo mwilini mwa mtu, kisha kwa hatu za taratibu akasogelea ujia wa kuingilia katika jumba hilo kubwa la kifahari. Alipofikia mahala pa kuingilia kwenye eneo kubwa la bustani ambalo watu kadhaa walikuwa wamekaeti huku kwaya ikiendelea kuimba nyimbo za maombolezo alipokelewa na vijana wawili, waliovalia suti nyeusi, akawatazama, walikuwa safi, hawakuwa na silaha yoyote ili mmoja alionekana na chuma katika ugoko wake, akajua ni ajali tu hiyo imemfanya awekewe chuma hicho.

Moja kwa moja akakuta kitabu cha maombolezo, akaweka jina lake halisi kabisa bila ubabaishaji, kisha akainuka kutoka eneo lile, muda huohuo alihisi simu yake ikifanya fujo mfukoni, akaitoa na kuifyatua tayari kwa mawasiliano, hakuona jina isipokuwa namba peke yake.

§§§§

JESCA GEN alikuwa akitembea kama mwehu barabarani, hakujiamini kama yuko hai, alijuwa wazi kuwa muda wowote atauawa kwani aliwajua watu hao kwa jinsi walivyo na mtandao wa siri ambao si rahisi kuugundua, karibu kila kona ya jiji la Johanesburg walikuwa na watu wao, ambao hata wakikuua na kuitupa maiti yako hapo hakuna wa kuwafatilia. Alivuka barabara ndogo ya mtaa Fulani huko nje kabisa ya jiji la Joh’burg, hakujua ni wapi anaelekea, yeye alikuwa akitafuta mahala japo apumzike usiku huo.

Nyumba ndogo ilikuwa mbele yake, nyumba pweke ambayo ndani yake kulikuwa na mwanga hafifu wa taa isiyo na nguvu, akaiendea na kugonga hodi, sauti ya mtu aliyeonekana kama mzee au mgonjwa ilimkaribisha, naye akaingia ndani bila woga.

“Karibu, wewe ni nani,?” alikuwa ni mzee aliyeketi kwenye maboksi na kibatari cha mafuta ya taa kikiwaka kando yake. Mzee Yule aliyekuwa akiongea kwa kizulu n akingereza kilichochanganywa ndani yake alionekana kama mzee asiye na msaada sana kwa Jesca.

“Naitwa Jesca au wengi uniita Cayla,” akajibu Jesca.

“We ni boer?” Yule mzee akauliza.

“Ndiyo mimi ni boer,”

“Umefata nini huku? Huku ni black suburb, boer hatakiwi kuonekana, wakikuona watakuua,” yule mzee akaeleza.

“Oh come on, nina shida na najua ni watu weusi watakaonisaidia kwa sasa,”

“We umechanganyikiwa?” Yule mzee akauliza.

“Hapana nahitaji sehemu ya kulala usiku huu tu kesho asubuhi nitaondoka,” Jesca akaomba.

“Pole sana, sikuwahi kufikiri kama hata ninyi boers huwa mnakosa pa kulala,”

Wakati wakionge hayo, Jesca alisikia muungurumo wa gari anayoijua, akasogea karibu na dirisha dogo na kuchungulia nje, aliijua ile gari vyema kwa maana aliitumia siku mbili tu zilizopita kwenda kumtafuta Daktari Nkosizulu na kumuua. Vijana wawili wakashuka wakiwa na bunduki mikononi mwao.

“Shiit, wamenifuata, sasa watanimaliza,” akajisemea lakini Yule babu akasikia.

“Unasemaje nani hao?”

“Boers, wanataka kuniua,” akajibu. Yule mzee akamwonesha ishara tu kuwa aingie kwenye moja ya mapazia yaliyokuwa hapo sebuleni, Jesca akafanya hivyo na mara ule mlango ukafunguliwa bila hodi, tochi yenye mwanga mkali ikamulika ndani ya kibanda kile, Yule mzee akaketi palepale wala hakuinuka.

“Niwasaidie nini?” akawauliza.

“Huna la kutusaidia masikini wewe!” mmoja wa wale vijana wazungu akaanza kupekuwa huku na kule ndani ya kinyumba hicho.

“Yuko wapi Yule mwanamke mzungu?” wakamuuliza Yule babu aliyejichokea.

“Mi nitajuaje, kwani hapa kaja mwanamke mzungu? Tangu lini ninyi boers mkaja huku?”

“Tunakuua we kizee,” mmoja akamwambia huku akimwonesheabunduki Yule mzee.

§§§§§

JESCA alijawa na huruma ya ghafla pale alipojificha ambapo haikuwa rahisi kwa yeyote kupagundua, ‘msimuue,’ alijisemea moyoni. Lakini bado wale jamaa walikuwa wakimsukasuka Yule mzee kutoka pale alipokuwa ameketi. Mmoja wa wale vijana akaweka bunduki yake usawa wa paji la uso la Yule mzee na kuiruhusu risasi iingie chemba tayari kusubiri amri.

“Utatuambia au la?” walimuuliza. Yule mzee alikuwa akitetemeka lakini hakuweza kujibu lolote.

“Noooooooooo!” Jesca alipiga kelele na kujitokeza kutoka pale alipojificha kuelekea walipo wale vijana ili kuwazuia kwa jaribip hilo. Mmoja wa wale vijana aligeuka na kumwona Jesca, akainua bunduki yake tayari kumlipua.

Jesca alijikuta akibanwa na kono moja lenye nguvu kutokea nyuma yake, akavutiwa nyuma ya ukuta wa kile chumba na risasi ya Yule kijana ikapita bila ya kufanya madhara. Kilichoshuhudiwa ni wale vijana wakipaa juu kwa zamu na kujibwaga chini wakiwa hawana maisha.

“Mr. Spark!!” Jesca aliita kwa kushtuka na kumrukia Kamanda Amata ambaye bado alikuwa na bastola yake mkononi, baada ya nukta chache akaipachika ndani ya koti lake.

“Nakutafuta Mr. Spark,”

“Najua, lakini kwanza tuzishighulikie hizi maiti, tuzibebe tukazitie kwenye ile gari waliyokuja nayo,” kamanda Amata akamwambia Jesca kisha wote wakatoka na kubeba zile maiti kwa zamu na kuzitupia kwenye buti la ile gari ya waliokuja nayo wenyewe.

“Halafu tunafanyaje?” Jesca akauliza.

“Ingia kwenye gari, endesha, tangulia mbele,” akamwamuru na kisha yeye akaitoa gari yake ndani ya shamba la mahindi lililozunguka nyumba ya huyo mzee. Hakuna aliyejua au kung’amua Amata kafika saa ngapi kwa maana gari hiyo alikuwa na uwezo wa kuondoa sauti na ikabaki ikitembea biloa sauti yoyote ya kushtua watu.

Mwendo wa dakika kumi na tano, Kamanda Amata akaipita ile gari na kumwamuru asimame, Jesca akashuka na kuingia kwenye gari ya Amata, kiti chenye starehe kikampokea naye akajitupa juu yake. Amata akachomoa bastola yake na kupiga tenki la mafuta hilo gari akaliacha likiteketea kwa moto, wakati yeye na Jesca wakirudi mjini.

“Ulikuwa wapi Mr…”

“Amata, Kamanda Amata,” kamanda akammalizia kujibu swali lake.

“Ina maana wewe ndiye mpelelezi Yule mwenye sifa nyingi huko Afrika Mashariki,” Jesca akauliza.

“Ndiyo, T.S.A 1 si cheo cha kawaida,” kamanda akajibu.

“Umejuaje kama niko huku?”

“Nimewafuatilia sana hawa jamaa tangu mjini mpaka sasa, waache waitumikie jehannam kwani ndiyo haki yao,” Amata akajibu.

“Amata, wanataka kuniua kwa ajili yako, juzi walikuja nyumbani kwangu kukuteka lakini hawakukupata, ulifanya vyema kuondoka dear,” Jesca alijieleza.

“Najua, usijali, nataka unifanyie kazi yangu moja tu,” Kamanda Amata akamgeuzia kibao.

“Ipi?” jesca akapigwa na butwaa.

“NImechunguza kila kitu kupitia kamera za usalama za pale Charlote Maxeke, na nimekuona wewe ukifuatana na vijana wawili, nimewaona mkitoka na kuondoka kwa mfuatano na gari ya Nkosizulu, baada ya, muda mfupi tu, na Yule daktari akauawa,” akaeleza Amata.

Jesca alibaki kajibana mikono midomoni, akishangaa kwa hilo analolieleza Amata.

“Sasa sikiliza, nataka ripoti ile aliyoiandika Dakt. Nkosizulu ili nikamilishe kazi yangu, wewe unajua nani umempa,” Kamanda akamalizia, wakati huo akiingia barabara kubwa nyingine na kuzidi kuja mjini.

Jesca alibaki kamtumbulia macho Amata kana kwamba alikuwa haelewi.

“Eti unasemaje?” akauliza.

“Nasema nataka lile faili la uchunguzi aliloandika daktari marehemu, ulilipeleka humu, sasa nenda kalifuate,” kamanda akamwuliza wakati huo wakisimama maegeshoni mwa hoteli ya Montecassino.

“Amata, ngome ile haipenyeki, Don Angelo tayari anataka kuniua, wananisaka kila kona, nitaingiaje pale na nitalipataje faili lile?” Jesca alilalamika.

“Utaenda huwendi?” Kamanda alimuuliza huku akimtazamishia domo la bastola. Jesca alilia machozi na kutetemeka.

Kamanda Amata akarudisha bastola yake kiunoni. Sasa sikiliza utafanya namna hii….

“Sasa sikiliza utafanya namna hii, wale jamaa wananitafuta, najua…”

“Tena wamenambia nisipowajulisha ulipo ndani ya siku nne wataniua,” Jesca akadakia.

“Ok, good! Sasa umenipata, waambia niko mahali Fulani waje wanichukue, najua wewe na mimi sote tutaenda kwa Don, kisha wewe utanipa ishara ya wapi hilo faili lipo kisha mi najua nini nitafanya,” kamanda Amata akatoa maelekezo.

“Mr. Spark!” Jesca akaita.

“Niite Kamanda Amata! Fanya nililokwambia…”

“Sikia Amata, usicheze na ngome ya Don, ukiingia pale hutoki, na ukizingatia wanakusaka kwa mengi maana sasa wamejua kuwa ni wewe uliyemuua Tracy Tasha ambaye alikuwa mtu wao wa kutegemea,” Jesca akaeleza bila kujua kuwa alikuwa akimuunganishia picha Amata kwa lile analolitafuta. Kamanda Amata akatikisa kichwa kuashiria kuwa amepata moja jumlisha moja, sasa jibu kichwani mwake lilikuwa mbili, tena mbili isiyoghoshiwa.

“Jesca, niambie kitu name nitakuhakikishi uslama wako,” kamanda akamwambia.

Jesca akatikisa kichwa kukubali kile anachotaka kuambiwa na Amata.

“Kuna uhusiano gani kati ya Don na Sir. Robinson Quebec?” swali hilo lilimshtua sana Jesca, akamtazama Amata usoni bila kummaliza.

“Unamjua Robinson?”

“Ndiyo namjua ijapokuwa sijawahi kumuona kwa macho,” akajibu. Kimya cha nukta kadhaa kikatawala kati ya wawili hao na kila mmoja alikuwa akiwaza lake kichwani.

“Huyo ni mtu hatari sana, Don ni mshirika wake wa karibu, Robinson ana mtandao wake hatari sana duniani kote, amehodhi migodi mingi ya almasi na dhahabu hasa huku Afrika, na anasaini mikataba na serikali nyingi kila kukicha, hata hapa Afrika ya Kusini anamiliki mgodi mmoja mkubwa wa dhahabu…” Jesca akanyamaza ghafla.

“Endelea nakusikiliza,” kamanada alimwambia huku saa yake ikiwa inarekodi mazungumzo hayo. Jesca akaendelea kuwa kimya kabisa.

“No, nimekueleza siri ambayo hatutakiwi kuitoa kwa yeyote,” Jesca akamwambia Amata.

“Ina maana na wewe ni mshirika wao?”

“Ndiyo,” Jesca akajibu na kumuonesha Amata sikio lake upande wa nyuma, kulikuwa na kitu kama pini iliyopachikwa kwa ufundi kabisa, kwa haraka Amata alielewa kuwa ile si pini ni chombo kiunachonasa na kurusha mawasiliano kwa njia ya sauti, hakitoki kirahisi, kwa jinsi walivyokiprogram ukikichomoa tu kinasababisha mlipuko na wewe mwenye nacho lazima upoteze maisha.

Kamanda Amata akamsukuma nyuma Jesca kwa nguvu.

“Ina maana yote tuliyoongea wameyasikia?” akamuuiliza.

“Hata hili pia,”

“Bastard!” alimtukana na kuchomoa bastola yake, alipotaka kumlipua Jesca tua akajikuta kazingirwa na vijana watano wenye silaha mikononi mwao.

“Tulia kama ulivyo, Mr. Spark wa bandia, leo ndio mwisho wako,” Kamanda Amata alijikuta akiloa jasho, aliwatazama wale vijana waliokuwa wamevalia nguo nyeusi na majamba koti marefu, walikuwa wakitisha, macho yao yalikuwa mithili yap aka, Yule kiongozi wao alipokuwa akiongea, Kamanda Amata aliweza kuyaona meno manne marefu mawili ya chini na mawili ya juu, aliwaelewa watu wa aina hiyo.

“Shiit!” akang’aka kwa sauti ya chini.

“Lete silaha yako,” wakamwamuru.

Akawapatia, kisha wakamchukua na kumfunga mikono nyuma, na Jesca naye vivyo hivyo wakawapakia garini na kuondoka nao. Kijana mmoja aliamuriwa kuingia katika gari ya Amata nili afuatane nao, lakini alishindwa kuiwasha kabisa. Kila alipojaribu ilimwandikia onyo kuwa hasirudie tena. Alipojaribu mara ya tatu, ile gari ikamwambia kuwa akijaribu mara ya nne na ya tano ingelipuka. Akaiacha na kumwambia kiongozi wao juu ya ule ujumbe nay eye akaja kuushuhudia. Wakaamua kuiacha na kuondoka zao, muhimu kwao haikuwa gari bali Amata na Jesca.

§§§§§

DEBRAH MBONGHENI aliondoka kwa Lereti usiku huo na kuelekea uwanja wa ndege hakuwa na haja ya kulala Durban, alitaka kurudi usiku huohuo kwa ndege na kuamkia Pretoria siku iliyofuata. Akiwa kwenye taxi iliyokuwa mwendo mkali kuelekea Uwanja wa Ndege wa Luis Botha, Debrah alikuwa kimya aliyejawa na mawazo mengi sana kichwabi mwake, alitaka kujua kuna nini ndani ya kesi hiyo hata yeye akatazwe kuendelea na uchunguzi lakini pia alijilaumu kwa nini kajiingiza tena kwenye sakata hilo ambalo alikwishaonywa juu ya maisha yake.

Ile gari ilikuwa ikiongeza kasi, alipochungulia kwenye speedomita akakuta imefikia kilomita 165 kwa saa. Akamshika bega dereva taratibu kutaka nkumwomba apunguze mwendo kwani ilikuwa ni hatari, lakini Yule dreava kana kwamba hakusikia ombi hilo, alikuwa ametulia kwenye usukani bila shaka yoyote.

Mara ghafla, mbele yao, Debrah aliona kama mtu kasimama katikati ya barabara, akapiga ukulele kutoka ndani ya gari, Yule dreva akapata mshtuko, ile gari ikayumba na kujipiga kwenye kingo ya barabara, ikabingirika na kudondokea barabara ya pili, kabla haijakaa sawa, lori kubwa la mafuta lilikuwa likipita kwa kasi, likaigonga na kusukuma upande mwingine. Ikaseleleka na kujizungusha huku na huko ikakutana na lori lingine uso kwa uso na kukanyagwa vibaya.

Debrah alibanwa na mabati ya gari ile, alipoangalia kiti cha dereva japo kwa taabu, hakumuona mtu. Kutokana na usiku ule kuwa mnene hakukuwa na msaada wa haraka, Debrah alikosa msaada, alipiga kelele lakini wapi, dakika hiyohiyo aliona kama miguu ya mtu aliyesimama, akajitahidi kuinua uso amuone lakini alishindwa. Yule mtu akamvuta taratibu Debra na kumtoa nje barabarani. Akapiga goti moja chini na kumtazama mwanamke huyo.

Debrah naye akajitahidi kuinua uso wake, lakini maumivu makali yalimfanya ashindwe kumudu hali hiyo.

“Unanikumbuka?” Yule mtu akamwuliza Debrah. Debrah akamtazama japo kwa tabu lakini aliweza kuiona sura yake, akapigwa na mshangao, akamkumbuka mtu huyo, alimwona siku mbili nyuma palepale Durban. Hakuweza kusema lolote, kinywani mwake na puani damu zilimtiririka polepole.

“Tulikwambia, uachane na swala hili lakini wewe ni mbishi, mkuu wako wa kazi alikwambi hili lakini bado, sasa sina budi kutekeleza agizo la mkubwa wangu, kwa kuwa wewe umeshindwa kutekeleza agizo la mkubwa wako,” Yule mtu akamaliza kusema kisha akamwinamia Debrah na kumng’ata kwa meno yake marefu na makali katika mshipa mkubwa wa damu sehemu za shingoni na kuanza kufyonza damu.

Debrah hakuweza hata kujitetea, alipoteza fahamu na mwisho hakujitambua kabisa, umauti ulimfika.

HOTELI YA MICHELANGELO

DON ANGELO alimtazama Kamanda Amata akiwa bado amefungwa mikono yake nyuma, uso wake ukiwa na michubuko kadhaa kwa kipigo alichopewa na wafuasi wa tajiri huyo.

“Yes, yes, yes, sasa uko mikononi mwangu, lazima dunia ijue kuwa mbwa mmoja mweusi anayejifanya anajua ameuawa kinyama. Najua huyo Malaya Jesca amekupa siri nzito na utamu wa kiuno chake pia amekupa, hongera kwa hilo, kama ulikuwa hujui basi kifo chako kilikuwa chini ya pua yake,” Don Angelo aliongea huku akizunguka zunguka, vijana wake walitulia kimya. Akamfuata Jesca na kumshika kidevu chake, akamtazamisha na sura yake ya kutisha.

“Mwanamke, umevunja kiapo ambacho unajua ujira wake, sasa ndicho kinachofuata,” akamtazama mmoja wa vijana wake.

“Muue huyo mwanamke!” akaamuru, Yule kijana akamwendea Jesca huku meno yake makali kama chui yakiwa nje.

“Vampire!” Kamanda Amata akatamka kwa sauti ndogo. Kwa nguvu zake zote alijitikisa kushoto na kulia, wale vijana waliokuwa pembeni yake wakajikuta wakianguka huku na huku, Kamanda Amata akaruka na kujikunja akawa mdogo kama samaki akapita kati kati ya mikono yake na kutua sakafuni sasa mikono yake ikiwa mbele na si nyuma tena. Yule kijana aliyekua akimwendea Jesca akajikuta haelewi la kufanya. Akachomoa kisu kutoka katika koti lake na kumshambulia Amata ambaye aliepa kwa ustadi na kujirusha upande mwingine wa sebule hiyo ya kisasa. Wale vijana wakaamka na kuanza kumfuata Amata.

Amata akainuka harka na kuwakimbilia, kabla hajawafikia akakanyaga kabati la vitabu, akajiinua na kukanyaga ukuta, akawa hewani na kujibinua sarakasi akiwaacha chini kisha akawapa mateke mawili ya maana yakawarudisha chini, naye akatua mblele ya Yule jamaa mwenye kisu. Kabla hajakaa sawa akampa kichwa kimoja kilichomtoa fahamu na kujibwaga juu ya meza ya kioo. Kamanda Amata akawahi kisu na kukikamata kwa kinywa chake, haraka akakata ile kamba ya plastiki iliyokuwa mikononi mwake. Alipoinuka, hakumuona Don, katoroka, mara milango ikafunguka vijana kama kumi wakaingia. Kamanda Amata akainua kila alichokiona na kuwarushia vijana wale wenye hasira wote walikuwa wamopja kwani walikenua na kuruhusu meno yao ya kutisha kuonekana nje.

“Amataaaaaaaa!” Jesca akaita, na wakati huo huo tayari alikuwa mbele ya Kamanda Amata, risasi tatui zikamwishia kifuani mrembo Yule, Kamanda Amata hakuwa na muda wa kupoteza, alimbwaga chini na mkononi mwake alimona kashika kipande cha karatasi, kwa kasi ya umeme. Alikinyakua kile kijikaratasi na kuruka sarakasi huku akishuhudia vioo vizito viukitawanywa kwa risasi za wale jamaa, alitua chini sakafuni na kujibingirisha huku akiwapa ngwala za maana na kuwabwaga vijana kama watatu hivi. Mbele yake aliona bastola iliyoanguka akaiwahi na kuinyakuwa mkononi mwake, risasi alizozitembeza ndani ya sebule hiyo ziliacha mifereji ya damu.

Kamanda Amata aliona ngoma nzito, akajirusha kwenye dirisha moja kubwa la kioo na kutoka na vioo vyake, akadondokea ghorofa nyingine iliyokuwa upande wa pili wa hoteli hiyo. Akahisi maumivu makali sehemu ya mgongo wake, lakini hakuyapa muda wa kuyasikiliza, akanyanyuka na kujirusha mpaka nyumba ya pili kutoka hapo alipoangukia, akakimbia kupitia juu ya paa la jingo hilo huku risasi zikipiga hapa na pale. Akafanikiwa kutokomea na kuwaacha wale jamaa wakiwa hawaamini kinachotokea.

Ndani ya lile jingo alilochomoka Kamanda Amata, aliwaacha wale vijana wakishangaa na kile kilichotokea, ilikuwa ni msambwe wa dakika moja na nusu lakini jasho lilimwagika na Amata wakamkosa. Don Angelo akajitokeza katika lifti maalumu na kurudi tena sebuleni huku kajishika kichwa kwa jinsi uharibifu ulivyotokea.

“Yuko wapi?” akauliza.

“Katoroka,” wakajibu, huku wengine wakiwa wanapokezana kuinyonya damu ya Debrah kabla haijapoa.

“Katoroka vipi mikononi mwenu?”

“Hata sisi hatujui ila katoroka na kama unavyoona vijana wetu wawili wamepoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya.

“Donald!!!” Don Angelo akaita kwa ukali.

“Yule kijana keishapewa siri kubwa na Jesca, nahitaji auawe popote alipo na muda wowote, kisha mwili wake muulete hapa,”

Don akamaliza kusema na wakati huohuo shughuli nyingine ndani ya sebule hiyo zikaanza ikiwamo kuziondoa zile maiti na kusafisha na tayari mafundi walikuwa wameanza kupachika vioo vipya….

ASUBUHI YA SIKU ILIYOFUATA habari ya kuokotwa mwili wa Debrah, askari shujaa wa kike katika jeshi la Afika ya kusini ilifika masikioni mwa wengi. Wanaomjua walisikitika kwa kifo chake kwani walimuelewa vema askari huyo matata ambaye Taifa hilo lilimtegemea sana katika kazi mbalimbali za kiintelijensia.

Waliopanga kifo hicho walifurahi kwa mara nyingine kwani walitimiza azma yao bila kukosea, daima ilikuwa kukosea kwao mwiko. Ni kundi hatari la mauaji ya siri, linalojua kazi yake vyema, likiwa chini ya tajiri mkubwa Don Angelo, asiyeonekana na watu, yeye daima hukaa ndani tu akiletewa kila huduma ndani, mwanamke yoyote aliyemtaka aliletewa kisha baada ya kumaliza haja zake alimtoa sadaka kwa vijana wake walimuua na kumyonya damu kwani kwao hiyo ilikuwa kama dini. Miili ya wafu wa namna hiyo iliokotwa mara nyingi tu katika viunga vya jiji la Johanesburg au hata nje yake.

Don Angelo alikuwa swahiba mkubwa wa Robinson Quebec walishirikiana mbinu chafu za kumuondoa tajiri Khumalo kwa hila ili Robinson ageuze mikataba ya ubia wake wa mgodi na kuumiliki yeye kama alivyopfanya katika mataifa mengi. Pembeni ya Robinson kulikuwa na huyu Don akimpa usaidizi wa kila jambo alilolihitaji ikiwamo kupata saini au dokumenti yoyote kutoka serikalini. Viongoza wa serikali walimwogopa tajiri huyu kwani ni kati ya wazungu mabeberu katika nchi hiyo waliojulikana kama ‘Boers’, walikwishaitawala nchi hiyo miaka na miaka hivyo walijua kila kitu, walimjua kila kiongozi, hawakubabaishwa, walifanya wanayoyataka bila kuzuiwa na mtu, ukijinya unajua siku ya pili huamki utakutwa kitandani mfu hukiwa huna hata tone la damu na jeraha shingoni.

Wanaintelijensia wa nchi hiyo walipochunguza vifo mbalimbali na kuona jeraha hilo walijua ni nani alisababisha, basi hakukuwa na upelelezi wa maana zaidi ya blah blah tu na kesi kupotelea hewani.

SIKU TATU NYUMA

Jioni ya siku moja huko Pretoria kwenye ofisi nyeti ya serikali aliingia kijana mmoja aliyevalia suti safi nyeusi na kofia aina ya pama nayo nyeusi. Ndani ya ofisi hiyo kulikuwa na mtu mmoja mwenye mwili mkubwa, Yule kijana aliingia kibabe, hakuzuiwa na mtu, kwani ukijaribu kumzuia yeye alitabasamu tu na meno yake manne marefu yalionekana nje, bila ubishi utakaa pembeni na ye atafanya yeke.

Dumisan alikuwa ameketi kitini, muda wake wa kutoka ofisini ulikuwa haujafika alipokutwa na kijana huyo.

Yule kijana akamwangalia Dumisan pa si na salamu yoyote, akatabasamu, kisha akamwambia maneno machache.

“Mwambie msichana wako aachane na kile anachokifanya huko Johanesburg, tunakupa saa nne tu, akikaidi tunamuua na we ukikaidi kesho huamki,” alipomaliza akaondoka zake bila kuaga. Dumisan hakuwa na swali moja kwa moja aliinua simu yake ya ofisi kwani alijua nini kinajiri, akampigia Debrah na kumtaka arudi haraka Pretoria, amri ambayo haikupokelewa vyema na mwanadada huyo.

ITAENDELEA

Mkono wa Jasusi Sehemu ya Nne

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment