Born to Die Sehemu ya Kwanza
NEW AUDIO

Ep 01: Born to Die

Born to Die Sehemu ya Kwanza
Born to Die Sehemu ya Kwanza

IMEANDIKWA NA : FRANK MASAI

Simulizi : Born To Die

Sehemu Ya Kwanza (1)

“What is your name? (Jina lako nani?)”

“I don’t know. (Sijui)”

“Pu pu pu.” Zilisikika sauti hizo kwenye chumba kimoja kidogo kilichokuwa na watu watano.

Sauti hizo zilikuwa ni sauti za kipigo kumwendea yule aliyekuwa anaulizwa maswali.

Jamaa hao watano, mmoja ambaye ndiye alionekana mkuu, alikuwa anauliza maswali, wengine wawili wamemshikilia kwa nguvu jamaa mwingine aliyekuwa anaulizwa maswali, huku wamemkunja mikono kwa nyuma na kufanya kifua na tumbo lake kubetuka vizuri kwa mbele jambo ambalo lilimpa yule jamaa wa tano kumshushia kipigo cha nguvu pale alipokaidi kujibu maswali yao.

“I am asking you again. If you don’t answer, we will kill you (Nakuuliza tena. Kama usipojibu, tutakuua)” Yule mkuu wao ambaye alivalia mavazi ya kijeshi, tena yale yenye nyota nyingi mabegani na kwenye mifuko ya shati lake, alimpa onyo jamaa yule aliyekuwa anapewa kipigo huku akiwa amechakaa uso kwa damu pamoja na kuvimba vibaya mno.

Alishapoteza matumaini ya kuishi kwani mwili wake ulikuwa umelegea kiasi kwamba alikuwa anawapa uzito wale waliokuwa wamemshikilia.

“What is your name (Jina lako nani)?” Jamaa aliulizwa swali.

“I don’t know Sir (Sijui Mkuu)” Alijibu yule jamaa kwa sauti ya chini iliyokuwa imeishiwa nguvu kabisa.

Yule mpigaji alivyoona hivyo, alinyanyua ngumi yake tayari kuendelea kuishindilia mwilini mwa yule jamaa.

“Stop, (Acha)” Yule mkuu alimkataza mpigaji.

“You are so rude, boy. Very good, (We’ ni mkorofi, kijana. Safi sana)” Mkuu yule aliongea huku akizunguka zunguka kile chumba kwa tambo.

“Release him. (Muachieni)”.Aliwaambia wale jamaa waliokuwa wamemshika na wao wakatii amri kwa kumwachia yule mtuhumiwa wao.

“You all, go outside (Ninyi nyote, nendeni nje)” Aliendelea kuwaamuru wale jamaa waliokuwamo mle ndani, nao wakatoka na kumuacha yule jamaa kalala chini akigugumia kwa maumivu.

“Okey. Now we’re alone. You’ve to tell me the truth.(Sawa. Sasa tupo peke yetu. Unatakiwa kuniambia ukweli,” Aliongea mkuu yule huku akichutama karibu na pale alipokuwa amelala yule jamaa.

“I’ve nothing to tell you (Sina cha kukuambia)” Alijibu jamaa yule kwa sauti ya ukakamavu lakini iliyojaa maumivu.

“That’s bad boy. So damn bad. (Hiyo mbaya kijana. Tena mbaya sana)” Aliongea yule mkuu huku akisimama toka eneo lile na kwenda kwenye jiko moja la umeme ambapo alikuwa ametenga birika la maji.

Akachukua birika lile na kwenda nalo kwenye meza iliyokuwamo mle, kisha akamimina maji yale kwenye kikombe na kuchukua kahawa kiasi kwenye kijiko na kuchanganya kwenye maji yaliyo kwenye kikombe.

Alivuta kiti kwa nyuma na kukikalia, kisha akafunua sahani moja iliyokuwepo mezani pale na kuchukua chapati moja.

Aliikunja chapati ile na kuanza kuila huku akishushia kwa kahawa aliyoichanganya muda mfupi uliopita.

Katikati ya ulaji wake, alimtupia jicho yule jamaa aliyekuwa amelala pale chini. Alimwona jinsi anavyomwangalia alavyo, naye akatumia udhaifu huo kuongea naye.

“Are you hungry? (Una njaa?)” Alimuuliza yule jamaa huku bado anatafuna kipande cha chapati alichokuwa kabwia mdomoni.

“Come on. Let’s eat. (Njoo. Njoo tule)” Aliongea yule mkuu na kunyanyuka pale kitini na kwenda kwenye kabati moja kuu-kuu la vyombo na kuchukua kikombe kimoja cha plastiki na kwenda nacho mezani.

“Don’t you want it? (Hautaki?)” Alimuuliza yule jamaa aliyekuwa amelala pale chini baada ya kumwona hajishughulishi kuitikia karibu yake.

Jamaa yule aliyekuwa chini alianza kuinuka pale alipokuwa na moja kwa moja akaelekea kuungana na yule mkuu kwenye meza ile.

“That’s my man. (Huyo ndiye mtu wangu)” Alimsifia jamaa alipokuwa ananyanyuka huku yeye akimimina maji kwenye kile kikombe alichokuja nacho mara ya pili.

Jamaa naye alivuta kiti kiuchovu na kukaa huku akimuelekea yule mwenyeji uso wake. Akapewa kahawa kwenye kikombe kile na kusogezewa sahani ya chapati ili ajilie.

Alikula kwa taratibu na kistaarabu kuliko alivyotegemea yule mkuu aliyekuwa anamuangalia kwa macho ya kumdadisi yule jamaa ambaye alikuwa kifua wazi na chini kavaa kombati ya jeshi yenye mabaka ya kijani.

“So.Tell me soldier boy. Who’re you and who sent you here, (Niambie kijana. Wewe ni nani na nani kakutuma hapa?)” Yule mkuu alimuuliza huku akiweka miguu yake mezani.

“I am nobody and nobody sent me here. (Mi si kitu na hakuna aliyenituma hapa)” Jamaa alijibu na kisha aliinamia kahawa yake na kuendelea kuinywa.

“You act like a taugh guy. Am I right boy? (Unajifanya kijana mgumu sana.Nadanganya kijana?)” Mkuu alimuuliza huku bado miguu yake ikiwa pale mezani anaitikisa-tikisa kwa mbwembwe.

“No. I just answer your questions. But if you like me to be a tough guy,I’ll be. But don’t blame me. (Hapana. Najibu maswali yako. Lakini kama unapenda niwe mgumu, nitakuwa. Lakini usinilaumu)” Jamaa alijibu huku anasogeza kikombe cha kahawa na sahani mbele kumuelekea yule mkuu.

“You never answer my questions boy. And don’t try me to make you like before. (Hujanijibu maswali yangu kijana. Na usinijaribu nikufanye kama hapo mwanzo)” Mkuu aliongea huku macho yake kamkazia yule jamaa ambaye alikuwa hataki kujitambulisha.

Jamaa alikaa kimya huku naye macho yake anamuangalia yule mkuu ambaye umri kiasi fulani ulikuwa umeenda lakini alikuwa bado mkakamavu.

Akiwa ndani ya mavazi yake ya nyota, mkuu yule alishusha miguu yake juu ya meza na kusogea mbele zaidi na kumkingia uso yule jamaa.

“Umetumwa na Hispania? Cuba au Korea?” Mkuu yule alimuuliza kwa lugha ileile ya kiingereza.

Jamaa akacheka kwa dharau kisha akamuangalia yule mkuu na kuhisi kama anapoteza dira.

“Kwa nini ziwe nchi hizo na siyo zile mnazowatengenezea silaha za maangamizi na kuwapa ili muone kama zinafanya kazi ipasavyo? Kwa nini zisiwe zile nchi ambazo mnazichukulia malighafi zake na kujilimbikizia nyie? Kwa nini zisiwe zile nchi ambazo kila siku zinalia na njaa huku zikipoteza watoto wake kwa waume kwa sababu ya vita ambavyo nyie ndio wachonganishi? Kwa nini zisiwe nchi mnazozuga mnatandaza demokrasia, kumbe mnatandaza vita? Kwa nini zisiwe hizi nchi mnazozitupia magonjwa kila kukicha?

Kwa nini zisiwe nchi hizo na badala yake zikawa nchi ambazo zinatetea msifanye maasi yenu?” Aliongea yule jamaa kwa sauti ya chini iliyoanza kupata ahueni baada ya maumivu kupoa kiasi. Aliongea kwa hasira na msisitizo ndani yake.

“Kwa hiyo umetokea Afrika,” Aliongea yule mkuu huku akirudisha mgongo wake kwenye kiti na kuweka miguu yake mezani tena na mikono yake akiipitisha shingoni na kuja kukutana nyuma ya kisogo chake.

“Well, well. Umetoka Afrika. Niambie sasa. Umetoka Kongo, Kameruni au Naijeria. Au labda umetoka Niger au Sudan,” Alizidi kubwabwaja yule mkuu.

“Nimetokea Afrika. Siwakilishi nchi wala Taifa,” Jamaa alijibu kwa nyodo na kwa kujiamini.

“Okey. Sasa ni muda wa kuwa siriazi. Nauliza na unajibu ipasavyo, sawa?” Mkuu alikuja juu sasa na kumtaka yule jamaa mwenye ngozi nyeusi awe siriasi kwa akifanyacho.

“Ni wewe ndiye haupo siriasi. Nipo siriasi hata kwenye kula. Ni vema uwahi kusema ulichokusudia kuliko kuniacha au kuendelea kuniuliza maswali. Sitataja jina langu, wala hutojua nipo hapa kwa ajili gani,” Jamaa aliweka msisitizo kwa akifanyacho.

“Utakufa kijana,” Mkuu aliongea huku akiendelea kumwangalia kwa uangalifu yule jamaa.

“I was BORN TO DIE,” Jamaa alimjibu mkuu na kumuacha mkuu akiwa kinywa wazi bila kusema neno.

Maneno yale yalidhihirisha kuwa jamaa haogopi wala kuhofia jambo lolote litakalokuja kumtokea mbeleni.

“Nakuuliza mara ya mwisho. Wewe ni nani na nani kakutuma,” Mkuu aliuliza kwa hasira na mwenye sura iliyokuwa katika hali ya isiyo na utani ndani yake.

“Go to hell (Nenda kuzimu),” Jamaa alijibu kama kumnong’oneza lakini sauti yake ikiwa yenye kiburi na wingi wa ujasiri.

Mkuu yule alionesha ghadhabu zake moja kwa moja pale alipoepua birika lile lenye maji ya moto na kummwagia jamaa yule kifuani.

“Damn shit. You stupid,” Jamaa alitoa ukelele mmoja wa maumivu huku akirudi nyuma na kiti chake.

“Nakuuliza tena blood foolish, we ni nani na misheni yako ni nini,” Mkuu aliuliza kwa sauti ya juu huku bado hasira zake zikiwa kileleni.

“I was Born To die. Hata ufanye nini hupati kitu,” Jamaa alimjibu kwa sauti ya juu na ya maumivu kutoka mwilini mwake.

Mkuu kuona hivyo,akawaita wale wasaidizi wake na walikuja na kumkamata tena jamaa na kumvutia hadi pale mezani na mikono yake wakaiweka juu ya meza.

Mkuu wa sehemu ile akachukua uma kwenye kabati lililopo mle ndani na kisha akaanza kuirusha rusha na kuidaka huku akizunguka mle ndani huku na huko na maongezi yake yakiwa ya shari zaidi.

“Unajidai mgumu sana kijana. Leo tutaona. Na utakufa sababu ya ujinga wako,” Mkuu aliongea huku akimwelekea pale mezani na kumuuliza tena maswali yale yale.

“I was Born To Die (Nimezaliwa kufa)” Jamaa alijibu hivyohivyo kila alipoulizwa swali jambo lililompa hasira yule mkuu na kuwaambia wale wasaidizi wake waweke vizuri mkono wa kulia wa yule jamaa.

Alipoona mkono umekaa sawia, alinyanyua juu ile uma aliyokuwa nayo na moja kwa moja akaituliza kwenye mkono wa jamaa.

“Aaaagh.You fuckin, your hurting me motherf**** (Aaagh. We mjinga unaniumiza (Akatukana),” Jamaa alitoa kilio hicho kwa nguvu huku misuli yake ya shingo ikichomoza kwa sababu ya kujikaza wakati ile uma inaingia mkononi.

“Niambie wewe ni nani?”

“Nimekwambia sijui, nimezaliwa kufa.” Jamaa alijibu huku akilia kwa sauti ya juu.

“Mpigeni huyu. Mi nitarudi baada ya dakika kumi.” Mkuu aliwapa ruhusa wale wasaidizi na yeye akatoka nje.

Hapo hapo jamaa yule akaanza kupokea kipigo cha nguvu kutoka kwa wale jamaa watatu.

Waliompiga kichwani, walimpiga.Waliompiga mateke walimpiga, ili mradi walimpiga hadi akalegea na kushindwa hata kuongea.

Dakika kumi baadaye, mkuu alirudi na kumkuta jamaa kachakaa kwa damu na vimbe mbalimbali zikizidi kuongezeka katika mwili wake.

“Vizuri sana,” Aliwapongeza wale wasaidizi na kumfuata jamaa pale pembezoni mwa kona ya kile chumba alipokuwa amekaa.

“Sasa niambie. Wewe ni nani?” Swali lilelile liliulizwa.

Jamaa akamwangalia usoni na kutabasamu, tabasamu ambalo lililopotoka, lilitoka na michirizi ya damu mdomoni mwake.

“Unajisumbua tu!. I was Born To Die” Jamaa akajibu kwa sauti ya chini na kisha akamtemea mate yalichanganyikana na damu usoni kwa yule mkuu.

“Big mistake (Kosa kubwa)” Mkuu alitamka na kutoa bastola yake kisha akampiga usoni kwa nguvu kwa kutumia kitako kile cha bastola.

Uso wa jamaa ukachanika lakini ndio kama alikuwa amempagawisha mkuu.

Akampiga tena upande mwingine wa uso wake napo akapachana. Jamaa sasa akawa anavuja damu uso mzima zaidi ya mara ya kwanza.

“Tell me, who’re you? (Niambie,wewe ni nani?)” Mkuu aliuliza lakini hakupata jibu bali mihemo ya kasi kutoka kwa yule jamaa.

“I will kill you, blood foolish.(Nitakuua mpumbavu wewe)” Mkuu alimuonya huku akiikoki bastola yake na kumwekea kichwani.

“I was Born To Die. I’ve nothing to loose (Nimezaliwa kufa, sina cha kupoteza)” Jamaa alijibu kwa kulegea na taratibu akainamisha kichwa kwa ajili ya kuipokea ile risasi.

Mkuu naye akaanza kukibonyeza kile kifyatulio cha risasi huku akiwa makini asiifyatue hovyo huenda yule jamaa atasema chochote. Lakini hadi amefikia nusu ya ile triger, hakuna neno lililomtoka yule jamaa.

Kijana yule akainua kichwa chake na kumtazama kijakazi mmoja mle ndani ambaye alikuwa na rangi nyeusi kama yeye. Jamaa akatabasamu na midomo yake ikapepesa kwa kunong’ona neno “AFRIKA”.

Kijakazi yule alikuwa anamtazama na wakati huo mkuu wake anafanya maamuzi yake ya mwisho.

DAKAR-SENEGAL.

Ni furaha kubwa ndiyo ilitawala katika familia moja iliyoko nchini Senegal katika Jiji la Dakar. Jiji ambao lilikuwa Magharibi mwa nchi ile ndogo Kijeografia.

Familia hiyo iliyokuwa na watoto watatu, wawili wakiwa wa kiume na mmoja wa kike. Na pembeni ilichagizwa na wazazi wote wawili, walionekana hawana tabu wala tatizo na mtu.

Mzee Madira, ndiye hasa alikuwa kichwa cha familia ile yenye nyuso na taswira ambazo muda wote hutoshuhudia zikikosa amani kwa jinsi zilivyopambwa na ahueni ya maisha yao.

Nyuso ambazo kwa kuziangalia usingeweza kusema ipo siku kila kitu kitapotea katika maisha yao na kubaki historia huku mwili pamoja roho ya mtu mmoja, ikiwa imekandamizwa na chuki pamoja na kisasi juu ya nchi yake.

Kila mara Mzee Madira alikuwa karibu na watoto wake wa kiume, mmoja akiwa na miaka 20 (Ishirini) na mwingine miaka 24 (Ishirini na nne) hasa katika kuwajenga kifikra na kuwapa nasaba za maisha ambazo wazazi wengi wa Kiafrika inakuwa ngumu kwa wao kufanya hivyo.

Mtoto wa kike mwenye miaka 14 (kumi na minne) yeye alikuwa anadeka miguuni kwa mama yake huku akipewa mafunzo mbalimbali na mama yule aliyekuwa na asili ya kiafrika karibu kila matendo.

Alikuwa ni mama anayeijali familia, naweza sema anajali familia kuliko anavyojijali yeye. Anajua kwenda na muda wa mume wake pale anapotoka kazini, na alikuwa anajua ni kiasi gani wanawe wanavyojisikia pale wanapotoka kwenye shughuli zao kama elimu na shamba.

Mzee Madira, alikuwa ni mfanyakazi wa serikalini kwenye idara ya kilimo na chakula huku mkewe, Mama Madira akiwa ni mama wa nyumbani aliyeacha kazi kwa hiyari yake kwa ajili ya kuhudumia familia yake, iliyokuwa na mtoto mmoja wa kike ambaye alikuwa bado hajafikia umri wa kufanya kazi za nyumbani kama kupika na kupika deki nyumba yao kubwa, ambayo wazazi wa familia ile waliijenga kwa nia ya kuondoa usumbufu wa kuhama hama na kupangisha.

Mnamo mwaka huohuo, ndipo matokeo ya kijana wao wa pili kuzaliwa ambaye aliitwa Peter, alifaulu mitihani yake ya kidato cha nne. Na mwaka uliofuata aliendelea kidato cha tano na cha sita katika shule moja ya Sekondari iliyopo Mjini Thies, Kilomita chache kutoka pale Dakar.

Kaka yake yeye aliamua kujihusisha na chama cha siasa kimoja ambacho kilikuwa ni chama pinzani katika serikali ya kipindi kile.

Chama hicho kilijikuchulia umaarufu nchini kutokana na sera zake kuvuta wananchi wengi ambao kila mara walikuwa wapo mstari wa mbele kuchukia mambo yanayofanywa na serikali ya kipindi kile.

Mambo hayo ambayo wananchi walikuwa wanayakataa, ndiyo ambayo chama kile kilikuwa mstari wa mbele kuyafichua kwa kuyaweka hadharani. Kwa sababu hiyo, chama kilijikuta kikijizolea wananchi wazalendo pamoja na vijana wengi ambao ndio nguzo ya chama hicho siku zote.


Bruno Madira. Jina halisi la kijana yule aliyeingia kwenye siasa ndiye alikuwa mwanzo wa maumivu ya familia ile ya Mzee Madira.

Chama kile cha siasa kilikuwa kinafanya maandamano ambayo yalikuwa yanakatazwa mara nyingi na chama kilichopo madarakani. Kitendo hicho kilikuwa kinasababisha askari kukaa kitako kwa ajili ya kuzuia maandamano hayo ambayo yaliitwa maandamano yasiyo rasmi.

Kwa kuwa yalikuwa si rasmi, basi askari na vichwa vilivyopo madarakani vilichukulia matendo yale kama kuchochea vurugu katika nchi ile ambayo suala la utu hupotea kabisa linapokuja suala la ubinafsi.

Kila andamano likitokea, askari walikuwa mbele kuvuruga andamano hilo kwa njia ya amani au kwa kutumia nguvu ambazo wao waliona ndio suruhisho juu ya waandamanaji hao.

Haijulikani nia na mawazo ya chama kile pinzani, lakini hata viongozi wao walikuwa mstari wa mbele kuchochea maandamano hayo, na saa nyingine walikuwa ndani ya maandamano hayo.

Walikamatwa mara nyingi na kufunguliwa mashitaka kwa kufanya makosa hayo. Lakini kwa kuwa walikuwa wamejidhatiti kwa chochote, waliweza kujinusuru katika kitanzi hicho cha makosa.

Haikufahamika ni vipi waliweza kujikwamua katika makosa yale na wengine wakabaki wanasotea mahabusu kwa sababu yao. Lakini ukichunguza kiundani zaidi, siasa ilichukuliwa kama bahari au ziwa, na wakati huo wananchi wake wakiwa ni chambo.

Ukitaka upate samaki kwenye vyanzo hivyo vya maji, ni lazima utumie chambo kuwanasa.

Naam, wananchi wanatumika kama chambo katika kazi za kisiasa. Chambo ambao walikuwa wanamezwa na samaki wa nchi ile. Lakini samaki hao hao licha ya kumeza chambo, ndio hao pia waliokuwa wanatakwa ili wamilikiwe na wenye vyama.

Na ndio maana wao walitoka na wengine kubaki, na baada ya kutoka,waliwapa majina ya majigambo wale waliobaki wakiumia kule walipowaacha.

Majina hayo hayo, ndiyo yaliwavuta wengi wengine na kujikuta wanaingia katika kupigana na nguvu iliyokamata kila samaki, au tuseme kila idara kama hujanielewa. Idara hizo zilifinyangwa kwa mikono iliyo madarakani, kisha zikatupwa kwenye mifuko ya makoti waliyoyavaa na kujifanya ni zao.

Kitu pekee kilichokuwa mioyoni mwa wananchi wengi waliokuwa wanakamatwa na kusweka rumande, na wengine kuongezeka kila kukicha,waliamini kuwa wanatetea wanyonge.

Ndio. Wanyonge ambao walikuwa hawawezi kufungua midomo yao na kusema kinachowasibu katika maisha yao japo nchi yao ilieleweka ni nchi ya Demokrasia.

Wanyonge hawa hawa, ndio sababu ya wale wanao watetea kutokwa uhai wao na kusababisha maumivu na dhoruba katika familia waliyoiacha nyumbani.

Siku zote mtetezi wa wanyonge hawa uondolewa mapema ili nafasi ya mmnyonyaji ibaki kuwa nyeupe na kufanya mambo yake bila kizuizi kutokana na kuziba vinywa vya watetezi hawa.

Vinywa hivi vya wanyonge huzibwa mara moja baada ya kugundulika vinaziba nyanja nyingi zenye maslahi ya watu binafsi.

Mbaya zaidi pale vinywa hivi vinapozibwa na kupotezwa, basi hupotezwa pia na chimbuko lake. Yaani kama ukipotezwa wewe, basi ujue huku nyuma wewe utakuwa sababu ya wazazi pamoja na ndugu zako wa karibu kupotezwa pia.

Si kwa sababu naumia sana wakati naongea haya, ila kilichomkuta kijana mdogo kabisa Peter Madira, ndicho kilichosababisha sasa hivi usome mkasa huu wenye wingi wa masumbuko na matatizo katika nchi nyingi, hasa barani Afrika.

Wakati Peter Madira akiwa mkoani akiendelea na elimu yake, huku nyumbani mambo yalikuwa yanendelea kubadilika kila kukicha.

Watu wenye mamlaka yao nchini, walikuwa kila siku wanamfuata Mzee Madira na kumuonya kuhusu matendo ya mwanaye Bruno ambaye alikuwa hakosi katika maandamano ya chama kile kama yakitokea.

Sababu kubwa ya Mzee Madira kupelekewa malalamiko na maonyo hayo, ni kwa kuwa yeye alikuwa ndani ya idara muhimu ya nchi ile iliyotaka kuwekeza kwenye kilimo. Hivyo walimchukulia kama mwenzao.

Mzee Madira alijaribu kumuhasa mwanaye katika kila afanyacho, lakini kijana yule nadhani alikuwa kala kiapo cha kunywa nyongo juu ya chama kile. Kwani hakusikia mzee wake na wala hakuwa tayari kusikia ya yeyote kwa muda ule.

Walikuja mara kadhaa watu wale na kuendelea kuleta taarifa juu ya mwana yule, huku wakizidi kuleta maneno yaliyomfanya Mzee Madira kushinda kajiinamia kama ziwa la mama lililonyonywa kwa muda mrefu.

Uso ulimbadilika kila alipofikiria maneno ya maonyo ya wale watu, lakini mwisho wa siku aliamua kuukubali ukweli kuwa siasa ni mchezo tu!. Kushinda au kushindwa ni moja ya matokeo.

Lakini yule aliyeshinda au kushindwa ni lazima awe ameumia vya kutosha, ni vipi anaumia?

Tunarudi palepale kwenye kutafuta chambo na kuwaweka kwenye ndoano kwa ajili ya kujivulia madaraka.


Hatimaye ikafika siku ya siku ambayo nadhani ilikuwa ni siku mbaya katika familia ya Madira.

Bruno hakuwa mtu wa nyumbani tena. Maskani yake yalibadilika na kuwa sehemu nyingine ambayo ingekuwa rahisi kwake kushiriki maadhimio mbalimbali ya chama alichokuwamo.

Chama kilipanga maandamano mengine juu ya wenzao wa mkoa fulani kukamatwa na kuteswa bila hatia. Taarifa zilipowafikia wakuu wa chama kile, moja kwa moja zikatolewa taarifa za maandamano kufanyika nchi nzima katika muda na siku moja.

Taarifa zikafika kwa vijana wale waliopewa jina zuri litumikalo jeshini, MAKAMANDA.

Vichwa vyao vikajaa uchungu na maumivu tele mioyoni mwao baada kusikia wenzao mikoani wanatawanya kwa nguvu na askari, tena kwa silaha za moto.

Kesho yake wakanyanyua mabango na kuingia mtaa hadi mtaa na mwisho wake wakaishia katikati ya mji na kuanza kuhamasisha na kuelimisha wananchi juu ya mambo yanayofanywa na madaraka yaliyopo. Sura ziliwachachamaa na kuwa na hali ya kujiamini hadi hata pale askari walipotokea, waliona hamna wa kuwadhuru.

Nafsi zao zikachochewa na hamasa hiyo. Na sasa akili zao zikawa kama mbogo waliojiruhiwa. Wakaanza kutema cheche za maneno kuwaendea wale askari ambao walikuwa wameshikilia mitutu yenye risasi za moto pamoja na mabomu ya machozi na viunoni mwao wakiwa wamefunga mkanda wa marungu.

Cheche hizo zikafika mbali usawa wa petroli na kuigusa petroli ile. Moto ukaanza kuwaka. Hapo walikuwa wanagusa madaraka yanayowaongoza.

Bruno akiwa mbele kabisa ya mstari ule na kuonekana kama ndio kinala wa yale maandamano, alishtukia anapigwa risasi ya kifua tena upande wa kushoto, moyo ulalapo. Ikawa tafrani katika maandamano yale.

Huku Bruno akiwa anagalagala chini baada ya kupigwa risasi ile, waandamanaji wenzake walikuwa wanakimbia kama nyumbu waliyemwona chui anawamendea. Ni wachache waliobaki wakihangaika na Bruno hadi akawakatia roho mikononi mwao.

Hakuna aliyeelewa ni kwa nini ile risasi ilifyatuliwa. Hata yule aliyeifyatua, alikiri kuwa haikuwa dhamira yake kufanya vile.

Jeshi la polisi likaingia doa juu ya kifo kile cha kijana wa Mzee Madira. Mzee ambaye alikuwa tegemeo katika wizara ya kilimo na chakula katika nchi ile.

Ni vipi jeshi la polisi litasafisha doa lile? Swali likaja vichwani mwa wahusika na jibu likapatikana na kufika katika vyombo vya habari.

Jibu likakandamizwa ya kuwa yule aliyefyatua risasi alikuwa ndio katoka mafunzo ya kiuaskari karibuni. Na waliongezea kuwa alikuwa amemaliza kidato cha nne palepale nchini.

Wakasema watamfikisha mahakamani na kummvua kazi yake aliyokuwa nayo.

Baada ya taarifa hiyo, kesi ikapelekwa mahakamani lakini mwisho wa siku haikujulikana iliisha vipi na mtuhumiwa alienda wapi. Historia ya Bruno ikaishia hapo lakini ikabaki vichwani mwa familia yake.


Licha ya Mzee Madira kumsihi sana mkewe, lakini ikawa kama anampiga simba kwa kutumia nyama. Mama Madira akavaa kibwebwe na kuingia ngomani kuicheza ngoma ambayo ilimtoa uwanjani mwana wake.

Akawa kinara wa maneno juu ya madaraka yaliyokuwa yanawaongoza huku akibebea bango kitendo cha askari wa kidato cha nne ambaye yeye anasema alikuwa amepata daraja la nne ya pointi ishirini na nane (Division IV-28), kupewa bunduki na wakati wanajua ndio katoka katika mafunzo.

Hali ya uwoga anayo, na uzoefu mdogo wa mambo yale ungeweza kusababisha kilichotokea.

Maneno yote hayo, yalimtoka Mama Madira, mama wa mtoto aitwaye Marehemu Bruno Madira.

Licha ya Mzee Madira kumsihi sana mkewe,lakini ikawa kama anampiga simba kwa kumrushia nyama. Mama Madira akavaa kibwebwe na kuingia ngomani kuicheza ngoma ambayo ilimtoa uwanjani mwana wake.

Akawa kinara wa maneno juu ya madaraka yaliyokuwa yanawaongoza huku akibebea bango kitendo cha askari wa kidato cha nne ambaye yeye anasema alikuwa amepata daraja la nne ya pointi ishirini na nane(Division IV-28),kupewa bunduki na wakati wanajua ndio katoka katika mafunzo. Hali ya uwoga anayo,na uzoefu mdogo wa mambo yale ungeweza kusababisha kilichotokea.

Maneno yote hayo,yalimtoka Mama Madira,mama wa marehemu Bruno Madira.

Mapigano yakawa mapigano katika familia ile ya Mzee Madira. Kichwa cha nyumba kinakataa hili na Msingi wa nyumba hutaki kuelewa. Na chama kile alichoingia kwa kupenda sifa au labda niseme kwa kumwongezea hamasa,ikampa ukatibu wa chama kile kwa wakina mama. Chama kikazidi kumpa kichwa yule mama.

Maonyo yale yale kuhusu mwanaye Bruno,ndio hayo hayo yaliyokuja kwa Mzee Madira kwenda kwa familia,lakini kwa wakati huu yalikuwa kuhusu mkewe.

Mzee wa watu kama kawaida,uso ukamshuka zaidi ya pale na zaidi ya siku zote. Yote haya kwa sababu alielewa njama na nia ya siasa katika maisha haya.Kila alipojaribu kumwelimisha mkewe,ikawa kama anampigia mbuzi gitaa ili akate mauno.Haikuwezekana na kamwe haikuwekana hadi pale yalipotukia yaliyopaswa kutokea.

Maonyo yale sasa yakabadilika na kuwa vitendo.Vitendo ambavyo vilimfanya Peter Madira abaki bila familia,Peter akabaki yatima. Na si tu! Yatima bali mpweke katika dunia hii,hana nyumba wala sehemu ya kuishi,hana mali wala fedha za kusogezea siku zake ziende.

Ataishi vipi katika dunia hii ya leo ambayo fedha ndizo sabuni za nafsi na roho?.Ukiwa na fedha waweza kuamuru bahari ihamie Jangwani nayo ikatii.Ukiwa na fedha chochote kinakuja kwa wakati na kikiisha unaagiza kingine kwa gharama yoyote.

Sasa Peter Madira hayo yote kwake yakawa ndoto.

Ile elimu aliyokuwa nayo, ikakatikia hewani baada ya familia yake kuteketea katika tathinia ya filamu hii iitwayo siasa. Hakumaliza kidato cha sita Peter Madira kwa sababu ya vifo vya familia yake. Na kamwe hakuthubutu kupeleka uso wake kule walipokuwa wanaishi wazazi wake,kwani amri ilipita kwenye vinywa vya watu kuwa familia yote ya Madira iangamie.

Sababu kubwa ya familia kuangamizwa, ilikuwa ni chokochoko za watu hawahawa wanaokuvika madaraka.

Wakampa kiasi cha fedha mama wa watu, namzungumzia Mama Madira. Pesa hiyo ilitakiwa itumike katika mikakati ya chama hicho. Mwisho wa siku, fedha hizo zikakwapuliwa na watu wasiojulikana. Mbinde ikaanzia hapo.

Mama wa watu akashikiwa bango kuwa kala fedha zile kwa sababu ya kulipa kifo cha mwana wake. Hakuna aliyemuelewa pale alipojitetea,na hakuna aliyekataa pale yale maneno yalipotolewa midomoni mwa wakina mama wenzake ambao walikuwa wa kwanza kumfariji wakati wa majonzi juu ya mwanaye ,na walikuwa wapo mstari wa mbele kumshawishi ajiingize kwenye chama.

Na zaidi walikuwa wa kwanza kumnyanyua juujuu kama ngamia anavyonyanyuka baada ya kupandishwa mzigo.Hayo yote ni pale alipozawadiwa madaraka ya chama pale mkoani alipoweka maskani yake.

Haohao ambao walikuwa wanapiga mayowe na sifa kedekede ya kuwa wanawake wanaweza,wakiwezeshwa na huku wamempamba mama wa watu kwa mashada ya maua shingoni. Ndio haohao walilianzisha sokomoko juu ya mama yule kuwa kala fedha za chama zilizotolewa kwa ajili yao.

Mama wa watu akabaki kama bubu huku kaduwaa. Ni kama Yesu alivyokuwa mbele ya makuhani akisikiliza tuhuma zao juu yake. Na mama yule ilikuwa vivyo hivyo. Akitaka kujitetea, mwingine kamdaka kishika tonge chake na kuanza kuongea yeye.

Kila akitaka kusema,anakatwa sauti yake kwa kelele kutoka kwa wale wakina mama. Ikawa kama wanamsuta Mama Madira.

Akabaki uso chini huku mkono ukiwa kwenye tama. Hana mtetezi na anaona kama muda hauendi ili aondoke kwenye ule mkutano mdogo uliyoitishwa kujadili kuhusu fedha hizo ambazo wenye madaraka kwao waliziona kama vijisenti.

Ukimya wa mama yule na kujishika tama,akaonekana kama ana kiburi. Wakamnyanyukia na kuanza kumpiga kichwa kwa kidole cha shahada.Naweza sema walikuwa wanampiga masingi au wanamsokola kwa alichokifanya.

Kila mwanamke akapita mbele yake na kumsokola na kisha kwenda nyumbani kwake.Hapo ndio ukawa mwisho wa mkutano ule ambao ulimtaka alipe vijisenti vyote alivyobugia.


Hatimaye mama wa watu akarudi nyumbani na kumkuta mumewe akiwa anaangalia taarifa ya habari na mwanaye wa kike akiwa kajifungia ndani kwa sababu alikuwa na mitihani ya kidato cha pili.

Mama baada ya kugundua kafanya makosa kwa kutomsikiliza mume wake, alipiga magoti na kumwomba msamaha. Mume naye hakuwa mtu wa makuu, akamnyanyua kwa kumshika mikono yake na kisha kwa kiganja chake cha mkono wa kulia,akamfuta mtiririko wa machozi uliokuwa umemtoka mama yule.

Akamkumbatia na kumwambia asijali, kesho mambo yote yataenda kama yalivyotakiwa kwenda. Mume akampa moyo mke kuwa atazilipa fedha ambazo zimepotea katika mazingira ya kutatanisha.

Maneno hayo ya faraja kutoka kwa mume, yakawa kama yamesikiwa na vimbelembele wanaojidai wana uchungu na chama.

Usiku huohuo wakavamia nyumba ya Mzee Madira na kuizingira, kisha wakaanza kuvugumisha mawe kuelekea nyumba ilipo.

Ilikuwa ni tukio la kushtukiza sana kwa ile familia,lakini Mzee Madira alikuwa kama kishaota jambo hilo. Alishampigia simu Peter na kumpa wosia wa nguvu sana wa kimaisha. Hata yule mtoto wao wa kike waliyemuita Christina, siku hiyo walimkumbatia chumbani kwao.

Hata mawe yale yalipoanza kuvunja vioo vya nyumba ile, Mzee Madira aliwaambia watulie MUNGU afanye yake. Naam, Mzee Madira alikabidhi maisha yake kwa MUNGU.

Pale chupa zilizojazwa petroli na kuwashwa moto, zilipoanza kutupiwa ndani mwao,wao walizidi kujikumbata huku wakizidi kumwomba MUNGU labda atazinusuru roho zao. Lakini haikuwa hivyo, chupa zilizidi kudondokea maeneo yote ya nyumba na mwisho wa siku zilidondokea jikoni ambapo kulikuwa na majiko mawili ya gesi.

Huko ndipo kukawa kuna kizungumkuti na mshikemshike hasa pale mitungi ya gesi iliposhika moto na kuanza kuteketea na mwisho wa siku kutoa mlipuko ambao ulifumua hadi bati.

Ilikuwa kama filamu, lakini hayo yote yalitokea huku wahusika waliokuwa wanarusha makombora hayo, na ambao walishauvaa moyo wa mtoto wa shetani wakiwa wanashuhudia yote hayo.

Na hata yule mtoto Christina alipotoka nduki kwa uwoga wa ule mlipuko,walimkamata na kuanza kumfanyia vitendo visivyoweza kuvumilika na kila binadamu kuviangalia.

Lilikuwa ni jopo la wahuni likifanya yote yale. Nyumba ikiwa inateketea kwa moto, Christina alikuwa kalazwa chini na kila mhuni alikuwa anamwingilia kimwili apendavyo.

Christina alifumba macho kwa maumivu ambayo hakuwahi kuyapata tangu anazaliwa. Pale alipoyafumbua macho yake, aliyafumbua kwa nguvu zote kana kwamba kaona kitu cha kustaajabisha, lakini haikuwa hivyo.

Alikodoa macho yake kwa nguvu kwa kuwa alikuwa kaingiziwa kitu kama kisu kwenye sehemu zake za uzazi. Mtu aliyefanya hivyo, hakuwa anahuruma. Alilarua kwa nguvu sehemu ile na kufanya kizazi cha mtoto yule mdogo kutoka nje. Ndio, alichana sehemu za siri za mtoto Yule mdogo.

Haikuwa kazi ndogo kwa Christina kubania pumzi ili imfikishe hata dakika mbili. Haikuwa kazi ndogo hata kidogo, nasema hata kidogo kwa msisitizo kwani Christina alikufa palepale huku nyumba ya wazazi wake ikiwa inamalizikia kuungua.

Hata Askari walipokuja kuhakiki maafa yale, waliambulia maiti tatu kama walivyotegemea. Mbili zikiwa zimekumbatiana lakini zikiwa nyeusi kwa kuungua na nyingine ikiwa nje haitamaniki, kwani mbwa nao walipita na kunyofoa baadhi ya viungo vya binti yule na kufanya kifungua kinywa.

Mwisho wa familia ile yenye furaha ukawa umefungwa kwa machungu hayo. Japo vilio vilikuwepo, lakini kama ukivipima vilio hivyo katika mzani wa moyo wa Mwenyezi MUNGU, sidhani kama vilikuwa vya kweli.


Peter alipata taarifa za vifo vya watu wake wa karibu, na kama jana yake alivyoongea na baba yake, hakuthubutu kugusa maeneo yale ambayo wazazi wake walikuwa wanaishi naye hapo mwanzo.

Kitu cha msingi alichokifanya Peter ni kuacha kabisa shule na kutokomea mbali na pale alipo,kwani kulikuwa hakuna wa kumwamini tena. Pesa ingetembea na yeye angechomewa utambi na kufanywa kama walivyofanywa wengine katika familia yake.

Pesa ambazo baba yake alimwingizia kwenye akaunti yake ya simu, alizitoa haraka kabla hazijafungiwa kwa sababu mikono inayomtafuta, imekanyaga na kusigina idara zote kama nilivyosema hapo mwanzo.

Umuhimu wa simu, ukawa haupo tena. Utauona vipi umuhimu huo kama watu wako muhimu wote wameteketea. Na hata hao rafiki ambao unawaamini tayari walishakuwa mfano kupitia mama yako, utaanzia wapi kuwapa nafasi na kuwaelezea shida yako?

Peter akasimama peke yake na kufuta chiozi lililokuwa linamtoka juu ya familia yake. Alitamani kulipa kisasi lakini alikumbuka maneno ya mwisho kutoka kwa baba yake kuwa hapaswi kumlaumu mtu bali anachotakiwa ni kuangalia maisha yake. Baba yake alimsisitizia kuwa haina haja ya kisasi bali msamaha kwa alichokiona.

Licha ya hayo yote, baba yake alimpa akili ya maisha ili ajikwamue pale alipokwama.Hakuacha kamwe kumwambia akae mbali na siasa ambazo yeye aliziona ni mchezo,tena mchezo wa kula uliwe.

Kula uliwe ni mchezo mchafu kabisa ambao unapingwa vikali na serikali za nchi nyingi duniani.Sasa mchezo huo Mzee madira anaufananisha na siasa.

Peter alijikuta anatabasamu mwenyewe pale alipokumbuka kitabu alichokisoma kidato cha nne.Kiliitwa An Enemy Of The People.

Watu waliiponda nyumba ya bwana yule waliyemuita adui wa watu.Namzungumzia Daktari Thomas. Aliitwa adui wa watu katika jiji ambalo alikuwa anaishi, lakini ukweli ni kwamba ni kwa sababu alisema ukweli.

Ukweli huohuo alioungea Daktari Thomas, ndio ambao Peter Madira aliufananisha na wa mama yake alivyokuwa anauropoka, na ndio huo ulichukua uhai wake.

Peter akakumbuka maneno ya mwisho aliyoyasema yule aliyeitwa adui wa watu kuwa, Dokta Thomas.

“A strongest man, is the one who stands alone”,yaani mtu shupavu,ni yule awezaye kusimama peke yake.

Akatabasamu kidogo baada ya maneno hayo na kisha akafuta tena machozi ambayo yalikuwa yakimtoka. Hapo hakuwa Peter tena,bali akawa binadamu shupavu ambaye anataka asimame peke yake.


Peter Madira akamuua kujichimbia zaidi mikoa mingine ya kule Senegal. Akaingia ndani zaidi hadi Kegougou, mji uliopo Kusini Mashariki mwa nchi ile. Ikiwa ni kilomita chache kuingia kwenye mpaka kati ya Senegal na Guinea.

Huko akaanza maisha upya huku akitafuta nafasi ya kujiendeleza zaidi kifikra kuliko kimasomo hasa ukizingatia urefu wa elimu yao.

Elimu yao ilikuwa ni ndefu na haina malengo katika anayeichukua. Unaweza kusoma masomo ya sayansi kidato cha nne lakini kidato cha sita ukajikuta upo katika masomo ya sanaa. Na baadaye ukiingia chuo, unapangwa kwenye kitengo ambacho hukuwahi kukifikiria katika maisha yako.

Peter hakuwaza hilo tena. Japo alikuwa anafedha kidogo, aliamua kujiendeleza katika mambo ya teknolojia ambayo ndiyo yalikuwa moyoni mwake.

Kule alipotoka, walikuwa hawana habari naye tena, hivyo waliamua kuacha kabisa mawazo ya kumfatilia kijana yule.

Sehemu mpya aliyokuwepo Peter, kukawa ni ahueni kiasi kwani hakufatiliwa. Lakini ahueni hiyo haikuwa pande zote za maisha yake. Pesa alizokuwa nazo, zikajichimbia kwenye mifuko ya wengine kwa yeye mwenyewe kuwalipa.

Alipanga chumba na kununua baadhi ya vitu muhimu vya ndani. Akaanza kujisomesha mambo ya teknolojia hasa kwa kutumia kompyuta.

Kuja kushtuka, kiasi kikubwa cha fedha kikawa kimepotea kwenye mambo hayo.

Lakini alishukuru MUNGU kwani ada ya elimu ile, aliimaliza yote na kodi ya nyumba ilikuwa inaweza kumfikisha hadi mwisho wa elimu yake akiwa palepale. Tatizo likawa ni wapi atapata chakula na hela ya usafiri.

Hapo mawazo yake yakarudi enzi zile wakati anaishi na familia yake. Alikuwa anakula na kusaza, anaenda anapotaka bila shida. Magari yalikuwepo na hela ya usafiri au mafuta ilikuwepo. Sasa hivi hata kupata mlo mmoja wa kubangaiza, kwake ikawa shida. Usafiri ukawa miguu yake. Ilimlazimu atembee kilometa nyingi ili kwenda alipokuwa anasoma.

Muda wa kuondoka kwake ukawa ni saa kumi za alfajiri na kufika asomapo ni saa mbili asubuhi. Akiwa hajala na mwenye kuchoka, analazimika kuingia darasani ili afanye kilichompeleka.

Kitu cha msingi ambacho Peter alikuwanacho tangu zamani, ni kujiweka safi. Peter alikuwa msafi wa mwili na pia mavazi. Ukichanganya na rangi ya maji ya kunde pamoja na tabasamu lake, huwezi kujua kama kijana huyu katembea kwa miguu kilometa kadhaa tena kwa masaa karibu matatu. Shida zikafichwa na muonekano wake, na maisha yakaendelea.


Wapo marafiki aliowapata Peter kipindi chote wakati anasoma masomo yake, lakini hakuwahi kuwaambia ukweli kuhusu maisha yake ya nyuma na kizuri zaidi hakuna aliyemfatilia.

Peter akawa huru kwa kila kitu akifanyacho ila hakusahau yaliyotokea katika maisha yake.

Hali ya kukaa na njaa pamoja na kutembea mwendo mrefu, ikaanza kutengeneza maswali katika vichwa vya marafiki aliokuwa amejijengea hasa pale mwili wake ulipoanza kupungua. Kila mmoja alijiuliza lakini hakuna aliyepata jibu.

Kila siku Peter alikuwa wa kwanza kwenda pale shuleni, lakini kila siku alikuwa wa mwisho kuondoka. Hiyo yote ni sababu hakutaka kuonekana na watu kama anapiga kiatu hadi anapoishi.

Wapo waliotamani kujua kwa nini Peter mwili wake unakuwa vile, na wapo waliotamani kujua mwisho wa Peter utakuwa ni nini. Hata wakufunzi waliokuwa wanamfunda katika masomo yake, walikuwa wanahamu kubwa ya kujua nini kinachomsibu,lakini hawakuthubutu kufungua kombe lao na kuweka kiulizo kwa Peter.

Kuna watu wengine wao walivutiwa na Peter japo walishindwa kwenda kumwambia moja kwa moja kwa sababu ya muonekano wake. Peter alionekana kama hana shida, hivyo iliwapa ugumu wale watoto wa kike kwenda kueleza hisia zao juu yake.

Mwili wa Peter kupungua, ikawa ni chanzo cha wenye hisia naye kuanza kuumia juu ya hilo.

Wakataka kuchimbua ukweli juu ya upungufu wa mwili ule ambao hapo mwanzo ulikuwa ni kivutio kikubwa katika mboni na kope za macho yao.

Vanessa Gomez. Binti wa tajiri mmoja wa Kihispania aliyekuwa ndani ya mahaba mazito juu ya Peter na siku zote alikuwa amepania kumwambia Peter juu ya hali hiyo.Lakini kesho ilipofika, miguu yake ilikuwa migumu na mizito kumuendea Peter. Ni kama chuma kinachong’ang’ania kutoka kwenye sumaku jinsi alivyokuwa pale alipomuona Peter.

Binti akajiona kweli alikuwa mdhaifu, akakaza moyo na kwa kuupiga konde huku akijisemea ipo siku.

Na kweli siku na siku zikapita, hatimaye mabadiliko ya mwili wa Peter yakawa yanamuumiza zaidi Vanessa. Ikabidi siku hiyo baada ya kumaliza vipindi, akatoka nje na kuwahi katika gari lake aina ya Rav 4 kisha akawa anamsubiri Peter ili amfatilie kwa nyuma hadi ajue anapoishi.

Huko ndani Peter alihakikisha kuwa wanafunzi wenzake wote wameondoka, ndipo naye kiunyonge akakakusanya vifaa vyake na kutoka nje, wakati huo kigiza cha saa moja ndicho kilikuwa machoni mwake.

Peter aliangaza huku na huko kuona kama kuna wanafunzi wanaomfatilia, naye alipoona hamna alianza safari yake taratibu kuelekea eneo ilipo barabara kuu.

Ndani a Rav 4, Vanessa alimuona Peter akielekea barabarani, hivyo moja kwa moja alijua anafata usafiri utakaompeleka anapoishi.

Mtoto wa kike akatekenya swichi ya gari yake kwa kutumia ufunguo. Taratibu akaingiza gia namba moja na kuanza kuelekea Peter alipokuwa anaelekea huku macho yake yakiwa makini ili yasimpoteze kijana yule.

Kinyume na mategemeo yake labda Peter atakaa kwenye vile vijumba vya barabarani kwa ajili ya kusubiria usafiri wa kumpeleka kwake, alimuona Peter akipita kile kinyumba na kuanza kunyoosha barabara.

Kila dakika Peter alizidi kuongeza mwendo na wakati huo alikuwa hajui kama anafuatiliwa na mtu ambaye anahisia kali za kimapenzi juu yake.

Vannesa alianza kustaajabu pale alipomuona Peter anaanza kutimua mbio huku madaftari yake akiwa kayashika vizuri kwa mkono wake wa kushoto. Kila Peter alipozidi kwenda mbele, ndipo kasi yake ya kukimbia ilizidi kuongezeka.

Vanessa naye alipoona hivyo, akakanyaga mafuta kiasi na kuongeza gia na kufika namba tatu. Hata pale Vanessa alipomfikia Peter, yeye Peter hakujali wala alikuwa hafatilii kama lile gari la pembeni yake.

Alichojua Peter, lile ni gari kama magari mengine hivyo yeye alijali mbio zake baridi. Yaani mbio zisizo na ushindani.

Ni hapo ndipo Vanessa aliamua kupiga honi ya gari lake kwa ajili ya kumtoa mawazoni Peter juu ya mbio zake.

Peter alisimama na kuangalia vizuri ndani ya gari lile, nalo baada ya kusimama usawa wake. Sura aliyoiona, haikuwa ngeni kwake wala hakuwa na swali la kuuliza wewe ni nani. Alichofanya ni kama kuishiwa nguvu kutokana na mtu kujua, tena mwanamke kujua kuwa siri yake ya kutembea kwa miguu.

“Hey Pity. Mambo vipi?” Sauti yenye ucheshi na wingi wa furaha, ilimsabahi kijana wa watu baada ya kioo cha gari ile kufunguka.

“Fresh. Nambie dada,” Peter naye alimjibu kwa sauti ya unyonge.

“Cool. Ingia basi ndani ya gari.” Vanessa naye alijibu salamu ya mtanashati yule huku akimfungulia mlango wa kushoto kwa ajili ya kuingia.

Peter alijua tayari kishauvagaa, kama aibu tayari ishamkumba hivyo aliona ni kheri akubaliane kuingia ndani ya gari labda angeweza kumwomba yule dada amfichie siri hiyo.

“Usijali Pity. Ni mimi pekee nayeweza kutambua shida zinazokusibu kwa wakati huu na kuzitatua kama utanipa nafasi hiyo. Ondoa shaka na aibu kwa sababu yangu.” Aliongea Vanessa baada ya kugundua hali aliyokuwa nayo Peter.

“Nimekuelewa. Kwa hiyo labda unataka nini sasa kwa sababu kama ulivyoniona, ndio nilikuwa nimekaza mwendo kuelekea nyumbani,” Peter aliongea huku akipotezea yale maneno mengine ya yule msichana kuhusu kusaidiwa.

“Unakaa wapi Pity,” Vanessa alimuuliza.

“Never mind (Usijali),” Peter alimjibu kifupi na kukaa kitako kwa ajili ya kufungua mlango na kutoka.

“Pity, please don’t (Pity, tafadhali acha),” Vanessa alimsihi Peter asifanye atakacho kukifanya.

“Okey. Niambie sasa shida yako dada,”.Peter aliongea kidogo kwa hasira na kwa sauti ya juu.

“Nataka tusaidiane Pity. Najua unashida, huu si mwili wako Pity.Please nipe nafasi,” Aliongea Vanessa kwa hisia zilizotoka ili kumchoma Peter na ajue umuhimu wake kwa wakati ule.

“Huwezi kunisaidia dada. Mimi si wa kusaidika, mtaniua nyie,” Aliongea Peter huku macho yake yakianza kupoteza rangi nyeupe na kuamia wekundu.

“Pity, jaribu kwangu. Naomba uniamini kidogo tu!” Aliongea Vanessa wakati huo gari lilikuwa pembeni mwa barabara na kuachwa likitoa mngurumo mdogo wa kupasha injini.

“Binadamu haaminiki dada. Wewe niache mimi niende zangu tu! Maana sioni sababu ya msingi kuwa humu kwenye gari lako.” Aliongea Peter lakini maneno yale yalikuwa kama yanaongeza chachu katika kachumbari.

Yalimfanya Vanessa achangamke zaidi na kuendelea kubembeleza ili mtoto yule wa kiume amuelewe.

Hatimaye Peter alikaa kimya na kusikiliza nia ya dada yule huku moyoni akijua labda malaika kamshukia kweli safari hii.

Kesho yake asubuhi na mapema, alikuwa tayari shuleni na wakati huo alikuwa anamwona Peter akishuka kwenye usafiri wa umati (Mfano: Daladala). Na baada ya kushuka alimwona anaelekea darasani huku akiwa katika mavazi yake nadhifu.

Vanessa naye alishuka katika gari lake na kuanza kuelekea alipokuwa anaelekea Peter.

“Hey Pity. Mambo vipi?” Vanessa alimmwita Peter na kumsalimia huku akimshika mkono.

“Poa, niambie Vanessa,” Peter alijibu salaam na kutoa salaam pia.

“Mmmh, ni poa. Ha haa,” Alijibu Vanessa akiongeza na kicheko kitamu huku mabega yake kayapandisha juu na mwili wake akiuzungusha zungusha kana kwamba anaona aibu.

“Nadhani jana ulifika salama nyumbani. Au nadanganya Vanessa,” Alisaili Peter.

“Salama sana na nililala vizuri mno.” Alijibu Vanessa na kisha walianza kwenda walipokuwa wanasomea.

“Haya bwana, sitaki kuuliza sana kwa nini ulilala vizuri,” Peter aliongea huku ametabasamu na macho kayaelekeza mbele bila kumwangalia Vanessa ambaye alikuwa anatamzama huku akishindwa kumtathimini Peter ni mtu wa aina gani.

“Najua hutaki kujua kwa sababu wewe ndiye sababu ya mimi kulala vizuri,” Vanessa naye alimjibu huku akizidi kwenda mbele na kuongeza utamu katika maneno yake.

“Ha ha haaa, nilijua utasema hivyo. Asante Vanessa.” Peter aliongea huku anamwangalia Vanessa usoni kwa tabasamu pana.

“Asante ya nini sasa,” Vanessa naye aliuliza huku pia ametabasamu.

“Ya mimi kuwa usingizi wako. Au haupendi hiyo asante,” Peter alijibu huku anashika kitasa cha mlango wa darasa wanalosomea.

“Mmmh, haya bwana. Basi leo tuwahi kutoka ili twende mahala tukaongee.” Alisema Vanessa na bila hiyana Peter alikubaliana na maneno yale huku akiwa makini sana yasije yakamtokea puani.

Waliingia darasani na kila mmoja alienda kukaa kwenye kompyuta anayotumia kila siku na kisha masomo yakaendelea hadi mida fulani ya mchana ambapo walitoka kwa ajili ya kumpumzika lakini kwa upande wa Peter na Vanessa, huo ndio ulikuwa mwisho wa vipindi vyao.


Walikuwa kwenye hoteli moja ndogo iliyopo mjini pale wakiwa wanajipatia chakula, ndipo Vanessa alipofungua mdomo wake na kuanza kuelezea maisha yake binafsi jinsi yalivyoenda.

“Peter. Nadhani wewe utakuwa ni mtu wa kwanza kusikia historia yangu ya maisha nikiwa na wazazi wangu. Namaanisha wewe ni mtu baki wa kwanza kujua historia yangu. Hiyo ni kwa sababu nataka kujua yako pia. Hii itaisaidia tuweze kuaminiana katika maisha haya.

Sina wa kumuamini katika mazingira haya. Ila kwa kuwa moyo wangu upo juu yako, nataka ujue haya nitakayokwambia,” Vanessa alianza hivyo na kuweka kituo kidogo kabla hajaendelea kuongea.

“Maisha yetu yamekuwa ni kuhama-hama. Mara ya kwanza tulianzia Kongo kuishi, huko baba akafanya kazi zake na kisha baada ya kuona yamekamilika, akahamia Naijeria na baadaye ndio tukaja huku.

Maisha yetu yamekuwa hivyo kila kukicha, na sasa anampango wa kuhamia Afrika mashariki na mara nyingi anapenda kwenda zile nchi zenye machafuko na vita. Huko kwake inakuwa rahisi kufanya anachotaka.” Peter akadakia na kumuuliza swali la kazi anayofanya baba yake.

Vanessa akaguna kidogo na kisha akamjibu Peter.

“Yeye anasafirisha malighafi za huku kama vile madini, meno ya tembo na ngozi za wanyama.” Aliongea Vanessa kumjibu Peter.

“Sasa kama kazi yake ni hiyo, kwa nini anachagua nchi zenye vita?”Peter alimuuliza tena Vanessa.

“Kule anasema kunakuwa hakuna ulinzi sana wa mali hizo kwa sababu wanakuwa wanawaza vita zaidi,” Vanessa alimjibu Peter lakini Peter alijua kuna la ziada kutoka katika kazi ile ya Baba wa Vanessa.

“Kwa hiyo baba yako akichukua mali hizo anapeleka wapi?”Peter aliuliza tena.

“Baba ni Muhispania lakini yupo karibu sana na Marekani, hivyo mali hizo anawauzia hao.” Vanessa alimjibu Peter na kumuacha atafakari yale majibu kwa muda.

“Mmh! Okay. Kwa hiyo uanataka kunimbia nini Vanessa,” Peter alisaili tena.

“Nachotaka ni wewe uniambie kinachokusibu. Huu kijana mdogo sana lakini yaonekana huna msaada wa karibu hasa wa wazazi. Hiyo ni sababu nilikuona jana unatembea kwa miguu. Nakuomba Pity, niambie ili tusaidiane,” Vanessa aliongea kwa msisitizo na kumwacha Peter akiwa amemkodelea macho bila majibu.

“Pity, niamini japo kidogo tu! Na hutojuta kuniamini. Tafadhali nakuomba.” Aliweka msisitizo Vanessa ili amvute Peter.

“Hivi wadhani yawezekana kweli kwa siku moja tu! ya urafiki wetu nikuamini hivyo Vanessa?” Aliuliza Peter kuonesha mashaka yake juu ya kitu akitakacho Vanessa.

“Pity, hakuna kitu kinachoitwa siku moja katika uaminifu. Hamna Peter nakataa. Kuamini ni hali ya moyo tu!,ila kama moyo wako haujaamua kuniamini, ni sawa tu, na wala usitie shaka.” Aliongea Vanessa na kumuacha Peter aendelee kuburudika na kinywaji alichoagiza.

Maneno ya mwisho kumtoka baba yake wakati anaongea na Peter, aliongelea sana kuhusu kuuamini mtu. Baba yake alimuhasa sana kutomuamini mtu ambaye hamjui, si kwa kuwa hamjui tu! Bali hata yule wa karibu.

“Hakuna mtu mbaye katika maisha haya aliyekaribu yako Peter. Siku zote hujiweka karibu ili ang’amue jambo toka kwako. Na watu hawa huwa wasafi katika ndimi zao na wenye kujua kutunga hadithi ambayo itakufanya nawe uweke hadithi yako hadharani.

Hapo tayari utakuwa umeishanasa pale mtu huyo atakapoamua kuitumia hadithi kukuumiza.” Peter alijikuta anakumbuka maneno ya baba yake na yeye mwenyewe alijihisi kutotaka kumwambia chochote Vanessa hasa historia yake ya nyuma.

“Nitapenda twende kwako sasa Pity, maana nina hamu kweli ya kujua chumba chako kilivyo.” Aliongea Vanessa na kumtoa katika mawazo marefu Peter.

“Okay. Vanessa. Nadhani tayari nipo safi. Twende zetu.” Aliongea Peter na kunyanyuka kitini ambapo alifuatiwa na Vanessa ambaye alitoa kiasi cha fedha ya vinywaji alivyotumia na kuiacha pale mezani.

Walienda moja kwa moja kwenye gari la Vanessa na kukwea tayari na safari ya kuelekea anapoishi Peter.

Ilikuwa ni safari ya ukimya mkubwa hasa ukizingatia walikuwa hawajazoena sana wale wawili waliokuwamo ndani ya gari lile.

Hadi wanafika maskani kwa Peter, hakuna aliyekuwa amemsemsha mwenzake zaidi ya mngurumo wa gari na tairi zake zikisemeshana na barabara.

“Waaou, Pity we ni msafi kwa kweli. Look at your room.” Aliongea Vanessa baada ya kuingia ndani ambapo alikuwa akipepesa-pepesa macho akivinjari muonekano wa chumba cha Peter.

“Asante Vanessa. Karibu sana kwangu napoishi.” Alimkaribisha Peter.

“Asante Pity.” Alishukuru Vanessa huku anakaa kwenye kitanda cha Peter.

“Waaou, Pity we ni msafi kwa kweli. Look at your room,” Aliongea Vanessa baada ya kuingia ndani ambapo alikuwa akipepesa-pepesa macho kuvinjari muonekano wa chumba cha Peter.

“Asante Vanessa. Karibu sana kwangu napoishi,” Alimkaribisha, Peter.

“Asante Pity.” Alishukuru Vanessa huku anakaa kwenye kitanda cha Peter.

“Wale ni wakina nani, Pity,” Alisaili Vanessa baada ya kuona picha moja ikiwa ukutani.

“Hiyo ni familia yangu. Huyu ni mama yangu, huyu baba na huyu ni kaka na dada yangu.” Alijibu Peter baada ya kuitoa picha ile ukutani na kwenda nayo pale alipokuwa amekaa Vanessa.

“Safi sana, na wewe upo wapi sasa,” Aliuliza tena Vanessa.

“Mimi ndiye niliwachukua picha hiyo kama ukumbusho wakati naelekea shule kuanza kidato cha tano,” Alijibiwa Vanessa.

“Kwa hiyo sasa hivi ndio upo kidato cha sita au?” Vanessa akazidi kuuliza maswali ambayo kiasi fulani yalitaka kumfanya Peter amwambie historia yake.

“Hapana Vanessa. Walifariki wote hao, na mimi ndio ukawa mwisho wa Elimu yangu.” Peter akajibu kiunyonge.

“Dah! Pole sana Peter. Usijali tupo pamoja,” Vanessa alimfariji Peter.

Kimya kitanda baina yao.

Ni mapigo ya moyo ya kila mtu ndio yalisikika kwa muda ule. Kulikuwa hakuna soga iliyokuwa inaendelea zaidi ya Vanessa kuwa anakitazama chumba kile na kutabasamu peke yake.

Peter alikuwa kimya muda wote akimwangalia Vanessa anachokifanya. Lakini macho yale ya Peter hayakuwa yakimtazama tu! Mwanadada yule aliyekuwa kabarikia urembo halisi wa kuzaliwa nao. Bali macho yake yalikuwa yakimtazama kwa sababu alikuwa kazama ndani ya fikra juu ya maisha yake endapo atamwambia dada yule.

Fikra zile zikampeleka mbali zaidi na kuyakumbuka maneno mengine ya baba yake.

“Angalia roho yako kama ipo sahihi kwa ukifanyacho. Ni roho pekee ndiyo itakufanya ujue kuwa hili ndilo ama hapana. Najua wajua kuwa huwezi kumtambua mtu kwa kumwangalia, lakini kuna muda roho ndiyo inakuongoza kumtambua mtu huyo.

Jali sana maamuzi yako kutoka nafsini kuliko kushinikizwa. Japo nimekwambia kuhusu kutomwamini mtu, lakini sijakwambia usimwamini mtu kabisa. Angalia roho na nafsi yako inataka nini. Kama utampata ambaye unadhani anafaa kupewa siri zako, mpe nafasi hiyo akutambue lakini uwe macho katika matendo yako. Kamwe usijejutia maamuzi ya nafsi na roho.”

“We Pity mbona hivyo?”Alishtushwa Peter toka katika mawazo yale na Vanessa, ambapo alikuwa anakumbuka maneno ya mzee wake.

“Kwani vipi Vanessa?”Peter naye akajidai hajui alichofanya.

“Yaani nimekuita karibu mara tano lakini wanitazama tu. Una nini Peter?” Vanessa aliuliza kwa uchungu jambo lililomfanya Peter ajione mwenye makosa kwa kumfanya dada yule aumie kwa hisia anazosababisha yeye.

“Vanessa, kaa tambua katika haya maisha kuna wanaoishi na waishio tu. Mimi ni mmoja wa watu tuishio hapa duniani. Yaani namaanisha, wale wanaoishi wanajua nini wanafanya lakini sisi tuishio,ni bora liende tu!

Sitaki kukuweka katika koma juu ya maneno yangu ila kaa ukijua kama kuna binadamu anawindwa, basi mimi ni mmojawapo,” Peter alikata shauri na kumweleza ukweli Vanessa mambo yanayomsibu huku akijisemea moyoni ya kuwa labda huyu atanisaidia.

“Familia yangu yote hii uionayo, imeteketea kwa sababu ya tamaa na chuki za watu binafsi ambao hawapendi kamwe kumwona binadamu mwenzao anafanikiwa.

Kaka yangu aliteketea kwa kupigwa risasi ya kifuani na askari wakati wa kuzuia maandamano ya chama kile cha siasa ambacho sasa hivi ndio kinapewa nafasi kubwa ya kuchukua madaraka.

Nilimzika kaka yangu kwa machungu huku nikiwa na kisasi toka moyoni na njia ya kutimiza kisasi hicho, niliona ni bora nisome kwa bidii ili niweze kufaulu na kwenda kusomea mambo ya sheria ambayo ningetetea wanyonge wote wanaoangaika kwa wakati huu na ujao.

Askari aliyebeba msalaba wa kumpiga risasi kaka yangu, haikufahamika aliishia wapi. Hali hiyo ikampa hasira mama. Naye akaingia kwenye siasa kwa kutumia chama kilekile.

Haikuchukua muda, naye wakamfunga mdomo wake na si yeye tu! Bali familia yangu yote ikatekezwa kwa moto ndani ya nyumba yetu huku mdogo wangu huyu wa kike, akibakwa na kuchanwa kizazi chake kama ndafu ya mbuzi.

Na magazeti yalivyo mashenzi kupindukia, yakaiweka picha ya mdogo wangu jinsi alivyo, tena ukurasa wa mbele. Hii hapa na hii ndiyo nyumba walimofia wazazi wangu.” Peter aliongea kwa uchungu, machozi yakiwa yanataka kutoka lakini akayazuia, na wakati huo anamkabidhi vipande vya magazeti kadhaa Vanessa.

“Pity. Unahitaji kutoa chozi juu ya hili. Nakuomba utoe chozi Peter, liache lidondoke.” Vanessa aliongea huku akimwangalia Peter ambaye alishindwa kuvumilia na kujikuta analia kwa sauti na uchungu mkali wa maumivu juu ya familia yake.

Alijitahidi sauti ile isitoke nje hivyo alilalia tumbo na mdomo wake akang’ata mto na kulia kwa nguvu sana.

Ni muda ambao Vanessa alionesha ujasiri wake kwa kutotoa chozi lolote bali kumnyanyua Peter kichwa chake na kisha akakiweka mapajani kwake na kuanza kumfariji kwa kuzirudisha nyuma nywele fupi za Peter huku Peter akiendelea kutoa kilio cha kwikwi.

“Leo hii mimi nasakwa pia niuawe na watu walewale walioiondoa familia yangu duniani. Kila mmoja pale nilipokuwa nasoma, alikuwa ananiangalia kwa kunitamani kama mnofu mbele ya simba. Kila mmoja aliniona mimi dili. Nikipatikana hai au mfu, zawadi itatolewa. Mimi nikawa wa kuchezewa bahati nasibu katika tumbo la nchi yangu. Kweli nimekuwa sandakalawe kwenye nchi yangu?” Peter aliongea kwa unyonge huku kalala majapajani kwa Vanessa baada kumaliza kilio chake.

“Pity. Hakuna anayejali thamani ya utu zaidi ya MUNGU. Siku zote watu huwa na utu kwa sababu wanajua MUNGU anawaona. Lakini kama wangeambiwa MUNGU hayupo, nadhani hakuna ambaye angekuwa hajamtoa mtu uhai wake.

Kila mtu ana-mabaya na machafu anayoihitaji kuyatimiza. Hapa kwenye gazeti naona wanamsifia mama yako katika kukiendesha kile chama kwa nidhamu. Hichi kitu ndicho kilitokea kwa mama yangu pia.” Aliongea Vanessa huku akiendelea kuzishika nywele za Peter.

Ghafla aliziacha nywele zile na kuangalia juu kama anakumbuka kitu fulani ambacho kakisahau.

“Kuna watu katika hii dunia ni wanafki sana. Wanajidai wao ni marafiki lakini ndio wenye chuki na roho ililotukuka kwa virusi vya uadui. Siku zote hukufuta machozi uliapo na wanakunyanyua pale ulipodondoka, lakini wakiwa na lengo moja tu! La kutaka kukujua wewe ni nani ili wakuangushe. Hao mimi nawaita mapanya buku, wanaong’ata huku wanakupuliza.

Ni kheri ukutane na simba ambaye unajua atakutafuna papo hapo kuliko ukutane na panya buku hilo. Ipo siku nitarudi na kumtafuna mzima mzima yule mshenzi wa washenzi,” Kufika hapo Peter alinyanyua kichwa chake kutoka mapajani kwa Vanessa na kisha akamwangalia usoni na kushindwa kumtafasiri ni mtu wa aina gani.

Hana machozi wala hana macho yanayoenda kutoka machozi bali uso uliojaa jazba na chuki zilizojidhihirisha kwa ndita zake kujikunja na misuli ya pembeni ya kichwa kumtoka.

“Vanessa, mbona unaongea hayo?” Peter alimuuliza baada ya kushindwa kumtafakari mwanadada yule.

“Maisha uliyopitia Peter, ni yenye machungu mengi lakini niliyopitia mimi nahisi yamezidi. Nilishuhudia mama yangu akiuawa kwa damu baridi. Mama yangu alichinjwa kama kuku, mama yangu alinyofolewa kichwa chake na kisha kikatupiwa mbwa ambao walikuwa wanamsaka porini. Kisa ni hawa tunaosema ni marafiki.

Hamna rafiki katika dunia hii. Hata wewe si rafiki, nitakuita rafiki siku nikifia mikononi mwako huku ukiwa unahangaika kuikoa roho yangu. Hapo ndipo nitasema wewe ni rafiki na nitakuwekea makao mema mbinguni kama kweli yapo,” Alizidi kutema maneno ya chuki Vanessa.

“Nakubaliana na wewe asilimia zote. Mimi mwenyewe simuamini mtu hata kidogo, hata wewe japo nimekwambia siri ambayo nimeificha kwa mwaka mmoja sasa. Ni msukumo tu ambao nadhani MUNGU kanitupia ndio umenifanya nikwambie. Lakini sikuamini hata chembe. Nitakuamini pale nitakapofia mikononi mwako wakati ukihangaika kuinusuru roho yangu isiache mwili.

Nitakuamini kama ukijua thamani ya chozi langu kudondoka na nitakuamini zaidi kama ukiamini nachokwambia.” Alinena Peter na kusimama kwa ajili ya kutaka kutoka nje lakini Vanessa akamuwahi kwa maneno.

“Ni msukumo wa moyo wangu juu yako ndio umenifanya nitake kujenga urafiki na wewe. Naomba urudi tuongee Pity, samahani kwa maneno yangu. Naomba urudi tafadhali.”Aliongea kwa upole Vanessa.

Peter alirudi pale kitandani na kukaa karibu na Vanessa, naye Vanessa kwa kudeka alilala mapajani kwa Peter na kuanza kutema maswahibu yaliyomsibu.

“Mama alikuwa na rafiki yake ambaye alimwamini sana pale Kongo tulipokuwa tunaishi. Alimuamini kwa kuwa alikuwa anamkwamua pale alipokwama na alikuwa nyenzo muhimu pale mama ambapo alikosa msaada.

Mama alimpa kila kitu yule rafiki yake, wakati huo mama alikuwa anafanya kazi shirika la kuhudumia watoto duniani. Yule rafiki yake yeye alikuwa mwanasiasa pamoja na mumewe.

Kama ni hela, mama na baba walikuwa nazo sana na siku zote watakuwa nazo kwa sababu wamejiwekea malengo ya kuwa nazo daima. Lakini fedha hizihizi ambazo ni makaratasi, ndizo zilizomuondoa mama duniani na ndizo zilizomwondoa baba pale Kongo.

CHUKI na WIVU.

Ogopa sana tabia hizi, ziogope kupindukia.

Yule rafiki wa mama alipopata ubunge na kupewa uwaziri, akafanya kama harambee ya kuondoa mabwanyenye, wao waliwaita wanyonyaji. Bila kutegemea, baba na mama wakapata taarifa kuwa nao wapo katika tifutifu hilo.

Tuliondoka usiku huohuo, wakati huo mimi nina miaka kumi na miwili, miaka saba sasa imepita. Tulichukua nguo kiasi na kisha tukapanda garini na kuanza safari ya kuhama ule mji.

Baada ya saa moja mara tukasikia kwenye radio kuwa barabara zote zimefungwa kwa ajili ya msako wa watu wanaobainika ni wanyonyaji.

Ikabidi tutelekeze gari na kuingia msituni huku baba akiwa mstari wa mbele kutuongoza.

Bado sijajua sababu ya yule aliyejiita rafiki wa mama kufanya vile, ila nadhani ni wivu hasa ukizingatia kuwa mama alikuwa msaada mkubwa kwake. Hivyo wivu ukazaa chuki na kutafuna utu wake ambao alijivika wakati ana matatizo.” Vanessa alikuwa akiongea kwa taratibu na wakati huo Peter alikuwa anampa faraja kwa kuzichezea nywele zake.

“Mwendo wa saa moja lingine, mara tukasika mbwa wanabweka nyuma yetu. Hapo tayari tukajua mambo yamewiva. Tayari tumeingia mapambanoni. Baba akanibeba na kuanza kukimbia huku mama akifuata kwa nyuma. Jinsi tulivyokuwa tunakimbia, ndivyo sauti za mbwa nazo zilivyozidi kusikika karibu yetu.

Wale mbwa walinusishwa harufu ya nguo za mama kwani walipofika walimdaka yeye na kuanza kumgalagaza pale chini.

Kwa ujasiri mkubwa, mama alikuwa anapambana nao kabla ya wale wamiliki hawajafika. Walikuwa mbwa watatu, hata baba alipojaribu kwenda kumsaidia mama ilishindikana kwa sababu wale mbwa walikuwa kama wana kichaa.

Nakumbuka mama alimwambia maneno machache tu, Baba ya kuwa aondoke eneo lile na kamwe asifikirie kisasi bali anilee mimi katika maadili mema.

Baada ya maneno hayo mama aliendelea kupambana na mbwa wale na alibahatika kumuua mmoja kwa kumng’ata shingoni kwa nguvu.Mama akawa anakunywa damu ya mbwa wakati huo sisi tumejificha kwenye kichaka kimoja mbali kidogo na pale.”

“Hadi wale wanaotutafuta walipofika eneo lile, walikuwa kama wamechelewa sana kwa kuwa mama alikuwa hajiwezi kabisa. Hawezi hata kuongea mama yangu. Alikuwa hawezi hata kusogeza mkono kwa jinsi alivyokuwa amechakazwa na wale mbwa pamoja na mchoko wa kukimbia porini,” Vannesa aliendelea kumsimulia Peter ambaye muda wote alikuwa akichezea nywele zilizokuwa na afya za binti yule.

“Pity, ukweli nakwambia,” Vanessa alinyanyuka na kukaa wima na kumwangalia Peter baada ya kusema hayo. Akaendelea, “Hii dunia inawatu makatili kuliko hata wanyama wa mwituni. Kuliko hata simba na chui. Kuliko hata risasi itokayo kwenye kinywa cha bunduki.” Maneno yalimtoka Vanessa yakiwa yamejaa dukuduku la wazi.

“Yule mama ambaye sasa eti ni Waziri wa jinsia na watoto, alichomfanya mama yangu, ni zaidi ya ukatili. Ni zaidi ya dhambi ile. Yule mama anastahili kufa Peter, nitamtafuta na nitamchinja kwa mikono yangu.” Vanessa alitema maneno huku kidole chake cha shahada kikiwa mbele kuonesha msisitizo.

“Mshenzi yule kumbe alikuwa anatufatilia kwa gari pale tulipokimbilia porini. Baada ya wale mbwa kumsulubu mama yangu, ndipo baadhi ya Polisi walitokea na kuwazuia kisha wakamsubiri bosi wao.

Wakati hayo yanafanyika, sisi tulikuwa kwenye kichaka kimoja kikubwa lakini chenye uwezo wa kuona matendo yanayotokea kwa pale mama alipo,” Sura ya Vanessa safari hii ilikuwa wazi imeghadhabika kwa jinsi alivyokuwa anasimulia kilichotokea.

“Baadae gari lilikuja na ndipo aliposhuka huyo Waziri wa Jinsia na Watoto. Kwa mbwembwe alimfuata mama ambaye alikuwa kapiga magoti huku uso wake kauinamisha kwa kuangalia kifua chake. Alikuwa hawezi hata kunyanyuka, yale magoti alipiga kwa kuwa askari walimlazimisha. Lakini baada ya kusikia sauti ya kike ikimuita na kumkashifu, ndipo aliponyanyua uso wake na moja kwa moja akakutana na mtu ambaye aliamini daima kuwa ni rafiki yake.

Pity, moyo wamwanadamu ni kiza kinene ambacho kinasababisha usione ya mbele. Moyo wa mwanadamu umegubikwa na weusi ambao ni MUNGU pekee ndiye ajuaye nini kilichomo humo. Hakuna rafiki katika dunia hii. Rafiki wa kweli ni moyo wako tu. Mimi si rafiki Pity, mimi ni mpitaji tu!. Ila nimekuamini na kukuambia haya ili ikiwezekana tusaidiane.” Sura kavu ya binti yule ilidhihirisha kuwa hakuwa mtu wa kawaida hata kidogo. Moyo wa Peter ulikumbwa na uoga mkubwa baada ya kuona mwanamke mrembo kama yule akiapa mambo ya ajabu ikiwemo kuua.

“Lakini kwa nini ufikirie kuua na wakati unaishi bila bugudha za hao watu? Kwa nini usisamehe na kuacha hayo yapite tu?” Peter alimshauri Vanessa.

“Hakuna kitu kinachoitwa msamaha katika maisha ya leo. Huyo unayemsamehe ndiye anayekuunguza tena. Jifunze kuwa na moyo mgumu. Moyo usiojali kilio cha mtu aliyekukosea, ukipata nafasi fanya kile ambacho umekusudia kufanya.” Vanessa alimjibu Peter kwa ujasiri.

Peter aliinama na kukumbuka maneno fulani ambayo aliwahi kuambiwa na baba yake. Maneno hayo yalikuwa ni kuhusu msamaha na visasi.

Aliponyanyua uso wake, alikuwa tayari ana cha kumshawishi Vanessa ili aondokane na moyo wa kisasi.

“Vanee,“ Peter alimuita Vanessa na kumuangalia usoni. Vanessa naye akamwangalia Peter na kutoa tabasamu hafifu. Peter akaendelea kuongea alichokusudia kukiongea. “Moyo wa mwanadamu ni nyongo iliyotumbuka. Moyo wa mwanadamu ni tungo isiyoeleweka. Maneno haya aliniambia baba yangu. Sikujua alichomaanisha papo kwa hapo hadi pale aliponifunulia mwenyewe.” Peter aliongea hayo huku akiwa makini na kucheza na akili ya Vanessa.

“Moyo wa mwanadamu ni mchungu kama vile nyongo ilitumbuka kwenye kitoweo. Umejaa chuki na wingi wa masimango. Umejaa ukali wa ajabu ambao huwezi kuutia kinywani na kuumeza. Huo ndio moyo wa binadamu. Kama ukiupa nafasi wa mambo kama hayo uyawazayo, kamwe hutookoa moyo wako kutoka kwenye kiza kilichouzingira. Acha maisha yako yatawaliwe na furaha kwa kile ulichonacho kuliko kutawaliwa na kisasi kwa kile ulichokipoteza.” Peter aliongea na kumuacha Vanessa akiwa kinywa wazi asijue cha kujibu.

“Moyo huuhuu, baba aliuita ni tungo isiyoeleweka. Leo waweza kuwa na hili lakini kesho ukawa na lile. Leo umepanga kulipa kisasi, lakini hujui kitakachokutokea mbele. Hicho kitakachokutokea ndicho kitakachobadili moyo wako. Mfano leo umepanga kisasi, vipi kesho ukifanikiwa kulipa kisasi? Moyo wako utakuwa huru kweli? Moyo wako utakuwa unafuraha kufanya kile ambacho mama yako alikukataza? Na je, vipi baada ya kisasi yakatokea mengine? Utaendelea kulipa kisasi chako? Kwa nini usifurahie japo furaha ndogo akupayo baba yako?

Umekosa mama, ndiyo nakubali. Lakini baba unaye. Mimi sina baba wala mama, lakini nafurahia uwepo wangu hadi sasa hivi napumua.” Hadi Peter anamaliza kumshauri Vanessa, dada huyu tayari alikuwa kama kagandishwa na barafu kwa maneno hayo.

“Pity. Nashindwa nikutafsirije.” Vanessa aliongea baada ya Peter kuweka kituo katika maongezi yake.

ITAENDELEA

Born to Die Sehemu ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment