Tutarudi na Roho Zetu
NEW AUDIO

Ep 01: Tutarudi na Roho Zetu

SIMULIZI Tutarudi na Roho Zetu
Tutarudi na Roho Zetu Sehemu ya Kwanza

IMEANDIKWA NA : BEN R. MTOBWA


Simulizi : Tutarudi Na Roho Zetu?

Sehemu Ya Kwanza (1)

KAMA maji ya bahari ya hindi yangekuwa na hisia, basi yangejisiskia fahari sana kwa kupata fursa nyingine ya kuiburudisha miili ya viumbe hawa wawili ambao walikuwa wakiogelea kandokando ya ufuko huku wakicheza na kucheka. Walifanya picha ya kuvutia sana, hasa sura zao nzuri zilipoibuka na kutoka majini na kumezwa na tabasamu lililosababishwa na mzaha waliokuwa wakifanyiana chini ya maji. Baada ya kuogelea kwa muda walirejea nchi kavu ambako walijibwaga juu ya mchanga ulioruhusu joto likaushe maji miilini mwao.

Ufuko pia ungekuwa na kila sababu ya kusherehekea johari ya kulaliwa na viumbe kama hawa kwani walioana kimaumbile kama pacha, ingawa hawakuwa mtu na dada yake. Walikuwa kama jozi ya kiatu cha kiume kwa cha kike. Mwanamume hakuwa mwingine zaidi ya yule kijana mwenye umbo refu, kakamavu, lililokaa kiriadhariadha na sura nzuri, yenye dalili zote za hekima, ushujaa na ucheshi. Kwa jina anaitwa Joram Kiango.

Naye msichana alibahatika kupewa umbo lenye kila kitu ambacho msichana anahitaji kuwa nacho, wakati huohuo akiwa na kile ambacho mvulana legelege asingekuwa nacho. Ni yule ambaye akutazamapo ungependa aendelee kukutazama, achekapo unafarajika, atembeapo unaburudika, yule ambaye kuna madai kwamba alikuja duniani kwa makosa baada ya kuumbwa ili awe malaika. Kama madai hayo si kweli, basi yako mbali sana na uongo. Hata jina lake halikutofautiana sana na sura yake. Wanamwita Nuru.

Baada ya kuhakikisha kuwa miili yao ilikuwa imekauka, wakajifuta vizuri; kisha wakayachukua mataulo yao na kwenda kwenye gari lao. Macho ya watu wengi, Waswahili kwa watalii ambao walikuwa katika ufuko huo, hayakukoma kuwafuata. Kutazamwatazamwa, hasa wanapokuwa pamoja, halikuwa jambo geni tena kwao. Mara kwa mara macho ya kiume yalimwandama Nuru, hali ya kike yakimfuata Joram, kila mahala walipopita. Walijifunza kuyazoea hata wakaanza kusahau kuwa wanatazamwa. Hivyo, walipolifikia gari waliingia na kulitia moto wakilielekeza mjini kwa mwendo usio wa haraka.

Hawakuwa na sababu yoyote ya kufanya haraka. Ratiba yao ya starehe ilikuwa ikielekea kwisha mapema zaidi ya walivyokusudia. Walikuwa wamekubaliana wakae katika miji yote mashuhuri hapa nchini kwa muda wa wiki nzima kila mji. Lakini hii ilikuwa wiki ya pili tu na tayari walikuwa wameishi Zanzibar, Moshi, Arusha, Dodoma, Mwanza na kujikuta wamerejea Dar es salaam. Kila mji waliuona unakinaisha baada ya siku mbili tu. Maisha ya hotelini waliyaona yanawafaa watu wavivu, nazo mbuga za wanyama ziliwasisimua watalii, ilihali miji iliwaridhisha wenyeji, na safari za hapa na pale zilikinaisha.

Hivyo, ingawa walirejea Dar es Salaam na kuendelea na starehe zao wakiishi katika hoteli ya Kilimanjaro na ingawa waliendelea kucheza na kucheka, na hakuna aliyetamka neno, lakini bado haikuwa siri tena kuwa maisha ya kula, kulala… kula tena, kulala tena yalianza kuwachosha. Maisha hayo yalianza usiku ule ambao Joram Kiango asingeweza kuusahau, usiku ambao hadi leo unamtia maumivu moyoni kila anapokumbuka alivyodhulumiwa haki na wajibu wake wa kuitia risasi katika kichwa cha Proper, yule katili ambaye, pamoja na kuwaangamiza watu wengi wasio na hatia, alimwua Neema Iddi kinyama. Ni siku hiyo ambayo Joram aliitupa bastola yake na kuamua kuishi kivivu kama wanavyoishi watu wengine. Msichana huyu Nuru alihusika sana katika mkasa huo ambao tayari mtu mmoja aliuandikia kitabu na kukiita SALAMU TOKA KUZIMU. Nuru alishindwa kuachana na Joram na hangeweza kustahimili kumwona Joram akiteseka na msiba huo peke yake.

Alimfuata na kumsihi hata palipopambazuka wakajikuta wako pamoja, juu ya kitanda kimoja.

Tangu hapo hawakuachana, Joram hakuwa mtu anayeweza kuachwa kirahisi. Naye Nuru kadhalika, alitofautiana sana na wale wanawake wazuri ambao uzuri wao ni pale wanapokuwa wamevaa nguo tu. Alikuwa na mengi ambayo aliyatenda kwa nia moja tu; kumfariji Joram naye Joram alijikuta akianza kujisamehe. Lakini asingeweza kusahau…


Walipowasili chumbani mwao walijipumzisha vitandani mwao kwa muda huku wakilainisha koo zao kwa vinywaji vitamu. Kisha wakafuatana bafuni na kuyaondoa maji ya chumvi miilini mwao kwa kuoga vizuri kwa sabuni. Baada ya hapo walikwenda katika chumba cha maakuli ambapo walikula na kujiburudisha kwa vinywaji vikali na maongezi laini.

Akiwa katika vazi lililomkaa vema, suti ya kijivu iliyooana na viatu vyeusi kama kawaida, alikuwa tishio kubwa kwa wanaume waliokuja na wasichana wao. Hata hivyo, walijifariji kwa kujua kuwa asingekuwa “mwendawazimu” wa kuvutwa na yeyote kwani aliyeketi nae hakuwa msichana wa kawaida. “Kwanini watu kama wale wanaishi hapa bongo?” mtu mmoja alimnong’oneza jirani yake. “Tazama wanavyopendeza! Wangeweza kwenda zao nje na kutajirika sana endapo wangecheza mchezo mmoja tu wa sinema”

“Kweli kabisa,” aliungwa mkono. “Hata maumbile yao yanafikiana. Yule dada anatosha kabisa kumtia mwanaume yeyote wazimu kiasi cha kumfanya auze nyumba.”

Maongezi hayo hayakumfikia Joram wala Nuru. Lakini alikwishazoea kuyasoma katika macho ya watazamaji wake. Hivyo, alitabasamu kidogo na kuagiza kinywaji kingine. Nuru alikuwa akiongea neno. Joram aliitika bila kumsikia. Waliendelea kunywa kwa muda hadi walipoamua kuwa wametosheka. Ndipo walipofuatana katika ukumbi wa muziki ambapo walisikiliza muziki na kucheza kwa saa kadhaa. Walipokinai walikiendea chumba chao ambacho kiliwalaki na kuwapa usiri. Katika usiri huo, kwa mara nyingine, miili yao iliburudika na kusherehekea afya zao.

Kesho yake, baada ya kifungua kinywa walitazamana katika hali ya kuulizana siku hiyo waitumie vipi. Nuru aliweza kuzisoma dalili za kuzikinai ratiba zao ambazo zilikuwemo katika macho ya Joram. Ingawa walikuwa wakistarehe na kujiburudisha furaha, ilikuwa dhahiri kuwa burudani hizo, kama zilikuwa zikiuburudisha mwili wa Joram, kamwe hazikuwa zikiburudisha akili yake. Ingawa uso wake ulitabasamu mara kwa mara, lakini roho yake iliwaka kwa hasira kali dhidi ya adui zake, adui wa taifa na maendeleo ya jamii, adui ambao walifanya maovu mengi yasiyokadirika na kumtia lile donda la rohoni kwa kumuua kikatili msiri wake mkuu, Neema. Kwa dhamira ya kumsahaulisha Joram uchungu huo ndipo Nuru akajitoa kwake mwili na roho. Lakini ilikuwa dhahiri kuwa jeraha hilo lilikuwa bichi katika roho ya Joram, na lisingepona kabisa isipokuwa kwa dawa moja tu:kulipiza kisasi. Hayo aliyaona wazi katika macho ya Joram ingawa alijisingizia kufurahia starehe zao.

Iko siku Nuru aliwahi kumwambia, “Sikia Joram. Huonekani kufurahia lolote tunalofanya. Kwa nini usiirudie ofisi yako na kuendeleza harakati zako? Nitakuwa kama alivyokuwa Neema. Nitakusaidia kwa hali na mali.”

Joram alicheka na kumjibu, “Mara ngapi nikwambie kuwa nimeacha shughuli hizo. Nitaendelea kustarehe hadi nitakapoishiwa na senti yangu ya mwisho.Ndipo nitakapotafuta kazi na kuifanya kwa Amani na utulivu kama vijana wenzangu.”

“Kwanini lakini? Kifo cha msichana mmoja tu kinakufanya usahau wajibu wako!”

“Sivyo Nuru. Isieleweke kuwa nimechukia kwa ajili ya kufiwa na Neema. Yeye ni mmoja tu kati ya mamia ya wasichana wanaouawa kwa dhuluma na ukatili ainaaina ulioko duniani. Ni mmoja tu kati ya maelfu ya vijana wanaoteseka kwa shida ambazo wanazipata kwa makosa ya watu wengine. Ni mmoja tu kati ya mamilioni ya binadamu wanaoumia kwa umasikini ambao hawakuuomba na dhiki ambazo hazina umuhimu wowote.”

“Sidhani kama nimekuelewa Joram, unazungumza kama mshairi.”

“Labda. Ninachotaka kusema ni kwamba bastola yangu haitoshi kukomesha maovu yote yanayotendeka hapa duniani. Kote Afrika, na duniani kwa ujumla, binadamu hawako sawa kiuchumi. Wako wanaoshinda njaa na kuna wanaomwaga chakula. Kama kweli nakusudia kuondoa dhuluma na ukatili kwa nchi dhidi ya nchi nyingine, basi sina budi kuukomesha pia ukatili dhidi ya mwingine. Maadamu hayo yako nje ya uwezo wangu, naona sina budi kusahau yaliyopita na kuanza kula na kunywa kama vijana wenzangu.”

“Hasira hizo Joram. Upende usipende ukweli ni huo huo: bastola yako haiwezi kuwaelekea viongozi wazembe na wenye choyo ambao wanasababisha hali ngumu kwa mwananchi. Lakini inawajibika kuwakomoa maadui ambao dhamira yao ni kuhakikisha hatulifikii lengo letu la kujenga taifa ambalo raia wake wanafaidi matunda ya uhuru wao. Unafahamu fika kuwa wanatunyima nafasi ya kufanya hayo”…

Maongezi hayo yalifanyika siku chache zilizopita. Nuru aliyakumbuka tena leo baada ya kuziona dalili za kukinai katika macho ya Joram. Alijua na kuamini, kama wanavyoamini watu wote wanaomfahamu Joram, kuwa starehe yake kuu ni pale anapopambana na adui na burudani yake ni hapo anapowashinda. Vinginevyo Joram alikuwa akijisingizia starehe.

“Leo wapi mpenzi”, Nuru aliona amchokoze.

“Leo najisikia kulala tu”.

“Kulala mchana! Tangu lini umeanza tabia hiyo?”

“Tangu nilipoacha kuwa Joram Kiango na kuamua kuwa kijana mtumiaji anayeitwa Joram Kiango.”

“Nilijua utachoka, Joram. Kwanini usirudi ofisini na kuanzia leo?”

“Sikia Nuru. Usianzishe tena ule ubishi ambao siupendi. Wakati wote nitakuwa hapa nikiendelea kutumia.”

“Sidhani kama unasema ukweli. Huonekani mtu wa kustarehe maishani.”

Joram hakumjibu. Alijilaza kitandani na kujisomea gazeti.

Kisha jirani yao wa chumba cha pili aliingia akiwa katokwa na macho. Hakujali kupiga hodi. Wala macho yake hayakuvutwa kuuhusudu uzuri wa Nuru kama ilivyokuwa kawaida yake. Badala yake alimwendea Joram kitandani akisema, “Hujasikia? Samora amekufa!Ndege yake imeanguka huko Afrika Kusini.”

“Amekufa!” Nuru alishangaa.

“Amekufa. Sio bure. Iko namna. Haiwezi kuwa ajali ya kawaida.”

“Afrika Kusini? Alienda fanya nini huko?” Joram aliuliza kwa utulivu. Hata hivyo macho yake yaliwaka kwa hasira, ingawa hakupenda kuidhihirisha kwa Nuru.

“Siku hizi hata taarifa za habari husikilizi Joram?” Nuru alisema.

“Samora hakwenda Afrika Kusini. Alikuwa akitoka Zambia ambako alikutana na rais Mobutu na Waziri Mkuu Mugabe kutafuta mbinu za kuiwekea Afrika Kusini vikwazo zaidi vya kiuchumi”.

“Wanasema chanzo cha ajali hakijapatikana. Bila shaka watakuwa wameisababishia ajali hiyo kwa njia moja au nyingie,” alisema kwa masikitiko.

“Nadhani wamezoea kutuangamiza wapendavyo. Kwao sisi ni sawa na vifaranga waliofugwa. Yeyote ambaye hawampendi wanamponda kwa urahisi. Jambo la kusikitisha ni kwamba sisi hatuwezi kuwafanya lolote. Baya zaidi ni kwamba hatujui tutaendelea kuuawa mpaka lini.Kwanza, walimuua Mondlane: Sasa wamemuua mrithi wake, Samora. Na siyo hao tu. Viongozi wengi wa Afrika wameondokea kuwa kama mifugo yao. Tunaorodha ndefu ya viongozi wetu wanaouawa au kupinduliwa kwa matakwa yao. Tutaendelea kuvumilia mpaka lini?” Nuru alikuwa kama mtu anayezungumza peke yake.

Lakini macho yake yalikuwa yakimtazama Joram. Alitamani aone kitu katika macho yake. Hakukiona. Jambo hilo lilimfanya ainame chini na kuruhusu matone kadhaa ya machozi yamdondoke.

Yalikuwa machozi ya hasira zaidi ya huzuni.


Kifo hiki cha kijana shujaa aliyeheshimiwa kote dunia, aliyependwa na wapenzi wake na kuogopwa na adui zake; kilifuatiwa na minong’ono mingi kote dunia. Watu walisema hili na lile, wakipingana na kuafikiana.

“Walimuua…”

“Bila shaka.”

“…Njama za Afrika Kusini.”

“Na vibaraka vyao.”

Siku chache baadae maongezi yalibadilika.

“Umesikia? Makaburu wanadai kuwa wataendelea kuwaadhibu viongozi na wananchi wote wa nchi za mstari wa mbele ambao wanajifanya vichwa ngumu.”

“Kweli? Washenzi sana wale. Wanaweza kufanya lolote”.

Na baada ya siku chache mambo yalianza kutukia. Duniani kote magazeti yalikuwa na habari ya kutisha:

Watu mia nne wamefariki, mia tisa kujeruhiwa na maelfu kuponea chupuchupu katika ajali isiyo ya kawaida iliyotokea huko Lagos Naijeria. Watu hao walikuwa katika uwanja wa mpira wakitazama shindano kati ya timu ya taifa ya nchi hiyo na Zaire. Dakika chache kabla ya mchezo huo kwisha, moto mkali ulilipuka na kuubomoa uwanja mzima na kusababisha maafa hayo. Wachunguzi wa mambo wanahisi kuwa huenda utawala wa Afrika Kusini unahusika.

Kabla watu hawajaisahau habari hiyo, ilifuata nyingine ya kutisha vilevile.

Harare.

Maghala manane ya serikali, ambayo yalikuwa yamehifadhi chakula, yameungua moto kwa pamoja. Chanzo cha moto huo hakijajulikana. Jambo la kushangaza ni jinsi maghala hayo yalivyoungua kwa pamoja ingawa yako katika wilaya mbalimbali za nchi hiyo. Kuna mashaka kuwa tukio hili kwa njia moja au nyingine linahusiana na yale maafa ya Nigeria.

Na baada ya siku chache;

Dar es Salaam.

Katika matukio ya kutisha na kushangaza yanayozidi kutokea nchi zenye msimamo wa kimapinduzi za Afrika, leo asubuhi Tanzania imepatwa na pigo zito la kusikitisha. Jengo la Benki kuu ambalo lilikuwa likikamilisha marekebisho, baada ya ule moto wa awali limeungua tena. Safari hii haielekei kuwa kuna matengenezo yoyote yanayoweza kulirekebisha zaidi ya kujengwa upya. Chanzo cha moto huu hakijafahamika.

Habari hizi ziliitisha Afrika na kuishangaza dunia. Kila mtu aliyezisikia redioni na kuzisoma magazetini alishangazwa na matukio haya ambayo mfano wake haukupata kutokea katika historia ya Afrika na dunia.

Ajali ni jambo la kawaida. Kadhalika, kuna watu wanaoamini kitu kinachoitwa ‘mkosi’ na ‘bahati mbaya.’Lakini mikosi mingi kiasi hiki na bahati mbaya kama hizi kuziandama nchi chache za Afrika, zenye msimamo mmoja katika suala la ukombozi, ni jambo ambalo lilisababisha nyongeza katika fikra za wasomaji na wasikilizaji wa vyombo vya habari. Kitu kinachoitwa ‘roho mbaya’ kilipenya katika fikra hizo, ingawa hakukuwa na hakika katika mawazo hayo. Baadhi hata waliwahi kutamka hadharani kuwa kuna mkono wa mtu katika matukio hayo.

Mawazo hayo yalifuatwa na hofu katika mioyo ya wananchi na serikali zao walipojiuliza,“Kipi kingefuata?”

“Joram, tutakaa kimya kusubiri maafa zaidi?” Nuru alimwuliza Joram baada ya kusoma habari hizi za tukio la Benki Kuu katika gazeti. Alijitahidi kustahamili kutosema lolote alipoyasoma matukio ya Lagos na Harare. Lakini hili la nyumbani lilimgusa zaidi. “Aibu iliyoje!” aliendelea. “Tuendelee kustarehe kwa vinywaji na muziki huku tukisubiri siku ambayo maafa mengine yatatokea! Haiwezekani Joram. Lazima tufanye jambo.”

Ndiyo. Habari hizo hazikumpendeza Joram. Hata hivyo, alizisoma kama raia wengine, bila ya kudhihirisha dalili yoyote ya nia ya kufanya lolote kama alivyokuwa awali. Jambo hilo lilimfanya Nuru atokwe na machozi. “Serikali inao polisi na wapelelezi wake, ambao inawalipa pesa nyingi,” Joram alisema. “Mimi ambaye nimeacha shughuli hizo nitasaidia nini?”

“Huwezi kusema hivyo Joram! Siamini kama moyo wako wa uzalendo umedidimia kiasi hicho.”

“Haujadidimia. Uko palepale, kama ilivyo mioyo ya wazalendo wengine.”

“Lakini wewe si mzalendo wa kawaida, Joram. Taifa linakuthamini na kukutegemea. Huwezi kulisaliti kiasi hicho bila sababu ya kuridhisha. Lazima ufanye jambo.”

“Ndiyo. Nitafanya jambo. Nitastarehe na kuendelea kustarehe kama wanavyofanya vijana wenzangu. Njoo kitandani, Nuru. Tafadhali, njoo tustarehe. Acha wenye shibe waendelee kulinda shibe yao. Wewe na mimi tuna nini katika nchi na dunia hii?”

“Joram…”

“Nuru, njoo tafadhali. Na kama umenichoka sema nimtafute Nuru mwingine ambaye hachoshwi na starehe.”

Nuru angependa kukataa. Lakini asingeweza. Akamfuata Joram kitandani na kujilaza kando yake huku machozi yakimtoka kama kondoo anayesubiri kuchunwa.

SURA YA PILI

KATI ya watu ambao wameisumbukia nchi hii, wakiziweka roho zao katika minada ya maafa na kwato za mauti kuilinda nchi isimezwe na jangwa la misukosuko inayosababishwa na majasusi hatari, ni mzee huyu; Mkwaju Kombora. Tangu utoto wake baada ya kumaliza kidato cha sita, alijikuta akitoka chuo hadi chuo, akifundishwa mbinu mbalimbali za kupambana na adui. Baada ya kuhitimu vizuri alijikuta kava magwanda ambayo mabega yake hayakukoma kubadilikabadilika hadi alipojikuta Inspekta wa kikosi hiki maalumu. Kupanda kwake ngazi mara kwa mara kulitokana na moyo wake wa kishujaa na juhudi zisizo kifani katika kuwakabili adui wa nchi. Mara kwa mara aliwashinda adui zake isipokuwa safari chache ambazo alielekea kukata tamaa. Hata hivyo, asingekosa kumshukuru Mungu kwani nyakati hizo alitokea kijana yule ambaye alisaidia kuwanasa adui kwa hila zake za kutatanisha, kijana ambae jina lake lisingeweza kumtoka akilini; Joram Kiango.

Kombora asingeusahau mchango wa kijana huyu katika mikasa ile ambayo Mswahili mmoja ameamua kuandika vitabu ili apate chochote kile na kuviita Dimbwi la Damu, Mikononi mwa Nunda, Najisikia kuua tena na Salamu kutoka Kuzimu. Hata hivyo, kama polisi wengine, Kombora asingeweza kutamka hadharani kuwa Joram alifanya lolote la haja isipokuwa alibahatisha na kuhatarisha maisha yake.

Lakini leo Kombora alitamani kumbembeleza Joram, hata kwa kumuangukia miguuni, endapo ingebidi, ili amsaidie kuutatua mkasa huu uliokuwa ukimtoa jasho yeye na polisi wenzake wote wa nchi zilizo mstari wa mbele kwenye ukombozi Kusini mwa Afrika.

Mambo mengi, yalikuwa yakitokea mazito na ya kutisha zaidi ya walivyoyafahamu wananchi wa kawaida ambao wanategemea gazeti, redio na televisheni ziwape habari. Kila mmoja alisikia mikasa ya kuteketea kwa mamia ya maisha ya watu wasio na hatia ambao walipata ajali ya kutatanisha katika uwanja wa mpira huko Naijeria. Pia, ni wengi waliosikia juu ya kuungua kwa maghala ya chakula bila sababu mahususi inayoeleweka huko Harare. Zaidi, hakuna Mtanzania ambaye hakupata kuzisikia habari za kuungua tena kwa jengo la Benki kuu lililokuwa likikamilishiwa shughuli za kujengwa upya.

Hayo ni maovu yaliyosikika katika vyombo vya habari na mitaani. Hayakumtisha sana Kombora. Lakini kulikuwa na haya ambayo bado yalikuwa siri mioyoni mwa wakubwa wachache wa ngazi za juu katika idara ya usalama, ambayo hayasemeki wala kutangazika.

Viongozi wanane wa vyama kadhaa vya wapigania uhuru wa Afrika Kusini na mwakilishi wa PLO hapa nchini, ambao walikuwa wakikutana kwa faragha katika jengo moja jijini Dar es Salaam, walifariki ghafla katika moja ya ajali hizo zisizoeleweka. Hakuna anayefahamu kikamilifu chanzo cha vifo hivyo, isipokuwa kwamba walikufa kwa kuungua moto uliolipuka ghafla katika chumba chao cha mkutano. Juhudi zote za kutafuta chanzo cha moto huo hazikuwa na mafanikio.

Zaidi ya hao, kuna wale mawaziri wa nchi zisizofungamana na upande wowote ambao walinusurika katika ajali ambayo haikutofautiana na hiyo ya Dar es Salaam. Mkutano wao uliandaliwa kufanyika katika chumba fulani katikati ya jiji la Lusaka. Wakati wakijiandaa kwenda huko lilitukia suala jipya ambalo liliuchelewesha msafara wao kwa zaidi ya nusu saa. Kuchelewa huko kuliyaokoa maisha yao kwani chumba hicho kililipuka kwa moto mkubwa uliyoyapoteza maisha ya wafanyakazi wawili wa chumba hicho na kuharibu vifaa vyote. Kama awali, chanzo cha moto huo hakikupata kufahamika.

Hayo ni baadhi tu ya mambo yaliyokuwa yakitokea. Kulikuwa na hisia kuwa mkono wa utawala wamakaburu wa Afrika Kusini ulikuwamo katika vitendo hivyo. Lakini hisia hizo hazikuwa na uhakika kamili, hasa baada ya ushahidi mdogo ulikuwa ukielekea kutoweka kwa njia nyingine ya kusikitisha.

Ushahidi huo ulielekea kuchipuka baada ya ule moto ulioteketeza Benki Kuu. Yuko askari mmoja aliyesema kuwa aliamini moto huo ulisababishwa na mtu mmoja aliyefika katika jengo hili usiku na kujiita kuwa ni mmoja kati ya mafundi ambao walikuwa wakishughulikia jengo hilo. Jengo lilikuwa chini ya ulinzi mkali wa askari huyo na alimwamuru kusimama mikono juu. Mtu huyo alisihi kwa maneno mengi kuwa, alisahau kitu muhimu sana kwake katika jengo hilo, jambo lililomfanya askari huyo amruhusu kuingia ndani baada ya kumkagua kwa makini. Mtu huyo aliingia harakaharaka na baada ya dakika kadhaa alirudi huku akiwa ameshika hirizi mkononi na kusema kwa furaha,”Nilikuwa nimesahau hii, ndugu yangu. Bila ya kuwa na hii mfukoni siwezi kuishi saa ishirini na nne.”

Askari huyo hakumwamini sana mtu huyo, kutokana na jinsi alivyomuona mkakamavu asiyehofu hata kuelekezwa mtutu wa bunduki. Hivyo, jengo hilo lilipolipuka moto saa kadhaa baadaye, alilielezea tukio hilo kwa wakubwa zake ambao walimweka kati ya watu ambao walilazimika kuongea na Kombora ana kwa ana. Baada ya kumsaili kwa mapana na marefu Kombora alielekea kuamini kuwa mtu huyo aliyeingia katika jengo hilo usiku alihusika, kwa njia moja au nyingine, katika janga hilo. Lakini pindi walipobuni mbinu za kuanzisha msako wakumtafuta, askari huyo aliyekuwa mtu pekee aliyewahi kumwona alikutwa akielea baharini pwani ya Magogoni, akiwa maiti. Hakuna aliyeweza kueleza kilichomtoa kwake Magomeni Mikumi na kuja kuogelea kwa mara ya mwisho Magogoni.

Ilikuwa dhahiri kuwa aliuawa.

Jambo hilo lilimfanya Inspekta Kombora na wenzake wazidi kuamini kwamba kulikuwa na namna katika ajali hizo zilizotokea katika miji mbalimbali ya Afrika huru. Juhudi zao za kutafuta chanzo na watendaji wa maafa hayo hazikuelekea kuzaa matunda yoyote zaidi ya hisia tu kwamba Afrika Kusini ilihusika. Hisia hizo ziliongezewa uzito na vitisho vilivyoletwa kwa njia mbalimbali zikitishia uhai wa maisha ya watu na nchi ambazo eti zingeendelea na msimamo wao wa kuibana Afrika Kusini. Licha ya kusababisha hofu na mashaka, vitendo hivyo, vingeweza kupunguza hamasa ya moyo wa kimapinduzi katika fikra za mashujaa endapo hisia hizo zingeachiwa kuendelea.

Ni hapo ndipo Kombora alipozikumbuka silaha zote na kutamani zielekezwe Afrika Kusini. Ni hapo pia alipowakumbuka mashujaa wote na kutamani waelekee Afrika Kusini. Na kati ya mashujaa hao jina la Joram Kiango lilitangulia kumjia akilini.

Hiyo ilikuwa baada ya kuwasiliana na wakuu wote wa vikosi maalumu vya upelelezi katika nchi zote zilizokwisha husishwa na maafa hayo ya kutatanisha. Walishauriana kuwa kila nchi ifanye juu chini kuhakikisha kisa cha maafa hayo kinafahamika na, ikiwezekana, maafa hayo yakomeshwe. Ndipo Kombora alipoanza kufanya kila juhudi. Tumaini pekee ambalo lilielekea kumpatia walao fununu, yaani yule askari mlinzi wa benki kuu, sasa lilikuwa limeuawa kwa hila. Harakati za kupeleleza nani alihusika katika kumuua hazikuzaa matunda yoyote. Hivyo, Kombora alijikuta hajapiga hatua yoyote katika jukumu hilo. Badala yake alijiona kama kiwete au mtu aliyepooza, ambaye anasubiri maafa ya moto unaomjia kasi.

“Joram lazima ashirikishwe,” Kombora alifoka kimoyomoyo.

Alikuwa na habari zote za Joram, kuwa tangu baada ya mkasa wa Salamu Toka Kuzimu aliiacha ofisi yake na kuanza maisha ya kipuuzi katika mahoteli na mabaa, akijistarehesha na yule msichana mzuri wa Arusha. “Yeye si mtu wa kuupoteza muda wake katika mabaa. Kipaji chake kinahitajika sana katika vita hivi. Lazima apatikane.”

Alimtuma mtu ambaye alizunguka katika hoteli kubwakubwa na kumpata Joram. Lakini, kama Kombora alivyotegemea, majibu ya Joram yalikuwa ya kijeuri kiasi kwamba mtu huyo alijiona mjinga na kurudi akiwa amechukia, jambo ambalo jioni hii lilimfanya Inspekta Kombora ayavue magwanda yake na kuvaa mavazi ya kawaida, kisha akajitoma katika ukumbi wa hoteli ya Embassy ambamo aliambiwa kuwa Joram alikuwamo.


Akiwa mtu ambaye halewi kwa urahisi, tunaweza kusema kuwa Joram alikuwa amechangamka pale Kombora alipoikaribia meza yake na kuomba kuketi.

“Karibu sana Inspekta, karibu uketi,” alisema kwa uchangamfu huku akimwita mhudumu wa hoteli hiyo. “Leo naweza kusema kuwa ni siku tukufu sana kwangu kutembelewa na Inspekta Mkuu. Habari za siku nyingi mzee?”

“Polepole kijana,” Kombora alisema. “Wanasema siku hizi hata kuta zina masikio”.

“Kwani kuna lolote la siri tunaloongea mzee? Siku hizi mambo yote ya siri nimeachana nayo. Nimeamua kuwaraia mwema na mtulivu kama ulivyokuwa ukinitaka niwe,” Lilikuwa jibu la Joram.

Kombora hakutia neno. Akamgeukia Nuru na kumsalimu, “Bila shaka huyu ndiye yule dada ambaye alikuwa na balaa la kulazimishwa kushirikiana na yule mwuaji aliyekusudia kuwaangamiza viongozi wengi wasio na hatia?” Joram na Nuru waliitika kwa vichwa. “Ni msichana shujaa sana. Msichana wa kawaida angeweza kupoteza kichwa chake mara baada ya kukabiliwa na mkasa mkubwa kama ule,” alimaliza akipokea kinywaji chake na kuanza kunywa.

“Sivyo mzee,” Nuru alijibu. “Kila nikifikiria kile kitendo naona aibu kubwa sana. Nisingestahili kukubali kulazimishwa kushiriki katika mauaji ambayo yangekuwa ya kinyama kama yale. Ingawa yule jasusi Proper alilaghai kuwa ungekuwa mzaha wa kawaida, lakini bado sikustahili kuafikiana naye. Uzalendo wangu ulitiwa dosari na kitendo kile. Najaribu kutafuta nafasi ya kuudhihirishia moyo wangu, lakini sijafanikiwa…”

“Joram ananinyima nafasi hiyo!” Nuru aliongeza baada ya kusita kidogo.

“Ni hilo tu ulilotaka kusema Nuru,” Joram alidakia. “Na hata Inspekta nadhani amefuata kujadili hilo. Sivyo mzee?”

Inspekta aliimeza bia iliyokuwa kinywani mwake. Kisha akajibu, “Kiasi ni kweli kuwa niko hapa kujadili hilo, kiasi siyo kweli.” Alisita kidogo na kuendelea,”Unajua hatujaonana kwa muda mrefu? Tangu ulipoondoka Arusha kwa hasira baada ya kuitupa bastola yako hatujaonana. Nilifika katika chumba cha dada huyu nusu saa baadaye na kuukuta ubongo ule na bastola. Nilidhani umemwua wewe. Lakini bastola yako haikuwa imefyatuliwa hata risasi moja. Mara kikatokea kile kitabu ambacho kilinifanya nielewe yote yaliyotokea. Ndipo nikaelewa kwanini umekasirika na kuamua kuwa mnywaji”.

“Niite mlevi, Inspekta, sijali.”

“Hapana. Wewe si mlevi na wala huwezi kuwa mlevi. Ni mnywaji tu, mnywaji ambaye hanywi kwa ajili ya kupenda kunywa, isipokuwa kwa ajili ya hasira baada ya kunyang’anywa fursa ya kuitia risasi kwa mkono wako katika kichwa cha yule mshenzi. Sivyo Joram!” Kombora alitulia akimtazama Joram. Mara akakumbuka kuwa alikuwa hajavuta sigara kwa muda mrefu. Akatoa moja na kuiwasha baada ya kuwataka radhi jirani zake.

“Kuacha hadhi yako ipotee kwa ajili ya kukosa nafasi ya kumwua mtu mmoja tu duniani!” Kombora aliendelea, “Sioni kama ni haki. Ziko nafasi nyingi za kufumua vichwa vya watu wenye haki kabisa ya kufumuliwa. Hati maalumu inatayarishwa ambayo itakuruhusu kufanya lolote kama afisa yeyote wa usalama mwenye jukumu maalumu. Zaidi kimetengwa kifungu maalumu cha fedha ambacho kitaingizwa katika akaunti yako ili pesa zisiwe kipingamizi…”

“Taratibu Inspekta,” Joram alimkatiza. “Vipi? Mbona mnanitendea mema mengi hivyo? Kama sikosei unachotaka kusema ni kwamba unaniomba nishiriki katika kutafuta kiini cha maafa haya yanayotendeka katika nchi za mstari wa mbele. Na kama sikosei mtu uliyemtuma kwangu amekupa majibu yangu rasmi, msimamo wangu ni uleule. Na utaendelea kuwa uleule. Kama mlimfahamu Joram ambaye alikuwa mpenzi wa Tanzania na Afrikakwa ujumla, lazima muelewe kuwa Joram huyo amekufa. Aliye hai, mbele yako, ni Joram mpya, Joram ambaye wala hana kiu ya kushiriki kwa njia moja au nyingine katika masuala yoyote ya nchi. Aliyeko mbele yako ni Joram wa mastarehe, Joram wa kutumia. Hata dada yangu Nuru hapa nadhani anaelewa.”

Ndipo Kombora alipoona ugumu wa kazi iliyokuwa mbele yake. Kumshawishi Joram ilikuwa sawa na kulilazimisha jabali lielee juu ya maji. Akiwa mtu ambaye hakuzowea kuwabembeleza binadamu wengine, hasa wanaume, Kombora alisema kwa sauti iliyoficha hasira na unyonge, “Pengine unajua unachokifanya. Lakini nadhani hujui kiwango gani cha madhara yanayolikaribia taifa hili endapo tutashindwa kuukomesha uovu huu unaonyemelea. Niruhusu nikusimulie mambo ya kutisha ambayo hayajavifikia vyombo vya habari.”

“Haitasaidia,” Joram alimjibu. “Utaupoteza bure muda wako. Ninachohitaji kusikia ni habari za burudani tu. Kama kuna burudani mpya ambayo sijaiona, kinywaji kipya ambacho sijakinywa au muziki mpya ambao sijausikia, nitafurahia endapo utanisimulia. Juu ya vifo vya marais na raia wenye hatia na wasio na hatia, si kazi yangu tena.”

“Hata hivyo, sauti yako haifanani kabisa na madai yako Joram. Kuna watu ambao silika yao ni kukesha katika mabaa na madansi, wewe si mmoja wao. Kuna wanaostarehe kusubiri maafa ya kusikitisha, wewe si mmoja wao, Joram. Kuna wanaofurahia ladha ya pombe na utamu wa muziki zaidi ya kazi na ushujaa, wewe si mmoja wao vilevile.”

“Zamani, Inspekta. Sasa hivi mimi ni mmoja wao na nitaendelea kuwa mmoja wao. Na kama huna maongezi mengine zaidi ya haya mzee nitashindwa kuendelea kukusikiliza,” Joram alimaliza akitoa sigara yake na kuiwasha.

Kombora hakujua afanye nini ili amshawishi Joram. Alimtazama Nuru kama aliyehitaji msaada wake. Akayaona macho yake mazuri yaliyojaa huzuni katika hali ya kukata tamaa. Hilo, kiasi lilimfariji Kombora. Alifahamu kuwa anaye msaidizi ambaye angesaidia katika juhudi zake za kumrejesha Joram Kiango katika dunia ya Joram Kiango. Akiwa si mgeni katika dunia hii Kombora alielewa kuwa mwanamke mzuri ni silaha. Hivyo, akamtupia Nuru jicho la kumtaka aelewe kuwa anautegemea msaada wake. Kisha akainuka na kuaga bila ya kumaliza kinywaji chake.

“Hukufanya vizuri, Joram,” Nuru alimwambia.

“Mfuate mkafanye vizuri”.

“Sivyo, sikia…”

Nuru akavunjika moyo. Uchungu mkubwa ukamwingia rohoni. Akajilazimisha kuendelea kunywa pombe, lakini haikumuingia. Baada ya jitihada nyingi alimtaka Joram radhi, akaondoka kutangulia chumbani kwao.

“SAMAHANI, naweza kuketi hapa?” mtu mmoja alisema akimsogelea Joram mara tu Nuru alipoondoka.

Alikuwa mtu wa umri wa kati. Sura yake ilionyesha dalili zote za kutosheka, macho yake yakionyesha kila dalili ya kuelemika. Kiasi alionekana kama ambaye pombe ilianza kumshinda nguvu, japo alitembea kwa uhakika.

Joram alimtazama kwa makini kabla ya kumjibu, “Una haki ya kukaa popote. Nchi huru hii.”

“Asante,” mtu huyo alijibu huku akijibweteka kitini. Baada ya dakika mbili tatu za kunywa na kuvuta kwa utulivu alimgeukia Joram na kumwambia, “Samahani. Sinabudi kulitoa dukuduku langu. Siku zote nimekuwa na hamu ya kuipata fursa hii ya kuketi nawe meza moja. Kama sikosei u Joram Kiango.”

Joram alimtazama mtu huyo kwa makini. Alipochelewa kumjibu mgeni wake aliendelea, “Tumekuwa tukikutana mara kwa mara katika majumba ya starehe. Kilichonifanya nikufahamu ni msichana huyo mzuri unayefuatana nae. Kwa kweli, sina budi kukupa pongezi zako. Wazuri nimewaona wengi, wa aina yake sikupata kumwona. Ulimpataje yule dada, Joram?”

Jambo moja lilimvutia Joram katika kumsikiliza mtu huyu. Jambo la pili lilijitokeza. Sauti. Ilikuwa sauti ya kawaida, ikizungumza kiswahili cha kawaida katika masikio ya watu wa kawaida. Lakini katika masikio ya Joram Kiango, Joram ambaye sasa alikuwa amekaa chonjo, sauti hiyo ilificha uhalisia fulani.

“Unadhani una haki gani ya kunifahamu, na kumfahamu msichana wangu hali mimi sikufahamu hata kidogo?” Alimwuliza.

Kama ambaye alilitegemea jibu hilo mgeni huyo alijibu mara moja, japo kwa kusitasita, “Mimi! kwa jina naitwa Ismail Chonde. Ni mfanyabiashara wa siku nyingi. Nimezaliwa na kukulia hapahapa ingawa siku hizi naishi Nairobi.”

“Na unawezaje kunifahamu kwa urahisi kiasi hicho?”

“Nasoma vitabu, nasoma magazeti. Hakuna asiyekufahamu Joram.” Sauti iliendelea kuwa na walakini katika hisia za Joram. “Inaelekea bado una maswali uliyotaka kuniuliza bwana Chonde. Nataka kumuwahi huyo msichana unayemwita mzuri”.

“Kweli. Inaonyesha aliondoka hapa akiwa amechukia.”

Joram alitabasamu. “Naona umeona mengi zaidi ya hilo.”

“Ndiyo, nimeona na kusikia mengi. Kwa kweli, endapo hutaniona mlevi, nilichokusudia kuongelea ni yule mzee aliyekuacha muda uliopita. Namfahamu yule. Ana madaraka makubwa serikalini. Kama sikosei alikuwa akikushawishi utoe mchango wako katika kupeleleza matukio haya. Na niliona akiondoka bila furaha. Yaelekea umemkatalia. Hivi kweli umekataa katakata?”

Joram alimtazama kwa makini zaidi. “Sielewi maswali yako yanaelekea wapi,” baadaye alisema.

“Inashangaza,” Chonde aliongeza. “Joram ninayemfahamu mimi hawezi kuipoteza nafasi nzuri kama hii ya kuonyesha ushujaa wake. Afrika iko katika mashaka makubwa. Watu wanakufa hovyo. Majumba yanalipuka hovyo. Bara zima liko mashakani. Joram ninayemfahamu mimi angeitoa hata roho yake kujaribu kupambana na hali hii.”

Joram aliipima sauti hiyo, akiilinganisha na uso wa msemaji. Ingawa aliongea kama mtu mwenye uchungu kwa nchi na bara lake, bado hisia fulani zilimfanya Joram aone kitu kama kebehi katika macho yake, kama kwamba alikuwa na hakika kuwa Joram na U Joram wake wote asingeweza kufanya lolote. Wazo hilo lilimuongezea Joram hamu ya kuendelea kumsikiliza.

“Bado sijaelewa unalotaka kusema,” alichochea.

“Sidhani kama wewe ni mzito wa kuelewa kiasi hicho.”

Wakatazamana, kila mmoja akimsoma mwenzake. Kisha Chonde aliangua kicheko kirefu kilichomwacha Joram akitabasamu. Baada ya kicheko hicho akaongeza, “Samahani endapo umeniona mhuni au mlevi. Sikuwa na nia mbaya zaidi ya kuzungumza nawe na kufahamiana. Kwa kheri.” Aliinuka na kuondoka akielekea maliwatoni. Mwendo wake ulikuwa wa kilevi zaidi ya sauti yake.

Joram aliendelea kunywa taratibu. Alipomwona rafiki yake huyo mpya akitoka nje ya hoteli na kusikia mlio wa gari likiondoka, akaenda mapokezi ambapo alimsalimu tena msichana aliyekuwa hapo na kumuuliza kwa upole, “Samahani dada. Hivi huyu bwana aliyetoka sasa hivi anakaa hoteli hii?”

“Yule, hakai hapa. Huwa anatokeatokea tu. Kila mara huja na msichana. Leo ndio kwanza nimemwona peke yake. Sijui wamekosana nini na msichana huyo, maana huyu bwana anaonekana pesa si moja kati ya matatizo yake,” msichana huyo alieleza.

“Pengine hawajakosana,” Joram alimchokoza.

“Wamekosana. Bila hivyo asingenikonyeza mara mbili.”

Joram alicheka. Maongezi hayo yalikatizwa kidogo kwa simu ambayo msichana huyo alikuwa akiijibu. Alipotaka kuanza tena maongezi iliingia simu nyingine. Ambayo msichana huyo alionekana kuifurahia zaidi. Alizungumza kwa furaha huku akitabasamu. Baada ya kutoa chombo cha kuongelea alimgeukia Joram na kusema, “Unaona? Nimekwambia leo hana mtu. Ananiambia nikimaliza kazi nimkute hoteliya New Africa, chumba namba 104.”

“Ndipo anapokaa?” Joram alihoji.

“Bila shaka.”

Baada ya mazungumzo hayo Joram aliirudia meza yake na kuendelea kunywa. Mawazo yake yalimfikiria Chonde. Hakuelewa dhamira ya maongezi yake yote yale ilikuwa nini hasa. Alishuku kuwa pengine alikusudia kupata undani wa Joram na uamuzi wake. Kwanini? Zaidi Joram alishuku kuwa mtu huyo hawakukutana kuzungumza kiajaliajali, bali alikuwa akimfuata yeye au Kombora kwa ajili hiyo. Juu ya yote hayo zile hisia za Joram katika sauti ya mtu huyo zilizidi kujiimarisha akilini mwake. Aliona kama ulikuwemo walakini fulani katika sauti ya kiswahili chake ambao uliutia dosari Utanzania wake. Hayo na kile alichoona katika macho ya mtu huyo vilimtia Joram hamu ya kumfahamu vizuri.

Hivyo, dakika tano baadaye alijikuta mitaani akielekea New Africa. Alipofika hapo alimwendea mfanyakazi wa mapokezi na kujitia akizungumza naye hili na lile huku macho yake yakiwa kazini kutazama endapo ufunguo wa chumba namba 104 ulikuwepo. Aliuona. Akauliza juu ya mtu wa chumba fulani ambacho aliona ufunguo wake haupo.

“Yuko ndani. Ameingia sasa hivi.”

“Ngoja nikamwone.”

Badala ya kwenda chumba hicho, Joram alipanda gorofani hadi chumba namba 104 ambacho kilikuwa kimefungwa. Kuacha kwake tabia ya kutembea na bastola hakukumfanya aache kutembea na vifaa vyake vidogovidogo, kama funguo malaya ambazo hazishindwi kuifungua kufuli yoyote ya kawaida. Hivyo, kitasa hicho cha mlango wa Chonde kilimpotezea nusu dakika tu.

Chumbani humo, Joram aliurudisha mlango na kuufunga kwa ndani. Kisha aliangaza huku na huko kwa makini. Kilikuwa chumba cha kawaida kama vilivyo vyumba vingine vya hoteli. Hivyo, Joram hakuwa na kazi ngumu zaidi ya kupekuwa magodoro na viti. Hakuona chochote. Ndipo alipoliendea Kabati na kulifungua. Ndani ya kabati hilo mlikuwa na sanduku kubwa ambalo pia Joram alilifungua. Mlikuwa na pesa za kutosha pamoja na mavazi. Vitu hivyo havikumvutia. Macho yake yalivutiwa na makaratasi mbalimbali ambayo aliyapekua kwa makini. Mengi yalikuwa makaratasi ya kawaida ambayo yalimwezesha kumfahamu mtu wake kuwa aliitwa Afith Chonde. Baada ya kupekuwa zaidi aliipata hati yake ya usafiri. Aliifunua harakaharaka huku akisoma mihuri mingi iliyopigwa katika hati hiyo kuonyesha nchi Chonde alizozitembelea. Alikuwa anatembea sana. Mihuri ya Nairobi, Lagos, Lusaka, Harare, London, New York, Hong Kong, Tripol n.k ilionekana waziwazi. Hilo lilimfanya Joram azidi kuvutiwa na mtu huyo. Hakuonekana kama mfanyabiashara mkubwa kiasi hicho. Zaidi ya vipindi alivyokuwa akitumia mji hadi mji vilikuwa vifupi mno kiasi kwamba Joram alishuku kuwa hakuwa akifanya biashara za kawaida. Hivyo, akaongeza umakini katika upekuzi wake.

Kama alivyotegemea, Joram aliigundua mifuko ya siri katika begi hilo, mifuko ambayo maafisa wa forodha wasingeweza kuipata bila ya ujuzi maalumu. Katika mifuko hiyo, Joram alipata bastola moja aina ya revolver, maandishi mbalimbali ambayo alijaribu kuyasoma hakagundua kuwa hawezi kwani yaliandikwa kimafumbomafumbo katika hali kamili ya kijasusi. Pamoja na kijaluba kidogo cha chuma ambacho kilikuwa kimefungwa kwa ufunguo. Kijaluba hicho kilimvutia Joram zaidi. Alihisi kuwa kilikuwa kimeficha mengi zaidi ya yale aliyokwishayaona. Hivyo, akaanza kuzijaribu funguo zake malaya. Zilimchukua dakika kadhaa kugundua kuwa kamwe asingeweza kukifungua kijisanduku hicho. Kilitengenezwa maalumu kupambana na hila zozote za kufunguliwa pasi ya utaalamu wa mwenyewe. Kiu ya Joram juu ya kumjua vyema mtu huyu ikazidi kuneemeka. “Vipi awe na kisanduku kama hicho? Kilificha nini? Na maandishi haya ya siri yanasema nini? Siyo bure. Liko jambo,” aliropoka.

“Ndiyo. Kuna jambo,” sauti ilizungumza nyuma ya Joram. Akageuka hima na kukutana na uso wa Chonde ambao ulikuwa ukimtazama kwa kebehi. Alikuwa kaketi juu ya kochi. Alivyoingia chumbani humo kwa ukimya kama jini na kuketi kwa utulivu kwa kipindi chote hicho ni jambo ambalo lilizidi kumwongezea Joram ushahidi kuwa alikuwa hachezi na binadamu wa kawaida. Joram akageuka na kumtazama Chonde huku akiruhusu moja ya zile tabasamu zake za kishujaa, tabasamu ambalo lilifuatwa na sauti yake tulivu akisema, “Tuseme nimefumaniwa”.

“Umefumaniwa. Na una bahati mbaya kuwa umefumaniwa na kifo. Binadamu hanichezei mimi na akaendelea kuishi,” Chonde alisema akianza kuinuka taratibu. “Ulijifanya umeacha maisha yako ya kuingilia mambo yasiyokuhusu. Kumbe ulikuwa ukijifurahisha kwa kujidanganya mwenyewe. Umekosea sana.” Akamtazama kwa dharau na kebehi. “Huwa nafurahia zaidi kuwaua watu wangu kwa mikono,” alisema akizidi kusogea.

Mzaha haukuwemo katika macho na sauti ya Chonde. Alionekana mtu anayejua anachokifanya, jambo ambalo lilimfanya Joram asogeze mkono kuiendea ile bastola ambayo ilikuwa imelala kando yake. Kama alikuwa ameuhisi wepesi wa Chonde basi alikuwa hajauona. Mara tu mkono huo ulipoifikia bastola tayari mguu wa Chonde ulitua juu ya mguu huo. Wakati huo huo Joram alipokea ngumi mbili ambazo zilizomfanya apepesuke na kuisahau bastola. Chonde hakuwa na roho mbaya kiasi hicho. Alimpa muda wa kujiandaa. Joram akavuta pumzi kwa nguvu na kuanza kumwendea Chonde. Alimshitua kwa mkono wa kulia, Chonde aliudaka na wakati huohuo kumkata Joram judo ya mgongo ambayo ilimfanya aanguke kifudifudi. Alipoinuka Chonde alikuwa akimsubiri huku akicheka, “Wanasema Tanzania kuna mtu mmoja tu wa kujihadhari nae, ambaye anaitwa Joram Kiango. Niko naye chumbani, sioni Ujoram wake.”

Maneno hayo yalimwuma Joram zaidi ya kipigo alichopokea. Akainuka ghafla na kumwendea Chonde akitumia mitindo yake yote ya kupigana. Vipigo kadhaa vilimpata Chonde. Lakini kwa jinsi vipigo hivyo vilivyopigwa kwa hasira havikuwa na madhara makubwa kwa Chonde. Dakika chache baadaye Joram alijikuta chali sakafuni, kasalimu amri. Chonde akaendelea kutabasamu.

Sasa Joram alimtazama Chonde kwa mshangao zaidi ya hasira. Ni mtu wa aina gani huyu anayeweza kumwadhibu kama mwanae? Bila shaka si mtu wa kawaida. Amejifunza mengi kama anavyoonekana kujua mengi. Pamoja na kwamba kipindi kirefu kilikuwa kimepita bila ya Joram kufanya mazoezi ya viungo wala akili, pamoja na kule kuzoea starehe za mahotelini na ulevi mwingi, bado hakuona kama binadamu yeyote angekuwa na haki au uwezo wa kumfanya apendavyo kama Chonde alivyokuwa amemfanya.

Ile hamu iliyokuwa imelala usingizini ikaibuka upya katika moyo wake, hamu ya mapambano, vitisho, maafa, damu, na mikasa, hamu ya kuwatia adabu watu wanaopenda kuwafanya vibaya binadamu wenzao. Chonde alionekana kama mmoja wao. Joram akamtazama tena na kutabasamu kwa uchungu huku akisema, “Haya, umeshinda. Kinachofuata?”

“Kifo chako,” Chonde alimjibu kijeuri. “Siwapendi vijana watundu kama wewe. Kufa, huna budi.”

“Kosa langu.”

“Unapenda kufa?”

Joram alifikiri kwa makini angefanya nini kuiahirisha hukumu hiyo ya kifo. Muda. Alihitaji muda ili ikiwezekana itokee njia moja au nyingine ya kuyaokoa maisha yake. Akaanza maongezi kwa sauti ambayo aliifanya dhaifu kuliko ilivyokuwa, akimwuliza Chonde hili na lile. Chonde alikuwa mgumu wa kutoa habari kama jabali. Kati ya maneno ya kashfa na matusi kwa Joram, nchi na bara zima hakutamka neno lolote ambalo lilimfanya Joram amjue yeye ni nani na anafanya nini katika ulimwengu wa ujasusi. Alichoambulia ni zile hisia tu kwamba Chonde hakuwa raia wa kawaida.

“Umeahirisha sana kifo chako,” Chonde alisema baadaye kama aliyekuwa akizisoma fikra za Joram. “Sasa iliyobaki ni kazi ndogo ya kukutoa uhai. Nitakuua kwa mkono wangu wa kushoto. Maiti yako itaokotwa kesho ikiwa imevunjikavunjika kama mtu aliyeanguka toka ghorofani. Kwa jinsi ulivyobadilika kitabia watu hawatashangaa kusikia kuwa umejirusha dirishani.”

Baada ya maneno hayo, aliinuka na kumwendea tena Joram kwa utulivu kama awali, lakini macho yake yalitangaza kitu kimoja tu, kifo.

Joram alijiandaa, akijua kuwa vita vilivyokuwa mbele yake vilikuwa vikubwa kuliko vyote alivyowahi kupambana navyo, vita vya kuitetea roho yake. Akaikusanya akili yake yote na kumsubiri Chonde kishujaa.

Mara mlango ukagongwa.

Chonde aligutuka kwa mshangao na kuutazama mlango huo. Joram hakuipoteza nafasi hiyo. Aliruka na kuufanya mguu wake utue katika shingo ya Chonde. Lilikuwa pigo ambalo Chonde hakulitegemea. Likamtia mweleka. Lakini pigo la pili alilitegemea, akalikwepa na kuachia judo ambayo Joram aliikinga. Papo hapo mlango ukagongwa tena na kufunguka ukiruhusu sura ya msichana mzuri kuingia.

Alikuwa yule msichana wa mapokezi wa hoteli ya Embassy. Alitokwa na macho ya mshangao kuona miili yenye jasho, michubuko na damu, ya wanaume hao, ikiwa tayari kuvamiana. Wote walimtazama msichana huyo, Chonde akimlaani, Joram akimshukuru. Akiwa kama hajui lipi la kufanya msichana huyo aliduwaa mlangoni, Mdomo wazi.

“Karibu ndani. Tulikuwa tukifanya mazoezi ya viungo na huyo rafiki yangu,” Chonde alimhimiza akivaa tabasamu ambalo lilificha kabisa mauaji yaliyokuwa katika uso huo dakika iliyopita. “Karibu ndani. Nawe ndugu yangu nenda zako sasa. Tutakutana siku nyingine”.

Joram aliyarekebisha mavazi yake na kutoka chumbani humo taratibu. Hakuwa amesahau kumwachia msichana huyo tabasamu jingine la shukrani.


“Nadhani hakuna njia nyingine zaidi ya kumlazimisha,” Kombora alikuwa akifoka katika kikao cha dharura kilichofanyika usiku huo. “Hawezi kuachwa aendelee kustarehe katika mabaa huku taifa na bara zima likiwa mashakani. Mchango wake unahitajika.”

Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi wote wa ngazi za juu katika idara zote za usalama nchini. Kiliitishwa ghafla baada ya kuokotwa barua moja ya vitisho katika ofisi ya Waziri Mkuu, barua ambayo iliandikwa kwa ufupi sana ikidai kuwa ajali za kimiujiza zingeendelea kuipata nchi ya Tanzania na zote zilizo mstari wa mbele, endapo serikali isingechukua hatua za haraka kukomesha msimamo wake wa kupinga utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini. Barua hiyo iliongeza kwamba safari hii moto ungeiteketeza hospitali ya Muhimbili, hoteli ya Kilimanjaro, Jengo la Kitega Uchumi na baadae Ikulu.

Aliyeiokota barua hiyo na kuisoma aliwaonyesha wakubwa wake ambao waliikabidhi kwa Waziri Mkuu. Baada ya kuisoma yeye pia, alikwenda Ikulu ambako alimpa Rais.

“Upuuzi ulioje huu. Hatutaacha kuwatetea ndugu zetu wanaoteswa bila makosa kwa ajili ya vitisho hivi. Havikuanza leo. Wala haviwezi kwisha leo. Tutapigana hadi mtu wetu wa mwisho katika kuilinda hadhi ya mtu mweusi katika bara letu hili.” Pengine Rais alijibu hivyo akifoka kwa hasira. “Barua hiyo wakabidhi watu wa usalama. Nadhani hawatakubali kuendelea kuchezewa kiasi hiki. Waambie kwamba hatutaki upuuzi wowote ulioandikwa katika waraka huu haramu utokee.” Huenda Rais aliongeza hayo.

Hakuna aliyeshiriki katika maongezi yao ya faragha, isipokuwa hisia hizo zinakuja kwa jinsi Waziri Mkuu alivyomwita Inspekta Kombora katika ofisi yake na kumkabidhi barua hiyo. Baada ya Kombora kuisoma kwa makini Waziri Mkuu alimwambia, “Ni barua ya khatari sana. Na imeandikwa na watu khatari, watu wenye kichaa. Kufuatana na hali ilivyo hatuwezi kukubali kuwa watumwa au mateka wa Makaburu kwa kuhofia ukatili wa vitisho vyao. Lazima tupambane nao ana kwa ana kama tunavyopambana nao katika uwanja wa mapambano. Tuliwashinda Msumbiji, Angola na Zimbabwe. Kwa nini tusiwashinde Namibia na Afrika Kusini? Tutawashinda. Wao wanajua hivyo, ndiyo sababu inayowafanya wakimbie toka katika uwanja wa mapambano na kuja huku kupigana kiuoga.”

“Kama tulivyoshuku kitambo, mikasa hii haikuwa ya kawaida. Kulikuwa na mkono wa mtu, mkono wa mtu huyu ambaye ameandika barua hii na kuthubutu kuipenyeza katika ofisi yangu. Ingawa haijafahamika mbinu gani wanatumia kuweza kuanzisha mioto hii, nadhani hutashindwa kufanya juu chini ili uugundue na kuukomesha kabisa upuuzi huu.”

Akijua uzito wa jukumu hilo ndipo Kombora aliporudi ofisini na kuitisha kikao hiki kilichokuwa kikiendelea. Walijadiliana kwa mapana na marefu kulikuwa na nini hasa hata majumba yalipuke moto ilihali uchunguzi kamili ulionyesha kuwa haikuwepo kasoro yoyote ya umeme. Hawakupata jibu. Walijaribu kuzijumuisha taarifa zote za upelelezi juu ya nani anaweza kuwa alihusika katika kusababisha mioto hiyo lakini bado hazikuwepo dalili zozote zilizoleta matumaini. Wakapanga mipango mipya. Wakawaandaa wapelelezi na vyombo kadha wa kadha katika majumba yaliyotajwa. Wakawekwa watu katika mahoteli, viwanja vya ndege na vituo vyote vya usafiri kuchunguza nani anaingia, nani ametoka na ameleta nini. Zaidi ya yote hayo, ndipo lilipotolewa tena pendekezo la kumshirikisha kila mtu mwenye uwezo wa kuchangia katika upelelezi. Hapo ndipo jina la ‘Joram’ lilipowatoka midomoni. Ikawashangaza wajumbe kusikia kuwa hata baada ya kuombwa na Kombora alikataa katakata kushiriki katika kazi hiyo. Joram waliyemfahamu alikuwa hangoji kuombwa au kutumwa bali alijituma. Vipi Joram huyu?

Ndipo mzee Kombora alipoibuka na uamuzi wa kumshurutisha. “Lazima tumlazimishe. Kama ameacha upelelezi kwa ajili ya mwanamke, basi atarudia upelelezi kwa ajili ya mwanamke. Yote hayo niachieni mimi,” Inspekta Kombora aliwaambia.

Baada ya kikao hicho, alimchukua msaidizi wake mmoja na kumpeleka chemba. “Sikia,” akamweleza, “Nakutaka uwe msiri wangu, wewe peke yako. Unaweza kutunza siri?”

“Bila shaka. Isipokuwa ya wizi na mauaji tu.”

“Hii si ya mauaji wala wizi. Nataka unisaidie kumteka mtu nyara.”

“Kuteka mtu nyara? Hiyo mbona haiko mbali sana na wizi? Na kama sikosei ni hatari zaidi ya wizi.”

“Ndiyo. Lakini mtu tunayemtaka atafurahi sana. Bado ni msichana mzuri sana,” Kombora alivuta pumzi kwa nguvu kisha akaongeza, “Nataka tumteke yule msichana wa Joram. Hiyo ndiyo njia pekee ya kumlazimisha.”

Baada ya kujadiliana kwa muda walielewana. Wakaandika barua ambayo ilikusudiwa iwe imetoka kwa mteka nyara akidai kuwa amemteka msichana huyo na angemwua endapo Joram angethubutu kujihusisha na upelelezi unaoendelea nchini dhidi ya maafa ya kutatanisha. Licha ya barua hiyo, pia waliandaa damu ambayo ilipatikana kwa msaada wa daktari mmoja wa hospitali yao Ocean Road ili waidondoshe chumbani humo kuonyesha kuwa kulikuwa na mapambano ambayo yalisababisha damu kumwagika.

“Tunacheza mchezo mchafu sana, mchezo wa aibu. Lakini hatuna budi,” Kombora alisema baada ya matayarisho yote ya kwenda katika chumba cha Joram.

Uchunguzi uliwapa fununu kuwa Joram alikuwa akiishi katika hoteli hiyo ya Embassy. Habari za mwisho usiku huo zilieleza kuwa Joram alipoachana na Kombora usiku huo alikuwa peke yake akinywa bia wakati msichana wake alipoondoka kwenda chumbani, na kwamba baada ya muda mrefu Joram alionekana akitoka nje na hadi sasa alikuwa hajarudi. Kombora alitegemea kuwa muda huo ulitosha kumfikia msichana huyo, kumshawishi na akikataa, kumlazimisha kisha kuondoka naye kwa siri kabla Joram hajarudi.

Walifanya hivyo.

Waliifika hoteli na kukiendea chumba chake kwa siri kubwa. Mlango waliukuta ukiwa wazi. Wakaufungua na kuingia huku wakiufunga nyuma yao. Macho yao yalivutwa na dalili za vurugu katika chumba hicho. Vitu vilikuwa vimetupwa ovyoovyo, matandiko yakiwa yamepinduliwa na masanduku kufunguliwa. Juu ya meza kulikuwa na karatasi yenye damudamu. Upande wa pili wa karatasi hiyo kulikuwa na maandishi ambayo yalikuwa barua ya wazi kwa Joram Kiango, barua ambayo haikutofautiana sana na ile ambayo Kombora aliiandaa:

Ndugu Joram,

Tunayo furaha kukufahamisha kuwa tumemchukua msichana wako na tutakuwa nae hadi hapo tutakapomaliza shughuli zetu. Hii ni kwa ajili ya kukuonya usithubuti kujihusisha na mambo yoyote yanayoitokea nchi hii. Endapo utakuwa mtoto mtiifu kama ulivyo siku hizi, hatadhurika, nawe utakuwa salama. Vinginevyo, utakipokea kichwa chake kwa njia ya posta na kisha kitafuata kifo chako.

Amri

Kombora aliisoma tena barua hiyo, kisha akamgeukia msaidizi wake na kumnong’oneza, “Tumechelewa sana. Wenzetu wametuwahi.” akampa barua hiyo ili aisome.

“Sasa tutafanya nini?” askari huyo aliuliza baada ya kuisoma.

“Rudisha kila kitu kama kilivyokuwa. Fanya hima tuondoke hapa haraka,” alimhimiza akianza kusogea mlangoni.

“Nilidhani tungemsubiri Joram!”

“Hakuna haja. Akirudi atajua la kufanya.” Wakatoka na kuifuata njia ya kawaida. Wakiwa katika mavazi ya kiraia, watu wachache sana waliwatupia macho zaidi ya mara moja. “Jambo moja la kupendeza ni kwamba,” Kombora alikuwa akisema. “Wamemchokoza Joram. Hawamfahamu vizuri. Wataujutia uamuzi wao”


Joram alifika chumbani kwake dakika kadhaa baadaye. Akiwa mchovu, jicho moja likiwa limevimba kwa pambano lake na chonde, alipitiliza hadi bafuni ili ayaepuke maswali ya Nuru. Huko ndani alioga vizuri, akaisafisha damu yote na kushevu kikamilifu. Kisha akarudi chumbani ambako macho yake yalivutwa na vurugu iliyokuwa imetokea.

Alitazama vitanda vyote na kutoiona dalili ya Nuru. Akaenda mezani ambako hakushangaa kukuta ujumbe ule ukiwa juu ya karatasi yenye damudamu. Akausoma kwa makini, akiuchunguza mwandiko huo ambao ulikorogwa katika hali ya kupoteza uhalisi wake. Akatikisa kichwa na kutokwa na tabasamu jembamba.

Usiku huo alilala huku kalisahau tabasamu hilo katika uso wake.

SURA YA NNE

ASUBUHI hiyo, baada ya kuoga na kufungua kinywa, Joram alichukua simu na kupiga namba mbili tatu akitaka kuzungumza na rafiki zake wa zamani. Alipowapata aliwapa maekelezo fulanifulani kwa lugha ambayo wangeielewa wao tu. Baada ya hapo akajitokeza mitaani na kuanza matembezi. Akiwa kavaa vizuri suti yake ya kijivu aina ya three peace, kofia ikiwa imezifunika nywele zake ili kuficha mchubuko uliokuwa upande wa kushoto na miwani myeusi ikilificha jicho lake ambalo lilikuwa halijatii dawa kikamilifu, alionekana kama alivyotaka, mwungwana asiye na tatizo lolote mwilini wala akilini.

Msafara wake wa kwanza uliishia Barabara ya Sokoine katika tawi la Benki ya Taifa ya Biashara City Drive. Aliingia ndani na kuomba kuonana na meneja. Akaelekezwa hadi katika chumba ambamo alikaribishwa vizuri na afisa huyo ambaye uso wake ulimdhihirishia Joram kuwa hakuwa akiwajibika ili kuitikiwa wito bali kuwajibika kulikuwemo katika damu yake tangu alipozaliwa.

“Nikusaidie nini ndugu yangu?”

“Naitwa Joram Kiango. Ninayo akaunti hapa.”

“Nakufahamu sana, ingawa ni mara yangu ya kwanza kukuona ukija huku kwetu. Mara nyingi unaishia huko huko kwenye pesa.” Baada ya kutabasamu kidogo kwa mzaha huo aliongeza harakaharaka. “Umefuata mkopo?”

“Hapana mzee,” Joram alimjibu. “Nikikopa nitashindwa kulipa. Ninachohitaji ni kutazama uwezekano wa kuweka mali yangu fulani ya thamani katika akaunti mnayoita Self-Custody. Ningependa mnifahamishe utaratibu ulivyo.”

Meneja alitikisa kichwa huku akisema, “Hilo tu? Kwanini wamekusumbua hadi huku? Utaratibu wake si mrefu sana. Ziko fomu maalumu ambazo utajaza. Baada ya hapo utakabidhiwa ufunguo mmoja, ufunguo wa pili tutakuwa nao. Utakwenda huko chini na kuhifadhi mali yako hadi siku ambayo utapenda kuikagua au kuichukua. Malipo yake ….”

Joram alimsikiliza kwa makini, akitupa swali moja moja. Kisha alimwomba meneja akatazame hali ilivyo huko chini kabla hajajaza fomu zozote. Meneja akainuka na kushuka nae hadi shimoni. Walipita vyumba vya kuhifadhi nyaraka, baadhi vinahifadhiwa pesa na kimoja alielezwa kuwa kiliazimwa na Benki Kuu baada ya jengo lao kuharibika kwa moto. Baada ya kupewa picha kamili ya ulinzi na usalama wa hifadhi hiyo Joram aliaga na kuahidi kuwa angerudi baadaye kukamilisha kazi hiyo.

Toka hapo Joram alipita hapa na pale akifanya hili na lile, sigara baada ya sigara zikiteketea mdomoni, mwendo wake ukiwa wa utulivu kama mtu asiye na tatizo lolote ulimwenguni. Ungemwona kamwe usingefikiria kama mtu ambaye usiku wa jana mpenzi wake alitekwa nyara, bila shaka baada ya kuteswa sana.

Ni hali yake hiyo ya utulivu ambayo ilimshangaza Inspekta Kombora alipokutana nae katika mtaa wa Samora. Kombora alisimamisha gari lake na kumfuata Joram kando ya duka alipokuwa kasimama. “Joram,” alisema baada ya kumsalimu. “Nasikia yule msichana wako ametekwa nyara”.

“Hata mimi nasikia hivyo,” lilikuwa jibu la Joram.

“Mbona hufanyi lolote.”

“Nifanye nini? Barua imenionya nisithubutu kufanya lolote. Vinginevyo, msichana wa watu atauawa. Unapenda afe, Inspekta?”

Kombora alitikisa kichwa kwa mshangao. “Joram niliyemfahamu mimi alikuwa hapokei amri kwa watu kama hao, hasa katika suala hili ambalo ni la uhai na kifo cha mtu na taifa zima. Mimi nilidhani wamekuchokoza. Nikategemea kuwa wangejutia uamuzi wao. Nilikosea?”

“Umekosea sana Inspekta. Joram unayezungumza naye si yule wa awali. Usishangae, Inspekta. Usiupoteze bure mshangao wako. Bado kuna mengi utayasikia juu ya Joram huyu ambayo yatakushangaza zaidi,” Joram alisema huku akitupa kipande kimoja cha sigara na kuwasha nyingine. Alipomuona Kombora kama mtu ambaye hajui la kufanya au asiyeyaamini masikio yake, akaamua kuondoka polepole. Kombora alimsindikiza kwa macho yake yaliyojaa mshangao na huzuni.

Baada ya pitapita hii ya hapa na pale, Joram alirejea chumbani kwake ambako alijipumzisha kwa muda.Wafanyakazi na baadhi ya wapangaji wenzake, ambao walikuwa wamemzoea Nuru, walimsumbua Joram kwa kutomuona.

“Anaumwa?”

“Hapana. Kapata safari ya ghafla.”

“Bila kuaga?”

“Ilikuwa ghafla.”

Aliujenga vyema uongo wake huo hadi ukafanana na ukweli. Jioni hiyo, baada ya kula, kuoga na kupiga simu nyingine alijitokeza mitaani na kuanza matembezi yake. Safari hii matembezi hayo yaliishia Ilala, nyumbani kwake. Alielekea chooni ambako alifunua mahala fulani pa siri ukutani na kutoa kijisanduku alichokuwa kakificha hapo. Alishangaa kukuta kikiwa kitupu bila ya bastola na risasi zake ambazo alikuwa ameziweka huko. Hifadhi hii ilikuwa siri yake binafsi. Mtu pekee ambaye aliifahamu siri hiyo ni Neema Idd ambaye sasa ni Marehemu. Mtu mwingine ambaye angeweza kufahamu ni Nuru. Uko usiku mmoja, kati ya zile chache ambazo waliwahi kulala katika nyumba hii, alimtoroka Nuru akidhani yuko usingizini, akaja hapa na kuisafisha bastola hii. Pengine Nuru aliwahi kumchungulia. Lakini Nuru huyo sasa yuko mikononi mwa wateka nyara. Nani mwingine aliyeijua siri hii? alijiuliza kwa hasira, hasira ambazo zilimfanya atupe kasha hilo na kutoka nje baada ya kuifunga milango yote kwa ukamilifu. Msafara huu uliishia katika hoteli ya Embassy. Akaagiza vinywaji na kuanza kunywa. Baada ya bia mbili akaenda kaunta kuzungumza na yule msichana wa mapokezi.

“Shem, za kutwa.”

“Nzuri sana, shemeji,” msichana huyo alizungumza kwa furaha huku akimtazama Joram kwa mshangao. “Pole sana shemeji,” aliongeza.

“Kwa?”

“Ule mchezo wa jana. Unajua mimi mpaka sasa siamini kama mlikuwa mnacheza tu. Nilidhani mlikuwa mnapigana. Yule bwana kashikilia kuwa ni mchezo tu”.

“Ulikuwa mchezo. Mazoezi ya viungo. Wazungu huita practice.”

“Mpaka mtoane damu?”

ITAENDELEA

Tutarudi na Roho Zetu Sehemu ya Pili

Isikupite Hii: Jinsi Ya Kumfanya Mwanamke Akupende Kwa Mara Ya Pili

Also, read other stories from SIMULIZI;

Leave a Comment